Tumia Mbinu Hizi Kufanya Ubunifu Katika Ujasiriamali

Ubunifu sio tukio bali mchakato unaohusisha nyanja nyingi….

Habari rafiki.

Nimeshaeleza kupitia makala zangu kadhaa, kuwa ubunifu ni uwezo wa kufikiri, kutafuta majibu na kutatua changamoto kwa namna ya kipekee; na kwamba ubunifu ni matokeo ya kuufikirisha ubongo ili kupata njia mpya na nzuri zaidi za kutatua changamoto au tatizo lililobainika. Nimeeleza pia kuwa ubunifu una nafasi kubwa katika ujasiriamali.

Ubunifu sio kitu rahisi ‘ki-vile’; yaani eti kila wakati uibuke na bidhaa mpya yenye utofauti, au huduma mpya, au mchakato mpya wa uzalishaji au utoaji huduma. La hasha! Hata hivyo, siyo kitu kigumu! Panahitajika maarifa tu. Yaani ujue mbinu ipi itakupatia mawazo mapya na ya maana ya kibunifu kuweza kukuletea tija katika biashara au shughuli yako.

Zifuatazo ni baadhi ya mbinu ambazo ukizitumia zitakusaidia kuongeza uwezo wako wa ubunifu:

Kwanza, Kukopi au kuiga mawazo ya wengine. Hii ni njia rahisi kabisa ya ubunifu. Hapa ni kwamba unaiga kitu ambacho wengine walishakifanya hapo kabla. Kuiga huku haina maana ya kukopi na ku-paste, hapana! Hapa ninamaanisha kwamba unachunguza kitu kizuri kilichofanyika mahala fulani, halafu unakiboresha kidogo, kisha unakizalisha na kukitumia kwako. Kuiga huku tunaita ‘kuiga kimkakati’, ambayo ni mbinu nzuri ya kufanya ubunifu.

Kwa mfano, Henry Ford, mwanzilishi wa Kampuni ya magari ya Ford, alitembelea kiwanda kimoja cha kusindika nyama, Marekani, akaona mtiririko wa utendaji kazi  na mpangilio wa mashine na wafanyakazi katika mnyororo mmoja, mtindo unaoitwa ‘assembly line production system’. Akavutiwa na ubora, uharaka, na unafuu wa gharama za uzalishaji kwa kutumia mtindo huu.

Aliporudi kwake, akatumia maarifa hayo kwenye kiwanda chake cha magari, kisha akaongeza ujuzi wake kidogo; akafanikiwa kupunguza muda na gharama kwa kiwango kikubwa. Huu ni ubunifu wenye tija unaotokana na kuiga.

Pili, kuuliza wateja wako. Ukiweka utaratibu wa kuwauliza wateja wako kwamba wangependa bidhaa au huduma zako ziweje, utapata mawazo mengi sana, ambayo ukiyachuja, unaweza kuyatumia kuboresha bidhaa au huduma zako.

Kwa mfano, wateja wanaweza kuuliza au kutaka vitu, urembo au madoido fulani yawepo katika bidhaa yako. Au wakataka uweke vitu fulani vitakavyoifanya bidhaa yako iwe rahisi kutumia, au yenye mvuto zaidi; kwa mfano, mpangilio wa rangi, harufu au ulaini wa kitambaa au bidhaa husika.

Hapa unatakiwa usikilize maoni yao kwa umakini uone ni maoni yapi ukiyafanyia kazi unaweza kuongeza ubora wa bidhaa yako na ukaongeza mauzo zaidi.

Tatu, wachunguze wateja wako. Usiishie tu kuwauliza, wachunguze pia! Angalia wanatumiaje bidhaa zako, au ni vitu gani wanavibadilisha wakishanunua bidhaa yako. Fanyia kazi majibu ya uchunguzi wako.

Hivi ndivyo mmiliki wa Kampuni ya nguo ya Marekani, Levi Strauss, alivyofanya baada ya wateja wake wa Jeans kuwa wanazichana Jeans zao sehemu fulanifulani. Alipoona hilo, haraka sana akaanza kutengeneza Jeans zilizochanywa, na mauzo yake yakapaa!

Nne, fuatilia malalamiko na changamoto za wateja. Sio wateja wote wanalalamikia bidhaa au huduma unazowapatia. Hivyo ukipata wanaolalamika usiwachukie, shukuru, na wasikilize kwa makini. Sikiliza, pia fumbua macho, uone matatizo au changamoto wanazolalamikia. Hapa utapata pa kuanzia kufanya ubunifu, na ukiweza kufanikiwa kuondoa changamoto hizo utaongeza imani ya wateja wako, wataona jinsi unavyowajali, na mauzo yatapanda sana.

Tano, unganisha au changanya bidhaa. Kuchanganya bidhaa moja na nyingine ni mbinu ya kuja na bidhaa mpya na yenye matumizi bora zaidi. Kwa mfano, simu za mwanzo za mkononi hazikuwa na kamera wala radio.

Hivyo, wabunifu katika Makampuni ya simu waliwaza na kuona uwezekano wa kuzalisha bidhaa moja yenye nyongeza ya vitu hivyo, ndipo wakaunganisha vitu hivyo na kuja na simu yenye kamera na radio. Na sasa vitu vingi zaidi vimeongezwa.

Ubunifu mwingine ni wa kuunganisha redio, cassete, mp3 au flash player, kupata bidhaa moja yenye upana zaidi wa matumizi. Uvumbuzi huu umewawezesha kuongeza thamani ya bidhaa hizo na  kuongeza mauzo pia.

Sita, punguza vitu kwenye bidhaa zako. Katika hili, jiulize, ni vitu gani ukiviondoa kwenye bidhaa, mchakato au njia za usambazaji wa bidhaa yako, itafanya bidhaa hiyo ipate ubora zaidi. Kwa mfano, Amazon waliamua kuondoa uuzaji wa vitabu kwa kutumia maduka halisi ya kuuza vitabu. Wakabakiza uuzaji vitabu kwa mtandao, online retailing.

Mfano mwingine ni uamuzi wa kuondoa mwamba wa mbele, au kiti cha kubebea mizigo, kwenye baiskeli. Kumbuka wasichana wengi, hasa warembo wa mjini, hawapendi baiskeli zenye mwamba au zenye kiti cha nyuma,wakitaka kuendesha baiskeli. Kwa kuviondoa vitu hivi utajikuta unaongeza mauzo yako kwa kiwango cha juu.

Saba, angalia washindani wako. Waangalie kwa umakini washindani wako. Unaona wanafanya nini? Kipi kipya wanachokuja nacho? Una kitu cha kujifunza? Unaweza kuiga kimkakati? Unaweza kuboresha ukaja na kitu kipya na bora zaidi? Basi fanya hivyo.

Nane, geuza bidhaa za kizamani kuwa za kileo. Angalia huduma, mchakato au bidhaa iliyokuwa inatumika zamani, ambayo inaonekana imepitwa na wakati, kisha angalia jinsi unavyoweza kukirudisha kitu hicho au fasheni hiyo ya zamani, kwa kuifanyia mabadiliko fulani,  ikawa bidhaa ya kileo na itakayowapa vionjo vipya watumiaji wa kileo.

Kwa mfano, ‘Dungarees dress’ ni vazi lililokuwa likivaliwa katika mazingira ya shamba au gereji, lakini wabunifu wamelichukua, wakalifanyia ukarabati kidogo, wakalitangaza kupitia kwa wasichana warembo, na sasa linapendwa na linavaliwa na warembo karibu kila mahala.

Kwa kumalizia, ubunifu ni chachu kubwa ya ujasiriamali na hivyo ili kuongeza tija katika bidhaa au huduma zako huna budi kuwa na maarifa na mbinu. Yaani ujue mbinu ipi itakupatia mawazo mapya na ya maana ya kibunifu kuweza kukufanya utengeneze bidhaa au utoe huduma bora zaidi itakayokuletea tija katika biashara au shughuli yako.

Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasirimali kivitendo. Anapatikana kwa simu: 0718219530; e-mail: nzyy2001@gmail.com

Wala Usitafute Mchawi; Biashara Yako Unaiua Wewe Mwenyewe!

Ukiwa makini katika utengenezaji wa bidhaa au huduma yako ‘wateja’ watakufuata hapo hapo ulipo!

Habari rafiki,

Wataaamu wa biashara wana msemo: “Biashara ni faida.” Mara zote tunapoanzisha biashara tunalenga kupata mafanikio; yaani tunatarajia kuwa baada ya kipindi fulani, cha kujituma na kupambana na changamoto nyingi, basi tuanze kuona matunda. Tunapenda tuone biashara zetu zikikua na kutupatia faida ya kutosha ii kuboresha maisha yetu.

Hata hivyo, katika mchakato wa uendeshaji wa biashara kuna wakati unaweza kugundua kuwa mambo hayaendi vizuri. Unaanza kuona idadi ya wateja inapungua, mauzo yanashuka, na faida pia inaenda chini. Unaanza kupatwa na mshangao na wasiwasi pia. Unaanza kujiuliza kulikoni?

Sasa, usipokuwa makini ni rahisi sana kutafuta majibu ya mkato. Hizi ni sababu rahisi ambazo hazizingatii uhalisia. Wafanyabiashara wengi tu, hasa wa nchi zetu za Kiafrika, wanaoishi vijijini na hata mijini, na hata wale wanaoonekana kulitaja sana jina la Mungu; wanatawaliwa sana na imani za ki-shirikina. Jambo lolote lisilo la kawaida likitokea utasikia, ‘aaah, si bure bwana, lazima kuna mkono wa mtu hapa’!

Kinachofuata ni kuanza kumtafuta huyo mtu; yaani mchawi aliye nyuma ya matatizo yanayotokea katika biashara yake. Katika kufanya ufuatiliaji, mfanyabishara analazimika kuingia gharama kubwa ya fedha, muda, na rasilimali nyingine, ambazo kimsingi zinatoka katika biashara yake hiyo hiyo.

