Jinsi Ushirikiano Unavyoweza Kuchochea Ubunifu

Habari rafiki,

Karibu tena katika makala nyingine inayolenga kukupatia maarifa ya ujasiriamali, ubunifu na stadi za maisha.

Biashara yoyote unayofikiria kuanzisha tarajia kukutana na ushindani, sasa au hata baadaye. Huwezi kulikwepa hili, ni suala la kawaida.

Je ukikutana na ushindani – tayari unaacha kufanya biashara? Hapana! Biashara ni akili na mipango. Ikitokea hali hii usikonde, unapaswa kuishughulisha akili yako. Inakupasa kupanga kufanya kitu tofauti.

Ushirikiano ni mkakati katika kukuza ubunifu katika biashara

Kuna mbinu za kiubunifu ambazo mjasiriamali akizitumia anaweza kuibuka na bidhaa au huduma ambazo ni za kipekee zinazoweza kumfanya ajipambanue miongoni mwa washindani.

Moja ya mbinu za kibunifu za kupambana na ushindani katika soko ni kutengeneza ushirikiano wa kibiashara kati ya makampuni au biashara zinazofanya shughuli tofauti-tofauti.

Ushirikiano huu utatengeneza nguvu moja kubwa ambayo itawasaidia wote kujiweka juu ya upinzani uliopo.

Kampuni za Mastercard, BancABC na Vodacom ni mfano mzuri wa makampuni yaliyojipambanua katika kujali suala la ubunifu kupitia ushirikiano, na kulitekeleza jambo hili kivitendo.

Mastercard ni kampuni iliyojikita katika teknolojia ya kuwezesha malipo ya kimataifa. BancABC inajishughulisha na utoaji wa huduma za kifedha, na Vodacom ni kampuni  ya mawasiliano ya simu za mkononi.

Suala ya ununuzi wa bidhaa hasa za kimataifa, kwa njia ya mtandao, nchini Tanzania halikuwa suala la kawaida; lilikuwa linatazamwa na wengi kama ndoto hivi, yaani haikuwa rahisi.

Ushirikino baina ya Makampuni haya matatu, yenye utaalamu na rasilimali tofauti, umefanikisha utengenezaji wa kadi ya kwanza iitwayo M-Pesa Virtual Card, inayowezesha manunuzi ya mtandaoni.

Kwa mujibu wa msemaji wa Vodacom, huduma ya M-Pesa kutoka Vodacom imeendelea kuwezesha upatikanaji wa uhakika wa huduma za kifedha. Hata hivyo imekuwa ni ngumu pale linapokuja suala la kulipia manunuzi mitandaoni, hasa kupitia tovuti za kimataifa.

Uzinduzi wa Virtual Card, mwaka 2018, kupitia M-Pesa ni ubunifu ulioleta mapinduzi makubwa katika manunuzi ya mtandaoni. Hili limewezesha kuondokana na kikwazo cha kulazimika kuwa na akaunti ya benki; na pia hatari ya kulazimika kuweka taarifa za kibenki, za mteja, mtandaoni.

Ubunifu wa kadi hii umelenga kuwawezesha wateja wa M-Pesa kufanya malipo kwenye tovuti za hapa nyumbani, na zile za kimataifa, bila kuhitaji kuwa na akaunti ya benki au kadi ya mkopo (credit card).

Kupitia ubunifu huu, mteja anaweza kutengeneza Virtual Card na kuijaza pesa kupitia mfumo wa M-Pesa, na ikawa tayari kwa matumizi. Hii inamaanisha kuwa sasa watu wengi zaidi wataweza kufanya malipo bila kuhitaji kuwa na pesa taslimu.

Sasa swali, je wewe mjasiriamali unayefanya shughuli yako yoyote ya kijiingizia kipato, una cha kujifunza kupitia ubunifu huu? Ukweli kipo cha kujifunza.

Wakati fulani huwa tunaambiwa kwamba kidole kimoja hakivunji chawa. Kwa hiyo wajasiriamali wanapaswa kuongozwa na mawazo chanya kila wakati. Wanatakiwa kuangalia pande zote ili waweze kuona nini kinafanyika, wapi, na kinafanywa na nani.

Uamuzi wa kuunda ushirikiano wa kibiashara ili kufanya uboreshaji wa bidhaa au huduma ni uamuzi unaotokana na uwepo wa watu wanaofikiri kwa mtazamo chanya, ndani ya Kampuni.

Hili linafanyika pale mjasiriamali mmoja mwenye ujuzi au bidhaa fulani anakaa na mjasiriamali mwingine mwenye ujuzi au bidhaa nyingine, na kufanya mjadala wenye lengo la kuunda bidhaa mpya itakayoongeza thamani ya bidhaa au huduma ya kila mshirika.

Ubunifu wa aina hii una nafasi kubwa ya kuwawezesha washirika kuunda bidhaa mpya inayoweza kuliteka soko vizuri na haraka zaidi, na kila mmoja akanufaika ipasavyo.

Hatua ya kuchukua; kama yalivyofanya makampuni haya matatu, mjasiriamali unapaswa kujifunza kutazama huku na kule ili uweze kuona ni kampuni au biashara gani unaweza kuhitaji kuomba ushirikiano nayo utakaowezesha wewe na yeye kunufaika kibiashara.

Ushirikiano wa makampuni katika masuala kama ya teknolojia, malipo, huduma za fedha n.k ni moja kati ya mikakati muhimu inayolenga kuongeza tija kwa makampuni  husika, lakini pia kwa wateja wao.

Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasirimali kivitendo. Anapatikana kwa simu: 0718219530; e-mail: nzyy2001@gmail.com

Je Changamoto Zina Athari Gani Katika Maisha Yako?

Habari rafiki,

Je umewahi kukutana na changamoto kubwa katika miasha yako iliyokutesa, ikakukatisha tamaa hadi kukuondoa katika reli? Kama ndiyo, naomba leo nikupe simulizi fupi ambayo huenda ikakuhamasisha uanze kufikiri ki-utofauti.

Hii ni hadithi inayomhusu binti mmoja aitwaye Sara, na baba yake Mzee Sotto. Siku moja Sara alimwendea baba yake huku akisononeka kuhusu ugumu  wa maisha.

Ukikutana na magumu ya maisha usilegee, pambana hadi kieleweke

Alipofika kwa baba yake alisema, “baba mbona maisha ni magumu hivi? Hata sijui nifanyeje. Yaani napambana na kujishughulisha kwa kiwango cha juu, muda wote, lakini wapi; likitoka tatizo moja linajitokeza jingine, nifanye nini?”

Baba yake, akiwa mpishi katika taasisi fulani, alimchukua binti yake Sara hadi jikoni. Alijaza maji katika masufuria matatu, akayaweka jikoni na kuwasha moto katika kila jiko.

Maji yalipochemka katika masufuria yale alichukua viazi akavitia katika sufuria moja. Akachukua mayai akayatia katika sufuria ya pili. Halafu tena akachukua punje za kahawa akazimwagia katika sufuria ya tatu.

Bila kusema lolote Mzee Sotto alivuta kiti akaketi. Binti yake naye akakaa huku akiendelea kutazama yale masufuria yakichemka asijue nini hasa baba yake  anakusudia kufanya.

