Jinsi Ubongo Unavyochakata Mawazo ya Kijasiriamali

Habari rafiki.

Karibu tena katika mfululizo wa makala za ujasiriamali zinazolenga kukupatia maarifa yatakayokusaidia kubuni au kuboresha biashara kwa ajili ya kuboresha maisha yako. Nimesema katika makala zilizopita kuwa tafiti zinaonesha kuwa ni adadi ndogo sana ya Watanzania wana elimu hii muhimu na kwamba wakiipata itawasaidia kufungua bongo zao, watapata uthubutu na ujasiri wa kuingia katika tasnia hii.

Leo nitazungumzia mahusiano ya ubongo na uumbaji wa mawazo ya kijasiriamali. Katika hatua za uanzishaji wa biashara, jambo la kwanza kabisa ni kupata wazo la nini unataka kufanya.

Akili hukaa ndani ya ubongo

Mawazo mbalimbali hutungwa ndani ya ubongo wa mwanadamu yakiwemo mawazo ya kibunifu kama kufungua biashara au kuanzisha stadi fulani, mfano uchoraji au uchongaji wa vinyago. Sayansi ya ubongo siyo rahisi sana, lakini kwa maelezo rahisi, yasiyo ya kisayansi sana, inaweza kueleweka. Vitu vinavyofanyika ndani ya ubongo hupangwa na kuratibiwa vizuri ili baadaye vijioneshe nje kama vitendo halisi.

Ndani ya ubongo kuna kitu kinaitwa akili.  Akili, au uwezo wa kufikiri na kuchambua mambo, kinatokana na michakato mbalimbali ndani ya ubongo. Kwa sehemu kubwa mwili wa binaadamu hujiendesha kwa kutumia akili au ufahamu. Huwezi kuishika akili, kama unavyofanya kwa ubongo. Bali, akili hujionesha kupitia mawazo, maneno na matendo ya binaadamu.

Mwandishi John F. Paul, katika kitabu kiitwacho ‘Weka Ufahamu Wako Huru’, anasema kuna sehemu tatu za akili ya mwanadamu na zina kazi tafauti. Kwa muktadha wa makala hii nitazungumzia na kuchambua sehemu mbili za mwanzo.

Sehemu ya kwanza ya akili inaweza kuitwa akili ya nje, ambayo  hufanya kazi wakati mtu yuko macho na ana ufahamu, yaani hajalala. Sehemu hii hufanya kazi ya kufikiri na kupambanua mijadala ya ndani ya ubongo ambayo huwatokea binaadamu kila siku; na pia hufanya kazi ya kutambua vitu vinavyotokea kupitia milango ya fahamu kama kuona, kusikia na kunusa, na kuvipatia majibu; kwa mfano kutambua sura au sauti ya mtu. Sehemu hii huhifadhi vitu kwa muda mfupi sana kabla ya kuvihamishia sehemu ya pili.

Sehemu ya pili ya akili ni ufahamu wa ndani. Hii ina kazi kubwa kwa binaadamu. Ina kazi ya huhifadhi kumbukumbu zote. Mawazo awazayo mtu kwa muda mrefu, na maneno anayosema mara nyingi huhifadhiwa hapa. Sehemu hii pia hupokea na kuhifadhi kumbukumbu kutoka sehemu ya kwanza ya akili, kwa mfano, wakati fulani unaweza kuona au kusikia kitu, taarifa au maarifa fulani, halafu ukayaona ya kawaida tu wakati huo. Kumbukumbu hii huhifadhiwa katika akili ya pili.

Sasa, hutokea siku moja unapata tatizo au unawaza kufanya kitu, unawazaa – lakini hupati jawabu. Mara, umetulia kidogo, unaona kitu kama video kikipita katika akili yako, kinayaleta kama picha yale uliyoyaona au kuyasikia zamani. Yanakuja kama kitu halisi ambacho kimeambatana na maarifa ya utatuzi wa tatizo. Unapata jawabu la tatizo au unapata maarifa ya kibunifu.

Lakini kingine muhimu ni kwamba sehemu hii hupokea pia na kuhifadhi kumbukumbu zote zinazotoka katika ulimwengu wa roho na hufanya zieleweke bayana. Kumbukumbu hizi zinaweza kuitwa maono au ufunuo.

Hizi huingia katika akili zikitokea katika ulimwengu wa roho na  huhifadhiwa  hapa; yaani mtu umekaa mahala, na hasa ukiwa peke yako, au unatembea au umejilaza tu; na wakati mwingine umelala usingizi, na ghafla wazo kubwa linakujia kama ndoto fulani hivi; wazo la maana ambalo hujawahi kulifikiria, kulisoma au hata kulisikia mahala popote, linakuja tu na unaona lina maana na unaweza kulitumia kupata manufaa.

