Ukitoa Msaada Huu Hakika Utakumbukwa Daima

Habari rafiki,

Kila mtu, bila kujali ana nini, hujikuta wakati fulani anahitaji msaada kutoka kwa rafiki, jirani au ndugu zake.

Msaada unaweza kuelezewa kama kitu anachotoa mtu au taasisi ili kutimiza haja fulani au kutatua tatizo la mtu au taasisi yenye uhitaji.

Wakati wa dharura au maafa misaada kama hii ni ya lazima

Sasa, tukiongelea suala la uhitaji, je ni wakati gani tunaweza kusema taasisi au mtu ana uhitaji ili apewe msaada? Je, ni wakati wowote tu? Je, ni wakati wa maafa au majanga? Au ni wakati gani?

Na kama utagundua, baada ya tathmini, kuwa ndugu, rafiki, au taasisi inahitaji msaada, je ni msaada gani utampatia? Je, ni pesa? Je, ni vifaa? Je, ni ushauri – au ni nini?

Kabla hujatoa maoni yako kwa maswali haya nakuomba ufuatilie hadithi hii fupi kutoka katika kitabu cha dini.

Hapo zamani za kale, katika kijiji kimoja, waliishi vijana wawili, Rahim na Rahman. Kila siku asubuhi vijana hawa waliondoka na mashoka yao kwenda msituni, jirani na kijiji chao, kuchanja kuni kwa ajili ya kuuza.

Inapofika mchana, baada ya kukata kuni za kutosha, vijana hawa walikuwa na tabia ya kukaa kando ya mto ili kula chakula walichofungashiwa asubuhi.

Baada ya mlo walizibeba kuni zao kuelekea sokoni kwa ajili ya kuziuza kabla ya kuanza safari ya kurudi nyumbani jioni.

Sasa, siku moja baada ya kukata kuni zao, waliketi kwa ajili ya mlo wa mchana. Kuinua macho, Rahim akamwona kijana mmoja aliyedhoofika, mchafu na mwenye mavazi duni, ingawa alionekana hana tatizo la kiafya.

Kijana huyu alitokea porini kuja upande wao na alipokaribia macho yake yote yalilenga bakuli lenye chakula. Alionekana ana njaa sana, na bila kupoteza muda alipeleka ombi la chakula ili akidhi njaa yake.

Rahim, huruma ilimshika na haraka aliuendea mkoba wa chakula akatoa kipande kimoja ili ampatie ‘ombaomba’ yule maskini.

Kabla Rahim hajampatia kipande kile, Rahman aliudaka mkono wake na kuuvuta, kisha akamwambia yule ombaomba, “hatuna chakula cha kutosha sisi.”

“Angalia, tunajituma kufanya kazi kutwa nzima, tumekaa hapa tupate mlo wetu halafu tutakwenda sokoni kuuza kuni; hivyo hatuna chakula cha kukupa wewe – lakini kama uko tayari nitakusaidia kitu.”

Rahman alimwonesha shoka na kumwambia, “nitakuazima shoka langu, nami nitakufundisha kukata kuni, kisha nitakufundisha jinsi ya kuuza kuni sokoni.”

Akamwambia kuwa akishauza kuni atapata pesa kwa ajili ya chakula na mahitaji mengine, na kwamba hatakuwa ombaomba tena na heshima yake itarudi.

Baada ya kuelewa somo, kwa shingo upande, ombaomba aliungana na Rahman, wakaenda msituni. Kijana akafundishwa kukata kuni na kuzifunga vizuri kwa ajili ya kuzipeleka sokoni.

Walipofika sokoni Rahman alimfundisha maskini yule mbinu za kuuza na kumwacha aendelee na mauzo. Ulipita muda mwingi bila kijana yule kuuza chochote hadi akapata hasira na kukata tamaa.

Alianza kuwaza, “yaani hawa vijana bora wangekuwa wakarimu – wangenipa chakula chao – ningekula nikashiba nakuachana nao, kuliko kuteseka namna hii hapa.”

Akiwa katika mawazo haya, ghafla likatokea gari likapiga breki karibu naye. Akashuka mzee mmoja aliyenunua kuni zake zote, akaziweka katika gari lake na kumkabidhi bunda la noti.

Akiwa haamini macho yake, alipokea pesa zile kwa furaha na haraka akamkimbilia Rahman kumwonesha alichopata.

Rahman alimpongeza kisha akampeleka kwenye duka la mashoka. Kijana alinunua shoka moja na kumshukuru Rahman kwa kumfundisha kazi na mbinu za kuuza.

Kwa vile alikuwa na njaa alinunua chakula cha kushiba, akala na kupumzika tayari kwa kazi ya kukata kuni kesho yake

Alipoondoka, Rahman alimgeukia Rahim na kumwambia, “angalia, tungempa chakula ombaomba yule angekula haraka, angeshiba na kurudi tena msituni kulala. Kesho angekuja tena kutuomba na angeendelea hivyo kila siku.”

“Kwa kumpatia ujuzi wa kukata kuni na kuuza, na kwa kumsaidia kupata shoka lake, tumempa vitu ambavyo vitampa chakula na mahitaji mengine siku zote – na sasa hatakuwa na njaa tena.”

Hatua ya kuchukua: msomaji unashauriwa kuzingatia msemo usemao “usimpe mtu samaki – bali mpe ndoana na mfundishe jinsi ya kuvua samaki.”

Hivyo… ndugu, rafiki au jirani akiwa na uhitaji unatakiwa kuwa makini ili umsaidie kitu ambacho kitampa suluhisho la kudumu la tatizo lake. Misaada mingine inalemaza akili kuliko kutatua matatizo. Je, nini maoni yako kwenye hili?

Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasirimali kivitendo.

Anapatikana kwa e-mail: nzyy2001@gmail.com; Mobile: 0718219530

Je, Mzazi Una Nafasi Gani Katika Kukuza Kipaji cha Mwanao?

Habari rafiki,

Karibu tena katika makala hii tujifunze stadi za maisha. Kwa mujibu wa Shirika la Afya Duniani (WHO) stadi za maisha ni elimu yenye lengo la kujenga tabia njema ya mtu na kumpa uwezo wa kubaini fursa na matatizo yake – na kujua mbinu za kushughulika nayo.

Lengo la stadi za maisha ni kukuza na kuendeleza stadi zinazohitajika katika maisha ya kila siku, mfano kufanya maamuzi.

Makala ya leo itajikita katika kitu kiitwacho ‘kipaji cha mtoto’ na nafasi ya mzazi katika kushughulika nacho.

Mchunguze mtoto – anapenda kujifunza nini? Huenda ndio kipaji chake – msaidie kukikuza

Mhubiri mmoja amewahi kusema kuwa Mungu alipomuumba mtu aliweka vipaji ndani yake. Kipaji ni uwezo asilia alionao mtu unaomwezesha kutenda mambo yenye matokeo makubwa kwa kutumia nguvu au rasilimali kidogo.

Kinachompa mtu huyu nguvu ya kuendelea kufanya ni ile motisha iliyomo ndani mwake.

Moja ya changamoto zinazowakabili wazazi kuhusu suala la vipaji ni kutokujua kama mtoto wake ana kipaji. Changamoto nyingine ni kushindwa kukinoa kipaji kilichogundulika na kukitumia kiuchumi kutengeneza pesa.

Mwandishi mmoja anasema kuwa kutokujua kipaji alichonacho mtu ni chanzo kimojawapo cha umaskini. Kwa hiyo ni jambo muhimu katika familia au jamii kuwa na utaratibu wa kuvibaini na kuviendeleza vipaji vya vijana wetu.

Nchi zilizoendelea kama Marekani zimepiga hatua kubwa katika hili ambapo katika nchi hizi, vijana huendelezwa katika fani au stadi wanazozipenda. Kwa kufanya hivi vipaji vyao hukuzwa kirahisi hadi kufikia uwezo wa juu.

Watu mashuhuri na wabunifu kama Steve Jobs, mwanzilishi wa Apple, na Mark Zuckerberg, mwanzilishi wa Facebook – ni mifano hai ya watu waliofanikiwa kiubunifu na kimaisha kupitia vipaji vyao – vilivyoendelezwa.

Tatizo tulilonalo katika nchi yetu, Tanzania, ni ushiriki mdogo wa wazazi kwenye maendeleo ya watoto wao walio na vipaji; yaani kushindwa kuvibaini, kuvikuza na kuvibadilisha kuwa pesa.

Tunao watoto wengi tu wenye vipaji, lakini ni wazazi wangapi  wanaojishughulisha kujua mtoto wake anapendelea nini kama ishara ya kipaji alicho nacho?

Na katika eneo la taaluma je, ni wazazi wangapi wanaofuatilia kujua mtoto wake anamudu au hamudu zaidi masomo gani ili ajipange kutoa ushauri au msaada?

Mzazi kuwa na taarifa hizi ni jambo muhimu kwani zinakusaidia kujua ni kwa namna gani umsaidie mwanao, kwa kushirikiana na walimu, ili kumpatia mtoto uelekeo ulio sahihi katika maisha yake.

Ikigundulika kuwa mtoto wako ni mzuri upande wa kipaji fulani, mfano kuchora, mzazi na mwalimu mna wajibu wa kumsaidia mtoto huyu kukinoa kipaji hiki – badala ya kulazimisha mtoto asome taaluma asiyoipenda.

Kuna tabia inayofanywa na wazazi wengi tu ya kumlazimisha mtoto kusomea fani ambayo ni chaguo la mzazi. Wapo wazazi eti kwa kuwa yeye amesomea fani ya uhandisi, kwa mfano, basi atashinikiza mtoto wake asome sana hisabati, ili naye aje asomee uhandisi.

Huenda mtoto huyu ana kipaji cha uigizaji, uandishi vitabu au ubunifu mitindo, na mwenyewe anakipenda kipaji chake; kitendo cha mzazi kumlazimisha kufanya kitu asichokipenda kina madhara makubwa.

Mtoto aliyelazimishiwa fani asiyoitaka anaweza kufaulu na hatimaye akaajiriwa katika kazi hiyo. Lakini atakapokuwa ndani ya ajira hiyo ufanisi wake utakuwa wa kiwango cha chini.

Huyu atafanya kazi kinyonge, na atakosa ubunifu kwa sababu kazi aifanyayo haina msukumo kutoka ndani.

Na ikitokea mtoto huyu akakosa kuajiriwa haitakuwa rahisi kwake kujiajiri mwenyewe kwa sababu ya kukosa hamasa na ubunifu kupitia fani aliyolazimishwa kuisomea.

Kijana mwenye kipaji halafu akasaidiwa kukikuza na kukinoa, huyu hawezi kukosa ajira. Kwa upande mmoja anaweza kuwavutia watu, kwa kipaji chake, na wakaamua kumwajiri katika kampuni zao.