Ukifuatilia kwa u-makini utaona hakuna msaada wowote unaotolewa na waganga wa kienyeji wanaofuatwa ili wamtafute huyo mchawi, na kisha wauondoe uchawi uliowekwa na huyo mchawi, kwa lengo la kuikwamisha biashara husika. Mfanyabishara atapewa madawa ‘kibao’, na masharti ‘lukuki’ akayatekeleze; lakini mwisho wake hakuna lolote linalobadilika.

Jambo kubwa ambalo wajasiriamali na wafanyabishara hawa wanasahau ni kwamba, mchawi mkubwa wa biashara zao ni wao wenyewe! Yaani mfanyabiashara, yeye mwenyewe, anaamua kujiroga halafu akiyumba ki-biashara, wala hakumbuki kuwa kajiroga mwenyewe – na ndipo badala ya kutafuta amejikwaa wapi, huamua kukimbilia kwa waganga wa kienyeji ‘kupiga bao’.

Nimesema, wafanyabiashara wengi wanajiroga wenyewe. Na wanafanya hivi kwa kushindwa kujua mambo muhimu, ya kawaida kabisa, ya uendeshaji wa biashara kitaalamu. Biashara ikiendeshwa kwa kufuata misingi yake na kuongezewa bidii, kujituma na nidhamu, utaona ‘inachanja mbuga’, na wala masuala ya waganga hayatajitokeza.

Ni misingi tu inayotakiwa kufuatwa. Msingi wa kwanza mkubwa ni mjasiriamali kutafuta elimu ya ujasiriamali au biashara. Ukipata elimu hii na ukaizingatia utapata mbinu nyingi za uendeshaji wa biashara yako kitaalamu. Kuna mambo mengine mengi yanayopatikana kupitia maarifa ya ujasiriamali. Kwa mfano je, eneo lako la biashara linashabihiana na aina ya biashara yako? Je, ulichunguza vizuri mahitaji ya wateja uliowalenga? Je. Ulichunguza vizuri washindani wako? Nakadhaika. Kama hukufanya haya, ulianza kujiroga mwenyewe mapema kabisa.

Swali jingine ni je, unatoa bidhaa bora zinazokidhi matakwa au mahitaji ya wateja wako? Je, bidhaa hizo zina ubora gani ukilinganisha na zile za washindani wako? Kama unauza bidhaa hafifu, ki-ujanjaujanja, tambua wateja watagundua, na baada ya muda ‘watasepa’!

Huduma bora kwa wateja ni jambo muhimu sana iwapo unataka kubakiza na kuvutia zaidi wateja wako. Huduma zako zikiwa mbovu, hata kama zina ubora mkubwa, utashangaa kuona wateja wanakupita, na kwenda kwa washindani wako; halafu unalalamika umerogwa! Kwa mfano, wapo watoa huduma kwa wateja, wakiwamo wamiliki wenyewe, hawana kauli nzuri wala uchangamfu kwa wateja. Wapo ambao hata neno ‘karibu’ tu, au ‘karibu tena’, hawana! Hapa unategemea nini?

Bei ya bidhaa ni moja kati ya mambo muhimu yanayogusa hisia za wateja. Angali bidhaa yako umeinunua au kuizalisha kwa gharama gani – halafu angalia uwezo wa wateja wako – halafu angalia pia bei za washindani wako zikoje, ili ujue bei gani ukiipanga itakupa faida bila kuwafukuza wateja wako. Usipozingatia hili, utaishia kusema umerogwa!

Fikiria pia, mteja amefika kwenye biashara yako, na umemwambia bei ya bidhaa. Mteja kwa kupungukiwa kidogo anakuomba umpunguzie, angalau kidogo; utasikia, “eeh bwana eeh, hiyo ndio bei, kama huna basi; we hujui gharama za bidhaa zimepanda?” Unachosahau hapa ni kwamba hauko peke yako unaeuza bidhaa hiyo; hivyo mteja ataondoka na hatarudi tena.

Tabia binafsi ya mmiliki wa biashara au mhudumu ni kigezo muhimu cha kuwavuta au kuwafukuza wateja kwenye biashara yake. Kwa mfano, hivi utajisikiaje unapokutana na mmiliki wa biashara fulani, unamsalimia vizuri tu, lakini yeye anakujibu ki-mkato, tena kwa maringo, akiwa haoneshi hata umuhimu wako? Je, utakuwa na hamu ya kununua kitu kwake?

Lazima ujue kuna vichocheo vya ukuzaji biashara ambavyo havina gharama kabisa; kama kuwajali, kushirikiana na kuwa karibu na mambo au shughuli za kijamii za watu wanaoizunguka biashara yako. Wasalimie watu kwa heshima, onesha unawajali, omba hata ushauri wao – maana hakuna ajuae kila kitu; huwezi kujua nani ana utaalamu gani utakaokufaa. Tabia hii inakujengea imani na ukaribu kwa jamii, na hatimaye inaijenga biashara yako.

Mwisho, nakuhimiza rafiki yangu ufuatilie makala zangu ili ujifunze mengi yahusuyo uendeshaji wa biashara, ubunifu na ujasiriamali kitaaamu; na hii itakuepusha na fikra za ki-shirikina. Ukweli, hizi ni imani tu ambazo zimejengeka katika nafsi za baadhi ya wafanyabishara zinazowafanya washindwe kuuona ukweli unaotokana na upungufu wao binafsi.

Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasirimali kivitendo. Anapatikana kwa simu: 0718219530; e-mail: nzyy2001@gmail.com

Kupitia Soka – Unaweza Pia Kujifunza Kupanga Mikakati Ya Biashara

Je ni striker anaenda kufunga au ni beki anazuia striker asipite? Mbinu zinahitajika hapa!

Habari rafiki,

Makala iliyopita nilizungumzia upangaji wa malengo ya biashara na umuhimu wake. Sasa, kinachofuata katika mchakato wa utekelezaji wa malengo ni kupanga mikakatiya utekelezaji. Mikakati ni njia mbalimbali zinazopangwa kiweledi zinazoweza kutumiwa na mjasiriamali katika kufikia malengo aliyojipangia. Mikakati iliyo bora ina nafasi kubwa zaidi kuwezesha malengo kufanikiwa. Kwa hiyo kwa kila lengo lililopangwa unatakiwa uwepo mkakati wa kuonesha jinsi lengo hilo litakavyotekelezwa, litatekelezwa lini, na nani atafuatilia utekelezaji.

Katika makala hii nitaonesha jinsi  mikakati inavyosaidia ‘kusukuma’ malengo ya biashara. Kufanya hili, naomba nitumie mfano mmoja rahisi wa upangaji wa mikakati, unaofanywa katika mpira wa miguu au soka, kwa lengo la kuusaka ushindi dhidi ya timu pinzani.

Zamani kidogo, katika kufuatilia masuala ya michezo nilikutana na makala moja ambayo, nilipoisoma niliona inaweza kutumika kuelezea vizuri dhana ya mikakati katika biashara. Kwa wapenzi wa soka wenye kumbukumbu, na hasa wapenzi wa timu ya Yanga, nadhani mtaielewa dhana hii kirahisi zaidi, na baadaye itakuwa rahisi kuutumia uelewa huu katika kutengeneza mikakati ya biashara zenu.

Mwandishi wa makala hiyo, Mohamed Hussein, aliandika kuhusu hatima ya timu ya Yanga, iliyokuwa anashiriki Ligi ya Mabingwa wa Afrika, mwaka 2018, wakati ikijiandaa kupambana na timu ya Township Rollers ya Botswana, katika mchezo wa marudiano wa kufuzu kucheza hatua ya makundi, uliopangwa kufanyika tarehe 17 Machi, 2018 huko Botswana.

Aliandika kujaribu kuwatoa hofu wapenzi wa soka hasa wale wa Yanga ambao walikuwa wanaonesha hofu ya wazi kwamba, kwa matokeo mabaya ya kufungwa mabao 2-1 nyumbani Tanzania katika mchezo wa kwanza, basi wengi waliamini kuwa Yanga tayari imeshatolewa, hasa ukizingatia kiwango hafifu walichokionesha katika mechi ya kwanza.

Akiwatia moyo, Mwandishi huyo alisisitiza kuwa yeye anaamini kuwa mpira unadunda, na lolote linaweza kutokea katika mpira, na kwamba kikubwa ni namna Yanga itakavyojipanga ki-mkakati, na jinsi itakavyochanga vizuri karata zake huko ugenini.

Alipendekeza mikakati ambayo aliamini ikizingatiwa na kocha, pamoja na wachezaji, ingeweza kuwafanya Yanga kutimiza lengo lao kuu ambalo ni kufuzu kuingia hatua ya makundi; na pia kutimiza lengo lao la muda mfupi – kushinda mechi ile. Alipendekeza mikakati ifuatayo:

  • Kwanza, Yanga wajitahidi kuuchezea sana mpira ili kuwapa presha wapinzani wao
  • Pili, wajitume sana mwanzoni ili wapate bao la mapema litakalowaongezea morali wao, huku likiwachanganya wapinzani wao
  • Tatu, Kocha apange kikosi cha mabeki wengi, na pale katikati ni lazima pawe na viungo wengi, ili waumiliki zaidi mpira, kisha kupokea na kutawanya mpira
  • Nne, Wachezaji wa mbele wajitahidi kuwa makini sana kumalizia nafasi walizotengenezewa
  • Tano, wachezaji wa mbele wasiwe wachoyo; na  mchezaji anapoona hayuko katika nafasi nzuri ya kufunga goli basi asisite kutoa pasi au ‘assist’ kwa mchezaji aliye katika nafasi nzuri zaidi

Ki-ukweli, mikakati hii ilibuniwa tu na mwandishi wa makala ile. Huenda kocha, wala wachezaji, hawakuwahi kuisoma. Hata kama waliisoma, huenda wao walikuwa na mikakati yao. Hilo si muhimu sana. Muhimu ni kwamba ni lazima tuwe na mikakati katika kila lengo tunalotaka litimie. Ndiyo, kwani utafanikisha vipi malengo yako bila mbinu za utekelezaji?