Sifa kubwa ya sehemu hii ni uwezo wa kuzitoa nje ya mwili kumbukumbu za mambo au mawazo yaliyohifadhiwa humo ili yawe kitu halisi au yajidhihirishe katika uhalisia au vitendo muda unapowadia.

Kwa hiyo, unapowaza au kutamka kwa muda mrefu kuhusu kitu fulani, akili huamini kuwa hicho ukiwazacho au kukitamkatamka ndicho unachokihitaji na kwa hiyo akili, kupitia nguvu ya uumbaji tuliyopewa na Mungu, itakihifadhi ili kitumike baadaye. Utendaji huu wa akili unashirikiana kwa kiwango kikubwa na mawazo na maneno yetu tunayosema kwa kurudiarudia na kwa msisitizo. Haya huhifadhiwa na akili ya ndani na huwa yanajidhihirisha kwa kutokea baadaye.

Kuna watu wanawaza na kujisemeasemea kuwa wanataka mafanikio makubwa ya kifedha, na wakifanikiwa watafanya mabadiliko makubwa kwao na kwa jamii zao. Haya ni maono. Watu hawa wana nafasi kubwa ya kutimiza ndoto zao. Ndio maana Mwandishi John F. Paul anatuhimiza tusitawaliwe na mawazo hasi; kwa mfano, “aah mimi sifai kwa lolote bwana, wala sidhani kama nitafanikiwa maishani”!

Anasema kuwa akili zetu hazikuumbwa ili kukaa na hasi, kwani unapokuwa mtu wa kuwaza au kusema hasi, kumbukumbu hizo zinahamishiwa sehemu ya pili ya akili na kuhifadhiwa, na baadaye kudhihirika au kutokea kiuhalisia. Anatuhimiza tuwaze au tuseme chanya. Mawazo au maneno chanya ni yale yaliyojaa imani, ujasiri na uhakika. Ni mawazo ya kutokubali kushindwa. Mfano, ukiwaza au kutamka mara kwa mara kuwa, “Niko imara katika nafsi, mwili na roho yangu, na nina uhakika wa kufanikisha jambo nililopanga kulifanya”, kumbukumbu hii huhifadhiwa akilini na mara nyingi hujidhihirisha baadaye.

Kuwaza chanya huzalisha matokeo chanya. Kwa wapenzi wa mpira wa miguu wanamfahamu sana mchezaji maarufu, mshambuliaji,  Mohamed Salah, ambaye kwa sasa anachezea timu ya Liverpool, ya Uingereza. Salah alishinda tuzo ya Mchezaji Bora wa mwaka wa ligi ya Uingereza (2018).  Akizungumza na waandishi wa habari, wakati akikabidhiwa tuzo hiyo, aliulizwa kama aliwahi kuwa na fikra au wazo la kufanya vizuri kiasi hicho wakati akijiunga na timu hiyo.

Akijibu swali hilo Mo Salah alisema, “Ndiyo, jambo hilo kwa muda mrefu limekuwa linazunguka akilini mwangu. Nikiwa club ya Chelsea na baadaye Roma, sikuweza kutimiza ndoto zangu, kwani niliwekwa benchi muda mwingi. Hata hivyo wazo la kufanya vizuri pindi nikipata fursa lilizunguka ndani ya ubongo wangu siku zote. Kwa hiyo nilipopata fursa ya kujiunga Liverpool, na wakaniamini, niliona huo ndio hasa wakati wa kutimiza ndoto zangu, na kweli zilitimia kiuhalisia, na haya ndiyo matunda yenyewe.”

Kwa kumalizia napenda kuweka msisitizo kuwa ili upate wazo bora la kijasiriamali unapaswa kuanza kuwaza chanya. Unapaswa pia  kujizoeza kuitumia vizuri milango yako ya fahamu ili uweze kutambua na kupambanua  vitu vinavyotokea kupitia milango hii. Lakini pia unatakiwa ujenge imani ya uwepo wa ulimwengu wa roho, na kwa imani hii utashushiwa maono au ufunuo utakaokuonesha kitu cha kufanya na nguvu ya kukidhihirisha kitu hicho kiuhalisia.

Nakukaribisha tena usome makala ijayo katika mfululizo wa makala zangu za ujasiriamali, ubunifu na stadi za maisha.

Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasirimali kivitendo.

Anapatikana kwa e-mail: nzyy2001@gmail.com

Zijuwe Sifa Muhimu Za Mjasiriamali

Karibu tena rafiki yangu katika mfululizo wa makala zangu za ujasiriamali.