Baada ya dakika thelathini hivi baba yake aliyasogelea yale masufuria na kuyachungulia kwa muda kisha akazima moto.

Baada ya muda kidogo aliopoa viazi kutoka katika sufuria ya kwanza na kuviweka katika sahani. Akaopoa mayai na kuyaweka katika sahani nyingine halafu akachota mchuzi wa kahawa na kuuweka katika kikombe.

Mzee Sotto alimgeukia binti yake na kumwambia, “Sara, unaona nini?” Sara akamjibu baba yake, “ninaona viazi, mayai na kahawa.”

Baba yake akadakia, “sasa angalia kwa umakini, kisha bonyeza kiazi kimoja.”  Sara akafanya hivyo na kugundua kuwa kiazi kile kilikuwa kimelainika.

“Sasa chukua yai moja, livunje kisha limenye.” Mzee Sotto akamwambia binti yake, naye akafanya hivyo na kugundua kuwa yai lilikuwa gumu na limeiva, likiwa na utando mweupe ukiwa umeifunika rangi ya njano ya kiini cha yai lile.

Mwisho mzee Sotto akamwelekeza bintiye kwenye kikombe cha kahawa na kumtaka aionje. Sara alifanya hivyo na kukutana na harufu na ladha nzuri ya kahawa iliyomtoa kijasho chembamba.

Baada ya haya yote Sara alimuuliza baba yake, “je baba hii ina maana gani?” Baba yake hakusita kumfafanulia.

Alimwambia kwamba  viazi, mayai na kahawa vyote vimepitia katika changamoto au mateso ya moto. Vimeunguzwa na maji yaliyochemka na kila kimoja kimeiva lakini kwa staili tofauti.

Viazi viliingia jikoni vikiwa vigumu na madhubuti lakini baada ya kuunguzwa na maji ya moto vimelainika na kutepeta.

Mayai yakiwa mabichi huonekana kama magumu. Lakini kiuhalisia kila yai lina ute ndani yake uliofunikwa kwa utando mwembamba mgumu ambao haulipi yai ulinzi wowote wa maana lisiweze kuvunjika na ute kusambaratika.

Hata hivyo yai hili dhaifu limebadilishwa na maji ya moto kuwa kitu kigumu na madhubuti nje na ndani.

Nayo kahawa, kabla ilikuwa ni kitu kisicho na thamani inayoonekana bayana lakini baada ya kupita katika maji ya moto imebadilika na kuwa kinywaji safi chenye ladha na harufu ya kuvutia.

Baada ya maelezo hayo Mzee Sotto alimgeukia bintiye na kumuuliza, “enhe Sara, sema sasa, wewe unaweza kujifananisha na nini hapa?” Je, changamoto ulizopitia zimekufanya kuwa kiazi, yai au kahawa?

Hatua ya kuchukua; kama alivyo Sara, binaadamu tunakutana na changamoto nyingi na hasa unapoanza kujibidisha katika utafutaji wa maisha.

Zipo changamoto za kawaida na zingine zinatisha. Unachopaswa kufanya ni kukabiliana na changamoto yoyote inayokuja mbele yako huku ukijiuliza, “je nataka hatimaye niwe kiazi, yai au kahawa?”

Je matatizo yatakufanya kuwa laini na legelege? Je yatakufanya kuwa shupavu na jasiri au yatakubadilisha kuwa kitu kipya chenye mvuto na tija? Jichunguze na uchukue hatua sahihi.

Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasirimali kivitendo.

Anapatikana kwa e-mail: nzyy2001@gmail.com

Je Sungusungu Anaweza Kukuzidi Ujasiri?

Habari rafiki,

Leo nataka kukusimulia hadithi fupi inayomhusu Mfalme mmoja maarufu. Katika moja ya makala zangu nimenukuu ripoti ya watafiti Donald Kuratco na Richard Hodge wakifafanua maana ya ujasiriamali.

Wanasema ujasiriamali ni mchakato endelevu unaohusisha kuwa na maono, kuweka malengo, kufanya mabadiliko na kutengeneza vitu vipya.

Wanaongeza kuwa ujasiriamali unahusisha nguvu, motisha, jitihada na uvumilivu kuweza kuunda na kuyatia katika matendo – mawazo na mbinu mpya za kutatua changamoto.

Ni kutokana na nukuu hii nimejikuta nakumbuka hadithi moja ya zamani inayomhusu Mfalme maarufu aliyeishi karne ya 14 katika nchi ambayo leo inaitwa Uzbekistan, bara la Asia.

Huyu anaitwa Mfalme Amir Timur, ambaye alisifika kwa kushinda mapambano mengi ya vita hadi kuweza kuikalia zaidi ya nusu ya ardhi yote ya eneo hilo wakati huo.

Pamoja na ujasiri – Sungusungu wana ushirikiano wa hali ya juu pia

Mfalme Timur alisifika kwa ushupavu wa hali ya juu aliokuwa nao. Alikuwa Kamanda imara asiyeweza kutikiswa na kitu chochote. Hakuna jambo au mtu aliyemtia woga, na alisifika kwa mbinu za uhakika za medani.

Je aliwezaje kuwa Mfalme mwenye nguvu, maarifa, ujasiri na uvumilivu kwa kiwango hicho? Sikiliza simulizi yake yeye mwenyewe.

Anasema mwanzoni alipokuwa anaongoza vikosi katika uwanja wa mapambano hakufanya vizuri. Alipata vipigo vingi na kuchakazwa vibaya.

Anakumbuka mpambano mmoja ambao vikosi vyake vilipata kichapo cha uhakika kilichosababisha yeye na askari wake kusambaratika, kukimbia na kujificha msituni.

Akili zilipomrudia vizuri alijikuta pembeni mwa kilima kimoja ambapo alijificha kuokoa maisha yake.

Akiwa amechoka huku njaa akimuuma alijiegemeza katika jiwe moja na  kuanza kutafakari mambo mbalimbali huku macho yake yakivinjari uzuri wa viumbe wadogo waliokatiza mbele yake.

Ghafla kuna kitu kilichogusa hisia zake. Alikuwa mdudu Sungusungu mweusi aliyekuwa amebeba punje ya nafaka iliyofanana na mchele.

Punje hiyo ilikuwa kubwa kuzidi umbo la mdudu huyo. Sungusungu alikuwa akijitahidi kuupandisha mzigo ule juu ya ukuta wa mwamba.

Alijaribu kwa mara ya kwanza kuupandisha mzigo lakini alipofika nusu ya ukuta ule mzigo ulidondoka chini. Sungusungu alirudi chini na kuunyenyua. Alipanda nao tena na kabla hajafika juu mzigo ulidondoka.

Sungusungu hakukata tamaa, alirudi tena hadi chini na kuuchukua tena mzigo wake, na wala hakufika mbali ukadondoka tena! Naye akaufuata tena!

Muda wote huu Mfalme Timur, kwa umakini mkubwa alikuwa anashuhudia yote haya. Kwa mujibu wa Mfalme, Sungusungu huyu alirudia zoezi hili karibia mara thelathini kabla ya kuufikisha mzigo juu ya ukuta.

Baada ya Sungusungu kufanikiwa kuna kitu kiligonga kama kengele ndani ya ubongo wa Mfalme. Alimuangalia Sungusungu yule kisha akajisemea kimoyomoyo, “Amir Timur, hivi kweli unaweza kuzidiwa na mdudu huyu?”  