Pamoja na mikakati yao je, Yanga walishinda mechi ile? Hapana, walipata droo ya bila kufungana, na hivyo kutolewa katika mashindano hayo. Hata hivyo walionesha kiwango kikubwa zaidi ya kile cha nyumbani.

Hivyo basi, kama katika soka mikakati ni jambo muhimu sana kuzingatiwa, basi mikakati ni muhimu vilevile katika biashara, ikiwa ni njia au mbinu ya kusaidia kusukuma malengo, na hasa lengo kuu kabisa la kupata faida kupitia wazo lako la biashara. Zaidi ya faida, malengo mengine yanaweza kuwa kuongeza mapato, kupunguza gharama ya uendeshaji na kuongeza ubunifu; ambayo yanahitaji mikakati pia.

Kwa mfano, kama lengo lako ni kuongeza mauzo, mikakati inayopaswa kuwekwa ni ile itakayosaidia kuwavuta wateja kwa wingi kuja kununua bidhaa yako, ambayo una uhakika inahitajika kwa wingi. Mikakati hiyo yaweza kuwa kama ifuatavyo:

  • Kuhakikisha bidhaa zako zina ubora wa hali ya juu
  • Kuziweka bidhaa zako mahala pa wazi ili wateja wasipate taabu kuziona
  • Kuitangaza biashara yako, na bidhaa zake, kwa kiwango cha juu
  • Kutoa huduma nzuri kwa wateja kabla, wakati na baada ya mteja kuondoka
  • Kujenga uhusiano mzuri na wateja ili wawe mabalozi kwa wateja wengine tarajiwa
  • Kutoa huduma kwa uaminifu ili wateja wawe na imani na wewe na biashara yako pia

Kwa hiyo, ili biashara yako ifanikiwe huna budi kujiwekea mikakati ya ushindi inayoakisi malengo yako, na inayoendana na changamoto zilizo mbele yako. Msisitizo mkubwa hapa uko katika kuifuata mikakati hiyo kivitendo. Elewa kwamba bila vitendo, mikakati hiyo itaishia kubaki kwenye makaratasi tu au  katika nadharia.

Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasirimali kivitendo. Anapatikana kwa simu: 0718219530; e-mail: nzyy2001@gmail.com

Anza Mwaka 2022 Kwa Kupanga Malengo Yanayotekelezeka!!

Ukipanga malengo yako jitahidi uyaandike, lakini pia yawe SMART

Habari rafiki,

Karibu tena katika mfululizo wa makala zangu zenye lengo la kuelimishana kuhusu masuala ya ujasiriamali, ubunifu na stadi za maisha. Napenda kuchukua fursa hii kukutakia heri ya mwaka mpya; mwaka wa 2022. Baada ya kukutakia heri hii, napenda kukukumbusha kwamba kuna kitu muhimu unapaswa kufanya, tena haraka, kama hujakifanya bado mwishoni mwa mwaka 2021. Kitu hicho ni kujipangia malengo utakayoyatekeleza mwaka huu, 2022.

Nimewahi kujadili katika moja ya makala zangu kuwa binaadamu wa kawaida huzalisha takriban mawazo 6,000 kila siku. Hii ni kwa mujibu wa tafiti kadhaa zilizowahi kufanyika. Na kwamba kila ukionacho hapa duniani, kilichoundwa, ni matokeo ya uwezo wa binaadamu kufikiri na hatimaye KUTENDA.

Kwa hiyo, kutoka katika mawazo yako mengi yanayopita ndani ya ubongo wako, huenda kuna wazo linatawala zaidi akili yako. Yaani kila ukilizungusha kichwani wazo hilo, na kulifanyia tathmini, unajiridhisha kuwa ni wazo litakalokupatia tija; hivyo kilicho muhimu baada ya hapo ni kuingia katika vitendo. Sasa, ili uweze kutenda kwa ufanisi, jambo mojawapo muhimu katika kufanikisha utekelezaji wa wazo lako ni kupanga malengo.

Malengo yanabebwa na mambo au kauli inayoelezea vitendo ambavyo vikifanyika kwa mpangilio fulani vitawezesha kufikia au kupata matokeo yaliyo katika ndoto au maono ya mtu. Malengo ndiyo mwongozo wa mahala unapotaka kufika. Baada ya kujua unataka kufanya nini, kupitia wazo lako bora ulilolichagua, mfano wazo la kufanya biashara fulani, au kuendesha mradi fulani; unapaswa sasa kulikatakata wazo lako na kuliweka katika malengo, ambayo ukiyatimiza, utakuwa umefanikisha ndoto yako.

Katika uandishi wa malengo, tunatangulia kuandika lengo kuu, halafu chini yake yanafuatia malengo saidizi.  Malengo ni kiasi au kiwango cha mafanikio ambayo mjasiriamali anataka kuyapata ndani ya kipindi fulani. Malengo huandikwa katika mtindo wa kauli zinazoashiria matokeo yatakayopatikana kutokana na matendo yaliyopangwa kufanywa.

Wataalamu wa biashara wanasisitiza kuwa malengo, yanapoandikwa, yanapaswa kutimiza vigezo fulani. Yakitimiza vigezo hivyo yanapewa hadhi, kitaalamu, ya kuitwa malengo ‘SMART’. Tunaambiwa ili malengo yawe ‘SMART’ yanatakiwa: yawe na ‘uhalisia’, yaani yaeleze bayana nini hasa kinatakiwa kutimizwa; yaweze ‘kupimika’, yaani uweze kupima kama umetimiza lengo au la, kwa mfano uweze kusema, ‘lengo limekamilika kwa asilimia tisini ya matarajio’.

Vilevile, malengo SMART yanatakiwa pia yawe na ‘muda wa utekelezaji’, yaani uweze kujua kila lengo litakamilika lini; na yawe ‘yanawezekana kufikiwa’, yaani yaliyo ndani ya uwezo wako, na yasiyokatisha tamaa. Ki-ukweli wajasiriamali wengi, hasa wadogo, pengine hata wa kati, hawana uwezo wa kutimiza vigezo vya uandishi wa malengo ‘SMART’. Wanaojaribu kuandika wanaandika kile tu wanachotaka kifanyike, basi, na wanaingia moja kwa moja katika vitendo.

Kwa mfano, mjasiriamali mmoja, rafiki yangu, ambaye ana kipaji cha usanii wa maigizo, alipata wazo la kuanzisha kikundi cha sanaa za maigizo. Kwa kuwa anapenda kuandika, ameandika ndoto yake kuwa ni: “Kumiliki kikundi cha sanaa za maigizo na kukifanya kitoe sanaa zenye ubora wa juu katika ukanda wa Afrika ya Mashariki.”

Ameandika  lengo kuu la biashara yake kama ifuatavyo: “Kutengeneza na kusambaza kazi za sanaa zenye ubora wa juu zitakazokidhi mahitaji ya wateja tarajiwa.” Kimsingi hii ndiyo dhima au ‘mission’ ya biashara yake.

Chini ya lengo hili kuu, ameorodhesha malengo madogomadogoambayo yakifanyiwa kazi yatawezesha kutimia au kufanikiwa kwa lengo kuu. Baadhi ya malengo hayo ni:

  • Kufanya utafiti ili kukusanya taarifa za mahitaji ya soko la sanaa hii na aina ya maudhui yanayohitajika kwa sasa.
  • Kubuni na kuandika miswada mizuri ya kazi hizo za sanaa.
  • Kuwa na timu nzuri ya wasanii wenye vipaji na nidhamu ya kazi hii.
  • Kuwa na timu ya wataalamu wa kutengeneza kazi mbalimbali zitakazotayarishwa.
  • Kufanya tafiti za maeneo yatakayotumika kuchezea kazi hizo.
  • Kusimamia utengenezaji wa kazi za sanaa zenye ubora.
  • Kupata masoko mazuri ya kuuzia kazi hizi.
  • Kufanya kikundi na kazi zake mbalimbali zifahamike kwa wateja
  • Kupata mapato makubwa kutokana na kazi za kikundi.

Unaweza kuona kuwa malengo haya yameandikwa ki-kawaida sana, na kwa kweli hayako ‘SMART’. Hivyo anapaswa kuyafanya yawe ‘SMART’. Hata hivyo anastahili pongezi! Angalau anaonesha kujua anachotaka kufanya ili atimize lengo kuu. Hayo ya kitaalamu zaidi anaweza kuelekezwa tu na akaelewa.

Katika malengo, kuna malengo ya muda mrefu na mengine ya muda mfupi, na kila lengo linaloonekana ni kubwa linaweza kuvunjwavunjwa tena kupata malengo madogo ambayo ni rahisi kuyatia katika vitendo. Ni muhimu kuandika orodha ya malengo unayokusudia kupata matokeo yake, kwa sababu, kila lengo lina mpango wa utekelezaji, unaolenga kuonesha nini kitafanyika ili kufanikisha lengo husika na kitafanyika kwa kiwango gani, upi ni muda wa kuanza na kukamilika, mtu au watu gani watakaohusika kutekeleza, pamoja na bajeti ya utekelezaji.

