Je, Biashara Yako Inaporomoka? Mchawi Wako Huyu Hapa!

Mpendwa rafiki,

Karibu tena katika makala nyingine inayolenga kukupatia maarifa ya ujasiriamali, ubunifu na stadi za maisha.

Mara zote tunapoanzisha biashara tunalenga kupata mafanikio; yaani tunatarajia kuwa baada ya kipindi fulani, cha kujituma na kupambana na changamoto nyingi, basi tuanze kuona matunda. Tunapenda tuone biashara zetu zikikua na kutupatia faida ya kutosha kuboresha maisha yetu.

Hata hivyo, katika uendeshaji wa biashara kuna wakati unaweza kugundua kuwa mambo hayaendi vizuri. Unaanza kuona idadi ya wateja inapungua, mauzo yanashuka, na faida pia inaenda chini. Unaanza kupatwa na mshangao na wasiwasi pia. Unaanza kujiuliza kulikoni?

Sasa, usipokuwa makini ni rahisi sana kutafuta majibu ya mkato. Hizi ni sababu rahisi ambazo hazizingatii uhalisia. Wafanyabiashara wengi tu, hasa wa nchi zetu za Kiafrika, wanaoishi vijijini na hata mijini, wanatawaliwa sana na imani za ki-shirikina. Jambo lolote lisilo la kawaida likitokea utasikia, ‘aaah, si bure bwana, lazima kuna mkono wa mtu hapa’!

Kinachofuata ni kuanza kumtafuta huyo mtu; yaani mchawi aliye nyuma ya Jambo hilo. Katika kufanya ufuatiliaji, mfanyabishara analazimika kuingia gharama kubwa ya fedha, muda, na rasilimali nyingine, ambazo kimsingi zinatoka katika biashara yake.

Ukifuatilia kwa u-makini utaona hakuna msaada wowote unaotolewa na waganga wa kienyeji wanaofuatwa ili wamtafute mchawi. Mfanyabishara atapewa madawa ‘kibao’, na masharti ‘lukuki’ ayatekeleze; lakini mwisho wake hakuna lolote linalobadilika.

Ukishindwa kufuata misingi ya biashara, rafiki yako mkubwa atakua huyu!

Jambo kubwa ambalo wajasiriamali na wafanyabishara hawa wanasahau ni kwamba, mchawi mkubwa wa biashara zao ni wao wenyewe; yaani mfanyabiashara, yeye mwenyewe anaamua kujiroga, halafu akiyumba ki-biashara, hakumbuki; na ndipo huamua kukimbilia kwa waganga wa kienyeji ‘kupiga bao’.

Wafanyabiashara wengi wanajiroga kwa kushindwa kujua mambo muhimu, ya kawaida kabisa, ya uendeshaji wa biashara kitaalamu. Biashara ikiendeshwa kwa kufuata misingi yake na kuongezewa bidii na nidhamu, utaona ‘inachanja mbuga’, na wala masuala ya waganga hayatajitokeza.

Ni misingi tu inayotakiwa kufuatwa. Msingi wa kwanza mkubwa ni mjasiriamali kutafuta elimu ya ujasiriamali au biashara. Ukipata elimu hii na ukaizingatia utapata mbinu nyingi za uendeshaji wa biashara yako kitaalamu.

Kuna mambo mengine mengi yanayopatikana kupitia maarifa ya ujasiriamali. Kwa mfano je, biashara yako inahitajika? Je, eneo lako la biashara linaendana na aina ya biashara yako? Je, ulichunguza vizuri mahitaji ya wateja uliowalenga? Je. Ulichunguza vizuri washindani wako? n.k. Kama hukufanya hivi ulianza kujiroga mapema kabisa.

Swali jingine ni je, unatoa bidhaa bora zinazokidhi matakwa au mahitaji ya wateja wako? Je, bidhaa hizo zina ubora gani ukilinganisha na zile za washindani wako? Kama unauza bidhaa hafifu, ki-ujanjaujanja, wateja watagundua, na baada ya muda ‘watasepa’!

Soma pia: Jinsi Ya Kupima Kama Wazo Lako La Biashara Litaleta Tija

Huduma bora kwa wateja ni jambo muhimu sana iwapo unataka kubakiza na kuvutia zaidi wateja wako. Huduma zako zikiwa mbovu, hata kama zina ubora mkubwa, utashangaa kuona wateja wanakupita, na kwenda kwa washindani wako; halafu unalalamika umerogwa!

Kwa mfano, wapo watoa huduma kwa wateja, wakiwamo wamiliki wenyewe, hawana kauli nzuri wala uchangamfu kwa wateja. Wapo ambao hata neno ‘karibu’ tu, au ‘karibu tena’, hawana! Hapa unategemea nini?

Bei ya bidhaa ni moja kati ya mambo muhimu yanayogusa hisia za wateja. Angali bidhaa yako umeinunua au kuizalisha kwa gharama gani – halafu angalia uwezo wa wateja wako – halafu angalia pia bei za washindani wako zikoje, ili ujue bei gani ukiipanga itakupa faida bila kuwafukuza wateja wako. Usipozingatia hili, utasema umerogwa tu!

Fikiria pia, mteja amefika kwenye biashara yako, na umemwambia bei ya bidhaa. Mteja kwa kupungukiwa kidogo anakuomba umpunguzie, angalau kidogo; utasikia, “eeh bwana eeh, hiyo ndio bei, kama huna basi, we hujui gharama za bidhaa zimepanda?” Unachosahau hapa ni kwamba hauko peke yako unaeuza bidhaa hiyo; hivyo mteja ataondoka na hatarudi tena.

Tabia binafsi ya mmiliki wa biashara au mhudumu ni kigezo muhimu cha kuwavuta au kuwafukuza wateja kwenye biashara yake.

Kwa mfano, hivi utajisikiaje unapokutana na mmiliki wa biashara fulani, unamsalimia vizuri tu, lakini yeye anakujibu ki-mkato, tena kwa maringo, akiwa haoneshi hata umuhimu wako? Je, utakuwa na hamu ya kununua kitu kwake?

Lazima ujue kuna vichocheo vya ukuzaji biashara ambavyo havina gharama kabisa; kama kuwajali, kushirikiana na kuwa karibu na mambo au shughuli za kijamii za watu wanaoizunguka biashara yako.

Wasalimie watu kwa heshima, onesha unawajali, omba hata ushauri wao – huwezi kujua nani ana utaalamu gani utakaokufaa. Tabia hii inakujengea imani na ukaribu kwa jamii, na hatimaye inaijenga biashara yako.

Mwisho, nakuhimiza rafiki yangu ufuatilie makala zangu ili ujifunze mengi yahusuyo uendeshaji wa biashara na ujasiriamali kitaalamu – na hii itakuepusha na fikra za ki-shirikina. Ukweli hizi ni imani tu ambazo zimejengeka katika nafsi za baadhi ya wafanyabishara zinazowafanya washindwe kuuona ukweli unaotokana na upungufu wao binafsi.

Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasirimali kivitendo.

Anapatikana kwa simu: 0718219530; e-mail: nzyy2001@gmail.com

Usihangaishwe Sana Na Jina, Au Kaulimbiu – Fanya Ubunifu!

Rafiki,

Karibu tena katika mfululizo wa makala zangu zenye lengo la kuelimishana kuhusu masuala ya ujasiriamali, ubunifu na stadi za maisha.

Moja ya mikakati muhimu katika kukuza biashara ni kufanya kitu kinachoitwa ‘positioning’. Hili ni neno linalotumiwa sana na watalamu  wa masoko, likimaanisha kuiweka bidhaa kwenye nafasi nzuri katika soko; yaani kuifanya bidhaa au kampuni ipokelewe vizuri katika nafsi au nyoyo za wateja, ikilinganishwa na bidhaa za washindani.

Kaulimbiu ya Precision Air ni, “Wewe ndio sababu ya sisi kuruka” – Je, hii pekee inatosha kukonga nyoyo za wateja?

Al Ries & Jack Trout (1981) ni waandishi wa kitabu kiitwacho, Positioning: the battle for your mind. Waandishi hawa waliandika kuwa ili positioning ifanikiwe, kitu cha msingi kabisa ni kutengeneza na kulitangaza ‘jina zuri’ (brand name) la bidhaa au kampuni yako.

Yaani, moja kati ya mbinu za kuifanya bidhaa au kampuni ipate mafanikio, ni kuwa na ‘ujumbe’ bayana, kupitia jina au kaulimbiu, ambao una nguvu ya kuteka hisia za wateja na kuwafanya waone uhusiano wa wazi kati ya ujumbe au meseji inayotumwa kwao – kuhusu bidhaa fulani, na manufaa yanayopatikana katika matumizi ya bidhaa hiyo.

