Habari rafiki,
Matokeo ya utafiti wa wataalamu wa ubunifu Beth Jarman na George Land yanaonyesha kwamba hadi kufikia umri wa miaka mitano, asilimia 98 ya watoto wana uwezo mkubwa wa ubunifu. Wanapokuwa watu wazima idadi hiyo hushuka kufikia asilimia 2 tu.

Wakiongozwa na udadisi na uthubutu, watoto huweza kutengeneza vitu mbalimbali kwa kutumia vifaa vinavyopatikana katika mazingira yao. Mtoto atajenga nyumba kwa kutumia miti, mbao au udongo; au atatengeneza vifaa vya jikoni kwa kutumia makopo au vifuu vya nazi; au atatengeneza mpira kwa kutumia makaratasi na vipande vya nguo.
Wakati anafanya ubunifu huu hebu mchunguze mtoto. Utakuta mtoto yuko ‘focused’ – yaani akili na viungo vyake vyote vimezama katika kuhakikisha anapata ufanisi mkubwa wa kile anachotengeneza, na mara nyingi huibuka na kitu fulani kipya.
Sasa, tafiti zinatuambia kuwa asilimia kubwa ya watoto ni wabunifu zaidi ya watu wazima; na ukifuatilia hili utakuta kuna sababu zake. Zifuatazo ni baadhi ya sababu hizo:
Akiwa mdogo, mtoto anaamini kila kitu kinawezekena na kinaweza kufanyika; yaani kila tatizo au changamoto ina utatuzi.
Watoto wengi ni wadadisi na wanatamani kupata majibu kwa kila wakionacho na ndio maana wanakuwa wabunifu. Kinachochochea ubunifu wao ni uwezo wao wa kuuliza maswali, ‘kwa nini’, na ‘nini kitatokea?’ Kwa mfano, kwa nini nikishika moto naungua? Au, hivi nini kitatokea nikichanganya sukari na chumvi?
Mwanzo maswali haya wanajiuliza wao wenyewe, na wasipopata majibu huwa wanayasogeza kwa watu wazima.
Kwa mfano mtoto mdogo aitwaye Richie Stachowshi alimuuliza baba yake, “hivi baba kwa nini watu hawawezi kuongea na kusikilizana wakiwa ndani ya maji?”
Hili ni swali fikirishi sana, na bahati nzuri baba yake alilipa uzito mkubwa. Utafutaji wa majibu kwa swali hili umewezesha kugunduliwa kwa kifaa cha kuongelea ndani ya maji bila kuhitaji watu au vifaa vya majini kuunganishwa kwa waya.
Watoto hufanya mambo yao kwa uhuru na hawaogopi kujaribu . Watoto wako huru kufanya chochote wanachohitaji na wala hawabanwi na hisia za kuwepo kwa vikwazo.
Ukweli watoto hawafikirii kuwa vitendo vyao vinaweza kuwaudhi au kuwaletea madhara wengine. Kila wanachokifanya wanafanya kwa nia njema kabisa. Akili yao inawaelekeza kuwa wao hawana uadui wala mgogoro na yeyote, hivyo hawana hatia kwa lolote wanalofikiria kufanya.
Watoto wanafanya vitu wakiwa hawabanwi na uwajibikaji kwa mtu yoyote na hivyo hawana hofu kwamba wanaweza kufanya makosa na wakawajibishwa. Vilevile, watoto hawana mawazo ya kufeli, wala hawajali matokeo ya kufeli. Wao kinachoingia katika anga zao wanaanza kukifanya. Kwamba watafaulu au watafeli – hilo kwao sio suala.
Kwa upande mwingine, watoto hawako ‘busy’ na majukumu ya kila siku ya utafutaji wa maisha au uwajibikaji, na kwa sababu hiyo wanapofikiria kufanya kitu wanapata nafasi nzuri ya kutuliza akili na kufanya vitu kwa umakini.
Katika ubunifu watoto wanaongozwa na ‘imaginations’ au fikra bunifu, hivyo wana uwezo wa kuunda picha ndani ya nafsi zao ya kitu wanachokitaka hata kama hawajawahi kukiona au hata kukisikia.
Asili ya watoto ni kujaribu. Na wakijaribu kufanya kitu kipya kwa kutumia njia fulani halafu wakiona hawapati matokeo, hujaribu njia tofauti hadi wapate walichokusudia.
Watoto wanakuwa wabunifu kwa kuwa muda mwingi wanafanya kazi za sanaa kwa vitendo. Watoto wanapenda kuchora, kupaka rangi, kufinyanga, kupika, kulea watoto n.k. Hivyo, kuchezeachezea sana kazi za sanaa huwapatia watoto uwezo mkubwa wa kujenga fikra bunifu.
Kazi za sanaa anazofanya mtoto zinavikomaza viungo vyake kama ubongo, macho na mikono, na kuvifanya viweze kushirikiana na kutegemeana katika kuumba; na hapo ndipo ubunifu unapojitokeza.
Mtafiti Suzan Engel anasema watoto wa miaka mitatu wanaelewa tofauti kati ya kitu halisi na kitu cha kufikirika au kuigiza. Ukichunguza hili utakubaliana naye.
Utaona, watoto wakiwa katika maigizo au michezo yao, suala la uhalisia sio muhimu sana – cha muhimu kwao ni kufanya kile hisia zao zinawatuma – basi! Kwa mfano, mtoto mmoja kujifanya punda na mwingine kujifanya mwenye punda, na hivyo kumpanda mwenzake mgongoni na kumswaga – hili kwao ni kitu cha msingi kuliko kufikiria uhalisia.
Kutokana na hili mwanasayansi Einstein anasisitiza kuwa kujenga fikra bunifu au ‘imaginations’ ni muhimu zaidi kuliko kuwa na ufahamu unaotokana na elimu au kujifunza. Ni hisia za ndani anazojenga mtu – ambazo hutoa msukumo katika ubunifu.
Hatua ya kuchukua ni kwamba sisi wajasiriamali, kama tunataka kuwa wabunifu ni lazima tuanze kufikiri na kutenda kama watoto. Watoto wana uthubutu na hamasa kubwa ya kutengenezea kazi za sanaa.
Tukitumia mitazamo na mbinu fulani wanazozitumia watoto tunaweza kujenga uwezo mkubwa wa ubunifu utakaotusaidia kuongeza thamani na tija katika kazi au biashara zetu.
Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasirimali kivitendo.
Anapatikana kwa e-mail: nzyy2001@gmail.com; Simu 0718219530