Kwa upande mwingine mtoto mwenye kipaji ana uwezo mkubwa wa kukitumia kipaji chake kujiajiri yeye mwenyewe – akajipatia kipato na kupiga hatua kubwa kimaendeleo.

Mfano mzuri wa hili ni mchoraji mahiri wa katuni, Masoud Kipanya.

Hatua ya kuchukua: mzazi usilazimishe mwanao aelekee upande wako kitaaluma wala kiujuzi. Msaidie kukijua kipaji chake, kisha msaidie kukinoa na kukibadilisha kuwa pesa.  

Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasirimali kivitendo.

Anapatikana kwa e-mail: nzyy2001@gmail.com; Simu 0718219530

Takwimu hizi kuhusu kustaafu zitakufumbua macho!

Habari,

Wafanyakazi wengi hutumia pengine zaidi ya nusu ya maisha yao, wakiwa katika ajira. Kutokana na hili, wengi hujikuta katika mshikamano mkubwa sana na kazi zao, kiasi cha wengine kusahau hata mambo yao binafsi, au kwamba iko siku watastaafu. Na kwa kuwa huutumia muda mwingi sana katika majukumu ya ajira zao, wakati wa kustaafu ukiwadia mara nyingi huwaacha wakiwa katika mazingira magumu. Wengi wao huwa kama wameshtukizwa hivi; kitu ambacho kuwaachia hofu na taharuki.

Kwa hiyo, kuyafahamu mapema, baadhi ya mambo yaliyopo au yajayo inasaidia sana katika kufanya maandalizi ya kuyapokea mambo hayo, au athari zake; pale yatakapotokea. Kwa muktadha huu, kuna takwimu hapa ambazo pamoja na kwamba zinaihusu zaidi Marekani, lakini zinaweza kuwa na manufaa hata kwetu. Matumizi ya takwimu za wengine husaidia pia kuwachochea watafiti wetu kupata pa kuanzia ili kuja na takwimu zetu.

Kwa mujibu wa tafiti kadhaa, ni asilimia 58 tu ya Wamarekani ambao wamejijengea tabia ya kuweka akiba kwa ajili ya maisha baada ya kustaafu. Kwa maana hiyo, asilimia 42 ya Wamarekani hawana mpango huo. Na sababu kubwa wanayoitoa ni kwamba fedha (mshahara) hautoshi hata kwa matumizi ya muhimu, sembuse kuweka akiba. Hata hivyo, wapo wanaodai kwamba jambo hilo (kuweka akiba) halina umuhimu sana kwao. Na hawa ndio wale, ambao wakistaafu hutegemea zaidi kuanza maisha yao mapya kwa pensheni peke zao tu; wengi wao wakiwa hawajajiandaa vya kutosha kwa maisha hayo, na hivyo hujutia baadaye, jinsi uzee unavyozidi kukomaa.

Upo utafiti pia uliofanywa Marekani, unaoonesha kwamba, kwa wale ambao wanaweka akiba ni asilimia 10 tu, ambao huweka akiba inayozidi asilimia 15 ya mapato yao ya kila mwezi; kwa ajili ya maandalizi ya kustaafu. Hii ina maana kwamba asilimia 90 ya Wamarekani huweka akiba chini ya asilimia 15 ya mapato yao. Naomba hapa kutumia mfano wa gharama za Tanzania kufafanua hili.

Yaani katika kundi hili; ina maana wafanyakazi wanaopata shilingi 1,000,000/-,wengi wao (asilimia 90) huweka akiba isiyozidi shilingi 150,000/- kwa mwezi. Hapa ina maana kwamba, wapo wanaohifadhi mpaka shilingi 10,000/- au chini ya hapo, kwa mwezi. Na kwa mtazamo wao, hiki ni kiasi kisichokidhi haja, linapokuja suala muhimu la kustaafu. Kwa takwimu hii tunaweza kujifunza kitu; kwamba ili tuweze kujiandaa vizuri kwa maisha ya kustaafu, kwanza tujijengee tabia ya kuweka akiba, lakini pia akiba hiyo iwe kiasi cha kutosha kwa kufanikisha maandalizi hayo muhimu.

Utafiti mwingine unaonesha kuwa Wamarekani kati ya asilimia 60 na 70, wamepata maarifa na mbinu za kustaafu kupitia njia ya mdomo pekee. Hii ina maana kwamba asilimia kubwa ya Wamarekani wanategemea zaidi mazungumzo yasiyo rasmi au marafiki, wengi wao wakiwa sio wataalamu wa masuala hayo; kwa ajili ya kupata maarifa au taarifa hizo. Hii inatuonesha umuhimu wa kuandaa mafunzo maalum, yaliyo rasmi kwa ajili ya wastaafu, ambayo yatatolewa pia na watu waliobobea katika fani hii, ili wastaafu wafundishwe ukweli wa mambo na uhalisia wa maisha ya kustaafu.

Kuna utafiti pia, unaosema kwamba asilimia kubwa tu, ya vijana (millenials) wa Marekani, ambao wanaishi kwa madeni yanayofikia dola 30,000 kwa mwezi (nje ya kodi na michango mingine ya kisheria); ilhali kipato (mshahara) chao ni dola 55,000 kwa mwezi. Nikitumia uwiano huo, naomba nitoe mfano wa Mtanzania, anayepokea shilingi 1,000,000/- kwa mwezi. Ukitoa madeni, ukatoa kodi, halafu ukatoa michango mingine ya kisheria; kijana huyu atapokea kama asilimia 30 tu, ya mshahara wake; yaani shilingi 300,000/- kwa mwezi.

Kwa mujibu wa utafiti huu, mengi ya madeni haya ya vijana ni fedha zilizokopwa kwa ajili ya kununua magari, sofa na fenicha za nyumbani, matembezi (trips), kununua mavazi na ‘simu kali’, na matanuzi; ingawa wapo wachache waliokopa kwa ajili ya kujiendeleza kielimu, na ujenzi wa nyumba. Kwa hiyo, bila kujali fedha imekopwa kwa ajili gani, kilicho muhimu hapa ni kwamba, kiasi cha fedha kinachobaki ni kidogo sana kumudu maisha ya kawaida kwa mwezi. Kwa kiasi hiki, sio rahisi kujiwekea akiba, hasa kwa maandalizi ya kustaafu.

Kwa mujibu wa utafiti uliofanyika mwaka 2020, nchini Marekani, kuhusu utayari wa wafanyakazi kustaafu; asilimia 73 ya wafanyakazi waliohojiwa walidai kwamba wakisikia suala la kustaafu hufadhaika. Kwa hiyo ni asilimia 27 tu ndio walioonesha kujiamini. Kuhusu suala hili hili, kuna utafiti ulioonesha kwamba asilimia takriban 60 ya Wamarekani waliohojiwa kuhusu suala la kustaafu, walisema suala hili huwakosesha usingizi, wanapolisikia.

Upo utafiti mwingine unaoonesha kwamba asilimia 70 ya Wamarekani waliohojiwa walisema kwamba wangependa kuwa na kitu cha kufanya (shughuli mbadala) baada ya kustaafu. Hii inaonesha kwamba, ukistaafu kinachobadilika ni aina ya kazi tu, lakini suala la kufanya kazi linabaki! Hata hivyo, asilimia 60 ya waliohojiwa walisema kwamba wakistaafu wangeanzisha aina ya shughuli iliyo tofauti na ile waliyokuwa wakifanya kabla, ambayo pia ni nyepesi.

Ukifuatilia takwimu hizi utaona kwamba maandalizi kwa ajili ya maisha ya kustaafu ni muhimu sana. Maandalizi yana nafasi kubwa ya kuwaondolea wafanyakazi hofu, wanaposikia suala la kustaafu. Hii ni hofu ya maisha nje ya ajira waliyoizoea. Wapo wengine wasio na maarifa juu ya mtindo gani wa maisha waishi sasa (kazini), ili maisha yao uzeeni yaendelee kunawiri. Kwa sababu hii ndio maana kuna haja kubwa kwa wafanyakazi kupatiwa maarifa kwa ajili ya kustaafu ili wajenge weledi na kujiamini, wakijiandaa kustaafu.

Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasirimali kivitendo. Anapatikana kwa e-mail: nzyy2001@gmail.com; Simu 0718219530

Ukijiandaa kustaafu tumia historia hii kujifunza ujasiriamali

Habari rafiki,

Ni kupitia ubunifu wazee hawa wa zamani waliweza kukabiliana na changamoto zilizowakabili

Hivi karibuni, serikali imepandisha kiwango cha kukokotoa mafao ya wastaafu hadi asilimia 33 kutoka asilimia 25. Wapo waliofurahia hatua hii, ingawa wapo pia wanaodai kiwango hiki bado hakiwawezeshi kupata kiinua mgongo kinachokidhi gharama za kuanzia maisha ya kustaafu. Wasiofurahia wanataka kiwango cha asilimia 50, kama zamani, au hata zaidi ya hapo.

Mstaafu mmoja anasema, “kwa mshahara wangu, nikistaafu natarajia kulipwa shilingi milioni 43 tu, kama kiinua mgongo. Na kwa kuwa sijajenga, sina mradi hapa ninapoishi, na nimepanga kurudi kwetu nikistaafu; fedha hiyo haitoshi kuanzia maisha hayo. Na ni wazi kwamba haitanifikisha popote.”

Kwa kigezo hiki peke yake, unapata picha kwamba wastaafu wanatakiwa kujiandaa, au kuandaliwa, ili wajipatie maarifa ya ubunifu wa miradi mapema sana, katika safari yao ya maisha. Hii itawafanya wawe na uwezo wa kubuni na kusimamia miradi yao wakiwa bado kazini, ili wakistaafu na kulipwa kiasi hicho kidogo, basi angalau wakitumie kuendeleza miradi yao, kuliko kuanzia sifuri.

Wafanyakazi wakipatiwa maarifa ya ubunifu, wanaweza kujijengea uwezo wa kufikiri na kutenda kijasiriamali; ikizingatiwa kwamba ubunifu na ujasiriamali ni chanda na pete! Na kwa kuwa tunaweza kujifunza ubunifu kupitia historia, naomba basi tujikumbushe kidogo historia ya ‘zama za mawe’.

Ki-ukweli, ubunifu ulianza toka enzi za mababu zetu. Binadamu, kila alipokabiliwa na changamoto, aliufikirisha ubongo wake na kujenga maono yaliyomletea taswira ndani ya akili yake, ya mchakato au vitu ambavyo alikuja kuvifanya hatimaye; vikamtoa katika hali ya uduni, na kumweka katika hali bora ya maisha.

Kila kitu walichokiona wazee wale, walikifanyia udadisi kisha wakavuta taswira, akilini, kujua ni jinsi gani kitu hicho kinaweza kutumika katika kutatua changamoto au matatizo yao.

