Je, Ni Salama Kuanzisha Biashara Nyingi Kwa Wakati Mmoja?

Rafiki mpendwa,

Karibu tena katika mfululizo wa makala zangu zenye lengo la kuelimishana kuhusu masuala ya ujasiriamali, ubunifu na stadi za maisha.

Makala ya leo inahusu mbinu za uendeshaji biashara. Kuna wakati nilimsikia mfanyabiashara mmoja akitoa ushauri kwa jamaa yake. Alimwambia: “Mfanyabiashara mzuri ni yule anayefanya biashara nyingi kwa wakati mmoja. Yaani, unatakiwa usitegemee biashara moja peke yake; unatakiwa uwe na vyanzo vingi vya mapato kwa wakati mmoja.”

Aliendelea kwa kusema: “Ukiwa na biashara nyingi, na unazifanya kwa pamoja, zinasaidiana kuingiza pesa, lakini pia zinakufanya usitetereke; kwani moja ikidorora, nyingine inakukomboa. Ukitegemea chanzo kimoja tu, ujuwe ukianguka ndiyo basi tena, umekwisha!”

Mjasiriamali ukiyasikia maneno haya harakaharaka, utaona ni maneno mazito. Ni ushauri uliojaa busara na nia njema kabisa, ukilenga kukuletea manufaa na kukuepusha na hatari katika biashara. Na wapo watu wengi tu wenye mtazamo huu; wasomi wa biashara, na fani nyingine, na wasio wasomi pia. Utasikia wakisema: “Usiweke mayai yote kwenye kapu moja, likianguka yote yanavunjika.”

Labda kuna ukweli katika mtazamo huu – lakini kuna tafiti zinazoonesha kuwa kuna tatizo mahala fulani.  Mwandishi mmoja anasema kwamba ni rahisi mtu kuanzisha biashara mpya kila baada ya muda fulani mfupi. Lakini swali la kujiuliza ni je, unapata mafanikio yaliyokusudiwa katika kila biashara? Mafanikio katika biashara ni pamoja na kumpatia mteja bidhaa au huduma bora; kuwapatia wadau mapato stahiki; kuwapatia wafanyakazi ujira bora; na kutengeneza faida ya kutosha.

Huwezi kuingia milango yote kwa mpigo; Chagua mmoja

Mtendaji Mkuu wa Kampuni ya Apple, Tim Cook aliwahi kusema: “Moja ya kanuni ambazo Steve Jobs alisisitiza  katika Kampuni hii ni umuhimu wa kuwa focused, yaani kujikita katika kufanya kile unachoweza kufanya vizuri sana.” Kumbuka, Marehemu Steve Jobs ni mwanzilishi mwenza, na baadaye Mtendaji Mkuu wa Apple.

Kwa mujibu wa Tim Cook, Steve Jobs alisisitiza hili kwa kusema, “Ni rahisi kuongeza biashara zaidi, lakini ni vigumu kubakia focused.” Maana ya kuwa focused, kwa mujibu wa Jobs, ni kusema ‘hapana’ kwa mawazo mia kadhaa yanayozunguka kila mara ndani ya akili yako; hata baada ya kuchagua kwa umakini wazo moja zuri uliloamua kulifanya ki-vitendo.

Tunaambiwa kwamba, Steve Jobs hakujishughulisha na wingi wa vitu anavyofanya, kwa mfano, umezalisha au umeuza vipande vingapi vya bidhaa, hapana! Yeye alijishughulisha zaidi na kufanya ‘kitu fulani kilicho bora’, hata kama ni kimoja tu.

Wafanyabiashara wengi wakubwa wamejikita katika jambo moja, wakijitahidi kulifanya jambo hilo kwa ubora zaidi kila siku. Angalia wafanyabiashara hawa wakubwa: Henry Ford alijikita kutengeneza magari; Pablo Picasso alijikita katika sanaa ya uchoraji na rangi; Bill Gates alijikita kwenye uzalishaji wa software; na Mark Zucherberg amejizatiti katika Facebook.

Kitu cha kuzingatia hapa ni kwamba, hawa wamefanikiwa kwa viwango hivyo kwa sababu walikuwa focused. Walikuwa na hamu, motisha  na mshawasha wa kupata kwanza hicho kimoja walichokuwa wanakipenda na kukimudu zaidi.

Tunaambiwa kuwa, wafanyabiashara wachache wakubwa unaowaona wanafanya biashara au wana Kampuni zaidi ya moja, mfano Mzee Reginald Mengi, Tanzania, hawakuanzisha biashara zote kwa pamoja. Walianza na moja, wakaipa uhai hadi ikaweza kusimama vizuri peke yake, ndipo ikaanzishwa nyingine.

Mfano mwingine ni Bw.Richard Branson. Tajiri huyu Mwingereza, kwa miaka kumi na tatu, aliifanya Kampuni ya Virgin ijishughulishe na muziki tu, Virgin Records, kabla ya kujitanua baadaye hadi kuanzisha Kampuni za usafirishaji na nyinginezo.

Ushauri unaotolewa hapa ni kwamba kufanya biashara nyingi kwa wakati mmoja inaweza kuonekana ni mbinu au ujanja wa kupunguza vihatarishi au risk ya kile kinachosemwa hapo juu kwamba, ‘Usiweke mayai yote kwenye kapu moja,…….’ Lakini upo ushahidi unaoonesha kuwa wafanyabiashara waliojaribu kufanya biashara nyingi kwa wakati mmoja, ama biashara zote zilidhoofika au zilikufa.

Tatizo kubwa katika hili ni kwamba mfanyabiashara anapoanza kufanya jambo moja na kabla hajaliwezesha kumpatia tija sahihi tayari amerukia jambo jingine – huyu anakosa maono na mwelekeo. Anakosa focus na hivyo anaanza kutangatanga asijuwe lipi alifanye, alifanye saa ngapi, na kwa kiwango gani.

Kikubwa zaidi ni kwamba rasilimali zinazohitajika kufanya haya zinaanza kugawanyika vipande vipande. Rasilimali hizo ni fedha, muda, akili, wafanyakazi, vifaa, majengo n.k.

Utakuta kila biashara mpya inayoanzishwa, kabla ya ile ya kwanza kukomaa, ina tabia ya kutaka kujitwalia rasilimali hizi na kujimilikisha yenyewe, na hivyo kuzinyima pumzi biashara zilizotangulia. Hapa, baada ya muda rasilimali zinakuwa kidogo kutosheleza mahitaji ya kila biashara, na hapo ndipo biashara zote zinakonda na kufa!

Mwandishi mmoja anasisitiza hili kwa kusema: “Angalia vitu kadhaa ambavyo vinamgusa mtu, au watu wanavipa umuhimu mkubwa, mfano mapenzi, kujali, umakini n.k. Jinsi unavyovitawanya vitu hivi kwa watu wengi zaidi ndivyo jinsi unavyofanya thamani yake ipungue.”

Kwa kumalizia, tunashauriwa kuwa focused, tusihangaike huku na kule wala kuondoa macho katika fursa iliyo wazi mbele yetu. Hivyo, jitahidi kuweka mkazo, macho, akili,  nguvu na rasilimali zote katika fursa moja yenye uhakika wa kukupatia faida kubwa mpaka uikamate vizuri na kuyaona bayana matokeo yaliyokusudiwa.

Baada ya kufanikisha biashara moja vizuri, basi hapo unaweza kuanzisha nyingine, ukiwa tayari umeshakusanya rasilimali mpya za kutosha kuanzisha na kuendesha biashara mpya kwa tija, bila kuiathiri biashara yako ya mwanzo.

Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasirimali kivitendo.

Anapatikana kwa simu: 0718219530; e-mail: nzyy2001@gmail.com

Jinsi Ya Kukabiliana Na Hisia Ya Kukata Tamaa

Rafiki,

Karibu tena katika makala nyingine inayolenga kukupatia maarifa ya ujasiriamali, ubunifu na stadi za maisha.

Nimewahi kumsikia mtu akisema, “yaani kujituma koote huku, jitihada zoote na nguvu nilizotumia kwenye kazi hii, sijaona mafanikio; ndio kwanza nazidi kupata hasara! Kwa kweli nimekata tamaa, na sidhani kama nitapoteza muda wangu tena katika jambo hili.”

Je, nini maana ya dhana ya kukata tamaa?

Kwa mujibu wa taaluma ya Saikolojia, kukata tamaa ni ile hali ya mtu kupoteza matumaini baada ya kushindwa kupata matokeo aliyotarajia; au kupata njia ambayo ingeweza kumfanya atatue au ajitoe katika matatizo, au apambane na changamoto.

Kukata tamaa kunasababisha kupotea kwa matumaini

Mtu akikosa matumaini au njia mbadala, akili hukosa mwelekeo. Yaani hapa, akili ya mtu inakosa uwezo wa kuona fursa ya kuendelea kusonga mbele katika kufikia mafanikio au utatuzi wa changamoto zilizo mbele yake.

Ki-ukweli, kukata tamaa ni jambo la kawaida, na karibia kila binaadamu hukata tamaa kwa namna moja au nyingine. Hata hivyo, wapo watu ambao wanaathirika sana na hali hii hadi wanapoteza hata hamu ya kuishi; lakini wapo vilevile watu wastahimilivu, ambao hujitahidi kupambana na kuishinda hali hii.

Kwa hiyo, hata katika ujasiriamali kuna watu ambao wakipatwa na misukosuko hukata tamaa na ‘kuweka silaha chini’. Hii si sawa!

Kwa mujibu wa mwandishi mmoja, kuna namna mbili za kukata tamaa.

Namna ya kwanza ni kukata tamaa kunakotokana na woga wa kuthubutu, ambapo mtu hukata tamaa kuanza kufanya jambo alilokusudia kulifanya, hata kabla hajalianza. Yaani akifikiria kuanza tu, anapatwa na kigugumizi, hofu na woga. Analokusudia kulifanya, hata kama mwanzoni aliona linawezekana, ghafla analiona gumu kama jabali lisiloweza kuvunjika; na yeye anajiona laini kama sponji.