Makala iliyopita niliandika kuhusu nini hasa maana ya ujasiriamali. Pamoja na maelezo mengine nilimnukuu pia Profesa Bruce Bachenheimer, wa Chuo Kikuu cha Pace, ambaye anafundisha ujasiriamali, ambaye anasema kitovu cha ujasiriamali kiko katika fikra, yaani namna ya kufikiri na pia kutenda.

Naendelea tena kukushirikisha ushauri kutoka kwa wadau wa masuala ya elimu, kwamba, juhudi zinatakiwa kufanywa kuwapatia vijana na watu wazima stadi za ujasiriamali.

Makala ya leo inahusu na itachambua sifa za mjasiriamali. Ili mtu aitwe mjasiriamali anapaswa kuwa na sifa fulani muhimu ambazo ukiziona kwake unaweza kabisa kumtofautisha na mtu asiye mjasiriamali.

Kuzijuwa sifa hizi ni muhimu kwa wajasiriamali walioanza ili waziboreshe, na kwa wale wajasiriamali tarajiwa, waweze kuzijenga tabia zao ili ziendane na sifa hizi, ambapo wataweza kunufaika baadaye kwa kuzitumia kuwa wajasiriamali.

Msomaji, bila shaka unawafahamu wajariamali na wafanyabishara wakubwa kutoka nchi zilizoendelea, kama Richard Branson, Mwingereza na mmiliki wa Virgin Group of Companies, inayofanya biashara mbalimbali ikiwemo ya usafirishaji wa anga, Virgin Atlantic Airlines, ambayo imepata umaarufu mkubwa nchini Uingereza, ikishindana kwa ukaribu na British Airways.

Lakini kwa hapa Tanzania kuna wajasiriamali na wafanyabishara wengi waliofanikiwa na kupata umaarufu kama Mzee Reginald Mengi, ambaye ni Mwenyekiti wa Makampuni ya IPP.

Kuna vitu vya kujifunza kupitia kwa watu waliofanikiwa kibiashara kama wazee hawa, ambao wote walianzia chini kabisa, yaani hawakurithi utajiri au mafanikio waliyonayo. Walianzia mahala fulani chini, wakajenga fikra na maono, wakafanya vitu fulani kwa utaratibu fulani na mwisho wakapata mafanikio hayo.

Kwa mfano, katika kitabu chake cha I can, I must, I will, Mzee Mengi anatueleza kuwa maisha yake yalianzia katika umaskini kiasi kwamba alikwenda shule akiwa pekupeku, bila viatu. Lakini baadaye alijigeuza kuwa mtu tofauti. Ukiwachunguza matajiri hawa, utagundua wana tabia au sifa fulani ambazo zimebeba mafanikio yao.

Kwa hiyo, sisi wengine ambao tuna hamu ya kupata mafanikio kama wao au zaidi hatuna budi kuzijua sifa hizo ili tuziige, zitusaidie kupiga hatua mapema. Kuiga kimkakati ni moja ya siri ya mafanikio.

Yawezekana wao walikuwa na vipaji tu vya kuweza kufanya mambo kwa utaratibu mzuri na wakapata mafanikio, na labda walikuwa na udhaifu ambao hawakuujua ambao uliwapunguzia kasi ya mafanikio yao. Na labda wangepata fursa ya kujifunza kutoka kwa waliowatangulia huwenda wangekuwa mbali zaidi katika safari yao ya mafanikio. 

Hivyo tujifunze kutoka wao, na wengine pia, ili pengine tusichelewe kufanikiwa.

Zifuatazo ni sifa au tabia muhimu za mjasiriamali; naomba tuzifuatilie kwa pamoja:

Kwanza, mjasiriamali anapaswa kuwa na nia ya dhati toka moyoni kutaka kuanziasha na kukuza kitu anachoota kukifanya (maono). Mjasiriamali anasukumwa na mawazo pevu. Kwa vile tayari ana maono, hawezi kurudishwa nyuma na wengine asifanye yale yaliyo moyoni mwake. Atapambana kutimiza ndoto zake.

Kauli mbiu ya Mzee Mengi, ya I Can, I Must, I Will, inaashiria ushupavu,kujiamini na utayari wa kuishi katika kile alichoamua kukifanya.

Pili, uwezo wa kudadisi na kuyasoma mazingira yake na kugundua mahitaji, matatizo au changamoto zilizomo kisha kuchukua hatua haraka. Kwa mfano, Mjasiriamali Reginald Mengi anasimulia kupitia kitabu chake cha I can, I must, I will, kuwa alipata msukumo wa kuanzisha biashara yake ya kwanza mwaka 1983 akiwa jijini Dar-Es-salaam.

Alikuwa ameishiwa kalamu ya wino, peni, na akapita katika maduka kadhaa akitaka kununua bila mafanikio. Alipotafakari ndipo anagundua kuwa kuna uhaba wa peni nchini, na akagundua kuwa kumbe peni walizotumia zilikuwa zikitoka nchi jirani.