Hawakuwa na udadisi tu, bali pia uthubutu wa kubadili taswira walizozijenga vichwani mwao kuwa vitu halisi. Ubunifu, hasa katika muktadha wa karne ya 21, unahusisha utengenezaji wa bidhaa, utoaji wa huduma au uboreshaji wa michakato ya uzalishaji na utoaji huduma – kwa utaratibu mpya, wenye lengo la kujiongezea thamani.

Kihistoria, tunaambiwa kuwa binaadamu walianza kubuni vifaa duni; lakini waliendelea kudadisi na kujifunza zaidi kwa lengo la kuboresha. Historia ya ubunifu na ugunduzi enzi hizo imegawanyika katika zama kadhaa kama ifuatavyo:

Moja, zama za kale za mawe. Tunaambiwa kuwa hizi zilikuwa zama za uwindaji na ukusanyaji, hasa vyakula, ambapo mwanadamu alitumia zana ghafi za mawe; yaani mawe yalitumiwa kama yalivyo kwa ajili ya kuulia wanyama, kukatia miti, kuchunia ngozi za wanyama, na kuchimbia vyakula vya mizizi.

Ubunifu wa mwanaadamu hapa ni yale maarifa ya kutumia vifaa hivyo duni kupata matokeo yenye tija zaidi, badala ya kutumia mikono mitupu, miguu au meno. Katika zama hizi binaadamu walikula vyakula vibichi, kwani hakukuwa na moto.

Mbili, zama za kati za mawe. Hapa, binaadamu aliishi kwa kuwinda na kukusanya pia. Lakini alianza kufikiri zaidi na kufanya ubunifu. Alifikiri na kugundua kuwa anaweza kuyakarabati mawe yakawa na umbo tofauti kwa malengo maalumu. Hivyo, ubunifu huu uliibua vifaa kama visu, sindano, mikuki na pinde. Vifaa hivi vilirahisisha ukataji wa nyama, uchongaji wa miti na uchunaji wa ngozi.

Ni katika zama hizi pia ambapo moto uligunduliwa na kumfanya binaadamu aanze kula chakula kilichopikwa au kuchomwa, aishi maeneo yenye baridi, afanye kazi hadi usiku, na aweze pia kusafisha maeneo, kwa moto, kwa ajili ya shughuli zake mbalimbali.

Kwa hiyo, katika kipindi hiki, mbali na ubunifu wa kutengeneza vifaa vya mawe; mfano mikuki na visu, lakini vilevile wazee hawa walifikiri tena na kugundua kwamba ili vifaa hivi viwe na ufanisi zaidi, waongeze ubunifu kwa kuvifanya viwe rahisi kubebeka (vidogo); rahisi kuua, kuchuna, au kukata (vikali); na rahisi kutumia (vyepesi).

Tatu, zama za mwisho za mawe. Hapa binaadamu aliweza kubuni na kutengeneza vifaa bora zaidi. Ubunifu wake ulikuwa wa juu zaidi ambapo aliweza kubuni na kuchonga vifaa vidogo zaidi kwa umbo, vyepesi kubeba, vikali zaidi, na vyenye maumbo tofauti kwa kazi tofauti.

Hivi ni vifaa kama mashoka, mikuki myepesi na mikali, na visu vikali na vyepesi zaidi, nakadhalika; vyote vikiwa vya mawe. Lakini pia, hamu ya kupata vifaa bora zaidi ilisababisha waende mbele zaidi ki-ubunifu kwa kuanza kuvichonga vifaa vya mawe na kuviunganisha kwenye vifaa vya miti, ili kuviongezea tija. Na huu ndio ukawa mwanzo wa ugunduzi wa kilimo, kwani vifaa hivi vilitumika kuparuria ardhi na kupandia mbegu ili kujipatia mazao.

Nne, zama za chuma. Hapa binaadamu aliufikirisha ubongo wake zaidi, akaja na mbinu za ziada. Alipata ujuzi wa kufua vyuma, kwa msaada wa moto, ambapo alifua mashoka, majembe, mikuki, sululu, nakadhalika; vyote vya chuma. Vifaa hivi viliwaongezea tija katika uzalishaji, hivyo wakaweza kuzalisha chakula kingi zaidi kwa matumizi yao.

Cha kujifunza hapa ni kwamba ubunifu ni kichocheo kikubwa cha maendeleo ya binaadamu. Ubunifu uliofanyika enzi za mababu zetu ulilenga kupata vifaa bora na vyenye tija zaidi, kupambana na changamoto, na hivyo kurahisisha maisha yao. Walifanikiwa kwa kiwango cha kutosha.

Sisi, jamii ya kileo, tunapaswa kuzijua jitihada zilizofanywa na mababu zetu, enzi hizo. Kipindi ambacho hakukuwa na taasisi maalumu za kielimu, lakini wazee wale walimudu kufikiri, kujifunza na kufanya vitu.

Kwa hiyo, wewe mstaafu mtarajiwa, ukiongozwa na historia hii, na kwa kuzingatia kiwango kiduchu cha malipo ya mafao utakayolipwa, ni muhimu ukajifunza, mapema, kufikiri na kuibua miradi binafsi ili kujiandaa kwa maisha ya kustaafu. Uzoefu wa kufanya mambo binafsi, ukiwa kazini, ndio chachu ya mafanikio katika maisha ya uzeeni. Jipange!

Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasirimali kivitendo. Anapatikana kwa e-mail: nzyy2001@gmail.com; Simu 0718219530

Elimu Hii Huwezi Kuipata Ndani Ya Darasa – 2

Habari rafiki,

Unaweza kufeli masomo darasani lakini ukiwa na mbinu za maisha nje ya darasa utatoboa tu!

Nimejadili kupitia makala iliyopita, kuwa elimu ya darasani katika dunia ya leo ni kitu muhimu sana, na kila mtu anapaswa kuipata. Na kwamba watu hutafuta kuelimika kupitia shule ili kurahisisha jitihada zao za kufaulu katika miasha, na hasa maisha ya kuajiriwa.

Kwa sababu hii, wanafunzi hujitahidi kusoma kwa bidii darasani ili wapate alama za juu, wawe wanafunzi bora, ili mwishowe wafanikiwe kupata kazi, na hasa kitu kiitwacho ajira. Na kwa sababu hii ndio maana wapo wanaoikosoa elimu hii. Wanasema kwa kiwango kikubwa, elimu hii haimuandai mwanafunzi kujenga upeo mkubwa wa kufikiri, kujitegemea, na kupambana ili apate mafanikio binafsi katika maisha yake.

Wanaema, elimu hii humuandaa mwanafunzi kupokea maelekezo maalum na kuyakariri, kisha kuyatumia kama yalivyo – katika ajira yake ya mshahara; basi! Na ataendelea hivyo hadi anapostaafu. Nimejadili sababu au vitu viwili katika makala iliyopita; vinavyohitajika katika maisha halisia, nje ya darasa, ili watu wavielewe na kuvitumia katika kupambana.

Katika sehemu hii ya pili nitajadili sababu nyingine nne zinazowafanya wengi wa vijana, tena wenye uwezo mkubwa darasani, kushindwa kuhimili maisha binafsi ya kujitegemea na kujikimu, baada ya shule, wakaishia kuzurura kutwa na vyeti, wakisaka ajira, pengine bila mafanikio.

Moja, shule zinahimiza mashindano, wakati maisha halisia ni matokeo ya ushirikiano.

Maisha ya shule ni ushindani mtupu. Kila wakati mtoto anataka apate maksi za juu kuliko wenzake. Wapo watoto ambao akiwa na kitabu au ‘notes’ zenye maelezo mazuri ya somo fulani hawezi kuwaazima wenzake. Kisa? – Anaogopa watamzidi! Katika dunia halisia maisha ni ushirikiano. Ukishindwa kutengeneza mshikamano na watu, maisha yako yatadoda; hasa wenye maono kama yako.

Mbili, shule ina walimu wapole, na wanaojali; wakati maisha halisia yana walimu wanoko!

Shuleni walimu wanafundisha kwa umakini, kwa utaratibu mzuri na kwa kutumia mbinu zinazompatia mwanafunzi mazingira mazuri ya kujifunza na kuelewa. Maisha halisia ni msitu mnene wenye wanyama wakali! Hapa hupati vitu ki-urahisi. Usipopambana unapigwa chini! Katika kupambana kuna mambo mengi. Utaanguka, utalia, utasota, utasononeka na unaweza kufeli vilevile. Katika maisha halisia unatakiwa kuwa tayari kuingia kuzimu kabla hujaingia peponi.

Tatu, shule zinatoa mafunzo kabla ya mtihani wakati maisha halisia hutoa mtihani kabla ya mafunzo.

Shuleni mwalimu anafundisha, anafafanua somo husika na kutoa muda wa kujiandaa kabla hajatoa mtihani. Hii ni njia rahisi ya kujifunza. Katika maisha halisia utakutana na majaribio (test) na mitihani mingi na ya kila aina. Kabla ya kupata mafunzo unapambana na mazingira magumu yenye changamoto kibao, ikiwapo ya kufeli.

Hii ni njia ngumu ya kujifunza – lakini ni njia nzuri zaidi kwa kuwa inatanguliza mateso na maumivu yanayokufanya uongeze umakini na usibweteke – na hapa ndipo somo lililokusudiwa hupenya kikamilifu.

Nne, shule inafundisha utii wakati maisha yanafundisha uasi na ukaidi. Shule zinawapa wanafunzi kanuni za kufuata. Wanapewa miongozo, taratibu na hata kanuni (formula) za masomo kama hisabati, fizikia na uchumi. Shule zina ratiba – saa ya kuingia darasani, saa ya kupumzika, saa ya kuondoka, sare za kuvaa nakadhalika.

Hivyo kila siku wanafunzi wanahimizwa utii. Ukiwa mkaidi unaadhibiwa na hata kufukuzwa shule. Kwa hiyo kuepuka hayo unalazimika kufuata sheria zote. Katika maisha halisia mafanikio yanakwenda kwa vijana ‘waasi’ na ‘wakaidi’. Hawa ni watu wasiopenda kufuata taratibu au sheria zilizowekwa. Hawa hupenda kusonga mbele huku wameelekea upepo unakotoka, wakiwa wanapambana nao.

Wakati fulani unahitaji ukaidi kufanikiwa katika maisha. Ukweli ni kwamba, vitu vinavyoonekana vya kawaida kwa wengi siyo lazima viwe sahihi. Ni ukaidi na uasi ndio humfanya mtu kuona, kuamini na kufanya kitu kilicho kinyume na taratibu zilizozoeleka.

Watu hawa, wana uwezo wa kutengeneza njia katikati ya majabari, matope na miiba. Mahali ambapo wengine wote wanaona hapawezekani kupitika, wao huiona njia, wakaisafisha na kuanzisha safari.