Ries na Trout walitoa mfano wa makampuni yaliyofeli kutokana na kile walichokiita kuchagua jina baya; yaani jina ambalo lilionekana kushindwa kuteka nyoyo za wateja na kuyapa makampuni hayo nafasi nzuri katika nafsi za wateja.

Moja ya makampuni waliyoyataja kuwa na jina baya ni Eastern Airlines au ‘Eastern’, ambayo ni kampuni ya usafirishaji ya Marekani, iliyoanzishwa mwaka 1926. Ries na Trout waliitabiria kifo kampuni hii kwa kigezo cha kuchagua jina hili; ambalo wanadai lilitoa picha au hisia kuwa kampuni hii ilikuwa kama ya kibaguzi, na ililenga kuwafikiria zaidi abiria wa ukanda wa mashariki, yaani East.

Utabiri wa waandishi hao ulitimia mwaka 1991, pale ambapo kampuni hii, ambayo ilijitangaza sana kama kampuni yenye marubani wenye sifa na uzoefu mkubwa, iliposhindwa kufua dafu, na kusambaratika.

Kwa maoni ya Ries na Trout, jina kama ‘Pan American’ lilifaa sana kuipa kampuni positioning yenye tija. Kumbuka Pan American nayo ilikuwa ni kampuni nyingine ya ndege huko Marekani.

Kwa mtazamo wa waandishi hawa, jina Pan American lilionesha umoja na mshikamano wa Wamarekani wote, hivyo kwa maoni yao, lilikuwa jina zuri kukonga nyoyo za abiria wengi. Hata hivyo, kinyume chake, Pan American nayo ilikufa mwaka 1991.

Hii inatoa picha kuwa jina peke yake halina maana sana katika mafanikio ya biashara au bidhaa. Pointi kubwa inayotolewa, kwa mujibu wa tafiti, ni kwamba kampuni hizi mbili, na zingine zilizofeli, zilifeli kutokana na kukosekana kwa ubunifu.

Makampuni yanahitaji ubunifu mkubwa kuliko mabadiliko ya majina au ‘brand names’. Mfano mkubwa ni kampuni ya Southwest Airlines ya Texas marekani; iliyoanza kutumia jina hili mwaka 1971. Ukiliangalia jina hili utaona halina utofauti sana na Eastern Airlines iliyokufa. Ni jina linaloonekana limekaa ki-kanda pia.

Lakini cha kushangaza, na kinyume na mawazo ya kina Ries na Trout, Southwest Airlines ni kampuni ya usafirishaji yenye mafanikio makubwa. Kampuni hii inasemwa kuwa kampuni kubwa duniani inayosafirisha abiria kwa gharama nafuu, ikianza na abiria wa Marekani, na baadaye mwaka 2014 ilianzisha safari za kimataifa.

Mwandishi mmoja aliandika, “usiangalie jina au kaulimbiu; angalia uwezo wa kampuni kutoa majawabu.”

Southwest Airlines imejizatiti na kujitofautisha katika ubunifu. Hawakuweka nguvu na rasilimali katika jina au brand name, hapana; wao wamepeleka nguvu zaidi katika ubunifu, ili kuongeza thamani ya bidhaa na huduma zao kwenye nafsi za wateja.

Kwa ubunifu wao, Southwest Airlines wamekuja na positioning yenye tija zaidi. Wamehakikisha kuwa mara zote ndege zao zinatua na kupaa kwa muda uliopangwa, hivyo hakuna ucheleweshaji usio na sababu. Wana mifumo inayohakikisha hakuna mzigo wowote wa abiria unapotea au kuharibika.

Wameondoa tozo zote ambazo zilionekana ni kero kwa abiria, na wanaajiri wafanyakazi wenye ujuzi, tabia njema, ucheshi, na walio rafiki kwa wateja. Lakini pia, wateja wamepewa fursa ya kujichagulia seat wakiwa ndani ya ndege, hivyo hawapangiwi pa kukaa.

Fundisho tunalopata hapa, kama wajasiriamali, ni kwamba, tusihangaike sana na majina, ingawa tusiyapuuze pia, lakini kikubwa zaidi kinachoweza kutusaidia kuja na majawabu, ni kubadili namna tunavyofikiri, kuzielewa fursa na changamoto zinazotukabili, na kuzitatua.

Ubunifu ni njia nzuri ya kutengeneza majawabu. Na manufaa makubwa ya kufanya ubunifu ni kumfanya mteja ajenge hisia chanya ndani yake kuhusu kampuni, bidhaa au huduma yako kwa kumpatia mteja ‘kile roho inapenda’.

Mtengenezee mteja hamu, uzoefu au ‘experience’ itakayomfanya atamani kurudi tena, na vilevile atamani kumleta rafiki au ndugu yake ili naye awe mteja wako.

Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasirimali kivitendo.

Anapatikana kwa simu: 0718219530; e-mail: nzyy2001@gmail.com

Jinsi Wasanii Wanavyofanya Ubunifu – Somo Kwa Wajasiriamali

Habari rafiki,

Karibu tena katika makala nyingine inayolenga kukupatia maarifa ya ujasiriamali, ubunifu na stadi za maisha.

Makala hii inalenga katika kujifunza ubunifu kutoka kwa wasanii. Kupitia mbinu mbalimbali zinazotumiwa na wasanii kusanifu au kuumba sanaa zao, sisi kama wajasiriamali tunaweza kujifunza na kupata maarifa yatakayotumika kuongeza thamani na tija katika biashara zetu.

Mwandishi mmoja anasema sanaa au art ni uwezo wa ki-ufundi anaoutumia mwanaadamu ili kuwasilisha fikra au mawazo yaliyo ndani ya akili yake. Uwezo huu unamfanya msanii aweze kusanifu kazi ya sanaa inayoweza kuvuta hisia za watu, kwa uzuri wake.

Hivyo, sanaa inahusisha uwezo wa kuvipa vitu maana au thamani fulani. Kazi yoyote ya sanaa inategemewa ioneshe ufundi wa hali ya juu ili iwe na mvuto kwa hadhira yake. Tunaweza kuona kazi za sanaa kupitia uchoraji, uchongaji, ushonaji, upigaji picha, ususi, upigaji na uchezaji wa muziki n.k.

Sasa tujiulize, je wasanii wanafanyaje au wanatumia mbinu gani ili kuibuka na kazi za sanaa zenye mvuto na ambazo mara nyingi zinakonga nyoyo za watu?

Kama nilivyoandika katika makala hii wasanii huanza ubunifu wao kwa kutengeneza wazo akilini na baadaye kulibadili wazo hilo kuwa kitu au sura halisi ya umbo, mchoro au kitu kingine chenye mvuto.

Wazo huzalishwa katika ubongo kutokana na msukumo kutoka ndani, na vichocheo vya nje

Wazo huanza na hamu au hamasa ya kufanya au kupata kitu, na huanza kama taswira au picha ya jambo au kitu, inayotokana na vitu vinavyoingia katika akili zetu kupitia milango ya fahamu au vinavyokuja kama ndoto kupitia ulimwengu wa roho.

Ili uweze kuja na wazo fulani la sanaa, na kisha kulibadilisha kuwa kitu halisi, kama kinyago au mchoro wa katuni, unapaswa kuwa na msukumo maalum kutoka ndani, au inspiration. Ni msukumo huu ambao huuchochea ubongo au akili kufanya kitu, na ndio husababisha ubunifu kufanyika kupitia viungo vingine, kama mikono.

Kwa muktadha wa sanaa, mbali na msukumo kutoka ndani, kuna vitu vinavyochochea moto wa ubunifu na kuwafanya wasanii waje na sanaa ‘za ajabu’!

Msanii mmoja anasema, “wasanii, wakati fulani, tunapata wazo la sanaa kutokana na mawazo yaliyopo tayari. Yaani, ukipata wazo fulani, ukaliona zuri, unaanza kulichambua na kulitazama kwa umakini kwa kutumia ‘macho ya udadisi’.”

Anasema ili kupata wazo la sanaa, tunatumia vizuri sana milango ya fahamu. Tunaangalia huku na huko, tunasikiliza hiki na kile, na kunusa kila kitu, na mwisho kupitia akili tunapata kitu cha kufanya. Ukipata wazo inabidi utulize akili ili upate uwezo wa kulichakata wazo lako na kuligeuza kuwa kitu halisi kitakachovuta hisia za watu.

Msanii mwingine anasema, “tunajifunza kupitia vitu vya kawaida tu vilivyomo katika mazingira yetu. Kuna kazi za sanaa kila mahala na nyingine zinaonekana kama makapi tu. Ukweli ni kwamba duniani hakuna makapi. Kila kitu kina thamani fulani. Sasa, uwezo wa kubadili makapi kuwa kazi ya sanaa ni moja ya mbinu muhimu za ubunifu.”