“Kama siyo, kwa nini sasa umejificha hapa? Ni mapambano mangapi umeshindwa hadi umesalimu amri? Je umeona ujasiri na uvumilivu wa Sungusungu? Umejifunza nini? Inuka, rudi katika uwanja wa mapambano!”

Baada ya mawazo haya kupita katika ubongo wake Timur alijiona mwepesi. Alipata nguvu na hamasa ya ajabu. Ndipo sasa aliinuka na kuanza kuwakusanya askari wake waliokuwa wamejificha pia.

Alichukua hatua ya kulisuka upya jeshi lake, kulijaza hamasa na ujasiri kama wa Sungusungu, na kulirudisha katika mapambano.

Kuanzia siku hiyo hakuwahi kushindwa vita yoyote. Alijifunza kutoka kwa Sungusungu ujasiri, uvumilivu na moyo wa kutokata tamaa. Aliweza kupambana na falme zote hadi akawa Mfalme mwenye nguvu zaidi katika eneo lote la Asia.

Hatua ya kuchukua; Ukiwa mjasiriamali kuna somo unaweza kujifunza hapa. Shughuli za ujasiriamali zina changamoto nyingi. Kuna kuteleza, kuchomwa miiba, kuanguka, n.k.

Kikubwa cha kuzingatia ni utulivu na uvumilivu. Ukipatwa na changamoto yoyote tulia kidogo halafu, kama Sungusungu, rudi chini okota mzigo wako anza kurudi tena juu.

Kama Sungusungu anaweza kuvumilia kwa kiwango hicho je wewe ni dhaifu kwa kiasi gani hadi ushindwe? Tafakari! 

Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasirimali kivitendo.

Anapatikana kwa e-mail: nzyy2001@gmail.com; 0718219530

Ukiendekeza Woga Hakuna Biashara Utakayoiweza

Ni kitu gani kinachokuzuia kuanzisha biashara au shughuli ya kijasiriamali uipendayo?

Watu wengi wenye ndoto ya kuingia katika biashara hudadisi sana suala la mtaji.

Utasikia, “kwa kweli natamani sana kufungua biashara ya vifaa vya magari – lakini mtaji ndio tatizo.” Ukimuuliza mtaji gani anataka kuwa nao, atakujibu, ‘pesa’!

Ingawa sababu hii siyo ya kubeza lakini sio sababu yenye mashiko. Tujilize, je pesa ikikosekana maana yake biashara haiwezi kufanyika?

Mfanyabiashara mmoja mashuhuri anasema, “huhitaji fedha ili kupata fedha…unachohitaji ni maarifa tu… ili kupata fedha.” Tafakari.

Yupo rafiki yangu mbaye kwake yeye mtaji , na hasa pesa, sio suala la kujadili. Anao ndugu wenye uwezo na wako tayari kumsaidia akitaka. Kutokana na hili, muda mrefu amekuwa akiongelea suala la kuingia katika biashara.

Ukiendekeza woga utakikimbia hata kivuli chako

Cha kushangaza ni kwamba nilipomuuliza mbona  anaonekana kujivutavuta wakati ana watu wa kumsaidia pesa, yaani mbona haanzishi biashara kama kweli anapenda kufanya hivyo?

Jibu lake lilikuwa, “aah rafiki yangu, biashara si mchezo, najipanga. Kila nikifikiria kuanza naogopa. Kuna kufeli ujue, na kufeli ni shida.”

Nilipomuuliza kwa nini anafikiria kufeli alijibu kuwa kwa biashara anayoifikiria hana uhakika kama atafanikiwa ikizingatiwa mzunguko mdogo wa fedha kipindi hiki. Na mtaji ukikata anaogopa hataaminiwa tena.

Kwa hiyo utaona hapa kuwa kumbe kitu kinachowasumbua watu vichwa ni woga tu! Yaani wanaogopa kufeli.

Ni sawa – wakati fulani kuogopa ni jambo muhimu. Kwa mfano huwezi kuacha kuogopa kupita hapo, hasa usiku, ukiambiwa kuwa nyumba fulani inalindwa na mbwa mkali anayeweza kukurarua ukijaribu kukatiza.

Kwa hiyo unaweza kuona kuwa huu ni woga halali. Hapa unaogopa balaa la kushambuliwa na mnyama mkali na pengine kuumizwa au kuuawa kabisa.

Sasa tujiulize, ni sahihi kuogopa kila kitu? Hapana! Woga ambao unakuzuia usichukue hatua ya kufanya mambo unayopasa kufanya ili upige hatua za kimaendeleo sio woga halali – ni woga wa ovyo.

Kwa hiyo, kama woga, na hasa woga wa kufeli ndio unaokuzuia kuanzisha biashara, unapaswa kuondoa woga huo. Hata hivyo, mtu anaweza kuuliza, “je nitauondoa vipi woga huo?”

Kuna njia mbili kuu za kuondokana na woga kama nitakavyozielezea hapa:

Njia ya kwanza ni kujiandaa kufanikiwa.

Na hapa kitu cha kwanza cha kufanya ili ujiandae kufanikiwa ni kujifunza jinsi ya kutia wazo lako katika vitendo.

Kwa kuwa tayari unajua kufeli, na athari zake, basi tambua sasa kuwa usipofanya chochote ujue tayari umeshafeli. Utakuwa umefeli pia kama utafanya vitu vya kijinga.

Kwa hiyo, ili ufanikiwe lazima uwe tayari kutafuta taarifa na maarifa. Vitu hivi vitakuwezesha kujua uanze kufanya nini, wapi, kwa vipi na nani atakuwa mteja wako.

Njia ya pili ni kubadili mtazamo wako kuhusu kufeli.

Ukiwauliza watu kwa nini wanaogopa kufeli majibu ya baadhi yao yanaweza kuwa, “ukifeli unadhalilika na hadhi yako inashuka” au “kufeli kunakufanya upoteze mtaji wako.”

Hata hivyo, ukweli ni kwamba hizi ni hisia tu. Ni hisia zinazowapata baadhi ya watu wanaoyatazama mambo kwa mtazamo hasi.

Jiulize hivi ukifeli ndio tayari umeshaanguka? Si kweli! Ukweli ni kwamba ukianguka na ukaendelea kugalagala chini hapo utakuwa umefeli.

Lakini ukianguka na kujitutumua hadi ukaweza kuinuka na ukasonga mbele – wewe ni mshindi, hivyo ongeza hatua, songa mbele!

Jiulize, je watu watakudharau ukifeli? Ndiyo wapo baadhi! Huwezi kuzuia watu kufikiri au kuwa na mitizamo yao. Hata hivyo jiulize tena, mitazamo yao inakuhusu au inakupunguzia nini wewe? Unakosaje usingizi kwa ajili ya watu hawa?

Kuhusu kupoteza mtaji wa fedha kutokana na kufeli – hili hutokea, lakini sio kila mara.

Na hata ikitokea mtaji wa fedha ukakata, bado kuna mtaji utakaobaki. Huu ni mtaji wa akili, afya, watu, na mawazo chanya uliyonayo kichwani.