Namna ya pili ya kukata tamaa ni kupoteza kujiamini, au kufa moyo, wakati wa kulitia wazo au jambo katika vitendo. Yaani mtu amekwisha anza utekelezaji wa ndoto au fursa ambayo kaiona na kujiridhisha kuwa itampatia mafanikio. Katika utekelezaji, kunatokea vikwazo au changamoto; sawa na mtu aliyeanza safari ya msituni, halafu njiani akakutana na mnyama mkali, akapatwa na woga na kuamua kukatisha safari, na kurudi alikotoka.

Mwanafalsafa mmoja anasema kuwa mwanadamu ni mwili, nafsi na roho. Nafsi na roho zinapokosa nguvu, binaadamu anakuwa na uwezo mdogo wa kufanya mambo au kukabili changamoto, hivyo kumfanya awe rahisi kukata tamaa. Nafsi na roho zinapokuwa na nguvu, mtu huyu anajenga ujasiri na uwezo mkubwa wa kutenda na kukabili changamoto.

Anasema kwamba, roho chakula chake ni imani, na kwamba kila binaadamu ana imani fulani. Anasema pia kwamba, nafsi chakula chake ni maarifa.

Anadai kwamba, kuwa na imani ni kujenga uhakika wa uwepo wa kitu ambacho kwa wakati huo hakionekani, ni cha kufikirika tu, ambacho kinakupa uwezo wa kufanya mambo fulani. Na maarifa ni ujanja wa kuzitumia kanuni au taarifa mbalimbali kupata kitu unachokitaka; hivyo mtu mwenye imani na maarifa anapata uwezo mkubwa wa kutokukata tamaaa.

 Kwa mujibu wa mtaalamu wa Saikolojia, kukata tamaa kunasababishwa na vitu vifuatavyo:

  • Kukosa maono. Mtu akikosa maono au mtazamo chanya, anakosa mwelekeo. Ukikosa mwelekeo unapatwa na hali ya kujiona huna uwezo, hii inasababisha upoteze uwezo wa kujiamini, na ukipoteza kujiamini unatengeneza mchafuko wa akili, inayokufanya uogope kusonga mbele.
  • Kuzungukwa na watu wasio sahihi. Hawa ni watu waoga tayari, na hivyo wanakufanya kuwa na hofu; na jinsi unavyozidi kukaa karibu na watu hawa unazidi kupatwa na hali hii na kushindwa kuchukua hatua.
  • Kukosa matumaini. Matumaini yakikosekana huwa yanaondoa motisha, na motisha ikiondoka, ujasiri na uwezo wa kujiamini vinaondoka.
  • Vikwazo au changamoto ambazo mtu anakutana navyo kabla au wakati wa kutekeleza ndoto yake. Kwa mfano, kama sheria au kanuni za kufanya biashara fulani ni ngumu kutekelezeka au zina urasimu mwingi, ikiwa ni pamoja na rushwa; vitu ambavyo vinavunja moyo.
  • Kuathirika kisaikolojia kunakomfanya mtu kujiona hana uwezo au ana uwezo mdogo wa kupambana. Hapa, mtu anajiona dhaifu na kwamba hata akijitahidi hawezi kufanya lolote, anaishia kukata tamaaa.
  • Udhaifu au uzembe wa mtu katika kuwashirikisha wenzake yale yanayomsibu na kumkatisha tamaa, ili atiwe moyo au apewe njia mbadala.

Je, maendeleo yanaweza kupatikana kwa mtu aliyekata tamaa? Si rahisi sana, kwa sababu mtu huyu anakuwa amepoteza matumaini na amekosa uwezo wa kufanya mambo au kutatua changamoto, hivyo anabakiza malalamiko na manung’uniko tu.

Mtu aliyekata tamaa anakosa ule msukumo wa ndani, au motisha ya kufanya mambo inakuwa haipo. Yaani anajiona hawezi na anajenga woga wa kuthubutu kuanza au kutekeleza shughuli fulani. Anaghubikwa na kulalamika kusikoisha. Kulalamika ni dalili ya mtazamo hasi, na hili huongeza hali ya kukata tamaa.

Je, nini siri ya kuepuka kukata tamaa? Mtaalamu wa Saikolojia anasema yafuatayo:

  • Weka dhamira yako, akili yako, nguvu zako na muda wako katika hilo ulilokusudia kulitimiza.
  • Jenga ujasiri. Siri ya kufaulu ni uwezo wa kivishinda vikwazo, na kuzidhoofisha nguvu za changamoto.
  • Usitarajie mafanikio yatakuja bila ujasiri na juhudi za kupambana. Usibweteke ukadhani mambo yatajileta yenyewe. Ili kufikia faraja unayoiona katika ndoto zako ni lazima upambane na pepo la kukatisha tamaa.
  • Mtafutaji kukumbana na vikwazo, changamoto na mikwamo ni kawaida; hivyo, ni roho ya uvumilivu, ujasiri na hamasa ndiyo itakayokuletea mafanikio.
  • Ukiona shida, mikwamo au changamoto zinazidi ujue hapo mafanikio yapo jirani; hivyo hapo, akili yako inapaswa ijitanue zaidi kupambana na kutafuta namna bora zaidi ya kutekeleza yaliyokusudiwa. Mwisho wa yote ni mafaniio.

Kwa kumalizia, kama wewe ni mjasiriamali au unakusudia kuanzisha shughuli yako ya kijasiriamali unatakiwa uwe na ujasiri. Unatakiwa utie nguvu, maarifa na imani katika kila ukifanyacho. Kukata tamaa ni tabia isiyofaa, na inapaswa kuepukwa kwa gharama yoyote.

Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasirimali kivitendo.

Anapatikana kwa simu: 0718219530; e-mail: nzyy2001@gmail.com

 

Jinsi Ya Kukabiliana Na Hofu Ya Kufeli Katika Biashara

Mtaalamu wa Saikolojia, Dr. Chris Mauki, amewahi kuandika kuhusu dhana ya hofu au mashaka. Akitoa ufafanuzi alisema na kusisistiza kuwa, “hofu au woga, ndio adui namba moja anayedhoofisha  nishati ya mwili wa mwanadamu kwa haraka pengine kuliko kitu kingine; na kwamba wengi wameshindwa kufikia malengo na ndoto zao katika maisha kwa sababu ya hofu, mashaka na woga.”

Hofu ni tatizo la kisaikolojia linalotibika

Hofu ni hulka ambayo humpata kila binaadamu, ingawaje kwa viwango vinavyotofautiana. Kwa mujibu wa historia, hata makamanda wa vita, walioogopwa sana, walikabiliwa na hofu! Waliogopa kushindwa vita, kuchukuliwa mateka au hata kuuawa. Lakini, tofauti ya hawa na wengine, ni ujasiri na hamasa ya kushinda waliyoijenga ndani yao kila siku.

Hata hivyo, wapo watu wengine ambao wameelemewa na tabia ya hofu kwa kiwango cha juu sana, kitu ambacho kinawaathiri, na kuwafanya washindwe kufuatilia hata mambo muhimu ya maisha yao.

Tunaambiwa na wataalamu kuwa, kama ulivyo wasiwasi na woga, hofu ni athari ya kisaikolojia ambayo hutokana na hisia au mawazo hasi. Ndio maana Mwandishi John F. Paul anatuhimiza tusitawaliwe na mawazo hasi. Anasema: “Akili zetu hazikuumbwa ili kukaa na hasi, kwani unapokuwa mtu wa kuwaza au kusema hasi, kumbukumbu hizo zinasafirishwa na  kuhifadhiwa katika akili (ubongo) ya ndani, na baadaye kudhihirika au kutokea kiuhalisia.”

Nimeeleza katika makala hii,bofya, kuwa kinachowakabili watu wengi, wakashindwa kuanza kufanya biashara ki-vitendo, ni hofu au woga wa kufeli, lakini vilevile wapo wanaoogopa vitu visivyojulikana.

Watu hawa badala ya kufikiria ni kwa namna gani watakabiliana na changamoto zinazoweza kujitokeza, wao wanajenga hofu ya kushindwa na wanaanza kuwaza madhara yatakayowapata watakaposhindwa.

Je, nini kifanyike kutatua tatizo la hofu ya kushindwa – linalowakabili wajasiriamali?

Hakuna mtu aliyezaliwa akiwa tayari ana ujasiri, yaani hana hofu wala woga. Hakuna! Ndio maana mtoto mchanga, kila anapoamka na kugundua mama yake hayupo karibu naye huanza kupiga kelele, akionesha dalili za woga au wasiwasi. Anapata hofu ya kupata madhara, akiamini kuwa bila mama yake, usalama wake ni mdogo.

Kama hofu ni athari ya kisaikolojia ambayo hutokana na hisia au mawazo hasi, basi mtu mwoga atakuwa amepata tiba ya kwanza ya hofu iwapo atabadili au atasaidiwa kubadili tabia; kutoka ile ya kujenga hisia hasi, zinazoleta hofu na mashaka, hadi tabia ya kujenga hisia chanya zinazotia ujasiri.

Tunaambiwa na Wanafalsafa, kuwa ukiwa mtu wa kuwaza chanya utakusanya kumbukumbu nyingi za mawazo chanya, ya kuweza kufanya, au kutatua changamoto, hata ambazo hazijawahi kutokea, na mara nyingi utafanikisha mambo.

Watu hujenga tabia hizi kupitia mazoea ambayo hujengwa kidogokidogo katika maisha yao. Kinachowafanya watu jasiri na shupavu kuonekana hawana woga au hofu ni mbinu ya kutumia dhana ya kitendo. Yaani kwa kila tishio au changamoto inayowakabili, wao hujiuliza, “je, naweza kufanya kitendo gani ili kushinda woga au hofu inayonikabili?

