Mambo haya huchangia wastaafu wengi kufilisika mapema

Mpango thabiti wa kustafu una nafasi kubwa ya kukujengea maarifa na tabia stahiki itakayokuepusha na majanga uzeeni

Habari,

Yupo mstaafu mmoja aliwahi kusema jambo fulani ambalo naona likidadavuliwa litasaidia kubadili namna wastaafu wanavyofikiri na wanavyofanya mambo yao, hasa ya kiuchumi, baaada ya kustaafu. Alisema, “nilipostaafu nililipwa pesa nzuri tu, mamilioni kadhaa. Lakini pia nilikuwa nimeshajenga na ninaendesha miradi midogomidogo; lakini cha kushangaza ndani ya mwaka mmoja mamilioni yangu yote yaliyeyuka na sikujua yameenda wapi.”

Aliongeza kwa kusema, “baada ya kugundua sina kitu mfukoni nilianza kutafakari…kwa nini? Nilianza kufanya utafiti mdogo, kuwafuatilia wastaafu wenzangu kadhaa, nikagundua siko peke yangu katika hali hii – na nilishangaa zaidi nilipowaona hata marafiki zangu waliosomea masuala ya fedha, nao ni matatizo tu. Fikiria mtu alikuwa na nafasi nzuri tu kazini halafu unamsikia akiomba hadi hela ya nauli; hili si jambo dogo!”

Naomba leo tujadili jambo hili, kwamba kwa nini watu wanaishiwa – tena muda mfupi sana baada ya kulipwa mafao yao ya kustaafu, pamoja na kwamba wengine tayari walishafungua miradi au biashara zao baada au hata kabla ya kustaafu, kwa lengo kwamba wajiingizie kipato endelevu kitakachochukua nafasi ya mshahara waliokuwa wakilipwa makazini kwao.

Kuna sababu kadhaa ambazo tunaweza kujadili hapa; kwamba huenda ndio sababu zinazofanya hali hii iwatokee wastaafu wengi.  Zipo sababu zilizo nje ya uwezo wa wastaafu, lakini pia zipo sababu ambazo tunaweza kuziita za kujitakia, au uzembe. Naomba tuzijadili hapa:

Moja, matumizi mabaya ya fedha baada ya kustaafu. Katika hili Mtafiti mmoja anasema: “Asilimia 46 ya familia za wastaafu hutumia, kwa mwezi, kiasi kikubwa zaidi cha fedha, kuliko kilichotumika wakati mstaafu akiwa kazini.” Ukiyachunguza matumizi haya utakuta yanachochewa na kitu kiitwacho ‘show-off’ (kujionesha).

Wapo wastaafu ambao huwekeza fedha zao katika anasa au ulimbukeni mwingine wa maisha, kwa ujinga tu au kukosa nidhamu. Nawafahamu wastaafu waliowekeza katika ulevi, ufuska au ununuzi wa vitu vya anasa, kwa lengo la kujitutumua tu, au kuwakoga wabaya wao.

Ipo simulizi ya kweli inayomhusu afisa mmoja mstaafu wa taasisi moja ya serikali. Huyu alijipenda sana, na hakupenda kupitwa na kitu kizuri. Na hili liliweza kwenda alivyotaka kwa kuwa nafasi yake ilimwezesha, kupitia marupurupu aliyokuwa akipata, kwa hiyo alizoea maisha ya kuonekana mtu wa ‘matawi ya juu’. Alipostaafu aliendeleza mtindo ule ule wa maisha; na sasa alifanya hivyo kwa kukopa bila mpangilio. Alilipwa mafao miezi 11 baadaye na baada ya kulipa madeni yake yote alibakiwa na shilingi milioni tano tu benki. Kiasi hiki cha pesa hakikumtosha mstaafu huyu, si kwa matumizi yake tu, bali hata kuendeshea miradi, hivyo aliishia kufilisika.

Mbili, kutaka kubakiza hadhi aliyokuwa nayo kazini. Hili linafanana kidogo na hilo la kwanza hapo juu. Wakati hilo la kwanza linawalenga mahasimu; hili la pili linafanywa na mstaafu kuwaonesha waliobaki kazini kuwa kustaafu hakujabadilisha hadhi yake, na hivyo bado anaweza kuishi kwa staili yake ile ile ya zamani, bila kugundua kuwa kinachotoka kwa sasa ni kikubwa kuliko kinachoingia; kupitia miradi au kutoka katika akiba ya pensheni ya mkupuo au ya kila mwezi. Ndio maana utakuta mstaafu ghafla kipato kinakata, halafu anaanza kushangaa.

Tatu, kubeba majukumu yaliyopaswa kuwa yamekamilika. Watu wengi huanzisha familia wakishapata ajira. Baada ya muda kidogo majukumu yanayohusu watoto huanza. Moja ya jukumu linalowatesa wafanyakazi wengi ni gharama za kuwasomesha watoto wao. Na kwa wale wanaopenda, au waliojaliwa kuzaa watoto wengi, hili ni tatizo jingine. Suala la elimu ya watoto ni jambo muhimu sana, ingawa si kazi rahisi, na hasa linapokuja suala la gharama.

Ndio maana suala la uzazi wa mpango huingia. Mpango huu unahusu idadi ya watoto wanaopaswa kuzaliwa, na wazaliwe lini; ili jukumu la kusomesha lifanyike ndani ya kipindi cha ajira. Ukikosea katika hili utajikuta unaingia katika kustaafu na mzigo huu, na fedha hizi zitatokana na mapato ya miradi yako, ambayo pengine bado haijakomaa sawasawa, au zitatokana na pensheni yako. Sasa, hali ikiwa hivi huwezi kuepuka kuishiwa baada ya muda mfupi, na kubaki ukishangaa.

Nne, mafao ya pensheni kuchelewa kulipwa. Kiuhalisia suala hili lina mchango mkubwa kwa wastaafu wengi kuishiwa fedha muda mfupi baada ya kustaafu. Ingawa na wastaafu wenyewe wanastahili lawama fulani hapa. Ni ukweli ulio wazi kuwa wastaafu wengi, wakiwa kazini huwa hawana utamaduni wa kujiwekea akiba yoyote, kwa ajili ya maandalizi ya kustaafu. Wanachokipata kazini, mshahara na malipo mengine, humalizikia huko huko kazini.

Hivyo, wanapostaafu mshahara hukoma hapohapo, na hivyo mapato ya familia huwa yamekatika. Sasa mstaafu huyu ambaye ana familia ikimtegema huwa hana cha kufanya. Kwa kuwa mafao huchelewa, anachofanya ni kujipeleka kwa wakopeshaji ambao hukopesha kwa riba kubwa. Wastaafu huwa hawana jinsi bali kukopa; ingawa huwa wanajifariji kwa fikra kuwa fedha watakazolipwa mafao ni nyingi sana. Lakini wastaafu wengi wamelizwa na wakopeshaji hawa kwa kiwango cha baadhi yao kufilisika!

Anamtaja mstaafu mmoja (tumwite Jeijei) kwamba alishawishiwa kukopa shilingi milioni 6 kutoka kwa mkopeshaji mmoja tapeli. Pensheni ya mzee huyu ililipwa miezi kumi tokea alipokopa kiasi hicho cha fedha. Kawaida ya wakopeshaji hawa humtaka mkopaji awape kadi yake ya benki ya akaunti ya mshahara, ambamo mafao yakilipwa yatapitia.

Kwa hiyo mafao yalipolipwa, mkopeshaji alimpigia hesabu jeijei, iliyofikia shilingi milioni 27! Mafao aliyolipwa Jeijei yalikuwa shilingi milioni 49, hivyo mkopeshaji alimbakizia Jeijei shilingi milioni 22 na presha juu yake! Takukuru ndiyo iliyomnusuru Jeijei. Iliingilia kati baada ya kupata malalamiko kupitia watoto wa Jeijei, akaweza kurudishiwa fedha yake; na ndipo alipoanza tena kupumua kwa faraja!

Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasirimali kivitendo. Anapatikana kwa simu: 0718219530; e-mail: nzyy2001@gmail.com

Mzazi Ukiwa Mzembe Ki-Malezi Utazodolewa na Wanao


Makabila mengi ya kiafrika yaliendesha mafunzo maalum kwa vijana kuwapatia stadi muhimu za maisha

Kimsingi, ni wajibu wa mzazi kumsaidia mtoto au kijana wake kuwa na taarifa au kukuza maarifa muhimu katika maisha yake. Na hili laweza kufanyika kupitia Stadi za Maisha. Haya ni maarifa ambayo yakitumika na kusimamiwa vizuri humjenga mtoto/kijana kuwa na mtazamo chanya kuhusu maisha yake binafsi na maisha yake ndani ya jamii.  

Stadi za Maisha ni moja ya masomo muhimu sana kwa mtoto/kijana kwani humpatia maarifa kuhusu anavyoweza kukabiliana na changamoto za maisha, na kupata uwezo wa kuziona fursa, na kuzikamata. Stadi hizi hujumuisha mbinu zinazoweza kumsaidia kuyafanya maisha yake yawe na uelekeo ulio sahihi, kujitambua, kuwa na nidhamu, na kufanya vitu sahihi, mahala sahihi na wakati sahihi.

Nimesema huu ni wajibu wako mzazi, kimsingi. Sasa, usipokuwa makini utajikuta unazodolewa na mwanao mwenyewe, na naomba usije kumlaumu mtu, pale mwanao atakapoanza kujitambua, kupata akili za ki-utu uzima, na kuanza kuhoji mambo. Watoto hawa hugundua kuwa udhaifu au upungufu wao katika maadili, kumbe umesababishwa na uzembe wa wazazi wao walioshindwa kutimiza wajibu.

Kiukweli wapo wazazi wanaojitahidi kuwalea watoto au vijana wao kimaadili lakini watoto hushindwa kuzingatia maelekezo, wakawa wakaidi, na kuishia kuharibika. Hii ni habari nyingine… inayopaswa kushughulikiwa ki-upekee. Lakini wapo pia wazazi, ambao kwa uzembe tu, huwafanya watoto wao wakose maarifa muhimu kwa maisha yao. Sasa, watoto wakijitambua, na wakagundua hili, mzazi kuwezi kukwepa kuzodolewa!

Hapo zamani kidogo, katika jamii za kiafrika kulikuwa na mila zilizohakikisha mtoto kabla ya kuingia katika umri wa kiutu uzima anapata maarifa au stadi ambazo zinalenga kumfanya awe mwanajamii anayejielewa, kujitambua na kuwajibika. Kulikuwa na ‘shule maalum’ za malezi ya vijana, kupitia matamasha ya jando na unyago. Cha kusikitisha, mila hizi zinazidi kumomonyoka kutokana na kasi ya ‘maendeleo’ ya utandawazi.

Hivi sasa, kutokana na sababu kadhaa, baadhi ya wazazi hawapati nafasi au hawajali au labda hawamudu kuwapatia watoto wao stadi hizi, na sasa baadhi ya vijana wameanza kulalamikia kuikosa haki yao hii. Wanawalaumu wazazi wao kwa uzembe au kushindwa kuwajibika.

Katika hili, kijana mmoja Alexis, anasema, “wazazi wangu walishindwa kunifundisha stadi muhimu za maisha, na sasa nimegundua kwa kuzikosa stadi hizo utotoni, naona nimepungukiwa vitu muhimu sana katika maisha yangu. Nilipowauliza kwa nini hawakujali kunipa maarifa hayo, walijibu kwamba hata wao hawakuwahi kufundishwa na wazazi wao. Nilisikitika!”

Kijana mwingine Gavin anasema, “najua wapo wazazi wanaowafundisha watoto/vijana wao stadi za maisha…lakini najua pia kuwa wapo ambao hawana muda huo kwa kuwa hata wao hawakuwahi kufundishwa, au hata kama walifundishwa…wao hawana uwezo wa kuwafundisha watoto wao, na hili ni tatizo! Hata hivyo, najua pia kuna watoto ambao ni wakaidi, hawataki kujifunza,…pamoja na jitihada za wazazi wao”

Akitoa maoni katika mdahalo mmoja, kijana Bitter anasema, “nimekuzwa na wazazi ambao msisitizo wao mkubwa ulikuwa kusoma kwa bidii ili nifaulu masomo yangu vizuri, na waliniambia kila mara, ‘elimu ndio kila kitu’! Kwa kuzingatia maelekezo yao, nimekuja kugundua kuna maarifa muhimu sana, nje ya darasa, sikuweza kuyapata, mfano ujenzi wa fikra tunduizi, uthubutu, ujasiri, uchambuzi, kutoa maamuzi na uwezo wa kujitegemea.

Akionesha madhara mengine ya kunyimwa stadi hizi, Kijana Bitter anasema, “kuna kitu muhimu ambacho nimekuja kugundua hivi karibuni, ambacho kimenisononesha sana. Nimegundua sikupewa hata stadi zinazonigusa moja kwa moja; kama kufanya usafi, kuoga, kupika, kufua, na hata kupiga mswaki. Sikuwahi kufikiria kitu hiki zamani, kwamba vitu hivi kumbe huwa vinafundishwa na wazazi majumbani, inasikitisha!”

Kijana mwingine anasikitika kwa kusema, “jinsi ninavyokuwa mtu mzima na kuanza kutambua mambo ndivyo ninavyobaini kuwa wazazi wangu hawakuwajibika ipasavyo kwangu. Ukweli, hawakunipa zana au ‘silaha’ kwa ajili ya kuyajenga na kuyalinda maisha yangu. Kuna mambo nahangaika kuyafanya mwenyewe hivi sasa, ingawa ukweli napata wakati mgumu, na wazazi wangu hawana namna ya kunisaidia, wameshachelewa!”

Sasa, ukifuatilia maoni haya utakubaliana na mimi kuwa baadhi ya watoto wanaofika katika umri wa kiutu uzima wakiwa hawana stadi muhimu za maisha, hawakutaka kuwa hivyo. Walijikuta hivyo ukubwani na baadaye kugundua kuwa kumbe wazazi wao kuna kitu hawakuwafanyia. Hata hivyo vijana hawa hawapaswi kukata tamaa na kuacha kufanya jambo. Wanapaswa kujiongeza.

Mchangiaji mmoja katika mjadala kuhusu suala hili anasema, “nawasikitikia na kuwapa pole vijana wote waliokosa stadi muhimu za maisha, kwa kuwa wazazi wao walishindwa kuwajibika. Hata hivyo, pamoja na wazazi kukunyima stadi hizi, angalau wape shukrani, kwani walikulea ukawa na afya njema, na pengine kuhakikisha umepata elimu nzuri ya darasani.”

“Kwa kuwa sasa wewe ni mtu mzima, na sasa unajitambua, na unatambua nafasi yako katika jamii, unapaswa kuchukua hatua haraka! Acha kulalamika na badala yake anza kujifunza mwenyewe vitu vyote ulivyovikosa utotoni. Hili linawezekana, na wapo waliobadili maisha yao kabisa hadi watu wakawashangaa!”

