Usikariri, Mtaji Wa Biashara Sio Pesa tu – Jiulize Una Nini Wewe?

Habari ndugu na rafiki,

Karibu tena katika mfululizo wa makala zangu zenye lengo la kuelimishana kuhusu masuala ya ujasiriamali, ubunifu na stadi za maisha.

Nimeandika huko nyuma kwamba ukishapata wazo zuri la biashara kinachofuata ni kulitia wazo hilo katika vitendo. Sasa, mara nyingi katika hatua hii huwa kunatokea changamoto. Yaani katika utekelezaji kunatokea vikwazo au changamoto ambazo wakati fulani zinamtia mjasiriamali hisia za kukata tamaa.

Changamoto inayoongoza kutajwa ni kukosekana kwa ‘mtaji’, na hapa ukifuatilia kwa makini, kinachoongelewa kama mtaji sio kingine, ni pesa au mkopo.

Fedha yaweza kutumika kama mtaji, lakini sio kila wakati

Utasikia: “Nina ndoto yangu, na ninatamani kuanzisha biashara…lakini aah, sina mtaji bwana…na sijui nitaupata wapi!” Hii ni kauli inayotolewa na watu wengi na huenda umeshawahi kumsikia mtu wako wa karibu akisema, au wewe mwenyewe umewahi kulalamikia suala hili.

Ukweli ni kwamba, watu ambao wanataka kweli kuingia kwenye biashara, huwa wanaingia na hawakubali sababu yoyote iwarudishe nyuma. Hii inamaanisha kwamba wale wanaokubali sababu yoyote iwazuie, au wale wanaosema hawajaweza kuanzisha biashara kwa sababu ya kukosa mtaji, kwa maana ya pesa, ujuwe hawa hawajadhamiria ipasavyo kuingia kwenye biashara ila tu wanatafuta sababu rahisi ya kushindwa kuanza.

Kama kweli mtu umedhamiria, na upo tayari kuingia kwenye biashara, hakuna kinachoweza kukuzuia kuingia na kuanza. Kukosekana mtaji, hasa pesa, haijawahi kuwa sababu halisi, kwa sababu wapo watu wengi walioweza kuanzisha na kukuza biashara zao wakiwa hawana pesa kama kianzio.

Mtaji ni neno ambalo watu wengi hawalifahamu vizuri maana yake au wanajichanganya katika matumizi yake, na hasa wanapolihusisha neno hilo na dhana ya pesa. Kwa lugha rahisi, mtaji ni kitu au rasilimali yoyote ambayo mtu anaweza kuitumia ili imwezeshe kuanzisha biashara.

Kitu au rasilimali hii ndio ambayo itamfanya mtu yeyote, kwa kuzingatia hali na mazingira yake, aweze kuanzisha biashara na kuifanya biashara yake ikue. Dhana ya pesa kama mtaji mara nyingi inajitokeza kwa kuwa pesa hutumiwa kama njia ya haraka zaidi pale ambapo mtu anataka kuibadilisha kuwa kitu au rasilimali nyingine kwa njia ya kufanya manunuzi ya bidhaa au huduma.

Kuna ushahidi mwingi tu unaoonesha kwamba mtaji sio pesa tu, yaani mtaji ni zaidi ya pesa. Bosco John ni Mjasiriamali aishiye Dar-es-salaam. Bosco anasema, mtaji sio pesa tu, hivyo ukikosa pesa usije ukaanza kulialia, na kuona huwezi kufanya lolote.” Anasisitiza kwa kusema kwamba, uwe na ajira, usiwe na ajira, binaadamu unapaswa kujitahidi kuiangalia dunia kwa mtazamo tofauti, kwani kila mtu ana uwezo wa kufanya makubwa.

Bosco anatoa mfano akisema, “mimi baada ya kuona sina pesa, wala hakuna ndugu wala rafiki yeyote mwenye uwezo wa kunisaidia mtaji (pesa) wa kuanzishia biashara, nilijiuliza swali moja tu; je, nina nini mimi ambacho ni cha kwangu?”

Anadai kwamba aligundua ana uwezo mzuri wa kuongea kiingereza, kwa kuwa aliwahi kufanya kazi za utunzaji bustani kwenye familia ya wazungu fulani, ambao baadaye walirudi kwao, na yeye kulazimika kurudi kijijini kwa wazazi wake. Pesa kidogo aliyoachiwa na wazungu wale aliwapelekea wazazi wake ili wafanye ukarabati wa nyumba yao iliyokuwa na hali mbaya, na iliyobaki ilitumika kununulia chakula, ikaisha.

Kwa hiyo, anasema kwamba baada ya kumalizana na wazazi alirudi mjini, ambapo katika pitapita yake mjini, akiwaza nini cha kufanya, alipumzika karibu kabisa na kibanda cha wasanii na wabunifu wa uchongaji vinyago. Hapo alishuhudia wazungu, na watalii wengine, waliokuja pale kutaka kununua, na pia kupata maelezo kuhusu vinyago hivyo.

“Niligundua kuwa kati ya wale wabunifu wa vinyago hakuna aliyekuwa na uwezo wa kuwaelewa vizuri wale wazungu. Kwa hiyo niliwaza kwamba hapa naweza kufanya kitu. Walipoondoka wale wageni niliwafuata wale wabunifu, nikaongea nao, na kuwaomba niwasaidie kuongea na wageni mbalimbali wasiojua Kiswahili,” anasema Bosco.

Baada ya kukubaliwa, Bosco anadai kuwa alitumia vizuri sana uwezo wake wa lugha ya Kiingereza, kuongea, kutoa maelezo na kufafanua mambo mengi yahusuyo vinyago. Hili lilisababisha  ongezeko kubwa la wateja, na mauzo ya vinyago pia yaliongezeka.

“Kwa kuwa wageni wale waliniamini na kuvutiwa na lugha na ucheshi wangu niliweza kuwashawishi wakanunua vinyago kwa bei ya juu kidogo, zaidi ya bei iliyopangwa na watengenezaji wa vinyago hivyo, kwa hiyo na mimi nikapata ‘dola’ kidogo ambazo wenyeji wangu waliridhia nichukue.” Bosco alidai.

Bosco anasisitiza, “ili ufanikiwe kimaisha usiwe mvivu wa kufikiri kwani uvivu wa kufikiri umewafanya Watanzania wengi kuonekana maskini, ilhali Taifa lina rasilimali nyingi. Tazama, mimi nimetumia uwezo wangu wa lugha na kuweza kutengeneza pesa, ambazo nimezitumia kuanzishia biashara niliyoipenda.”

Anashauri, “ifikie mahala elimu inayotolewa shuleni imjenge mtoto kuwa mdadisi, mgunduzi na mwenye uthubutu, badala ya kuwa tegemezi. Awe amefaulu au amefeli masomo ya shule, awe na pesa au hana, aweze kutumia uwezo wake wa kufikiri na kujiuliza ni kitu gani afanye kiweze kumuondoa kwenye umaskini na utegemezi.”

Ushauri wangu, hasa kwa vijana, jiulize una nini? Je, una kipaji au ujuzi wowote? Kwa mfano, kuimba, kuchora, uwezo wa kuongea, ujuzi wa kuchonga n.k. Hivi vyote mwanzoni siyo pesa, lakini ukiwa makini na mwenye uthubutu unaweza kuvigeuza vitu hivi kuwa biashara ambayo itakupatia kipato. Ukipata pesa unaweza sasa kuitumia kuimarisha kipaji chako au kufanya mradi mwingine wowote.

Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasirimali kivitendo.

Anapatikana kwa e-mail: nzyy2001@gmail.com; Simu: 0718219530

 

Jinsi Hamu Ya Kujifunza Inavyomchochea Mjasiriamali Kufanya Ubunifu

Rafiki mpendwa,

Karibu tena katika mfululizo wa makala zangu zenye lengo la kuelimishana kuhusu masuala ya ujasiriamali, ubunifu na stadi za maisha.

Katika makala hii nitazungumzia jinsi ambavyo mjasiriamali anavyoweza kujenga uwezo wa ubunifu kutokana na hamu au hamasa ya kujifunza aliyojijengea ndani yake. Matokeo ya kujifunza ni kupata elimu au maarifa na kuitumia elimu hiyo kufanya mabadiliko yenye tija.

Elimu, kwa maana pana, ni tendo au uzoefu wenye athari ya kujenga akili, tabia ama uwezo wa kimaumbile wa mtu binafsi. Katika dhana ya kiufundi, elimu ni njia ambayo hutumiwa makusudi na jamii kupitisha maarifa, ujuzi na maadili kutoka kizazi kimoja hadi kingine.

Ukipenda kutembelea maonesho ya biashara utajifunza mengi

Kujenga hamu au hamasa ya kujifunza ni moja ya njia muhimu za kuelimika na kuweza kufanya mabadiliko mbalimbali. Umuhimu wa kujifunza unaweza kuthibitishwa kupitia kwa Mjasiriamali na Mbunifu, Bi. Subira Mwaruka, ambaye ni mbunifu wa vikapu vya kupikia.

Kwa kawaida kikapu ni chombo kinachotumika hasa na kina mama wakienda sokoni au gengeni kununua chakula kwa matumizi ya familia. Je, umewahi kufikiria kuwa kikapu kinaweza kutumika kuivishia chakula? Huwezi kuamini, lakini Subira, akinukuliwa na gazeti moja, anasema kwamba kikapu maalumu alichobuni kina uwezo wa kuivisha hata maharage.