Tunaambiwa na wataalamu kuwa, kwa kila woga au hofu inayompata binaadamu, huwa kuna kitendo anachoweza kufanya kuondoa au kupunguza hofu hiyo. Kwa mfano, mwanafunzi mwenye hofu ya kufanya mtihani wake kwa kuogopa kufeli, anaweza kuondokana na hofu hii kwa kujisomea kwa bidii na kufanya mazoezi mengi zaidi. Hiki ni kitendo cha kuondoa hofu. Kwa kadri  mtu anavyochelewa kufanya kitendo husika ndivyo ambavyo hofu inavyozidi kuongezeka.

Tiba ya pili ya hofu ni ile ya kujibidisha kujenga imani ya uwepo, nyuma yetu,  wa nguvu ya muumba wetu. Mungu mwenyewe, moja kwa moja, kupitia neno lake, ametupa hamasa na nguvu ya kushinda. Kwa hamasa hii hakuna sababu ya mjasiriamali kujenga hofu ya kuthubutu kufanya jambo ili kutimiza ndoto yake.

Kwa mfano, neno la Mungu, kupitia Isaya 41:10, Mungu anatuhamasisha kwa kusema: “Usiogope, kwa maana mimi ni pamoja nawe; usifadhaike, kwa maana mimi ni Mungu wako, nitakutia nguvu, maana nitakusaidia, naam nitakushika kwa mkono wa kuume wa haki yangu….”

Kwa kumalizia, napenda kuwahamasisha wajasiriamali kuwa kuendekeza hofu ni halili za mtu anayewaza hasi, na tumehimizwa hapa kujenga tabia ya kuwaza chanya. Tumesisitizwa pia kuwa ili tukabiliane na hofu tusichelewe kufanya kitendo husika, cha kuondoa hofu; lakini pia tuifanyie kazi hamasa tuliyopewa na Mungu, inayolenga kututia nguvu, ujasiri na uthubutu wa kuanza kufanya yaliyo katika ndoto zetu.

Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasirimali kivitendo.

Anapatikana kwa e-mail: nzyy2001@gmail.com; Mob: 0718219530

Je, Mikakati Ya Biashara Ni Nini? Tujifunze Kupitia Soka

Rafiki mpendwa,

Karibu tena katika mfululizo wa makala zangu zenye lengo la kuelimishana kuhusu masuala ya ujasiriamali, ubunifu na stadi za maisha.

Makala iliyopita nilizungumzia upangaji wa malengo ya biashara na umuhimu wake. Sasa, kinachofuata katika mchakato wa utekelezaji wa malengo ni kupanga mikakati ya utekelezaji.

Mikakati ya uhakika ni chachu ya ushindi katika vita..

Mikakati ni njia mbalimbali zinazopangwa kiweledi zinazoweza kutumiwa na mjasiriamali katika kufikia malengo aliyojipangia. Mikakati iliyo bora ina nafasi kubwa zaidi kuwezesha malengo kufanikiwa. Kwa hiyo kwa kila lengo lililopangwa unatakiwa uwepo mkakati wa kuonesha jinsi lengo hilo litakavyotekelezwa, litatekelezwa lini, na nani atafuatilia utekelezaji.

Katika makala hii nitaonesha jinsi  mikakati inavyosaidia ‘kusukuma’ malengo ya biashara. Kufanya hili, naomba nitumie mfano mmoja rahisi wa upangaji wa mikakati, unaoweza kufanywa katika mpira wa miguu au soka, kwa lengo la kuusaka ushindi dhidi ya timu pinzani, au kuwa bingwa wa mashindano hayo.

Mikakati – Tujifunze kutoka katika Soka.

Katika kufuatilia masuala ya michezo nimekutana na makala moja, ambayo, nilipoisoma nimeona inaweza kutumika kuelezea vizuri dhana ya mikakati katika biashara. Kwa wapenzi wa soka, na hasa wapenzi wa timu ya Yanga, nadhani mtaielewa dhana hii kirahisi zaidi, na baadaye itakuwa rahisi kuutumia uelewa huu katika kutengeneza mikakati ya biashara zenu.

Mwandishi wa makala hiyo, Mohamed Hussein, aliandika kuhusu hatima ya timu ya Yanga, iliyokuwa anashiriki Ligi ya Mabingwa wa Afrika, mwaka 2018, wakati ikijiandaa kupambana na timu ya Township Rollers ya Botswana, katika mchezo wa marudiano , wa kufuzu kucheza hatua ya makundi, uliopangwa kufanyika tarehe 17 Machi, 2018 huko Botswana.

Aliandika kujaribu kuwatoa hofu wapenzi wa soka hasa wale wa Yanga ambao walikuwa wanaonesha hofu ya wazi kuwa, kwa matokeo mabaya ya kufungwa mabao 2-1 nyumbani Tanzania, katika mchezo wa kwanza, basi wengi waliamini kuwa Yanga tayari imeshatolewa, hasa ukizingatia kiwango hafifu walichokionesha katika mechi ya kwanza.

Akiwatia moyo, Mwandishi huyo alisisitiza kuwa yeye anaamini kuwa mpira unadunda, na lolote linaweza kutokea katika mpira, na kwamba kikubwa ni namna Yanga itakavyojipanga ki-mkakati, na jinsi itakavyochanga vizuri karata zake huko ugenini.

Alipendekeza mikakati ambayo aliamini ikizingatiwa na kocha, pamoja na wachezaji, ingeweza kuwafanya Yanga kutimiza lengo lao kuu ambalo ni kufuzu kuingia hatua ya makundi; na pia kutimiza lengo lao la muda mfupi – kushinda mechi ile. Alipendekeza mikakati ifuatayo:

  • Kwanza, Yanga wajitahidi kuuchezea sana mpira ili kuwapa presha wapinzani wao
  • Pili, wajitume sana mwanzoni ili wapate bao la mapema litakalowaongezea morali wao, huku likiwachanganya wapinzani wao
  • Tatu, Kocha apange kikosi cha mabeki wengi, na pale katikati ni lazima pawe na viuongo wengi, ili waumiliki zaidi mpira, kisha kupokea na kutawanya mpira
  • Nne, Wachezaji wa mbele wajitahidi kuwa makini sana kumalizia nafasi walizotengenezewa
  • Tano, wachezaji wa mbele wasiwe wachoyo; na mchezaji anapoona hayuko katika nafasi nzuri ya kufunga goli basi asisite kutoa pasi au ‘assist’ kwa mchezaji aliye katika nafasi nzuri zaidi

Ku-ukweli, mikakati hii ilibuniwa tu na mwandishi wa makala ile. Huenda kocha wala wachezaji hawakuwahi kuisoma. Hata kama waliisoma, huenda wao walikuwa na mikakati yao. Hilo si muhimu sana. Muhimu ni kwamba ni lazima tuwe na mikakati katika kila lengo tunalotaka litimie. Ndiyo, kwani utafanikisha vipi malengo yako bila mbinu za utekelezaji?

Pamoja na mikakati yao, je, Yanga walishinda mechi ile? Hapana, walipata droo ya bila kufungana, na hivyo kutolewa katika mashindano hayo. Hata hivyo walionesha kiwango kikubwa zaidi ya kile cha nyumbani.

Hivyo basi, kama katika soka mikakati ni jambo muhimu sana kuzingatiwa, basi mikakati ni muhimu vilevile katika biashara, ikiwa ni njia au mbinu ya kusaidia kusukuma malengo, na hasa lengo kuu kabisa la kupata faida kupitia wazo lako la biashara. Zaidi ya faida, malengo mengine yanaweza kuwa, kuongeza mapato, na kupunguza gharama ya uendeshaji; ambayo yanahitaji mikakati pia.

Kwa mfano, kama lengo lako ni kuongeza mauzo, mikakati inayopaswa kuwekwa ni ile itakayosaidia kuwavuta wateja kwa wingi kuja kununua bidhaa yako, ambayo una uhakika inahitajika kwa wingi. Mikakati hiyo yaweza kuwa kama ifuatavyo:

  • Kuhakikisha bidhaa zako zina ubora wa hali ya juu
  • Kuziweka bidhaa zako mahala pa wazi ili wateja wasipate taabu kuziona
  • Kuitangaza biashara yako, na bidhaa zake, kwa kiwango cha juu
  • Kutoa huduma nzuri kwa wateja kabla, wakati na baada ya mteja kuondoka
  • Kujenga uhusiano mzuri na wateja ili wawe mabalozi kwa wateja wengine tarajiwa
  • Kutoa huduma kwa uaminifu ili wateja wawe na imani na wewe na biashara yako pia

Kwa hiyo, ili biashara yako ifanikiwe huna budi kujiwekea mikakati ya ushindi inayoakisi malengo yako, na inayoendana na changamoto zilizo mbele yako. Msisitizo mkubwa uko katika kuifuata mikakati hiyo kivitendo, kwani bila vitendo mikakati hiyo itaishia kubaki katika nadharia tu.

Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasirimali kivitendo.

Anapatikana kwa simu: 0718219530; e-mail: nzyy2001@gmail.com

Jinsi Ya Kupanga Malengo Ya Biashara Yako

Habari ndugu na rafiki,

Karibu tena katika mfululizo wa makala zangu zenye lengo la kuelimishana kuhusu masuala ya ujasiriamali, ubunifu na stadi za maisha.

Makala ya leo nitazungumzia jinsi ya kupanga malengo ya biashara.Tumeona katika makala za nyuma kuwa baada ya kuchagua wazo moja bora kati ya mawazo mengi yanayopita ndani ya ubongo wako, na baada ya kufanya tathmini ya wazo hilo na kujiridhisha kuwa litakupatia tija; kinachofuata sasa ni kuingia katika vitendo. Jambo mojawapo muhimu katika kufanikisha utekelezaji wa wazo la biashara ni kupanga malengo.