Hapo ndipo wazo likamjia la kuingia katika biashara ya utengenezaji wa peni. Uamuzi huu ulilenga kutatua shida za wananchi waliokuwa na uhitaji wa bidhaa hii, lakini pia ulikuja kuwa chanzo cha yeye kujitengenezea kipato chake. Na huu ndio ujasiriamali wenyewe.

Richard Branson alithubutu na akaweza

Tatu, uwezo wa kuthubutu. Hii ni tabia ya mtu ambaye ana uthubutu wa kuanzisha jambo akijua kabisa kuwa mbele yake kuna vihatarishi (risks) na vikwazo. Anaanza tu akiwa amejiandaa kukabiliana na chochote kitakachotokea.

Richard Branson alipoamua kuanzisha biashara ya usafiri wa ndege, Virgin Atlantic Airways, alijua kulikuwepo na kampuni yenye jina kubwa, British Airways, ikiwa tayari na mafanikio makubwa, lakini alijitosa, akathubutu, na mwisho ameweza na anasonga mbele.

Nne, mjasiriamali anapaswa kuwa na uwezo wa kupanga (planning). Mtaji utoke wapi, nini kifanyike kwa utaratibu gani, mipango ya kuitangaza biashara, mipango ya mauzo, mipango ya manunuzi, kodi, ubunifu, na usimamizi wa  rasilimali zote (watu, fedha, muda, vitu nk). Wataalamu wanasema ukishindwa kupanga umepanga kufeli.

Tano, mtazamo chanya. Mjasiriamali akiwa na sifa hii anakuwa na fikra za kusonga mbele, hakati wala kukatishwa tamaa, hata pale mambo yanapokwenda vibaya au anapokabiliwa na changamoto au matatizo katika biashara au kazi yake, yeye anashikilia tu msimamo wake hadi afikishe mzigo mwisho wa safari.

Sita, hamu ya kujua kupitia kujifunza. Richard Branson amekuwa muumini mkubwa wa kujifunza kupitia waliofanikiwa, hasiti wala kuona aibu kuuliza au kuhoji ili apate kufahamu mambo kwa kina. Lakini anasoma sana, vitabu, majarida n.k. kupata maarifa mapya kila siku. Hii ni sifa muhimu sana.

Saba, mjisiriamali anatakiwa awe anafikiri sana. Richard Branson anaamini kuwa huwezi kufanya maamuzi sahihi haraka haraka. Anaamini maamuzi madogo madogo ndiyo yanaweza kufanyika bila kufikiri sana, lakini maamuzi makubwa na ya msingi yanahitaji muda wa kufikiri.

Hivyo kufikiri kunakuwezeha kuangalia pande nyingi za fursa, tatizo au changamoto kabla ya kutoa uamuzi. Maamuzi mabaya yanaweza kuidhuru biashara yako.

Nane, imani katika ubunifu. Kama ndio unaanza, au bila kujali mafanikio uliyokwisha pata, lazima uelewe kuwa kila siku mambo na vitu vinabadilika na usipokuwa mbunifu utapitwa na wakati.

Richard Branson anaamini sana katika ubunifu na ugunduzi. Mbunifu ni mtu mwenye uwezo wa kuangalia vitu, changamoto au matatizo kwa jicho la kidadisi, lenye nia ya kuleta mabadiliko au utofauti fulani utakaoleta matokeo bora zaidi.

Tisa, mjasiriamali hapendi kuridhika au kubweteka. Kuna watu wakizoea kufanya kitu kwa utaratibu fulani, ni vigumu sana kuwaondoa kutoka kwenye mazoea hayo. Hawa watu ni waoga kuanzisha kitu kipya kwa vile tu hawajawahi kukifanya au hakipo katika mazingira waliyoyazoea, na wakiweza kufanya kitu kidogo basi wanaona inatosha.

Richard Branson anapenda kujaribu kila anachowaza, wala habweteki, na tabia hii imemsaidia kufanikisha mengi.

Kumi, mahusiano mazuri na wadau. Wadau ni watu au taasisi ambazo zina mahusiano ya karibu na mjasiriamali, mfano wateja, wafanyakazi, wabia n.k. Mjasiriamali anapaswa kuwafahamu wadau wake wote ili atengeneze mkakati mzuri wa mahusiano nao. Ongea vizuri, msikilize na mwelewe kila mdau upate mchango wake. Tumia uwezo wako wa kushawishi kusukuma mambo yaende.

Kumi na moja, uwezo wa uongozi na uratibu wa kazi. Mjasiriamali anapoanzisha au kuendesha shughuli yake anakuwa na watu wanaomsaidia kufanya mambo yaende. Hawa ni wafanyakazi au wasaidizi wake. Kwa hiyo anatakiwa awe na upeo mkubwa wa usimamizi, uongozi na uratibu mzuri wa kazi ili kazi ifanyike kama ilivyopangwa, kwa wakati, na kwa ubora.