Hatua ya kuchukua; kufeli kunaweza kukunyong’onyeza ukajiona una mkosi, hata hivyo kufeli siyo mwisho wa maisha. Kufeli ni fursa ya kukufanya ujikusanye na kujipanga upya.

Ukifeli inuka, kusanya upya nguvu, akili, na maarifa ili kujiinua na kusonga mbele. Usiogope kufeli, ogopa kuendekeza woga.

Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasirimali kivitendo.

Anapatikana kwa e-mail: nzyy2001@gmail.com; 0718219530

Ukizijua Tabia Hizi 5 Za Wateja Biashara Yako Itapaa

Habari rafiki yangu,

Karibu tena katika mfululizo wa makala zangu zenye lengo la kukusaidia ili uweze kuchukua hatua ya kubuni, kuanzisha, kuboresha au kuongeza thamani ya shughuli yako ya kijasiriamali.

Makala ya leo inalenga katika uboreshaji wa huduma kwa wateja. Kumbuka tunapoongelea biashara kimsingi tunaongelea mteja – kwa kuwa hakuna biashara pasipokuwa na mteja, na mteja ndiyo pesa yenyewe.

Mteja hupitia hatua tano katika mchakato wa manunuzi – ambazo ni vyema wewe mjasiriamali unayeuza bidhaa au kutoa huduma ukazifahamu ili zikusaidie kumjua vizuri na kumpatia huduma au bidhaa kwa kiwango stahiki.

Kabla mteja hajatoa uamuzi wa kununua hutafuta taarifa zilizo sahihi..

Usipozijua hatua hizi utaendelea kutoa huduma kwa mazoea na mwisho utashangaa jinsi unavyopoteza wateja wako kiasi cha kudhania kuwa kuna mkono wa mtu. Hatua hizi ni kama ifuatavyo:

Moja, mteja kugundua uhitaji. Hiki ndicho kitu cha kwanza kabisa kinachopita katika ubongo wa mteja. Yaani, kabla mteja hajaingia katika duka lako huwa ana tatizo linalohitaji kutatuliwa.

Kwa mfano anawaza, “ninahitaji kuwasiliana na rafiki zangu kwa njia ya Wasap, lakini sina Smartphone – hivyo kuna haja ya kununua chombo hicho.”

Mbili, mteja kutafuta taarifa kuhusu bidhaa au huduma. Mteja akishagundua anahitaji kununua bidhaa fulani, mara nyingi huwa hakurupuki. Mteja ana tabia ya kutaka kujua anachotaka kununua.

Hapa ndipo mteja huanza kutafuta mtoa huduma atakayempatia taarifa za kutosheleza za bidhaa anayoitaka.

Kama anataka kununua Smartphone, kwa mfano, mteja huwa na maswali yake ambayo angetaka yajibiwe.

Kwa mfano, kuna aina ngapi za simu ya aina hii, na nini ubora wa kila aina? Je simu zinauzwa bei gani? Je simu ipi ina kamera nzuri zaidi? Ni simu ipi inatunza chaji kwa muda mrefu zaidi, n.k.

Kwa hiyo mteja anapoingia dukani kwako au anapokupigia simu anakuwa na maswali yake. Anataka majibu ili kupata taarifa. Mara nyingi katika hatua hii mteja huonekana kama siyo mnunuzi. Anauliza maswali yake mengi ili ajue.

Sasa, kwa upande wa mtoa huduma, hatua hii ni ya muhimu sana. Katika hatua hii mteja anatakiwa kuhudumiwa vizuri sana. Mteja anapotafuta taarifa jitahidi azipate kiurahisi, kwa usahihi na kwa wakati.

Kiukweli, hatua hii ndiyo hasa huduma kwa mteja huanzia. Mtoa huduma usingojee hadi mteja anapoingia dukani kwako akiwa na fedha, kununua, ndipo ujitutumue kutoa huduma nzuri – hapana! Utakuwa umechelewa.

Mteja akigundua taarifa unazompa hazina mpangilio, hazina usahihi na kuna aina fulani ya ubabaishaji hatavutika, ataondoka na utamkosa!

Tatu, mteja kufanya tathmini ya taarifa. Mteja anapokusudia kununua bidhaa fulani anaweza kutafuta taarifa kutoka sehemu nyingi. Akisharudi kwake hukaa na kufanya tathmini ya taarifa hizo.

Hapa mteja hufanya ulinganisho wa taarifa za bidhaa ili apate kutoa uamuzi wa bidhaa ipi aliyoipenda zaidi na atainunua wapi.

Nne, mteja kufanya uamuzi wa kununua. Akimaliza ulinganisho kutokana na taarifa kutoka maeneo kadhaa, ndipo sasa hujikusanya tayari kufanya manunuzi.

Uamuzi wa kununua unatokana na kuridhishwa na taarifa alizopata katika hatua ya pili. Kwa hiyo kama wewe ni mtoa huduma na ulijitahidi kumpatia mteja huyu taarifa sahihi kwa staili na mbinu nzuri, tunatarajia mteja huyu atachagua kuja kwako.

Tano, mteja kufanya tathmini baada ya kununua. Mteja keshanunua bidhaa kwako na ameondoka. Hapa mtoa huduma usidhani umemaliza. Jiandae kwa lolote litakalokuja wakati wowote kutoka kwa mteja huyu.

Jiandae kwa kitu kiitwacho mrejesho. Mteja akishanunua huanza kuitumia bidhaa hiyo na kupima ubora, urahisi wa kuitumia au madhara inayosababisha.

Mteja huwa anafanya tathmini ya uhalisia wa bidhaa aliyonunua ikilinganishwa na taarifa alizopewa na mtoa huduma.  Na hapa ndipo suala la uadilifu wa mtoa huduma linapojitokeza.

Kama mtoa huduma ulitoa taarifa za uongo basi huu ndio wakati wa kuumbuka. Na ikitokea kwamba bidhaa iliyonunuliwa haifanyi kazi kwa kiwango kilichoahidiwa, mteja huyu hukasirika.

Mteja akikasirika anaweza kutoa maamuzi ambayo yanaweza kuidhuru biashara yako. Mteja anaweza kuamua kutokurudi tena kununua. Lakini pia anaweza kuwashawishi rafiki zake wasije kununua hapo.

Kibaya zaidi ni pale ambapo ataamua kuisema biashara yako vibaya kwa watu wengine. Utafiti unaonesha kuwa mtu akipewa huduma nzuri huwaambia watu watatu – lakini akipewa huduma mbovu huwaambia watu kumi.

Ushauri kwa Wajasiriamali: ni vyema wewe mjasiriamali unayeuza bidhaa au kutoa huduma ukazifahamu hatua hizi ili zikusaidie kumjua vizuri mteja na kumpatia huduma au bidhaa kwa kiwango stahiki.

Usipozijua hatua hizi utaendelea kutoa huduma kwa mazoea na itakugharimu.

Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasirimali kivitendo.

Anapatikana kwa e-mail: nzyy2001@gmail.com

Ubunifu: Somo Kutoka Kwa Wajapan Na Matikiti-Maji Ya Mraba

Habari rafiki,

Napenda kukukaribisha tena katika mfululizo wa makala zangu zenye lengo la kukupa hamasa wewe msomaji wangu ili uweze kuchuku hatua ya kubuni, kuanzisha, kuboresha au kuongeza thamani ya shughuli yako ya kijasiriamali.