Malengo ya uhakika huzaa matokeo bora

Malengo yanabebwa na mambo au kauli zinayoelezea vitendo ambavyo vikifanyika kwa mpangilio fulani vitawezesha kufikia au kupata matokeo yaliyo katika ndoto au maono ya mtu. Malengo ndiyo mwongozo wa mahala unapotaka kufika. Baada ya kujua unataka kufanya nini, kupitia wazo lako bora la biashara ulilolichagua, sasa unapaswa kulikatakata wazo lako na kuliweka katika malengo, ambayo ukiyatimiza, utakuwa umefanikisha ndoto yako.

Katika uandishi wa malengo, tunatangulia kuandika lengo kuu, halafu chini yake yanafuatia malengo saidizi.  Malengo ni kiasi au kiwango cha mafanikio ambayo mjasiriamali anataka kuyapata ndani ya kipindi fulani. Malengo huandikwa katika mtindo wa kauli zinazoashiria matokeo yatakayopatikana kutokana na matendo yaliyopangwa kufanywa.

Wataalamu wa biashara wanasisitiza kuwa malengo, yanapoandikwa, yanapaswa kutimiza vigezo fulani. Yakitimiza vigezo hivyo yanapewa hadhi, kitaalamu, ya kuitwa malengo ‘SMART’. Tunaambiwa ili malengo yawe ‘SMART’ yanatakiwa: yawe na ‘uhalisia’, yaani yaeleze bayana nini hasa kinatakiwa kutimizwa; yaweze ‘kupimika’, yaani uweze kupima kama umetimiza lengo au la, kwa mfano uweze kusema, ‘lengo limekamilika kwa asilimia tisini’.

Malengo ‘SMART’ yanatakiwa pia yawe na ‘muda wa utekelezaji’, yaani uweze kujua kila lengo litakamilika lini; na yawe ‘yanawezekana kufikiwa’, yaani yaliyo ndani ya uwezo wako, na yasiyokatisha tamaa.

Ki-ukweli wajasiriamali wengi, hasa wadogo, pengine hata wa kati, hawana uwezo wa kutimiza vigezo vya uandishi wa malengo ‘SMART’. Wanaojaribu kuandika wanaandika kile tu wanachotaka kifanyike, basi, na wanaingia moja kwa moja katika vitendo.

Kwa mfano, mjasiriamali mmoja, rafiki yangu, ambaye ana kipaji cha usanii wa maigizo, alipata wazo la kuanzisha kikundi cha sanaa za maigizo. Kwa kuwa anapenda kuandika, ameandika yafuatayo:

Ndoto yake ni: “Kumiliki kikundi cha sanaa za maigizo na kukifanya kitoe sanaa zenye ubora wa juu katika ukanda wa Afrika ya Mashariki.”

Ameandika  lengo kuu la biashara yake kama ifuatavyo: “Kutengeneza na kusambaza kazi za sanaa zenye ubora wa juu zitakazokidhi mahitaji wa wateja tarajiwa.” Kimsingi hii ndiyo dhima au ‘mission’ ya biashara yake.

Chini ya lengo hili kuu, ameorodhesha malengo madogomadogo ambayo yakifanyiwa kazi yatawezesha kutimia au kufanikiwa kwa lengo kuu. Baadhi ya malengo hayo ni:

  • Kufanya tafiti ili kukusanya taarifa za mahitaji ya soko la sanaa hii na aina ya maudhui yanayohitajika kwa sasa.
  • Kubuni na kuandika miswada mizuri ya kazi hizo za sanaa.
  • Kuwa na timu nzuri ya wasanii wenye vipaji na nidhamu ya kazi hii.
  • Kuwa na timu ya wataalamu wa kutengeneza kazi mbalimbali zitakazotayarishwa.
  • Kufanya tafiti za maeneo yatakayotumika kuchezea kazi hizo.
  • Kusimamia utengenezaji wa kazi za sanaa zenye ubora.
  • Kupata masoko mazuri ya kuuzia kazi hizi.
  • Kufanya kikundi na kazi zake mbalimbali zifahamike kwa wateja
  • Kupata mapato makubwa kutokana na kazi za kikundi.

Unaweza kuona kuwa malengo haya yameandikwa ki-kawaida sana, na kwa kweli hayako ‘SMART’. Hivyo anapaswa kuyafanya yawe ‘SMART’. Hata hivyo anastahili pongezi! Angalau anaonesha kujua anachotaka kufanya ili atimize lengo kuu. Hayo ya kitaalamu zaidi anaweza kuelekezwa tu na akaelewa.

Katika malengo, kuna malengo ya muda mrefu na mengine ya muda mfupi, na kila lengo linaloonekana ni kubwa linaweza kuvunjwavunjwa tena kupata malengo madogo ambayo ni rahisi kuyatia katika vitendo.

Ni muhimu kuandika orodha ya malengo unayokusudia kupata matokeo yake, kwa sababu, kila lengo lina mpango wa utekelezaji, unaolenga kuonesha nini kitafanyika ili kufanikisha lengo husika na kitafanyika kwa kiwango gani, upi ni muda wa kuanza na kukamilika, mtu au watu gani watakaohusika kutekeleza, pamoja na bajeti ya utekelezaji.

Tunaambiwa na wataalamu kuwa ukishaweka malengo lazima pia uandike, kwa kila lengo, ni kwa namna gani utapima kama lengo lako limefanikiwa au hapana. Lazima uwe na kipimo cha mafanikio kitakachokuonesha hali halisi ya utendaji wako, kwa kujiuliza, je, unatimiza malengo au unakwama, kwa kiasi gani, na sababu zake ni nini?

Unaweza kujiuliza pia, je, ni malengo, labda yamekuwa makubwa sana, au tatizo ni changamoto zimezidi? Au labda ni uwezo wako wa kutenda ndio umekuwa mdogo? Hii inasaidia kujitathmini na kujipanga vizuri zaidi.

Ukishaweka malengo, una wajibu mkubwa wa kufuatilia kwa ukaribu utekelezaji wake, ukiongozwa na mpango wa utekelezaji. Ufuatiliaji ni shughuli inayofanyika mfululizo ikilenga kuona ni kwa kiwango gani yaliyopangwa yanatekelezwa.

Lengo la ufuatiliaji ni pamoja na kutathmini endapo yaliyopangwa yanatekelezwa vizuri, kwa kuzingatia muda, bajeti na rasilimali zingine. Ufuatiliaji unaweza kufanywa kila siku, kila wiki, kila mwezi au baada ya miezi kadhaa, na unatusaidia kubaini pengo kati ya yaliyopangwa kufanyika na yaliyotekelezwa, na sababu zake pia.

Kwa kumalizia, napenda kusisitiza kuwa malengo ndiyo mwongozo wa mahala unapotaka kufika. Kupanga malengo ni jambo muhimu lisilopaswa kupuuzwa. Baada ya kujua unataka kufanya nini, kupitia wazo ulilolichagua, unapaswa kulipanga wazo lako katika malengo, ambayo ukiyatimiza, utakuwa umefanikisha ndoto yako. Na unapaswa kujitahidi kuyafanya malengo yako yawe SMART.

Makala ijayo nitaelezea kuhusu mikakati katika biashara na umuhimu wake katika kufanikisha malengo.

Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasirimali kivitendo.

Anapatikana kwa simu: 0718219530; e-mail: nzyy2001@gmail.com

 

 

 

Ukishaiona Fursa, Acha Kusitasita – Anza Mara Moja!

Habari rafiki,

Karibu tena katika mfululizo wa makala zangu zenye lengo la kuelimishana kuhusu masuala ya ujasiriamali, ubunifu na stadi za maisha.

Katika makala iliyopita niliongelea kuhusu mambo ya kuzingatia katika mchakato wa kulipa uhai wazo lako la biashara, yaani kuliweka katika vitendo, baada ya kulifanyia utafiti na kujiridhisha. Nilikupatia mambo ya kuzingatia, kwa kuwa tayari umeridhika, kwamba wazo lako ni fursa sahihi, na umeamua kuanza kulitekeleza.

Makala hii inalenga kupiga hatua moja muhimu, mbele ya uamuzi wako wa kuanza utekelezaji. Nina maana kwamba – kuamua kuanza, na kitendo chenyewe cha kuanza, ni vitu tafauti. Upo ushahidi wa watu walioamua kuanza, lakini hawakuwahi kuanza kivitendo. Kuanza ni ‘kuyakabili maji‘.

Maji ukiyavulia nguo huna budi kuyaoga

Yupo mtu, rafiki yangu, alionesha hamu kubwa ya kuanzisha biashara ya ndoto yake, akapitia hatua zote muhimu, kama utafiti n.k., lakini ulipofikia wakati wa kuanza – kuna kitu fulani kilimuingia, ghafla, katika fikra zake. Mara akapata woga na hofu, akalegea. Kigugumizi kikamshika, akaanza kusitasita. Kisa? Anaogopa kufeli!

Ni ukweli, kwamba kupata taarifa muhimu za wazo lako, kupitia utafiti, haimaanishi kuwa wazo lako lazima lifanikiwe. Linaweza kufeli vile vile. Na hii ni kwa sababu yale majibu uliyoyapata ni maoni au hisia tu za watu uliowasiliana nao, au maandishi uliyosoma.

Unapoingia katika utekelezaji, mazingira yanaweza kubadilika na usipate yale uliyoyatarajia. Kwa hiyo kufeli ni kitu ambacho kinatokea.

Ninachotaka kusisitiza hapa ni kwamba  huwezi kufaulu chochote duniani kama hutathubutu kuanza kufanya, huwezi! Na hakuna mtu yoyote ambaye hakuwahi kuonja ‘kushindwa’, hakuna! Na wapo walioshindwa mara nyingi, akiwemo Richard Branson, tajiri niliyemjadili katika moja ya  makala zangu, bofya.

Kinachowakabili watu wengi, wakashindwa kuanza, ni woga wa kufeli. Ndiyo, watu wengi wanaogopa kuanza wakihofia watafeli, na hivyo wanaogopa gharama za kufeli. Sasa tujiulize swali.  Kama kuna gharama za kufeli baada ya kuthubutu kuanza, je hakuna gharama za kutokuanza kabisa?