Kumi na mbili, mjasiriamali ana uwezo wa kutumia alichonacho kusonga mbele. Mjasiriamali hasubiri hadi awe na kila rasilimali mkononi. Anaanza na kile kidogo alichonacho kisha anatia nguvu, bidii na ubunifu. Anayasoma mazingira, anaongea na wadau na kutoa ushawishi na mwisho anajenga kikubwa juu ya kile kidogo alichoanza nacho.

Kumi na tatu, mjasiriamali anatambua kufeli kupo. Katika Kitabu chake, Mzee Mengi anasema, kitakwimu, biashara nyingi zinazoanzishwa hufeli.

Hata hivyo mjasiriamali wa kweli analitambua hili na wala haliogopi! Anachokitanguliza yeye ni shauku yake ya kutimiza maono na malengo yake, akizingatia kujenga nidhamu, umakini na kuchukua kila tahadhari kwa kila anachofanya.

Kwa mfano, Richard Branson anasema amewahi kuanzisha biashara kadhaa ambazo zilifeli; zikiwemo Virgin Cars, Virgin Publishing na Virgin Clothing. Lakini anasema aliendelea kuwa na mtazamo chanya, hakuogopa wala kukata tamaa, bali alijengea hamasa zaidi na motisha binafsi kuendelea kufanya kila alichoona kinawezekana.

Kumi na nne, mjasiriamali anatakiwa kuwa muadilifu. Yaani anatakiwa aaminike na awe na sifa au tabia zinazomfanya aheshimiwe.

Anatakiwa awe mkweli katika kila anachofanya au kuwafanyia wadau wake. Ina maana mafanikio yako yanatokana na imani (trust), yaani idadi ya watu wanaokuamini na wako tayari kufanya kazi na wewe, kukukopesha bidhaa au pesa, kununua bidhaa zako au kukupa msaada wakati wa matatizo.

Kumi na tano, mjasiriamali anatakiwa kujichanganya na watu wengine (networking). Mzee Reginald Mengi anasema yeye amekuwa na tabia ya unyenyekevu na ukaribu kwa watu wote. Anasikiliza maoni yao, hata yale yanayompinga, na tabia hii imemfanya aweze kuwa na mahusiano mazuri na watu wa aina na rika zote, na hii imemsaidia sana kukuza biashara zake.

Kwa hiyo, kuzijuwa sifa hizi ni muhimu kwa kila mtu anayefikiria kuingia katika fani hii; na kwa walio ndani ya fani tayari basi wajiboreshe zaidi waweze kupiga hatua kubwa. Usikose makala ijayo katika mfululizo wa makala zangu za ujasiriamali na ubunifu.

Mwandishi wa makala hii ni Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasiriamali.

Anapatikana kwa e-mail: nzyy2001@gmail.com

Je, Nini Maana Ya Ujasiriamali?

Habari rafiki yangu.

Karibu tena katika mfululizo wa makala za ujasiriamali na ubunifu.

Makala iliyopita niliandika kuhusu umuhimu wa vijana na watu wazima kupata maarifa au elimu ya ujasiriamali kwani ni muhimu. Na nilieleza kwamba tafiti zinaonesha kuwa vijana wengi wanaohitimu katika ngazi mbalimbali za elimu wanakabiliwa na changamoto ya ajira.

Lakini pia, kwa mujibu wa tafiti, watu wazima walio katika ajira mbalimbali wanakabiliwa na changamoto ya ufahamu mdogo wa stadi muhimu za maisha ya kijasiriamali.

Mwisho, niliwashirikisha ushauri kutoka kwa wadau wa masuala ya elimu, kwamba, juhudi zinatakiwa kufanywa kuwapatia vijana na watu wazima stadi hizi.

Kwa kuzingatia ushauri huu, blog yangu ya Mbunifu Blog itajikita katika kutoa stadi za ujasiriamali, ubunifu, uvumbuzi na stadi za maisha kwa ujumla, ambazo zitasaidia kuamsha bongo na kukufanya wewe msomaji uchukue hatua katika kubuni, kuanzisha, kuboresha na kuongeza thamani ya shughuli au biashara zako.

Makala ya leo itajikita katika kufafanua kwa kina nini hasa maana ya  ujasiriamali kwa ujumla ili msomaji wangu uweze kujua ili akiamua kuchukua hatua basi ziwe kweli hatua za kijasiriamali kisawasawa.

Ujasiriamali ni neno pana sana ingawa mara nyingi linatumika kumaanisha uwezo wa mtu kuanzisha na kuendesha biashara yake.