Makala ya leo inalenga kuamsha ari na hamasa ya ubunifu katika ujasiriamali na kuibadili hamasa hiyo kuwa kitu halisia, yaani bidhaa iliyobuniwa.

Kuna aina mbili za mikakati ya ubunifu. Aina ya kwanza ni ubunifu unaotokana na hisia au fikra za mbunifu mwenyewe. Yaani mbunifu anapata wazo la kuunda bidhaa au kitu anachodhani kitakuwa na manufaa kwa mtumiaji.

Mkakati wa pili ni ubunifu unaosukumwa na mahitaji ya soko. Yaani taarifa kutoka sokoni zinaonesha kuwepo kwa mahitaji ya bidhaa ya aina fulani, kisha  mbunifu anatia jitihada katika kufikiri ili aweze kutengeneza bidhaa hiyo.

Naomba leo nikushirikishe simulizi ya kibunifu kutoka Japan. Inasemekana kuwa Wajapan wanapenda kutumia nafasi ndogo katika maduka yao (Supermarkets) ili kuuza bidhaa nyingi katika chumba kidogo – na huu ni mkakati wa kupunguza gharama.

Ukiishughulisha akili yako vizuri unaweza kuibua ubunifu wa vitu visivyotarajiwa

Wafanyabiashara hawa waligundua kuwa Matikiti Maji huchukua nafasi kubwa katika duka kwa kuwa yana umbo la duara. Kwa hiyo ili kuendana na udogo wa nafasi iliyopo ilikuwa lazima wanunue matikiti machache tu ya kutosha eneo dogo kwa ajili hiyo.

Siku moja Mfanyabiashara mmoja wa Matikiti Maji alisikika akijisemea, “yaani  ingewezekana  Matikiti haya yakawa na umbo la mraba nadhani tungeweza kuyanunua kwa wingi zaidi kwani yangepangika kiurahisi katika nafasi ndogo dukani.”

Hata hivyo hakuna Mfanyabiashara yeyote wa matunda haya aliyewahi kufikiri kuwa wazo la kuzalisha Tikiti Maji la mraba lingeweza kufanyika.

Kwa upande wa pili walikuwepo wakulima wa Matikiti – waliopenda kuuza matikiti mengi zaidi ili wajipatie kipato zaidi. Hii kwao ilikuwa ni changamoto; hivyo hawakukubali haraka fikra kwamba si rahisi kuzalisha matikiti ya mraba.

Baadhi ya wakulima hao walianza kusugua bongo zao. Walifikiri, “kama maduka ya matunda yanahitaji matikiti ya mraba, je tunawezaje kuzalisha matikiti hayo?” Walikuna vichwa, na kuanzisha mjadala kuhusu suala hili.

Matokeo ya kufikiri na kujadiliana yalibainisha kuwa inawezekana kuzalisha tikiti la mraba. Mmoja wao alikuja na wazo.

Alipata wazo la kutengeneza boksi au fremu ya mraba. Alifafanua kuwa tunda dogo la tikiti likiwekwa ndani ya fremu hiyo linaweza kukua huku likichukua umbo la boksi hilo, hivyo tunda litakuwa na umbo la mraba.

Wakulima kadhaa walifanya majaribio na kufanikiwa kuzalisha tikiti la mraba. Ugunduzi huu uliwafurahisha sana wakulima kwa kuwa waliweza kusafirisha matunda mengi zaidi kwenda sokoni.

Lakini pia wanunuzi walifurahi kwa kuwa waliweza kuhifadhi matunda mengi katika maduka yao kuliko zamani.

Tuna jambo kubwa la kujifunza kutoka kwa Wajapani. Ukikabiliwa na changamoto unapaswa kujizoeza au kujenga tabia ya kujiuliza maswali. Kwa mfano, Je kuna njia bora na rahisi zaidi ya kutatua changamoto hiyo? Si rahisi kufanya kitu bila kujiuliza maswali.

Ukishajiuliza maswali ndipo unaanza kufikiria njia za utatuzi. Unapaswa kujiepusha na fikra kuwa kuna jambo au changamoto ambayo haiwezekani kupatiwa jawabu. Huu ni mtazamo hasi wa kufikiri, na ukiwa unafikiri hasi huwezi kufanya kitu.

Jifunze kufikiri kwa mtazamo chanya. Jifunze kusema kuwa kila kitu kinawezekana na kisha tia juhudi na maarifa. Kila mtu, kila siku, ajifunze kufikiri kwa mtazamo chanya. Jiepushe kuishi kwa mazoea.

Yaani unapaswa kuacha kufikiri kikawaida na badala yake jenga hali ya kufikiri kimkakati na kutafuta njia bora zaidi za kufanya mambo.

Ukiongeza bidii ya kuhoji jinsi unavyofikiri na kutenda, kila mara, utashangaa utakavyomudu kuibuka na mawazo mengi bunifu yatakayosaidia kuboresha utendaji, bidhaa na huduma.

Hatua ya kuchukua; jitahidi kuiga mfano wa ubunifu wa Tikiti Maji la mraba katika kuziangalia changamoto zako. Baadhi ya watu waliposikia wazo la kuzalisha Tikiti la mraba – haraka sana walihitimisha kuwa jambo hilo linahitaji sayansi na teknolojia kubwa sana – hivyo haliwezekani.

Kumbe kuna wakulima wa kawaida kabisa waliojiongeza kidogo tu wakafikiri kiutofauti na kupata jawabu ambalo ni rahisi kabisa – kutumia boksi la mbao au chuma, la mraba, kuzalisha tikiti la mraba, na kuweza kutatua changamoto ya usafirishaji na uhifadhi katika Supermarket.

Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasirimali kivitendo.

Anapatikana kwa e-mail: nzyy2001@gmail.com

Kwa Nini Elimu Nzuri Ya Darasani Siyo Mwarobaini Katika Maisha? (2)

Habari rafiki

Ni matumaini yangu kuwa unaendelea vyema na shughuli zako kwa ajili ya kusukuma mbele gurudumu la maendeleo.

Hii ni sehemu ya pili ya makala haya ambapo katika sehemu ya kwanza nilijadili vitu vinavyotofautisha elimu inayotolewa darasani na elimu inayopaswa kutolewa kiuhalisia.

Nilisema elimu ya maisha halisia ndiyo humfanya mtu aweze kujitambua, kuziona fursa, kupambana na kufanya vitu.

Kukosekana kwa elimu ya maisha halisia ndiyo sababu hasa zinayowafanya ‘vipanga’ darasani kushindwa kuhimili maisha binafsi ya kujitegemea – wakaishia kuishi kwa kuwatumikia wengine kwa maisha yao yote.

Maisha halisia yamejaa mitihani ambayo lazima ufaulu kabla hujapata maarifa ya mafanikio

Nilieleza kwamba elimu ya darasani haimuandai mwanafunzi kujenga upeo mkubwa wa kufikiri, kujitegemea na kupambana ili apate mafanikio binafsi katika maisha yake. Nilijadi sababu mbili.

Sasa, katika sehemu hii ya pili ya makala haya nitajadili sababu nyingine nne zinazowafanya ‘vipanga’ darasani kushindwa kuhimili maisha binafsi ya kujitegemea, kama ifuatavyo:

Tatu, shule inahimiza mashindano – wakati maisha halisia ni matokeo ya ushirikiano.