Ukweli ni kwamba, ukithubutu kuanza unaweza kufeli, lakini usipothubutu kabisa, ni wazi kuwa hapo tayari umeshafeli! Ndiyo, utafaulu vipi ilhali hujafanya lolote?

Cha muhimu hapa ni ile hamasa uipatayo unapowaza kuwa: “Aah, ni kweli sikufaulu, lakini angalau nilithubutu kuanza.” Kumbukumbu hii huwa inajijenga ndani ya ubongo na kumpa mtu ujasiri kwa jambo lolote linaloweza kumkabili hapo baadaye, hapati hofu wala kigugumizi kuchukua hatua.

Kushindwa baada ya kuthubutu kunakufanya ujifunze. Ukiwa makini utagundua ulipojikwaa, na kwa hiyo utarudi katika utafiti na kuongeza mbinu zaidi ikiwa ni pamoja na kuomba ushauri zaidi kwa wadau.

Na vilevile, unapoanza kufanya ujue kuna mtu au watu wanakuona na kukufuatilia hata kama wewe mwenyewe huna habari. Wapo watu waliopata fursa za biashara ya ubia, au misaada, baada ya watu kuona na kuhamasishwa na uthubutu, hamasa na jitihada waliziona kwa huyo aliyefeli. Wakaunganisha nguvu na maarifa, wakapiga hatua.

Mjasiriamali maarufu wa Afrika ya Kusini, Vusi Thembekwayo, ana utaratibu wa kukaa na wajasiriamali wanaoanza na kusikiliza mawazo yao, ili, akiridhika na fursa iliyomo katika mawazo hayo, basi anawekeza kwao, na kuwezesha biashara kuanza.

Lakini Vusi amekuwa anasisitiza akisema: “I love people who have tried and failed”, akimaanisha kuwa anapenda kuwapa nafasi wale waliowahi kujaribu na wakafeli.

Anasema kwamba pesa yake ataipeleka kwa mtu aliyeonja kufeli, ambaye tayari anajua ‘upande wa pili wa kufanikiwa’.  Anasema, “kama hujawahi kufeli utaweza vipi kujifunza kufanikiwa?”

Mwandishi na mbunifu, George B. Shaw anasema kwamba mtu aliyetumia maisha yake yote kufanya makosa, kwa kujaribu,  sio tu atapata heshima, lakini pia atafanywa kuwa mtu muhimu na wa maana kuliko yule aliyetumia muda wake bila kujaribu chochote. 

Anaongeza: “Ni heshima kubwa kutumia muda wote wa maisha yako kuthubutu kufanya mambo na kuishia kufeli, kuliko kutumia muda huohuo kwa kutokufanya chochote.”

Mchezaji maarufu wa mpira wa kikapu, wa Marekani, Michael Jordan, anasema, “katika kipindi changu cha uchezaji wa mchezo huu, nimeshindwa karibu mara 9000 kuuingiza mpira ndani ya kikapu.”

Anasisitiza akisema, “vilevile, mimi na wenzangu tumepoteza michezo 300 hivi kwa kushindwa, na karibia mara 26, nimeshindwa kuingiza kapuni mipira ambayo wenzangu walinipasia, na ambayo nilikuwa na uhakika ningefunga. Ukweli nimeshindwa sana, tena mara nyingi, lakini nadhani kushindwa huko ndiko kulikonipa mafanikio yangu haya.”

Historia inathibitisha kuwa watu wengi waliopata mafanikio walipitia magumu. Walipitia vikwazo na changamoto nyingi kabla hawajafanikiwa.

Walishinda kwa sababu hawakukubali kukatishwa tamaa na kufeli kwao. Tafiti za kihistoria zinaonesha kuwa hata wababe wa vita, kama watu wengine, huwa wana hofu; wanaogopa kushindwa na yatokanayo na kushindwa.

Hata hivyo, cha ziada walichonacho ni kwamba hawaruhusu woga au hofu iwatawale. Hawa huwa wana ujasiri. Ujasiri una tabia ya kupambana na hofu, na kuishinda.

Kwa hiyo, kwa kumalizia, napenda kusisitiza kuwa suala hapa si kuamua kuanza, bali… kuanza! Nina maana kwamba – kuamua kuanza, na kitendo chenyewe cha kuanza, ni vitu tafauti.

Kusitasita kunatokana na hofu. Hofu ya kufeli na kuogopa gharama za kufeli. Kwa hiyo kinachotakiwa ni ujasiri na uthubutu.

Kinachotakiwa ni kujenga uwezo wa kupambana na hofu ya kufeli, huku ukiamini kuwa kufeli, kama kutatokea, kutakufanya ujifunze na kukupa hamasa ya kuanza upya, na mwisho wake ni mafanikio.

Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasirimali kivitendo.

Anapatikana kwa e-mail: nzyy2001@gmail.com

Jinsi Ya Kuliweka Wazo La Biashara Katika Vitendo

Habari ndugu na rafiki,

Napenda kukukaribisha tena katika mfululizo wa makala zangu zenye lengo la kuamsha bongo zetu na kuwafanya wasomaji wachukue hatua katika kubuni, kuanzisha, kuboresha na kuongeza thamani ya shughuli zao za kijasiriamali.

Makala ya leo inahusu mambo ya kuzingatia katika mchakato wa kulipa wazo lako la biashara uhai, yaani kutafsiri ndoto au taswira kuwa kitu halisi nje ya ubongo. Katika makala iliyopita, bofya, nilielezea namna mbili za ujengaji taswira au picha ndani ya ubongo; ya kwanza inayolenga kupata matokeo, na ya pili inayolenga kuzijua na kuzifuata, akilini, njia au mbinu za utekelezaji, ili kupata kitu halisi.

Sasa basi, baada ya mjasiriamali kufanya utafiti na kujiridhisha kuwa wazo lake ni bora, anatakiwa aanze kulitia katika vitendo, akiongozwa na taswira mbili alizokwishazijenga ndani yake.

Wataalamu wa biashara wanatueleza kuwa, jambo kubwa na muhimu linaloweza kumletea mjasiriamali mafanikio siyo tu ubora wa wazo lake la biashara, wala umakini aliotumia kutafiti wazo hilo, ili kujiridhisha – bali ni nia, uthubutu na hamasa aliyonayo ya kubadili wazo hilo kuwa kitu halisi, au vitendo. Wazo zuri litabaki kuwa zuri tu kichwani kama halitatiwa katika utekelezaji.

Kiukweli, si jambo jepesi, ki-vile, kubadili wazo la biashara kuwa kitu halisia. Kuna ugumu wake! Mtaalamu mmoja amelinganisha jambo hili na zoezi la mama mjamzito kutunga mimba na hatimaye kujifungua. Katika kujifungua kuna uchungu unatangulia ndipo mtoto apatikane, na baada ya hapo kuna changamoto za malezi ya mtoto anayezaliwa.

Hivyo, kama mama anavyojiandaa kujifungua, ujasiri anaouonesha katika kujifungua, na uvumilivu katika malezi, ndivyo ambavyo mjasiriamali anapaswa kuwa katika kipindi cha kuanza utekelezaji wa wazo lake.

Kwa hiyo, tufanye kwamba tayari umeshaamua kuanza, na tayari una taarifa muhimu, sasa  basi kuna mambo kadhaa unayotakiwa kuyazingatia ili ndoto yako iingie katika matendo kukuwezesha kuona au kupata kitu halisi.

Ukishaamua, tia nia, hamasa na ujasiri – utashinda

Mambo hayo ni kama ifuatavyo:

Kwanza, amini unaweza. Huwezi kuchukua hatua ya kufanya jambo lolote kama hujiamini. Lazima uamini kuwa unaweza kuhimili changamoto za uamuzi ulioufanya. Lazima ubebe majukumu hayo na uwajibike kwa kila ukifanyacho.

Pili, jiandae kupambana na changamoto. Unapoanza utekelezaji wa wazo lako kuna changamoto ‘kibao’ utakutana nazo. Ukilijua hili na kulikubali mapema utapata hamasa itakayokufanya usiyumbe na kutoka kwenye mstari. Hamasa itakupa uwezo wa kupambana na kushinda changamoto hizo.

Tatu, jiwekee malengo. Malengo ndiyo mwongozo wa mahala unapotaka kufika. Baada ya kujua unataka kufanya nini, kupitia wazo lako bora la biashara, sasa unapaswa kulikatakata wazo lako na kuliweka katika malengo, ambayo ukiyatimiza, utakuwa umefanikisha ndoto yako. Anza na lengo kuu, kisha  weka malengo saidizi. Hakikisha malengo yako yanalingana na kitu unachotaka kitimie.

Nne, weka mikakati ya kufikia malengo. Mikakati ni njia au mbinu mbalimbali zinazoweza kutumiwa na mjasiriamali kufikia malengo aliyojipangia. Utaalamu unatuelekeza kuwa ili lengo kuu la biashara litimie, hatuna budi kujiwekea mikakati ya ushindi, inayoendana na changamoto zilizo mbele yetu. Msisitizo mkubwa uko katika kuitia mikakati hiyo katika vitendo, kwani bila hivyo mikakati hiyo itabakia nadharia tu.  Katika makala zijazo tutajadili kwa kina kuhusu malengo na mikakati.

Tano, kaa katika malengo yako. Kama mjasiriamali, safari yako inaanza na malengo ya kutekeleza kufikia ndoto yako. Kinachofuata ni kuheshimu malengo yako. Unapaswa kupambana na vipingamizi au changamoto zinazojitokeza. Hupaswi kuyumbayumba, hata ukiona fursa mpya, unayodhani labda ni bora zaidi. Baki njia kuu hadi utimize malengo yako.

Sita, tumia rasilimali zako zote kwa umakini. Safari ya kutimiza ndoto yako inahitaji matumizi sahihi ya rasilimali. Rasilimali hizi ni pamoja na muda, fedha, vifaa au mashine, majengo na wafanyakazi. Rasilimali hizi zikitumika kwa kiwango cha juu zitakupatia matokeo sahihi.

