Jinsi Ya Kupunguza Gharama Za Biashara Yako…(1)

Habari rafiki,

Karibu tena katika makala nyingine inayolenga kukupatia maarifa ya ujasiriamali, ubunifu na stadi za maisha.

Ukiweza kupunguza gharama (costs) za uendeshaji – unakaribisha mafanikio

Ukiwa mjasiriamali au mfanyabiashara kuna gharama ambazo utakutana nazo, na hakuna biashara yoyote ambayo haihusishi gharama. Kwa hiyo ni muhimu sana kwa mfanyabiashara kuzifahamu gharama zinazohusiana na biashara zao.

Katika biashara kuna aina mbalimbali za gharama. Zipo zinazoonekana wazi; na zipo pia zilizojificha, ambazo ni vigumu kubainika kirahisi.

Mfano wa gharama zilizo wazi ni pamoja na gharama za bidhaa au malighafi, mishahara ya wafanyakazi, mashine na vifaa vya uzalishaji; na gharama za umeme, maji na usafiri. Gharama zilizojificha ni pamoja na riba, tozo (charges) na kamisheni za benki; gharama za miamala ya simu; na gharama ya bidhaa iliyoharibika.

Mfanyabiashara unapaswa kuzijua gharama hizi ili unapopiga hesabu za biashara yako uweze kujua kwa usahihi mchango wa gharama hizo katika faida au hasara utakayopata. Kumbuka faida au hasara katika biashara inapatikana kwa kutoa gharama kutoka kwenye mapato.

Katika biashara, kuna gharama zinazobadilika na zile zisizobadilika- kutegemeana na kiwango cha uzalishaji wa bidhaa au michakato ya uendeshaji wa biashara.

Kwa mfano, kama unazalisha sabuni za mche kiwandani kwako, ukizalisha miche 100 unaweza kuingia gharama ya jumla ya shilingi 20,000 (malighafi, umeme, maji n.k). Lakini ukizalisha miche 1000 gharama inapanda na kuwa shilingi 180,000. Huu ni mfano wa gharama zinazobadilika kutegemeana na ongezeko la uzalishaji.

Gharama zisizobadilika ni zile zinazobakia vilevile kila mwezi bila kujali kiasi cha biashara au uzalishaji uliofanyika. Kwa mfano, kodi ya pango, mishahara ya wafanyakazi, malipo ya bima n.k.

Baada ya kuzijua gharama za uendeshaji wa biashara, sasa tujikite katika kupanga mikakati ya kuzidhibiti au kuzipunguza.

Kumbuka, katika mazingira magumu ya biashara kila pesa ina thamani. Kwa hiyo mfanyabiashara unapaswa kuwa makini sana. Yaani, hata pesa ndogo kabisa iingiayo kama mauzo, au pesa kidogo inayotoka kama gharama; vina maana sana katika tathmini ya mafanikio ya biashara hiyo.

Kwa hiyo, ni wajibu wako kila baada ya muda fulani kupima gharama zilizotumika na kufanya tathmini. Kila mara jiulize je, gharama zangu ni sahihi na zenye ulazima? Je, kuna chochote cha kurekebisha ili kupunguza gharama hizi? Jibu utakalopata lifanyie kazi haraka.

Makala hii itakupatia njia nne kati ya kumi za kudhibiti au kupunguza gharama za uendeshaji wa biashara; na makala ijayo itakupatia njia sita.

Moja, punguza gharama za manunuzi ya bidhaa. Hapa unashauriwa kutafiti kidogo na kisha kununua katika maduka au wagavi wenye bei nafuu, au wanaotoa punguzo (discount) ukinunua bidhaa nyingi.

Mbili, punguza gharama za usafirishaji wa bidhaa. Unashauriwa hapa kuwatumia wasafirishaji wenye bei nafuu. Tafuta usafiri unaolingana na ukubwa au uzito wa bidhaa zako, au changia usafiri na mwenzio mnaofanyia biashara sehemu moja.

Tatu, punguza gharama za uzalishaji. Hapa unashauriwa kukodi eneo au chumba cha biashara chenye unafuu kinacholingana na aina na ukubwa wa biashara yako. Malighafi ya uzalishaji itumike kwa uangalifu ili yote itumike, isije ikaharibika au kwisha muda wake.

Vilevile, malighafi iliyobaki, au bidhaa, zitunzwe vizuri zisiharibike na kuleta hasara. Unapaswa pia kusimamia vizuri wafanyakazi na rasilimali nyingine ili zitumike kwa kiwango cha juu katika uzalishaji au utoaji huduma.

Nne, punguza matumizi ya fedha. Ushauri hapa ni pamoja na kujiepusha na mikopo isio muhimu. Ukilazimika kukopa, angalia riba ni kiasi gani, na je biashara yako ina uwezo wa kumudu riba hiyo bila kuathiri mzunguko wa fedha?

Kama umeamua kukata bima ya biashara yako, chunguza gharama yake ili upate bima yenye tija lakini yenye unafuu.

Hatua ya kuchukua: mjasiriamali unapaswa kuwa makini sana katika kuzijua au kuzibaini gharama za biashara yako na kupanga mikakati ya kuzidhibiti au kuzipunguza kwani zinaathiri faida ya biashara yako. Makala ijayo tutamalizia njia zilizobaki.

Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasirimali kivitendo.

Anapatikana kwa simu: 0718219530; e-mail: nzyy2001@gmail.com

Jinsi Vifungashio Vinavyoongeza Thamani Ya Bidhaa Yako

Habari rafiki,

Karibu tena katika makala nyingine inayolenga kukupatia maarifa ya ujasiriamali, ubunifu na stadi za maisha.

Nianze makala ya leo kwa kusema kwamba kufikiri ni kitu muhimu sana kwa binaadamu. Na ukweli hakuna binaadamu asiyefikiri, kwani chochote unachoamua kufanya ni matokeo ya kufikiri au kuwaza. Kufikiri kunazalisha mawazo ambayo yanaweza kugeuzwa kuwa vitu au matendo halisi.

Hata hivyo, watu wanatofautiana katika kufikiri. Wapo wanaofikiri ki-kawaida tu na hawana kitu kinachowasumbua sana kichwani. Kila kitu kinachopita katika bongo zao kinaonekana ni cha kawaida tu. Lakini wapo watu wanaofikiri kwa umakini na kwa kina. Huku ni kufikiri kimkakati. Watu hawa wana malengo yao ambayo kupitia kufikiri yanaweza kufikiwa.

Wapo watu ambao wanaufikirisha sana ubongo wao kwa lengo la kufanya vitu vitakavyoleta utofauti katika jamii au maisha yao. Hawa wanalenga kufanya ubunifu au uvumbuzi. Matokeo ya kufikiri huku ni kupata kitu kipya au njia mpya na nzuri zaidi za kutatua changamoto.

Sasa basi, moja kati ya njia muhimu katika kukuza biashara au ujasiriamali ni kufanya ubunifu. Yaani kuja na mawazo ambayo yataleta utofauti katika bidhaa, huduma au mchakato wa uzalishaji au utoaji huduma.

Utofauti kati ya bidhaa moja na nyingine unaweza kupatikana katika mwonekano tu wa bidhaa hiyo. Na vitu vinavyobadili mwonekano ni pamoja na vifungashio vya bidhaa hizo.