Mbali na huyo, kuna msanii aliyesema, “kazi ya sanaa ni matokeo ya ‘kuiga kimkakati’. Kuiga kunakupa uwezo wa kujifunza wengine wamefanya nini na kwa utaratibu gani. Kuiga kimkakati kunamfanya msanii  kufanya ubunifu kwa kuchanganya maarifa aliyoiga na maarifa yake binafsi kupata kitu kipya kabisa.”

Yupo msanii aliyesema, “nimefanikiwa kutengeneza kazi nzuri za sanaa kwa sababu napenda kukutana na wasanii wenzangu. Kila wakati napenda kujua wenzangu wanafanya nini ili niweze kujifunza chochote kipya. Siwaoni wasanii wenzangu kama washindani, bali wenzangu. Hivyo tumekuwa tukishirikiana na kubadilishana mawazo kila siku.”

Akisistiza matumizi mazuri ya milango ya fahamu kujifunza, msanii mmoja anasema, “mimi napenda sana kutembelea maeneo mbalimbali. Nashiriki sana maonesho ya sanaa ili nione kazi za wengine. Lakini pia napenda kutembelea mbuga za wanyama na misitu ya asili. Huko huwa natazama na kusikiliza kila kitu kwa umakini, na kwa kweli huwa napata vitu vingi ambavyo huwa vyanzo vya ubunifu ninaoufanya.”

Msanii mwingine anasema, “mimi mara nyingi hupata mawazo ya ubunifu ghafla tu. Yaani sina hili wala lile, naona picha au taswira tu inapita kichwani, ya kitu kizuri. Sasa, ikitokea hivi, haraka sana huwa naandika au kuchora wazo hilo ili lisipotee, na hapohapo huwa naanza kufikiria jinsi nitakavyolifanya wazo hilo liwe kitu halisi, na mara nyingi nimesanifu vitu vya maana kupitia mazingira haya.”

Kwa kumalizia napenda kuwashauri wajasiriamali  kuwa wadadisi na kujifunza ubunifu kutoka kwa wasanii. Wasanii wamekuwa na hamasa kubwa ya kututengenezea kazi za sanaa zenye mvuto. Tukitumia mbinu mbalimbali wanazozitumia wasanii tunaweza kujenga uwezo mkubwa wa ubunifu utakaotusaidia kuongeza thamani na tija katika biashara zetu.

Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasirimali kivitendo.

Anapatikana kwa e-mail: nzyy2001@gmail.com; Simu 0718219530

Je, Utajuaje Kama Biashara Yako Inakua?

Habari rafiki,

Karibu tena katika mfululizo wa makala zangu zenye lengo la kuelimishana kuhusu masuala ya ujasiriamali, ubunifu na stadi za maisha.

Kutambaa kwa mtoto ni kiashiria muhimu cha ukuaji wa mtoto huyo

Kuanzisha biashara na kuilea hadi ianze kuleta matunda sio jambo dogo. Kuendesha biashara kuna changamoto nyingi ambazo ni lazima mjasiriamali apambane nazo hadi hatua ya mwisho. Kumbuka katika mapambano kuna kushinda na wakati mwingine kushindwa; hiki ni kitu cha kawaida katika biashara, kikubwa ni kutokata tamaa.

Jinsi unavyopambana na changamoto, na jinsi unavyozishinda, ndivyo unavyozidi kusonga mbele katika safari ya mafanikio. Mafanikio hujionesha kwa kigezo cha ukuaji wa biashara yako; ambayo kimsingi ni moja ya malengo muhimu ya kuanzisha biashara yoyote.

Ni muhimu kufahamu kwa uhakika kwamba biashara unayoifanya inakua au hapana. Kwa sababu, jinsi biashara yako inavyozidi kukua ndivyo unavyozidi kupiga hatua na kuboresha maisha yako. Usipolijua hili unaweza kushindwa kuchukua hatua stahiki mapema na ghafla ukajikuta katika hali mbaya.

Sasa je, utajuaje kuwa biashara yako inakua? Kuna viashiria au vigezo kadhaa ambavyo vinaweza kukuonesha kuwa biashara yako inakua, kama ifuatavyo:

Moja, ongezeko la wateja. Ni kawaida sana unapoanza biashara yoyote kujikuta unamaliza siku nzima ukiwa na wateja wawili au watatu tu; lakini, ukichungulia kwa washindani wako, unaona wateja wanagongana vikumbo, wakiingia na kutoka. Hili ni jambo la kawaida. Hata hivyo, jinsi muda unavyozidi kwenda, na kama una mikakati sahihi, utaanza kuona mabadiliko.

Ukiona idadi ya wateja inazidi kuongezeka siku hadi siku, wiki hadi wiki, mwezi hadi mwezi, na kadhalika, hapa unapata picha kuwa biashara yako inakua, na sababu yake ni kwamba watu wengi zaidi wanazidi kuifahamu, na labda wanavutiwa na bidhaa au huduma zinazotolewa.

Mbili, ongezeko la mauzo ya bidhaa. Unapofanya biashara unafanya mauzo ya bidhaa au huduma. Jinsi wateja wanavyonunua kwa wingi ndivyo unavyoingiza mapato zaidi. Katika hali ya kawaida ongezeko la mauzo ni kigezo muhimu cha ukuaji wa biashara.

Tatu, ongezeko la faida. Kila mtu anayeanzisha biashara analenga kupata faida, na hili ndilo hasa lengo kuu la biashara. Mfanyabiashara unapaswa kupima faida unayopata kila baada ya muda fulani kwa kuangalia mapato yanayoingia ikilinganishwa na gharama mbalimbali za uendeshaji wa biashara. Ukiridhika kuwa unapata faida basi ujue biashara yako inakua.

Nne, kupanuka kwa biashara. Biashara nyingi zinapoanzishwa zinaanza na tawi moja tu eneo fulani. Baada ya kuona faida inaongezeka, na ongezeko la mahitaji ya wateja, wafanyabiashara hushawishika kufungua matawi ya biashara zao katika eneo hilo hilo au eneo jingine. Hiki ni kiashiria cha kutanuka kwa biashara, na ni kielelezo cha ukuaji pia.

Tano, ongezeko la mtaji wa kuendesha biashara. Wakati fulani watu huanza biashara kwa mtaji unaotokana na kuuza rasilimali zao fulani, kwa mfano shamba. Wengine huamua kukopa katika taasisi za fedha. Moja ya lengo muhimu la mfanyabiashara ni kuona mtaji unaongezeka ili aweze kuitanua zaidi biashara yake. Mara nyingi faida hurudishwa katika biashara kuongeza  mtaji.

Sita, kuongezeka kwa idadi na ubora wa bidhaa. Mtaji unapokuwa mdogo bidhaa zinakuwa kidogo na pengine zenye ubora wa kawaida. Lakini jinsi mtaji unavyoongezeka mfanyabiashara anapata pia uwezo wa kuongeza bidhaa zaidi na zenye ubora zaidi. Hiki ni kigezo kuwa biashara yake inakua.

Saba, ongezeko la mahitaji ya wafanyakazi. Biashara inapoanza, inaanza ikiwa ndogo, na wakati mwingine mwanzilishi ndiye anakuwa mfanyakazi yeye mwenyewe; yaani hahitaji msaidizi. Lakini baada ya muda anaanza kuzidiwa na kazi, na hivyo anaona hawezi tena kumudu akiwa peke yake. Hapo anaanza kuajiri wasaidizi. Ukiona unaanza kuhitaji wafanyakazi zaidi maana yake biashara yako inakua.

Nane, ongezeko la mchango wa biashara yako katika maendeleo ya jamii. Biashara zote zinafanyika katika maeneo ya watu; yaani katika jamii. Katika jamii kuna mahitaji mbalimbali hasa ya huduma za jamii kama hospitali au shule. Serikali mara nyingi inashindwa kutimiza mahitaji haya, na kuwahimiza wananchi kuchangia.

Sasa, wachangiaji wakubwa wa huduma hizi ni wafanyabiashara. Hata kukitokea dharura utakuta viongozi wanapita kwa wafanyabiashara kuomba msaada. Ki-ukweli, biashara ikiwa changa michango hii inakuwa ni changamoto kubwa. Ikifikia mahala ukaona kutoa misaada kwa ajili ya maendeleo ya jamii haikutii ‘presha’ sana, hiki ni kiashiria kuwa biashara yako anakua.