Tuliona kupitia makala iliyopita kuwa kwa tafsiri ya kawaida ujasiriamali ni uwezo wa kuwaza na kutenda kimkakati unaomfanya mtu kubuni, kuanzisha, kuboresha na kuongeza thamani ya biashara au kazi.

Kwa ufupi, ujasiriamali ni uwezo wa kugeuza changamoto mbalimbali zilizipo katika jamii yetu kuwa fursa. Kumbuka tunaishi katika jamii zenye matatizo na changamoto nyingi, ambazo zinahitaji utatuzi.

Profesa Bruce Bachenheimer, wa Chuo Kikuu cha Pace, ambaye anafundisha ujasiriamali, anasema kitovu cha ujasiriamali kiko katika fikra, yaani namna ya kufikiri na pia kutenda.

Ujasiriamali umeelezewa pia kwa muktadha wa karne ya 21 ambapo watafiti Donald Kuratco na Richard Hodge (2004) wanasema kuwa ujasiriamali imekuwa ajenda kuu katika kusukuma ukuaji wa uchumi, kukuza ubunifu na kupunguza umasikini.

Wanasema ujasiriamali ni mchakato endelevu unaohusisha kuwa na maono, kuweka malengo, kufanya mabadiliko na kutengeneza vitu vipya. Ujasiriamali unahitaji nguvu, motisha, jitihada na uvumilivu kuweza kuunda na kuyatia katika matendo mawazo mapya na mbinu za kutatua matatizo.

Kiukweli, huwezi kusema kiuhakika kuwa kuna watu wamebarikiwa saana, hivyo wamekuwa wa kipekee na hivyo wakaweza kuwa wajasiriamali walio na mafanikio, hapana! Ujasiriamali unahitaji mtu aamue, atengeneze hamasa, motisha na msukumo wa ndani, atie jitihada na kisha abadili maono kuwa matendo, kitu ambacho kila mtu akiamua anaweza.

Ujasiriamali ni zaidi ya kuanzisha biashara. Ujasiriamali unahusisha tabia na uwezo wa kuzitafuta fursa, kuamua kujitosa katika lindi la tope ukijua kuwa unaweza kuzama, na uwezo wa kung’ang’ania na kuifuatilia fursa uliyoiona hadi uone matunda yake.

Ujasiriamali ni tabia na mazoea ya  mtu ambaye ana uthubutu. Watu hawa ni wabunifu na wanapenda kufanya vitu tofauti ki-utofauti. Ujasiriamali ni ujasiri, na wajasiriamali wakati wote wanakimbizana kufanya vitu ambavyo wengine ama hawavioni au wanaogopa kuvikabili.

Mfano ni mfanya biashara Reginald Mengi, aliyeamua kuingia katika biashara ya vyombo vya habari katika kipindi ambacho tayari Tanzania ilikuwa ina vyombo vingi vya habari na ushindani ulikuwa mkubwa.

Hata wasaidizi wake walimshangaa kwani wao walishazoea kwamba wao shughuli yao ni uzalishaji wa bidhaa za matumizi ya nyumbani kama sabuni, detergents, dawa za meno na vitu kama hivyo.

Kwa kuwa ujasiriamali ni uwezo wa mtu kutazama, kuona na kuthubutu kuanzisha jambo lenye manufaa kwake na kwa jamii, ndiyo maana Waziri wa Habari, Sanaa, Utamaduni na Michezo wa Tanzania Mh. Harrison Mwakyembe alisikitishwa sana na tabia ya Watanzania kushindwa kuziona fursa muhimu na kuzichangamkia.

Akizungumza baada ya ziara ya Rais wa FIFA nchini Tanzania, Bw. Gianni Infantino, mwaka jana, Waziri Mwakyembe alinukuliwa akisikitishwa na Watanzania kushindwa kutumia fursa ya ugeni ule kufanya tukio la kijasiriamali la kuwaingizia kipato na kutangaza bidhaa zetu.

Waziri alidai, “kweli Watanzania hatuna elimu ya ujasiriamali, tumeshindwa kuiona fursa hii muhimu. Tumeishia tu kujaa Uwanja wa Ndege na kumshangilia Infantino lakini hakuna hata kanga, kitenge, tisheti wala kinyago kilichoandaliwa kwa ajili ya kutangazwa na kuuzwa kwa wageni wale.”

Aliendelea kusema, “wenzetu Nigeria waliitumia vizuri sana fursa hii, wao walikuwa wameandaa bidhaa nyingi walizoziuza kwa wageni hao ikiwa ni pamoja na vitenge na tisheti vilivyoitangaza pia nchi yao. Tisheti zao ziliandikwa, kwa kiingereza, ‘Karibu Infantino kwenye nchi ya Soka’”.