Ubunifu wa vifungashio huongeza thamani ya bidhaa

Katika jitihada za kuboresha biashara au bidhaa, mjasiriamali unapaswa kulifikiria sana suala la vifungashio. Vifungashio hutumika kutofautisha bidhaa yako na nyingine nyingi zilizoko sokoni –  kupitia muundo, ubora, rangi, dizaini, pamoja na maelezo yanayobebwa na bidhaa hiyo.

Dhana ya vifungashio inaweza kuwekwa katika makundi matatu yanayoelezea thamani ambayo bidhaa inapata kupitia vifungashio hivyo.

Kundi la kwanza, ambalo ni la msingi kabisa ni la kutoa hifadhi kwa bidhaa. Kimsingi vifungashio ni vitu vinavyotengenezwa kwa ajili ya kuhifadhia bidhaa, na hasa kuifanya bidhaa isiharibike kwa urahisi. Vifungashio vinarahisisha usafirishaji wa bidhaa kwa kuifanya ibebeke ki-urahisi lakini pia kuilinda na madhara kama kuvunjika, kulowana, kupigwa vumbi au kushambuliwa na wadudu.

Kundi la pili ni la kisheria au ki-taalamu zaidi. Hapa vifungashio vinatumika kutoa maelezo ya bidhaa husika ili wateja wajue kilichomo ndani ya bidhaa hiyo. Maelezo haya yanahusu malighafi zilizotumika kutengeneza bidhaa husika ambapo mteja huamua kununua au kuacha kulingana hisia ya faida au madhara yanayoweza kuletwa na vitu vilivyomo katika bidhaa hiyo.

Pamoja na hilo, vifungashio vinawekewa pia maelezo ya lini bidhaa hiyo imetengenezwa, na lini muda wake utaisha; vinawekewa alama za uthibitisho wa ubora, mfano TBS; na pia maelezo ya watu gani wanakatazwa kuitumia bidhaa hiyo, mfano watoto au wajawazito.

Kundi la tatu la dhana ya vifungashio linahusisha kitu kiitwacho ‘fahari ya macho’; yaani burudani au hisia ambayo macho yanapata kutokana na jinsi bidhaa ilivyopambwa.

Kifungashio kizuri kinategemea uwezo wa ubunifu alionao mjasiriamali husika; yaani uwezo wa kuitazama dunia kwa jicho la udadisi na kuja na vitu ambavyo watu wengine wakiviona watashangaa, watapata hamasa, na  mwisho wataamua kununua bidhaa hiyo.

Vifungashio bora sio suala la viwanda vikubwa tu; hata wajasiriamali  wadogo wa nyumbani wanahusika!

Katika hili ni kwamba mjasiriamali anatakiwa awe mbunifu na aweze kuipamba bidhaa yake kwa michoro, rangi, vikolokolo, na marembo anuwai ambayo yakitua katika macho ya mteja yatamfanya ashindwe kujizuia kuondoka na bidhaa hiyo, bila hata kujali kilichomo ndani.

Kwa hiyo, ili kuwa na uhakika wa soko la bidhaa zako, mjasiriamali unapaswa kuboresha eneo la vifungashio. Wapo wateja ambao hata kama bidhaa ina ubora mkubwa, hawako tayari kuinunua endapo tu imewekwa katika vifungashio duni, hivyo ukiboresha eneo hili thamani ya bidhaa yako inaongezeka; na mauzo pia yanapaa.

Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasirimali kivitendo.

Anapatikana kwa simu: 0718219530; e-mail: nzyy2001@gmail.com

Hivi Ndivyo Vihatarishi Katika Biashara Yako – Jipange!

Habari rafiki,

Nimeandika huko nyuma kuwa uthubutu ni sifa mojawapo kubwa ambayo mjasiriamali anapaswa kuwa nayo. Usipokuwa na hulka ya kuthubutu huwezi kuwa na uwezo wa kuanzisha kitu – maana kila wakati ukifikiria kuanza unaona haiwezekani, unakata au kukatishwa tamaa, na mwisho hakuna kinachofanyika.

Ukivijua mapema vihatarishi vya biashara yako unaweza kujikinga usidhurike

Sasa basi, unapokuwa tayari umethubutu na uko tayari kuanza kufanya kitu; kwa mfano kufungua biashara ya uzalishaji au uuzaji bidhaa, hutakiwi kuingia kichwakichwa. Unapaswa kuzijua ‘risk’ au vihatarishi vilivyopo ndani au nje ya biashara yako.

Usipovijua vihatarishi na ukajipanga mapema kuviepuka au kukabiliana navyo – vitakapokufikia vitakuwa vimekushtukiza pasipo kujiandaa, na madhara yake yatakuwa makubwa.

Vihatarishi ni matukio ambayo yanaweza au yasiweze kutokea; na yakitokea yanaweza kusababisha hasara; kwa mfano usumbufu, gharama, upotevu wa muda, au kuikosa fursa muhimu. Katika dunia hii ya utandawazi, vihatarishi  vinapaswa kuangaliwa kwa ukaribu na umakini mkubwa.

Ki uhalisia, kila biashara inakabiliwa na vihatarishi ambavyo kimsingi, mtu akikusudia na akiwa makini, anaweza kuvifahamu mapema kabisa, na jinsi vinavyoweza kuiathiri biashara yake, na akaweza kuchukua hatua kuzuia ili visimletee madhara au kufanya madhara yasiwe makubwa.

Tuchukue mfano wa mtu anayesafiri kwenda katika kijiji cha mbali, akikatiza katika msitu mnene. Huyu anapaswa kuulizia au kukisia tu, kabla ya safari, uwepo wa vitu katika msitu huo vinavyoweza kumletea madhara. Hivi ndio viashiria vya hatari, au vihatarishi – kwa mfano uwepo wa wanyama wakali.

Ukivijua vihatarishi mapema unapata fursa ya kujipima kama unaweza kuvikabili au la. Kama unaweza kukabiliana navyo basi unapanga mikakati hiyo na kusonga mbele. Kama huwezi, basi unaachana na safari hiyo. Usipovijua vihatarishi, ukaingia tu msituni, una hatari ya kutofika mwisho wa safari au ukafika ukiwa na majeraha; kwani hutakuwa umejiandaa.

Vifuatavyo ni baadhi ya vihatarishi vinavyozikabili biashara:

Moja, kuzalisha au kuuza bidhaa zenye kasoro au zilizo na viwango duni. Hii inashusha ubora wa bidhaa na hamu ya wateja kwa bidhaa hizo; na madhara yake ni kukimbiwa na wateja.

Mbili, kushindwa kukadiria ipasavyo mahitaji ya bidhaa sokoni. Hii inaweza kuwa kuzalisha juu au chini sana ya kiasi kinachotakiwa na wateja. Ukizalisha kiasi kingi sana na wanunuzi ni wachache, bidhaa inakuharibikia au ‘inashikilia pesa/mtaji’. Ukizalisha bidhaa kidogo hutawatosheleza wateja – na huwenda wakakukimbia, na mauzo yatashuka pia.

Tatu, Kupanga bei bila kuzingatia uhalisia wa soko. Kitisho hapa ni kukosa au kukimbiwa na wateja, na hasa pale washindani wako wanapokuwa na  uwezo wa kupunguza bei – na hasa wanapokuwa wamezalisha kwa gharama nafuu zaidi.