Ushauri wangu ni kwamba, wewe kama mjasiriamali unapaswa kuvifahamu na kuviangalia viashiria hivi kwa umakini ili ujipime kama kweli biashara yako inakua au la. Usijipime kwa kiashiria kimoja tu ukaridhika, bali angalia vigezo vingi kwa pamoja ndiyo utapata picha kamili. Baada ya hapo chukua hatua stahiki.

Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasirimali kivitendo.

Anapatikana kwa simu: 0718219530; e-mail: nzyy2001@gmail.com

Ubunifu – Je, Kuna Kitu Cha Kujifunza Kutoka Kwa Wasanii?

Habari rafiki,

Karibu tena katika makala nyingine inayolenga kukupatia maarifa ya ujasiriamali, ubunifu na stadi za maisha.

Nimeandika huko nyuma kwamba ubunifu ni matokeo ya kuufikirisha ubongo ili kupata njia mpya na nzuri zaidi za kuleta mabadiliko, kutatua changamoto au kuondoa tatizo lililojitokeza katika biashara, kazi au jamii.

Wasanii wanafanya ubunifu mkubwa kukidhi kiu na matarajio ya wateja wao

Ili kupata maarifa mapya ya kuendesha biashara zao, wafanyabiashara wajanja wameanza kuitazama fani ya sanaa kwa jicho maalum. Wameanza kuiona sanaa kama chanzo cha kukuza maarifa ya ubunifu na kuboresha ustawi wa biashara zao.

Msanii maarufu wa Marekani, Andy Warhol anaandika, “biashara yenye mafanikio ni matokeo ya sanaa bora.” Andy Warhol amepata umaarufu kwa utengenezaji wa kazi za sanaa na ubunifu kama michoro, mapambo na maandishi, ambayo amekuwa akiyauza kwa makampuni ya kibiashara yasiyo na utaalamu huo; kwa lengo la  kuzitangaza  bidhaa zao na kuwavuta wateja.

Sasa, kama ambavyo wasanii wanajitahidi kuipenyeza sanaa katika biashara, kwa lengo la kuzipa bidhaa thamani zaidi, ndivyo ambavyo wajasiriamali wanatakiwa kuipokea sanaa na mbinu za ubunifu kama kichocheo cha ukuaji wa biashara zao. Yaani, wajasiriamali wanapaswa kujifunza kufanya ubunifu kwa staili inayotumiwa na wasanii.

Kama wasanii, wajasiriamali wanapaswa kujijengea mtazamo chanya na tabia za kibunifu ili waweze kuitazama dunia kwa jicho tofauti, la kidadisi, lenye lengo la kupata maaarifa ya kuunda vitu vipya, bora zaidi na vyenye thamani.

Kwa hiyo, kama ubunifu ni matokeo ya kuufikirisha ubongo ili kupata njia mpya na nzuri zaidi za kuleta mabadiliko, kumbe yafaa tujifunze jinsi wasanii wanavyofikiri na kutenda na hivyo kuweza kuja na kazi nzuri za sanaa na ubunifu; na hii itasaidia kuamsha akili za wajasiriamali ili nao waanze kufikiri na kutenda kama wasanii, hatimaye nao waje na ubunifu bora kwa manufaa ya biashara zao na jamii.

Maana ya sanaa au ‘art’ ni shughuli ya kibunifu inayotafsiri uwezo wa kufikiri au kutenda alionao msanii. Uwezo huu unamfanya msanii aweze kubuni kazi ya sanaa inayoweza kuvuta hisia za watu. Sanaa inahusisha uwezo wa kuvipa vitu maana au thamani fulani. Kazi za sanaa ni pamoja na uchoraji, uchongaji, ushonaji, upigaji picha, muziki (kupiga au kucheza) n.k.

Wasanii huwa wanajenga ndani yao hamasa ya kuumba vitu visivyo vya kawaida, au vya aina yake. Yaani, kwa makusudi au uthubutu walionao wanadhamiria kuvunjavunja fikra za mazoea na kuja na vitu vipya ambavyo pengine havijawahi kuwepo.

Sasa, kuna sifa walizonazo wasanii ambazo zinawafanya wawe na uwezo wa kufikiri kwa umakini na kujenga tabia inayowafanya kila mara wafanye vitu ‘vya aina yake’. Lengo langu hapa ni kuwapa maarifa haya wajasiriamali ili wakizijua sifa hizi wazitumie kufanya ubunifu zaidi kwenye biashara zao ili zipate thamani zaidi.

Zifuatazo ni baadhi ya sifa hizi:

Moja, wasanii wanapenda sana kuja ki-utofauti. Yaani wakati mwingi wanakuwa na hamu ya kuunda vitu vipya vyenye mvuto na thamani kubwa kwa walengwa.

Pili, wasanii wanajali sana maslahi ya wateja wao; yaani wana uwezo wa kuchunguza mahitaji na hisia za watu kwa jicho la udadisi, na kuzivaa hisia zao kwa lengo la kuzitafutia majawabu. Kwa uwezo huu mara nyingi wanakuja na kazi za sanaa ‘zinazochota’ hisia za watu na kuwapa burudani kubwa.

Tatu, wasanii ni mafundi stadi wazuri. Hawa wanatengeneza kazi zao kwa kuunganisha fikra au akili zao na mikono yao; yaani wakipata fikra au wazo la nini cha kufanya, wana uwezo mkubwa wa kubadilisha wazo hilo kuwa kitu halisia.

Nne, wasanii wanafanana sana na watoto. Tafiti zinaonesha kuwa kila mtoto ni msanii, isipokuwa tatizo lililopo ni jinsi ambavyo watoto wanaendeleza uwezo wa usanii wakiwa watu wazima. Kwa kuwa na sifa hii, wasanii wengi wanakuwa na uthubutu wa kufanya kila kinachokuja katika fikra zao, bila kusitasita au kujiuliza maswali mengi.

Tano, wasanii wanafanya kazi za sanaa kutoka moyoni; yaani kwa kutumia hisia zaidi kuliko kufundishwa na mtu. Wanaangalia mtiririko wa matukio na kukisia kitu kinachoweza kugusa hisia za watu, halafu wanafanya majaribio kuthibitisha ukweli wa hisia zao; kisha haraka wanatoa uamuzi na kuzitia hisia zao katika vitendo.

Sita, wasanii hawasumbuliwi sana na mazingira yenye utata, yasiyo bayana, au yasiyotabirika. Wao wanajitosa tu. Kuna wakati wakiwaza kufanya ubunifu fulani wanapata hisia zinazopingana na ukweli fulani wanaoujua kiuhalisia, lakini hili haliwasumbui; wao wanao uwezo wa kufumba macho hadi wafanye walichokikusudia.

Saba, wasanii wana uwezo wa kufikiri na kutenda kwa kutumia mitazamo tofauti. Wana uwezo wa kuunganisha nukta au dots, na kufanya mambo nje kabisa ya muktadha uliozoeleka. Wakati fulani ukiwauliza waliwezaje kuja na ubunifu wa kiwango hicho kwenye sanaa zao, watakujibu, ‘aah, mimi nimeona tu kazi niliyoifanya – kwamba, kumbe ina thamani mbele za watu; lakini kujua nimeifanya kwa utaratibu gani, sijui cha kukwambia.’

Ushauri wangu: Kila mjasiriamali azisome sifa hizi za wasanii ambazo zinawafanya wawe na uwezo mkubwa wa ubunifu unaowapa furaha na raha wateja au wapenzi wao. Kwa kuziiga sifa hizi kila mjasiriamali atazidi kujijengea uwezo wa ubunifu utakaomwezesha kila siku aje ki-utofauti na kuiongezea thamani biashara yake.

Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasirimali kivitendo.

Anapatikana kwa simu: 0718219530; e-mail: nzyy2001@gmail.com

Unapofanya Ununuzi Wa Bidhaa Au Malighafi Zingatia Haya

Rafiki mpendwa,

Karibu tena katika mfululizo wa makala zangu zenye lengo la kuelimishana kuhusu masuala ya ujasiriamali, ubunifu na stadi za maisha.

Katika makala hii ya leo nitazungumzia suala la ununuzi wa bidhaa au malighafi kwa ajili ya uendeshaji wa biashara. Kumbuka unapofanya biashara yoyote, iwe ya kununua na kuuza, au ya kuzalisha mali na kuuza, ni lazima utafanya zoezi la ununuzi. Hivyo katika ununuzi lazima ujipange vizuri ili ununuzi unaoufanya uiletee biashara yako tija ya kutosha.

Chagua wagavi wa bidhaa kwa umakini usije iangamiza biashara yako

Usipokuwa makini na ukafanya ununuzi bila kufikiria wala kupangilia, ukanunua kiholela, utajikuta katika matatizo, na huenda hili peke yake likaifanya biashara yako iyumbe hadi kufa.

