Habari rafiki,
Sababu kubwa inayofanya watu wachelewe kufanya – waahirishe kufanya – au wasifanye kabisa kazi au majukumu waliyopanga au kupangiwa kufanya ni moja tu…ukosefu wa nidhamu!
Hili huonekana wazi katika kazi mbalimbali za kuajiriwa, ambapo, mwajiriwa asipotimiza wajibu wake kabisa au akichelewa kufanya kazi yake kwa ubora au muda uliopangwa, anaadhibiwa kwa mujibu wa taratibu za kinidhamu.
Kwa hiyo kumbe nidhamu ni jambo muhimu sana katika kufanikisha utendaji wa kazi yoyote.

Kifupi, nidhamu ni ile nguvu ya ndani iliyojengeka kwa mtu inayomsukuma mtu huyo kufanya mambo kwa wakati, umakini, ujuzi na usahihi wa hali ya juu ili kufikia kusudio fulani.
Yaani nidhamu ni kitu kinachotoa msukumo au uwezo binafsi unaomwezesha mtu kuinuka na kufanya kitu au kazi anayopaswa kufanya – na aifanye bila kujali anajisikia kufanya au la.
Nidhamu inaelezewa pia kama ile hali ya mtu kuwa na utii, heshima, unyenyekevu na umakini katika kufuata kanuni, sheria na miongozo mbalimbali ili kuyafikia malengo tarajiwa.
Kwa sababu hiyo, ndio maana mtu mwenye kiburi na dharau; ambaye hafuati sheria na kanuni; na anayefanya mambo ya aibu mbele za watu, husemwa kuwa hana nidhamu. Nidhamu humfanya mtu aheshimike na aonekane wa kipekee tofauti na wengine.
Watu wengi hupenda kupata matokeo mazuri katika kazi, biashara, masomo, ndoa na mambo ya kijamii. Hata hivyo, tatizo linalowakabili wengi, wakashindwa kupata matokeo hayo, ni kushindwa kuwekeza katika kujenga nidhamu binafsi.
Hebu mfikirie mtu anayeamka mwenyewe saa kumi alfajiri akikatiza usingizi wake – akitoka nje usiku wenye baridi kali au mvua ikinyesha – ili akafanye kazi au jukumu alilojipangia au kupangiwa kufanya.
Huyu, sio kwamba anafanya hivyo kwa sababu anajisikia sana kufanya kazi hiyo; au sio kwa vile ni muhimu sana kazi hiyo kufanyika; au siyo kwa sababu asipofanya kazi hiyo atamuudhi mtu fulani – hapana.
Kwa sababu… wapo watu ambao hukaidi au kuchelewa kufanya kazi zao muhimu au kazi walizopangiwa kufanya na viongozi wao kwa sababu hawajisikii tu; na wakati mwingine wako tayari hata kuadhibiwa kwa kosa hilo.
Kwa hiyo, kitu kinachomfanya mtu ainuke na kujituma kufanya kazi au kutimiza wajibu bila kujali mazingira yanayomzunguka ni nidhamu binafsi aliyojijengea yeye mwenyewe.
Utakuta mtu huyu kabla ya kulala usiku, anajipa ‘ahadi’ ya dhati kabisa kuwa ni lazima aamke alfajiri sana, bila kujali mazingira, na aanze kufanya kazi aliyojipangia au kupangiwa kufanya.
Ile ahadi anayojipa mtu – kwamba ni lazima ainuke ili afanye kitu fulani bila kujali hali – ndiyo nidhamu yenyewe – na ndiyo msukumo au kichocheo kinachomwezesha kuinuka na kufanya.
Nidhamu ni chumvi au kirutubisho kinachounganisha malengo mazuri aliyojiwekea mtu na bidii anayoweka katika kutekeleza au kuyafikia malengo hayo.
Nidhamu ni nguvu au msukumo unaokuwezesha kuwa na uthibiti wa mambo au maamuzi yako mwenyewe pasipo kulazimishwa na nguvu ya mazingira yanayokuzunguka.
Nidhamu hujenga nguvu ya mwili na akili, na hali ya kujiamini, na humfanya mtu ajipambanue miongoni mwa wengi kama mtu aliyekamilika na kukomaa.
Kwa hiyo, hatua ya kuchukua leo ili uweze kufanikisha kazi au biashara yako ni lazima ujenge nidhamu binafsi. Ni nidhamu ndiyo itakupa msukumo wa kutenda kwa wakati, umakini, ujuzi na usahihi wa hali ya juu ili kuyatimiza malengo yako.
Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasirimali kivitendo.
Anapatikana kwa e-mail: nzyy2001@gmail.com; Mobile: 0718219530