Kwa hiyo, kwa kuwa tumeona mapungufu katika elimu ya darasani na kwamba haimuandai kwa ukamilifu mwanafunzi kujenga upeo mkubwa wa kufikiri na kujitegemea, ni wakati sasa wa kujiongeza, kwa kumpatia mbinu za ziada, za kuelimika kupitia elimu ya maisha halisia, na jinsi ya kuzitumia kwa ajili ya mustakabali wa maisha yake.

 Makala haya yameandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasirimali kivitendo. Anapatikana kwa simu: 0718219530; e-mail: nzyy2001@gmail.com

Elimu Hii Huwezi Kuipata Ndani Ya Darasa.

Yapo mengi ya kujifunza katika mazingira yaliyo nje ya darasa….

Habari rafiki

Elimu ya darasani katika dunia ya leo ni kitu muhimu sana, na kila mtu anapaswa kuipata. Elimu hii inampatia mwanafunzi maarifa muhimu ya kusoma, kuandika na kuhesabu. Elimu hii inatoa pia maarifa katika fani mbalimbali kama sayansi, uchumi, siasa, biashara n.k.

Watu hutafuta kuelimika kupitia shule ili kurahisisha jitihada zao za kufaulu katika miasha, na hasa maisha ya kuajiriwa; ndio maana wakimaliza shule tu, vijana huanza kutafuta kazi!

Kwa sababu hii, wanafunzi hujitahidi kusoma kwa bidii darasani ili wapate alama za juu, wawe wanafunzi bora, ili mwishowe wafanikiwe kupata kazi. Wanafunzi wazuri sana darasani huitwa ‘vipanga’, na wale wasiojiweza huitwa ‘vilaza’, kama utani hivi!

Sasa kuna dhana iliyojengeka kuwa ukiwa ‘kipanga’ darasani basi tayari umeshajijengea msingi wa mafanikio katika maisha. Je kuna ukweli katika hili? Watafiti wana hoja tofauti. Wao baada ya uchunguzi wamegundua kuwa kwa kiwango kikubwa ‘vipanga’ darasani huishia kufeli katika maisha ya uhalisia.

Wanasema kwamba maisha halisia huongozwa na kujituma, kujitegemea na kupata rikizi kupitia fikra na jitihada binafsi. Na kwamba ‘Vipanga’ wanaoonekana kufanikiwa, huwa wamebebwa tu na taasisi wanazofanyia kazi, zinazowalipa ujira mkubwa na marupurupu mengi; ingawa wapo wengine wanaofanikiwa kupitia njia haramu.

Ukweli mchungu ni kwamba kwa kiwango kikubwa, elimu ya darasani haimuandai mwanafunzi kujenga upeo mkubwa wa kufikiri, kujitegemea, na kupambana ili apate mafanikio binafsi katika maisha yake.

Elimu hii humuandaa mwanafunzi kupokea maelekezo maalum, kuyakariri na kuwa tayari kuyatumia kama yalivyo – katika eneo la kazi analopangiwa; na akisha fanya hivi analipwa ujira wake na kuendesha maisha hadi anapostaafu.

Katika makala haya nitajadili vitu vinavyohitajika katika maisha halisia, nje ya darasa, ili watu wavielewe na kujifunza, na wavitumie kama nyenzo za kuwawezesha kupambana na kujitegemea katika maisha.

Nitaonesha tofauti ya elimu kama inavyotolewa darasani na elimu inayopaswa kutolewa ili kumfanya mtu aweze kujitambua, kupambana na kufanya vizuri katika maisha halisia.

Na ukweli, hizi ndizo sababu hasa zinazowafanya ‘vipanga’ darasani kushindwa kuhimili maisha binafsi ya kujitegemea – wakaishia kuishi kwa kuwatumikia wengine kwa maisha yao yote. Hii ni sehemu ya kwanza ya makala haya ambapo nitaanza kwa kujadili sababu mbili; na katika sehemu ya pili nitajadili sababu tano.

Moja, shule zinahimiza wanafunzi wasifeli, wakati kiuhalisia maisha yanachochewa na matokeo ya kufeli.

Nilisoma na kijana mmoja aliyekuwa na uwezo sana darasani. Huyu, akipata chini ya maksi 90, alikuwa anaugua! Na hakuwa peke yake; yaani kupata maksi 85 kwa mfano, ni kufeli! Wanafunzi wazuri hawapendi kufeli, na ikitokea wakafeli huchukia sana.

Hata hivyo, kiuhalisia katika maisha ya kawaida, kufeli ni chachu ya mafanikio. Kufeli ni kichocheo. Watu wenye upeo mpana wa elimu ya maisha hukumbatia kufeli. Watu hawa ni shupavu katika kujaribu vitu hata kama hawana uhakika wa kufaulu. Na ikitokea wakafeli hawachukii wala hawakondi, bali hutabasamu tu huku wakitafakari kwa nini wamefeli.

Hali hii kuwapa faraja na fursa ya kujipima ili kujua walipojikwaa. Kisha huanza upya huku wakijiepusha na uwezekeno wa kurudia makosa ya nyuma. Hivyo kufeli kwa watu hawa ndio siri hasa ya mafanikio yao katika maisha.

Mbili, shule inawapa wanafunzi ramani au dira; wakati maisha yanawaacha wahangaike wenyewe.

Shuleni unahimizwa usome kwa bidii, upate gredi nzuri ili upate kazi nzuri kisha ulipwe mshahara mzuri; na ukistaafu ulipwe mafao mazuri ya uzeeni hadi kifo chako. Kwa hiyo, shule anakupatia mwongozo wa kufuata, na ukiweza kuufuata kwa umakini unapata matokeo yanayofahamika yanayokufanya uishi vizuri baada ya hapo kwa msaada wa mwajiri wako.

Kwa bahati mbaya maisha halisia hayana ramani wala mwongozo. Wale wanaofuata ramani mara nyingi hawapati mafanikio. Mafanikio huenda kwa watu wasiofuata ramani. Hawa ni wale wanaojitambua na kujua wanataka nini katika njia ya mafanikio. Hawaongozwi na ramani kwa sababu ramani ina kawaida ya kuwapeleka watu kule ambako kila mtu anakwenda.

Ramani inatabirika na ndiyo maana kila mtu anaifuata. Na kwa vile kila mtu anaifuata njia hiyo inakuwa nyembamba, yenye mbanano inayowafanya wengi wao wakose hewa na kuishia njiani. Ili ufanikiwe katika maisha halisia unapaswa kujitambua, kujiamini na kuwa tayari kutimiza ndoto zako bila kulazimika kupita katika njia zilizopo zinazotabirika.

Jitokeze, fuata ndoto zako bila kujali kama utafanikiwa au la; na amini kuwa jinsi unavyofuata maelekezo ya ndoto zako ndivyo unavyozidi kuunganisha nukta zinazokupeleka katika mafanikio. Kwa leo niishie hapa, usikose sehemu ya pili, tujadili zaidi…

Hatua ya kuchukua: Kwa kuwa ni ukweli mchungu kwamba elimu ya darasani haimuandai mwanafunzi kujenga upeo mkubwa wa kufikiri na kujitegemea, inatupasa sasa kuikumbatia elimu ya maisha halisia ambayo itakupatia mbinu bora za kupata mafanikio halisia.

Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasirimali kivitendo. Anapatikana kwa simu: 0718219530; e-mail: nzyy2001@gmail.com

Tumia Mbinu Hizi Kufanya Ubunifu Katika Ujasiriamali

Ubunifu sio tukio bali mchakato unaohusisha nyanja nyingi….

Habari rafiki.

Nimeshaeleza kupitia makala zangu kadhaa, kuwa ubunifu ni uwezo wa kufikiri, kutafuta majibu na kutatua changamoto kwa namna ya kipekee; na kwamba ubunifu ni matokeo ya kuufikirisha ubongo ili kupata njia mpya na nzuri zaidi za kutatua changamoto au tatizo lililobainika. Nimeeleza pia kuwa ubunifu una nafasi kubwa katika ujasiriamali.

Ubunifu sio kitu rahisi ‘ki-vile’; yaani eti kila wakati uibuke na bidhaa mpya yenye utofauti, au huduma mpya, au mchakato mpya wa uzalishaji au utoaji huduma. La hasha! Hata hivyo, siyo kitu kigumu! Panahitajika maarifa tu. Yaani ujue mbinu ipi itakupatia mawazo mapya na ya maana ya kibunifu kuweza kukuletea tija katika biashara au shughuli yako.

Zifuatazo ni baadhi ya mbinu ambazo ukizitumia zitakusaidia kuongeza uwezo wako wa ubunifu:

Kwanza, Kukopi au kuiga mawazo ya wengine. Hii ni njia rahisi kabisa ya ubunifu. Hapa ni kwamba unaiga kitu ambacho wengine walishakifanya hapo kabla. Kuiga huku haina maana ya kukopi na ku-paste, hapana! Hapa ninamaanisha kwamba unachunguza kitu kizuri kilichofanyika mahala fulani, halafu unakiboresha kidogo, kisha unakizalisha na kukitumia kwako. Kuiga huku tunaita ‘kuiga kimkakati’, ambayo ni mbinu nzuri ya kufanya ubunifu.

Kwa mfano, Henry Ford, mwanzilishi wa Kampuni ya magari ya Ford, alitembelea kiwanda kimoja cha kusindika nyama, Marekani, akaona mtiririko wa utendaji kazi  na mpangilio wa mashine na wafanyakazi katika mnyororo mmoja, mtindo unaoitwa ‘assembly line production system’. Akavutiwa na ubora, uharaka, na unafuu wa gharama za uzalishaji kwa kutumia mtindo huu.

Aliporudi kwake, akatumia maarifa hayo kwenye kiwanda chake cha magari, kisha akaongeza ujuzi wake kidogo; akafanikiwa kupunguza muda na gharama kwa kiwango kikubwa. Huu ni ubunifu wenye tija unaotokana na kuiga.

Pili, kuuliza wateja wako. Ukiweka utaratibu wa kuwauliza wateja wako kwamba wangependa bidhaa au huduma zako ziweje, utapata mawazo mengi sana, ambayo ukiyachuja, unaweza kuyatumia kuboresha bidhaa au huduma zako.

Kwa mfano, wateja wanaweza kuuliza au kutaka vitu, urembo au madoido fulani yawepo katika bidhaa yako. Au wakataka uweke vitu fulani vitakavyoifanya bidhaa yako iwe rahisi kutumia, au yenye mvuto zaidi; kwa mfano, mpangilio wa rangi, harufu au ulaini wa kitambaa au bidhaa husika.

Hapa unatakiwa usikilize maoni yao kwa umakini uone ni maoni yapi ukiyafanyia kazi unaweza kuongeza ubora wa bidhaa yako na ukaongeza mauzo zaidi.