Tunaambiwa na wataalamu kuwa ukishaweka malengo lazima pia uandike, kwa kila lengo, ni kwa namna gani utapima kama lengo lako limefanikiwa au hapana. Lazima uwe na kipimo cha mafanikio kitakachokuonesha hali halisi ya utendaji wako, kwa kujiuliza, je, unatimiza malengo au unakwama, kwa kiasi gani, na sababu zake ni nini hasa? Unaweza kujiuliza pia je, malengo yako labda yamekuwa makubwa sana, au tatizo ni changamoto zimezidi? Au labda ni uwezo wako wa kutenda ndio umekuwa mdogo? Hii inasaidia kujitathmini na kujipanga vizuri zaidi.

Ukishaweka malengo, una wajibu mkubwa wa kufuatilia kwa ukaribu utekelezaji wake, ukiongozwa na mpango wa utekelezaji. Ufuatiliaji ni shughuli inayofanyika mfululizo ikilenga kuona ni kwa kiwango gani yaliyopangwa yanatekelezwa. Lengo la ufuatiliaji ni pamoja na kutathmini endapo yaliyopangwa yanatekelezwa vizuri, kwa kuzingatia muda, bajeti na rasilimali zingine. Ufuatiliaji unaweza kufanywa kila siku, kila wiki, kila mwezi au baada ya miezi kadhaa, na unatusaidia kubaini pengo kati ya yaliyopangwa kufanyika na yaliyotekelezwa, na sababu zake pia.

Napenda kumalizia kwa kusema kwamba malengo ndiyo mwongozo wa mahala unapotaka kufika. Kupanga malengo ni jambo muhimu lisilopaswa kupuuzwa. Baada ya kujua unataka kufanya nini, kupitia wazo ulilolichagua, unapaswa kulipanga wazo lako katika malengo, ambayo ukiyatimiza, utakuwa umefanikisha ndoto yako. Na unapaswa kujitahidi kuyafanya malengo yako yawe SMART. Kwa hiyo kama una wazo tayari uliloingia nalo mwaka 2022, unapaswa sasa kuliwekea mpango ili liweze kutekelezeka kwa ufanisi.

Makala ijayo nitaelezea kuhusu mikakati katika biashara na umuhimu wake katika kufanikisha malengo. Naomba uungane na mimi kujadili pia. Heri ya mwaka mpya!!!!!

Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasirimali kivitendo. Anapatikana kwa simu: 0718219530; e-mail: nzyy2001@gmail.com

Hii Ndio Siri Kuu Ya Kuishinda Changamoto Ya Ushindani Katika Biashara

Mafanikio yako yatatokana na mbinu za ziada – na kufanya mambo kwa njia tofauti na washindani wako

Rafiki,

Nakukaribisha kwa mara nyingine, katika mfululizo wa makala zangu zenye lengo la kuelimishana kuhusu masuala ya ujasiriamali, ubunifu na stadi za maisha. Mengi yameandikwa kuhusu changamoto mbalimbali zinazowakabili wafanyabishara wakiwa wanaendesha biashara zao. Moja kati ya changamoto hizo ni ushindani katika biashara. Kiuhalisia, unapoamua kuingia katika biashara ujue kwamba unaingia katika ushindani na wenzako uliowakuta katika biashara hiyo, au wengine ambao unaingia pamoja nao, au wale ambao wataingia baadaye kufanya biashara kama yako.

Kwa maana hiyo huwezi kukwepa suala la ushindani katika biashara. Na kama ni hivyo basi, unachotakiwa kufanya ni kutafuta mbinu zitakazokuwezesha kufanya vizuri ndani ya ushindani uliopo. Kila siku ushindani katika biashara unaongezeka, kwa kuwa kila siku kumekuwa na biashara mpya zinazoanzishwa. Si ajabu kukuta watu zaidi ya kumi mkifanya biashara ya aina moja, tena kwenye mtaa mmoja.

Wapo wafanyabiashara walioshindwa kupiga hatua kutokana na kuzidiwa na nguvu ya ushindani. Hata hivyo, kuna njia au mbinu ambazo zikitumika zitawafanya wafanyabishara kuushinda ushindani. Na mbinu kubwa na muhimu katika uendeshaji wa biashara ni kujitahidi kuwa tofauti na wengine. Unatakiwa ujipange ili utoe kitu tofauti kitakachokufanya ujipambanue miongoni mwa wenzako. Unatakiwa uhakikishe unafahamika kwa vitu au kitu fulani kizuri au chenye thamani zaidi kwa mteja kuliko wenzako. Zifuatazo ni baadhi ya mbinu hizo:

Kwanza, toa bidhaa au huduma zenye ubora. Hakikisha wateja wako wanapata bidhaa au huduma bora zaidi ya washindani wako, na wanaridhika. Jitahidi kufumbua macho na kutega masikio yako vizuri ili uyaone au kuyasikia yote yanayolalamikiwa kuhusu bidhaa au huduma yako, kisha yafanyie kazi haraka.

Kwa mfano, kama unazalisha na kuuuza vifaa vya ujenzi, mfano tofali, jitahidi ufyatue tofali zenye ubora unaofaa, kuzidi washindani wako; yaani mali ghafi unayotumia iwe yenye viwango na vipimo stahiki. Tofali yenyewe iwe na vipimo sahihi vya urefu, upana na kina. Tofali iwe imemwagiliwa maji ya kutosha kuifanya iive na kukomaa vizuri na iwe imara kabisa. Ukiwapa wateja bidhaa zenye ubora, sifa hii itaenea kidogokidogo hadi itamfikia kila mtu, na hapo bidhaa yako itajitofautisha na zile za washindani, zilizo chini ya kiwango.

Pili, jifunze udhaifu wa washindani wako. Inawezekana wote mkawa mnatoa bidhaa bora kabisa. Lakini kwa uchunguzi wako ukagundua wenzio wanatoa lugha mbaya kwa wateja wao. Ukigundua hilo lifanyie kazi haraka. Ongeza ukarimu kwa wateja. Wakaribishe vizuri, ongea nao ki-ustaarabu, waoneshe kuwa unawajali na upo kwa ajili yao. Onesha unajali muda wao na usiwacheleweshe wateja wako bila sababu, n.k. Utaona matokeo yake.

Tatu, kuwa mbunifu. Nimeandika huko nyuma umuhimu wa ubunifu katika ujasiriamali, na nikasisitiza kuwa ujasiriamali na ubunifu ni chanda na pete. Biashara yoyote inayoendeshwa kiubunifu ni rahisi kuushinda ushindani na kusonga mbele. Mbunifu kila wakati ana jicho la udadisi. Ukiwa na jicho dadisi utajua wateja wako wanataka nini, kwa utaratibu gani na kwa wakati gani. Utajua ni kitu gani ambacho ukikiongeza au kukipunguza katika bidhaa au huduma yako kitawafanya wateja waridhike zaidi.

Kwa mfano, Zuhura Abdi ni mjasiriamali mdogo. Zuhura anatengeneza maandazi na kuyauza kila siku asubuhi, ikiwa ni huduma ya kifungua kinywa kwa jirani zake. Janeth John, baada ya kuona Zuhura anafanya biashara yenye faida, naye anaanza kupika maandazi, kama ya Zuhura, na kuyauza asubuhi pembeni kwa Zuhura, kwa staili ileile. Hapa utaona kuwa ushindani unaanza, na mauzo ya wote yanakuwa ya wastani. Wanagawana wateja na kuanza kutafutana uchawi.

Roza Jacob, naye anatamani kufanya biashara ya aina hii.  Lakini yeye, kabla ya kuanza anafanya utafiti kidogo, na kugundua kuwa baadhi ya walaji wa maandazi wanalazimika kula maandazi kwa kuwa hawazioni chapati zikiuzwa. Lakini pia anagundua kuna mahitaji ya vitafunwa hivi wakati wa jioni kwa kuwa baadhi ya wateja hupendelea kunywa chai na maandazi au chapati wakati wa jioni.

Roza anaamua kuuza maandazi na chapati, lakini anaziongezea bidhaa zake ladha kidogo ya viungo fulani. Lakini pia anaboresha usafi, na kuongeza ukarimu na lugha nzuri kwa wateja. Na badala ya kuuza asubuhi tu, yeye anaanza kuuza jioni pia. Huu ni aina ya ubunifu ambao unamtofautisha Roza na wenzake, na anafanikiwa ‘kuwazoa’ wateja wote wa Zuhura na Janeth.

Mfano mwingine unatoka kwa Mjasiriamali Furaha Tonya, niliyemfahamu kupitia gazeti moja.. Furaha anasema aliamua kuanzisha biashara ya kuuza dagaa waliokaangwa baada ya kugundua hii ni fursa bayana. Yeye pia alifanya utafiti kidogo na kugundua kwamba wafanyabishara wengi wa dagaa wanauza dagaa ghafi, hasa waliokaushwa kwa jua na kuanikwa juu ya mchanga. Lakini pia aliona dagaa wakiuzwa kwa mafungu, bila hata kufungashwa.

Anadai aliamua kuwaza ki-ubunifu, akitaka ajitofautishe na wengine. Kwa hiyo anasema, “niliwatembelea wauzaji wa jumla wa dagaa hadi nikawajua wanaouza dagaa walioanikwa kwenye virago au maturubai maalumu, hivyo dagaa hawa hawana mchanga au uchafu mwingine.” Anaongeza, “nilipogundua baadhi ya wafanyabiashara wanakaanga dagaa kwa mafuta yanayotokana na wanyama, mimi nikaona nijitofautishe; nikaanza kuwakaanga dagaa kwa kutumia mafuta ya mbegu za mimea, ambayo hayana madhara au ‘rehemu’ kwa mlaji.”

Anasema, “ubunifu wa ziada niliouweka ni pamoja na kubuni vifungashio vyenye ubora, na kuweka pia alama za utambulisho wa bidhaa yangu, au nembo maalum. Ukweli niliweza kuongeza thamani ya bidhaa yangu kwa kiasi kikubwa. Wateja waliongezeka sana na mauzo yalipanda zaidi ya mara mbili, na bado ubunifu unaendelea.”