Saba, ipende biashara yako. Ili ufanye biashara yako kwa ufanisi unapaswa kuithamini biashara hiyo. Upendo huu utakupatia motisha na hamasa ya kuziona fursa nyingi zinazoweza kuiboresha biashara yako, lakini pia hamasa itakupatia nguvu ya kupambana na changamoto.

Nane, usikate tamaa. Safari ya kutimiza malengo ina milima na mabonde; ina miiba na visiki, na hata wadudu wenye sumu kama nge. Ukikosa ushujaa utapata hofu kisha utakata tamaa, na hivyo utashindwa kuendelea. Chagua uvumilivu na jipe matumaini ya kushinda.

Tisa, boresha biashara yako jinsi inavyokua. Jinsi unavyoendelea kufanya biashara yako na kupata taarifa mbalimbali, jifunze kuunganisha nukta au doti. Kuunganisha nukta ni kuangalia matukio mbalimbali, kuyalinganisha, na kuona kama yana uhusiano ambao unaweza kutumika kupata kitu kipya na bora zaidi. Hii ni dhana ya kibunifu inayomfanya mtu ajiongeze.

Kumi, ongeza juhudi na maarifa. Mafanikio yoyote yanachochewa na juhudi na nidhamu, lakini pia mchakato wa kujifunza, ambao hauna, na hautakiwi kuwa na mwisho. Kujifunza kila siku kunampatia mtu uwezo mpana wa kufanya mabadiliko. Hivyo, ongeza maarifa kwa kusoma vitabu, kusikiliza radio au runinga au kuingia katika mitandao yenye mafunzo.

Kumi na moja, jenga himaya ya washauri. Mjasiriamali usijidanganye kuwa una maarifa yote, kwa kuwa wazo ulilochagua umelibuni wewe, na pengine umelifanyia utafiti, hivyo hakuna kipya unachohitaji. Hii si sahihi! Wazo na matokeo ya utafiti wakati mwingine havioani kabisa na hali halisi kivitendo.

Unapaswa kujenga tabia ya kujifunza kutoka kwa waliotangulia, wenye uzoefu wa biashara uliyoamua kuifanya. Waliotangulia pengine kuna wakati walianguka, lakini wakajifunza kitu, kisha mambo yakakaa vizuri. Usingoje hadi uanguke, utakuwa umechelewa.

Rais wa Richmel Media, Rich Melcombe, anashauri kuwa kama unataka kuwa mjasiriamali mwenye mafanikio wasikilize wote, kwani hujuwi nani atakupa wazo litakalokuonesha fursa au litakalokuepusha na hatari au tishio. Hata hivyo, unapaswa kupima ushauri huo na kujiridhisha.

Kwa kumalizia, napenda kuwahamasisha wajasiriamali ambao tayari wana wazo zuri na bora, ambalo linaendelea kuzunguka ndani ya akili zao, walifanyie utafiti, na halafu, wakijiridhisha, wasipoteze muda, waanze utekelezaji kivitendo, mara moja, ili wazo lao libadilike kuwa kitu halisi.

Nakukaribisha tena katika makala zangu zijazo ili tuendelee kujifunza pamoja mada hizi za ujasiriamali, ubunifu na stadi za maisha.

Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasirimali kivitendo.

Anapatikana kwa e-mail: nzyy2001@gmail.com

 

 

 

 

Jinsi Ya Kupima Kama Wazo Lako La Biashara Litaleta Tija

Habari ndugu na rafiki yangu,

Karibu tena katika mfululizo wa makala zangu, kupitia Blog ya Mbunifu Blog, zenye lengo la kuamsha bongo za wasomaji wangu na kuwafanya wachukue hatua katika kubuni, kuanzisha, kuboresha na kuongeza thamani ya shughuli zao za kijasiriamali.

Makala ya leo inahusu upimaji wa wazo lako la biashara. Kabla ya kuendelea tujikumbushe mambo muhimu kutoka makala zilizotangulia. Katika makala hii, bofya, niliweka msisitizo kuwa ili upate wazo bora la kijasiriamali unapaswa kuanza kuwaza chanya.

Unapaswa pia  kujizoeza kuitumia vizuri milango yako ya fahamu ili uweze kutambua na kupambanua  vitu vinavyotokea kupitia milango hii. Lakini pia unatakiwa ujenge imani ya uwepo wa ulimwengu wa roho, na kwa imani hii utashushiwa maono au ufunuo utakaokuonesha kitu cha kufanya na nguvu ya kukidhihirisha kitu hicho kiuhalisia.

Na katika makala hii nyingine, bofya, nilikufafanulia mazingira yanayosaidia au kuchochea akili ya binaadamu kuibuka na fikra au mawazo ambayo kati ya hayo, baada ya tafakuri, linaweza kuibuka au kuchaguliwa wazo moja lenye manufaa makubwa kuweza kumletea mtu mafanikio likiweza kutiwa katika matendo.

Baada ya kuwaza chanya, na kuyatumia vizuri mazingira yanayochochea akili kupata fikra, tayari sasa una wazo ambalo ukitulia, ukiinama, ukiinuka, unaridhika kuwa wazo lako ni bora na litatimiza ndoto zako.

Unapopata wazo la biashara unakuwa umeliunda wazo hilo kichwani. Unaona jinsi unavyoweza kuyatia yale unayoyaota katika vitendo, na jinsi unavyoweza kufanikiwa kupata matokeo. Ndio maana mara nyingi watu wenye uthubutu mkubwa wakifikia hatua hii hutamani kuanza utekelezaji mara moja! Hawataki kupoteza muda kuangalia hiki au kile, hapana, wao wanataka kuanza, mengine yatajulikana mbele kwa mbele. Hii si sawa!

Wataalamu wa biashara wanashauri kwamba mjasiriamali apatapo wazo au mawazo kadhaa ya biashara yanayomtia hamasa, anapaswa kujipanga vizuri ili aweze kujua ni wazo au biashara gani anayoweza kuifanya kwa ufanisi zaidi na ikamletea tija. Mtaalamu wa Uchumi kutoka Chuo Kikuu Mzumbe, Profesa Honest Ngowi, katika andiko lake moja anasema, “Ni muhimu kujiridhisha kwanza kabla ya kushughulikia fursa husika.”

Uamuzi sahihi ni zao la uchunguzi makini

Kujiridhisha kuna maana ya kukusanya taarifa muhimu zitakazompatia mjasiriamali uelewa wa kutosha wa mazingira na tasnia nzima ambamo biashara yake imo.

Anatakiwa kuzijua fursa, vitisho, udhaifu na uwezo wake wa kukabiliana na changamoto zote zitakazojitokeza wakati wa utekelezaji wa wazo lake. Akijiridhisha kwamba tayari amepata taarifa hizo, amezielewa na anajiona ana uwezo mkubwa kuliko udhaifu, basi hilo ni wazo zuri na bora kutiwa katika vitendo.

Sasa basi, ili kupata taarifa hizo muhimu, kuna maswali ya kujiuliza na kutafiti, na inashauriwa kuwa majibu ya utafiti huo yaandikwe ili yaje kuwa dira au kioo, kwa mjasiriamali, anapoelekea katika utekelezaji. Kuna watu wanaruka hatua hii kwa kudhani wanafahamu vya kutosha mambo hayo; na wengine wanaogopa kuujuwa ukweli, au wana hofu, kwa kuwa wakijua watakata tamaa.

Lakini ukweli unabaki kuwa utafiti ni muhimu kwani unatoa mapema picha ya kufanikiwa au kushindwa kwa biashara yako. Utafiti unazalisha taarifa na takwimu ambazo zinampatia mjasiriamali uwezo na ujasiri wa kuanza kivitendo.

Jingine la msingi ni kwamba, utafiti, ukifanywa kwa umakini, una msaada mkubwa wakati wa uandishi wa mpango wa biashara, ambao nitauelezea katika makala zangu hapo baadaye. Mwandishi William Pirraglia anasema, “Ili uandike mpango bora wa biashara unapaswa kufanya utafiti makini wa maeneo yote muhimu ya biashara yako, na unapaswa kutumia muda mwingi hapa, kuliko hata wakati wa uandishi wa mpango wa biashara.”

Yafuatayo ni baadhi ya maswali yanayotakiwa kupatiwa majibu:

Kwanza, biashara, bidhaa au huduma unayotaka kuuza ina manufaa gani kwako, kwa jamii na kwa wateja wako? Je, ni bidhaa inayohitajika kwa sasa au unadhani watu wakiijuwa, kisha wakaijaribu au kuionja, wataihitaji?

Pili, je unategemea nani watakuwa wateja wa bidhaa au huduma yako, je, ni watu wazima, watoto, wanawake n.k., na je wana uwezo, kifedha, kununua? Nani ni watumiaji wa bidhaa, nani wanaotoa pesa, na nani wanashawishi ununuzi ufanyike? Je, nini mtazamo wa wateja tarajiwa kwa bidhaa au huduma yako? Je, unadhani wataipokea na wakawa radhi kulipa?

Tatu, Je una ujuzi na maarifa ya kutosha kufanya biashara hiyo? Kama huna, je una uwezo wa kupata ujuzi huo wakati ukiendelea na biashara?

Nne, uwezo wa mtaji. Je, mtaji kiasi gani unahitajika kuanzisha biashara hiyo na unaweza kupatikana wapi, na kwa masharti gani? Je unaweza kumudu masharti hayo?

Tano, sehemu ya kufanyia biashara. Je, biashara yako utaifanyia sehemu au eneo gani? Je, eneo au chumba kina nafasi ya kutosha kulingana na saizi ya biashara yako? Je, wateja wako wanaweza kuifikia sehemu hiyo kiurahisi? Nini unaweza kufanya kuboresha eneo hilo?