Nne, kutoa huduma mbovu kwa wateja. Huduma mbovu zinazotolewa na wafanyabiashara ni nyingi, na ukweli zina madhara makubwa kwa biashara. Kwa mfano; kushindwa kumkaribisha na kumkarimu mteja, kauli chafu, dharau, maringo, kutoa majibu ya mkato, kutomsikiliza mteja n.k. Madhara ya haya ni kuwafukuza wateja na kushuka kwa mauzo.

Tano, Kufanya biashara zaidi ya moja kwa wakati mmoja hata kabla ya mojawapo kuanza ‘kuchanganya’. Hatari hapa ni kwamba biashara hizi zinaanza kunyang’anyana rasilimali – fedha, muda, akili n.k. Mara nyingi biashara zote hizi hudhoofu, na kufa.

Sita, kushindwa kuweka kumbukumbu za biashara. Kwa mfano, kumbukumbu za mapato, matumizi, wadai, wadaiwa n.k, kila yanapotokea. Hatari hapa ni kukosa kujua nini kinaendelea katika biashara yako. Unakosa mwongozo au dira ya mwenendo mzima wa biashara, na mwisho wake ni hasara.

Saba, kupuuza masuala ya kisheria. Unapofanya biashara unapaswa kuwa na leseni, kulipa kodi, kulipia huduma unazopewa, kama maji na umeme, na kuwalipa mishahara wafanyakazi – kama umeajiri. Ukipuuza, unakabiliwa na kitisho cha faini, kufungiwa biashara au kukatiwa huduma.

Hatua ya kuchukua: Hivi ni baadhi tu ya vihatarishi vya biashara. Hivyo, chunguza biashara yako, chunguza mazingira yako, chunguza uwezo wako wa hali na mali; kisha angalia kama utabaini kitu chochote kinachoweza kuwa kitisho kwa biashara yako, halafu chukua hatua haraka!

Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasirimali kivitendo.

Anapatikana kwa simu: 0718219530; e-mail: nzyy2001@gmail.com

 

Maswali Haya Yatakupatia Msukumo Katika Kufanya Ubunifu

Habari rafiki,

Kwa mjasiriamali, ubunifu ni jambo lisiloepukika kama unataka kupiga hatua au kama unataka kuushinda ushindani wa biashara.

Katika makala ya leo nitakushirikisha nadharia iitwayo Heuristic Framework For Innovation. Yaani, mbinu za kinadharia za kuongeza uwezekano wa kuibua  ubunifu wenye tija unaoweza kutibu changamoto au kuibua fursa katika ujasiriamali.

Ni hivi, baada ya mjasiriamali kufikiri kwa kina, anaweza kupata wazo la kufanya ubunifu fulani. Unaweza kuwa ubunifu wa kazi ya sanaa au mchakato wa utoaji huduma; au ubunifu wa bidhaa au teknolojia mpya; au ubunifu wa kuongeza thamani ya bidhaa ambayo inadhaniwa itaziba pengo la mahitaji ya wateja au jamii. Kwa hiyo, kuna mfumo au mbinu ambayo ikitumika inasaidia kulisimamia zoezi hili la ubunifu kwa ufanisi zaidi.

Mchakato wa ubunifu usipopangiliwa vizuri – utakuchanganya akili!

Mfumo au framework hii ina maswali kadhaa ambayo yakijibiwa yanasaidia kukusanya taarifa zinazoendana na mazingira ya biashara au kampuni husika. Yaani, bila kujali ni mchakato (process) gani itatumika kufanya ubunifu huo, maswali haya yakiulizwa na kupatiwa majibu yanaongeza uwezekano wa kufanyika ubunifu wenye tija.

Maswali yaliyomo katika mfumo huu yanasaidia kubaini maeneo ya hatari hata kabla ya kuanza kwa zoezi la utekelezaji wa ubunifu husika. Kuyajua mapema maeneo hatarishi kunasaidia kujipanga vizuri na kuja na mbinu mbadala za kufanikisha ubunifu tarajiwa.

Yafuatayo ni maswali yaliyomo katika framework hii:

Moja, je ubunifu – au bidhaa tarajiwa italeta au kuongeza tija katika Kampuni au biashara yako? Yaani, bidhaa, teknolojia, au huduma utakayoibuni itaendana na maono au dira ya biashara au Kampuni yako? Na je, italingana au kukubaliana na tamaduni zetu kama jamii?

Pili, je ubunifu huo utaleta manufaa kwako? Yaani; utasaidia kutimiza malengo yako –  kwa mfano, kuongeza wateja, kukuza mapato na faida, kupunguza gharama, au kuongeza ubora na kasi ya utoaji huduma? Je ubunifu huo utasaidia kukuinua kibiashara dhidi ya washindani wako?

Tatu, je ubunifu huo unahitajika sokoni? Yaani; Je ubunifu utasaidia kuziba pengo la mahitaji yaliyopo sokoni sasa ambayo yalikuwa hayajashughulikiwa? Je, utasaidia kuzalisha bidhaa au huduma inayohitajika katika soko jingine ambalo ulikuwa haujaliteka?

Nne, Je, ubunifu utafanyika kwa utaratibu gani? Yaani; Je unaweza kufanya ubunifu huu wewe wenyewe, kwa kutumia maarifa uliyonayo? Au labda inabidi watafutwe watu wengine waje watoe ushirikiano kufanikisha ubunifu huu?

Tano, Je, unaweza kuyapima mafanikio ya ubunifu huu? Hapa maana yake ni kwamba ili ujiridhishe kuwa umefanya ubunifu wa maana ni lazima uwe na kipimo cha kukuwezesha kujua kama umefanya ubunifu sahihi na wenye kutoa majawabu yaliyokusudiwa. Kipimo kinaweza kuwa ongezeko la wateja wanaoihitaji bidhaa iliyobuniwa.

Sita, Je una rasilimali za kutosha kufanya ubunifu huu kwa ufanisi? Yaani, kama ni Kampuni, je uongozi wa juu unaunga mkono ubunifu huu na uko tayari kutoa fedha, muda au msaada mwingine kuufanikisha? Kama ni biashara binafsi, je uwezo au rasilimali zipo? Je, nini kifanyike kuyaweka mambo sawa?

Saba, je kuna vikwazo au changamoto zipi ambazo unaweza kukutana nazo katika zoezi hili? Yaani ni lazima kufikiri kwa umakini ili kujua kama kuna kitu kitakachokwamisha ubunifu huu huko mbele. Kumbuka ubunifu unahusisha matumizi ya akili, muda na fedha. Sasa usipojipanga vizuri utajikuta unaingia katika matatizo.

Hatua ya kuchukua: Mjasiriamali unapaswa kujenga tabia ya kufikiri kila siku. Unapaswa kuitumia vizuri milango yako ya fahamu ili uweze kupata mawazo ambayo yatakuonesha kitu cha kufanya katika kuanzisha au kuboresha biashara yako.

Ukishapata wazo, ukaliona bora, unatakiwa sasa uone jinsi utakavyolifanya liwe kitu halisi kwa kulifanyia utafiti au tathmini kabla ya kulibadilisha kuwa bidhaa au ubunifu utakaoziba pengo la mahitaji ya wateja au jamii. Hivyo framework hii inatupatia mbinu za kusukuma mbele jitihada za kufanya ubunifu wenye tija.

Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasirimali kivitendo.

Anapatikana kwa simu: 0718219530; e-mail: nzyy2001@gmail.com

 

Jinsi Ya Kutumia Mbinu Za Kijeshi Kuboresha Biashara! …(3)

Rafiki,

Makala iliyopita nilikuletea sehemu ya pili ya mada hii,  inayohusu mambo ambayo wafanyabiashara au wajasiriamali wameyachukua au wanaendelea kujifunza kutoka katika majeshi.

Nilikushirikisha kaulimbiu nyingine tatu, kati ya 11, kama zinavyotumika jeshini na namna ambavyo zinaweza kutoa mchango katika kukuza au kuboresha maarifa ya ujasiriamali.

Kisha nikasema, wewe  kama mjasiriamali una cha kujifunza; kwamba kama unataka kuiinua au kuiendeleza biashara yako, unapaswa kujiongeza na kupanga mikakati yako ya biashara kwa uhakika na umakini, na kuitekeleza kwa ujasiri na uhodari, na bila chembe ya woga.

Hivyo, leo tena nitaendelea nilipoishia katika makala iliyopita, na nitakupatia kaulimbiu nyingine tano, za mwisho; kwa mujibu wa mpiganaji mmoja kutoka kikosi maalum cha jeshi la Marekani (Special US Force) ambaye baadaye aliamua kujikita katika ujasirimali.

Rambo ni ‘askari’ aliyeheshimu matendo zaidi – hakupenda maneno mengi, au longolongo

Saba,”Deeds and Not Words.” Yaani; Yanatakiwa Matendo, Na Siyo Maneno.” Kaulimbiu hii ilitungwa na kikosi maalum cha jeshi la majini (Navy) la Canada. Msisitizo wa slogan hii upo katika kuhimiza matendo. Askari hawa wakipanga kufanya operation fulani, kwao hilo ni deni – ni lazima lilipwe!

Sasa, wewe kama mjasiriamali una cha kujifunza. Kwa mfano, kama umewaahidi wateja wako kwamba utawapelekea bidhaa walizonunua hadi kwao, fanya hivyo, usianze kuleta ‘longolongo’. Kama umewaahidi wateja wako kuwa utawapatia huduma bora, ya haraka na kwa upendo, basi timiza ahadi hiyo; yaani fanya, na onesha matokeo kivitendo.

Nane, “If You Wish For Peace, Prepare For War.” Yaani; “Kama Unataka Amani, Jiandae Kwa Vita.” Slogan hii inatoka kikosi cha Navy, UKMsisitizo hapa upo katika kufanya maandalizi mazuri wakati wa amani ili vita ikitokea ikute uko tayari kupambana, kushinda, na kubaki na amani yako.

Kama mjasiriamali, unapaswa kujiandaa na majanga au dharura mbalimbali zinazoweza kutokea na kuiathiri biashara yako. Majanga kama mafuriko, vimbunga, kuyumba kwa uchumi wa nchi n.k.

Au, kwa mfano, ulikuwa unazalisha na kuuza mifuko ya plastic, Tanzania – na ghafla, Serikali inapiga marufuku matumizi ya mifuko hii nchi nzima, je, utafanya nini? Ulijiandaa?

Kwa hiyo, mjasiriamali unapaswa kujenga tabia ya kuweka akiba, ili dharura ikitokea basi akiba ikusaidie kuinusuru biashara yako. Kwa mfano, ikitokea ukashtakiwa kwa masuala ya ki-biashara, ukatakiwa kulipa, basi uwe tayari, ili ukilipa ubaki na amani yako.

Tisa, “Learn To Suffer Without Complaining.” Yaani; Jifunze Kutaabika Pasipo Kulalamika.” Slogan hii imetoka Jeshi la Nchi Kavu la Ujerumani. Kinachohimizwa hapa ni uvumilivu na ubunifu.

Kwa mjasiriamali, siyo kila ukipata tatizo, basi kazi ni kulalamika tu, hapana. Utalalamikia mangapi? Kumbuka matatizo yapo kila siku. Badala ya kulalamika, tumia akili zaidi ili upate utatuzi.

Kwa mfano, utasikia mfanyabiashara analalamika, ‘aah bwana, wateja wangu wanapungua kila siku, hapa siyo bure, kuna namna!” Hapana, acha kulalamika –  jifunze kujua sababu, na  kutafuta majawabu!

Kumi, “No Mission Too Difficult, No Sacrifice Too Great – Duty First!” Yaani; “Ukitimiza Wajibu Wako Hakuna Kitu Kisichowezekana.” Hii slogan inatoka Jeshi la Uingereza. Kinachohimizwa hapa ni kujituma kufanya kazi. Kwamba ukijitoa, na ukatimiza wajibu, lazima utatimiza malengo yako.

Kwa mfano, unapaswa kutimiza wajibu wako kwa wateja, wadau, wafanyakazi wako, wakopeshaji na wabia kama wapo, na vyombo vya serikali pia. Ukifanya hivi, kila kitu kitakuwa chepesi, na biashara yako itashamiri.

Kumi na moja, “The Hard We Shall Do Today, The Wonders We Shall Do Tomorrow.” Yaani; “Jinsi Unavyojituma Leo, Unajiandaa Kufanya Maajabu Kesho!” Slogan hii imetoka Kikosi cha Wahandisi cha Jeshi la Israel.

Hapa, Wajasiriamali tunahimizwa  kujizoeza kukabiliana na vitu au mambo magumu. Jinsi unavyojituma kupambana na changamoto leo, kesho, mwezi ujao, na mara kwa mara, ndivyo unavyojijenga ki-uwezo, na baada ya muda utafanya kitu ambacho kitamshangaza kila mtu.

Hatua ya kuchukua: Tumia mifano ya kaulimbiu hizi ili kujijengea tabia zinazofanana na za kijeshi zitakazokupa motisha, hamasa na ujasiri wa kupambana na changamoto mbalimbali katika ujasiriamali.

Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasirimali kivitendo.

Anapatikana kwa simu: 0718219530; e-mail: nzyy2001@gmail.com

 

Jinsi Ya Kutumia Mbinu Za Kijeshi Kuboresha Biashara! …(2)

Habari rafiki,

Makala iliyopita nilikuletea sehemu ya kwanza ya mada hii,  inayohusu mambo ambayo wafanyabiashara au wajasiriamali wameyachukua au wanaendelea kujifunza kutoka katika majeshi.

Nilitoa mfano wa dhana ya mkakati, au kupanga mikakati; kwamba ni dhana ambayo imezaliwa kutoka jeshini katika karne ya 18; na ni dhana iliyosambaa taratibu kutoka jeshini hadi ikafika katika nyanja za biashara.

Kisha nikakushirikisha kaulimbiu tatu, kati ya 11, kama zinavyotumika jeshini na namna ambavyo zinaweza kutoa mchango katika kukuza au kuboresha maarifa ya ujasiriamali.

Kabla sijaanza kuongelea kaulimbiu hizo, nilikupatia takwimu zifuatazo: “Asilimia 60 ya makampuni makubwa 500 yaliyokuwepo duniani katika mwaka 1970, hayapo kabisa leo.” Sio kwamba yamebadilisha majina, la hasha, yamekufa!