Hatua ya kuchukua ni kwamba, mjasiriamali unapaswa ujifunze kujitofautisha na wenzako. Usifanye biashara kwa mazoea, yaani kufanya mambo yaleyale, katika mazingira yaleyale, kila siku, ukitegemea kupiga hatua. Fungua akili, tega masikio na fumbua macho yako ili ujifunze na kufanya ubunifu kila siku. Kuna namna nyingi za kujitoutisha kulingana na biashara yako – na kila mtu anaweza kufanya hili, na kupata manufaa makubwa.

Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasirimali kivitendo. Anapatikana kwa simu: 0718219530; E-mail: nzyy2001@gmail.com

Je Biashara Yako Inapiga Hatua? Thibitisha Kwa Kuchunguza Vitu Hivi…

Kuna vipimo vya aina nyingi kuthibitisha ukuaji wa biashara yako

Habari rafiki,

Ki-ukweli, kuanzisha biashara na kuilea hadi ianze kuleta matunda sio jambo dogo. Kuendesha biashara kuna changamoto nyingi ambazo ni lazima mjasiriamali apambane nazo hadi hatua ya mwisho. Kumbuka katika mapambano ya maisha kuna kushinda na wakati mwingine kushindwa; na hiki ni kitu cha kawaida katika biashara pia; kikubwa ni kutokata tamaa.

Katika biashara, jinsi unavyopambana na changamoto na jinsi unavyozishinda ndivyo unavyozidi kusonga mbele katika safari ya mafanikio. Mafanikio hujionesha kwa kigezo cha ukuaji wa biashara yako; ambayo kimsingi ni moja ya malengo muhimu ya kuanzisha biashara yoyote.

Ni muhimu kufahamu kwa uhakika kwamba biashara unayoifanya inakua au hapana. Kwa sababu, jinsi biashara yako inavyozidi kukua ndivyo unavyozidi kupiga hatua na kuboresha maisha yako. Usipolijua hili unaweza kushindwa kuchukua hatua stahiki mapema, na ghafla ukajikuta katika hali mbaya.

Sasa je, utajuaje kuwa biashara yako inakua? Kuna viashiria au vigezo kadhaa ambavyo vinaweza kukuonesha kuwa biashara yako inakua; kama ifuatavyo:

Moja, ongezeko la wateja. Ni kawaida sana unapoanza biashara yoyote kujikuta unamaliza siku nzima ukiwa na wateja wawili au watatu tu. Lakini, ukichungulia kwa washindani wako, unaona wateja wanagongana vikumbo, wakiingia na kutoka. Hili ni jambo la kawaida. Hata hivyo, jinsi muda unavyozidi kwenda, na kama una mikakati sahihi, utaanza kuona mabadiliko.

Ukiona idadi ya wateja inazidi kuongezeka siku hadi siku, wiki hadi wiki, mwezi hadi mwezi, na kadhalika, hapa unapata picha kuwa biashara yako inakua, na sababu yake ni kwamba watu wengi zaidi wanazidi kuifahamu, na labda wanavutiwa na bidhaa au huduma zinazotolewa hapo.

Mbili, ongezeko la mauzo ya bidhaa. Unapofanya biashara unafanya mauzo (fedha unayoingiza kwa mwezi kulinganisha na miezi ya nyuma) ya bidhaa au huduma. Jinsi wateja wanavyonunua kwa wingi ndivyo unavyoingiza mapato zaidi. Katika hali ya kawaida ongezeko la mauzo ni kigezo muhimu cha ukuaji wa biashara.

Tatu, ongezeko la faida. Kila mtu anayeanzisha biashara analenga kupata faida, na hili ndilo hasa lengo kuu la biashara. Mfanyabiashara unapaswa kupima faida unayopata kila baada ya muda fulani kwa kuangalia mapato yanayoingia ikilinganishwa na gharama mbalimbali za uendeshaji wa biashara. Ukijiridhisha kuwa unapata faida basi ujue biashara yako inakua.

Nne, kupanuka kwa biashara. Biashara nyingi zinapoanzishwa zinaanza na tawi moja tu eneo fulani. Baada ya kuona faida inaongezeka, na ongezeko la mahitaji ya wateja, wafanyabiashara hushawishika kufungua matawi ya biashara zao katika eneo hilo hilo au eneo jingine. Hiki ni kiashiria cha kutanuka kwa biashara, na ni kielelezo cha ukuaji pia.

Tano, ongezeko la mtaji wa kuendesha biashara. Wakati fulani watu huanza biashara kwa mtaji unaotokana na kuuza rasilimali zao fulani, kwa mfano shamba. Wengine huamua kukopa katika taasisi za fedha. Moja ya lengo muhimu la mfanyabiashara ni kuona mtaji unaongezeka ili aweze kuitanua zaidi biashara yake. Mara nyingi faida hurudishwa katika biashara kuongeza  mtaji.

Sita, kuongezeka kwa idadi na ubora wa bidhaa. Mtaji unapokuwa mdogo bidhaa zinakuwa kidogo na pengine zenye ubora wa kawaida. Lakini jinsi mtaji unavyoongezeka mfanyabiashara hupata pia uwezo wa kuongeza bidhaa zaidi na zenye ubora zaidi, na pengine huwa na uwezo wa kufanya ufungashaji (packaging) bora zaidi. Hiki ni kigezo kuwa biashara yake inakua.

Saba, ongezeko la mahitaji ya wafanyakazi. Biashara inapoanza, inaanza ikiwa ndogo, na wakati mwingine mwanzilishi ndiye anakuwa mfanyakazi yeye mwenyewe; yaani hahitaji msaidizi. Lakini baada ya muda anaanza kuzidiwa na wingi au mahitaji ya ujuzi wa ziada katika kazi, na hivyo huona hawezi tena kumudu akiwa peke yake. Hapo anaanza kuajiri wasaidizi. Ukiona unaanza kuhitaji wafanyakazi zaidi maana yake biashara yako inakua.

Nane, ongezeko la mchango wa biashara yako katika maendeleo ya jamii. Biashara zote zinafanyika katika maeneo ya watu; yaani katika jamii. Katika jamii kuna mahitaji mbalimbali hasa ya huduma za jamii kama hospitali au shule. Serikali mara nyingi hushindwa kutimiza mahitaji haya peke yake, na hivyo huwahimiza wananchi kuchangia.

Sasa, wachangiaji wakubwa wa huduma hizi ni wafanyabiashara. Hata kukitokea dharura utakuta viongozi wanapita kwa wafanyabiashara kuomba msaada. Hivyo, biashara ikiwa changa michango hii huwa ni changamoto kubwa kwa mfanyabiashara. Ikifikia mahala ukaona kutoa misaada kwa ajili ya maendeleo ya jamii haikutii ‘presha’ sana, hiki ni kiashiria kuwa biashara yako anakua.

Ushauri wangu ni kwamba, wewe kama mjasiriamali unapaswa kuvifahamu na kuviangalia viashiria hivi kwa umakini ili ujipime kama kweli biashara yako inakua au la. Usijipime kwa kiasharia kimoja tu ukaridhika, bali angalia vigezo vingi kwa pamoja ndiyo utapata picha kamili. Baada ya hapo unapaswa kuchukua hatua stahiki yenye lengo la kuboresha zaidi. Wapo ambao huridhika, wakiona tayari ‘wamekua’ – wanakosea sana watu hawa!

Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasirimali kivitendo. Anapatikana kwa simu: 0718219530; e-mail: nzyy2001@gmail.com

Je, uko tayari kuyumbishwa na mawazo ya wengine?

Ukiwa na msimamo huwezi kuondolewa kwenye reli kirahisi

Habari,

Katika utafutaji wa maisha au kujiandaa na maisha ya kustaafu, wapo wafanyakazi ambao hujitahidi kufikiri ili kupata mawazo mbalimbali ambayo yanaweza kubadilishwa kuwa fursa zitakazowaingizia kipato ili kubadili maisha yao kabla na hata baada ya kustaafu.

Katika mchakato wa kubadili mawazo kuwa fursa ya kibiashara watu hufanya uchunguzi au utafiti ili kuona uwezekano wa mawazo yao kuwa bidhaa au huduma ya kuwaingizia kipato.

Katika mchakato wa utafiti, pamoja na mawazo yako, ni wazi kuwa utahitaji pia kupata mawazo ya watu wengine. Na wakati mwingine kabla hata hujaomba ushauri au maoni ya wengine, tayari wapo watu ambao tayari wameshafika kwako ili kutoa maoni yao; mengine chanya na mengine hasi.

Watu wengi huguswa au hujali maoni yanayotolewa na watu wengine, ambayo husifia au kukosoa kile wanachokusudia kufanya. Hili ni jambo zuri, kwani ubora wa kitu au kazi fulani unaweza kuchangiwa kwa kiasi kikubwa na mawazo ya wengine. Mawazo mchanganyiko yanayoletwa na watu mbalimbali huifanya akili ya binaadamu kujituma zaidi katika jitihada za kuchuja ili kupata wazo lililo na ubora zaidi.

Hata hivyo, wapo watu ambao mawazo ya wengine huwaondoa kwenye reli, au  malengo yao na hivyo kuwakwamisha. Na hapa ndipo linapokuja suala la mtu kuwa ‘focused’. Kuwa focused ni kujikita katika kufanya kitu ambacho umepanga kukifanya hadi ukifikishe hatima iliokusudiwa.

Ki-ubinadamu tu, watu huathiriwa sana na mawazo au mitazamo ya watu wengine. Hii ni pamoja na mitazamo ya watu walio karibu nao, ambao wengine wana ushawishi mkubwa juu yao. Watu kama wazazi, marafiki, majirani na washirika wa kibiashara huathiri sana maamuzi ya mtu.