Sita, kujua taratibu za kisheria. Je, biashara unayotaka kufanya inaruhusiwa kisheria? Nini miongozo au masharti yanayoongoza ufanyaji wa biashara yako? Je, unaweza kuyamudu masharti hayo bila kuathiri tija unayotarajia?

Saba, Ushindani katika biashara. Je, unawajua washindani wako wa sasa? Wapo kiasi gani katika eneo lako? Je, wanauza, na wana wateja kiasi gani? Je, wateja wao wanaridhika na bidhaa au huduma za washindani wako? Je, ushindani utaongezeka? Kama ndiyo, je una mbinu gani kumudu ushindani wa sasa na wa baadaye ili uweze kuuza kwa faida?

Nane, wagavi (suppliers) wa bidhaa zako. Je, unatarajia kununua wapi bidhaa zako? Je, ni kiwandani, kwa mawakala au maduka ya jumla? Je, wauzaji hawa wapo wengi kiasi gani, na bei zao zikoje? Je, bei hizo zitakupa faida? Je, mgavi yupi anaweza kukupatia bidhaa kwa unafuu zaidi? Je, wewe utauza bidhaa yako kwa bei gani? Je, kwa kiasi gani bei yako itawavutia wateja wako?

Tisa, usafirishaji wa bidhaa kuja eneo lako la biashara. Je, wapo wasafirishaji wanaoweza kukubebea bidhaa zako? Wapo wangapi? Wanatoza bei gani, na je una uwezo wa kumudu gharama hii?

Kumi, Umiliki wa biashara yako. Je, biashara yako utaiendesha peke yako, au kwa ubia na mtu au watu wengine? Kama ni ubia, nini nafasi ya kila mbia? Kwa kiasi gani mnaaminiana na mtamudu kwenda pamoja?

Kumi na moja, kuitangaza biashara. Kwa kuwa biashara ni wateja, na ili wateja waijuwe ni lazima uitangaze. Je, bidhaa yako utaitangaza kwa njia gani? Njia hizo zina gharama kiasi gani, na je una uwezo wa kumudu gharama hizo?

Kumi na mbili, wafanyakazi. Zipo biashara ambazo huwezi kufanya peke yako, ni lazima utahitaji wafanyakazi. Je, utahitaji kuajiri? Je, wapo watu wenye ujuzi na tabia stahiki kukusaidia katika biashara yako? Je, wafanyakazi watakuwa na gharama kiasi gani? Je utaimudu gharama hiyo?

Kumi na tatu, uwepo wa huduma za kijamii zinazowezesha biashara. Je, eneo lako lina huduma muhimu kama umeme, maji, mtandao wa intaneti n.k.? Kama hazipo, je, unaweza kumudu gharama ya kuzileta huduma hizo?

Kumi na nne, usalama wa eneo lako la biashara. Usalama ni kitu muhimu sana kwa mjasiriamali mwenyewe, bidhaa pamoja na wateja. Je, biashara yako itakuwa salama? Je, kuna vyombo vya dola karibu vitakavyotoa msaada endapo usalama wako utatishiwa? Je, unaweza kumudu kuajiri watu wako kwa ajili ya suala la ulinzi na usalama wa biashara yako?

Ndugu msomaji wangu, haya ni baadhi ya maswali muhimu ambayo ni vizuri ukajiuliza na kujijibu. Ili upate majibu yenye usahihi wa kutosha ni lazima utafiti. Kuna njia nyingi za kupata taarifa ambazo unaweza kuzitumia kujua haya.

Njia rahisi zaidi ni kuwajuwa wadau wote wanaohusika katika biashara yako na kuongea nao moja kwa moja au kuwaandikia hojaji ya maswali haya, huku na wewe ukiandika au kukariri majibu yao kwa lengo la kuyapima na kutoa uamuzi wako wa mwisho, kwamba wazo lako litaweza kutiwa katika vitendo au hapana.

Karibu tena katika makala zijazo zitakayozidi kukupa maarifa ya ubunifu wa biashara na ujasiriamali.

Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasirimali kivitendo.

Anapatikana kwa e-mail: nzyy2001@gmail.com

 

 

Mazingira Yanayochochea Kuibuliwa kwa Mawazo ya Biashara

Habari rafiki.

Karibu tena katika mfululizo wa makala za ujasiriamali zinazolenga kukupatia maarifa yatakayokusaidia kubuni au kuboresha biashara kwa ajili ya kuboresha maisha yako. Makala ya leo inalenga kukufahamisha mazingira ambayo yanachochea kupatikana kwa mawazo ya biashara au ubunifu.

Binaadamu wa kawaida huzalisha mawazo kila siku. Kwa mujibu wa tafiti mbalimbali, wataalamu wanatuambia kuwa ki-kawaida binaadamu huzalisha takriban mawazo 60,000 kila siku. Haya ni mawazo kwa ujumla wake, yapo mazuri, yapo mabaya, yapo ya manufaa na yapo pia ya kuleta uharibifu. Kila ukionacho hapa duniani ni matokeo ya uwezo wa binaadamu kufikiri na kutenda.

Kuna mazingira yanayochochea akili ya binaadamu kuibuka na fikra au mawazo  ambayo kati ya hayo, baada ya tafakuri, linaweza kuibuka au kuchaguliwa wazo moja lenye manufaa makubwa zaidi kuweza kumletea mtu mafanikio likiweza kutiwa katika matendo.

Mazingira hayo ni kama ifuatavyo:

Kwanza kabisa, ni mazingira asilia, yaani yasiyo ya kawaida. Katika mazingira haya, wazo linakuja lenyewe tu, kama mwizi, na linakuja kama tone dogo. Wakati fulani wazo linakuja na kutoka na kwa hiyo utulivu ukipatikana wazo linapata mashiko.

Nimeeleza huko nyuma kuwa  mawazo ya aina hii huingia katika akili yakitokea katika ulimwengu wa roho na  huhifadhiwa  katika akili ya ndani; yaani mtu umekaa mahala, na hasa ukiwa peke yako, au unatembea au unaendesha gari taratibu au uko chooni, au umejilaza tu; na wakati mwingine umelala usingizi, na ghafla wazo kubwa linakujia kama ndoto fulani hivi; wazo la maana ambalo hujawahi kulifikiria, kulisoma au hata kulisikia mahala popote, linakuja tu na unaona lina maana na unaweza kulitumia kupata manufaa.

Kinachotakiwa hapa ni utayari wa kuhifadhi kumbukumbu ya wazo jipya, kwani wakati mwingine unaweza kulisahau, na hasa wazo linalipitia katika ndoto, usiku. Ukiweza, jizoeze kutembea au kuwa karibu na note book na kalamu kwa ajili hii, na hii ni rahisi kwa sasa hasa kwa watu wenye umiliki wa simu janja (smart phones).

Pili, ni mawazo yanayotokana na matumizi sahihi ya milango ya fahamu. Uwezo wa kupepesa macho au kutega masikio na kubaini changamoto zinazowakabili watu kila siku katika maisha yao. Haya ni mahitaji ya jamii unayoweza kuyaona au kuyasikia. Hapa unatumia zaidi milango ya fahamu, kama macho au masikio. Uwezo huu unaanzia katika kuyaona mahitaji yako binafsi na halafu kuchunguza mahitaji ya wengine. Kwa kufanya hivi utapata mawazo mengi ambayo yakichujwa vizuri litapatikana moja litakalotatua tatizo.

Tatu, Kutumia ujuzi, elimu au hobby uliyonayo. Kwa mfano, kama wewe ni fundi wa kushona nguo, au ujenzi, au una hobby ya kuchora, usibweteke, tumia maarifa au ujuzi wako kupata wazo la biashara inayoendana na fani yako. Kwa ujuzi au uzoefu huo unaweza kuibua wazo la kufungua kituo cha ushonaji au uchoraji na kuanza kupata kipato.

Nne, Kushiriki maonesho, semina na mikusanyiko. Ukiwa na mazoea ya kushiriki mikusanyiko mbalimbali, inayohusisha wataalamu, au maonesho ya biashara, utapata jukwaa litakalokuwezesha kuona, kusikia au kuhisi vitu vitakavyokupatia wazo la biashara.

Maonesho kuibua mawazo

Katika maonesho utaona, utasikia

Tano, ujio wa teknolojia mpya katika soko au jamii. Hapa, angalia staili ya maisha ya watu kwa sasa na teknolojia wanayoitumia au kuipenda. Kwa mfano, zamani katika sherehe mbalimbali vilitumika vyombo vya bati au plastiki na vijiko vya chuma, kulia chakula, ambavyo vilikuwa na changamoto nyingi. Lakini baada ya kuingia teknolojia mpya, watu wakapata wazo la kutumia vyombo vya chakula vya ‘kutumia na kutupa’, disposable tools, na hili limeweza kutengeneza fursa kwa watu kuanzisha biashara ya vifaa hivi.

Sita, uwepo wa habari na taarifa mbalimbali. Kwa kufuatilia habari au taarifa katika vyombo vya habari ni rahisi sana kuibua wazo la biashara. Vyombo kama magazeti, majarida, redio, TV na kadhalika ni vyanzo vikubwa vya maarifa na taarifa. Ukiwa makini na mdadisi lazima utapata pa kuanzia na mwisho kujenga wazo lenye manufaa.

Saba, kuwashirikisha wataalamu wa fani mbalimbali katika matatizo yako au yanayoikabili jamii. Kwa mfano, wewe ni mkulima wa mazao halafu unagundua shamba lako au mashamba ya jirani zako yanakabiliwa na tatizo la wadudu au ugonjwa fulani wa mazao kila mwaka. Hapa unaweza kuamua kumshirikisha mtaalamu wa wadudu au magonjwa ya mazao, na kwa kushirikiana mkaja na wazo la kuanzisha duka la madawa au pembejeo za kilimo.

Nane, Kujenga uhusiano na mawasiliano bora na watu au taasisi mbalimbali. Ukiwa na mtandao mkubwa na wahusiano mazuri na wadau utapata maarifa au taarifa zitakazokuwezesha kuibua wazo la biashara.