Tatu, wachunguze wateja wako. Usiishie tu kuwauliza, wachunguze pia! Angalia wanatumiaje bidhaa zako, au ni vitu gani wanavibadilisha wakishanunua bidhaa yako. Fanyia kazi majibu ya uchunguzi wako.

Hivi ndivyo mmiliki wa Kampuni ya nguo ya Marekani, Levi Strauss, alivyofanya baada ya wateja wake wa Jeans kuwa wanazichana Jeans zao sehemu fulanifulani. Alipoona hilo, haraka sana akaanza kutengeneza Jeans zilizochanywa, na mauzo yake yakapaa!

Nne, fuatilia malalamiko na changamoto za wateja. Sio wateja wote wanalalamikia bidhaa au huduma unazowapatia. Hivyo ukipata wanaolalamika usiwachukie, shukuru, na wasikilize kwa makini. Sikiliza, pia fumbua macho, uone matatizo au changamoto wanazolalamikia. Hapa utapata pa kuanzia kufanya ubunifu, na ukiweza kufanikiwa kuondoa changamoto hizo utaongeza imani ya wateja wako, wataona jinsi unavyowajali, na mauzo yatapanda sana.

Tano, unganisha au changanya bidhaa. Kuchanganya bidhaa moja na nyingine ni mbinu ya kuja na bidhaa mpya na yenye matumizi bora zaidi. Kwa mfano, simu za mwanzo za mkononi hazikuwa na kamera wala radio.

Hivyo, wabunifu katika Makampuni ya simu waliwaza na kuona uwezekano wa kuzalisha bidhaa moja yenye nyongeza ya vitu hivyo, ndipo wakaunganisha vitu hivyo na kuja na simu yenye kamera na radio. Na sasa vitu vingi zaidi vimeongezwa.

Ubunifu mwingine ni wa kuunganisha redio, cassete, mp3 au flash player, kupata bidhaa moja yenye upana zaidi wa matumizi. Uvumbuzi huu umewawezesha kuongeza thamani ya bidhaa hizo na  kuongeza mauzo pia.

Sita, punguza vitu kwenye bidhaa zako. Katika hili, jiulize, ni vitu gani ukiviondoa kwenye bidhaa, mchakato au njia za usambazaji wa bidhaa yako, itafanya bidhaa hiyo ipate ubora zaidi. Kwa mfano, Amazon waliamua kuondoa uuzaji wa vitabu kwa kutumia maduka halisi ya kuuza vitabu. Wakabakiza uuzaji vitabu kwa mtandao, online retailing.

Mfano mwingine ni uamuzi wa kuondoa mwamba wa mbele, au kiti cha kubebea mizigo, kwenye baiskeli. Kumbuka wasichana wengi, hasa warembo wa mjini, hawapendi baiskeli zenye mwamba au zenye kiti cha nyuma,wakitaka kuendesha baiskeli. Kwa kuviondoa vitu hivi utajikuta unaongeza mauzo yako kwa kiwango cha juu.

Saba, angalia washindani wako. Waangalie kwa umakini washindani wako. Unaona wanafanya nini? Kipi kipya wanachokuja nacho? Una kitu cha kujifunza? Unaweza kuiga kimkakati? Unaweza kuboresha ukaja na kitu kipya na bora zaidi? Basi fanya hivyo.

Nane, geuza bidhaa za kizamani kuwa za kileo. Angalia huduma, mchakato au bidhaa iliyokuwa inatumika zamani, ambayo inaonekana imepitwa na wakati, kisha angalia jinsi unavyoweza kukirudisha kitu hicho au fasheni hiyo ya zamani, kwa kuifanyia mabadiliko fulani,  ikawa bidhaa ya kileo na itakayowapa vionjo vipya watumiaji wa kileo.

Kwa mfano, ‘Dungarees dress’ ni vazi lililokuwa likivaliwa katika mazingira ya shamba au gereji, lakini wabunifu wamelichukua, wakalifanyia ukarabati kidogo, wakalitangaza kupitia kwa wasichana warembo, na sasa linapendwa na linavaliwa na warembo karibu kila mahala.

Kwa kumalizia, ubunifu ni chachu kubwa ya ujasiriamali na hivyo ili kuongeza tija katika bidhaa au huduma zako huna budi kuwa na maarifa na mbinu. Yaani ujue mbinu ipi itakupatia mawazo mapya na ya maana ya kibunifu kuweza kukufanya utengeneze bidhaa au utoe huduma bora zaidi itakayokuletea tija katika biashara au shughuli yako.

Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasirimali kivitendo. Anapatikana kwa simu: 0718219530; e-mail: nzyy2001@gmail.com

Kustaafu: Tukio jema linalowaogofya wafanyakazi wengi!

Muda wa kustaafu ukikaribia, hisia kali hutawala akili za wafanyakazi

Katika historia ya maisha ya mfanyakazi, kustaafu kazi ni tukio mojawapo kubwa. Tukio hili humaanisha kumalizika kwa maisha ya kiutumishi ya mfanyakazi, na mwanzo wa maisha ya binafsi nje ya utumishi. Mara nyingi kustaafu kunaelezewa kama kuondoka kazini na kuingia ‘uraiani’, baada ya mfanyakazi kuitumia akili na nguvu zake kwa muda mrefu, kufanya uzalishaji kwa mwajiri; na kwa wengi ni baada ya kufikisha umri wa miaka 60. Kuna watu wanaoitazama dhana ya kustaafu kama kipindi cha mpito kutoka katika dunia ya majukumu au kazi ngumu kuingia katika dunia nyepesi, iliyo na mapumziko mengi.

Kwa wafanyakazi wengi, kazi (ajira) ni kitu kinachowapa uhakika wa kufikia kilele cha uhuru wao kifedha, kiuongozi, kujitegemea, na kujiweka katika jamii inayotoa ulinzi, unaomfanya kujiona kama sehemu ya kundi fulani kubwa. Kutokana na mambo haya, wafanyakazi wengi wamejikuta katika mshikamano mkubwa sana na kazi zao. Wamejikuta katika mazingira ya kubanwa mno na kazi, wengine hata kusahau mambo yao binafsi, kwa kuwa wanaona kazi ndio kila kitu katika kujihakikishia kipato na maisha yao kwa ujumla. Kwa hiyo utakuta watu hawa wanatumia muda mwingi sana katika majukumu ya ajira zao.

Kutokana na hilo, inaaminika kwamba kitu chochote kinachoweza kumtenganisha mfanyakazi huyu na kazi (ajira) yake; kitu hicho kina nafasi kubwa ya kumjengea mtu huyu hisia hasi dhidi ya kitu hicho. Na mfano mmojawapo mkubwa wa kitu hicho ni tukio la KUSTAAFU! Kustaafu huchukuliwa kama kitu au tukio baya linalompata mfanyakazi, na hivyo kumwondolea motisha au mshikamano uliokuwepo kati yake na kazi yake.

Tukio la kustaafu linapokuja, humlazimisha mfanyakazi kutengana na kitu (kazi) alichokizoea, na alichokuwa karibu nacho kwa miaka mingi, kama chanda na pete. Kumbuka wapo wanaoishi ndani ya ajira kwa miaka 38 au zaidi. Mfanyakazi anapostaafu hulazimika kutengana na kipato cha uhakika cha kila mwezi, mazingira na watu aliowazoea, taratibu zilizopangiliwa za utendaji kazi, na hadhi yake kwa wafanyakazi au kwa jamii inayomzunguka, inayotokana na nafasi aliyonayo kazini.

Hisia hasi inayojengeka kwa mfanyakazi kuhusu tukio la kustaafu linalomnyemelea  ndiyo kwa neno moja huitwa HOFU. Hii ni hofu ya kustaafu inayompata mfanyakazi aliyezoea, na kujenga fungamano zito, kati yake na kazi yake. Mfanyakazi huyu huanza kuona jinsi  anavyoweza kushindwa kuishi sawasawa nje ya mazoea aliyojijengea kwa miaka yote aliyokuwa ndani ya ajira. Na hili huanza kumtesa kisaikolojia!

Mwandishi J.C. Raymond, aliyefanya utafiti kuhusu hofu zinazowapata wafanyakazi wanaokaribia kustaafu, anaandika kwamba hofu ni hisia hasi zinazompata mtu anayefikiria au kutarajia kukumbwa na maafa au tukio baya. Hofu ni hali inayompata mtu, ikiwa ni mapokeo ya akili yake kuhusu tishio fulani linalomkabili; analolijua au hata asilolijua. Na mara nyingi hofu humkosesha mtu huyu amani na utulivu. Athari nyingine za hofu kwa tishio fulani(hasa la ghafla) ni ongezeko la mapigo ya moyo na  upumuaji, misuli kukakamaa, na pengine maumivu ya kichwa; ikiwa ni maandalizi ya mwili kukabiliana na tishio hilo.

Kwa mujibu wa mwandishi T.Y. Ode, baadhi ya vyanzo vya hofu ya kustaafu ni pamoja na: mazoea ya kuishi kwa mshahara tu, fikra za kutokuwa na kipato cha kutosha, hisia za kushindwa kuchangamana vyema na jamii mpya, hisia za kutokuwa na mipango ya maisha mapya, wasiwasi wa kutokuwa na nyumba binafsi ya kuishi, ukosefu wa maarifa wa kuyatumia mafao ya kustaafu, mzigo wa wategemezi, na wasiwasi juu ya staili mpya ya kuishi na ndugu na marafiki baada ya kustaafu.

Naye mwandishi Amadi Machima anasema kustaafu huambatana na matukio ya kupungua kwa kipato cha uhakika, mabadiliko ya hadhi katika ofisi na jamii, mabadiliko ya mtindo wa maisha, ongezeko la muda wa mapumziko, na ongezeko la uwezekano wa kushambuliwa na magonjwa; vitu ambavyo humtia mtu hofu. Kwa hiyo, kwa kuwa suala la kustaaafu huambatana na hofu, ndio maana kuna watu wanaona kwamba ni muhimu kuwafanyia wastaafu tarajiwa maandalizi maalum, ili waingie katika maisha ya kustaafu kwa mguu mzuri.

Machima anasema kipindi cha kustaafu huandamana na changamoto, bila kujali jinsi mstaafu alivyojiandaa . Moja ya changamoto hizo inatokana na ukweli kwamba wafanyakazi hupenda sana uhakika wa ajira zao (job security), ambayo hupotea mara tu wanapostaafu. Hii humfanya mfanyakazi kujikuta akipotea kutoka katika dunia inayotabirika, na kuingia katika dunia isiyotabirika. Hali hii pia huwa kichocheo cha hofu, na hasa kwa wafanyakazi waliokuwa na majina au vyeo vikubwa.