Yaani, unachemsha maharage kwenye moto wa kawaida, mfano gesi, kwa dakika tano hivi, halafu yakishachemka, unaipua na kuyafunika maharage yako ndani ya kikapu hiki, na baada ya kama masaa mawili, ukiyatoa maharage katika kikapu utakuta yameiva kabisa.

Anasema kuwa chakula kilichopikwa katika kikapu hiki, mfano wali, hakina ukoko, hakiungui na wala hakipotezi ladha yake.

Subira anasema, “kila penye nia pana njia, kwani jitihada zangu za kutamani kujifunza na kufanya vitu ki-utofauti, imenisaidia sana kuwa mbunifu.” Anadai pia kuwa hamu aliyonayo na jitihada za kuhudhuria maonesho yanayowakutanisha wajasiriamali kutoka nchi mbalimbali imemuwezesha kujifunza mengi na kuwa mdadisi.

“Kila ninapohudhuria maonesho, hulazimika kutafuta kitu kipya cha kujifunza, ambacho ni kigeni katika soko la Tanzania. Ukweli nina hamu ya kujifunza kitu kipya kila siku, hivyo mawazo ya ki-bunifu nayo huja kila siku, “ anadai Subira.

Subira, mbunifu wa teknolojia ya vikapu vya kupikia anasema kwamba hii ni teknolojia nzuri na rahisi ambapo kikapu, kilichotengenezwa kwa ukindu au malighafi nyingine, hufanyiwa utaalamu ambao hukifanya kiwe na uwezo wa kutunza joto la chakula muda mrefu, kiasi cha kuweza kuivisha chakula cha aina yeyote ile.

Anasema, “kuna material (malighafi) tunaiweka kwa utaalamu ndani ya kikapu, inayofanya kiweze kutunza joto kwa muda wote.” Anadai kwamba ujuzi huu aliupata baada ya kuhudhuria maonesho ya Wajasiriamali huko Kenya. Huko aliona vitu ambavyo wengine wanafanya. Aliona jinsi wanavyoongeza thamani ya bidhaa za kawaida zikawa bidhaa bora na zenye tija na mvuto zaidi kwa wateja.

Subira amepata faida kubwa baada ya kupata maarifa haya kupitia elimu. Yeye binafsi ameongeza thamani ya vikapu vyake na kuongeza mauzo kwa kiwango kikubwa.

Lakini pia, ubunifu wake umefanya matumizi ya vikapu vyake kuokoa matumizi ya nishati ya mkaa na kuni. Anasema ubunifu huu umempunguzia mama muda mwingi wa kukaa katika moto, na kumuepusha na magonjwa yatokanayo na moto au moshi.

Zaidi ya hayo, ameongeza kipato kwa kujiajiri katika kazi ya kutengeneza na kuuza vikapu, na pia anaendelea kutoa mafunzo ya ujasiriamali na ubunifu kwa Wajasiriamali wengine waliopata hamasa ya kupata ujuzi huu.

Kwa hiyo, kuna somo kubwa la kujifunza kupitia kwa Bi. Subira. Kwanza, Mjasiriamali unapaswa kujitambua na kujitengeneza. Unapaswa kujenga hamu ya kutaka kujua mambo mbalimbali yanayolenga kuongeza thamani ya vitu, na kutatua changamoto zilizopo. Unapaswa kuwa na hamasa ya kujifunza vitu vipya, kila siku.

Pili, unapaswa kufungua milango yako yote ya fahamu ili iweze kuona, kusikia, kunusa na kuhisi vitu vyenye manufaa, na kuvifanyia kazi.

Ukijenga hamasa ya kujifunza na kuvuna maarifa, utapata uwezo wa udadisi utakaokufanya uanze kuona au kusikiliza vitu kwa mtazamo tofauti, mtazamo wa ki-dadisi, wenye lengo la kujifunza zaidi, kujenga taswira akilini, na kufanya vitu vitokee kiuhalisia. Na hii ndio hasa dhana ya ubunifu.

Nakukaribisha tena msomaji wangu katika mfululizo wa makala zangu za ujasiriamali, ubunifu na stadi za maisha, ili uendelee kupata maarifa na kufanya mabadiliko yako binafsi na jamii kwa ujumla.

Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasirimali kivitendo.

Anapatikana kwa e-mail: nzyy2001@gmail.com

 

Hivi Ndivyo Vichocheo Vya Upatikanaji Wa Mawazo Ya Ubunifu

Habari ndugu na rafiki,

Napenda kukukaribisha tena katika mfululizo wa makala zangu zenye lengo la kuamsha bongo zetu na kuwafanya wasomaji wachukue hatua katika kubuni, kuanzisha, kuboresha na kuongeza thamani ya shughuli zao za kijasiriamali.

Nimeeleza huko nyuma kuwa binaadamu wa kawaida huzalisha takriban mawazo 60,000 kila siku. Na kwamba kila ukionacho hapa duniani, kilichoundwa, ni matokeo ya uwezo wa binaadamu kufikiri na kutenda.

Yapo mazingira yanayochochea akili ya binaadamu kuibuka na fikra au mawazo  ya ki-bunifu ambayo yakitiwa katika matendo yanaweza kumletea mtu mafanikio au kuleta mabadiliko makubwa katika jamii, au kuongeza thamani ya vitu, bidhaa au huduma kwa wateja.

Baadhi ya mazingira hayo ni kama ifuatavyo:

Kwanza kabisa, ni mazingira asilia. Haya ni mazingira yasiyo ya kawaida, ambapo wazo linakuja lenyewe tu. Kama nilivyoeleza katika makala hii, bofya, wazo la ki-bunifu linaingia katika akili ya mtu likitokea katika ‘ulimwengu wa roho’; yaani mtu umekaa mahala, huna hili wala lile, mara ghafla wazo zuri  linakujia kama ndoto hivi. Kikubwa hapa, wazo zuri likiingia tu, liandike haraka.

Ukizoea kutembelea Misitu, utaona Miti ya ajabu, itakayokupa hamasa ya ubunifu

Pili, kujifunza kupitia milango ya fahamu. Mungu katupatia milango ya fahamu kama macho, pua, na masikio. Kila siku ‘ukiwa’ na macho, masikio na pua, utajifunza mengi. Angalia huku na kule, sikiliza, au nusa kila mahala; utaona, utasikia na kuhisi vitu mbalimbali, na utapata picha au taswira ndani ya akili yako. Baadaye, ukitulia na kuchakata taswira hizo unaweza kuja na ubunifu wa maana kabisa.

Tatu, kujifunza ubunifu kupitia kazi za sanaa. Hapa unatakiwa kujizoeza kusoma, kutazama au kusikiliza kazi mbalimbali za sanaa, za sasa na hata za zamani. Mwandishi mmoja amewahi kusema kuwa duniani ‘hakuna makapi’. Anasema, “pitia magazeti, majarida, hifadhi za muziki, michoro, au kumbukumbu zozote za sasa na zamani, na vitu utakavyoviona vitakupatia mwanzo wa kufanya ubunifu wako”.

Kwa mfano, anasema kwamba unaposikiliza muziki wa zamani, kwa umakini – mapigo ya muziki au ‘beat’, na sauti ya mwimbaji, au ‘lyrics‘, vinaweza kukusisimua kisaikolojia na bila kujitambua ukapata msukumo fulani akilini, na ukaja na wazo la kibunifu ambalo hujawahi kulitarajia kabisa. Hivyo, anasema, “uwezo wa kubadili ‘makapi’kuwa kazi ya sanaa ni moja ya mbinu za ubunifu”.

Soma pia: Ubunifu huu utakufungulia zaidi fursa za biashara

Nne, kujifunza kupitia kuiga kazi za ubunifu za wengine. Kuna maarifa kibao katika kuiga. Kuiga kunakupa uwezo wa kujifunza wengine wamefanya nini, na vilevile kuiga kunamsaidia mbunifu kuona ni kwa vipi anaweza kuchanganya maarifa aliyoiga na maarifa yake binafsi, kupata kitu kipya.

Kwa mfano, Mwandishi mmoja anasema kwamba kuiga kazi za wengine sio wizi, bali ni njia ya kujifunza na kukua. Kikubwa ni kwamba usiige kila kitu, bali chukua kitu kilichopo, kigeuze kulia-kushoto, chini-juu, au nje-ndani, na utajikuta una kitu kipya kabisa cha kwako.

Tano, jichanganye na wabunifu wengine. Hapa unatakiwa ujenge mazoea ya kukaa na kuongea na wabunifu wazuri waliopo, usikilize mawazo na mbinu zao. Wabunifu wenzio sio washindani; hawa ni wenzako. Ukiwa nao unaweza kutoa mawazo, maoni au ushauri wako halafu ukasikiliza ya kwao. Hili pia linaweza kuzaa ushirikiano utakaowezesha kufanya kazi fulani pamoja.

Sita, shiriki maonesho ya kazi za sanaa na ubunifu. Hapa utaona kazi za wengine, utapata fursa ya kukutana na kuongea na wabunifu wengine na kujua wanafanya vipi ubunifu wao.

Saba, jivue kitanzi cha mazoea. Mara nyingi binaadamu hujisikia amani zaidi anapokua katika mazingira aliyoyazoea, au ‘confort zone’.  Hapa, mtu unajiona uko salama kabisa. Ni kweli? Hapana, hauko salama! Unapaswa kutoka katika mazingira haya na kujaribu kufanya kitu tofauti.

Kama ulizoea kuchora, waweza kujaribu kuchonga pia, au kufuma n.k. Kwa kujaribu kufanya kitu tofauti unaweza kupata msukumo mpya na ukajikuta unafanya kitu ambacho hukutarajia kabisa, kwenye hiyo hiyo fani yako.