Kwa mfano, kila unachofikiria au kupanga kufanya unakutana na mawazo pingamizi au hasi kutoka kwa marafiki, washirika na hata wazazi. Watakwambia, kwa mfano, “aah, mradi wa kuku kipindi hiki..? Hapana, achana nao, sasa hivi kuku wanashambuliwa na magonjwa kibao, usipoangalia utakata mtaji wako.”

Au kwa mfano, una kipaji cha kuimba na unaamua kumshirikisha rafiki yako, ukitarajia atakuunga mkono, na pengine kukuunganisha na taasisi zinazosaka na kukuza vipaji. Lakini kinyume chake utasikia, “mmh, kuimba? Utaweza rafiki yangu? Sidhani, na kwa jinsi ninavyoifahamu sauti yako siyo rahisi ukampata hata huyo ‘producer’ wa kukurekodi.” 

Kwa kauli hizi, kama una ‘roho nyepepi’ ni lazima utakata tamaa na utaogopa kuchukua hatua ya kuendelea na wazo lako, au kukuza kipaji chako. Watu wanaokwambia haya, kwa mtazamo wao wanaona wanakusaidia, ili pengine usipoteze muda na rasilimali zako bure; ingawa wapo pia ambao ki-ukweli hawakutakii mema!

Kwa hiyo nikwambie kitu sasa; ukiwa mtu wa kuingiwa na woga au kusikiliza sana watu wengine wanasema nini juu yako au juu ya mipango au kitu unachotaka kufanya, hakika utakuwa mtumwa. Labda kama wewe mwenyewe umeamua – lakini kitendo cha kukubali kuwa mtumwa wa mawazo ya wengine ni ujinga.

Kilichopo ni kwamba, hupaswi kujali sana watu wanasema au kufikiri nini juu yako. Unachotakiwa kufanya hapa ni kujitambua. Hukatazwi kufumbua macho na masikio ili kusikia au kuona. Lakini unapaswa kujitambua wewe ni nani na una uwezo gani binafsi. Jitahidi kujua unataka kwenda wapi na kuwa mtu wa aina gani sasa na baadaye – na amini  katika uwezo ulionao wa kukufikisha huko.

Kwa mfanyakazi ambaye umeshajijengea uwezo na fikra za kijasiriamali, ukiwa na lengo la kuyakabili ipasavyo maisha baada ya kustaafu, kilicho muhimu ni kujipima, na kujua uwezo ulionao, wa kuhimili  ‘ushawishi’ kutoka kwa watu wengine, yaani uwezo wa kusikiliza na kukubali kukosolewa, kupingwa na kupokea mawazo hasi.

Kama mjasiriamali unatakiwa kuwa tayari kukabiliana na kila aina ya ushawishi na kujitahidi kuushinda au kupunguza athari zake – kabla haujaathiri maamuzi yako ya msingi unaodhani ni sahihi na yana nafasi kubwa ya kupatia manufaa. Unapaswa kujua uchukue ushauri kiasi gani kutoka kwa wateja, marafiki, wafanyakazi, ndugu na hata wapita njia.

Wakati fulani jifunze kuwapuuza kabisa watu wanaokwambia kuwa wazo lako ni baya au halifai. Na hawa wako wengi tu, na wapo wasiokwambia hata sababu. Wanaweza kuwa sahihi; lakini kikubwa ni kwamba hili ni wazo lako wewe, na huenda umelitafakari kwa muda mrefu na kulifanyia utafiti. Kinachotakiwa ni kulitia wazo lako katika vitendo na kusonga mbele.

Jifunze kusema, “sipendi hayo ‘makelele’ yenu – na sitaki yaniondoe katika reli, uamuzi au mipangilio ya miasha yangu.”

Wapo watu  ambao wanachokiweza zaidi ni kukosoa, kutoa mawazo hasi, kuponda na kukatisha tamaa wenzao. Ingia kwenye mitandao ya kijamii uone jinsi watu wanavyochangia mada au maoni ya wenzao, ndio utajua ninachosema hapa. Mtu anaposti bidhaa au huduma yake vizuri tu, ili kuanza kuwataarifu wateja wake tarajiwa – utasikia, “bidhaa mbovu hiyo nani atanunua?”

Kwa hiyo, kama wewe una kipaji chako; una kitu unakiweza na unataka kukifanya kwa ajili yako au jamii yako, tengeneza au fanya kitu hicho na wapatie watu. Huenda sio wote watakipenda kwa sasa, lakini wapo watakaokipenda, na wengine watakuja baadaye.

Msanii maarufu wa sanaa za uchoraji, And Warhol anasema: “Tengeneza kazi ya sanaa – wape watu. Halafu wakati watu wanafikiria kama wataipenda au la – tengeneza kazi nyingine – na nyingine tena – wape!”

Hatua ya kuchukua hapa ni kwamba, kama wewe ni mfanyakazi na umeamua sasa kuanza kufanya ujasiriamali ukijiandaa kustaafu, unatakiwa kujiamini na kuamini kile unachotaka kufanya. Elewa kuna wakosoaji wengi. Usiwe mwepesi kupelekwa nje ya kile unachoamini au ulichopanga kufanya. Jitahidi kuwa focused; na utashinda!

Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasirimali kivitendo. Anapatikana kwa e-mail: nzyy2001@gmail.com; Simu 0718219530

Je Utagunduaje Kuwa Biashara Yako Inakua?

Kukua kwa biashara ni matokeo ya mikakati maalum

Habari,

Kuanzisha biashara na kuilea hadi ianze kuleta matunda sio jambo dogo. Kuendesha biashara kuna changamoto nyingi ambazo ni lazima mjasiriamali apambane nazo hadi hatua ya mwisho. Kumbuka katika mapambano kuna kushinda na wakati mwingine kushindwa; hiki ni kitu cha kawaida katika biashara, kikubwa ni kutokata tamaa.

Jinsi unavyopambana na changamoto na jinsi unavyozishinda ndivyo unavyozidi kusonga mbele katika safari yako ya mafanikio. Mafanikio hujionesha kwa kigezo cha ukuaji wa biashara yako; ambayo kimsingi ni moja ya malengo muhimu ya kuanzisha biashara yoyote.

Ni muhimu kufahamu kwa uhakika kwamba biashara unayoifanya inakua au hapana. Kwa sababu, jinsi biashara yako inavyozidi kukua ndivyo unavyozidi kupiga hatua na kuboresha maisha yako. Usipolijua hili unaweza kushindwa kuchukua hatua stahiki mapema na ghafla ukajikuta katika hali mbaya.

Sasa je, utajuaje kuwa biashara yako inakua? Kuna viashiria au vigezo kadhaa ambavyo vinaweza kukuonesha kuwa biashara yako inakua. Ukiweka umakini utagundua viashiria vifuatavyo:

Moja, ongezeko la wateja. Ni kawaida sana unapoanza biashara yoyote kujikuta unamaliza siku nzima ukiwa na wateja wawili au watatu tu; lakini, ukichungulia kwa washindani wako, unaona wateja wanagongana vikumbo, wakiingia na kutoka. Hili ni jambo la kawaida. Hata hivyo, jinsi muda unavyozidi kwenda, na kama una mikakati sahihi, utaanza kuona mabadiliko.

Ukiona idadi ya wateja inazidi kuongezeka siku hadi siku, wiki hadi wiki, mwezi hadi mwezi, na kadhalika, hapa unapata picha kuwa biashara yako inakua, na sababu yake ni kwamba watu wengi zaidi wazidi kuifahamu, na labda wanavutiwa na bidhaa au huduma zinazotolewa.

Mbili, ongezeko la mauzo ya bidhaa. Unapofanya biashara unafanya mauzo ya bidhaa au huduma. Jinsi wateja wanavyonunua kwa wingi ndivyo unavyoingiza mapato zaidi. Katika hali ya kawaida ongezeko la mauzo ni kigezo muhimu cha ukuaji wa biashara.

Tatu, ongezeko la faida. Kila mtu anayeanzisha biashara analenga kupata faida, na hili ndilo hasa lengo kuu la biashara. Mfanyabiashara unapaswa kupima faida unayopata kila baada ya muda fulani kwa kuangalia mapato yanayoingia ikilinganishwa na gharama mbalimbali za uendeshaji wa biashara. Ukiridhika kuwa unapata faida basi ujue biashara yako inakua.

Nne, kupanuka kwa biashara. Biashara nyingi zinapoanzishwa zinaanza na tawi moja tu eneo fulani. Baada ya kuona faida inaongezeka, na ongezeko la mahitaji ya wateja, wafanyabiashara hushawishika kufungua matawi ya biashara zao katika eneo hilo hilo au eneo jingine. Hiki ni kiashiria cha kutanuka kwa biashara, na ni kielelezo cha ukuaji pia.

Tano, ongezeko la mtaji wa kuendesha biashara. Wakati fulani watu huanza biashara kwa mtaji unaotokana na kuuza rasilimali zao fulani, kwa mfano shamba. Wengine huamua kukopa katika taasisi za fedha. Moja ya lengo muhimu la mfanyabiashara ni kuona mtaji unaongezeka ili aweze kuitanua zaidi biashara yake. Mara nyingi faida hurudishwa katika biashara kuongeza  mtaji.

Sita, kuongezeka kwa idadi na ubora wa bidhaa. Mtaji unapokuwa mdogo bidhaa zinakuwa kidogo na pengine zenye ubora wa kawaida. Lakini jinsi mtaji unavyoongezeka mfanyabiashara anapata pia uwezo wa kuongeza bidhaa zaidi na zenye ubora zaidi. Hiki ni kigezo kuwa biashara yake inakua.

Saba, ongezeko la mahitaji ya wafanyakazi. Biashara inapoanza, inaanza ikiwa ndogo, na wakati mwingine mwanzilishi ndiye anakuwa mfanyakazi yeye mwenyewe; yaani hahitaji msaidizi. Lakini baada ya muda anaanza kuzidiwa na kazi, na hivyo anaona hawezi tena kumudu akiwa peke yake. Hapo anaanza kuajiri wasaidizi. Ukiona unaanza kuhitaji wafanyakazi zaidi maana yake biashara yako inakua.