Na nilieleza sababu kubwa ya kufanya yapotee ni kwamba yalikosa mikakati na umakini; yaani hayakuwekeza zaidi katika kupanga mikakati na mbinu bora za kuboresha uzalishaji na utoaji huduma. Kifupi ni kwamba, hayakujiongeza!

Kisha nikasema, wewe  kama mjasiriamali una cha kujifunza katika hili, kwamba kama unataka kuiinua au kuiendeleza biashara yako, unahitajika utengeneze mkakati wako wa biashara kwa uhakika na umakini mkubwa.

Hivyo, leo nitaendelea nilipoishia katika makala iliyopita, na nitakupatia kaulimbiu nyingine tatu, kwa mujibu wa mpiganaji mmoja kutoka kikosi maalum cha jeshi la Marekani (Special US Force) ambaye baadaye aliamua kujikita katika ujasirimali.

Nne, “Peace Through Strength.”  Yaani; “Kuwa na Amani Ndani Ya Uwezo”. Kaulimbiu hii ilitungwa na tume maalum ya jeshi la Marekani, iliyoundwa na Rais George Bush, 2003, kujadili maoni ya Urusi; wakati  wa sakata lililozaa vita kati ya Marekani na Iraq.

Kwa kaulimbiu hii, Wamarekani wanamaanisha kuwa wanapenda amani ingawa wana nguvu kubwa. Yaani, wanadai, “kimsingi tunapenda amani na hatutaki kupigana na wewe; ila ukitaka mapambano tuko tayari,  kwa sababu tukipigana ni lazima tutakushinda. Je, wewe unataka kufanya nini – unataka amani au vita?”

Kwa hiyo, somo tupatalo hapa ni kwamba, wewe kama mjasiriamali jitahidi kujiongezea ‘nguvu’ ili ujihalalishie amani. Tengeneza mikakati thabiti. Jenga uhusiano mzuri na kila mtu, hata washindani wako – ukiwa na lengo la kudumisha amani, lakini pia ukiwa tayari ‘kupambana kiakili” itakapolazimu, ili kulinda maslahi ya biashara yako.

Tano, “Come And Take Them!” Yaani; “Jaribu Kusogea Uone cha Moto” Hii ni kaulimbiu ya kutoka katika jeshi la Ugiriki, chini ya mpiganaji shupavu, Mfalme Leonidas, aliyeongoza vita kujibu uvamizi wa jeshi la Persia au Iran, miaka 2490 iliyopita.

Leonidas, akiwa na askari wapatao elfu sabini, alikaidi amri ya kuweka silaha chini, iliyotolewa na Kamanda wa vita wa Persia, Mfalme Xerxes; aliyekuwa na askari laki tatu. Alipopinga amri ya kujisalimisha, maadui walimsogelea, na ndipo alipotamka maneno hayo, akiwa amepandisha mori!

Kwa ujasiri alisema, “njooni muwachukue au muwauwe askari wangu! Njooni mchukue ardhi yetu yote! Njooni mchukue kila kitu chetu!” Akimaanisha, ‘sogeeni niwaoneshe’! Alipomaliza kusema haya, hamasa kubwa ilimjaa, yeye na askari wake, na walitoa kipigo cha nguvu kwa maadui; na kuwaangamiza kwa maelfu!

Sasa, kwa ujasiri kabisa, kimoyomoyo, mjasiriamali unapaswa kuwaambia washindani au mshindani wako:” Wewe si una nguvu? Njoo utuoneshe unachotuzidi. Njoo basi uwachukue wateja wetu! Njoo utunyang’anye mtaji wetu! Njoo utunyang’anye wafanyakazi wetu bora! Tunaweza tusiwe na nguvu, lakini ukijaribu kutuhujumu, fahamu tutakushinda!

Hapa wajasiriamali tunapata somo kwamba tunatakiwa kuwa na moyo wa chuma kama wa Leonidas. Huu ni moyo wa uthubutu, ujasiri na ukakamavu; kuweza kujilinda na kukabiliana na changamoto yoyote, hasa kutoka kwa washindani, bila kujali ukubwa wao. Hakika ukiwa na ujasiri, biashara yako haitayumba.

Sita,Better To Die Than To Be A Coward.” Yaani: “Afadhali Kufa Kuliko Kuwa Mwoga.” Kualimbiu hii imetoka katika Jeshi la Uingereza. Ni katika kikosi cha askari waliopata sifa ya ujasiri wa hali ya juu katika mapigano. Wanaweza kuingia popote, katika mazingira yoyote; bila kusitasita, na wakaangamiza.

Hapa wajasiriamali tunafundishwa ujasiri; yaani kama una tabia ya woga, basi hufai, bora ufe kabisa!. Unatakiwa upambane. Kwani unaogopa nini? Kwa mfano unataka mkopo; huna sababu ya kuogopa kuingia katika benki yoyote na kuomba. Usiogope kujaribu chochote, usiwaze kuwa labda utakataliwa, au utajibiwa vibaya, hapana! Afadhali kukataliwa kuliko kuacha kujaribu.

Hatua ya kuchukua: Tumia mifano ya kaulimbiu hizi ili kujijengea tabia zinazofanana na za kijeshi zitakazokupa motisha, hamasa na ujasiri wa kupambana na changamoto mbalimbali katika ujasiriamali. Makala ijayo nitamalizia kaulimbiu tano za mwisho.

Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasirimali kivitendo.

Anapatikana kwa simu: 0718219530; e-mail: nzyy2001@gmail.com

 

Jinsi Ya Kutumia Mbinu Za Kijeshi Kuboresha Biashara! …(1)

Habari rafiki,

Kuna mbinu au mambo mengi ambayo wafanyabiashara au wajasiriamali wameyachukua au wanaendelea kujifunza kutoka katika majeshi.

Kwa mfano, neno mkakati, au kupanga mikakati, ni dhana ambayo imezaliwa kutoka jeshini. Mkakati ni neno lililoanzia jeshini katika karne ya 18; na ni dhana iliyosambaa taratibu kutoka jeshini hadi ikafika katika nyanja za biashara.

Ushindi katika mapambano ni zao la mikakati makini  ujasiri, na ujanja wa medani

Kwa muktadha wa  kijeshi, neno mkakati linamaanisha  mbinu au ‘sanaa’ ya kiongozi wa jeshi (General). Yaani, ni mbinu za upangaji wa vikosi vya jeshi kwa maandalizi ya vita, iliyojumuisha; kuweka mipango na kufanya kampeni kwa ajili ya mapambano, kupanga taratibu za kusogeza vikosi na vifaa eneo la mapambano, na kupanga mbinu za kuwahadaa na kuwapiga chenga maadui.

Katika makala ya leo naomba tujifunze kaulimbiu za kijeshi na namna ambavyo zinaweza kutoa mchango katika kukuza au kuboresha maarifa ya ujasiriamali.

Kabla sijaanza kuongelea kaulimbiu hizo, napenda nikushirikishe takwimu zifuatazo: “Asilimia 60 ya makampuni makubwa 500 yaliyokuwepo duniani mwaka 1970, hayapo kabisa leo.” Sio kwamba yamebadilisha majina, la hasha, yamekufa!

Ni sawa na simulizi tunazopewa kuwa hapo zamani kulikuwa na tawala zenye nguvu kama Roma, Ugiriki, na Persia/Iran, lakini tawala au empire hizi, na umaarufu au maguvu yake, ziliporomoka na kubaki si chochote.

