Habari rafiki yangu,
Karibu tena katika makala nyingine inayolenga kukupatia maarifa ya ujasiriamali, ubunifu na stadi za maisha.
Kutokana na hamasa, ukosefu wa ajira au hali ngumu ya maisha, vijana na watu wazima pia wameendelea kuzitafuta fursa na kuingia katika ujasiriamali au biashara kwa lengo la kujipatia kipato na kuboresha maisha yao.

Hata hivyo, tafiti zinaonesha kuwa biashara nyingi zinazoanzishwa hufa ndani ya kipindi cha miaka mitano tangu kuanzishwa kwake. Je unalijua hili? Fuatana na mimi ili uzifahamu sababu hizi, na ukizijua itakusaidia kujipanga ili usifikwe na dhahama hii. Kusudi langu hapa ni kwamba maarifa haya yatakusaidia kuchukua tahadhari mapema, na hii itakusaidia kuinusuru biashara yako iondokane na hatari ya kufa.
Wataalamu wanatuambia kuwa biashara nyingi hufa kutokana na matatizo yanayotokana, kwa kiasi kikubwa, na wafanyabiashara wenyewe. Maana yake hapa ni kwamba mchawi wa biashara huwa hatoki nje, bali yumo ndani ya mfanyabiashara mwenyewe. Ni sawa na msemo maarufu usemao, “kikulacho ki nguoni mwako.”
Zifuatazo ni baadhi ya sababu hizo ambazo mojamoja, au kwa pamoja, zinaweza kusababisha biashara yako kufa:
Moja, kutokuwa na elimu au uelewa mzuri wa biashara. Nimeandika huko nyuma kuhusu umuhimu wa elimu ya ujasiriamali. Nimeeleza kuwa elimu ya ujasiriamali inahitajika na ina umuhimu mkubwa, kwani ina msaada mkubwa katika kumpatia mjasiriamali umahiri katika kuanzisha, kuendesha, kuchambua na kutathmini mwenendo wa biashara yake, na kufanya marekebisho mapema ikibidi.
Nimesema kwamba elimu hii inamjengea mjasiriamali uwezo wa kujiamini, kuhoji na kutambua fursa na changamoto kwa uhakika. Elimu hii inamsaidia mfanyabiashara kufungua na kutanua akili yake ili ifikie uwezo wa juu wa kufikiri na kutafakari mambo. Kwa hiyo nikahimiza kuwa kila mtu anapaswa kuitafuta kwa bidii.
Elimu au maarifa ya ujasiriamali yanapatikana kwa kujifunza kupitia mitandao, vitabu, majarida, blog, kuhudhuri semina na kupitia kwa wajasiriamali waliofanikiwa, au hata waliofeli.
Pili, kukosa umakini katika matumizi ya rasilimali na hasa fedha. Ukiwa mfanyabiashara unapaswa kuwa na nidhamu ya hali ya juu katika matumizi ya rasilimali zako. Ukitumia fedha bila mpangilio mzuri zitapotea au utaziweka katika matumizi yasiyo ya lazima na hazitaweza kuzalisha tija katika biashara yako. Hii ni hasara tayari. Rasilimali nyingine ni muda, nyenzo za kutendea kazi, wafanyakazi n.k. Hivi vyote vinahitaji umakini wa hali ya juu katika mipangilio na matumizi yake.
Tatu, kukosekana kwa ubunifu. Nimeandika kupitia makala zangu umuhimu wa ubunifu katika uendeshaji wa biashara. Kuna ushindani mkubwa ziku hizi katika kila biashara unayopanga kufanya. Hivyo unapaswa kuja na vitu vya ki-bunifu kila siku ili uushinde ushindani huo. Jifunze kujitofautisha na kujiongeza ili ufanye vitu kwa ubora na umahiri wa juu.
Nne, kushindwa kulijua soko la bidhaa zako na kuitangaza biashara. Unapoanzisha biashara yoyote unapaswa kujua soko lako ni lipi; yaani nani atanunua bidhaa yako?. Hili linahitaji utafiti kidogo. Usipolijua soko utashindwa kupata wateja na biashara itayumba. Vivyo hivyo, ukishindwa kuitangaza biashara au bidhaa yako ni wazi haitajulikana.
Tano, kushindwa kutoa huduma nzuri kwa wateja. Kumbuka wateja ndio pesa katika biashara. Jiulize, bila mteja kuja, pesa itaingiaje katika droo yako ya dukani? Jifunze jinsi ya kuwavuta wateja na kuwabakiza. Usifanye mambo yatakayowafukuza wateja wako, hakikisha wanavutiwa na huduma zako na wanakusaidia kuitangaza kwa wenzao pia.
Sita, kukosa vipaumbele. Hili ni tatizo kwa wajasiriamali wengi. Wapo wanaotaka kufanya kila kitu kwa wakati mmoja. Yaani wangependa kuanzisha biashara zaidi ya moja kwa wakati mmoja. Ukifanya hivi ujue zitakwama zote! Kufanya hivi ni kukosa ‘focus’ yaani ni kupapasapapasa tu. Weka vipaumbele; yaani chagua uanze na ipi, kwa kuanzia – halafu angalia nini kifuatie baada ya hii kusimama chenyewe.
Saba, kushindwa kupambana na changamoto za biashara. Katika biashara kuna changamoto nyingi. Ndio maana nimekuwa nahimiza kujifunza ubunifu. Mbunifu ni mtu anayefikiri ki-udadisi kila siku. Kwa kufanya hivi ni wazi utavibaini vihatarishi au changamoto zinazonyemelea biashara yako na kuja na mbinu za kupambana nazo kabla hazijakufanya ukwame katika biashara yako.
Nane, uchaguzi mbaya wa eneo la biashara. Katika kusaka eneo la biashara unaweza kujikuta umepata eneo lililo mbali na wateja wako, au lisilo salama, au lililokatazwa kisheria. Hili likitokea kuna hatari ya kukosa wateja au kupata hasara, na kufanya biashara yako izorote hadi kufa.
Tisa, kushambuliwa na majanga ya asili kama mafuriko n.k. Hii ni sababu inayotokana na mazingira yaliyo nje ya mfanyabiashara, ingawa mfanyabiashara ana nafasi ya kuweza kufanya kitu mapema ili kuokoa biashara yake isiathirike. Kwa mfano, huwa kuna tahadhari zinazotolewa na watabiri wa hali ya hewa wakisema kutakuwa na mvua kubwa na vimbunga, hivyo watu wahame au wachukuwe tahadhari fulani. Usipochukua tahadhali ni wazi madhara yatakupata.
Ushauri wangu: Biashara nyingi hufa katika kipindi kifupi baada ya kuanzishwa kutokana na matatizo ambayo yanaweza kuzuilika; yaani yamo ndani ya uwezo wa mfanyabiashara mwenyewe. Kwa hiyo ni muhimu kila mfanyabiashara awe makini na mdadisi katika kuzibaini fursa na changamoto mbalimbali zinazojitokeza, na kufanya vitu sahihi, kila siku katika uendeshaji wa biashara.