Hapa Waziri Mwakyembe anatukumbusha na kutuelimisha Watanzania kujua maana na mbinu za ujasiriamali. Anatuhamasisha kuwa na maono na uthubutu wa kufanya mambo ambayo pengine wengine hawajayaona au hawana msukumo wa kuyaanzisha.

Anaungana na mtazamo wa Profesa Bruce Bachenheimer, wa Chuo Kikuu cha Pace ambaye anasema kitovu cha ujasiriamali kiko katika fikra, yaani namna ya kufikiri na pia kutenda.

Kwa kumalizia napenda kukuhimiza msomaji wangu kusoma kwa kina na kuelewa maana ya ujasiriamali na umuhimu wake pia, na kisha kuanza kujijengea uwezo wa kufikiri kijasiriamali ambao utakupatia msukumo na uthubutu wa kuanzisha au kuboresha shughuli yoyote yenye manufaa kwa jamii.

Pia usikose kuungana nami katika makala inayofuata katika mfululizo wa elimu hii ya ujasiriamali na ubunifu.

Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, Mtaalamu wa fani ya biashara na mjasiriamali.

Anapatikana kwa e-mail: nzyy2001@gmail.com

Je Elimu Ya Ujasiriamali Ina Umuhimu Kwa Jamii?

Habari za leo rafiki yangu.

Napenda kukukaribisha ujiunge na mimi ili tuwe pamoja katika kusaka maarifa muhimu yahusuyo ujasiriamali, ubunifu na stadi za maisha.

Hii ni makala yangu ya kwanza katika blog yangu hii mpya. Napenda kukuahidi kwamba nitakuja na makala nzuri nzuri zenye kutia hamasa zitakazokupatia hamu ya kuthubutu na kuanza kufanya au kuboresha vitu muhimu vinavyohusu maisha yako.

Tafiti zinaonesha kuwa vijana wengi wanaohitimu katika ngazi mbalimbali za elimu wanakabiliwa na changamoto ya ajira. Lakini pia watu wazima walio katika ajira mbalimbali wanakabiliwa na changamoto ya ufahamu mdogo wa stadi muhimu za maisha ya kijasiriamali.

Ushauri kutoka kwa wadau wa masuala ya elimu ni kwamba juhudi zinatakiwa kufanywa kuwapatia vijana na watu wazima stadi hizi.

Kwa kuzingatia ushauri huu, blog yangu ya Mbunifu Blog itajikita katika kutoa stadi za ujasiriamali, ubunifu, uvumbuzi na stadi za maisha kwa ujumla, ambazo zitasaidia kuamsha bongo na kuwafanya wasomaji wachukue hatua katika kubuni, kuanzisha, kuboresha na kuongeza thamani ya shughuli au biashara zao.

Hivyo kama wewe msomaji ni kijana uliye katika au umehitimu ngazi fulani ya elimu, sekondari au chuo, au wewe ni mtu mzima na tayari uko katika ajira rasmi au isiyo rasmi, ukifuatilia makala zangu utapata mengi ya kujifunza katika maeneo tajwa hapo juu, na ukichukua hatua utafanikiwa katika kuboresha maisha yako ya sasa au ya baadaye.

Leo nitaanza na ufafanuzi wa elimu ya ujasiriamali kwa ujumla na kuona kama kuna umuhimu wowote wa watu kujifunza elimu hii.

Kwa tafsiri ya kawaida ujasiriamali ni uwezo wa kuwaza na kutenda kimkakati unaomfanya mtu kubuni kuanzisha, kuboresha na kuongeza thamani ya kitu au kazi.

Kwa ufupi, ujasiriamali ni uwezo wa kugeuza changamoto mbalimbali zilizopo katika jamii yetu kuwa fursa. Kumbuka tunaishi katika jamii zenye matatizo na changamoto nyingi, ambazo zinahitaji utatuzi.

Msingi wa ujasiriamali ni kutambua au kuziona fursa, ikifuatiwa na uthubutu wa kuchukua hatua katika kuifanya fursa fulani ilete manufaa katika jamii.

Kwa mfano, ukichunguza kijijini au mtaani kwako, ukagundua kuwa watu kila siku wanabeba viroba vya nafaka kwenda kijiji au mtaa wa tatu kukoboa au kusaga nafaka hizo, na wanalalamikia uchovu, muda unaopotea na usumbufu, utabaini kuwa hapa panahitajika mashine ya kukoboa na kusaga nafaka.

Ukichukua hatua na kufunga mashine hizo, utakuwa umetatua shida za wananchi, lakini pia utakuwa unatengeneza kipato chako. Na huu sasa ndio ujasiriamali wenyewe.