Nane, ongezeko la mchango wa biashara yako katika maendeleo ya jamii. Biashara zote zinafanyika katika maeneo ya watu; yaani katika jamii. Katika jamii kuna mahitaji mbalimbali hasa ya huduma za jamii kama hospitali au shule. Serikali mara nyingi inashindwa kutimiza mahitaji haya, na kuwahimiza wananchi kuchangia.

Sasa, wachangiaji wakubwa wa huduma hizi ni wafanyabiashara. Hata kukitokea dharura utakuta viongozi wanapita kwa wafanyabiashara kuomba msaada. Hivyo, biashara ikiwa changa michango hii inakuwa ni changamoto kubwa. Ikifikia mahala ukaona kutoa misaada kwa ajili ya maendeleo ya jamii haikutii ‘presha’ sana, hiki ni kiashiria kuwa biashara yako anakua.

Ushauri wangu ni kwamba, wewe kama mjasiriamali unapaswa kuvifahamu na kuviangalia viashiria hivi kwa umakini ili ujipime kama kweli biashara yako inakua au la. Usijipime kwa kiasharia kimoja tu ukaridhika, bali angalia vigezo vingi kwa pamoja ndiyo utapata picha kamili. Baada ya hapo chukua hatua stahiki.

Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasirimali kivitendo. Anapatikana kwa simu: 0718219530; e-mail: nzyy2001@gmail.com

Mambo haya huchangia wastaafu wengi kufilisika mapema -2  

Usipojipanga mapema, na kupata maarifa na taarifa sahihi, utabaki kushangaa unapogundua kibubu chako cha kustaafu kimekauka bila kujua sababu

Habari,

Katika makala kuhusu kustaafu, iliyopita, tulimnukuu mstaafu mmoja akisema kwamba alipostaafu alilipwa mamilioni mengi ya pesa. Hata hivyo, ingawa alikuwa ameshajenga na tayari anaendesha miradi yake midogomidogo; cha kushangaza, ndani ya mwaka mmoja, mamilioni yake yote yalikuwa yameyeyuka na wala hakujua yameenda wapi. Alipogundua hana kitu mfukoni ndipo alianza kutafakari…kwa nini?

Kuna sababu ambazo tunadhani huenda ndio chanzo cha tatizo hili; la wastaafu kufilisika muda mfupi tu baada ya kutoka kazini, na kubaki wakisononeka, na hivyo kuishi maisha duni uzeeni. Katika makala iliyopita tumejadili sababu nne. Naomba leo tujadili sababu moja zaidi.

Tano, kutaka kufanya miradi mingi kwa wakati mmoja. Katika hili yupo mstaafu mmoja, baada ya kupata mafao yake, aliitwa na rafiki yake wa karibu ambaye alimpa ushauri kuhusu uwekezaji wa pesa hizo. Alimwambia: “Mfanyabiashara mzuri ni yule anayefanya biashara nyingi kwa wakati mmoja. Yaani, usitegemee biashara moja peke yake; unatakiwa uwe na vyanzo vingi vya mapato kwa wakati mmoja.”

Alimwambia: “Ukiwa na biashara nyingi, na unazifanya kwa pamoja, zinasaidiana kuingiza pesa, lakini pia zinakufanya usitetereke; kwani moja ikidorora, nyingine inakukomboa. Ukitegemea chanzo kimoja tu, ujuwe ukianguka ndiyo basi tena; umekwisha. Usiweke mayai yote kwenye kapu moja, likianguka yote yanavunjika!”

Wapo pia, watu ambao huamua kuwekeza katika miradi fulani kwa kufuata ushawishi wa ndugu, bila wao binafsi kujiridhisha. Hivyo hujikuta wanaingiza fedha zao kwenye miradi inayonyonya fedha zao, badala ya kuwaingizia kipato. Kila mshauri huja na ushawishi wake, wa mradi au biashara anayosema inatoka, na itakutoa! Na wewe kwa kuwa una hela benki, tayari unakubali na kuingiza fedha huko, na kujikuta una miradi mingi kwa wakati mmoja.

Kiuhalisia, kabla hujafanya uwekezaji wowote ni vizuri ukafanya utafiti wa kutosha, ili ujiridhishe. Ujue soko likoje na changamoto zake, ujue washindani wako, ujue wateja wako wakoje, na ni wengi kiasi gani; na taratibu nyingine za uendeshaji wa biashara. Usione rafiki yako anatengeneza fedha kupitia biashara au mradi fulani ukadhani ni rahisi, hivyo ukataka na wewe uifanye; hapana!

Mstaafu huyo alipoyasikia maneno haya, kwamba anatakiwa kuwa na biashara nyingi kwa wakati mmoja, aliona huu ni ushauri uliojaa busara na nia njema kabisa; ukilenga kumletea manufaa na kumuepusha na hatari katika uendeshaji biashara. Na wapo watu wengi tu wenye mtazamo huu; wasomi wa biashara, na fani nyingine; na hata wazoefu wa biashara.

Labda kuna ukweli katika mtazamo huu – lakini kuna tafiti zinazoonesha kuwa kuna tatizo mahala fulani.  Mwandishi mmoja anasema kwamba ni rahisi mtu kuanzisha biashara mpya kila baada ya muda fulani mfupi. Lakini swali la kujiuliza ni je, unapata mafanikio yaliyokusudiwa katika kila biashara?

Mafanikio katika biashara ni pamoja na kumpatia mteja bidhaa au huduma bora; kuwapatia wadau mapato stahiki; kuwapatia wafanyakazi ujira bora; na kutengeneza faida ya kutosha.

Mtendaji Mkuu wa Kampuni ya Apple, Tim Cook aliwahi kusema: “Moja ya kanuni ambazo Steve Jobs alisisitiza  katika Kampuni hii ni umuhimu wa kuwa focused, yaani kujikita katika kufanya kile unachoweza kufanya vizuri sana.” Kumbuka, Marehemu Steve Jobs ni mwanzilishi mwenza, na baadaye Mtendaji Mkuu wa Apple.

Kwa mujibu wa Tim Cook, Steve Jobs alisisitiza hili kwa kusema, “Ni rahisi kuongeza biashara zaidi, lakini ni vigumu kubakia focused.” Maana ya kuwa focused, kwa mujibu wa Jobs, ni kusema ‘hapana’ kwa mawazo mia kadhaa yanayozunguka kila mara ndani ya akili yako; hata baada ya kuchagua kwa umakini wazo moja zuri uliloamua kulifanya ki-vitendo.

Tunaambiwa kwamba, Steve Jobs hakujishughulisha na wingi wa vitu anavyofanya, kwa mfano, umezalisha au umeuza vipande vingapi vya bidhaa, hapana! Yeye alijishughulisha zaidi na kufanya ‘kitu fulani kilicho bora’, hata kama ni kimoja tu.

Wafanyabiashara wengi wakubwa wamejikita katika jambo moja, wakijitahidi kulifanya jambo hilo kwa ubora zaidi kila siku. Angalia wafanyabiashara hawa wakubwa: Henry Ford alijikita kutengeneza magari; Pablo Picasso alijikita katika sanaa ya uchoraji na rangi; Bill Gates alijikita kwenye uzalishaji wa software; na Mark Zucherberg amejizatiti katika uendeshaji wa Facebook.

Kitu cha kuzingatia hapa ni kwamba, hawa wamefanikiwa kwa viwango hivyo kwa sababu walikuwa focused. Walikuwa na hamu, motisha  na mshawasha wa kupata kwanza hicho kimoja walichokuwa wanakipenda na kukimudu zaidi.

Tunaambiwa kuwa, wafanyabiashara wachache wakubwa unaowaona au kuwafahamu wakifanya biashara au wana Kampuni zaidi ya moja, mfano Marehemu Reginald Mengi, hawakuanzisha biashara zote kwa pamoja. Walianza na moja, wakaipa uhai hadi ikaweza kusimama vizuri peke yake, ndipo ikaanzishwa nyingine.

Mfano mwingine ni Bw.Richard Branson. Tajiri huyu Mwingereza, kwa miaka kumi na tatu, aliifanya Kampuni ya Virgin ijishughulishe na muziki tu, Virgin Records, kabla ya kujitanua baadaye hadi kuanzisha Kampuni za usafirishali na nyinginezo. 

Ushauri unaotolewa hapa ni kwamba kufanya biashara nyingi kwa wakati mmoja inaweza kuonekana ni mbinu au ujanja wa kupunguza vihatarishi au risk ya kile kinachosemwa hapo juu kwamba, ‘Usiweke mayai yote kwenye kapu moja’, lakini upo ushahidi unaoonesha kuwa wafanyabiashara waliojaribu kufanya biashara nyingi kwa wakati mmoja; ama biashara zote zilidhoofika au zilikufa.

Tatizo kubwa katika hili ni kwamba mfanyabiashara anapoanza kufanya jambo moja na kabla hajaliwezesha kumpatia tija sahihi tayari amerukia jambo jingine – huyu anakosa maono na mwelekeo. Anakosa focus na hivyo anaanza kutangatanga asijuwe lipi alifanye, alifanye saa ngapi, na kwa kiwango gani.

Kukibwa zaidi ni kwamba rasilimali zinazohitajika kufanya haya zinaanza kugawanyika vipande vipande. Rasilimali hizo ni fedha, muda, akili, wafanyakazi, vifaa, majengo nakadhalika. 