Kwa sababu hizi, kuna umuhimu mkubwa wa kuwasaidia wastaafu hawa kujipanga kabla ya kuingia rasmi katika maisha ya kustaafu. Kujipanga mapema na kusaidiwa kwa ushauri maalumu kuna uwezekano mkubwa wa kumpunguzia mstaafu huyu hofu ya kustaafu. Hili linahusu mambo kadhaa kama: jinsi ya kutengeneza na kusimamia mpango wa kustaafu unaohusisha uzalishaji na usimamizi wa kipato binafsi baada ya kustaafu, taarifa kuhusu mchakato mzima wa maandalizi ya kustaafu, maarifa kuhusu hifadhi ya jamii, maarifa ya jinsi ya kushughulika na magonjwa ya uzeeni, na stadi za maisha ya kijasiriamali.

Kupata ushauri kuhusu kustaafu ni huduma ya msingi sana ambayo humwandaa na kumuweka sawa mstaafu tarajiwa ili ayajue mapema mambo yote ya msingi yanayohusu maisha ya kustaafu, ili akistaafu aende kuishi maisha yenye na amani. Ushauri, hasa kuhusu masuala ya kiuchumi, kisaikolojia, na kijamii ni muhimu sana, kumwondolea mstaafu hofu, hivyo kumtia matumaini kwamba maisha ya kustaafu sio ya kuogopesha kwa kiasi hicho! Mfanyakazi akipata ushauri huu anapata maarifa yanayomfanya ajitengenezee mpango wa maandalizi ya kustaafu miaka kadhaa kabla ya kustaafu.

Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasirimali kivitendo. Anapatikana kwa simu: 0718219530; e-mail: nzyy2001@gmail.com

Je, Unaweza Kutajirika Kwa Kubebwa Na Bahati?

Je, mafanikio ya huyu Simba yanatokana na bahati?

Habari rafiki,

Suala la kuzaliwa lina maajabu yake. Tunapozaliwa huwa hatujui endapo tunazaliwa katika familia tajiri au maskini. Hatujui kama tunazaliwa watoto wa kiume au wa kike, wala hatujui kama tunazaliwa walemavu wa viungo au akili…au tunazaliwa tukiwa wakamilifu. Hatujui pia kama tunazaliwa katika nchi yenye amani au nchi yenye vita, machafuko au majanga ya asili. Huwa tunazaliwa tu, na kujikuta tupo duniani!

Bila kujali tunavyozaliwa na mazingira tunayojikuta tumo, wapo watu katika mazingira hayo hayo wanaofanikiwa kimaisha na wapo wanaofeli na kuishia kuishi maisha duni, maisha yao yote. Sasa tujiulize, kuna kitu gani nyuma ya hali hii?

Marehemu Reginald Mengi ni mfano wa watu waliozaliwa katika umaskini lakini wakaja kuishi katika utajiri mkubwa. Katika kitabu chake cha I can, I must, I will, Mzee Mengi anaandika, “…nimezaliwa katika umaskini wa kutupwa. Familia yetu iliishi kwenye vibanda vya udongo tukichanganyika na ng’ombe, mbuzi na kuku…” Kuna mengi ya kujifunza kupitia Mzee huyu!

Sikiliza sasa. Katika maisha ya mafanikio kuna vitu viwili ambavyo hujadiliwa sana. Vitu hivi ni bahati na bidii. Inasemekana kuwa kuna watu wanafanikiwa kwa bahati na wengine wanapambana (bidii), ili kufanikiwa. Hebu na sisi tujadili hapa!

Tuchukue mfano mmoja. Unasafiri masaa mengi porini bila chakula na unajikuta una njaa kali. Ghafla unafika chini ya mti, na unaona una matunda yaliyokomaa, yakining’inia. Unagundua kumbe ni maembe. Ukiamua kufanya kitu…, kwa mfano kuyapiga au kuutingisha mti, ni wazi maembe yatadondoka, na utatuliza njaa yako. Kitendo hiki huitwa bidii.

Ukiamua kukaa chini ya mwembe, bila kufanya kitu, ukitarajia muujiza utokee, hilo linaweza lisitokee; na ni wazi utashinda na njaa. Hata hivyo, inawezekana ukajilaza tu chini ya mwembe, halafu ghafla ukaja upepo ukadondosha maembe, ukaokota ukala ukashiba. Likitokea hili unaweza usione umuhimu wa kufanya kitu. Na hii ndio huitwa bahati!

Huu ni mfano wa matokeo ya kutegemea bidii au bahati katika maisha. Kilicho wazi hapa ni kwamba binaadamu hatuna uwezo wa kudhiti bahati. Mwandishi mmoja anasema tunachoweza kudhibiti ni ile nguvu, bidii na maarifa tunayoyatia katika kufanya jambo lifanikiwe. Mara nyingi tunapowaona watu waliofanikiwa kama Bill Gates au Reginald Mengi tunaishia kusema aah hawa wana bahati bwana, au wamezaliwa katika familia tajiri. Je, ni kweli? Tuna kitu cha kujifunza kutoka kwao.

Mwandishi huyo anasema, “hata hicho kinachoitwa bahati…mara nyingi huwa upande wa watu waliopania hasa kushinda…watu wanaojituma na kupambana! Hawa ni watu wanaojiuliza…hivi mimi nataka nini hasa katika maisha yangu…na nifanye nini ili nifanikiwe?” Anasema majibu ya maswali haya ndio hujenga msingi wa matendo na msukumo wa ndani.

Reginald Mengi na Bill Gates wamefanana katika mambo mawili hivi. Wote ni matajiri… na wote wametoka familia duni. Lakini je utajiri wao umetokana na nini? Ki-uhalisia watu hawa wamesotea utajiri wao. Wamepitia vikwazo vingi, wamejituma, wamekesha nakadhalika.

Bill Gates anasema, “…sikutoka katika familia yenye uwezo mkubwa…hata hivyo kilichoniinua ni uwezo wangu mkubwa wa kuutumia ubongo, masikio na macho yangu kuona fursa. Nilipouona mlango niliurukia haraka, nikakutana na watu, nikajifunza, nikafanya bidii nakadhalika.”

Mwanasaikolojia mmoja anasema, “wapo watu wanaishi na umaskini mkubwa. Hawa, sio kwamba hawana bahati, hapana; tatizo ni kwamba wamekosa uwezo wa kujaribu au kuthubutu, kama wa Mzee Mengi.” Mengi mwenyewe anakiri kuwa pamoja na kuzaliwa familia maskini, kila siku walipambana na umaskini, bila kuchoka!

Kuhusu bidii na bahati, Mjasiriamali Sam Parr, anayemiliki Hustle Con anasema, “ kila nilivyojituma kufanya mambo ndivyo nilivyopata bahati zaidi. Jinsi nilivyoushughulisha ubongo ndivyo nilivyoziona fursa zaidi. Jinsi nilivyolala muda mfupi ndivyo nilivyotimiza malengo. Jinsi nilivyoweka akiba ndivyo nilivyoongeza mtaji. Jinsi nilivyojifunza ndivyo nilivyofahamu mengi.”

Bila kujali mazingira mtu aliyomo, kinachomtofautisha mmoja na mwingine ni jinsi anavyomudu kuzitumia fursa zinazojitokeza, kwa jinsi na kwa wakati zinapojitokeza.

Mwandishi mmoja anasema Bahati na Bidii ni watoto mapacha. Lakini Bidii ni mkubwa…kazaliwa mapema zaidi ya Bahati. Bahati ni mdogo wa Bidii, na mara zote hujiweka mgongoni mwa Bidii. Anasema, “Bidii mara zote hushinda bila kujali mazingira. Kama unajituma, unatoka jasho kwa kile unachokipenda, ni wazi utafanikiwa, na kwa upande mwingine watu watakuona una bahati…ingawa wewe ndani yako utakuwa unaiona bidii yako, kama sababu.”

“Na kama itatokea bahati haiko upande wako, wewe unayejituma, basi kuna nguvu ya asili ambayo huja kufidia hili. Hii nguvu hukaa upande wako, ikakupa hamasa ya kutokata tamaa, kutia bidii na maarifa zaidi, kuamka mapema na kulala saa mbaya, ili kupambana na ‘balaa’ la kukosa bahati.” Matokeo ya hamasa hii huwa ni mafanikio!

Yuko Mwandishi kaandika, “wapo watu ambao wala hawafanyi jitihada kubwa. Hawana mipango ya maana wala maarifa ya kutosha, lakini kila wanachoanzisha kinafanikiwa tu.” Anasema hawa ni watu wenye bahati ya kipekee. Ni bahati isiyotokana na mapambano!

Hata hivyo anasema bahati ya aina hii ina walakini. Inatokana na kitu kiitwacho ‘ngekewa’. Ni mazingira yasiyotabirika. Mazingira ya aina hii yana hatari mbele yake. Bahati ya aina hii inaweza kupotea saa yoyote bila kutarajiwa. Lakini mafanikio yanayotokana na bidii, hudumu, na hata balaa likitokea sababu yake hufahamika, na hufanyiwa kazi.

Wale wanaotaja sana bahati katika shughuli zao ni wale waliojikita zaidi katika imani ya ‘nguvu’ maalum iliyopo kwa ajili ya kuwapigania katika mipango yao. Wapo waliozama sana katika imani hii ambao muda wao mwingi huutumia kuongea na ‘nguvu’ hii maalum, bila kujituma, na hawa huishia katika umaskini mkubwa wa kipato.

Mwandishi mmoja anasema kimsingi unaweza kufanikiwa kwa bahati, wakati fulani, kama mfano wa ‘mtu na maembe’ hapo juu, lakini kiujumla chachu ya mafanikio muda wote ni bidii. Kama unataka kufeli basi wewe endelea kuamini katika bahati.

Hata hivyo kuna wakati unaweza kufanya bidii sana, na bado ukafeli. Ikitokea hivi unatakiwa kutulia…hii huwa ni kwa muda tu! Cha kufanya hapa; tia bidii zaidi, jifunze zaidi, wasiliana na watu zaidi, fumbua macho, masikio na ubongo zaidi, halafu muombe Mungu zaidi…hakika utafanikiwa!

Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasirimali kivitendo. Anapatikana kwa simu: 0718219530; e-mail: nzyy2001@gmail.com

Unapojiandaa kustaafu kuna mambo hutakiwi kuyapuuzia!

Furaha kama hii baada ya kustaafu hutokana na maandaliazi yaliyofanywa mapema!

Habari rafiki,

Naomba leo niongee na nyie, wafanyakazi wapya, na hasa mliokaribia kustaafu; ili mjifunze mapema, na hivyo mchukue hatua. Wapo wafanyakazi ambao miaka mitatu hadi mitano, baada ya kustaafu, unamkuta ana maisha ya kusikitisha; yaani yuko hoi bin taaban!