Ununuzi una taratibu na kanuni zake ambazo unapaswa kuzifuata ili kila unachopanga kununua kiweze kuwa na manufaa na kiongeze tija kwenye biashara unayoifanya. Kwa hiyo makala hii itakupitisha katika taratibu za ununuzi ambazo ukizifuata zitaisaidia biashara yako, kama ifuatavyo:

Moja, kujua unataka kununua nini. Kuna watu wanakurupuka katika kufanya mambo. Suala la ununuzi halitaki kukurupuka. Unapaswa kujua kwa uhakikika unataka kununua nini na kwa sababu gani. Unapofanya ununuzi wowote, unatumia rasilimali fedha; hivyo ikitokea ukanunua bidhaa au malighafi isiyohitajika kwa wakati huo utakuwa umeiingiza biashara yako katika hasara.

Pili, kupanga muda wa kununua bidhaa. Ukishajua unataka kununua nini kulingana na mahitaji na vipaumbele vyako, unapaswa  sasa kujua muda sahihi wa kuagiza bidhaa au malighafi hizo.

Ukiagiza mapema sana kabla hujafanya maandalizi mengine, ujue bidhaa au malighafi zitakaa stoo bila sababu na huenda baadhi yake zikaharibika au kupitwa na wakati. Hii ni hasara tayari kwa biashara. Lakini, kubwa ni kwamba bidhaa zilizonunuliwa mapema sana zinakuwa ‘zimeikamata pesa’, ambayo huenda ingetumika kununua kitu kingine muhimu zaidi na kuifanya pesa izunguke.

Vilevile ukishindwa kununua bidhaa au malighafi kwa wakati, hadi zikaisha stoo, ni wazi utakuwa katika hatari ya kushindwa kukidhi mahitaji ya wateja wako, na hapa kuna hatari ya kukimbiwa na wateja kwa kushindwa kuwaridhisha.

Tatu, kujua wagavi sahihi wa bidhaa au malighafi unayotaka kununua. Unapopanga kufanya ununuzi wowote ni lazima ufanye utafiti kidogo kujua walipo wagavi sahihi wa bidhaa zako. Sio kila muuzaji wa bidhaa ana sifa za kukupatia bidhaa unazohitaji, wapo wengine hawana sifa hizo, na wengine ni wababaishaji tu.

Utafiti utakaofanya utakusaidia kujua ni wapi utapata bidhaa kwa ubora na bei nafuu. Utajua pia tabia za wagavi na jinsi unavyoweza kunufaika kutokana na tabia zao, kwa mfano wapo wagavi ambao ni waaminifu na wanapokuuzia kitu wana uhakika kina ubora sahihi, lakini wapo wababaishaji pia.

Wapo pia wagavi ambao ukinunua kitu wanakupa maelekezo mazuri ya namna ya kutumia, na pia vitu gani uvifanye au usivifanye ili usiingie katika hasara; lakini wapo pia wasiojali kabisa.

Nne, kupanga kiasi sahihi cha kununua. Unapotaka kununua bidhaa lazima uwe unajua kwa usahihi unahitaji bidhaa kiasi gani, kulingana na mahitaji ya wateja wako au mahitaji ya uzalishaji unaoenda kuufanya.

Usipozingatia hili utajikuta unanunua bidhaa au malighafi nyingi bila sababu, na kuna hatari ya kuharibika au ku-expire, lakini vilevile pesa ya ziada iliyotumika ingeweza kufanya mambo mengine. Kwa upande mwingine, ukinunua bidhaa kidogo hutakidhi mahitaji ya wateja wako, au hutafanya uzalishaji sahihi wa bidhaa kiwandani.

Tano, kujua ubora wa bidhaa au malighafi unayonunua. Ubora ni suala ambalo lina umuhimu mkubwa na linasisitizwa sana kwa sababu linagusa maslahi mapana ya wateja. Ukizalisha au kuuza bidhaa hafifu unawahujumu wateja wako, lakini pia unaweza kusababisha madhara makubwa, hata kifo au ulemavu kwa wateja wako.

Kwa hiyo unapaswa kujiridhisha kuwa unanunua bidhaa au malighafi zenye ubora unaofaa kabla ya kuwapelekea wateja wako.

Sita, fanya utafiti wa bei za bidhaa au malighafi unazonunua. Katika uendeshaji wa biashara, bei ndio hasa inayokupa mwongozo au kipimo kuwa utazalisha faida au hasara. Hii ni bei ya kununua na bei ya kuuzia bidhaa.

Ukinunua kwa bei ya juu na kukawa na gharama nyingine juu yake, kisha ukauza kwa bei ndogo, hapo ni wazi utapata hasara. Hivyo fanya ununuzi kwa mgavi atakayekuuzia kwa bei nafuu, ambayo  itakupatia faida ukiuza kwa wateja wako.

Saba, angalia huduma zinazotolewa na mgavi baada ya kununua bidhaa. Wapo wagavi ambao ukishampatia pesa tu basi wewe na yeye hamjuani tena. Hata kama utagundua tatizo katika bidhaa uliyonunua hutapata msaada wake. Hivyo uwe makini na wagavi wa aina hii. Nunua kwa mgavi anayejali maslahi yako na wateja wako pia.

Kwa mfano, umenunua bidhaa halafu ukakwama kuitumia kutokana na teknolojia iliyotumika, mgavi mzuri yuko tayari kukupatia ufafanuzi hapohapo, kwa simu, na wakati mwingine anaweza kutuma mtu aje kwako. Au kama bidhaa ina matatizo wagavi wengine wapo tayari kubadilisha na wakakupatia bidhaa nyingine. Hawa ndio wagavi unaotakiwa kuwajua na kuwakumbatia.

Nihitimishe kwa kukuhimiza wewe mjasiriamali kuwa makini sana katika suala na ununuzi kwani bila kufanya hivyo utaingia kwenye hasara ambayo itakugharimu na kuiyumbisha biashara yako.

Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasirimali kivitendo.

Anapatikana kwa simu: 0718219530; e-mail: nzyy2001@gmail.com

 

 

Je, Wajua? Hizi Ndizo Sababu Za Biashara Nyingi Kufa

Habari rafiki yangu,

Karibu tena katika makala nyingine inayolenga kukupatia maarifa ya ujasiriamali, ubunifu na stadi za maisha.

Kutokana na hamasa, ukosefu wa ajira au hali ngumu ya maisha, vijana na watu wazima pia wameendelea kuzitafuta fursa na kuingia katika ujasiriamali au biashara kwa lengo la kujipatia kipato na kuboresha maisha yao.

Umakini unatakiwa katika uendeshaji wa biashara la sivyo itadorora hadi kufa

Hata hivyo, tafiti zinaonesha kuwa biashara nyingi zinazoanzishwa hufa ndani ya kipindi cha miaka mitano tangu kuanzishwa kwake. Je unalijua hili? Fuatana na mimi ili uzifahamu sababu hizi, na ukizijua itakusaidia kujipanga ili usifikwe na dhahama hii. Kusudi langu hapa ni kwamba maarifa haya yatakusaidia kuchukua tahadhari mapema, na hii itakusaidia kuinusuru biashara yako iondokane na hatari ya kufa.

Wataalamu wanatuambia kuwa biashara nyingi hufa kutokana na matatizo yanayotokana, kwa kiasi kikubwa, na wafanyabiashara wenyewe. Maana yake hapa ni kwamba mchawi wa biashara huwa hatoki nje, bali yumo ndani ya mfanyabiashara mwenyewe. Ni sawa na msemo maarufu usemao, “kikulacho ki nguoni mwako.”

Zifuatazo ni baadhi ya sababu hizo ambazo mojamoja, au kwa pamoja, zinaweza kusababisha biashara yako kufa:

Moja, kutokuwa na elimu au uelewa mzuri wa biashara. Nimeandika huko nyuma kuhusu umuhimu wa elimu ya ujasiriamali. Nimeeleza kuwa elimu ya ujasiriamali inahitajika na ina umuhimu mkubwa, kwani ina msaada mkubwa katika kumpatia mjasiriamali umahiri katika kuanzisha, kuendesha, kuchambua na kutathmini mwenendo wa biashara yake, na kufanya marekebisho mapema ikibidi.

Nimesema kwamba elimu hii inamjengea mjasiriamali uwezo wa kujiamini, kuhoji na kutambua fursa na changamoto kwa uhakika. Elimu hii inamsaidia mfanyabiashara kufungua na kutanua akili yake ili ifikie uwezo wa juu wa kufikiri na kutafakari mambo.  Kwa hiyo nikahimiza kuwa kila mtu anapaswa kuitafuta kwa bidii.