Anasema, “ni kweli kama mtoto, ulipaswa kupendwa, kupewa malezi bora, kufundishwa maadili n.k. Lakini kama hukupata bahati hii utotoni, usianze kulia-lia. Kubali hili limeshatokea, kilichobaki ni kufanya kitu. Cha kuzingatia ni kwamba stadi yoyote unayoihitaji sasa, ambayo hukuipata utotoni, jiwekee mpango na mkakati wa kuipata. Na hata wale waliopatiwa stadi hizi, bado kuna haja ya kujifunza zaidi ili kujenga umahiri.”

Hatua ya kuchukua: wakati kijana unaweza kuungwa mkono, na kusikitikiwa na kila mtu, pale utakapoonesha kusononeshwa na matokeo ya wazazi wako kushindwa kuwajibika na kukupatia maarifa muhimu kwa ajili ya maisha yako, kwa upande mwingine unapaswa kukumbuka msemo huu, ‘yaliyopita si ndwele, tugange yajayo’!

Ukishalijua hili, una wajibu sasa wa kulibeba jukumu hili wewe mwenyewe. Unapaswa kutafuta njia mbalimbali za kukupatia maarifa na stadi zote ulizozikosa. Uzuri, tayari sasa unajua unahitaji nini katika maisha yako, au unataka kuwa nani, na unataka kukuza vipaji gani, hivyo chukua hatua!

Wakati fulani inabidi tuwasamehe wazazi wetu kwa kushindwa kuwajibika. Wazazi wengine walijaribu kufanya walichoweza, kulingana na jinsi wao wenyewe walivyolelewa, habati mbaya hawakufikia viwango stahiki. Pamoja na hayo, ujumbe muhimu kwao ni kwamba wanapaswa kuujua ukweli huu, na kujifunza kwamba walishindwa kutimiza wajibu.

Mzazi unapaswa kujua kuwa suala sio kuzaa na kumleta mtoto duniani – hapana. Kilicho muhimu ni kuhakikisha kuwa mtoto, mapema kabisa, anasimamiwa ipasavyo ili aweze kuwa na maarifa na taarifa zote muhimu kumfanya awe kijana anayejitambua, kufanya mambo kwa usahihi na kuyamudu vyema mazingira yake. Usipofanya jukumu lako hili ujue utalaumiwa, utaaibika na utazodolewa hata na mwanao mwenyewe!

Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasirimali kivitendo.

Anapatikana kwa e-mail: nzyy2001@gmail.com; Simu 0718219530

Nini Nafasi Ya Nidhamu Kufanikisha Biashara au Kazi?

Habari rafiki,

Sababu kubwa inayofanya watu wachelewe kufanya – waahirishe kufanya – au wasifanye kabisa kazi au majukumu waliyopanga au kupangiwa kufanya ni moja tu…ukosefu wa nidhamu!

Hili huonekana wazi katika kazi mbalimbali za kuajiriwa, ambapo, mwajiriwa asipotimiza wajibu wake kabisa au akichelewa kufanya kazi yake kwa ubora au muda uliopangwa, anaadhibiwa kwa mujibu wa taratibu za kinidhamu.

Kwa hiyo kumbe nidhamu ni jambo muhimu sana katika kufanikisha utendaji wa kazi yoyote.

Shule ni moja ya taasisi zinazomjenga mtoto kuwa na maadili na nidhamu binafsi

Kifupi, nidhamu ni ile nguvu ya ndani iliyojengeka kwa mtu inayomsukuma mtu huyo kufanya mambo kwa wakati, umakini, ujuzi na usahihi wa hali ya juu ili kufikia kusudio fulani.

Yaani nidhamu ni kitu kinachotoa msukumo au uwezo binafsi unaomwezesha mtu kuinuka na kufanya kitu au kazi anayopaswa kufanya – na aifanye bila kujali anajisikia kufanya au la.

Nidhamu inaelezewa pia kama ile hali ya mtu kuwa na utii, heshima, unyenyekevu na umakini katika kufuata kanuni, sheria na miongozo mbalimbali ili kuyafikia malengo tarajiwa.

Kwa sababu hiyo, ndio maana mtu mwenye kiburi na dharau; ambaye hafuati sheria na kanuni; na anayefanya mambo ya aibu mbele za watu, husemwa kuwa hana nidhamu. Nidhamu humfanya mtu aheshimike na aonekane wa kipekee tofauti na wengine.

Watu wengi hupenda kupata matokeo mazuri katika kazi, biashara, masomo, ndoa na mambo ya kijamii. Hata hivyo, tatizo linalowakabili wengi, wakashindwa kupata matokeo hayo, ni kushindwa kuwekeza katika kujenga nidhamu binafsi.

Hebu mfikirie mtu anayeamka mwenyewe saa kumi alfajiri akikatiza usingizi wake – akitoka nje usiku wenye baridi kali au mvua ikinyesha – ili akafanye kazi au jukumu alilojipangia au kupangiwa kufanya.

Huyu, sio kwamba anafanya hivyo kwa sababu anajisikia sana kufanya kazi hiyo; au sio kwa vile ni muhimu sana kazi hiyo kufanyika; au siyo kwa sababu asipofanya kazi hiyo atamuudhi mtu fulani – hapana.

Kwa sababu… wapo watu ambao hukaidi au kuchelewa kufanya kazi zao muhimu au kazi walizopangiwa kufanya na viongozi wao kwa sababu hawajisikii tu; na wakati mwingine wako tayari hata kuadhibiwa kwa kosa hilo.

Kwa hiyo, kitu kinachomfanya mtu ainuke na kujituma kufanya kazi au kutimiza wajibu bila kujali mazingira yanayomzunguka ni nidhamu binafsi aliyojijengea yeye mwenyewe.

Utakuta mtu huyu kabla ya kulala usiku, anajipa ‘ahadi’ ya dhati kabisa kuwa ni lazima aamke alfajiri sana, bila kujali mazingira, na aanze kufanya kazi aliyojipangia au kupangiwa kufanya.

Ile ahadi anayojipa mtu – kwamba ni lazima ainuke ili afanye kitu fulani bila kujali hali – ndiyo nidhamu yenyewe – na ndiyo msukumo au kichocheo kinachomwezesha kuinuka na kufanya.

Nidhamu ni chumvi au kirutubisho kinachounganisha malengo mazuri aliyojiwekea mtu na bidii anayoweka katika kutekeleza au kuyafikia malengo hayo.

Nidhamu ni nguvu au msukumo unaokuwezesha kuwa na uthibiti wa mambo au maamuzi yako mwenyewe pasipo kulazimishwa na nguvu ya mazingira yanayokuzunguka.

Nidhamu hujenga nguvu ya mwili na akili, na hali ya kujiamini, na humfanya mtu ajipambanue miongoni mwa wengi kama mtu aliyekamilika na kukomaa.

Kwa hiyo, hatua ya kuchukua leo ili uweze kufanikisha kazi au biashara yako ni lazima ujenge nidhamu binafsi. Ni nidhamu ndiyo itakupa msukumo wa kutenda kwa wakati, umakini, ujuzi na usahihi wa hali ya juu ili kuyatimiza malengo yako.

Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasirimali kivitendo.

Anapatikana kwa e-mail: nzyy2001@gmail.com; Mobile: 0718219530

Utafiti Kupita Kiasi Huzorotesha Utekelezaji

Habari rafiki,

Karibu tena katika mfululizo wa makala zangu zenye lengo la kuelimishana kuhusu masuala ya ujasiriamali, ubunifu na stadi za maisha.

Katika makala hii nitazungumzia tathmini ya wazo la biashara na yatokanayo na tathmini hiyo; na nitaongozwa na msemo wa kiswahili usemao, “ukimchunguza sana bata huwezi kumla.”

Nimeandika huko nyuma kuwa unapopata wazo la biashara unakuwa umeliunda wazo hilo kichwani, na unaona jinsi unavyoweza kulitia wazo hilo katika vitendo, na jinsi unavyoweza kufanikiwa kupata matokeo.