Nane, jizoeze kutembea na ‘note book’, peni au kamera. Walio na ‘simu janja’ hawana tatizo katika hili. Katika kutembea utaona mengi na utasikia mengi pia. Sasa, chochote utakachokiona au kukisikia, na ukavutiwa nacho; kwa mfano, mchoro mzuri, kinyago cha kuvutia, au mapambo juu ya ukuta au nguo n.k., basi usipoteze muda, andika, rekodi au piga picha, kisha hifadhi.

Tisa, jizoeze kutembelea fukwe, misitu, mbuga za wanyama, bustanini, na sehemu kama hizo. Huko, utaona vitu usivyozoea kuviona, piga picha, hifadhi. Utasikia sauti za ajabu za wanyama, ndege, wadudu, n.k., rekodi. Utaona miti iliyojikunja kiajabu, au mawe yenye maumbo ya kipekee, piga picha. Ukirudi nyumbani, ukatulia na kuvifanyia tafakuri vitu hivi, utapata mahala pa kuanzia kufanya ubunifu wa ajabu kwenye biashara, sanaa au fani yako yoyote!

Kumi, soma ripoti za tafiti mbalimbali. Kila mwaka wanavyuo wanakuja na ripoti mbalimbali zinazotoa mapendekezo ya namna ya kutatua changamoto au matatizo ya jamii au wateja wa bidhaa fulani. Ripoti hizi ni vyanzo vizuri vya mawazo ya ubunifu.

Ushauri kwa wajasiriamali: Nimeandika katika makala zangu kwamba ujasiriamali na ubunifu ni chanda na pete, huwezi kuvitenganisha kama unataka kupata tija ya maana katika biashara yako. Hivyo nasisitiza wajasiriamali wajifunze ubunifu kwa nguvu zote ili waweze kuongeza ubora na thamani ya bidhaa, michakato au huduma wanazotoa kwa wateja wao; na wakifanya hivi hakika watajiongezea tija.

Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasirimali kivitendo.

Anapatikana kwa simu: 0718219530; e-mail: nzyy2001@gmail.com

 

 

 

 

Je, Kwa Nini Ni Muhimu Watu Wapate Maarifa Ya Ubunifu?

Habari ndugu na rafiki,

Karibu tena katika mfululizo wa makala zangu zenye lengo la kuelimishana kuhusu masuala ya ujasiriamali, ubunifu na stadi za maisha.

Wapo watu ambao wana vipaji vya ubunifu. Wanaweza kufikiri ki-ubunifu na wakaja na mawazo mazuri ya ubunifu ambayo yakifanyiwa kazi yanazaa kitu au bidhaa mpya, au hata uvumbuzi.

Esther Mahlangu wa Afrika Kusini, amepata umaarufu na pesa kwa ubunifu wa kuchora urembo magari.

Watu hawa, tunaweza kuwaweka kwenye kundi maalumu; la watu wenye maono, ambao kupitia ‘ulimwengu wa roho wao hupata picha au taswira ya vitu ambavyo baadaye wanavifanya kuwa vitu halisia.

Lakini wapo watu ambao hawaoneshi uwezo wa ubunifu, wala hawajawahi kufikiria kubuni chochote. Hawa, wakiwezeshwa, wanaweza kuwa wabunifu wazuri; yaani  wamekosa tu mwongozo na hamasa ya kufikiri ki-ubunifu, kitu ambacho kikipatikana kitawafanya hawa nao waweze kuwa wabunifu.

Kifupi ubunifu ni uwezo wa mtu kuanzisha au kuvumbua kitu chochote kipya, chenye utofauti na ubora zaidi, ambacho kina thamani au kinaongeza thamani ya kitu kilichopo, kwa manufaa ya mtu mwenyewe, wateja, na jamii kwa ujumla.

Mwandishi mmoja anasema kwamba licha ya kuwa na utitiri wa wahitimu wa Vyuo Vikuu, bado Tanzania tuna wasomi wachache sana ambao ni wabunifu. Ukweli, wengi ni watazamaji tu, hawana maarifa ya ki-bunifu kuweza kutatua changamoto zinazoikabili jamii, wala kuja na kitu kipya cha kuboresha maisha yao binafsi, mazingira yao au maisha ya jamii kwa ujumla.

Mwandishi anasema, “tuna wasomi wengi nchini Tanzania na wanazidi kuongezeka. Wapo wenye diploma, digree moja au hata zaidi. Sasa uliza je, wamewahi kugundua kitu gani chenye manufaa kwa jamii, kabla au baada ya kupata elimu hiyo? Ukweli unaweza usipate wengi.”

Anaongeza kwa kusema kwamba tatizo kubwa ni ukosefu wa fikra bunifu ndani ya vichwa vya wasomi wetu. Watu wamesoma masomo ya fani zao tu, bila kupata maarifa, ujuzi, na uwezo wa kuja na ubunifu.

Hii ina maana kwamba wasomi wameongezeka lakini hawana majibu ya matatizo ya jamii. Wana elimu ya nadharia zaidi na maneno meengi yasiyotekelezeka. Hii inaweza kuitwa elimu ya bandia, isiyo na manufaa ya maana.

Elimu ya kweli ni ile inayochimbua maarifa, ung’amuzi, ugunduzi na ubunifu, ambao kila mtu huja na vitu au mbinu zinazoweza kumsaidia kukabiliana na changamoto zilizo katika mazingira yake na kuisaidia jamii hiyo kupiga hatua.

Kwa hiyo ipo haja kubwa ya kuwapatia wasomi wetu, wajasiriamali, wasanii mbalimbali, pamoja na wananchi wa kawaida maarifa ya ubunifu ili wapate uwezo wa kufikiri; yaani wawe na ‘jicho la udadisi’.

Na hiki ndicho ninachokifanya hapa kupitia katika makala zangu za ujasiriamali, ubunifu na stadi za maisha – kuwasaidia watu kufikiri na kutenda ki-ubunifu! Na ninakuomba rafiki yangu tuwe pamoja ili tupate maarifa haya.

Jicho la udadisi lina nafasi kubwa katika kumtengenezea mtu uwezo wa kuchambua maarifa, uwezo wa ung’amuzi, na uwezo wa uvumbuzi; ambao mwisho wake ni kujenga uwezo wa kutatua changamoto mbalimbali.

Jicho la udadisi litawafanya wale waliosoma kidogo masomo kama stadi za kazi, wakiwa shule ya msingi au sekondari, wapate uwezo wa kujenga kitu kikubwa zaidi, cha ki-bunifu, juu ya ujuzi walionao wa stadi za kazi.

Kwa kutumia jicho la udadisi, wasomi na wasio wasomi wanaweza kuwa na uwezo wa kulitazama soko au jamii yao ki-udadisi, wakajua soko linahitaji nini, lina changamoto zipi, au bidhaa gani inaweza kuongezewa ubora au thamani, au mchakato upi ufanyiwe maboresho zaidi.

Ili mtu awe mbunifu sharti apewe maarifa ya kufikiri; yaani kufikiri ki-ubunifu; kutengeneza maono na kujenga picha au taswira akilini, na kuitafsiri kivitendo. Hii inasaidia kumfanya awe na uwezo wa kutoa sababu ya vyanzo vya changamoto au matatizo ya jamii, na kuwa na maarifa ya kutatua matatizo hayo.

Mtu akishajenga utamaduni wa ubunifu anapata uwezo wa kupambana na mazoea, hivyo anakuwa mdadisi, na udadisi unamfanya kila wakati ajiulize maswali, kwa mfano, “je, kwa nini kitu au mchakato huu uko hivi, na mimi nifanye nini ili kuongeza thamani, ubora, tija, au ufanisi wa kitu hicho.” Atajiuliza tena, “je, niongeze au nipunguze nini ili nilete manufaa au thamani kubwa zaidi ya hii ya sasa?”

Kwa kujiuliza maswali haya, na mengine, mbegu ya udadisi inapata uimara zaidi. Na jinsi mtu anavyozidi kujishughulisha na ubunifu, akili inajengeka na kupata hamasa, na hivyo anapata uwezo wa kuja na ubunifu au uvumbuzi mkubwa zaidi.

Kwa hiyo, kwa mfano, Wajasiriamali wakipata maarifa ya jinsi ubunifu unavyofanyika, na mbinu zake, watahamasika kuja na mikakati ya makusudi katika kufanya ubunifu, katika jitihada zao za kuboresha bidhaa au huduma wanazowapa wateja wao.

Wakihamasika, Wajasiriamali watafanya ubunifu wakiwa na mipango mahsusi na ya makusudi ya kufanya ubunifu huo; na hii itasaidia kuufanya ubunifu usiwe jambo la kubahatisha, bali jambo lililopangiliwa na kusimamiwa kimkakati.

Kwa kumalizia, napenda kusisitiza kuwa maarifa ya ubunifu ni muhimu kwa kila mtu, na hasa wajasiriamali. Hivyo, nachukua fursa hii kukuhimiza wewe mjasiriamali kujenga hamasa binafsi ya kujifunza maarifa haya, yatakusaidia!

Uwezo wa Ubunifu ukikomaa ndani ya mtu ni rahisi sana mtu huyu kupata nguvu, hamasa na msukumo wa kuingia au kujizatiti katika ujasiriamali na kuendesha biashara kwa tija ya kutosha.

Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasirimali kivitendo.