Elimu au maarifa ya ujasiriamali yanapatikana kwa kujifunza kupitia mitandao, vitabu, majarida, blog, kuhudhuri semina na kupitia kwa wajasiriamali waliofanikiwa, au hata waliofeli.

Pili, kukosa umakini katika matumizi ya rasilimali na hasa fedha. Ukiwa mfanyabiashara unapaswa kuwa na nidhamu ya hali ya juu katika matumizi ya rasilimali zako. Ukitumia fedha bila mpangilio mzuri zitapotea au utaziweka katika matumizi yasiyo ya lazima na hazitaweza kuzalisha tija katika biashara yako. Hii ni hasara tayari. Rasilimali nyingine ni muda, nyenzo za kutendea kazi, wafanyakazi n.k. Hivi vyote vinahitaji umakini wa hali ya juu katika mipangilio na matumizi yake.

Tatu, kukosekana kwa ubunifu. Nimeandika kupitia makala zangu umuhimu wa ubunifu katika uendeshaji wa biashara. Kuna ushindani mkubwa ziku hizi katika kila biashara unayopanga kufanya. Hivyo unapaswa kuja na vitu vya ki-bunifu kila siku ili uushinde ushindani huo. Jifunze kujitofautisha na kujiongeza ili ufanye vitu kwa ubora na umahiri wa juu.

Nne, kushindwa kulijua soko la bidhaa zako na kuitangaza biashara. Unapoanzisha biashara yoyote unapaswa kujua soko lako ni lipi; yaani nani atanunua bidhaa yako?. Hili linahitaji utafiti kidogo. Usipolijua soko utashindwa kupata wateja na biashara itayumba. Vivyo hivyo, ukishindwa kuitangaza biashara au bidhaa yako ni wazi haitajulikana.

Tano, kushindwa kutoa huduma nzuri kwa wateja. Kumbuka wateja ndio pesa katika biashara. Jiulize, bila mteja kuja, pesa itaingiaje katika droo yako ya dukani? Jifunze jinsi ya kuwavuta wateja na kuwabakiza. Usifanye mambo yatakayowafukuza wateja wako, hakikisha wanavutiwa na huduma zako na wanakusaidia kuitangaza kwa wenzao pia.

Sita, kukosa vipaumbele. Hili ni tatizo kwa wajasiriamali wengi. Wapo wanaotaka kufanya kila kitu kwa wakati mmoja. Yaani wangependa kuanzisha biashara zaidi ya moja kwa wakati mmoja. Ukifanya hivi ujue zitakwama zote! Kufanya hivi ni kukosa ‘focus’ yaani ni kupapasapapasa tu. Weka vipaumbele; yaani chagua uanze na ipi, kwa kuanzia – halafu angalia nini kifuatie baada ya hii kusimama chenyewe.

Saba, kushindwa kupambana na changamoto za biashara. Katika biashara kuna changamoto nyingi. Ndio maana nimekuwa nahimiza kujifunza ubunifu. Mbunifu ni mtu anayefikiri ki-udadisi kila siku. Kwa kufanya hivi ni wazi utavibaini vihatarishi au changamoto zinazonyemelea biashara yako na kuja na mbinu za kupambana nazo kabla hazijakufanya ukwame katika biashara yako.

Nane, uchaguzi mbaya wa eneo la biashara. Katika kusaka eneo la biashara unaweza kujikuta umepata eneo lililo mbali na wateja wako, au lisilo salama, au lililokatazwa kisheria. Hili likitokea kuna hatari ya kukosa wateja au kupata hasara, na kufanya biashara yako izorote hadi kufa.

Tisa, kushambuliwa na majanga ya asili kama mafuriko n.k. Hii ni sababu inayotokana na mazingira yaliyo nje ya mfanyabiashara, ingawa mfanyabiashara ana nafasi ya kuweza kufanya kitu mapema ili kuokoa biashara yake isiathirike. Kwa mfano, huwa kuna tahadhari zinazotolewa na watabiri wa hali ya hewa wakisema kutakuwa na mvua kubwa na vimbunga, hivyo watu wahame au wachukuwe tahadhari fulani. Usipochukua tahadhali ni wazi madhara yatakupata.

Ushauri wangu: Biashara nyingi hufa katika kipindi kifupi baada ya kuanzishwa kutokana na matatizo ambayo yanaweza kuzuilika; yaani yamo ndani ya uwezo wa mfanyabiashara mwenyewe. Kwa hiyo ni muhimu kila mfanyabiashara awe makini na mdadisi katika kuzibaini fursa na changamoto mbalimbali zinazojitokeza, na kufanya vitu sahihi, kila siku katika uendeshaji wa biashara.

Jihadhari, Ubunifu Huu Una Madhara – Achana Nao!

Rafiki mpendwa,

Karibu tena katika makala nyingine inayolenga kukupatia maarifa ya ujasiriamali, ubunifu na stadi za maisha.

Ubunifu wa namna hii una tija, kwani unampatia mbunifu kipato, na furaha kwa mteja

Ubunifu ni uwezo wa mtu kuanzisha au kuvumbua kitu chochote kipya, chenye utofauti na ubora zaidi, ambacho kina thamani au kinaongeza thamani ya kitu kilichopo, kwa manufaa ya mtu mwenyewe, wateja na jamii kwa ujumla.

Ubunifu ni matokeo ya kuufikirisha ubongo ili kupata njia mpya na nzuri zaidi za kuleta mabadiliko, kutatua changamoto au kuondoa tatizo lililojitokeza katika jamii. Kuna kauli moja inayosema kwamba ubongo wa mtu anayefikiri sana unaweza kuwasha taa kwa jinsi unavyofua umeme.

Kwa hiyo, kufikiri ni kitu muhimu sana kwa kuwa kunasababisha ubunifu kutokea na mwisho wake ni utatuzi wa changamoto au upatikanaji wa bidhaa au huduma mpya zenye manufaa kwa jamii. Huu tunaweza kuuita ubunifu chanya; yaani ni ule unaoleta maendeleo na mabadiliko yanayojenga.

Soma pia: Je, Kwa Nini Ni Muhimu Watu Wapate Maarifa Ya Ubunifu?

Hata hivyo, upo ubunifu usio na manufaa kwa wateja wala kwa jamii. Huu tunaweza kuuita ‘ubunifu hasi’; yaani ni ubunifu wenye madhara, usio na tija yoyote.

Kwa mfano, kwa mujibu wa gazeti moja, Asasi za Kiraia kutoka Tanzania, Kenya, Msumbiji, Uganda na Afrika Kusini zilikutana nchini Kenya, na kukubaliana kuupinga mradi wa majaribio ya mbegu za mahindi zilizobadilishwa vinasaba, kwa teknolojia ya uhandisi-jeni (genetic engineering), kupitia mradi wa WEMA – kwa kuwa teknolojia hiyo si rafiki.

Mradi huo unajinasibu kuwa ukikamilika mbegu hizo zitaleta suluhisho la usalama wa chakula katika kukabiliana na changamoto za mabadiliko ya tabia nchi kama ukame, wadudu na magugu vinavyowasumbua wakulima wa nchi zetu.

Hata hivyo, ubunifu huu kupitia tafiti za WEMA umetiliwa shaka kubwa na wachunguzi kutoka   Asasi hizo za Kiraia, baada ya kujiuliza maswali kadhaa. Kwa mfano je, ni kwa namna gani mbegu za WEMA zitarekebisha mabadiliko ya tabia nchi?

Kwa nini tusije na ubunifu wa kupata suluhisho la kweli la kukabiliana na tabia nchi moja kwa moja, badala ya kujificha kwenye kubadilisha vinasaba katika mbegu, au viumbe?

Maswali hayo yametoa hitimisho kuwa ubunifu huu ni mbinu tu za makampuni makubwa ya nchi tajiri kutaka kujilimbikizia biashara ya mbegu barani Afrika na kuwafanya wakulima wetu waendelee kuwa tegemezi wa mbegu za makampuni hayo kila mwaka.

Pamoja na sababu hiyo, kuna madhara mengine pia yanayohusishwa na vyakula vinavyotokana na teknolojia hii ya GMO, kama vile mzio au ‘allergy’- pamoja  na ugonjwa wa kansa -vikisababishwa na mabadiliko ya tabia za vinasaba vya mazao hayo, au ‘gene mutation’.

Mbali na ubunifu wa mbegu, kuna ubunifu mwingine hasi unaofanywa na baaadhi ya ‘wataalamu’ wetu mitandaoni. Katika hali ya kawaida mitandao ya kijamii inapaswa kutumika katika kupashana habari. Lakini hivi sasa kuna ‘wajanja’ wachache ambao wameanza kucheza na akili za watu mitandaoni. Wanatumia uwezo wao wa ubunifu kuingiza maudhui ya uongo au uzushi mitandaoni.