Maisha ya shule ni ushindani mtupu. Kila wakati mtoto anataka apate maksi za juu kuliko wenzake. Wapo watoto ambao akiwa na kitabu chenye maelezo mazuri ya somo fulani hawezi kuwaazima wenzake – anaogopa watamzidi.

Katika dunia halisia maisha ni ushirikiano. Ukishindwa kushikamana na kushirikiana na watu mambo yako yatadoda. Lazima ujifunze kutengeneza mshikamano na watu wanaokuzunguka na hasa wenye maono kama yako.

Nne, shule zina walimu wazuri na rafiki – wakati maisha halisia  yana walimu wanoko!

Shuleni walimu wanafundisha kwa umakini, kwa utaratibu mzuri na kwa kutumia mbinu zinazompatia mwanafunzi mazingira mazuri ya kujifunza na kuelewa.

Maisha halisia ni msitu mnene wenye wanyama wakali. Hapa hupati vitu ki-urahisi. Usipopambana unapigwa chini! Katika kupambana kuna mambo mengi. Utaanguka, utalia, utasota, utasononeka na unaweza kufeli vilevile.

Katika maisha halisia unatakiwa kuwa tayari kuingia kuzimu kabla hujaingia peponi – hivyo ni lazima ujiandae kikamilifu.

Tano, shule zinatoa mafunzo kabla ya mtihani – wakati maisha halisia hutoa mtihani kabla ya mafunzo.

Shuleni mwalimu anafundisha, anafafanua somo husika na kutoa muda wa kujiandaa kabla hajatoa mtihani. Hii ni njia rahisi ya kujifunza shuleni.

Katika maisha halisia utakutana na test na mitihani mingi na ya kila aina. Kabla ya kupata mafunzo unapambana na mazingira magumu yenye changamoto kibao, ikiwa ni pamoja na kufeli.

Hii ni njia ngumu ya kujifunza – lakini ni njia nzuri zaidi kwa kuwa inatanguliza mateso na maumivu yanayokufanya ujenge ushupavu na usibweteke – na hapa ndipo somo linapenya kikamilifu.

Sita, shule inafundisha utii – wakati maisha yanafundisha uasi na ukaidi.

Shule zinawapa wanafunzi kanuni za kufuata. Wanapewa miongozo, taratibu na hata formula za masomo kama hisabati, fizikia na uchumi.

Shule zina ratiba – saa ya kuingia darasani, saa ya kupumzika, saa ya kuondoka, sare za kuvaa n.k.

Hivyo kila siku wanafunzi wanahimizwa utii. Ukiwa mkaidi unaadhibiwa na hata kufukuzwa shule. Kwa hiyo kuepukana na hayo unalazimika kufuata sheria na miongozo yote.

Katika maisha halisia, mafanikio yanakwenda kwa waasi na wakaidi. Hawa ni watu wasiopenda kufuata taratibu au sheria zilizowekwa. Hawa hupenda kusonga mbele huku wameelekea upepo unakotoka, wakipambana nao.

Inahitaji ukaidi kufanikiwa katika maisha. Vitu vinavyoonekana vya kawaida kwa wengi siyo lazima viwe sahihi; ni ukaidi na uasi ndio humfanya mtu kuamini na kufanya kitu kilicho kinyume na maoni ya wengi.

Hawa wana uwezo wa kutengeneza njia katikati ya majabari, matope na miiba. Mahali ambapo wengine wote wanaona hapawezekani kupitika, watu hawa huiona njia, wakaisafisha na kuanzisha safari.

Hatua ya kuchukua: Kwa kuwa tumeona mapungufu katika elimu ya darasani na kwamba haimuandai mwanafunzi kujenga upeo mkubwa wa kufikiri na kujitegemea, ni wakati sasa wa kuzingatia mbinu za kuelimika kupitia elimu ya maisha halisia.

Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasirimali kivitendo.

Anapatikana kwa simu: 0718219530; e-mail: nzyy2001@gmail.com

Kwa Nini Elimu Nzuri Ya Darasani Siyo Mwarobaini Katika Maisha? (1)

Habari rafiki

Elimu ya darasani katika dunia ya leo ni kitu muhimu sana, na kila mtu anapaswa kuipata. Elimu hii inampatia mwanafunzi maarifa muhimu ya kusoma, kuandika na kuhesabu. Elimu hii inatoa pia maarifa katika fani mbalimbali kama sayansi, uchumi, siasa n.k.

Watu hutafuta kuelimika kupitia shule ili kurahisisha jitihada zao za kufaulu katika miasha, na hasa maisha ya kuajiriwa; ndio maana wakimaliza tu shule wengi huanza kutafuta kazi!

Mifumo mingi ya utoaji elimu darasani humfanya mwanafunzi kuwa tegemezi darasani na hata katika maisha

Kwa sababu hii, wanafunzi hujitahidi kusoma kwa bidii darasani ili wapate alama za juu, wawe wanafunzi bora, ili mwishowe wafanikiwe kupata kazi.

Wanafunzi wazuri sana darasani huitwa ‘vipanga’, na wale wasiojiweza huitwa ‘vilaza’.

Sasa kuna dhana iliyojengeka kuwa ukiwa ‘kipanga’ darasani basi tayari umeshajijengea msingi wa mafanikio katika maisha. Je kuna ukweli katika hili?

Watafiti wana hoja tofauti. Wao baada ya uchunguzi wamegundua kuwa kwa kiwango kikubwa ‘vipanga’ darasani huishia kufeli katika maisha ya uhalisia.

Maisha halisia ni maisha ya kujituma, kujitegemea na kupata rikizi kupitia fikra na jitihada binafsi.

Vipanga’ wanaoonekana wamefanikiwa basi wanakuwa wamebebwa tu na taasisi wanazofanyia kazi, zinazowalipa ujira mkubwa na marupurupu mengi; ingawa wapo wengine wanaofanikiwa kupitia njia haramu.

Ukweli mchungu ni kwamba elimu ya darasani haimuandai mwanafunzi kujenga upeo mkubwa wa kufikiri, kujitegemea, na kupambana ili apate mafanikio binafsi katika maisha yake.

Elimu hii inamuandaa mwanafunzi kupokea maelekezo maalum, kuyakariri na kuwa tayari kuyatumia kama yalivyo – katika eneo la kazi analopangiwa; na akisha fanya hivi analipwa ujira wake na kuendesha maisha hadi anapostaafu.

Katika makala haya nitajadili vitu vinavyohitajika katika maisha halisia ili watu wavielewe na kujifunza, na wavitumie kama nyenzo za kuwawezesha kupambana na kujitegemea katika maisha.

Nitaonesha tofauti ya elimu kama inavyotolewa darasani na elimu inayopaswa kutolewa ili kumfanya mtu aweze kujitambua, kupambana na kufanya vizuri katika maisha halisia.

Na ukweli, hizi ndizo sababu hasa zinazowafanya ‘vipanga’ darasani kushindwa kuhimili maisha binafsi ya kujitegemea – wakaishia kuishi kwa kuwatumikia wengine kwa maisha yao yote.

Hii ni sehemu ya kwanza ya makala haya ambapo nitaanza kwa kujadili sababu mbili; na katika sehemu ya pili nitajadili sababu tano.