Sasa tujiulize, kwa nini? Sababu kubwa ni kwamba zilikosa mikakati sahihi na umakini. Kwa vile zilijiona zinashinda kila vita, zilibweteka na kuona hazina mshindani, na hivyo hazikuwekeza zaidi katika kupanga mikakati na mbinu bora zaidi. Kifupi, hazikujiongeza!

Hivyo, wewe kama mjasiriamali,  na unataka kuiinua au kuiendeleza biashara yako, unahitajika utengeneze mkakati wako wa biashara kwa uhakika na umakini mkubwa.

Sasa, ninazo  kaulimbiu au slogan 11, kwa mujibu wa mpiganaji mmoja kutoka kikosi maalum cha jeshi la Marekani (Special US Force) ambaye baadaye aliamua kujikita katika ujasirimali. Leo nitajadili slogan tatu, na zilizobaki nitaziongelea katika makala nyingine.

Moja, “Stay Alert; Stay Alive” (Yaani; Kaa macho, uishi salama). Tumeona hapo juu kuwa makampuni 500 yameondoka katika biashara ndani  miaka ya 49 iliyopita, kisa? Hayakukaa macho, na hivyo yalikufa.

Makampuni kama ‘Blockbuster’ au ‘Borders’ yalikuwa ndio ‘habari ya mjini’ wakati huo. Hawa walikuwa kila mahala. Walikuwa na majina makubwa, kaulimbiu kubwa na kila kitu. Blockbuster, (kampuni ya Marekani ya uuzaji na ukodishaji wa DVD, video, na filamu), haikuwahi kufikiria kwamba Netflix, (kampuni ndogo iliyofanya hayohayo), wanaweza kufanya chochote.

Wala Borders (wauzaji wakubwa wa vitabu na muziki) hawakuwahi kufikiria kwamba Amazon (wadogo, waliofanya hayohayo) wanaweza kuwa tishio. Hawakuwahi kufikiria kuwa wateja wanaweza kuwapita wao na kwenda kununua mahala pengine, yaani kwa washindani wao ‘dhaifu’.

Lakini ilitokea! Kisa? Blockbuster na Borders hawakuwa ‘alert’. Hawakujali kujua kinachoendelea katika soko, hawakufuatilia kujua hisia za wateja, hawakujali timu za mauzo zinafanya nini, hawakujali kujua tabia za wafanyakazi zikoje. Hawakujishughulisha na ushauri wa washirika wao, wala masuala ya kisheria n.k. Hivyo baada ya muda walizama na kupotea.

Pili, “whatever it takes….”Ikiwa na maana: “Yaani hata iweje..” Kaulimbiu hii inatoka kikosi au Batallion namba 1 ya Jeshi la Wanaanga, Marekani. Kwa lugha rahisi, wanahimizwa kufanya chochote kinachowezekana au kutumia mbinu yoyote, ili kufanikisha malengo yao.

Kwa mjasiriamali ni kwamba bila kujali chochote, fanya vitu vitakavyokuletea tija katika biashara yako. Yaani, tumia mbinu yoyote halali ili upate matokeo.

Kwa mfano, bila kujali kuwa itakuchukua mwezi mzima kuifanyia utafiti bidhaa unayokusudia kuizalisha, au kuwafahamu vizuri washindani wako; au itakulazimu kufanya kazi masaa 18 kila siku ili kupata ulichokusuadia, basi usijali, fanya hivyo.

Vilevile, hata kama itakulazimu kuendesha gari masaa 8 ukiwa unamfuata mteja wako muhimu mmoja, ambaye unadhani atasaidia kukuongezea ushawishi na mapato katika biashara yako, basi usijali, fanya hivyo!

Kwa hiyo, sababu kubwa kwa nini wajasiriamali wengi hawafanikiwi ni kwamba hawajitoi vya kutosha kusema ‘what ever it takes’.

Tatu, “the only easy day was yesterday”. Ikiwa na maana: “Siku rahisi zaidi ilikuwa jana”. Hii kaulimbiu imetoka katika  Kambi ya Mafunzo ya Jeshi la Maji, Marekani. Ujumbe wa kaulimbiu hii ni kwamba, kama ulidhani mafunzo yalikuwa magumu jana, basi ujuwe kuwa leo ndio itakuwa balaa!

Sasa kama mjasiriamali, kauli  hii inakuhimiza kuongeza uvumilivu, juhudi, bidii na kujituma. Ina maana pia kujiongeza, kwa kufanya maboresho katika kila unachofanya. Kama tayari unajua jinsi ya kutatua changamoto za jana, ujuwe sasa unatakiwa ujiandae vizuri zaidi ili uweze kutatua changamoto za leo. Na changamoto za leo zitakuwa ngumu zaidi ya zile za jana.

Ujumbe kwa wajasiriamali; weka mikakati, na endelea kuboresha kila unachofanya, taratibu, kila siku. Usipofanya hivi utabaki na njia zako za kizamani za kufanya mambo, na utasambaratika.

Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasirimali kivitendo.

Anapatikana kwa simu: 0718219530; e-mail: nzyy2001@gmail.com

 

 

Ukiwa Na Macho Ya Namna Hii, Utatengeneza Fursa Nyingi za Biashara

Rafiki,

Ukifuatilia  makala zangu utagundua kuwa  nimeweka msisitizo katika kujenga uwezo wa ubunifu miongoni mwa wajasiriamali, na kwamba ubunifu ni tabia muhimu sana katika utatuzi wa changamoto zinazoikabili jamii, lakini pia katika kuzalisha fursa mbalimbali za biashara.

Kama nilivyoeleza huko nyuma, fursa ya biashara ni tunda la wazo zuri la biashara. Watu wengi wanachanganya matumizi ya maneno haya; yaani wanasema wazo la biashara ndio fursa ya biashara. Ukweli haya ni maneno yenye maana tofauti, ingawa yana uhusiano wa karibu.

Kupata wazo la biashara ni hatua ya kwanza kabisa katika mchakato wa uanzishaji wa biashara. Wazo ni dhana ,au concept, ambayo inaweza kutumika katika kuanzisha uzalishaji wa bidhaa au utoaji huduma.

Katika kuhangaika ili apate kitu cha kufanya, mjasiriamali makini  hutengeneza hamu au hamasa ndani ya ubongo wake ambayo mwisho wake huzaa mawazo mengi  ya vitu vya kufanya. Kutokana na mawazo haya, mtu huyu hatimaye huchagua wazo moja analovutiwa nalo zaidi ili aje kulitekeleza kivitendo baadaye.

Hata hivyo, wazo peke yake kichwani halina thamani yoyote. Na ukweli ni kwamba, mawazo mengi ya biashara huendelea kuogelea tu, katika akili za watu, bila kuleta manufaa yoyote – hadi pale yanapotiwa katika vitendo.

Sasa, wazo la biashara lililoundwa akilini, halafu likafanyiwa utafiti au tathmini, na likaonekana linawezekana kufanyika – na linaweza kuleta manufaa kwa jamii; na faida au tija kwa mjasiriamali – ndio huzaa kitu kiitwacho fursa.