Kwa mfano, wapo wabunifu hasi ambao wanatumia ubunifu wao kuwachafua viongozi wa dini, siasa, au watu wengine maarufu. Wabunifu hawa wanacheza na programu za kompyuta ambapo huweza kutengeneza picha au video ikionesha kiongozi wa dini au taasisi fulani akiwa katikati ya machangudoa, na maneno chini ya picha yameandikwa, “mchungaji abambwa uchochoroni.”

Wakati fulani ufuatiliaji ukifanyika inagundulika kuwa hakukuwa na kitu kama hicho bali ni mchezo tu umefanywa ‘kiubunifu’ kumchafua mhusika kutokana na bifu tu lililokuwepo kati ya mchungaji na watu fulani.

Vile vile kuna vijana, kupitia programu za kompyuta, wamebuni nyenzo fulani katika simu za mkononi ambayo inamfanya yule anayekupigia simu asikie, kupitia simu yake, sauti za vilio na kwaya za maombolezo, kuonesha kuwa aliyekupigia yupo kwenye msiba, lakini kumbe amefanya usanii tu, ili usigundue kuwa yupo kwenye ‘faragha’ zake.

Ki-msingi huu nao ni ubunifu, lakini tujiulize je, ni ubunifu wenye manufaa? Jibu ni hapana. Ubunifu huu una madhara; wenye lengo la kuwafundisha watu uongo, hasa vijana au wanandoa, na hivyo unachochea vitendo vya kihuni.

Ushauri wangu: makala zangu zinasisitiza watu wajifunze kufanya ubunifu. Na kama wewe una kipaji au maarifa ya kufanya ubunifu basi jitahidi ubunifu wako uwe wenye tija; yaani ujikite katika kuleta mabadiliko chanya. Haya ni mabadiliko yanayolenga kuondoa changamoto zilizopo au kuongeza thamani ya kitu au bidhaa kwa manufaa yako mwenyewe, wateja na jamii kwa ujumla, na siyo kuleta madhara.

Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasirimali kivitendo.

Anapatikana kwa simu: 0718219530; e-mail: nzyy2001@gmail.com

Jinsi Ubunifu Unavyoweza Kuboresha Huduma Kwa wateja

Habari rafiki yangu,

Karibu tena katika makala nyingine inayolenga kukupatia maarifa ya ujasiriamali, ubunifu na stadi za maisha.

Makala ya leo itazungumzia suala muhimu sana la huduma kwa wateja, na namna ambayo ubunifu unavyoweza kuchangia katika kuboresha huduma hii na kumfanya mteja ajisikie ametendewa haki stahiki.

Siri kubwa ya mafanikio ya mjasiriamali ni huduma bora kwa mteja

Kila mtu anajua siku zote kuwa bila mteja hakuna biashara yoyote inayoweza kufanyika. Kusema kweli, biashara nyingi zinafanikiwa kwa sababu ya uwepo wa wateja. Kwa hiyo, kitu cha msingi katika biashara yoyote inayofanyika ni mteja, kwa sababu mteja ndiye anayeleta pesa katika biashara, na tunajua bila pesa au mapato hakuna biashara yoyote hapo.

Kwa bahati mbaya, pamoja na umuhimu huo wa mteja, biashara nyingi zimekuwa zikiendeshwa kimazoea. Suala zima la utoaji wa huduma bora, itakayomfanya mteja  aweze kurudi kwa mara nyingine, na labda amkaribishe rafiki au ndugu yake kuja kununua hapo, limekuwa likipewa uzito mdogo na wengi. Na hili limesababisha wajasiriamali wengi wapoteze wateja wao bila kujijua.

Jamier Yale Scott. (2002), anasema, “huduma kwa wateja ni mfululizo wa shughuli iliyoundwa ili kuongeza kiwango cha mteja kuridhika – yaani, hisia kuwa bidhaa au huduma imekutana na matarajio ya mteja.”

Kwa hiyo, ili uweze kuongeza kiwango cha mteja kuridhika, unapaswa kuwa mbunifu wakati wa utoaji huduma. Kumbuka wateja huvutiwa sana na vitu fulani hivi, ambavyo hufanywa au kusemwa na watoa huduma vikiwa na lengo la kuwatia hamasa wanunuzi, au wanunuzi tarajiwa, ili wavutike na kupenda kununua hapo.

Baadhi ya vitu au kauli ambazo Mjasiriamali anaweza kuzitumia zinaweza kumfanya mteja ashawishike kununua hata kama hakupanga kununua wakati huo, au ashawishike kurudi tena, au amshawishi rafiki yake aje kununua.

Kwa hiyo, kwa kuzingatia umri wa mteja, nafasi yake katika jamii, jinsia yake, n.k, mtoa huduma anaweza kuja na ubunifu wa maneno au kauli fulani ambazo zina mvuto au ushawishi kwa mteja, kama ifuatavyo:

Moja, kumkaribisha mteja mtu mzima unaweza kusema: “Oh, baba yangu, karibu sana, shkamoo. Pole sana na mvua, naona hali ya hewa leo siyo yenyewe! Nikusaidie nini mzazi wangu?” Ki-msingi hapa unamchota mteja wako kisaikolojia ajione anahudumiwa na mwanae kabisa, na hivyo si rahisi mteja huyu kuondoka bila kununua chochote.

Mbili, kumsifia mteja wako, wa kike kwa mfano. Hii inahusika zaidi wakati umeshamkaribisha vizuri na tayari amechagua nguo au viatu anavyovipenda. Kama anataka kujaribu nguo au viatu, waweza ingilia kati kisanii kwa kumsifia; “hakika dada yangu nguo na viatu ulivyochagua vimekupendeza ‘kinoma’, utafikiri vilitengenezwa kwa ajili yako, au walijua umbo na rangi ya ngozi yako. Yaani usiponunua ukweli utakuwa hukujitendea haki. Nakushauri ununue!”

Hii inachochewa na ukweli kuwa kina dada wengi wanapenda kusifiwa na kuonekana wamependeza. Hata hivyo, umakini unatakiwa hapa, hasa kumsoma vizuri mteja wako ili kujua umsifie maeneo gani na kwa kutumia maneno gani, usije ukajikuta umemkwaza.

Tatu, kumtia moyo mteja wako aliyeshindwa kufikia bei: Kuna wakati unaona kabisa mteja wako amevutiwa na bidhaa fulani, lakini ulipomtajia bei unagundua kuwa pesa aliyonayo ni ndogo sana ikilinganishwa na gharama ya bidhaa hiyo; usimkatishe tamaa.

Unaweza kumwambia, “pole sana mama yangu, ukweli ‘hand bag’ hii ingekufaa sana, lakini usijali kwa kuwa leo umepungukiwa. Naomba kafanye maarifa tena na siku ukifanikiwa usiache kuja, na mimi nakuahidi nitakujali kidogo katika bei.”

Vile vile, huwenda mteja wako kakuta bidhaa imeisha dukani kwako. Ongea naye ukimpa matumaini, “samahani sana mzee wangu, bidhaa uliyotaka imetuishia, lakini tayari tumeshaagiza, na mapema wiki ijayo ukija utaipata, pole sana kwa usumbufu, tafadhali njoo wiki ijayo!”

Kwa kumpa maneno mazuri mteja wako, unamteka kisaikolojia. Hata kama angeweza kwenda kununua sehemu nyingine, anaweza kusubiri hadi wiki ijayo aje anunue kwako.

Nne, kuomba msamaha haraka kama bidhaa ina mapungufu. Inapotokea kwenye biashara yako kukawa na upungufu fulani, omba msamaha haraka. Tuchukulie unafanya biashara ya kuuza chakula halafu ikatokea chakula hicho hakijaiva kizuri, ongea na mteja, “oh, samahani sana mteja wangu, sikutarajia hali hii, naahidi hali hii haitajitokeza tena, tafadhali usisite kurudi, utakuta mabadiliko.”

Kama utakuwa mnyenyekevu, ukaomba msamaha na kuahidi kesho utampatia huduma bora zaidi, ni wazi atakuelewa, na atapunguza hasira. Kwa kumueleza hayo, hiyo itamfanya mteja kujenga imani kubwa na wewe, na ni wazi atakuwa mteja wako siku nyingine.

Tano, kumuaga vizuri mteja wako. Hili si jambo dogo, lina umuhimu sana! Kwa kumuaga vizuri mteja wako unajibandika picha yako katika ubongo wake wakati anaondoka. Na kila anapotaka kununua kitu, picha ya kwanza inayokuja kichwani mwake ni ya kwako. Ongea naye vizuri, kwa mfano, “asante sana kwa ‘kuniungisha’, karibu tena mama yangu, nakutakia siku njema.”