Hata hivyo wataalamu wa biashara wanashauri kwamba mjasiriamali apatapo wazo au mawazo kadhaa ya biashara yanayomtia hamasa, anapaswa kujiridhisha kwanza kabla ya kuanza utekelezaji kivitendo.

Yaani mjasiriamali anatakiwa kufanya utafiti ili kukusanya taarifa muhimu zitakazompatia uelewa wa kutosha wa biashara na mazingira yake.

Akijiridhisha kwamba tayari amepata taarifa hizo na kuzielewa – basi anaweza kuanzisha vitendo.

Ukweli ni kwamba kufanya utafiti ni hatua muhimu katika kuifanikisha biashara. Utafiti huzalisha taarifa na takwimu ambazo humpatia mjasiriamali nguvu na ujasiri wa kuanza utekelezaji.

Ukifika kituoni usiendekeze mno uchunguzi wa mabasi…utaishia kuachwa!

Hata hivyo, utafiti au uchunguzi unaofanyika ukizidi kiasi unakwamisha uwezekano wa wazo zuri kutiwa katika matendo. Kwa mujibu wa Mwanasaikolojia Barry Schwartz, utafiti haupaswi kwenda ndani sana kwani utakwamisha utekelezaji.

Kuchukua muda mrefu katika hatua ya kufikiri, kukusanya na kuchambua taarifa kuna madhara ya kuchelewesha au kukwamisha kabisa utekelezaji. Na kitu chochote kinachosababisha hatua stahiki isichukuliwe ni adui wa mafanikio yako.

Maana yake ni kwamba mjasiriamali anakuwa na nia nzuri tu ya kupata taarifa nyingi na muhimu kuhusu uwezekano wa biashara husika kufanikiwa ili akifanya maamuzi – yawe bora zaidi.

Hata hivyo, kinachojitokeza ni kwamba jinsi anavyokusanya taarifa nyingi zaidi ndivyo anavyotengeneza ugumu katika kutoa maamuzi ya utekelezaji. Ni ukweli pia kuwa taarifa nyingine humtia mhusika woga au kumkatisha tamaa.

Sasa, kama kufanya utafiti mwingi huzorotesha utekelezaji – kumbe jambo hili linapaswa kuangaliwa kwa tahadhari. Hii ina maana kuwa pamoja na umuhimu wa utafiti ipo haja ya kuufanya utafiti huu kwa kiasi tu ili kuacha nafasi ya kufanyika kwa haraka maamuzi ya utekelezaji.

Ndiyo maana mtaalamu mmoja wa ujasiriamali anasema kwamba kitu cha msingi na muhimu kabisa baada tu ya kupata wazo – ni uamuzi wa kuanza utekelezaji mara moja.

Anasema, “fanya utafiti kiasi ili kupata ushahidi fulani kuwa wazo lako ni la maana na lina mashiko. Ukishapata ushahidi huu basi anza utekelezaji, tena usisitesite.

Hili linatiwa nguvu na kaulimbiu ya kampuni ya viatu vya michezo, Nike, inayosema ‘just – do – it! Yaani; ‘usichelewe, anza kufanya’. Maana yake ni kwamba kama una wazo zuri na kila linavyozunguka kichwani mwako linakupa ushawishi ulifanye – basi anza kulifanya haraka.

Wataalamu wa saikolojia wanasema kuwa ukianza mapema kulitia wazo lako katika vitendo, akili na mwili vinapata msukumo wa ziada wa kuendelea kulifanya jambo hilo.

Vilevile kwa kuanza mapema kulitia wazo lako katika vitendo unapata nafasi nzuri ya kujipima ili kuthibitisha kama unalipenda wazo hilo na unalifurahia; lakini pia unaendelea kujifunza huku ukiendeleza utendaji.

Kimsingi wazo hilo ni la kwako na huenda umechukua muda mrefu kabisa kulifikiria na kulitafakari kabla ya kuamua kuwa ni wazo la maana ambalo unapaswa kulitia katika vitendo.

Ushauri kwa wajasiriamali ni kwamba ni jambo zuri na la maana kufanya utafiti wa wazo lako kabla ya kulitia katika utekelezaji. Hata hivyo utafiti huu usiwe wa kina mno kiasi cha kukukatisha tamaa au kuchelewesha utekelezaji.

Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasirimali kivitendo.

Anapatikana kwa e-mail: nzyy2001@gmail.com

Tukimuiga Huyu – Mafanikio Hayatachelewa

Habari rafiki,

Makala ya leo itazungumzia kitu muhimu sana katika jitihada za kujikwamua katika maisha kupitia ujasiriamali. Kitu hicho ni uthubutu na kuchangamkia fursa.

Utakumbuka, tarehe 9 mwezi Mei mwaka huu (2019) ilikuwa ni siku muhimu katika historia ya nchi yetu, ambapo tulishuhudia mfanyabishara maarufu, Mzee Reginald Mengi, akizikwa kijijini kwao Kisereni, Machame.

Tukitumia vizuri bongo zetu tutapata mahala pa kuanzia kuyafikia  mafanikio

Umuhimu wa siku ile ulitokana na sifa alizokuwa nazo mzee huyu hasa katika kujitoa na kuwasaidia watu wenye shida mbalimbali, na hasa walemavu. Mengi ametuachia urithi katika mambo mengi ikiwa ni pamoja na udadisi, ujasiri na uwezo wa kuthubutu katika jitihada za kujinasua kutoka katika umaskini.

Kutokana na sifa hizi, watu wengi ndani na nje ya Tanzania walivutiwa na mawazo na matendo yake, na hata alipofariki, shughuli ya maziko ilikuwa kubwa, na watu kwa maelfu walihudhuria kutoa heshima zao za mwisho.

Wakati wa mazishi, huko Machame, wapo watu walikwenda huko kwa lengo moja tu la kumuaga mtu waliyempenda, basi! Lakini wapo watu wenye hulka ya ujasiriamali ambao nao walikwenda.

Watu hawa, pamoja na upendo waliokuwa nao, na hamu ya kutoa heshima zao kwake, lakini waliona kitu cha ziada katika msiba huu. Waliona fursa ya biashara; yaani, kama alivyokuwa Reginald Mengi, walipata wazo kuwa hata msiba ni fursa ya biashara.

Mjasiriamali unapaswa kuwa na maono na uwezo wa kufikiri haraka, kutengeneza wazo, kulichuja – ili kuona kama wazo hilo linaweza kuzaa fursa ya kupata pesa. Hili hata Mzee Mengi alilisisitiza sana.

Sasa, katika hili, yupo mjasiriamali mmoja raia wa Uganda, Molakya Godfrey, aliyetengeneza pesa nyingi kupitia msiba huu – pale alipoungana na waombolezaji wengine huko kijijini Kisereni.

Molakya alisikia na kuona taarifa za kifo cha Mzee Mengi kupitia Facebook. Aliona aina ya mapokezi aliyopewa kuanzia uwanja wa ndege, jinsi watu walivyojipanga barabarani na baadaye siku ya kuagwa, jijini Dar-es-salaam, kabla ya kupelekwa kijijini kwao.

Molakya aligundua kuwa Mzee huyu ni kipenzi cha watu wengi ndani na nje ya Tanzania, na hivyo alipata wazo kuwa kuna kitu anaweza kufanya kutengeneza pesa kupitia msiba huu. Wakati wengine waliwaza msiba tu, yeye alienda zaidi ya hapo, aliona kuna fursa pia.

Molakya aliamua kuichangamkia fursa hii bila ajizi. Hivyo alikuna kichwa na kugundua bidhaa ambazo aliamini akizitengeneza zitaendana na shughuli ya msiba na vilevile zitavuta hisia za waombolezaji, na hivyo zitapata soko.