Watu wengi hupata taabu sana kutengeneza wazo la biashara linaloweza kufinyangwa kuwa fursa. Wanajitahidi kutazama huku na huko, au kusikiliza hiki na kile; lakini macho yao hayaoni, wala masikio yao hayasikii kitu.

Ukiiitazama kwa umakini, picha hii ina vitu vitatu; hebu vitaje!

Kwa ukweli, mawazo mengi yanayoweza kubadilishwa kuwa fursa yanakuja kwa msaada wa  macho maalumu au ‘macho ya ubongo’.. Haya ni macho ya ziada yanayoweza kubaini kitu kilichojificha ndani ya kitu kilicho mbele ya macho ya kawaida. Mtu mwenye macho maalum ana uwezo mkubwa wa ubunifu pia.

Kwa mfano, kila siku ukitoka katika safari zako unapita pembeni ya uwanja wa mpira na kukuta idadi kubwa ya watu wakiangalia mazoezi au mechi. Je, hapa unaona nini? Ukisema naona watu wengi, ukaishia hapo, basi wewe una macho ya kawaida. Lakini kama una  macho ya ubongo, mkusanyiko huu huushtua ubongo, nao huzaa wazo – ambalo nalo huzaa fursa ya biashara.

Au, kwa mfano, ukiona hali ya hewa inabadilika katika mji unaoishi; kutoka hali ya joto kali kuwa baridi kali, je unaona nini? Kama unaona baridi tu, basi unatumia macho ya kawaida (japo baridi haionekani). Lakini kama unatumia macho ya ubongo, utakuwa unaona fursa ya biashara; yaani fursa ya kupata pesa kwa kuuza mavazi au vinywaji vinavyopambana na baridi.

Kuna kijana mmoja, msomi tu,  ambaye alikuwa akiishi na baba yake mjini. Nyumba yao iko kando ya mtaa wenye idadi kubwa ya watu, wakienda na kurudi, siku nzima; na sehemu ya mbele ya nyumba hiyo kulikuwa na baraza kubwa tu.  Kwa kuwa kijana huyu hakuwa na macho ya ubongo, aliona watu wengi na baraza tu, basi. Hivyo hakufanya chochote, huku akiwa hana kazi!

Lakini kijana mmoja alikuja mjini kutoka kijiji fulani. Alipopita eneo hilo, kwa macho ya kawaida  aliona idadi kubwa ya watu na kisha akaliona baraza lile; na ghafla, kwa macho ya ubongo, aliona uwezekano wa fursa kubwa pale. Alipata wazo la kufungua genge; kuuza vyakula mchanganyiko.

Alifanya utafiti kidogo akaona faida itapatikana kwa kuwa washindani hawakuwepo, na mahitaji yalikuwa makubwa. Akamtafuta mwenye nyumba, akaomba nafasi ile, akapewa. Akafanya ukarabati na kuanza biashara kidogokidogo, na baada ya muda si mrefu mambo yakamnyookea.

Hatua ya kuchukua: Ni lazima tubadili namna tunavyoyaona mambo au tunavyoitazama dunia. Kila tunapotazama kitu, lazima tufanye hivyo kwa kuyashirikisha macho ya ubongo. Haya ni macho maalum yanayotusaidia kwenda mbele zaidi ya macho ya kawaida, na kutengeneza mawazo ambayo huzaa fursa.

Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasirimali kivitendo.

Anapatikana kwa simu: 0718219530; e-mail: nzyy2001@gmail.com

 

 

Ubunifu Huu Utakufungulia Zaidi Fursa Za Biashara

Rafiki,

Karibu tena katika makala nyingine inayolenga kukupatia maarifa ya ujasiriamali, ubunifu na stadi za maisha.

Bidhaa hii ni zao la ubunifu mkubwa. Kama chombo kimoja, inaweza kucheza: redio, rekodi/santuri, CD, kaseti, flash na memory card.

Kupitia makala zangu mbalimbali nimesisitiza umuhimu wa mjasiriamali kujenga hulka ya ubunifu. Hulka hii inamjengea mjasiriamali udadisi unaomsaidia kugundua udhaifu au upungufu katika vitu au huduma; au ‘mwanya’ katika soko la bidhaa, ambao yeye anaweza kuuziba.

Mjasiriamali ukiwa mdadisi, unaweza kugundua mapungufu ya washindani wako na hata bidhaa au huduma zao, na wewe ukajipanga kuja na kitu chenye utofauti kitakachowavuta wateja kuhamia kwako, na hivyo kujitengenezea fursa na kipato zaidi.

Kwa hiyo, unapoliangalia soko, na kugundua limepungukiwa vitu fulani muhimu, basi ni jukumu lako kujaza upungufu huo kwa kuingiza sokoni vitu tofauti, au kuvifanya vitu vilevile ki-utofauti.

Kuna njia au mbinu nyingi za ki-bunifu ambazo ukizitumia unaweza kutengeneza au kuziona fursa nyingi za kibiashara, au ukaja na bidhaa au huduma ambazo ni za kipekee zinazoweza kukufanya ujipambanue miongoni mwa washindani.

Kwanza, ongeza hadhi ya bidhaa. Hapa, unachukua bidhaa duni na ‘kuivalisha’ madoido yanayoiongezea thamani; kisha unainadi, siyo kama duni, bali kama bidhaa yenye thamani kubwa.

Kwa mfano, achali ya embe au mango pickle ni zao la maembe yaliyoongezewa thamani  kwa rosti ya viungo,  kisha  kuhifadhiwa ndani ya vinegar au siki. Ukiikuta achali hii super market, ina thamani kubwa, kuliko vipande vya maembe pekee.

Pili, shusha hadhi ya bidhaa. Hapa unaifanya bidhaa ambayo inaonekana ya thamani iwe bidhaa ya kawaida. Kwa mfano, Kampuni ya ndege ya Marekani, People Express Airlines,  iliamua kuondoa vitu visivyo vya lazima, vilivyoingizwa ndani ya bei ya tiketi, na kuifanya nauli iwe kubwa sana. Kwa mfano chakula, magazeti na vijarida. Uamuzi huu uliifanya kampuni hii kuwa kimbilio la watu wa kawaida.

Tatu, unganisha bidhaa kadhaa kuwa bidhaa moja, na ziuze kama bidhaa moja. Kwa mfano, bidhaa kama mashine ya photo-kopi inakuja na printer na scanner; kama bidhaa moja. Pia, angalia picha hapo juu.

Nne, tenganisha bidhaa moja kuwa bidhaa kadhaa tofauti. Hii ni kinyume cha namba tatu hapo juu. Kwa mfano, ukigundua soko limejaa bidhaa fulani iliyounganisha pamoja vitu vitatu, na wateja wanalalamikia bei, unaweza kutenganisha vitu hivyo kuja na bidhaa mojamoja, na kila moja ikawa na bei yake ndogo.

Tano, panua wigo wa soko la bidhaa zako. Hapa unatanua wigo kwa kuuza bidhaa zako katika maeneo makubwa; yaani unamuuzia kila mtu, na kila mahali, au ‘broadcasting’.  Kwa mfano, Television ya ITV Tanzania inarusha matangazo yake nchi nzima.

Sita, punguza wigo wa soko la bidhaa zako, au ‘narrowcasting’.  Hapa, unapunguza wigo kwa  kuzifanya bidhaa ziwafikie idadi fulani tu, tena ndogo, ya wateja. Kwa mfano, katika  visimbuzi (decorder) fulani vya TV kuna chaneli maalum kwa ajili ya wapenzi wa michezo tu; ambao hulipia kununua vifurushi maalum, ili kuweza kuona.