Anapatikana kwa simu: 0718219530; e-mail: nzyy2001@gmail.com

 

 

 

Zijue Changamoto Za Biashara Mapema Ili Ujipange Kupambana Nazo

Rafiki,

Karibu tena katika makala nyingine inayolenga kukupatia maarifa ya ujasiriamali, ubunifu na stadi za maisha.

Katika moja ya makala zangu, bofya, niliandika kuhusu jinsi ya kukabiliana na hisia za kukata tamaa katika safari ya ujasiriamali. Nilieleza kuwa, pamoja na mambo mengine, watu wengi hukata tamaa wakati wa kulitia wazo au jambo katika vitendo. Yaani katika utekelezaji kunatokea vikwazo au ‘changamoto’ ambazo zinamtia mjasiriamali hofu na hisia za kukata tamaa.

Ukizijua changamoto mapema utajipanga kupambana nazo

Neno changamoto linaweza kuelezewa kama  mazingira kinzani yanayoleta upinzani kwenye maisha au mipango ya mtu. Wakati mwingine changamoto zinaelezewa kama matatizo au vikwazo vinavyojitokeza ili kupima uwezo wa mtu au taasisi kutumia akili na maarifa kukabiliana nazo..

Changamoto katika biashara, na maisha kwa ujumla, haziwezi kukwepeka, zipo kila siku, kwa sababu ni sehemu ya maisha. Hata hivyo uwepo wa changamoto wakati mwingine husababisha kuzaliwa kwa fursa ambazo humpasa mtu kuufikirisha ubongo wake vizuri zaidi ili aweze kuzivuna.

Kwa hiyo, ili mtu aweze kuzikabili changamoto na kuzitumia kuvuna fursa zinazoweza kujitokeza, hana budi kujiandaa. Yaani maandalizi ni lazima ili uweze kukabiliana na changamoto. Na huwezi kufanya maandalizi kwa kitu usichokijua. Lazima uzijue mapema changamoto mbalimbali zinazoambatana na ujasiriamali au uendeshaji wa biashara, kisha uweke mikakati na rasilimali kukabiliana nazo.

Usipozijua mapema na ukajiandaa, zitakapojitokeza zitakuwa zimekushtukiza, kama ajali, ukiwa huna kinga yoyote, na hiki huwa chanzo cha wajasiriamali wengi kupata hofu na kukata tamaa, na wengine kuamua kuachana na shughuli hiyo.

Katika uendeshaji wa biashara au ujasiriamali fahamu kuwa kuna vitu vingi ambavyo vinaweza kukuletea changamoto. Katika makala hii nitaeleza baadhi ya changamoto hizo:

Kwanza, changamoto za mitaji au mikopo. Hapa nazungumzia zaidi mtaji kwa maana ya fedha. Licha ya kuwepo fursa nyingi za kukopa, vijana wengi wanashindwa kupata mikopo hii kwa kukosa dhamana. Wanaofanikiwa kukopa wanalalamikia riba kubwa zinazotozwa na mabenki au taasisi za fedha kitu ambacho hakizifanyi biashara zao kupiga hatua ya maana.

Pili, urasimu mkubwa wakati wa ufuatiliaji wa huduma mbalimbali, mfano vibali, katika maofisi, hasa ya serikali. Katika ufuatiliaji wa huduma hizi kuna muda mwingi unapotea, nenda rudi ni nyingi na zinachosha.

Utasikia; mhusika kasafiri, ulipaswa kujaza fomu hii na sio hiyo, mtandao wa kompyuta uko chini, nenda kalete hiki au kile katika ofisi kadhaa nyingine, acha namba ya simu tutakupigia (wala hawapigi!), na mengine mengi. Huu unaitwa urasimu. Usipokuwa mvumilivu utapata jazba, utakata tamaa na huenda ukaachana na ufuatiliaji wa suala lako; na ikiwa hivyo basi tayari umekwama!

Tatu, changamoto za eneo la biashara. Ni muhimu kupata eneo zuri la kufanyia biashara yako. Lakini unaweza kujikuta umepata eneo lililo mbali na wateja wako, au lisilo salama, au lililokatazwa kisheria. Imeshawatokea wafanyabiashara fulani kuvunjiwa vibanda vyao kupisha ujenzi wa barabara. Ni hasara. Wakati mwingine wapangishaji wanataka ulipe kodi ya miezi sita hata mwaka mmoja, wakati mtaji wako ni mdogo.

Vilevile, kama unafanya biashara ambayo inahitaji umeme au maji kwa uendeshaji wake, ukiwa katika eneo mbali na huduma hizi utashindwa kutoa huduma zako au utaingia gharama kubwa sana kupata huduma hizi.

Nne, ushindani katika bei za bidhaa. Kwa kawaida bei hupangwa kwa kuzingatia gharama zilizotumika hadi kuzalisha au kuifikisha bidhaa au huduma sokoni. Changamoto ni pale unapolazimika kuuza kwa bei ya chini kutokana na washindani wako kushusha bei kwa lengo la kukuondoa sokoni, au wao wamenunua kwa gharama za chini zaidi.

Tano, wagavi kupandisha bei ya bidhaa. Hapa unajikuta unashindwa kupanga bei ambayo itafidia gharama za ununuzi au uzalishaji wa bidhaa zako. Wakati wateja wamezoea kupata bidhaa kwa bei fulani, ukiongeza bei kidogo tu, bidhaa hainunuliwi kwa spidi ya mwanzo.

Sita, kushindwa kupanga bei stahiki ya bidhaa au huduma. Uzoefu mdogo wa soko, na washindani wako, unaweza kusababisha mjasiriamali kushindwa kupanga bei stahiki, akaishia kupanga bei ndogo au kubwa na kuishia kupata hasara au kufukuza wateja.

Saba, wagavi kuchelewa kuleta au kutoleta kabisa bidhaa ulizoagiza, wakati tayari umeshawapa matarajio wateja wako, na wanangojea bidhaa yako; au wagavi kuleta bidhaa isiyo sahihi, (size, model, uzito, ujazo, aina, au iliyokwisha muda wake, n.k). Hapa una hatari ya kupoteza wateja wako.

Nane, kufurika ghafla kwa bidhaa yako sokoni, mfano umenunua bidhaa kwa bei fulani, halafu ghafla washindani wako wakaleta bidhaa nyingi zaidi, soko likafurika na bei ikashuka, hasa kwa biashara ya mazao ya chakula ya msimu, kama nyanya, maembe na mbogamboga.

Tisa, matakwa ya sheria. Usipoyaelewa mapema na ukayafanya kwa wakati unaweza kuingia kwenye gharama ya penalty, au ukafikishwa mahakamani au kufungiwa biashara yako. Mfano kodi, tozo, returns, leseni, vibali n.k.

Kumi, upatikanaji wa taabu wa malighafi. Mjasiriamali anayezalisha bidhaa kutokana na malighafi fulani, mfano ufyatuaji wa tofali. Wakati fulani kunakuwa na uhaba wa kokoto, mchanga, hata sementi hivyo kuzorotesha uzalishaji na kusababisha usumbufu kwa wateja wako.

Kumi na moja, uwezo wa kuwavuta na kuwabakisha wateja. Hii ni changamoto ambayo usipohakikisha ubora wa bidhaa au huduma zako, kuwafanya wateja wapate wanachokitaka kwa wakati na ubora, hawataridhika, na unaweza ‘kuwafukuza’ wote.

Kumi na mbili, majanga ya asili, ujambazi/wizi n.k. Haya hutokea pasipo kutarajiwa. Kwa mfano mvua kubwa, au mafuriko. Majanga kama mafuriko husababisha usafiri kuwa mgumu na hivyo kusababisha kushindwa kufuata bidhaa sokoni, au wateja kushindwa kuja kununua. Mafuriko pia yanaweza kusomba au kuozesha bidhaa zikawa haziwezi kuuzika, na hasara yake ikawa kubwa.

Kwa hiyo basi, baada ya kuzijua unachopaswa kufanya ni maandalizi. Yaani tayari unazijua changamoto zilizo mbele yako, kulingana na aina ya biashara unayotaka kufanya, ni lazima sasa uweze kukabiliana na changamoto hizo kwa kujiandaa. Angalia uwezo ulionao, na rasilimali pia, kisha weka plani itakayokufanya uzishinde changamoto hizo mapema.

Kwa kufanya hivi utajikuta unaanza kuendesha shughuli au biashara yako bila presha wala gharama zisizokuwa na msingi, na utakuwa na uhakika wa kuwavuta na kuwabakisha wateja wako. Usipozijua mapema na ukajiandaa, zitakapojitokeza zitakuwa zimekushtukiza, kama ajali, ukiwa huna kinga yoyote.

Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasirimali kivitendo.

Anapatikana kwa simu: 0718219530; e-mail: nzyy2001@gmail.com

 

Je, Tunaweza Kujifunza Ubunifu Kupitia Historia Ya Zama Za Mawe?

Habari rafiki,

Karibu tena katika mfululizo wa makala zangu zenye lengo la kuelimishana kuhusu masuala ya ujasiriamali, ubunifu na stadi za maisha..

Nimeeleza katika makala zangu za nyuma kuwa ubunifu ni matokeo ya kuufikirisha ubongo ili kupata njia mpya na nzuri zaidi za kuleta mabadiliko, kutatua changamoto au kuondoa tatizo lililojitokeza. Nimeeleza pia kuwa ubunifu na ujasiriamali ni chanda na pete!

Vifaa hivi, pamoja na uduni wake ni matokeo ya ubunifu wa mwanadamu wa kale

Ubunifu wa binaadamu haukuanza leo, ulianza toka enzi za mababu zetu hapo mwanzo wa historia ya mwanadamu.