Alitengeneza bidhaa kadha wa kadha, ikiwa ni pamoja na vifaa vya kubebea funguo (key holders) na beji za kuvaa shingoni zenye ujumbe na michoro ya kuvutia iliyopambwa na picha ya marehemu Mengi. Alitengeneza pia picha mbalimbali za Reginald Mengi akiwa katika matukio fulani, na zingine akiwa na familia yake.

Anasema, “nikiwa Mganda nimeona niichangamkie fursa hii, kupitia kwa mtu anayependwa na Watanzania wengi kujitengenezea kipato kwa ajili ya maisha yangu.”

“Na ninafanya hivi nikiwa nayaenzi maisha yake ambayo yaliongozwa na falsafa ya kuzitafuta, kuziona na kuzichangamkia fursa, kama yeye mwenyewe alivyoamini na kufanya.” Alisema Molakya.

Ki ukweli, wazo lake lilizaa matunda kwani wananchi na wageni waliokuwa wamejipanga katika mistari kutoa salamu zao za mwisho kwa marehemu walizichangamkia sana bidhaa hizo, kwani kila mmoja alitamani kuondoka katika msiba huo akiwa na kumbukumbu muhimu ya tukio hilo.

Katika hili Molakya anatupa somo muhimu sana. Sifa kuu ya mjasiriamali, kama alivyokuwa Mzee Mengi, ni uwezo wa kufumbua macho na masikio – kuona na kusikia, ili kugundua fursa zilizojificha na kuzikamata – na mwisho kuzibadili fursa hizo kuwa kitu halisi chenye thamani.

Tumuige Molakya kwa yale aliyofanya katika msiba huu ambapo pamoja na kushiriki kikamilifu kama muombolezaji, lakini pia alitumia fursa hiyo kujitengenezea kipato kwa ajili ya kuboresha maisha yake.

Hivyo, kama alivyofanikiwa Molakya, kila mtu anaweza kufanikiwa, na hivi ndivyo nguvu ya kuthubutu inavyowea kuleta matokeo bora na mazuri katika maisha yetu.

Soma pia: Ukiwa Na Macho Ya Namna Hii, Utatengeneza Fursa Nyingi za Biashara

Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasirimali kivitendo.

Anapatikana kwa simu: 0718219530; e-mail: nzyy2001@gmail.com

Haya Ndiyo Manufaa Ya Kuanza Utekelezaji Haraka!

Habari rafiki,

Kuna methali ya Kiswahili inayosema, “maji ukiyavulia nguo huna budi kuyaoga.” Maana ya methali hii, kwa muktadha wa ujasiriamali, ni kwamba ukishapata wazo, ukalifanyia utafiti na kuona linaibua fursa ya kibiashara, hutakiwi kuanza kujizungushazungusha.

Unachotakiwa ni kuanza utekelezaji mara moja. Nimeandika huko nyuma kuwa baada ya kuridhika kuwa wazo lako lina tija unaweza kuamua kuanza utekelezaji. Lakini, kuamua peke yake hakutoshi. Wapo walioamua – lakini hawakufanya kitu!

Sasa ninachosisitiza hapa ni kule kujenga ujasiri wa kuanza mara moja. Yaani ukishajiridhisha tu, basi anza utekelezaji. Usianze kusubiri hadi kila rasilimali itimie. Kuna baadhi ya vitu unaweza usiwe navyo mwanzoni, lakini ukishaanza utashangaa vinaanza kujitokeza.

Hapa ndipo umuhimu wa kuanza kidogokidogo unapoleta maana. Anza kidogo-kidogo, na kwa kufanya hivyo unajenga hamasa binafsi, ndani yako, ya kufanikiwa. Uthubutu na hamasa unayoijenga ina tabia ya kusababisha milango iliyoonekana migumu, kuanza kufunguka yenyewe.

Ukishajitupa majini utagundua kumbe hauko peke yako – wapo watu wanakuona – pokea mikono yao!

Yaani unapoanza tu utashangaa kuona unaanza kupata marafiki ambao hukutarajia kuwa na uhusiano nao. Wengine ni watu wanaofanya biashara kama yako, wanakuja wenyewe tu; na bila hiyana wanakupa miongozo mbalimbali. Hii inatokea, na ukiwa makini utanufaika.

Ukiwa mnyenyekevu, utaona unaanza kupata taarifa au maarifa kutoka kwa watu waliowahi kufanya biashara hiyo huko nyuma. Watakujulisha wateja wako wapi, tabia zao, na nini ufanye au usifanye, ili kuweza kuliteka soko.

Utaanza kujua kwa undani taratibu za kisheria zinazohusiana na biashara yako na nini ufanye au usifanye ili usiingie kwenye mitafaruku na serikali, taasisi au jamii inayokuzunguka.

Kupitia wateja au majirani zako, unapata fursa ya kuanza kuwajua vizuri washindani wako wa kibiashara, wana uwezo gani na wanatumia mbinu gani kunasa wateja na kupambana na changamoto zinazojitokeza.

Utaanza kuwajua zaidi wagavi (suppliers) wa bidhaa zako, na usishangae kuona wengine wanakuja wenyewe tu kuanzisha uhusiano na kujua mahitaji yako ya bidhaa, ili ukihitaji wakuletee.

Kama unafanya biashara ya kuzalisha bidhaa, unaanza kupata taarifa za mashine, malighafi na vipuri bora, rahisi na vya bei nafuu, kwa ajili ya kuzalisha bidhaa yako.

Utashangaa unapoanza tu hata kama hukujua utapata wapi wafanyakazi wenye sifa, unaanza kupata taarifa za wafanyakazi wanaoweza kukusaidia kuendesha biashara. Inabaki kazi yako tu kuwachunguza na pengine kuchagua.

Unaanza kupata taarifa za kina kuhusu eneo lako la biashara, changamoto zake, na jinsi unavyoweza kuzitatua. Watu usiotarajia wanakuletea taarifa hizi, wanakuachia wewe uamuzi wa nini cha kufanya.

Unaanza kujua kwa usahihi bei za malighafi au bidhaa, na wapi zinapatikana kwa wingi, ubora zaidi na unafuu wa bei.

Mwanzo ni mgumu. Huwezi kuanza biashara kwa kuwa na wateja wengi mara moja. Lakini ukishaanza tu unaanza kujenga mtandao wako. Kwa hiyo, jinsi unavyokua ndivyo mtandao unavyokuwa mkubwa, mradi tu ujuwe mbinu za kuujenga na kuukuza.

Unaanza kujua udhaifu ulionao au walionao wasaidiazi wako. Udhaifu huu utaujua kupitia kwa wateja, washindani na hata wagavi wa bidhaa. Unaanza pia kugundua vihatarishi vya biashara yako na changamoto zilizomo.

Kwa hiyo, unapoanza kufanya biashara kwa vitendo ujue kuna watu wanakufuatilia hata kama wewe mwenyewe huna habari. Wapo wenye nia nzuri na nia mbaya. Umakini unatakiwa katika hili. Ukiwa mjanja utapata watu watakaokusaidia, kwa mfano vyanzo vya mtaji n.k.

Mwisho, mjasiriamali hapa unahimizwa kujenga uthubutu. Yaani ukishapata wazo, ukaridhika kuwa ni wazo zuri, hiyo ni fursa tayari! Hivyo kinachofuata ni kuanza haraka. Ukishaanza tu utashangaa kuona mambo yanajitokeza bila hata kutarajia, ambayo yanaipalilia njia yako kuelekea mafanikio. Tumia akili yako vizuri kuchuja kila kitu na kufanya kilicho sahihi.