Kwa kuona umuhimu wa ujasiriamali hasa kwa vijana walio katika shule na vyuo, tayari serikali ya Tanzania kupitia wizara husika imeanza kuhimiza mafunzo ya ujasiriamali kwa wanafunzi hawa ili wakimaliza shule au chuo waweze kuwa na uwezo wa kuzisaka na kuziona fursa na hivyo kuweza kujiajiri au kuajiriwa.

Kumbukumbu zinaonesha kuwa mwaka 1997 Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi nchini Tanzania ilianzisha somo la stadi za kazi katika mtaala wa elimu ya msingi, kwa lengo la kuwawezesha vijana kuwa na mtazamo chanya katika ulimwengu wa kazi, kutambua na kuendeleza vipaji vyao na kupata stadi za maisha zitakazowafanya wawe na uwezo wa kuona vitu ambavyo pengine wasingeweza kuviona pasipo elimu hii.

Kumbukumbu zinaonesha pia kuwa mwaka 2004 serikali ilianza kutambua na kuipa uzito elimu ya ujasiriamali katika mfumo rasmi na usio rasmi wa elimu – lengo likiwa kuwawezesha wanafunzi katika ngazi zote za elimu kupata elimu hii.

Kutokana na mabadiliko mbalimbali ya mifumo ya kisiasa na uchumi wa dunia matumaini ya kila aliyehitimu masomo yake kuajiriwa yanazidi kuyeyuka, kwa kuwa nafasi za ajira zilizopo hazitoshi kumeza idadi kubwa ya wahitimu wanaomaliza kila mwaka.

Hata wahitimu walioweza kupata ajira, wengi wanalalamikia mishahara midogo, wakati mwingine hailipwi kwa wakati, hivyo kuwafanya wasiweze kumudu kutatua matatizo yao ya msingi.

Hivyo waliokosa ajira na walioajiriwa wote wanakabiliwa na msongo wa mawazo – vyuma vimekaza! Kwa hiyo utatuzi wa changamoto hizi unaweza kupatikana kupitia elimu ya ujasiriamali.

Dunia, Tanzania ikiwemo, imejaa fursa nyingi za kiuchumi na kibiashara. Kinachotakiwa ni watu kuamka. Vijana wanapaswa kujenga uwezo na tabia za kijasiriamali; kupepesa macho, kutazama, kuona na kufikiri ki-utofauti ili kuweza kuziona fursa hizi kwa lengo la kuzivuna.

Akitoa maoni yake kuhusu Sera mpya ya Taifa ya maendeleo ya Vijana Tanzania, mwaka 2018, mmoja wa wawakilishi wa vijana, kutoka mkoa wa Simiyu, Elizabeth Laurent, alisisitiza kuwa moja ya changamoto zinazowakabili vijana ni ukosefu wa elimu ya ujasiriamali. Aliongeza kuwa hilo halitakiwi kusahaulika ili kuwaweka vijana kwenye ramani ya fursa za maendeleo.

Makamu wa pili wa Rais wa Zanzibar, Balozi Seif Ally Iddi, wakati akifungua mafunzo ya fursa kwa vijana wajasiriamali mjini Unguja, mwishoni wa mwaka 2017, alisema Tanzania imebarikiwa kuwa na idadi kubwa ya wajasiriamali, lakini ni asilimia ndogo tu ya hao wana ujuzi au elimu ya ujasiriamali, usimamizi wa biashara, taarifa sahihi za biashara na maarifa yanayohitajika kuanzisha na kukuza biashara yenye ushindani.

Hivyo aliwataka vijana kuona umuhimu wa elimu hii ili kuzifanya biashara zao ziendelee kupanuka na ziweze kuhimili ushindani katika soko.

Nihitimishe kwa kusema kuwa kama umefuatilia vizuri makala hii utakubaliana na mimi kuwa elimu ya ujasiriamali inahitajika na ina umuhimu mkubwa.

Hili linasisitizwa na Mjasiriamali mzoefu Ally Mbuyu ambaye anawahimiza wajasiriamali kuitafuta na kuipata elimu hii ili iwapatie uwezo wa kuanzisha, kuendesha, kuchambua na kutathmini mwenendo wa biashara zao, na kufanya marekebisho ikibidi.

Elimu hii itamjengea mjasiriamali uwezo wa kujiamini, kuhoji na kutambua fursa kwa uhakika.

Elimu hii itasaidia kufungua na kutanua akili zetu ili zifikie uwezo wa juu wa kufikiri na kutafakari mambo, kwa hiyo kila mtu anapaswa kuitafuta kwa bidii.

Katika makala zinazofuata nitazidi kuzama ndani katika kuhakikisha wasomaji wangu mnapata mambo mbalimbali mazuri zaidi kuhusu elimu hii muhimu.

Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasiriamali.

Anapatikana kwa e-mail: nzyy2001@gmail.com