Historia ya mwanadamu inatufundisha namna mwanaadamu alivyoanza na alivyoendelea kujinasua kutoka katika changamoto mbalimbali za kimaisha na kimazingira, kwa kufanya ubunifu na ugunduzi.

Kila alipokabiliwa na changamoto hakubweteka, aliinamisha kichwa chini, akaufikirisha ubongo wake na kujenga maono yaliyomletea taswira au picha, ndani ya akili yake, ya mchakato au vitu ambavyo alikuja kuviunda hatimaye; vikamtoa katika hali ya uduni aliyokuwa nayo, na kumweka katika hali bora zaidi ya maisha.

Changamoto ziliwasaidia kupata ‘macho’ yaliyowafanya kuona mawe, mifupa ya wanyama, udongo wa mfinyanzi, na miti kwa ‘jicho la udadisi’ lenye nia ya kuleta mabadiliko au utofauti fulani ulioleta matokeo bora zaidi katika kupambana na changamoto hizo.

Kila kitu walichokiona walikifanyia udadisi kisha wakavuta picha au taswira, akilini, kujua ni jinsi gani kitu au kifaa hicho kinaweza kutumika kutatua changamoto au matatizo yao.

Udadisi ulichangamsha bongo zao na kuzifanya zifikiri kwa kina ili kutoa majawabu, na kisha mikono ilichukua jukumu lake; kuanza kufinyanga, kuchonga, kutoboa, kuunganisha, kushona n.k. ili kupata vitu halisi.

Kwa hiyo, sio udadisi tu waliokuwa nao, bali pi uthubutu na hamasa ya kubadili taswira walizojenga vichwani mwao kuwa vitendo au vitu halisi. Kumbuka nimeandika katika makala hii, bofya, kuwa, ‘wazo zuri litabaki kuwa zuri tu kichwani kama halitatiwa katika vitendo au utekelezaji.’

Nimeandika pia huko nyuma kuwa ubunifu, hasa katika muktadha wa karne ya 21, unahusisha utengenezaji wa bidhaa, utoaji wa huduma au uboreshaji wa michakato ya uzalishaji na utoaji huduma – kwa utaratibu mpya, wenye lengo la kuongeza thamani ya bidhaa, huduma au michakato mbalimbali. Hapa, ongezeko la thamani linalenga hasa kuvutia wateja zaidi na kuongeza mauzo.

Hata hivyo, historia ya ubunifu wa mwanaadamu inatupeleka hadi zama za mawe ambapo tunaoneshwa historia ndefu ya maendeleo ya teknolojia. Tunaambiwa kuwa binaadamu walianza kubuni vifaa duni; lakini waliendelea kudadisi na kujifunza zaidi kwa lengo la kuboresha juhudi zao za ubunifu na ugunduzi wa vifaa mbalimbali, kwa ajili ya matumizi yao. Nitaielezea kifupi historia hii.

Historia ya ubunifu na ugunduzi enzi hizo imegawanyika katika hatua au ‘zama’ kadhaa kama ifuatavyo:

Moja, zama za kale za mawe. Tunaambiwa kuwa hizi zilikuwa zama za uwindaji na ukusanyaji wa vitu, hasa vyakula, ambapo mwanadamu alitumia zana za mawe ambazo zilikuwa ghafi; yaani mawe yalitumiwa kama yalivyo kwa ajili ya kuulia wanyama, kukatia matawi ya miti, kuchunia ngozi za wanyama, na kuchimbia vyakula vya mizizi.

Ubunifu wa mwanaadamu hapa ni yale maarifa ya kutumia vifaa hivyo duni kupata matokeo fulani yenye tija zaidi, badala ya kutumia mikono mitupu, miguu au meno. Katika zama hizi binaadamu walikula vyakula visivyopikwa, au vibichi, kwani hakukuwa na moto.

Mbili, zama za kati za mawe. Hapa, binaadamu aliishi kwa kuwinda na kukusanya pia. Lakini alianza kufikiri zaidi na kufanya ubunifu. Aliweza kufikiri na kugundua kuwa anaweza kuyafanyia ukarabati mawe yakawa na umbo fulani tofauti kwa lengo maalumu la matumizi.

Hivyo, ubunifu huo ulisababisha kupatikana vifaa kama visu, sindano, mikuki na hata pinde. Vifaa hivi vilirahisisha ukataji wa nyama, uchongaji wa miti na uchunaji wa ngozi za wanyama.

Ni katika zama hizi pia ambapo moto uligunduliwa na kumfanya binaaadamu aanze kula chakula kilichopikwa au kuchomwa, aishi maeneo ya baridi bila matatizo, aongeze muda wa kufanya kazi hadi usiku, na aweze pia kusafisha maeneo yake, kwa moto, kwa ajili ya shughuli zake mbalimbali.

Kwa hiyo, katika kipindi hiki, mbali na ubunifu wa kutengeneza vifaa mbalimbali kutokana na mawe; mfano mikuki, visu n.k., lakini vilevile watu hawa walifikiri tena na kugundua kwamba ili vifaa hivi vifanye kazi kwa ufanisi zaidi, waongeze ubunifu kwa kuvifanya viwe: rahisi kubeba (vidogo); rahisi kuua, kuchuna, kukata nyama na miti (vikali); na rahisi kutumia (vyepesi).

Tatu, zama za mwisho za mawe. Hapa binaadamu aliweza kubuni na kutengeneza vifaa bora zaidi. Hapa ubunifu wake ulikuwa wa juu zaidi ambapo aliweza kubuni na kuchonga vifaa vidogo kwa umbo, vyepesi kubeba, vikali zaidi, na vyenye maumbo tofauti kwa kazi mbalimbali.

Hivi ni vifaa kama mashoka, mikuki myepesi na mikali, na visu vikali na vyepesi zaidi n.k., vyote vya mawe. Lakini pia, hamu ya kupata vifaa bora zaidi ilipelekea waende mbele zaidi ki-ubunifu kwa kuanza kuvichonga vifaa vya mawe na kuviunganisha kwenye vifaa vya miti, kupata vifaa vyenye tija zaidi. Na huu ndio ukawa mwanzo wa ugunduzi wa kilimo, kwani vifaa hivi vilitumika kwa kuparua ardhi na kupanda mbegu ili kupata mazao.

Nne, zama za Chuma. Hapa binaadamu aliufikirisha ubongo wake zaidi, akaja na mbinu za ziada za ubunifu na ugunduzi. Aliweza kupata ujuzi wa kufua vyuma, kwa msaada wa moto, ambapo alifua vitu kama mashoka, majembe, mikuki, sululu, mapanga n.k., vyote vya chuma. Vifaa hivi viliwaongezea tija na uwezo katika uzalishaji, kwa kuongeza uwezo wa kuzalisha chakula kingi zaidi kwa matumizi yao.

Cha kujifunza hapa ni kwamba ubunifu ni kichocheo kikubwa cha maendeleo ya binaadamu. Ubunifu uliofanyika enzi hizo za nyuma ulilenga kupata vifaa bora zaidi ili kurahisisha maisha na kupambana na changamoto zilizowakabili. Walifanikiwa kwa kiwango cha kutosha.

Kwa hiyo, sisi, hasa wajasiriamali wa kileo tunapaswa kujua historia ya ubunifu na kujifunza. Tunapaswa kujua jitihada zilizofanywa na mababu zetu enzi hizo ambazo hakukuwa na taasisi maalumu za kielimu.

Kwa vile wazee wetu walifanya ubunifu kupambana na changamoto zao, na wakafanikiwa; sisi tunapaswa kufanya jitihada kubwa zaidi katika ubunifu ili tuweze kushindana ki-uhakika katika soko lenye ushindani mkubwa – na kukidhi haja za wateja wenye mahitaji, matamanio na uelewa mkubwa zaidi wa bidhaa na huduma wanazozitaka.

Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasirimali kivitendo.

Anapatikana kwa simu: 0718219530; e-mail: nzyy2001@gmail.com

Ubunifu Katika Mapenzi – Je, Wajasiriamali Tuna Cha Kujifunza Kwenye Hili?

Rafiki mpendwa,

Karibu tena katika mfululizo wa makala zangu zenye lengo la kuelimishana kuhusu masuala ya ujasiriamali, ubunifu na stadi za maisha.

Nikiwa napitia makala mbalimbali katika gazeti moja la michezo nilikutana na makala moja iliyonivutia. Makala hii naweza kusema inahusu ‘mbinu za mchezo wa ndoa’. Hata hivyo, kichwa cha habari cha makala hiyo kilikuwa, ‘njia za ubunifu za kuyafanya mahusiano yako yasichoshe’.

Ubunifu katika mahusiano ya ki-mapenzi ni chachu ya kudumisha mapenzi yenu

Nilivutiwa na waudhui ya makala hiyo kwa kuwa yalisisitiza umuhimu wa watu kuwa wabunifu na kwamba wasiridhike kufanya vitu au mambo kwa mtindo uleule, kila siku. Mwandishi wa makala hiyo, nadhani amebobea katika utaalamu wa ‘mahaba’, lakini pia anajua umuhimu wa suala zima la ubunifu katika maisha ya binaadamu.

Maudhui ya makala ile yanatoa mafunzo mengi, sio tu kwa wanandoa – ili wadumishe ndoa zao na kujenga upendo endelevu, bali pia yanatoa mafunzo mengi kwa wajasiriamali.