Utakuta kila biashara mpya inayoanzishwa, kabla ya ile ya kwanza kukomaa, ina tabia ya kutaka ‘kujitwalia’ rasilimali hizi na kujimilikiasha yenyewe, na hivyo kuzinyima pumzi biashara zilizotangulia. Hapa, baada ya muda rasilimali zinakuwa kidogo kutosheleza mahitaji ya kila biashara, na hapo ndipo biashara zote ‘zinakonda’ na kufa!

Hivyo, Mstaafu unashauriwa kuwa focused. Yaani, usihangaike huku na kule wala kuondoa macho katika fursa moja iliyo wazi mbele yako. Jitahidi kwanza kuweka mkazo, macho, akili, nguvu na rasilimali zote katika fursa moja yenye uhakika wa kukupatia faida kubwa; mpaka uikamate vizuri, na kuyaona bayana matokeo yake.

Baada ya kufanikisha mradi au biashara hiyo vizuri, basi hapo sasa unaweza kuanzisha nyingine; ukiwa tayari umeshakusanya ujuzi na rasilimali mpya za kutosha kuanzisha na kuendesha biashara mpya kwa tija, bila kuiathiri biashara yako ya mwanzo.

Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasirimali kivitendo. Anapatikana kwa e-mail: nzyy2001@gmail.com; Simu 0718219530

Biashara Nyingi Hukabiliwa na Changamoto Hizi; Jipange Kuzikabili

Unapokumbwa na changamoto katika maisha ya biashara njia mojawapo ya kujinasua ni kuomba msaada kwa wadau

Habari,

Katika makala hii, ya siku za nyuma, niliandika kuhusu jinsi ya kukabiliana na pepo la kukata tamaa katika safari ya ujasiriamali. Nilieleza kuwa, pamoja na mambo mengine, watu wengi hukata tamaa wakati wa kulitia wazo au jambo katika vitendo. Yaani katika hatua ya utekelezaji kunatokea vikwazo au ‘changamoto’ ambazo humtia mjasiriamali hofu na hisia za kukata tamaa.

Neno changamoto linaweza kuelezewa kama  mazingira kinzani yanayoleta upinzani kwenye maisha au mipango ya mtu. Wakati mwingine changamoto zinaelezewa kama matatizo au vikwazo vinavyojitokeza ili kupima uwezo wa mtu au taasisi kutumia akili na maarifa kukabiliana nazo..

Changamoto katika biashara, na maisha kwa ujumla, haziwezi kukwepeka, zipo kila siku, kwa sababu ni sehemu ya maisha. Hata hivyo uwepo wa changamoto wakati mwingine husababisha kuzaliwa kwa fursa ambazo humpasa mtu kuufikirisha ubongo wake vizuri zaidi ili aweze kuzivuna.

Kwa hiyo ili mtu aweze kuzikabili changamoto na kuzitumia kuvuna fursa zinazoweza kujitokeza, hana budi kujiandaa. Yaani maandalizi ni lazima ili uweze kukabiliana na changamoto. Na huwezi kufanya maandalizi kwa kitu usichokijua. Lazima uzijue mapema changamoto mbalimbali zinazoambatana na ujasiriamali au uendeshaji wa biashara, kisha uweke mikakati na rasilimali kukabiliana nazo.

Usipozijua mapema na ukajiandaa, zitakapojitokeza zitakuwa zimekushtukiza, kama ajali, ukiwa huna kinga yoyote, na hiki huwa chanzo cha wajasiriamali wengi kupata hofu na kukata tamaa, na wengine kuamua kuachana na shughuli hiyo.

Katika uendeshaji wa biashara au ujasiriamali fahamu kuwa kuna vitu vingi ambavyo vinaweza kukuletea changamoto. Katika makala hii nitaeleza baadhi ya changamoto hizo:

Kwanza, changamoto za mitaji au mikopo. Hapa nazungumzia zaidi mtaji kwa maana ya fedha. Licha ya kuwepo fursa nyingi za kukopa, vijana wengi wanashindwa kupata mikopo hii kwa kukosa dhamana. Wanaofanikiwa kukopa wanalalamikia riba kubwa zinazotozwa na mabenki au taasisi za fedha kitu ambacho hakizifanyi biashara zao kupiga hatua ya maana.

Pili, urasimu mkubwa wakati wa ufuatiliaji wa huduma mbalimbali, mfano vibali, katika maofisi, hasa ya serikali. Katika ufuatiliaji wa huduma hizi kuna muda mwingi hupotea; nenda rudi ni nyingi sana na zinachosha.

Utasikia mhusika kasafiri; au ulipaswa kujaza fomu hii na sio hiyo; au mtandao wa kompyuta uko chini, au nenda kalete hiki au kile katika ofisi kadhaa nyingine, acha namba ya simu tutakupigia (wala hawapigi!); na mengine mengi. Huu unaitwa urasimu. Usipokuwa mvumilivu utapata jazba, utakata tamaa na huenda ukaachana na ufuatiliaji wa suala lako; na ikiwa hivyo basi tayari umekwama!

Tatu, changamoto za eneo la biashara. Ni muhimu kupata eneo zuri la kufanyia biashara yako. Lakini unaweza kujikuta umepata eneo lililo mbali na wateja wako, au lisilo salama, au lililokatazwa kisheria. Imeshawatokea wafanyabiashara fulani kuvunjiwa vibanda vyao kupisha ujenzi wa barabara nakadhalika. Hii ni hasara kubwa. Wakati mwingine wapangishaji wanataka ulipe kodi ya miezi sita au hata mwaka mmoja, wakati mtaji wako ni mdogo.

Vilevile, kama unafanya biashara ambayo inahitaji umeme au maji kwa uendeshaji wake, ukiwa katika eneo mbali na huduma hizi utashindwa kutoa huduma yako; au utaingia gharama kubwa sana kupata huduma hizi kwa haraka.

Nne, ushindani katika bei za bidhaa. Kwa kawaida bei hupangwa kwa kuzingatia gharama zilizotumika hadi kuzalisha au kuifikisha bidhaa au huduma sokoni. Changamoto ni pale unapolazimika kuuza bei ya chini kutokana na washindani wako kushusha bei kwa lengo la kukuondoa sokoni; au pengine wao wamenunua kwa gharama za chini zaidi.

Tano, wagavi kupandisha bei ya bidhaa. Hapa unajikuta unashindwa kupanga bei ambayo itafidia gharama za ununuzi au uzalishaji wa bidhaa zako. Wakati wateja wamezoea kupata bidhaa kwa bei fulani, ukiongeza bei kidogo tu, bidhaa hainunuliwi kwa spidi ya mwanzo.

Sita, kushindwa kupanga bei stahiki ya bidhaa au huduma. Uzoefu mdogo wa soko, na washindani wako, unaweza kusababisha mjasiriamali kushindwa kupanga bei stahiki, akaishia kupanga bei ndogo au kubwa na kuishia kupata hasara au kufukuza wateja.

Saba, wagavi kuchelewa kuleta au kutoleta kabisa bidhaa ulizoagiza, wakati wateja wako tayari umeshawapa matarajio, na wanangojea bidhaa yako; au wagavi kuleta bidhaa zisizo sahihi, (size, model, uzito, ujazo, aina, au ziliyokwisha muda wake, n.k). Hapa kuna hatari ya kupoteza wateja wako.

Nane, kufurika ghafla kwa bidhaa zako sokoni; mfano umenunua bidhaa kwa bei fulani, halafu ghafla washindani wako wakaleta bidhaa nyingi zaidi, soko likafurika na bei ikashuka, hasa kwa biashara ya mazao ya chakula ya msimu, kama nyanya, maembe na mbogamboga.

Tisa, matakwa ya sheria. Usipoyaelewa mapema na ukayafanya kwa wakati unaweza kuingia kwenye gharama ya penalty, au ukafikishwa mahakamani au kufungiwa biashara yako. Mfano kodi, tozo, returns, leseni, vibali n.k.

Kumi, upatikanaji wa taabu wa malighafi. Mjasiriamali anayezalisha bidhaa kutokana na malighafi fulani; mfano ufyatuaji wa tofali. Wakati fulani kunakuwa na uhaba wa kokoto, mchanga, hata sementi hivyo kuzorotesha uzalishaji na kusababisha usumbufu kwa wateja wako.

Kumi na moja, uwezo wa kuwavuta na kuwabakisha wateja. Hii ni changamoto ambayo usipohakikisha ubora wa bidhaa au huduma zako, kuwafanya wateja wapate wanachokitaka kwa wakati na ubora, hawataridhika, na unaweza ‘kuwafukuza’ wote.

Kumi na mbili, majanga ya asili, ujambazi au wizi n.k. Haya hutokea pasipo kutarajiwa. Kwa mfano mvua kubwa, au mafuriko. Majanga kama mafuriko husababisha usafiri kuwa mgumu na hivyo kusababisha kushindwa kufuata bidhaa sokoni, au wateja kushindwa kuja kununua. Mafuriko pia yanaweza kusomba au kuozesha bidhaa zikawa haziwezi kuuzika, na hasara yake ikawa kubwa.

Kwa hiyo basi, baada ya kuzijua unachopaswa kufanya ni maandalizi. Yaanitayari unazijua changamoto zilizo mbele yako, kulingana na aina ya biashara unayotaka kufanya, ni lazima sasa uweze kukabiliana na changamoto hizo kwa kujiandaa. Angalia uwezo ulionao, na rasilimali pia, kisha weka plani itakayokufanya uzishinde changamoto hizo mapema.

Kwa kufanya hivi utajikuta unaanza kuendesha shughuli au biashara yako bila presha wala gharama zisizokuwa na msingi, na utakuwa na uhakika wa kuwavuta na kuwabakisha wateja wako. Usipozijua mapema na ukajiandaa, zitakapojitokeza zitakuwa zimekushtukiza, kama ajali hivi, ukiwa huna kinga yoyote (off-guard).

Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasirimali kivitendo. Anapatikana kwa simu: 0718219530; e-mail: nzyy2001@gmail.com