Moja, shule zinahimiza wanafunzi wasifeli, wakati kiuhalisia maisha yanachochewa na matokeo ya kufeli.

Nilisoma na kijana mmoja aliyekuwa na uwezo sana darasani. Huyu, akipata chini ya maksi 90, alikuwa anaugua!

Na hakuwa peke yake; yaani kupata maksi 85 kwa mfano, ni kufeli! Wanafunzi wazuri hawapendi kufeli, na ikitokea wakafeli huchukia sana.

Hata hivyo, kiuhalisia katika maisha ya kawaida, kufeli ni chachu ya mafanikio. Kufeli ni kichocheo. Watu wenye upeo mpana wa elimu ya maisha hukumbatia kufeli.

Watu hawa ni shupavu katika kujaribu vitu hata kama hawana uhakika wa kufaulu. Na ikitokea wakafeli hawachukii wala hawakondi, bali hutabasamu tu huku wakitafakari kwa nini wamefeli.

Hali hii huwapa faraja na fursa ya kujipima ili kujua walipojikwaa. Kisha huanza upya huku wakijiepusha na uwezekeno wa kurudia makosa ya nyuma. Hivyo kufeli kwa watu hawa ndio siri hasa ya mafanikio yao katika maisha.

Mbili, shule inawapa wanafunzi ramani au dira; wakati maisha yanawaacha wahangaike wenyewe.

Shuleni unahimizwa usome kwa bidii, upate gredi nzuri ili upate kazi nzuri kisha ulipwe mshahara mzuri; na ukistaafu ulipwe mafao mazuri ya uzeeni hadi kifo chako.

Kwa hiyo, shule anakupatia mwongozo wa kufuata, na ukiweza kuufuata kwa umakini unapata matokeo yanayofahamika yanayokufanya uishi vizuri baada ya hapo kwa msaada wa mwajiri wako.

Kwa bahati mbaya maisha halisia hayana ramani wala mwongozo. Wale wanaofuata ramani mara nyingi hawapati mafanikio. Mafanikio huenda kwa watu wasiofuata ramani.

Hawa ni wale wanaojitambua na kujua wanataka nini katika njia ya mafanikio. Hawaongozwi na ramani kwa sababu ramani ina kawaida ya kuwapeleka watu kule ambako kila mtu anakwenda.

Ramani inatabirika na ndiyo maana kila mtu anaifuata. Na kwa vile kila mtu anaifuata njia hiyo inakuwa nyembamba, yenye mbanano inayowafanya wengi wao wakose hewa na kuishia njiani.

Ili ufanikiwe katika maisha halisia unapaswa kujitambua, kujiamini na kuwa tayari kutimiza ndoto zako bila kulazimika kupita katika njia zilizopo zinazotabirika.

Inuka, jitoe, fuata ndoto zako bila kujali kama utafanikiwa ua la, na amini kuwa jinsi unavyofuata maelekezo ya ndoto zako ndivyo unavyozidi kuunganisha nukta zinazokupeleka katika mafanikio.

Kwa leo niishie hapa. Katika sehemu ya pili ya makala haya nitajadili sababu nyingine tano zinazowafanya ‘vipanga’ darasani kushindwa kuhimili maisha binafsi ya kujitegemea na kupiga hatua katika maisha halisia.

Hatua ya kuchukua: Kwa kuwa ni ukweli mchungu kwamba elimu ya darasani haimuandai mwanafunzi kujenga upeo mkubwa wa kufikiri na kujitegemea, inatupasa sasa kuikumbatia elimu ya maisha halisia ambayo inakupa maarifa na mbinu za kupata mafanikio halisia.

Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasirimali kivitendo.

Anapatikana kwa simu: 0718219530; e-mail: nzyy2001@gmail.com

Zijue Stadi Muhimu Za Maisha Kwa Kijana…(3)

Habari rafiki,

Katika sehemu ya kwanza na ya pili ya makala hii nimejadili jumla ya stadi tisa za maisha ambazo yampasa kijana mwenye umri wa miaka 13 hadi 19 kuzijua ili aweze kujitambua mapema na kuwajibika ipasavyo.

Sasa, kama wewe ni mzazi basi ujuwe una wajibu wa kuhakikisha kijana wako anapata stadi hizi ili zimsaidie kuwa kijana bora, anayejitambua na anayeweza kuwa tegemeo kwa jamii na Taifa.

Maarifa ya kufikiri na kuitazama dunia kwa jicho la udadisi ni muhimu sana kwa kijana

Na kama wewe ni kijana uliye katika umri huu, kuna mambo au stadi ambazo unapaswa kuzifahamu ili upate maarifa sahihi juu ya maisha yako na uweze kuwajibika kikamilifu.

Katika makala hii nitajadili stadi nyingine nne, ikiwa ni nyongeza ya zile tisa zilizojadiliwa katika sehemu ya kwanza na ya pili, kama ifuatavyo:

Kumi, maarifa ya kujiepusha na hatari. Haya ni maarifa muhimu sana kwani yanalenga kumhakikishia kijana usalama wake. Mzazi unapaswa kumsaidia kijana wako kujiepusha na hatari kwa kuchukua tahadhari mapema.

Mshauri kijana wako ajiepushe na kutembea peke yake usiku au mchana kwa maeneo yenye viashiria vya hatari. Dunia imebadilika, hivyo kijana asipende kusafiri na watu asiowajua, hasa usiku.

Anaposafiri kwenda mahala ambapo hapendelei kwenda mara kwa mara ni vyema akamtaarifu ndugu au rafiki, ili lolote likitokea iwe rahisi kufuatilia.

Kama anasafiri na akafika usiku sana mwisho wa safari yake, inashauriwa akodi gari linaloeleweka kumpeleka nyumbani au loji, la sivyo ni bora angojee kuche ndipo aondoke kituoni.

Usalama binafsi maeneo ya nyumbani ni muhimu. Mhimize kijana ajenge tabia ya kufunika mashimo au mitaro iliyo maeneo ya nyumbani. Vitu kama mawe, magogo, visiki n.k, viondolewe au vipangwe ki-usalama.

Vifaa vya kulipuka vinavyotumia gesi au umeme viachwe vikiwa salama kila wakati kijana akiwa nyumbani au akisafiri, kuepusha balaa la moto.

Kujiepusha na wezi au vibaka nyumbani kijana anapaswa kujua umuhimu wa kuimarisha milango na madirisha kwa vyuma (grill) kupunguza athari za wezi.

Kumi na moja, elimu ya utatuzi wa matatizo. Kijana akianza maisha yake hapaswi kurudi-rudi nyumbani au kupiga-piga simu kila wakati kuomba msaada akipatwa na matatizo. Anapaswa kuyatatua yeye mwenyewe!

Mfundishe kijana wako kuyakabili matatizo na siyo kuyakimbia. Tatizo likimjia awe na uwezo wa kujua na kupima uzito wa tatizo. Akishajiridhisha na uwepo wa tatizo atafute limesababishwa na nini.

Akijua chanzo cha tatizo atumie akili yake kuorodhesha njia kadhaa za utatuzi – kisha kati ya njia hizo achague moja yenye tija na gharama nafuu zaidi.

Anaweza kuomba ushauri lakini uamuzi wa mwisho ni vyema uwe wa kwake mwenyewe, kwani hiki ndicho kipimo cha kukomaa kiakili.