Ushauri kwa Wajasiriamali: Ubunifu ni jambo lisiloepukika kama unataka kupiga hatua na kama unataka kuushinda ushindani wa biashara. Eneo moja muhimu sana ni hili la huduma kwa wateja. Jitahidi kufikiri kwa kina ni mbinu zipi utaziweka ili kumfanya mteja ajisikie ni mtu muhimu anapokaribia biashara yako. Tafadhali fanya ubunifu kila siku, itakulipa!

Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasirimali kivitendo.

Anapatikana kwa e-mail: nzyy2001@gmail.com

 

Je, Waijua Siri Ya Kupambana na Ushindani Wa Biashara? Jitofautishe!

Rafiki mpendwa,

Karibu tena katika mfululizo wa makala zangu zenye lengo la kuelimishana kuhusu masuala ya ujasiriamali, ubunifu na stadi za maisha.

Katika moja ya makala zangu nimeandika kuhusu changamoto mbalimbali za biashara. Moja kati ya changamoto hizo ni ushindani katika biashara.

Ukifanya vitu tofauti hakuna mtu wa kukuzuia kupata ushindi

Kumbuka unapoamua kufanya biashara ujue kwamba unaingia katika ushindani na wenzako uliowakuta katika biashara hiyo, au wengine ambao wataingia baadaye kufanya biashara kama yako. Kwa hiyo huwezi kukwepa suala la ushindani. Unachotakiwa kufanya ni kutafuta mbinu zitakazokuwezesha kufanya vizuri ndani ya ushindani uliopo.

Kila siku ushindani katika biashara unaongezeka, kwa kuwa kila siku kumekuwa na biashara mpya zinazoanzishwa. Si ajabu kukuta watu zaidi ya kumi wakifanya biashara ya aina moja kwenye mtaa mmoja. Wapo wafanyabiashara walioshindwa kupiga hatua kutokana na kuzidiwa na nguvu ya ushindani.

Hata hivyo, kuna njia au mbinu ambazo zikitumika zitawafanya wafanyabishara kuushinda ushindani. Na mbinu kubwa katika uendeshaji wa biashara ni kujitahidi kuwa tofauti na wengine. Unatakiwa ujipange ili utoe kitu tofauti kitakachokufanya ujipambanue miongoni mwa wenzako. Unatakiwa uhakikishe unafahamika kwa kitu fulani kizuri au chenye thamani zaidi kwa mteja kuliko wenzako.

Zifuatazo ni baadhi ya mbinu hizo:

Kwanza, toa bidhaa au huduma zenye ubora. Hakikisha wateja wako wanapata bidhaa au huduma bora zaidi ya washindani wako, na wanaridhika. Jitahidi kufumbua macho na kutega masikio yako vizuri ili uyaone au kuyasikia yote yanayolalamikiwa kuhusu bidhaa au huduma yako, kisha yafanyie kazi haraka.

Kwa mfano, kama unazalisha na kuuuza vifaa vya ujenzi, mfano tofali, jitahidi ufyatue tofali zenye ubora unaofaa, kuzidi washindani wako; yaani mali ghafi unayotumia iwe yenye viwango na vipimo stahiki. Tofali yenyewe iwe na vipimo sahihi vya urefu, upana na kina. Tofali iwe imemwagiliwa maji ya kutosha kuifanya iive na kukomaa vizuri na iwe imara kabisa.

Ukiwapa wateja bidhaa zenye ubora, sifa hii itaenea kidogokidogo hadi itamfikia kila mtu, na hapo bidhaa yako itajitofautisha na zile za washindani, zilizo chini ya kiwango.

Pili, jifunze udhaifu wa washindani wako. Inawezekana wote mkawa mnatoa bidhaa bora kabisa. Lakini kwa uchunguzi wako ukagundua wenzio wanatoa lugha mbaya kwa wateja wao. Ukigundua hilo lifanyie kazi haraka. Ongeza ukarimu kwa wateja. Wakaribishe vizuri, ongea nao ki-ustaarabu, waoneshe kuwa unawajali na upo kwa ajili yao. Onesha unajali muda wao na usiwacheleweshe wateja wako bila sababu, n.k. Utaona matokeo yake.

Tatu, kuwa mbunifu. Nimeandika sana umuhimu wa ubunifu katika ujasiriamali, na nikasisitiza kuwa ujasiriamali na ubunifu ni chanda na pete. Biashara yoyote inayoendeshwa kiubunifu ni rahisi kuushinda ushindani na kusonga mbele.

Mbunifu kila wakati ana jicho la udadisi. Ukiwa na jicho la ki-dadisi utajua wateja wako wanataka nini, kwa utaratibu gani na kwa wakati gani. Utajua ni kitu gani ambacho ukikiongeza au kukipunguza katika bidhaa au huduma yako kitawafanya wateja waridhike zaidi.

Kwa mfano, Zuhura Abdi ni mjasiriamali mdogo. Zuhura anatengeneza maandazi na kuyauza kila siku asubuhi, ikiwa ni huduma ya kifungua kinywa kwa jirani zake. Janeth John, baada ya kuona Zuhura anafanya biashara yenye faida, naye anaanza kupika maandazi, kama ya Zuhura, na kuyauza asubuhi pembeni kwa Zuhura, kwa staili ileile. Hapa ushindani unaanza, na mauzo ya wote yanakuwa ya wastani. Wanagawana wateja na kuanza kutafutana uchawi.

Roza Jacob, naye anatamani kufanya biashara ya aina hii.  Lakini yeye, kabla ya kuanza anafanya utafiti kidogo, na kugundua kuwa baadhi ya walaji wa maandazi wanalazimika kula maandazi kwa kuwa hawazioni chapati zikiuzwa. Lakini pia anagundua kuna mahitaji ya vitafunwa hivi wakati wa jioni kwa kuwa baadhi ya wateja hupendelea kunywa chai na maandazi au chapati wakati wa jioni.

Roza anaamua kuuza maandazi na chapati, lakini anaviongezea ladha kidogo ya viungo fulani. Lakini pia anaboresha usafi na kuongeza ukarimu na lugha nzuri kwa wateja. Na badala ya kuuza asubuhi tu, yeye anaanza kuuza jioni pia. Huu ni aina ya ubunifu ambao unamtofautisha Roza na wenzake, na anafanikiwa ‘kuwazoa’ wateja wote wa Zuhura na Janeth.

Mfano mwingine unatoka kwa Mjasiriamali Furaha Tonya, mkazi wa Mwanza. Furaha anasema aliamua kuanzisha biashara ya kuuza dagaa waliokaangwa baada ya kugundua hii ni fursa bayana. Yeye pia alifanya utafiti kidogo na kugundua kwamba wafanyabishara wengi wa dagaa wanauza dagaa ghafi, hasa waliokaushwa kwa jua na kuanikwa juu ya mchanga. Lakini pia aliona dagaa wakiuzwa kwa mafungu, bila hata kufungashwa.

Anadai aliamua kuwaza ki-ubunifu, akitaka ajitofautishe na wengine. Kwa hiyo anasema, “niliwatembelea wauzaji wa jumla wa dagaa hadi nikawajua wanaouza dagaa walioanikwa kwenye virago au maturubai maalumu, hivyo dagaa hawa hawana mchanga au uchafu mwingine.”

Anaongeza, “nilipogundua baadhi ya wafanyabiashara wanakaanga dagaa kwa mafuta yanayotokana na wanyama, mimi nikaona nijitofautishe; nikaanza kuwakaanga dagaa kwa kutumia mafuta ya mbegu za mimea, ambayo hayana madhara au ‘rehemu’ kwa mlaji.”

Anasema, “ubunifu wa ziada niliouweka ni pamoja na kubuni vifungashio vyenye ubora, na kuweka pia alama za utambulisho wa bidhaa yangu, au nembo maalum. Ukweli niliweza kuongeza thamani ya bidhaa yangu kwa kiasi kikubwa. Wateja waliongezeka sana na mauzo yalipanda zaidi ya mara mbili, na bado ubunifu unaendelea.”

Ushauri wangu; mjasiriamali unapaswa ujifunze kujitofautisha na wenzako. Usifanye biashara kwa mazoea, yaani kufanya mambo yaleyale, katika mazingira yaleyale, kila siku. Fungua akili, tega masikio na fumbua macho yako ili ujifunze na kufanya ubunifu kila siku. Kuna namna nyingi za kujitoutisha kulingana na biashara yako – na kila mtu anaweza kufanya hili. Ukijitofautisha hakika utaushinda ushindani.

Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasirimali kivitendo.

Anapatikana kwa simu: 0718219530; e-mail: nzyy2001@gmail.com