Maana yake ni kwamba pesa zote za mafao alizolipwa ‘zimekata’. Sasa, hebu tujiulize pamoja, je tatizo huwa ni nini hasa? Ukifuatilia, utagundua kwamba wengi wa wastaafu hawa hawakujiandaa vyema kustaafu. Walipuuzia mambo fulani na sasa ‘wanavuna walichopanda’!

Moja ya mambo ya msingi katika maandalizi ya kustaafu ni ujenzi wa tabia ya kuweka akiba. Tabia hii ina manufaa ya aina mbili. Kwanza unajizoeza kutumia fedha kwa umakini. Hizi ni fedha ‘ulizokataa’ kuzitumia ovyo – ili uzitumie kuweka akiba. Pili unajikusanyia mtaji ambao unaweza kuutumia kufanya uwekezaji, ukiwa ndani ya ajira, na hivyo unaanza kuzoea uendeshaji wa biashara au miradi mapema.

Sasa, suala la kujinyima, ili hatimaye zipatikane fedha za kuweka akiba, huwashinda wengi. Kati ya hao wapo wanaolalamika kwamba kwa kipato chao kidogo sio rahisi kubakiwa na pesa kwa ajili ya kuweka akiba. Hata hivyo, ukiwafuatilia utagundua wengi wao wanakosa nidhamu tu katika matumizi ya ‘hicho kidogo walicho nacho’. Na ufumbuzi wa tatizo hili ni kuwekeza katika mbinu za kuweka akiba kwa maandalizi ya kustaafu.

Mara nyingi kitu kigumu ambacho huwakabili wafanyakazi wengi kuhusu uwekaji akiba ni kuanza! Kitendo cha kujinyima, kuanza, na kujijengea mazoea ya kuweka akiba; ikiwa ni kwa asilimia ya kipato, au kiwango fulani cha fedha ambacho mtu anajipangia kila mwezi, ni hatua muhimu sana katika safari ya kutimiza malengo ya kustaafu.

Kwa hiyo, ili upate fedha za kuhifadhi, hatimae kuwekeza; njia mojawapo ya kufanya ni kupunguza matumizi. Zifuatazo ni baadhi ya njia rahisi za kukuwezesha kubana matumizi na hivyo kubakiwa na fedha kwa ajili ya kuweka akiba. Naomba sasa tuzijadili hapa:

Moja, jifunze kupanga bajeti kwa kila kipato unachoingiza, na ujue jinsi ya kutofautisha matumizi muhimu, ya kawaida, na ya akiba. Halafu, ukishakuwa na bajeti, jitahidi kuishi ndani ya bajeti yako. Na kila wiki chagua siku moja ya kufanya tathmini (mapitio) ya bajeti yako, ukilinganisha matumizi halisi na bajeti uliojipangia.

Pili, weka utaratibu mzuri wa manunuzi au maandalizi ya chakula. Kama kawaida, chakula ni jambo muhimu kwa maisha, na matumizi kwa ajili hii yanaweza kuwa makubwa. Hata hivyo, ili mfanyakazi uweze kubakiwa na fedha za kuweka akiba, unapaswa kuwa makini katika matumizi haya. Jenga utamaduni wa kununua chakula nafuu cha wiki nzima, kisha andaa chakula mwenyewe nyumbani, badala ya ‘kutoka’ kila unapotaka mlo, na hapa utapunguza sana gharama, ukabakiwa na kiasi cha kuweka akiba.

Tatu, jizoeze kufanya kazi zaidi. Swali: je, unaweza kulihusisha jambo hili na zoezi la kubana matumizi? Jibu ni ndio – kuna uhusiano! Unapokuwa umebanwa sana na kazi (uko bize), kazini na nyumbani, siku za kazi na hata za mapumziko, muda wa matumizi ya fedha yasiyo na maana hupungua sana.

Ukipenda kukaa bila kujishughulisha, unampa shetani nafasi ya kukutumia kwa mambo yake maovu. Ni kwamba, ukiwa huru mno, utatamani utafute marafiki, muende sehemu, na hapo ndipo mambo yanayolazimisha matumizi mabaya huanza.  

Nne, jizoeze kuwa na subira kabla ya kulipia bidhaa au huduma. Kwa mazoea tu, tukipita madukani tunatamani sana vitu, hasa tukiwa na pesa. Ndio maana unashauriwa ukitamani kitu usinunue hapo hapo, kiandike mahala kisha nenda, kaa siku kadhaa nyumbani; ukitafakari. Njia hii itakuepusha kununua bila mpangilio, na utaokoa fedha nyingi.

Tano, kushindwa kufanya vitu wewe mwenyewe. Katika hili wapo watu majumbani, utasikia, “nyasi zimezidi, mwite yule kijana mtaa wa pili aje atufyekee; au mpigie yule ‘binti mfuaji’ aje achukue hizi nguo chafu akafue; au mwiteni yule ‘mchimba vyoo’ aje atuchimbie shimo la takataka!”, nakadhalika.

Ni kweli, kuna vitu vya kitaalamu sio kila mtu anaweza kuvifanya. Hapa utalazimika kulipa ili vifanywe na wengine. Lakini unaweza pia ukawa umezidiwa na kazi, ukakosa muda wa kufanya kazi inayopaswa kufanywa muda huo. Kwa mazingira haya utalazimika kutoa fedha.

Kinachogomba hapa, ni ile tabia ya wafanyakazi ambao huendekeza uvivu au uzembe! Kisa? Ana ‘chenji’ mfukoni. Haya ni matumizi yasiyofaa! Hizi ni fedha ambazo zingeokolewa kwa kujituma tu, kufanya kazi fulani mwenyewe. Tena kuna kazi zingine ukizifanya mara kwa mara ni mazoezi tosha, kiafya.

Sita, gharama za mitoko kwa ajili ya kujiburudisha. Kufanya matembezi (mitoko) kwa lengo la kubadilisha hali ya hewa au kujifunza ni jambo zuri tu, hasa kwa wafanyakazi ambao huwa bize sana kazini. Watu wengi huamua kutoka na familia zao kwenda kutembea mjini, mbuga za wanyama au ‘beach’.

Kumbuka, kitu kizuri namna hii hakipatikani bure! Hata hivyo ukiwa makini unaweza kupata unachokitaka, na bado ukabakiwa na fedha mfukoni. Mara nyingi malipo ya kiingilio huwa nafuu kidogo. Gharama kubwa huenda katika usafiri, chakula, vinywaji na malazi. Kuepuka hili, wapo wanaofungasha chakula na vinywaji, kama inaruhusiwa; hivyo kupunguza matumizi. Na kwa kufanya hivi wanaokoa fedha nyingi. 

Saba, gharama za kufanyia mazoezi katika gym. Gym ni eneo linalotumika kufanyia mazoezi ukiwa ndani ya ukumbi. Unaweza kufanya mazoezi ya kila aina hadi kukimbia kwa spidi yoyote unayotaka. Wapo wanaolipia gym ada ya miezi kadhaa, na wapo wanaonunua vifaa na kuviweka nyumbani, kufanyia mazoezi.

Tatizo lililopo, ni kwamba wapo wanaolipia ada kwa ajili hii, ingawa hawafanyi mazoezi. Fikiria pia, mtu ana ukumbi umejaa mashine zote za mazoezi, lakini zinapigwa vumbi tu! Huyu bora angejiwekea ratiba ya jogging au kutembea kila siku, na angeokoa fedha nyingi, ambazo zingewekwa akiba au kuwekezwa kwa ajili ya kustaafu.

Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasirimali kivitendo. Anapatikana kwa simu: 0718219530; e-mail: nzyy2001@gmail.com

Wala Usitafute Mchawi; Biashara Yako Unaiua Wewe Mwenyewe!

Ukiwa makini katika utengenezaji wa bidhaa au huduma yako ‘wateja’ watakufuata hapo hapo ulipo!

Habari rafiki,

Wataaamu wa biashara wana msemo: “Biashara ni faida.” Mara zote tunapoanzisha biashara tunalenga kupata mafanikio; yaani tunatarajia kuwa baada ya kipindi fulani, cha kujituma na kupambana na changamoto nyingi, basi tuanze kuona matunda. Tunapenda tuone biashara zetu zikikua na kutupatia faida ya kutosha ii kuboresha maisha yetu.

Hata hivyo, katika mchakato wa uendeshaji wa biashara kuna wakati unaweza kugundua kuwa mambo hayaendi vizuri. Unaanza kuona idadi ya wateja inapungua, mauzo yanashuka, na faida pia inaenda chini. Unaanza kupatwa na mshangao na wasiwasi pia. Unaanza kujiuliza kulikoni?

Sasa, usipokuwa makini ni rahisi sana kutafuta majibu ya mkato. Hizi ni sababu rahisi ambazo hazizingatii uhalisia. Wafanyabiashara wengi tu, hasa wa nchi zetu za Kiafrika, wanaoishi vijijini na hata mijini, na hata wale wanaoonekana kulitaja sana jina la Mungu; wanatawaliwa sana na imani za ki-shirikina. Jambo lolote lisilo la kawaida likitokea utasikia, ‘aaah, si bure bwana, lazima kuna mkono wa mtu hapa’!

Kinachofuata ni kuanza kumtafuta huyo mtu; yaani mchawi aliye nyuma ya matatizo yanayotokea katika biashara yake. Katika kufanya ufuatiliaji, mfanyabishara analazimika kuingia gharama kubwa ya fedha, muda, na rasilimali nyingine, ambazo kimsingi zinatoka katika biashara yake hiyo hiyo.

Ukifuatilia kwa u-makini utaona hakuna msaada wowote unaotolewa na waganga wa kienyeji wanaofuatwa ili wamtafute huyo mchawi, na kisha wauondoe uchawi uliowekwa na huyo mchawi, kwa lengo la kuikwamisha biashara husika. Mfanyabishara atapewa madawa ‘kibao’, na masharti ‘lukuki’ akayatekeleze; lakini mwisho wake hakuna lolote linalobadilika.

Jambo kubwa ambalo wajasiriamali na wafanyabishara hawa wanasahau ni kwamba, mchawi mkubwa wa biashara zao ni wao wenyewe! Yaani mfanyabiashara, yeye mwenyewe, anaamua kujiroga halafu akiyumba ki-biashara, wala hakumbuki kuwa kajiroga mwenyewe – na ndipo badala ya kutafuta amejikwaa wapi, huamua kukimbilia kwa waganga wa kienyeji ‘kupiga bao’.

Nimesema, wafanyabiashara wengi wanajiroga wenyewe. Na wanafanya hivi kwa kushindwa kujua mambo muhimu, ya kawaida kabisa, ya uendeshaji wa biashara kitaalamu. Biashara ikiendeshwa kwa kufuata misingi yake na kuongezewa bidii, kujituma na nidhamu, utaona ‘inachanja mbuga’, na wala masuala ya waganga hayatajitokeza.