Alianza kwa kuandika, “ili mahusiano ya ndoa yawe bora na yalete msisimko, ubunifu ni kitu muhimu sana. Bila kuwa mbunifu, makini na mwenye kujua jambo gani lifanyike, ulifanye vipi, na kwa wakati gani, basi mahusiano yako hayataweza kukupa kitu bora unachotamani kukipata.”

Aliongeza kwa kusema, “ili mwenzio asikuchoke katika mahusiano inabidi ujue kucheza na akili yake.” Hata hivyo, tathmini zinaonesha kuwa watu wengi walio katika mahusiano kwa zaidi ya miaka mitatu wanakabiliwa na tatizo la kuchokana.

Hili linachangiwa na wapenzi husika kutokuwa wajanja na wabunifu. Yaani, mambo yale ya jana na juzi wanataka wayafanye leo na kila siku, na matokeo yake ni kwamba mahusiano yao yanapoteza ladha na ule msisismko uliokuwepo zamani.

Mwandishi anasisitiza kuwa hata kama matendo yako ni mazuri kwa kiwango gani lakini kama unayafanya mambo kila siku kwa mtindo ule ule yatachosha tu. Akitoa mfano wa chakula unachokipenda sana anasema, “japo kinakupa msisimko kinywani mwako na utamu katika ulimi wako, lakini kama utakula kila siku kwa mtindo huohuo mmoja wa mapishi kitapoteza ile thamani iliyopo katika fikra zako.”

Kwa maelezo hayo, Wajasiriamali hapa tunapata mafunzo makubwa. Kupitia mfano huu utaona umuhimu wa kufikiri kwa kina tena mfululizo, ili kila siku uje na vitu vipya au ufanye vitu vilivyopo kwa mtindo tofauti. Hii itasaidia kuongeza thamani ya vitu hivyo katika hisia na mitazamo ya wateja wako.

Mwandishi hakuishia hapo, anasisitiza, “tambua mahusiano ya raha yanatakiwa yajengwe katika msingi wa ubunifu na ujanja. Kama huwezi kumfanya mwenzio ajihisi ana amani na raha kila siku, huwezi kuwa na udhibiti halisi juu yake – atakuwa na wewe ndani, mtalala kitanda kimoja, ndani ya shuka moja, ila ndani ya nafsi yake bado atakuwa anahangaika na kuweweseka juu ya nani ampe raha halisi. Hivyo ukitaka mahusiano yadumu, jifunze utundu, mfanyie mwenzio utundu fulani hivi, hadi apagawe.”

Hapa kuna mafunzo makubwa kwa wajasiriamali. Usione kwa kuwa watu wanaijua bidhaa au huduma yako na labda huja kuinunua, basi ukadhani wataifurahia bidhaa yako siku zote. La hasha! Huenda tayari wameshakinaishwa nayo, na labda tu hawajapata bidhaa mbadala mahala pengine. Sasa basi, ikitokea wakaipata, wataachana na bidhaa yako na huenda wasirudi tena.

Mwandishi anadai, “kupendana haitoshi, kulala pamoja haitoshi, kujifunika shuka moja haitoshi; nenda zaidi ya hapo umfanye mwenzio akuone kama kitabu kipya ama filamu mpya au safari ambayo hujawahi kusafiri. Mtilie utundu na chachandu!”

Lakini pia, tunaambiwa na wataalamu wa saikolojia kwamba kuna ushahidi kuwa wapenzi husalitiana huku wakiwa bado wanapendana, kisa? Kukosa ubunifu katika mahusiano!

Mjasiriamali pia una hatari kubwa ya ‘kusalitiwa’ na hata kukimbiwa na wateja wako kwa kuwa wateja mara zote wanapenda kupewa huduma au vitu vipya, vyenye radha na vionjo tofauti. Wanapenda ‘chachandu’. Wakigundua huna kipya – wewe kila siku mtindo wako ni uleule, bidhaa au huduma zako zina radha, rangi, au muundo ule ule kila siku, watachoka, watakinai, na mwisho ‘watasepa’!

Mwandishi anasema mapenzi ni sanaa, na daima hakuna sanaa bila ubunifu, utundu na ufundi. Kwa hiyo unapaswa kuwa mbunifu kwa kila jambo la kimapenzi ili mwenzio ajione yuko katika msitu wenye vitu vya kustaajabisha, kuvutia na kutia hamasa katika maisha yake.

Vivyo  hivyo kwa ujasiriamli, ambapo ujasiriamali ukifanywa kwa mtindo wa usanii – ubunifu hujitokeza; ambao utakufanya kila siku utengeneze fikra mpya kisha uje na vitu vipya, bidhaa au huduma, ili mteja wako ajione yuko katika msitu wa kustaajabisha na kutia hamasa kila siku.

Mteja huyu atajenga utii au ‘loyalty’ kwa bidhaa au biashara yako, na atahamasika kuwavuta wenzake kuzipenda na kuzinunua bidhaa au huduma zako, na mwisho wa yote ni kwamba biashara yako ‘itapaa’!

Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasirimali kivitendo.

Anapatikana kwa simu: 0718219530; e-mail: nzyy2001@gmail.com

Je, Unazijua Mbinu Za Kufanya Ubunifu Katika Ujasiriamali?

Habari rafiki.

Karibu tena katika mfululizo wa makala zangu zenye lengo la kuelimishana kuhusu masuala ya ujasiriamali, ubunifu na stadi za maisha.

Ukiufikirisha ubongo utakuja na ubunifu wa kipekee!

Nimeshaeleza kupitia makala hii  ya nyuma, kuwa ubunifu ni uwezo wa kufikiri, kutafuta majibu na kutatua changamoto kwa namna ya kipekee; na kwamba ubunifu ni matokeo ya kuufikirisha ubongo ili kupata njia mpya na nzuri zaidi za kutatua changamoto au tatizo lililojitokeza. Nimeeleza pia kuwa ubunifu una nafasi kubwa katika ujasiriamali.

Ubunifu sio kitu rahisi ‘ki-vile’; yaani kila wakati uibuke na bidhaa mpya yenye utofauti, au huduma mpya, au mchakato mpya wa uzalishaji au utoaji huduma. Sio kitu kidogo; hata hivyo siyo kitu kigumu! Panahitajika maarifa na mbinu tu. Yaani ujue mbinu ipi itakupatia mawazo mapya na ya maana ya kibunifu kuweza kukuletea tija katika biashara au shughuli yako.

Zifuatazo ni baadhi ya mbinu ambazo ukizitumia zitakusaidia kuongeza uwezo wako wa ubunifu:

Kwanza, Kukopi au kuiga mawazo ya wengine. Hii ni njia rahisi kabisa ya ubunifu. Hapa ni kwamba unaiga kitu ambacho wengine walishakifanya hapo kabla. Kuiga huku haina maana ya kukopi na ku-paste, hapana! Hapa ninamaanisha kwamba unachunguza kitu kizuri kilichofanyika mahala fulani, halafu unakiboresha kidogo, kisha unakizalisha na kukitumia kwako. Kuiga huku tunaita ‘kuiga kimkakati’, ambayo ni mbinu nzuri ya kufanya ubunifu.

Kwa mfano, Henry Ford, mwanzilishi wa Kampuni ya magari ya Ford, alitembelea kiwanda kimoja cha kusindika nyama, Marekani, akaona mtiririko wa utendaji kazi  na mpangilio wa mashine na wafanyakazi katika mnyororo mmoja, mtindo unaoitwa ‘assembly line production system’. Akavutiwa na ubora, uharaka, na unafuu wa gharama za uzalishaji kwa kutumia mtindo huu.

Aliporudi kwake, akatumia maarifa hayo kwenye kiwanda chake cha magari, kisha akaongeza ujuzi wake kidogo; akafanikiwa kupunguza muda na gharama kwa kiwango kikubwa. Huu ni ubunifu wenye tija unaotokana na kuiga.

Pili, kuuliza na kusikiliza wateja wako. Ukiweka utaratibu wa kuwauliza wateja wako kwamba wangependa bidhaa au huduma zako ziweje, utapata mawazo mengi sana, ambayo ukiyachuja, unaweza kuyatumia kuboresha bidhaa au huduma zako.

Kwa mfano, unaweza kuwauliza wateja, au wao wanaweza kuuliza au kutaka vitu, urembo au madoido fulani yawepo katika bidhaa yako. Au wakataka uweke vitu fulani vitakavyoifanya bidhaa yako iwe rahisi kutumia, au yenye mvuto zaidi; kwa mfano, mpangilio wa rangi, harufu au ulaini wa kitambaa au bidhaa husika.

Hapa unatakiwa usikilize maoni yao kwa umakini uone ni maoni yapi ukiyafanyia kazi unaweza kuongeza ubora wa bidhaa yako na ukaongeza mauzo zaidi.

Tatu, wachunguze wateja wako. Usiishie tu kuwauliza, wachunguze pia! Angalia wanatumiaje bidhaa zako, au ni vitu gani wanavibadilisha wakishanunua bidhaa yako. Fanyia kazi majibu ya uchunguzi wako.

Hivi ndivyo mmiliki wa Kampuni ya nguo ya Marekani, Levi Strauss, alivyofanya baada ya wateja wake wa Jeans kuwa wanazichana Jeans zao sehemu fulanifulani. Alipoona hilo, haraka sana akaanza kutengeneza Jeans zilizochanywa, na mauzo yake yakapaa!