Soma pia: Ukishaiona Fursa, Acha Kusitasita – Anza Mara Moja!

Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasirimali kivitendo.

Anapatikana kwa e-mail: nzyy2001@gmail.com

Jinsi Ya Kupunguza Gharama Za Biashara Yako…(2)

Habari rafiki,

Makala iliyopita ilikuwa ni sehemu ya kwanza ya mada hii. Kama utakumbuka, nilizungumzia gharama za uendeshaji wa biashara – na nikasema kuna gharama za aina nyingi ambazo mfanyabiashara unapaswa kuzifahamu ili unapopiga hesabu za biashara yako uweze kujua kwa usahihi mchango wa gharama hizo katika faida au hasara utakayopata.

Chunguza biashara yako uone ni gharama zipi unaweza kuzipunguza – fanya hivyo!

Nikasema tena kuwa baada ya kuzijua gharama za uendeshaji wa biashara yako, kinachofuata ni kupanga mikakati ya kuzidhibiti au kuzipunguza. Hii inatokana na ukweli kwamba mfanyabiashara haupaswi kuidharau pesa yoyote inayoingia au kutoka katika biashara yako. Kwani kila pesa ina maana!

Kwa hiyo, nilihimiza kuwa ni wajibu wako kila baada ya muda fulani kupima gharama zilizotumika na kufanya tathmini kujua kama gharama zako ni sahihi na zenye ulazima, na kama kuna chochote cha kurekebisha, kifanyike ili kupunguza gharama hizi.

Katika makala iliyopita nilikupatia njia nne za kudhibiti au kupunguza gharama za uendeshaji wa biashara. Sasa makala hii itakupatia njia sita zaidi kama ifuatavyo:

Tano, punguza gharama za matangazo. Utakumbuka kuwa moja ya mikakati ya biashara ni matangazo. Hata hivyo usikurupuke katika hili.

Kama ni lazima utangaze kwa malipo, tafuta chombo cha gharama nafuu zaidi; kwa mfano, kipi ni rahisi zaidi kati ya vipeperushi, gazeti, radio, TV au mitandao ya kijamii? Kama unaweza kujichanganya na watu, au networking, je, unaweza kutumia njia ya mdomo na ikalipa? Chunguza, chukua hatua.

Sita, fanya kazi kwa muda uliopangwa, yaani usipoteze muda bila sababu. Muda uliopotea hovyo ni gharama iliyojificha, au ni pesa iliyopotea. Panga muda wa kuanza kazi, kupumzika na kumaliza, kwa kila mmoja. Punguza vitu vinavyoiba muda wa kazi, mfano kupiga soga au stori.

Saba, punguza wigo wa utoaji huduma. Wakati fulani mfanyabiashara anakuwa ameatamia vitu au tenda nyingi peke yake hadi zinamwelemea. Ikitokea hivi matokeo yake ni kutoa huduma duni, zisizo za haraka na wakati fulani gharama zake zinakuwa kubwa. Inashuriwa kugawa kazi au tenda hizi kwa wenzio ili kupunguza gharama za uendeshaji.

Nane, boresha matumizi ya nafasi ofisini, katika karakana au kiwandani. Kama umepanga ofisi, tumia nafasi kwa umakini, na kama inawezekana rudisha nafasi isiyotumika kwa mwenyewe. Tunza vifaa, mafaili, fenicha na bidhaa kwa umakini ili nafasi itumike kwa kiwango cha juu. Tumia nafasi au chumba kimoja kwa matumizi zaidi ya moja.

Tisa, ajiri wafanyakazi kulingana na mahitaji halisi na kwa kuzingatia mchango wa kila mmoja ukilinganisha na gharama zao. Usiajiri mfanyakazi mwenye elimu au ujuzi mkubwa bila sababu kwani unaweza kulazimika kumlipa zaidi.

Ajiri mtu mmoja mwenye ujuzi na uwezo wa kufanya kazi mbili au tatu (multi-tasking). Mfano dereva mwenye ujuzi wa ufundi wa mashine au magari n.k. Wasaidie wafanyakazi kuwa na afya bora, kwani afya duni ni hasara kiutendaji.

Kumi, punguza gharama kwa kujali vitu vinavyoonekana vidogovidogo. Kumbuka msemo wa ‘bandubandu humaliza gogo’ .

Kwa mfano, jenga tabia ya kutumia taa zinazotumia umeme kidogo, energy servers, lakini pia taa au feni zisiwashwe bila sababu. Ikibidi tumia karatasi pande zote mbili. Tumia usafiri wa umma, badala ya gari la ofisi kwa kila safari. Dhibiti matumizi ya maji yasipotee bure.

Ndugu yangu, hizi ni baadhi tu ya njia za kupunguza gharama za uendeshaji wa biashara, ziko nyingi; hivyo ichunguze biashara yako uone gharama zinazojitokeza, kisha ziorodheshe na uzifanyie tathmini stahiki.

Hatua ya kuchukua: mjasiriamali unapaswa kuwa makini sana katika kuzijua au kuzibaini gharama za biashara yako na kupanga mikakati ya kuzidhibiti au kuzipunguza kwani zina athari kubwa kwa faida ya biashara yako.

Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasirimali kivitendo.

Anapatikana kwa simu: 0718219530; e-mail: nzyy2001@gmail.com

Jinsi Ya Kupunguza Gharama Za Biashara Yako…(1)

Habari rafiki,

Karibu tena katika makala nyingine inayolenga kukupatia maarifa ya ujasiriamali, ubunifu na stadi za maisha.

Ukiweza kupunguza gharama (costs) za uendeshaji – unakaribisha mafanikio

Ukiwa mjasiriamali au mfanyabiashara kuna gharama ambazo utakutana nazo, na hakuna biashara yoyote ambayo haihusishi gharama. Kwa hiyo ni muhimu sana kwa mfanyabiashara kuzifahamu gharama zinazohusiana na biashara zao.

Katika biashara kuna aina mbalimbali za gharama. Zipo zinazoonekana wazi; na zipo pia zilizojificha, ambazo ni vigumu kubainika kirahisi.

Mfano wa gharama zilizo wazi ni pamoja na gharama za bidhaa au malighafi, mishahara ya wafanyakazi, mashine na vifaa vya uzalishaji; na gharama za umeme, maji na usafiri. Gharama zilizojificha ni pamoja na riba, tozo (charges) na kamisheni za benki; gharama za miamala ya simu; na gharama ya bidhaa iliyoharibika.

Mfanyabiashara unapaswa kuzijua gharama hizi ili unapopiga hesabu za biashara yako uweze kujua kwa usahihi mchango wa gharama hizo katika faida au hasara utakayopata. Kumbuka faida au hasara katika biashara inapatikana kwa kutoa gharama kutoka kwenye mapato.

Katika biashara, kuna gharama zinazobadilika na zile zisizobadilika- kutegemeana na kiwango cha uzalishaji wa bidhaa au michakato ya uendeshaji wa biashara.

Kwa mfano, kama unazalisha sabuni za mche kiwandani kwako, ukizalisha miche 100 unaweza kuingia gharama ya jumla ya shilingi 20,000 (malighafi, umeme, maji n.k). Lakini ukizalisha miche 1000 gharama inapanda na kuwa shilingi 180,000. Huu ni mfano wa gharama zinazobadilika kutegemeana na ongezeko la uzalishaji.

Gharama zisizobadilika ni zile zinazobakia vilevile kila mwezi bila kujali kiasi cha biashara au uzalishaji uliofanyika. Kwa mfano, kodi ya pango, mishahara ya wafanyakazi, malipo ya bima n.k.

Baada ya kuzijua gharama za uendeshaji wa biashara, sasa tujikite katika kupanga mikakati ya kuzidhibiti au kuzipunguza.