Tisa, Kufuatilia tafiti  mbalimbali za kitaalamu. Zipo taasisi nyingi au vyuo vikuu vinavyofuatilia na kuchunguza matatizo au changamoto mbalimbali zinazoikabili jamii na kutoa mapendekezo ya utatuzi. Ukiweza kutafuta ripoti za tatifi hizi na kuzisoma utapata maarifa mengi yatakayokuwezesha kuja na wazo fulani la biashara.

Kumi, tumia kipaji au haiba uliyonayo. Kwa mfano, unaweza kusikia watu wakikwambia, “Aah, we kijana una uwezo mkubwa wa kuchekesha.” Au watu wanakwambia, “Aah, we binti umeumbika au wewe ni mcheshi sana!” Ukituliza akili hapa utapata wazo la kitu cha kufanya chenye manufaa. Tumia sifa hizi kujiweka karibu na taasisi  zinazohitaji watu wa aina yako, ambao kwa kutumia haiba au kipaji chako, kwa pamoja, mtatengeneza kipato. Mchekeshaji, MC Pilipili, anadai kuwa akiwa shule alisikia watu wakisema kuwa maneno yake yana mvuto na ana uwezo wa kuchekesha, akapata wazo, akalifanyia kazi, na sasa anafaidi matunda.

Kumi na moja, tumia vitu unavyopenda kutazama, kusoma au kusikiliza. Kila mtu anapendelea kutazama au kusikiza vitu fulani. Wapo wanaopenda muziki, filamu, mitandao ya kijamii, intaneti na kadhalika. Kuna maarifa mengi katika vitu hivi. Ukitazama kwa lengo maalum na ukitia umakini katika kufuatilia vitu hivi utapata mawazo mengi yatakayokuwezesha kupata wazo moja bora la kulifanyia kazi.

Nakukaribisha tena usome makala ijayo katika mfululizo wa makala zangu za ujasiriamali, ubunifu na stadi za maisha.

Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasirimali kivitendo.

Anapatikana kwa e-mail: nzyy2001@gmail.com

Jinsi Ya Kubuni au Kuunda Wazo la Biashara

Habari rafiki.

Karibu tena katika makala nyingine inayolenga kukupatia maarifa ya ujasiriamali, ubunifu na stadi za maisha. Makala yangu iliyopita nimezungumzia jinsi ubongo unavyochakata mawazo ya kijasiriamali hadi kusababisha kupatikana kwa wazo la kitu cha kufanya.

Nimesisitiza umuhimu wa kuwaza chanya, kuitumia vizuri milango ya fahamu pamoja na kuamini katika ulimwengu wa roho. Makala ya leo nitazungumzia kwa undani jinsi ya kubuni  wazo la biashara, nikihusisha ubongo.

Wazo la biashara linaanza na hamu au hamasa ya kufanya au kupata kitu, na huanzia ndani ya ubongo. Wazo la biashara linaanza na taswira au picha ya jambo au kitu, inayotokana na vitu vinavyoingia katika akili zetu kupitia milango ya fahamu au vinavyokuja kama ndoto kupitia ulimwengu wa roho. Hii inahusisha kuviona vitu ndani ya ubongo wako kwa kutumia jicho la ubongo, ufahamu au akili.

Jicho la ubongo hutoa taswira ya jambo au kitu cha kibunifu unachoweza kukifanya au kukiunda baadaye kuwa kitu halisia. Unapotengeneza taswira ya kitu ndani ya ubongo na ukatia nia, unaanza kuona uwezekano wa kitu hicho kuwa kitu halisi au kutokea baadaye.

Unapoanza kuhisi kuwa kitu fulani kitatokea kiuhalisia unaanza kutengeneza motisha, hamu au nguvu ya msukumo wa kufanya kitu hicho ili kupata matokeo.

Ubongo hutafsiri taswira kuwa halisia

Watafiti wa ubongo wa binaadamu wanasema kwamba taswira inayojengwa ndani ya ubongo, na picha halisi inayotokea kwa nje, vinasafiri kwa kupishana, yaani kimoja kinaingia, kingine kinatoka.. Wataalamu hao wanatueleza kuwa ndani ya ubongo kuna chembe hai (neurons) ambazo zikichochewa zinasafirisha taarifa kutoka katika akili ya ndani, ambazo zinasaidia kutoa tafsiri ya taswira iliyojengwa kwenye akili ya ndani, kuwa vitu halisi kwa nje.

Tukijenga taswira akilini mwetu, ya jambo au kitu fulani, basi michakato ndani ya ubongo inazichochea hizi chembehai, ambazo zikifanya kazi pamoja zinaunda visiwa vya kumbukumbu ndani ya akili vinavyouandaa mwili kufanya jambo, hapo baadaye, linalolingana na taswira iliyojengwa ndani ya ubongo.

Kwa mujibu wa wataalamu wa ubongo, kuna namna mbili za kujenga taswira katika ubongo. Namna ya kwanza ni taswira inayolenga kupata na kuyaona matokeo. Hii inahusisha ile hali ya kujiona kuwa tayari umeshafanya kitu hicho, unachotamani kitokee, na tayari umeshafanikiwa kutimiza lengo lako.

Kwa mfano, Kama wewe ni mwanariadha, unajenga picha katika akili yako kuwa unashiriki mbio na hapo ulipo tayari unaongoza mbio hizo. Unaona jinsi ‘unavyojifua’ ili usipitwe na washindani wako, kisha unajiona umegusa kamba na kumaliza mbio ukiwa wa kwanza, na sasa unakabidhiwa kombe – na tayari unashangiliwa kila kona, ukiwa shujaa!

Kwa mujibu wa wataalamu, ukishikilia taswira hiyo na ukaifanya irudierudie ndani ya akili yako, halafu ukatia imani, nia, hamasa na nguvu, kuna uwezekano mkubwa ndoto hiyo  ikatimia kiuhalisia. Kwa hiyo kama una uwezo au kipaji fulani, ni vizuri ukachora taswira ya kitu unachotaka ukifanye au ukipate, ili ikusaidie ‘ku-focus’ na kutia bidii. Piga picha ya ushindi ukitumia mfano huo hapo juu.

Namna ya pili ya ujengaji  taswira ni ule unayoonesha njia itakayotumika kupata matokeo tarajiwa. Hii inahusisha kufikiria na kujenga picha ya njia zote utakazotumia kufikia matokeo tarajiwa. Taswira hii inalenga katika kuzifuata na kuzitimiza hatua zote unazokusudia kupitia ili kupata matokeo.

Kumbuka, kujenga taswira au picha akilini hailazimishi au siyo garantii kuwa utapata matokeo unayoyaota. Kitu kikubwa ni kwamba kuyafikia matokeo kunategemea sana uwepo wa vichocheo. Vichocheo vya mafanikio ni pamoja na kuweka malengo sahihi, kuweka mikakati thabiti, kutia bidii, kujituma, kuwa na nidhamu na kujenga motisha binafsi.

Kwa hiyo, mawazo ya biashara yanayolenga matokeo mazuri, na mikakati yake, huwa yanakuja kwa mtindo huu ndani ya bongo zetu ambapo yanaanza kama picha hivi ambayo inakuonesha taswira ya kitu ulichopania kufanya.

Ndani ya taswira hiyo unaiona biashara yako jinsi inavyokwenda, mfano, kama unasemasema au unawaza kumiliki biashara ya vinywaji, ndani ya akili yako unaiona bidhaa yako. Unaona magari yaliyobeba bidhaa yako yakitoka kiwandani kuja katika eneo lako la biashara, unaona wateja wako wanakuja na kununua, unaona pesa zinavyoingia, unaona jinsi mtaji wako unavyokuwa, na mwisho unahisi furaha unayoipata.

Maono haya yanaunda, ndani ya akili yako ya ndani, visiwa vya kumbukumbu vinavyouandaa mwili kufanya haya unayoyaona kama picha – yaje nje na yatokee katika uhalisia.

Mwandishi mmoja anasema kuwa mtu hutambua kwanza fursa ndani ya moyo wake, na baadaye kuilezea kwa mdomo au kuichora au kuiandika, kisha huchukua hatua ya kuitia katika vitendo. Kutokana na picha uliyoijenga unaanza kuumba mawazo yenye mantiki ambayo unaweza kuyatekeleza kivitendo.

Maono ni mawazo yenye ushawishi na msukumo mkubwa wa kufanikisha jambo unalolitaka maishani. Maono yanatengeneza wazo, mfano la biashara, sanaa au ubunifu, ambalo likichakatwa linatoa matokeo bayana. Akili yako husikiliza mawazo yako kwa umakini mkubwa, mithiri ya amri iliyotolewa na kiongozi wako, na hulazimika kuitekeleza amri hiyo ipasavyo.

Kwa hiyo ndugu msomaji, kila ukionacho hapa duniani ni matokeo ya wazo la mtu fulani. Vitu kama magari, ndege, kompyuta, taasisi mbalimbali au sanaa, ni matokeo ya mawazo ya mtu mmoja au kikundi. Nilitoa mfano wa mjasiriamali maarufu Tanzania Mzee Mengi, kuwa alianza na wazo, biashara yake ya mwanzo, ya utengenezaji wa kalamu, kisha akaamua kuingia katika vitendo.

Hivyo basi napenda, kwa kumalizia, nisisitize  kuwa ili tuje na wazo zuri la biashara na tulitie katika vitendo kuna umuhimu wa kuanza kujenga taswira zote mbili kama nilivyoainisha hapo juu, kisha tuvifanyie kazi vichocheo vya mafanikio ambavyo ni pamoja na kuweka malengo sahihi, kuweka mikakati thabiti, kutia bidii, kujituma, kuwa na nidhamu na kujenga motisha binafsi.

Nakukaribisha tena usome makala ijayo katika mfululizo wa makala zangu za ujasiriamali, ubunifu na stadi za maisha.

Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasirimali kivitendo.

Anapatikana kwa e-mail: nzyy2001@gmail.com