Nne, fuatilia malalamiko na changamoto za wateja. Sio wateja wote wanalalamikia bidhaa au huduma unazowapatia. Hivyo ukipata wanaolalamika usiwachukie, shukuru, na wasikilize kwa makini. Sikiliza, pia fumbua macho, uone matatizo au changamoto wanazolalamikia. Hapa utapata pa kuanzia kufanya ubunifu, na ukiweza kufanikiwa kuondoa changamoto hizo utaongeza imani ya wateja wako, wataona jinsi unavyowajali, na mauzo yatapanda sana.

Tano, unganisha au changanya bidhaa. Kuchanganya bidhaa moja na nyingine ni mbinu ya kuja na bidhaa mpya na yenye matumizi bora zaidi. Kwa mfano, simu za mwanzo za mkononi hazikuwa na kamera wala radio.

Hivyo, wabunifu katika Makampuni ya simu waliwaza na kuona uwezekano wa kuzalisha bidhaa moja yenye nyongeza ya vitu hivyo, ndipo wakaunganisha vitu hivyo na kuja na simu yenye kamera na radio. Na sasa vitu vingi zaidi vimeongezwa.

Ubunifu mwingine ni wa kuunganisha redio, cassete player,  na mp3 au flash player; kupata bidhaa moja yenye upana zaidi wa matumizi. Uvumbuzi huu umewawezesha kuongeza thamani ya bidhaa hizo na  kuongeza mauzo pia.

Sita, punguza vitu kwenye bidhaa zako. Katika hili, jiulize, ni vitu gani ukiviondoa kwenye bidhaa, mchakato au njia za usambazaji wa bidhaa yako, itafanya bidhaa hiyo ipate ubora zaidi. Kwa mfano, Amazon waliamua kuondoa uuzaji wa vitabu kwa kutumia maduka halisi ya kuuza vitabu. Wakabakiza uuzaji vitabu kwa mtandao, online retailing.

Mfano mwingine ni uamuzi wa kuondoa mwamba wa mbele, au kiti cha kubebea mizigo, kwenye baiskeli. Kumbuka wasichana wengi, hasa warembo wa mjini, hawapendi baiskeli zenye mwamba au zenye kiti cha nyuma, wakitaka kuendesha baiskeli. Kwa kuviondoa hivi utajikuta unaongeza mauzo yako kwa kiwango cha juu.

Saba, angalia washindani wako. Waangalie kwa umakini washindani wako. Unaona wanafanya nini? Kipi kipya wanachokuja nacho? Una kitu cha kujifunza? Unaweza kuiga kimkakati? Unaweza kuboresha ukaja na kitu kipya na bora zaidi? Basi fanya hivyo.

Nane, geuza bidhaa za kizamani kuwa za kileo. Angalia huduma, mchakato au bidhaa iliyokuwa inatumika zamani, ambayo inaonekana imepitwa na wakati, kisha angalia jinsi unavyoweza kurudisha bidhaa, kitu au fasheni hiyo ya zamani, kwa kuifanyia mabadiliko fulani,  ikawa bidhaa ya kileo na itakayowapa vionjo vipya watumiaji wa kileo.

Kwa mfano, ‘Dungarees dress’ ni vazi lililokuwa likivaliwa shamba au katika magereji, lakini wabunifu wamelichukua, wakalifanyia ukarabati kidogo, wakalitangaza kupitia kwa wasichana warembo, na sasa linapendwa na linavaliwa na warembo kila mahala.

Kwa kumalizia, ubunifu ni chachu kubwa ya ujasiriamali na hivyo ili kuongeza tija katika bidhaa au huduma zako huna budi kuwa na maarifa na mbinu. Yaani ujue mbinu ipi itakupatia mawazo mapya na ya maana ya kibunifu kuweza kukufanya utengeneze bidhaa au utoe huduma bora zaidi itakayokuletea tija katika biashara au shughuli yako.

Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasirimali kivitendo.

Anapatikana kwa simu: 0718219530; e-mail: nzyy2001@gmail.com

Je, Nini Nafasi Ya Ubunifu Katika Kukuza Ujasiriamali?

Habari rafiki,

Makala ya leo itazungumzia nafasi ya ubunifu katika kuanzisha na kuboresha ujasiriamali. Kwanza nianze na maana ya ubunifu.

Ubunifu ni uwezo wa kufikiri, kutafuta majibu na kutatua changamoto kwa namna ya kipekee. Ubunifu ni matokeo ya kuufikirisha ubongo ili kupata njia mpya na nzuri zaidi za kutatua changamoto au tatizo lililojitokeza.

Tumeona katika makala zilizotangulia kuwa mawazo mbalimbali  hutungwa ndani ya ubongo wa mwanadamu. Ubongo unapofikirishwa kwa bidii huzaa mawazo mengi ambayo hayajapata uhalisia, yakiwemo mawazo ya kibunifu – kama kufungua biashara fulani au kuanzisha stadi fulani; mfano uchoraji, uchongaji au ushonaji.

Ubunifu wa utoaji huduma huongeza tija katika ujasiriamali

Ubunifu unahusisha utengenezaji wa bidhaa, utoaji wa huduma au uboreshaji wa michakato ya uzalishaji na utoaji huduma – kwa utaratibu mpya, wenye lengo la kuongeza thamani ya bidhaa, huduma au michakato mbalimbali. Ni uundaji na uingizaji katika soko, ama kwa matumizi ya kawaida au matumizi ya kibiashara wa bidhaa, huduma au mchakato mpya wa kuzalisha au kutoa huduma.

Ubunifu haumaanishi, kila wakati, uundaji wa kitu kipya kabisa, hapana! Ubunifu, wakati fulani, ni uwezo wa kuja na wazo, bidhaa, huduma au mchakato ambao unaingizwa kwenye taasisi au biashara kwa mara ya kwanza, bila kujali kwamba wazo au kitu hicho kimewahi kuwepo au kutumika katika taasisi au biashara nyingine.

Ubunifu una nafasi kubwa sana katika ujasiriamali. Nimesisitiza katika makala yangu iliyopita kwamba ujasiriamali na ubunifu ni kama chanda na pete. Hili linaweza kuthibitishwa kama ifuatavyo:

Kwanza, pale Mjasirimali anapokuja na wazo la kuunda au kuingiza bidhaa mpya katika soko lililopo, tayari huu ni ubunifu wa aina yake. Kwa mfano, Richard Branson, ameweza kubuni na kuunda roketi maalum, SpaceShipTwo, kupitia kampuni ya Virgin Galactic, ambacho ni chombo cha kwanza ambacho Bilionea huyo amesema kitaweza kusafirisha abiria kwenda kutalii katika anga za juu, mbali na dunia.

Pili, Mjasiriamali anafanya ubunifu wakati anaingiza njia au mbinu mpya za uzalishaji au utengenezaji wa bidhaa. Kwa mfano, Mc Donalds, mmiliki wa Kampuni ya utengenezaji na usindikaji wa vyakula, ya Marekani; inasemekana yeye ndiye mjasiriamali wa kwanza kuanzisha usindikaji wa chakula kiwandani kwa mfumo unaoweza kuitwa ‘mnyororo wa uzalishaji’, yaani ‘moving assembly line production system’.

Mfumo huu unatoa nafasi kwa mashine na wafanyakazi walio katika mnyororo huo, kila mmoja kufanya kazi moja tu maalum katika mnyororo mzima wa uzalishaji– kitu ambacho kinapunguza muda, kuongeza kasi, na kupunguza gharama za uzalishaji.

Hapa chakula kinatengenezwa kwa mtiririko maalum; yaani kuanzia malighafi, mfano ngano na malighafi nyingine, zinapoingizwa kiwandani hadi chakula kamili, mfano mkate au hamburger, kinapotoka kikiwa kimewekwa katika vifungashio tayari kuingia sokoni.

Tatu, Mjasiriamali anafanya ubunifu pale anapohamisha bidhaa au huduma zake ili ziuziwe katika soko jipya. Ina maana kuwa bidhaa zilezile alizonazo, anafanya utafiti na kugundua kundi jipya la watu, mahala fulani, ambako kuna ushindani mdogo; kisha anazipeleka bidhaa zake huko, ambako hatimaye zinapata wateja wengi wapya.

Kwa mfano, Kampuni ya uuzaji wa kinywaji cha kahawa, Starburcks Coffee, ya Marekani, ilifanikiwa kuingiza bidhaa yake nchini China, pamoja na kwamba Wachina walikuwa na kahawa yao walioithamini. Lakini pia Kampuni ya Australia, Red Bull, ilimudu kupenya soko la Marekani kiasi ambacho Wamarekani wengi wanadhani ni Kampuni ya Marekani.

Nne, Mjasiriamali anafanya ubunifu pale anapogundua uwepo wa chanzo kipya na cha gharama nafuu cha mali ghafi za uzalishaji.

Kwa mfano, Kampuni ya usafirishaji wa anga ya Canada, Air Canada, baada ya kuteswa na  gharama kubwa za mafuta, petroli,  na tozo za uchafuzi wa mazingira nchini humo, Kampuni hiyo iliamua kuanza kutumia mafuta mbadala, biofuel, yanayotokana na mimea, ambayo ni rahisi zaidi.

Tano, Mjasiriamali anafanya ubunifu pale anapogundua njia au mbinu mpya za usambazaji wa bidhaa au huduma zake. Kwa mfano, Mkurugenzi wa Open Kitchen Company, Bi Upendo Mwalongo.

Tunaambiwa, yeye alianzia uuzaji wa chakula ndani ya mgahawa wake, uliopo Sinza Mori, jijini Dar-es-salaam. Lakini baadaye aligundua uwepo wa mahitaji ya chakula chake mbali na mgahawani kwake, ndipo alifikiri kwa kina na kupata wazo la kibunifu, la kuuza chakula kupitia mitandao ya kijamii, hasa Instagram.