Ni misingi tu inayotakiwa kufuatwa. Msingi wa kwanza mkubwa ni mjasiriamali kutafuta elimu ya ujasiriamali au biashara. Ukipata elimu hii na ukaizingatia utapata mbinu nyingi za uendeshaji wa biashara yako kitaalamu. Kuna mambo mengine mengi yanayopatikana kupitia maarifa ya ujasiriamali. Kwa mfano je, eneo lako la biashara linashabihiana na aina ya biashara yako? Je, ulichunguza vizuri mahitaji ya wateja uliowalenga? Je. Ulichunguza vizuri washindani wako? Nakadhaika. Kama hukufanya haya, ulianza kujiroga mwenyewe mapema kabisa.

Swali jingine ni je, unatoa bidhaa bora zinazokidhi matakwa au mahitaji ya wateja wako? Je, bidhaa hizo zina ubora gani ukilinganisha na zile za washindani wako? Kama unauza bidhaa hafifu, ki-ujanjaujanja, tambua wateja watagundua, na baada ya muda ‘watasepa’!

Huduma bora kwa wateja ni jambo muhimu sana iwapo unataka kubakiza na kuvutia zaidi wateja wako. Huduma zako zikiwa mbovu, hata kama zina ubora mkubwa, utashangaa kuona wateja wanakupita, na kwenda kwa washindani wako; halafu unalalamika umerogwa! Kwa mfano, wapo watoa huduma kwa wateja, wakiwamo wamiliki wenyewe, hawana kauli nzuri wala uchangamfu kwa wateja. Wapo ambao hata neno ‘karibu’ tu, au ‘karibu tena’, hawana! Hapa unategemea nini?

Bei ya bidhaa ni moja kati ya mambo muhimu yanayogusa hisia za wateja. Angali bidhaa yako umeinunua au kuizalisha kwa gharama gani – halafu angalia uwezo wa wateja wako – halafu angalia pia bei za washindani wako zikoje, ili ujue bei gani ukiipanga itakupa faida bila kuwafukuza wateja wako. Usipozingatia hili, utaishia kusema umerogwa!

Fikiria pia, mteja amefika kwenye biashara yako, na umemwambia bei ya bidhaa. Mteja kwa kupungukiwa kidogo anakuomba umpunguzie, angalau kidogo; utasikia, “eeh bwana eeh, hiyo ndio bei, kama huna basi; we hujui gharama za bidhaa zimepanda?” Unachosahau hapa ni kwamba hauko peke yako unaeuza bidhaa hiyo; hivyo mteja ataondoka na hatarudi tena.

Tabia binafsi ya mmiliki wa biashara au mhudumu ni kigezo muhimu cha kuwavuta au kuwafukuza wateja kwenye biashara yake. Kwa mfano, hivi utajisikiaje unapokutana na mmiliki wa biashara fulani, unamsalimia vizuri tu, lakini yeye anakujibu ki-mkato, tena kwa maringo, akiwa haoneshi hata umuhimu wako? Je, utakuwa na hamu ya kununua kitu kwake?

Lazima ujue kuna vichocheo vya ukuzaji biashara ambavyo havina gharama kabisa; kama kuwajali, kushirikiana na kuwa karibu na mambo au shughuli za kijamii za watu wanaoizunguka biashara yako. Wasalimie watu kwa heshima, onesha unawajali, omba hata ushauri wao – maana hakuna ajuae kila kitu; huwezi kujua nani ana utaalamu gani utakaokufaa. Tabia hii inakujengea imani na ukaribu kwa jamii, na hatimaye inaijenga biashara yako.

Mwisho, nakuhimiza rafiki yangu ufuatilie makala zangu ili ujifunze mengi yahusuyo uendeshaji wa biashara, ubunifu na ujasiriamali kitaaamu; na hii itakuepusha na fikra za ki-shirikina. Ukweli, hizi ni imani tu ambazo zimejengeka katika nafsi za baadhi ya wafanyabishara zinazowafanya washindwe kuuona ukweli unaotokana na upungufu wao binafsi.

Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasirimali kivitendo. Anapatikana kwa simu: 0718219530; e-mail: nzyy2001@gmail.com

Kupitia Soka – Unaweza Pia Kujifunza Kupanga Mikakati Ya Biashara

Je ni striker anaenda kufunga au ni beki anazuia striker asipite? Mbinu zinahitajika hapa!

Habari rafiki,

Makala iliyopita nilizungumzia upangaji wa malengo ya biashara na umuhimu wake. Sasa, kinachofuata katika mchakato wa utekelezaji wa malengo ni kupanga mikakatiya utekelezaji. Mikakati ni njia mbalimbali zinazopangwa kiweledi zinazoweza kutumiwa na mjasiriamali katika kufikia malengo aliyojipangia. Mikakati iliyo bora ina nafasi kubwa zaidi kuwezesha malengo kufanikiwa. Kwa hiyo kwa kila lengo lililopangwa unatakiwa uwepo mkakati wa kuonesha jinsi lengo hilo litakavyotekelezwa, litatekelezwa lini, na nani atafuatilia utekelezaji.

Katika makala hii nitaonesha jinsi  mikakati inavyosaidia ‘kusukuma’ malengo ya biashara. Kufanya hili, naomba nitumie mfano mmoja rahisi wa upangaji wa mikakati, unaofanywa katika mpira wa miguu au soka, kwa lengo la kuusaka ushindi dhidi ya timu pinzani.

Zamani kidogo, katika kufuatilia masuala ya michezo nilikutana na makala moja ambayo, nilipoisoma niliona inaweza kutumika kuelezea vizuri dhana ya mikakati katika biashara. Kwa wapenzi wa soka wenye kumbukumbu, na hasa wapenzi wa timu ya Yanga, nadhani mtaielewa dhana hii kirahisi zaidi, na baadaye itakuwa rahisi kuutumia uelewa huu katika kutengeneza mikakati ya biashara zenu.

Mwandishi wa makala hiyo, Mohamed Hussein, aliandika kuhusu hatima ya timu ya Yanga, iliyokuwa anashiriki Ligi ya Mabingwa wa Afrika, mwaka 2018, wakati ikijiandaa kupambana na timu ya Township Rollers ya Botswana, katika mchezo wa marudiano wa kufuzu kucheza hatua ya makundi, uliopangwa kufanyika tarehe 17 Machi, 2018 huko Botswana.

Aliandika kujaribu kuwatoa hofu wapenzi wa soka hasa wale wa Yanga ambao walikuwa wanaonesha hofu ya wazi kwamba, kwa matokeo mabaya ya kufungwa mabao 2-1 nyumbani Tanzania katika mchezo wa kwanza, basi wengi waliamini kuwa Yanga tayari imeshatolewa, hasa ukizingatia kiwango hafifu walichokionesha katika mechi ya kwanza.

Akiwatia moyo, Mwandishi huyo alisisitiza kuwa yeye anaamini kuwa mpira unadunda, na lolote linaweza kutokea katika mpira, na kwamba kikubwa ni namna Yanga itakavyojipanga ki-mkakati, na jinsi itakavyochanga vizuri karata zake huko ugenini.

Alipendekeza mikakati ambayo aliamini ikizingatiwa na kocha, pamoja na wachezaji, ingeweza kuwafanya Yanga kutimiza lengo lao kuu ambalo ni kufuzu kuingia hatua ya makundi; na pia kutimiza lengo lao la muda mfupi – kushinda mechi ile. Alipendekeza mikakati ifuatayo:

  • Kwanza, Yanga wajitahidi kuuchezea sana mpira ili kuwapa presha wapinzani wao
  • Pili, wajitume sana mwanzoni ili wapate bao la mapema litakalowaongezea morali wao, huku likiwachanganya wapinzani wao
  • Tatu, Kocha apange kikosi cha mabeki wengi, na pale katikati ni lazima pawe na viungo wengi, ili waumiliki zaidi mpira, kisha kupokea na kutawanya mpira
  • Nne, Wachezaji wa mbele wajitahidi kuwa makini sana kumalizia nafasi walizotengenezewa
  • Tano, wachezaji wa mbele wasiwe wachoyo; na  mchezaji anapoona hayuko katika nafasi nzuri ya kufunga goli basi asisite kutoa pasi au ‘assist’ kwa mchezaji aliye katika nafasi nzuri zaidi

Ki-ukweli, mikakati hii ilibuniwa tu na mwandishi wa makala ile. Huenda kocha, wala wachezaji, hawakuwahi kuisoma. Hata kama waliisoma, huenda wao walikuwa na mikakati yao. Hilo si muhimu sana. Muhimu ni kwamba ni lazima tuwe na mikakati katika kila lengo tunalotaka litimie. Ndiyo, kwani utafanikisha vipi malengo yako bila mbinu za utekelezaji?

Pamoja na mikakati yao je, Yanga walishinda mechi ile? Hapana, walipata droo ya bila kufungana, na hivyo kutolewa katika mashindano hayo. Hata hivyo walionesha kiwango kikubwa zaidi ya kile cha nyumbani.

Hivyo basi, kama katika soka mikakati ni jambo muhimu sana kuzingatiwa, basi mikakati ni muhimu vilevile katika biashara, ikiwa ni njia au mbinu ya kusaidia kusukuma malengo, na hasa lengo kuu kabisa la kupata faida kupitia wazo lako la biashara. Zaidi ya faida, malengo mengine yanaweza kuwa kuongeza mapato, kupunguza gharama ya uendeshaji na kuongeza ubunifu; ambayo yanahitaji mikakati pia.

Kwa mfano, kama lengo lako ni kuongeza mauzo, mikakati inayopaswa kuwekwa ni ile itakayosaidia kuwavuta wateja kwa wingi kuja kununua bidhaa yako, ambayo una uhakika inahitajika kwa wingi. Mikakati hiyo yaweza kuwa kama ifuatavyo:

  • Kuhakikisha bidhaa zako zina ubora wa hali ya juu
  • Kuziweka bidhaa zako mahala pa wazi ili wateja wasipate taabu kuziona
  • Kuitangaza biashara yako, na bidhaa zake, kwa kiwango cha juu
  • Kutoa huduma nzuri kwa wateja kabla, wakati na baada ya mteja kuondoka
  • Kujenga uhusiano mzuri na wateja ili wawe mabalozi kwa wateja wengine tarajiwa
  • Kutoa huduma kwa uaminifu ili wateja wawe na imani na wewe na biashara yako pia

Kwa hiyo, ili biashara yako ifanikiwe huna budi kujiwekea mikakati ya ushindi inayoakisi malengo yako, na inayoendana na changamoto zilizo mbele yako. Msisitizo mkubwa hapa uko katika kuifuata mikakati hiyo kivitendo. Elewa kwamba bila vitendo, mikakati hiyo itaishia kubaki kwenye makaratasi tu au  katika nadharia.

Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasirimali kivitendo. Anapatikana kwa simu: 0718219530; e-mail: nzyy2001@gmail.com