Habari rafiki,
Ujana unaelezewa kama kipindi cha maisha ya mtu kati ya utoto na utu uzima, ingawa umri ambao mtu anahesabiwa kuwa ni kijana unatofautiana duniani kote.
Kwa mujibu wa Benki ya Dunia, mtu anakuwa kijana akiwa na umri kati ya miaka 15 na 24. Na kwa mujibu wa Alternative Homes for Youth, umri wa kijana ni kati ya miaka 13 na 19.
Kwa muktadha wa makala hii nitajadili stadi muhimu ambazo kijana wa kiume na kike anatakiwa kuwa nazo anapokuwa katika umri wa miaka 13 hadi 19. Kwa kiingereza kijana huyu anaitwa teenager.
Kama wewe ni kijana uliye katika umri huu, kuna mambo au stadi ambazo unapaswa kuzifahamu ili upate maarifa sahihi juu ya maisha yako na uweze kuwajibika kikamilifu.

Na kama wewe ni mzazi basi ujuwe una wajibu wa kuhakikisha kijana wako anapata stadi hizi ili zimsaidie kuwa kijana bora, anayejitambua na anayeweza kuwa tegemeo kwa jamii na Taifa.
Maisha yanakwenda mbio sana na siku hazigandi. Kijana utashangaa, kabla hujakaa sawa, tayari unajikuta wewe ni mtu mzima. Sasa, kama hukujiandaa vyema, ukapata stadi muhimu, utajikuta unaonekana kituko.
Kwa upande wa mzazi, usije kushangaa kumwaona kijana wako anaishi maisha ya ovyo, yasiyo na mpangilio wala maadili; yaani anakuwa na tabia zinazoudhi na zisizompatia heshima katika jamii anamoishi.
Sasa, kama unataka kumsaidia mwanao asipatwe na fedheha katika maisha yake, wala asikutie aibu wewe mzazi wake, basi msaidie kupata stadi hizi.
Katika makala hii nitajadili stadi tano kama ifuatavyo:
Moja, usafi binafsi na utanashati. Nimejadili huko nyuma kuwa mtoto anaanza kufundishwa suala la usafi kabla hajatimiza miaka 10.
Mtoto anapofikisha umri wa ujana bado mzazi unapaswa kutia msisistizo ili kijana aweze kufanya usafi mwenyewe pasipo kusimamiwa. Hivyo msisitize kijana wako kuwa mtanashati.
Kwa kijana wa kiume na kike; vitu kama kuoga, kufua, kupiga pasi, kukunja nguo na kuzipanga kabatini, kunyoa au kuchana nywele n.k, ni vya lazima.
Kwa wasichana kuna masuala kama kusuka na yale yanayohusu usafi wakati wa hedhi, kwake yeye binafsi na kwa mazingira.
Pili, usafi na uboreshaji wa mazingira. Kijana wako anatakiwa kujua kufanya usafi na kuboresha mazingira ya ndani na nje ya nyumba.
Ajue kukwatua majani kando ya nyumba; kuzoa taka na kuzihifadhi sehemu sahihi; usafi wa chumba, choo na jiko; na kuondoa vikolokolo vilivyozagaa bila utaratibu nje na ndani ya nyumba.
Tatu, elimu ya afya binafsi na huduma ya kwanza. Kuwa na uwezo wa kujali afya yake binafsi na ya wenzake ni kitu cha msingi kwa kijana.
Elimu ya lishe bora, yaani ale chakula gani na kwa utaratibu gani; maarifa ya kuepuka magonjwa; na jinsi ya kutibu magonjwa madogomadogo kama mafua, homa na michubuko ni vitu muhimu kufahamu.
Maarifa ya kutoa huduma ya kwanza; kama kusafisha kidonda, kufunga bandeji na kumsaidia mtu aliyeungua kawaida na moto ni muhimu pia. Ajue pia kuwa tatizo likizidi uwezo wake atafute msaada wa daktari.
Nne, maarifa ya jamii na tabia njema. Usisubiri hadi kijana wako apewe majina ya ajabu-ajabu kutokana na tabia zake. Mfundishe mwanao tabia na maadili mema.
Mfundishe heshima na unyenyekevu kwa watu wote. Mfundishe kusalimia kila mtu kulingana na umri wake. Mpe maarifa ya kumkaribisha mgeni na kumhoji ili apate taarifa muhimu.
Msaidie kijana wako ajue kuishi vizuri na watu wote, na ajue kujenga urafiki bora. Ajue pia kutoa mawazo yake na kuheshimu mawazo ya wengine, na kujiepusha na lugha chafu kama matusi, kejeli na umbeya.
Tano, maarifa ya kupangilia mambo yake. Mtu akizoea kufanya mambo bila mpangilio hupoteza muda na rasilimali nyingine bila sababu.
Mfundishe kijana wako kuwa na mpangilio wa kazi na vitu vyake. Ajue ratiba ya kufanya kazi zake; yaani nini kifanyike, wakati gani, na kwa utaratibu gani.
Ajue kuweka kila kitu mahala pake, yaani vitu vinavyofanana vikae sehemu moja. Mpangilio mzuri unapendezesha mazingira, unafanya kila kitu kujulikane kilipo, unaondoa msongo wa mawazo na kufanya vitu vifanyike kwa wakati.
Hatua ya kuchukua leo. Malezi kwa kijana wako ni wajibu wako mzazi. Lakini pia ni wajibu wa kijana mwenyewe kujitambua mapema na kuchukua hatua ya kujifunza stadi muhimu za maisha.
Ukitimiza wajibu wako mapema na ukamfanya kijana wako kuwajibika utamtengeneza kuwa mtu bora katika jamii.
Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasirimali kivitendo.
Anapatikana kwa e-mail: nzyy2001@gmail.com; Simu 0718219530