Kumbuka, katika mazingira magumu ya biashara kila pesa ina thamani. Kwa hiyo mfanyabiashara unapaswa kuwa makini sana. Yaani, hata pesa ndogo kabisa iingiayo kama mauzo, au pesa kidogo inayotoka kama gharama; vina maana sana katika tathmini ya mafanikio ya biashara hiyo.

Kwa hiyo, ni wajibu wako kila baada ya muda fulani kupima gharama zilizotumika na kufanya tathmini. Kila mara jiulize je, gharama zangu ni sahihi na zenye ulazima? Je, kuna chochote cha kurekebisha ili kupunguza gharama hizi? Jibu utakalopata lifanyie kazi haraka.

Makala hii itakupatia njia nne kati ya kumi za kudhibiti au kupunguza gharama za uendeshaji wa biashara; na makala ijayo itakupatia njia sita.

Moja, punguza gharama za manunuzi ya bidhaa. Hapa unashauriwa kutafiti kidogo na kisha kununua katika maduka au wagavi wenye bei nafuu, au wanaotoa punguzo (discount) ukinunua bidhaa nyingi.

Mbili, punguza gharama za usafirishaji wa bidhaa. Unashauriwa hapa kuwatumia wasafirishaji wenye bei nafuu. Tafuta usafiri unaolingana na ukubwa au uzito wa bidhaa zako, au changia usafiri na mwenzio mnaofanyia biashara sehemu moja.

Tatu, punguza gharama za uzalishaji. Hapa unashauriwa kukodi eneo au chumba cha biashara chenye unafuu kinacholingana na aina na ukubwa wa biashara yako. Malighafi ya uzalishaji itumike kwa uangalifu ili yote itumike, isije ikaharibika au kwisha muda wake.

Vilevile, malighafi iliyobaki, au bidhaa, zitunzwe vizuri zisiharibike na kuleta hasara. Unapaswa pia kusimamia vizuri wafanyakazi na rasilimali nyingine ili zitumike kwa kiwango cha juu katika uzalishaji au utoaji huduma.

Nne, punguza matumizi ya fedha. Ushauri hapa ni pamoja na kujiepusha na mikopo isio muhimu. Ukilazimika kukopa, angalia riba ni kiasi gani, na je biashara yako ina uwezo wa kumudu riba hiyo bila kuathiri mzunguko wa fedha?

Kama umeamua kukata bima ya biashara yako, chunguza gharama yake ili upate bima yenye tija lakini yenye unafuu.

Hatua ya kuchukua: mjasiriamali unapaswa kuwa makini sana katika kuzijua au kuzibaini gharama za biashara yako na kupanga mikakati ya kuzidhibiti au kuzipunguza kwani zinaathiri faida ya biashara yako. Makala ijayo tutamalizia njia zilizobaki.

Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasirimali kivitendo.

Anapatikana kwa simu: 0718219530; e-mail: nzyy2001@gmail.com

Jinsi Vifungashio Vinavyoongeza Thamani Ya Bidhaa Yako

Habari rafiki,

Karibu tena katika makala nyingine inayolenga kukupatia maarifa ya ujasiriamali, ubunifu na stadi za maisha.

Nianze makala ya leo kwa kusema kwamba kufikiri ni kitu muhimu sana kwa binaadamu. Na ukweli hakuna binaadamu asiyefikiri, kwani chochote unachoamua kufanya ni matokeo ya kufikiri au kuwaza. Kufikiri kunazalisha mawazo ambayo yanaweza kugeuzwa kuwa vitu au matendo halisi.

Hata hivyo, watu wanatofautiana katika kufikiri. Wapo wanaofikiri ki-kawaida tu na hawana kitu kinachowasumbua sana kichwani. Kila kitu kinachopita katika bongo zao kinaonekana ni cha kawaida tu. Lakini wapo watu wanaofikiri kwa umakini na kwa kina. Huku ni kufikiri kimkakati. Watu hawa wana malengo yao ambayo kupitia kufikiri yanaweza kufikiwa.

Wapo watu ambao wanaufikirisha sana ubongo wao kwa lengo la kufanya vitu vitakavyoleta utofauti katika jamii au maisha yao. Hawa wanalenga kufanya ubunifu au uvumbuzi. Matokeo ya kufikiri huku ni kupata kitu kipya au njia mpya na nzuri zaidi za kutatua changamoto.

Sasa basi, moja kati ya njia muhimu katika kukuza biashara au ujasiriamali ni kufanya ubunifu. Yaani kuja na mawazo ambayo yataleta utofauti katika bidhaa, huduma au mchakato wa uzalishaji au utoaji huduma.

Utofauti kati ya bidhaa moja na nyingine unaweza kupatikana katika mwonekano tu wa bidhaa hiyo. Na vitu vinavyobadili mwonekano ni pamoja na vifungashio vya bidhaa hizo.

Ubunifu wa vifungashio huongeza thamani ya bidhaa

Katika jitihada za kuboresha biashara au bidhaa, mjasiriamali unapaswa kulifikiria sana suala la vifungashio. Vifungashio hutumika kutofautisha bidhaa yako na nyingine nyingi zilizoko sokoni –  kupitia muundo, ubora, rangi, dizaini, pamoja na maelezo yanayobebwa na bidhaa hiyo.

Dhana ya vifungashio inaweza kuwekwa katika makundi matatu yanayoelezea thamani ambayo bidhaa inapata kupitia vifungashio hivyo.

Kundi la kwanza, ambalo ni la msingi kabisa ni la kutoa hifadhi kwa bidhaa. Kimsingi vifungashio ni vitu vinavyotengenezwa kwa ajili ya kuhifadhia bidhaa, na hasa kuifanya bidhaa isiharibike kwa urahisi. Vifungashio vinarahisisha usafirishaji wa bidhaa kwa kuifanya ibebeke ki-urahisi lakini pia kuilinda na madhara kama kuvunjika, kulowana, kupigwa vumbi au kushambuliwa na wadudu.

Kundi la pili ni la kisheria au ki-taalamu zaidi. Hapa vifungashio vinatumika kutoa maelezo ya bidhaa husika ili wateja wajue kilichomo ndani ya bidhaa hiyo. Maelezo haya yanahusu malighafi zilizotumika kutengeneza bidhaa husika ambapo mteja huamua kununua au kuacha kulingana hisia ya faida au madhara yanayoweza kuletwa na vitu vilivyomo katika bidhaa hiyo.

Pamoja na hilo, vifungashio vinawekewa pia maelezo ya lini bidhaa hiyo imetengenezwa, na lini muda wake utaisha; vinawekewa alama za uthibitisho wa ubora, mfano TBS; na pia maelezo ya watu gani wanakatazwa kuitumia bidhaa hiyo, mfano watoto au wajawazito.

Kundi la tatu la dhana ya vifungashio linahusisha kitu kiitwacho ‘fahari ya macho’; yaani burudani au hisia ambayo macho yanapata kutokana na jinsi bidhaa ilivyopambwa.

Kifungashio kizuri kinategemea uwezo wa ubunifu alionao mjasiriamali husika; yaani uwezo wa kuitazama dunia kwa jicho la udadisi na kuja na vitu ambavyo watu wengine wakiviona watashangaa, watapata hamasa, na  mwisho wataamua kununua bidhaa hiyo.

Vifungashio bora sio suala la viwanda vikubwa tu; hata wajasiriamali  wadogo wa nyumbani wanahusika!

Katika hili ni kwamba mjasiriamali anatakiwa awe mbunifu na aweze kuipamba bidhaa yake kwa michoro, rangi, vikolokolo, na marembo anuwai ambayo yakitua katika macho ya mteja yatamfanya ashindwe kujizuia kuondoka na bidhaa hiyo, bila hata kujali kilichomo ndani.