Saba, uza kwa pamoja bidhaa nyingi zinazoendana, katika eneo moja. Yaani; badala ya kuwa na bidhaa moja tu, weka vitu vyote vinavyoendana na uviuze pamoja. Kwa mfano, kama unauza vifaa vya ujenzi, basi unakuwa na kila kitu kinachohusiana na ujenzi, kama tofali, mbao, sementi, nondo, vifaa vya mabomba, vifaa vya umeme n.k.

Nane, uza vitu vingi vya bidhaa fulani ya aina moja tu, sehemu moja. Hapa unaamua kuuza bidhaa fulani tu moja, ambayo wewe unaifahamu vizuri na unaweza kuitolea ufafanuzi wa kina kwa wateja wako. Kwa mfano, unauza aina mbalimbali za makapeti tu, au nguo za watoto tu, basi!

Tisa, safirisha bidhaa kwenda soko la mbali. Hapa unaamua kupeleka bidhaa zako soko jingine ambalo unaweza kuziuza bidhaa hizo kwa faida zaidi. Kwa mfano, ukigundua kuwa eneo fulani nje ya nchi kuna watu wengi wa asili ya Tanzania, unaweza kufungua mgahawa wa chakula cha Kitanzania ukauza vizuri katika soko hilo.

Soma pia: Je unazijua mbinu za kufanya ubunifu katika ujasirimali?

Ushauri: mjasiriamali, kila wakati jitahidi kufumbua macho na masikio, uone matundu au gaps, katika soko na uone namna ya kuziba matundu hayo kwa kufanya ubunifu au kuja ki-utofauti.

Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasirimali kivitendo.

Anapatikana kwa simu: 0718219530; e-mail: nzyy2001@gmail.com

 

Je, Una Uthubutu Wa Kutenda?– Jifunze Kutoka Kwa Reginald Mengi

Rafiki,

Karibu tena katika makala nyingine inayolenga kukupatia maarifa ya ujasiriamali, ubunifu na stadi za maisha.

Makala ya leo itazungumzia kitu muhimu sana katika jitihada za kujikwamua katika maisha kupitia ujasiriamali.

Napenda tujifunze uwezo wa kuthubutu kupitia kwa aliyekuwa mjasiriamali na mfanyabiashara maarufu, Marehemu Reginald Mengi, aliyekuwa Mwenyekiti wa makampuni ya IPP.

Uwezo wa kuthubutu unamfanya mtu awe na ujasiri wa kupambana

Wapo watu wengi katika nchi yetu wanaishi na umaskini mkubwa. Watu hawa, sio kwamba wameumbwa hawana bahati, hapana; bali tatizo ni kwamba wamekosa uwezo wa kujaribu au kuthubutu.

Kuthubutu maana yake ni uwezo wa kuchukua hatua za makusudi katika kutenda jambo fulani. Inahusisha kuamua kufanya jambo kwa ujasiri, bila woga, bila kusitasita, wala kujali watu wanasema nini.

Ukweli huwezi kufanya kitu chochote kama una udhaifu katika uthubutu. Ni watu wenye ujasiri tu ndio wanaoweza kuthubutu kuanzisha kitu na kukisimamia hadi kikaleta manufaa.

Jambo kubwa la kwanza ambalo mjasiriamali anapaswa kuwa nalo ni uwezo wa kujenga wazo la kitu anachotaka kufanya. Akishakuwa na wazo zuri, kinachofuata ni kulitia wazo hilo  katika vitendo ili kupata kitu halisi.

Sasa, inapofikia hatua hii ndio ‘shughuli’ inaanza, yaani hapa ndipo penye shida.

Hapa ‘mjasiriamali’ anaanza kufikiria changamoto kibao zilizo mbele yake, na ugumu uliopo katika kupambana nazo. Akiinama, akiinuka, anaona kuna uwezekano mdogo wa kufanikisha ndoto yake. Anaanza kujiona dhaifu, woga unamwingia, na mwisho anakata tamaa.

Hii haikuwa hivyo kwa mzee Reginald Mengi. Moja ya sifa kubwa na urithi aliotuachia ni uwezo wa uthubutu. Mafanikio yake, kwa kiasi kikubwa yametokana na uthubutu.

Kwa mujibu wa mwandishi mmoja maarufu, Mzee Mengi alikuwa na uthubutu wa ajabu. Ameweka historia kuwa Mtanzania wa kwanza mweusi aliyefungua milango ya kuanzisha na kuendesha biashara kubwa Tanzania.

Wakati anajitosa kuanzisha biashara, mwanzoni mwa miaka ya tisini, nchi hii ilikuwa ikiendeshwa kijamaa, na sekta binafsi ilikuwa bado inaonekana adui kwa nchi. Utajiri na umiliki binafsi wa mali ulichukuliwa kama ubepari, na ubepari ulilinganishwa na unyama.

Kwamba Mzee Mengi alikabiliana na vikwazo au changamoto hizi; bila woga wala kusitasita, au kukata tamaa – na kisha akafanikiwa, ni jambo la kishujaa na la kuigwa.

Uthubutu na ujasiri wa mzee huyu unaonekana katika maeneo yafuatayo:

  • Alithubutu kuanzisha biashara ya vyombo vya habari. Suala la kuanzisha vyombo vya habari vya binafsi, kipindi hicho, lilikuwa jambo gumu sana. Jambo hili lilihusu kuandika na kutangaza, kwa uwazi, habari zilizogusa maslahi ya watawala, matajiri na hata viongozi wa dini. Hili halikuwa jambo dogo, na wala halikuwa limezoeleka!
  • Alianzisha biashara ya magazeti, wakati kulikuwa na ushindani tayari wa magazeti ya umma na yale ya mashirika ya dini.
  • Alikuwa Mtanzania wa kwanza kuwa na uthubutu wa kuanzisha na kurusha, nchi nzima, ‘broadcasting’, matangazo ya redio binafsi, kupitia Radio One.
  • Alikuwa Mtanzania wa kwanza kuanzisha TV binafsi yenye uwezo wa kurusha matangazo ya TV, ‘broadcasting’, nchi nzima, kupita ITV.
  • Alikuwa Mtanzania wa kwanza kunzisha na kumiliki vyombo vya habari (redio na magazeti) nje ya Tanzania, katika masoko magumu kama ya Uganda, na hasa Kenya. Ukiangalia siasa za nchi hizo na urasimu wake – halafu yeye akaweza kupata leseni na vibali vingine, ni jambo la ki-jasiri hasa!

Kupitia kwa Mzee Mengi, wajasiriamali tunapata kitu kikubwa cha kujifunza. Kwamba tusiogope kuthubu. Hata kama tunaona kuna changamoto nyingi na nzito, tunapaswa kujipa moyo na ujasiri, na hivyo kusonga mbele.

Hivyo, kama alivyofanikiwa Mzee Mengi, kila mtu anaweza kufanikiwa, na hivi ndivyo nguvu ya kuthubutu inavyoweza kuleta matokeo bora na mazuri katika maisha yetu.

Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasirimali kivitendo.

Anapatikana kwa simu: 0718219530; e-mail: nzyy2001@gmail.com