Kwa hiyo, ubunifu na uvumbuzi umefanya mageuzi makubwa kwa makampuni, viwanda na biashara mbalimbali duniani. Mfano mmoja ni jinsi ubunifu  ulivyoiinua Kampuni ya Apple kwa kuipandisha sokoni Ipod, na kuifanya Walkman ya Kampuni ya Sony ‘ipotelee mbali’. Ipod na Walkman ni vifaa vya kusikilizia muziki.

Hapa tunaweza kusema kwa uhakika kuwa Kampuni ya Apple ilijenga nguvu kubwa ya kuweza kuwashinda wapinzani wao wa kibiashara, Sony, kwa kupitia ubunifu, wakaweza kuja na ‘music system’ bora na ya kisasa zaidi.

Tukiangalia mifano hapo juu tunaona kwamba ubunifu una nafasi kubwa sana katika kuboresha au kukuza ujasiriamali. Tumeona jinsi biashara hizo zilivyofanya ubunifu wenye lengo la kujiongezea tija na kuushinda upinzani katika soko.

Funzo: Mjasiriamali, kila wakati unatakiwa uwe karibu na hisia za wateja wako, na hisia zako pia,  kuweza kubaini mahitaji ni yapi na changamoto gani zilizopo, halafu utumie uwezo wako wa kufikiri na kubuni, ili uje na bidhaa, mbinu au njia ambazo zitatatua changamoto hizo, na mwisho kukuongezea kipato zaidi.

Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasirimali kivitendo.

Anapatikana kwa simu: 0718219530; e-mail: nzyy2001@gmail.com

Je, Unaujua Uhusiano Kati Ya Ujasiriamali Na Ubunifu?

Karibu tena rafiki yangu katika mfululizo wa makala zangu za ujasiriamali, ubunifu na stadi za maisha.

Kama utakumbuka, katika makala hii, bofya, niliongelea ubunifu kama moja ya sifa za Mjasiriamali. Nilimuongelea pia Mjasiriamali Bw. Richard Branson, kwamba ni muumini mzuri wa dhana ya ubunifu katika biashara na ndio maana ana mafanikio makubwa.

Makala ya leo inalenga kuzama ndani zaidi ili kuona uhusiano uliopo kati ya ujasiriamali na ubunifu. Naomba kwanza tujikumbushe kuhusu dhana ya Ujasiriamali.

Neno Ujasiriamali ni muungano wa maneno mawili ya Kiswahili. La kwanza ni ‘ujasiri’- likiwa na maana ya  uwezo wa kuthubutu kufanya kitu au shughuli fulani.  Neno la pili ni ‘amali’- likiwa na maana ya matendo au shughuli inayompatia mtu riziki au kipato.

Ujasiriamali ni mchakato ambapo mtu anatengeneza wazo, kisha anaandaa na kuratibu ubunifu, uboreshaji na uvumbuzi ili kujenga thamani ya kitu au bidhaa itakayompa faida au kutoa manufaa, kulingana na malengo aliyojiwekea. Ujasiriamali unajenga uthubutu na uwezo wa kibunifu wa kuyabadili matatizo au changamoto kuwa fursa, hasa katika jamii.

Ubunifu ni chachu ya mafanikio ya mjasiriamali

Ujasiriamali unahusika na utengenezaji wa ukwasi au uwezo wa mali kwa kuunda na kuuza bidhaa au huduma kupitia mbinu za kibunifu, kwa mfano kutengeneza bidhaa zenye ubora kwa uwingi sahihi, kupanga bei sahihi, au kubuni namna bora ya kuzitangaza na kuzisambaza bidhaa kwa wanunuzi ili kukidhi mahitaji ya soko lililogunduliwa.

Kwa hiyo, kwa ujumla ujasiriamali ni ile hali ya kuwa na ujasiri, uthubutu au mshawasha wa kutafuta na kupata riziki kwa kufanya shughuli fulani. Ni uwezo wa kutambua fursa za biashara haraka na kujenga uthubutu wa kuzitekeleza fursa hizo pindi zinapojitokeza; na uwezo wa kupambana na kuvishinda vikwazo vinavyoweza kuzuia utekelezaji wa fursa hizo.

Kwa kuwa ujasiriamali unafanywa na mjasiriamali, ni vizuri pia tumjue huyu mjasiriamali kwa muktadha wa ubunifu. Mtaalamu mmoja anasema Mjasiriamali mhimili wake mkuu ni ubunifu. Ubunifu unawezesha kuzalishwa kwa bidhaa mpya, kugunduliwa kwa njia mpya za uzalishaji na utoaji huduma, kutafutwa kwa masoko mapya na utumiaji mpya wa rasilimali zinazomzunguka mjasiriamali.

Mjasiriamali wa ukweli ni yule anayekuwa na uwezo wa kubuni, kwa kuwa ubunifu ni sehemu muhimu ya mchakato wa ujasirimali, na hakuna mafanikio ya maana katika ujasiriamali kama hakuna mchango wa ubunifu.

Mbunifu ni mtu mwenye uwezo wa kuangalia vitu, changamoto au matatizo kwa jicho la kidadisi, lenye nia ya kuleta mabadiliko au utofauti fulani utakaoleta matokeo bora zaidi.

Kwa mfano,  mjasiriamali mmoja, mama lishe, alikuwa anapika chakula kwa kutumia kuni. Baada ya muda akasikia wateja wake wakilalamikia chakula chake, wakidai kinanuka moshi. Alipochunguza akagundua ni kweli, na kwamba hii ni changamoto; na haraka sana akachemsha bongo na kugundua cha kufanya.

Kisha, haraka sana, akabadilisha na kuanza kupikia mkaa. Alipofuatilia akagundua hakuna tena ile harufu ya moshi na malalamiko yameisha. Huu ndio ubunifu wa kijasiriamali tunaouongelea hapa. Uwezo wa kupepesa macho na kuinua masikio na pua kupata taarifa, na kuzitumia taarifa hizo kutengeneza kitu tofauti,au kuondoa changamoto fulani.

Mfano mwingine wa ubunifu ni ule uliofanywa na Mjasiriamali mmoja baada ya changamoto alizokutana nazo; ambazo zilimfanya aongeze mbinu au njia ya ziada ya kuwafikia wateja wake, baada ya kugundua wanahitaji huduma yake.  Huyu ni Mkurugenzi wa Open Kitchen Company, Bi Upendo Mwalongo.

Tunaambiwa, yeye alianzia uuzaji wa chakula ndani ya mgahawa wake, uliopo Sinza Mori, Dar-es-salaam. Lakini alipohitaji kuwahudumia pia wateja wake wa mbali, waliomuhitaji pia, alifikiri kwa kina na kupata wazo la kibunifu, la kuuza chakula kupitia mitandao ya kijamii.

Lakini pia, yupo mbunifu Teddy Bernad ambaye ni Mjasiliamali wa viungo vya chakula hapa nchini. Tunaambiwa kuwa, kutokana na umahiri wa utengenezaji wa viungo hivyo, amepachikwa jina la Malkia wa viungo. Teddy ni msomi na anautumia usomi wake kufanya ujasiriamali wenye tija, unaobebwa na ubunifu.

Akizungumzia uwezo wake wa ubunifu Teddy anasema: “Nilikuwa na utundu tu wa kuchanganyachanganya viungo, na kitu kilichotokea kiliwavutia wateja wangu. Nilipogundua hilo ilinibidi nifanye jitihada kujifunza kwa kina darasani na mitandaoni masomo ya usindikaji chakula “.

Anaeleza kwamba utundu wake, ukichanganywa na ujuzi wa darasani, vimemuongezea sana uwezo wake wa ubunifu na kumfanya kuwa mjasiriamali wa uhakika.

Kwa mfano anasema,”watu wengi wamezoea kula chapati za kukanda tu na mafuta ki-kawaida, ila kuna chapati ambazo unaweza kupika ukachanganya mdalasini, hiriki, garam-masala, au kiungo kingine, zikawa na ubora wa hali ya juu.”

Kwa hiyo, kumbe utundu ukiboreshwa na ukatumiwa vizuri, hutia chachu uwezo wa mjasiriamali kufanya ubunifu wenye manufaa.

Mjasiriamali anatakiwa ajitahidi kuwa tofauti au kufanya mambo ki-utofauti ikilinganishwa na washindani wake. Kufanya ubunifu wa kweli ni kuwa na uwezo wa kutengeneza au kutoa huduma bora, ya kipekee, na kwa njia tofauti na washindani wako. Na hili linatakiwa kuwa zoezi endelevu linalolenga kuendelea kuboresha.

Tunaambiwa na wataalamu kuwa taasisi, au biashara yoyote itaanguka haraka sana kama haifanyi ubunifu. Ubunifu ni roho ya mafanikio ya mjasiriamali.

Kwa kumalizia, napenda kusisitiza kwamba ujasiriamali na ubunifu ni kama chanda na pete. Mjasiriamali anapaswa kuwa na maarifa na msukumo wa kufanya ubunifu utakaomsaidia kuitazama jamii; kisha kuzitazama bidhaa au huduma zake kwa jicho la kidadisi kwa lengo la kujenga mawazo au mbinu za kibunifu za kuboresha, na kutatua matatizo au changamoto zinazojitokeza.

Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasirimali ki-vitendo.

Anapatikana kwa simu: 0718219530; e-mail: nzyy2001@gmail.com