Kwa hiyo, ili kuwa na uhakika wa soko la bidhaa zako, mjasiriamali unapaswa kuboresha eneo la vifungashio. Wapo wateja ambao hata kama bidhaa ina ubora mkubwa, hawako tayari kuinunua endapo tu imewekwa katika vifungashio duni, hivyo ukiboresha eneo hili thamani ya bidhaa yako inaongezeka; na mauzo pia yanapaa.

Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasirimali kivitendo.

Anapatikana kwa simu: 0718219530; e-mail: nzyy2001@gmail.com

Unapofanya Ununuzi Wa Bidhaa Au Malighafi Zingatia Haya

Rafiki mpendwa,

Karibu tena katika mfululizo wa makala zangu zenye lengo la kuelimishana kuhusu masuala ya ujasiriamali, ubunifu na stadi za maisha.

Katika makala hii ya leo nitazungumzia suala la ununuzi wa bidhaa au malighafi kwa ajili ya uendeshaji wa biashara. Kumbuka unapofanya biashara yoyote, iwe ya kununua na kuuza, au ya kuzalisha mali na kuuza, ni lazima utafanya zoezi la ununuzi. Hivyo katika ununuzi lazima ujipange vizuri ili ununuzi unaoufanya uiletee biashara yako tija ya kutosha.

Chagua wagavi wa bidhaa kwa umakini usije iangamiza biashara yako

Usipokuwa makini na ukafanya ununuzi bila kufikiria wala kupangilia, ukanunua kiholela, utajikuta katika matatizo, na huenda hili peke yake likaifanya biashara yako iyumbe hadi kufa.

Ununuzi una taratibu na kanuni zake ambazo unapaswa kuzifuata ili kila unachopanga kununua kiweze kuwa na manufaa na kiongeze tija kwenye biashara unayoifanya. Kwa hiyo makala hii itakupitisha katika taratibu za ununuzi ambazo ukizifuata zitaisaidia biashara yako, kama ifuatavyo:

Moja, kujua unataka kununua nini. Kuna watu wanakurupuka katika kufanya mambo. Suala la ununuzi halitaki kukurupuka. Unapaswa kujua kwa uhakikika unataka kununua nini na kwa sababu gani. Unapofanya ununuzi wowote, unatumia rasilimali fedha; hivyo ikitokea ukanunua bidhaa au malighafi isiyohitajika kwa wakati huo utakuwa umeiingiza biashara yako katika hasara.

Pili, kupanga muda wa kununua bidhaa. Ukishajua unataka kununua nini kulingana na mahitaji na vipaumbele vyako, unapaswa  sasa kujua muda sahihi wa kuagiza bidhaa au malighafi hizo.

Ukiagiza mapema sana kabla hujafanya maandalizi mengine, ujue bidhaa au malighafi zitakaa stoo bila sababu na huenda baadhi yake zikaharibika au kupitwa na wakati. Hii ni hasara tayari kwa biashara. Lakini, kubwa ni kwamba bidhaa zilizonunuliwa mapema sana zinakuwa ‘zimeikamata pesa’, ambayo huenda ingetumika kununua kitu kingine muhimu zaidi na kuifanya pesa izunguke.

Vilevile ukishindwa kununua bidhaa au malighafi kwa wakati, hadi zikaisha stoo, ni wazi utakuwa katika hatari ya kushindwa kukidhi mahitaji ya wateja wako, na hapa kuna hatari ya kukimbiwa na wateja kwa kushindwa kuwaridhisha.

Tatu, kujua wagavi sahihi wa bidhaa au malighafi unayotaka kununua. Unapopanga kufanya ununuzi wowote ni lazima ufanye utafiti kidogo kujua walipo wagavi sahihi wa bidhaa zako. Sio kila muuzaji wa bidhaa ana sifa za kukupatia bidhaa unazohitaji, wapo wengine hawana sifa hizo, na wengine ni wababaishaji tu.

Utafiti utakaofanya utakusaidia kujua ni wapi utapata bidhaa kwa ubora na bei nafuu. Utajua pia tabia za wagavi na jinsi unavyoweza kunufaika kutokana na tabia zao, kwa mfano wapo wagavi ambao ni waaminifu na wanapokuuzia kitu wana uhakika kina ubora sahihi, lakini wapo wababaishaji pia.

Wapo pia wagavi ambao ukinunua kitu wanakupa maelekezo mazuri ya namna ya kutumia, na pia vitu gani uvifanye au usivifanye ili usiingie katika hasara; lakini wapo pia wasiojali kabisa.

Nne, kupanga kiasi sahihi cha kununua. Unapotaka kununua bidhaa lazima uwe unajua kwa usahihi unahitaji bidhaa kiasi gani, kulingana na mahitaji ya wateja wako au mahitaji ya uzalishaji unaoenda kuufanya.

Usipozingatia hili utajikuta unanunua bidhaa au malighafi nyingi bila sababu, na kuna hatari ya kuharibika au ku-expire, lakini vilevile pesa ya ziada iliyotumika ingeweza kufanya mambo mengine. Kwa upande mwingine, ukinunua bidhaa kidogo hutakidhi mahitaji ya wateja wako, au hutafanya uzalishaji sahihi wa bidhaa kiwandani.

Tano, kujua ubora wa bidhaa au malighafi unayonunua. Ubora ni suala ambalo lina umuhimu mkubwa na linasisitizwa sana kwa sababu linagusa maslahi mapana ya wateja. Ukizalisha au kuuza bidhaa hafifu unawahujumu wateja wako, lakini pia unaweza kusababisha madhara makubwa, hata kifo au ulemavu kwa wateja wako.

Kwa hiyo unapaswa kujiridhisha kuwa unanunua bidhaa au malighafi zenye ubora unaofaa kabla ya kuwapelekea wateja wako.

Sita, fanya utafiti wa bei za bidhaa au malighafi unazonunua. Katika uendeshaji wa biashara, bei ndio hasa inayokupa mwongozo au kipimo kuwa utazalisha faida au hasara. Hii ni bei ya kununua na bei ya kuuzia bidhaa.

Ukinunua kwa bei ya juu na kukawa na gharama nyingine juu yake, kisha ukauza kwa bei ndogo, hapo ni wazi utapata hasara. Hivyo fanya ununuzi kwa mgavi atakayekuuzia kwa bei nafuu, ambayo  itakupatia faida ukiuza kwa wateja wako.

Saba, angalia huduma zinazotolewa na mgavi baada ya kununua bidhaa. Wapo wagavi ambao ukishampatia pesa tu basi wewe na yeye hamjuani tena. Hata kama utagundua tatizo katika bidhaa uliyonunua hutapata msaada wake. Hivyo uwe makini na wagavi wa aina hii. Nunua kwa mgavi anayejali maslahi yako na wateja wako pia.

Kwa mfano, umenunua bidhaa halafu ukakwama kuitumia kutokana na teknolojia iliyotumika, mgavi mzuri yuko tayari kukupatia ufafanuzi hapohapo, kwa simu, na wakati mwingine anaweza kutuma mtu aje kwako. Au kama bidhaa ina matatizo wagavi wengine wapo tayari kubadilisha na wakakupatia bidhaa nyingine. Hawa ndio wagavi unaotakiwa kuwajua na kuwakumbatia.

Nihitimishe kwa kukuhimiza wewe mjasiriamali kuwa makini sana katika suala na ununuzi kwani bila kufanya hivyo utaingia kwenye hasara ambayo itakugharimu na kuiyumbisha biashara yako.

Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasirimali kivitendo.

Anapatikana kwa simu: 0718219530; e-mail: nzyy2001@gmail.com