Kumi na mbili, maarifa ya kujifunza. Dunia inakimbia kasi mno na kila siku teknolojia anabadilika. Mhimize kijana wako kujifunza kila siku vitu vyenye tija kwa maisha yake.

Mhimize asikubali kupitwa na wakati kwenye fani yake au fani mtambuka. Mhimize kusoma, kusikiliza na kutazama kwa kuelewa – vitabu, magazeti na vyombo kama redio, TV na mitandao ya kijamii.

Kumi na tatu, elimu ya kujiajiri. Katika umri wa miaka 13 hadi 19 kijana anatakiwa kuwa katika mafunzo ya maandalizi ya maisha yake binafsi.

Kama kijana amefanikiwa kujiunga na elimu ya sekondari au hajapata fursa hii, ni wajibu wa mzazi kuanza taratibu kumuandaa kijana wake kujitegemea.

Ili aweze kujitegemea ni lazima apatiwe stadi za kumwezesha kujiajiri. Na ili aweze kujiajiri kijana anapaswa angalau kuwa na maarifa yafuatayo;

  • Mbinu za ujasiriamali na ubunifu,
  • Mbinu za mawasiliano na watu au taasisi,
  • Mbinu za kufikiri, kuchambua mambo na kutatua matatizo,
  • Jinsi ya kutumia teknolojia kwa manufaa,
  • Uandilifu, uaminifu na uwezo wa kuthamini kazi,
  • Mbinu za kuyazoea mazingira tofauti-tofauti ya kazi,
  • Kujitambua, kutambua vipaji vyake na mbinu za kukuza vipaji.

Hatua ya kuchukua. Pamoja na msaada wa taasisi za elimu, bado malezi kwa kijana wako ni wajibu wako mzazi. Unapaswa, mapema kabisa, kumsaidia  kijana wako kuwajibika na kuwa kijana bora wa kutegemewa katika jamii.

Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasirimali kivitendo.

Anapatikana kwa e-mail: nzyy2001@gmail.com; Simu 0718219530

Zijue Stadi Muhimu Za Maisha Kwa Kijana…(2)

Habari rafiki,

Katika sehemu ya kwanza ya makala hii nilijadili stadi tano za maisha ambazo yampasa kijana mwenye umri wa miaka 13 hadi 19 kuzijua ili aweze kujitambua mapema na kuwajibika ipasavyo.

Kwa mujibu wa Alternative Homes for Youth, mtu anakuwa kijana akiwa na umri kati ya miaka 13 na 19.

Sasa, kama wewe ni kijana uliye katika umri huu, kuna mambo au stadi ambazo unapaswa kuzifahamu ili upate maarifa sahihi juu ya maisha yako na uweze kuwajibika kikamilifu.

Stadi za mawasiliano yenye tija ni muhimu sana kwa kijana

Na kama wewe ni mzazi basi ujuwe una wajibu wa kuhakikisha kijana wako anapata stadi hizi ili zimsaidie kuwa kijana bora, anayejitambua na anayeweza kuwa tegemeo kwa jamii na Taifa.

Katika makala hii nitajadili stadi nne zaidi, ikiwa ni nyongeza ya zile tano zilizojadiliwa katika sehemu ya kwanza, kama ifuatavyo:

Sita, maarifa ya usimamizi wa mambo ya nyumbani. Wapo wazazi ‘wanaowapenda sana watoto wao. Wanawafanyia vijana wao kila kitu, hivyo kuwanyima maarifa muhimu. Wanachokisisitiza wao ni bidii ya kusoma, basi.

Sasa, piga picha. Kijana wako tayari amemaliza chuo na kapata kazi katika kampuni. Huyu sasa anaanza maisha yake binafsi, na mzazi haupo naye.

Kijana huyu alizoea mteremko. Alizoea kufanyiwa kila kazi, ikiwa ni pamoja na usafi wake binafsi na hata kuandaa mlo. Sasa ghafla anajikuta yuko peke yake; na maisha yanapaswa kuendelea. Kijasho kinaanza kumtoka!

Kuepusha dhahama hii, mfundishe kijana wako maarifa ya kuishi peke yake, yaani kujitegemea. Kwa mfano, mjengee nidhamu ya kulipa kodi ya nyumba; bili za umeme na maji na vitu kama hivyo.

Ajuwe utunzaji wa nyumba na kufanya marekebisho madogo-madogo kama ya vitasa, swichi, holder za taa n.k.

Maarifa haya kijana akiyajua mapema yatampunguzia kuchanganyikiwa na kuona maisha magumu, wakati hali halisi haiko hivyo.

Saba, elimu ya chakula na lishe. Haya ni maarifa muhimu kabisa kwa kuwa chakula ni maisha.

Kijana anapaswa kujua chakula kinanunuliwa wapi kwa gharama nafuu. Mfundishe kijana namna na umuhimu wa kujiandalia chakula chake nyumbani, badala ya kula magengeni au hotelini.

Ajue kuchagua chakula sahihi, kilicho kamili, kwa ajili ya kujenga afya yake. Mfundishe kutumia vifaa vya jikoni kama jiko la gesi, blender, microwave na jiko la mkaa, kwa maandalizi ya chakula.

Msaidie ajue namna ya kutunza chakula kisiharibike kwa kutumia friji au kukausha chakula kwa jua au moto. Msaidie pia ajue kusoma lebo za maelekezo ya matumizi ya chakula na dawa.

Nane, stadi za mawasiliano. Katika umri huu kijana wako anajiandaa kuanza kujitegemea. Kwa hiyo atalazimika kutafuta taarifa na maarifa kwa watu wengine.

Mawasiliano ni stadi muhimu sana kijana kuwa nayo. Kijana ajue kuongea na kusikiliza kwa umakini.

Kabla ya kufanya mawasiliano yoyote kijana ajue anataka kupeleka ujumbe gani na kwa nani. Hii itamsaidia kujua atumie njia gani kuufikisha ujumbe huo ili apate mrejesho chanya.

Katika dunia ya sasa ya utandawazi na matumizi ya mitandao ya kijamii ni muhimu sana kumtahadhalisha kijana wako ili asijiingize katika matumizi ya hovyo ya mitandao hii, kwani ina madhara. Akiitumia vizuri atanufaika.

Tisa, elimu ya tabia na maadili mema. Tabia ya mtu hujionesha kwa mambo anayofanya, namna anavyoongea, anaongea nini, na jinsi anavyoishi na wenzake.

Msaidie kijana wako kuwa na tabia njema. Ajue kuwasiliana vyema na watu wote. Ajue kuomba akiwa na shida, na kushukuru akipewa msaada. Awe mkweli, asimamie anayoyaamini, na akubali kukosolewa akikosea.

Hatua ya kuchukua leo. Malezi kwa kijana wako ni wajibu wako mzazi, hivyo unapaswa kutimiza wajibu wako mapema ili umsaidie kijana wako kuwajibika na kuwa kijana bora wa kutegemewa katika jamii.

Katika sehemu ya tatu ya makala hii nitajadili stadi zilizobaki ambazo ni muhimu kwa kijana wako.

Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasirimali kivitendo.

Anapatikana kwa e-mail: nzyy2001@gmail.com; Simu 0718219530