Habari rafiki,
Karibu tena katika makala hii tujifunze stadi za maisha. Kwa mujibu wa Shirika la Afya Duniani (WHO) stadi za maisha ni elimu yenye lengo la kujenga tabia njema ya mtu na kumpa uwezo wa kubaini fursa na matatizo yake – na kujua mbinu za kushughulika nayo.
Lengo la stadi za maisha ni kukuza na kuendeleza stadi zinazohitajika katika maisha ya kila siku, mfano kufanya maamuzi.
Makala ya leo itajikita katika kitu kiitwacho ‘kipaji cha mtoto’ na nafasi ya mzazi katika kushughulika nacho.

Mhubiri mmoja amewahi kusema kuwa Mungu alipomuumba mtu aliweka vipaji ndani yake. Kipaji ni uwezo asilia alionao mtu unaomwezesha kutenda mambo yenye matokeo makubwa kwa kutumia nguvu au rasilimali kidogo.
Kinachompa mtu huyu nguvu ya kuendelea kufanya ni ile motisha iliyomo ndani mwake.
Moja ya changamoto zinazowakabili wazazi kuhusu suala la vipaji ni kutokujua kama mtoto wake ana kipaji. Changamoto nyingine ni kushindwa kukinoa kipaji kilichogundulika na kukitumia kiuchumi kutengeneza pesa.
Mwandishi mmoja anasema kuwa kutokujua kipaji alichonacho mtu ni chanzo kimojawapo cha umaskini. Kwa hiyo ni jambo muhimu katika familia au jamii kuwa na utaratibu wa kuvibaini na kuviendeleza vipaji vya vijana wetu.
Nchi zilizoendelea kama Marekani zimepiga hatua kubwa katika hili ambapo katika nchi hizi, vijana huendelezwa katika fani au stadi wanazozipenda. Kwa kufanya hivi vipaji vyao hukuzwa kirahisi hadi kufikia uwezo wa juu.
Watu mashuhuri na wabunifu kama Steve Jobs, mwanzilishi wa Apple, na Mark Zuckerberg, mwanzilishi wa Facebook – ni mifano hai ya watu waliofanikiwa kiubunifu na kimaisha kupitia vipaji vyao – vilivyoendelezwa.
Tatizo tulilonalo katika nchi yetu, Tanzania, ni ushiriki mdogo wa wazazi kwenye maendeleo ya watoto wao walio na vipaji; yaani kushindwa kuvibaini, kuvikuza na kuvibadilisha kuwa pesa.
Tunao watoto wengi tu wenye vipaji, lakini ni wazazi wangapi wanaojishughulisha kujua mtoto wake anapendelea nini kama ishara ya kipaji alicho nacho?
Na katika eneo la taaluma je, ni wazazi wangapi wanaofuatilia kujua mtoto wake anamudu au hamudu zaidi masomo gani ili ajipange kutoa ushauri au msaada?
Mzazi kuwa na taarifa hizi ni jambo muhimu kwani zinakusaidia kujua ni kwa namna gani umsaidie mwanao, kwa kushirikiana na walimu, ili kumpatia mtoto uelekeo ulio sahihi katika maisha yake.
Ikigundulika kuwa mtoto wako ni mzuri upande wa kipaji fulani, mfano kuchora, mzazi na mwalimu mna wajibu wa kumsaidia mtoto huyu kukinoa kipaji hiki – badala ya kulazimisha mtoto asome taaluma asiyoipenda.
Kuna tabia inayofanywa na wazazi wengi tu ya kumlazimisha mtoto kusomea fani ambayo ni chaguo la mzazi. Wapo wazazi eti kwa kuwa yeye amesomea fani ya uhandisi, kwa mfano, basi atashinikiza mtoto wake asome sana hisabati, ili naye aje asomee uhandisi.
Huenda mtoto huyu ana kipaji cha uigizaji, uandishi vitabu au ubunifu mitindo, na mwenyewe anakipenda kipaji chake; kitendo cha mzazi kumlazimisha kufanya kitu asichokipenda kina madhara makubwa.
Mtoto aliyelazimishiwa fani asiyoitaka anaweza kufaulu na hatimaye akaajiriwa katika kazi hiyo. Lakini atakapokuwa ndani ya ajira hiyo ufanisi wake utakuwa wa kiwango cha chini.
Huyu atafanya kazi kinyonge, na atakosa ubunifu kwa sababu kazi aifanyayo haina msukumo kutoka ndani.
Na ikitokea mtoto huyu akakosa kuajiriwa haitakuwa rahisi kwake kujiajiri mwenyewe kwa sababu ya kukosa hamasa na ubunifu kupitia fani aliyolazimishwa kuisomea.
Kijana mwenye kipaji halafu akasaidiwa kukikuza na kukinoa, huyu hawezi kukosa ajira. Kwa upande mmoja anaweza kuwavutia watu, kwa kipaji chake, na wakaamua kumwajiri katika kampuni zao.
Kwa upande mwingine mtoto mwenye kipaji ana uwezo mkubwa wa kukitumia kipaji chake kujiajiri yeye mwenyewe – akajipatia kipato na kupiga hatua kubwa kimaendeleo.
Mfano mzuri wa hili ni mchoraji mahiri wa katuni, Masoud Kipanya.
Hatua ya kuchukua: mzazi usilazimishe mwanao aelekee upande wako kitaaluma wala kiujuzi. Msaidie kukijua kipaji chake, kisha msaidie kukinoa na kukibadilisha kuwa pesa.
Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasirimali kivitendo.
Anapatikana kwa e-mail: nzyy2001@gmail.com; Simu 0718219530








