Kijana – Ukigundua Mzazi Wako Hakukupatia Malezi Bora – Fanya Haya!

Ni raha iliyoje kuwa na mzazi anayewajibika kuhakikisha mwanae anapata stadi zote muhimu ili maisha yake yawe katika mstari sahihi. Je mzazi wako anafanya hayo?

Kimsingi, ni wajibu wa mzazi kumsaidia mtoto au kijana wake kuwa na taarifa au kukuza maarifa muhimu katika maisha yake. Na hili laweza kufanyika kupitia Stadi za Maisha. Haya ni maarifa ambayo yakitumika na kusimamiwa vizuri humjenga mtoto/kijana kuwa na mtazamo chanya kuhusu maisha yake binafsi na maisha yake ndani ya jamii.  

Stadi za Maisha ni moja ya masomo muhimu sana kwa mtoto/kijana kwani humpatia maarifa kuhusu anavyoweza kukabiliana na changamoto za maisha, na kupata uwezo wa kuziona fursa, na kuzikamata. Stadi hizi hujumuisha mbinu zinazoweza kumsaidia kuyafanya maisha yake yawe na uelekeo ulio sahihi, kujitambua, kuwa na nidhamu, na kufanya vitu sahihi, mahala sahihi na wakati sahihi.

Nimesema huu ni wajibu wa mzazi, kimsingi. Sasa, wapo wazazi waliokosa umakini wakajikuta wanazodolewa na watoto wao wenyewe, halafu wanaanza kulalamika; pale watoto wao wanapoanza kujitambua, kupata akili za ki-utu uzima, na kuanza kuhoji mambo. Watoto hawa hugundua kuwa udhaifu au upungufu wao katika maadili, kumbe umesababishwa na uzembe wa wazazi wao walioshindwa kutimiza wajibu.

Kiukweli wapo wazazi wanaojitahidi kuwalea watoto au vijana wao kimaadili lakini watoto hushindwa kuzingatia maelekezo, wakawa wakaidi, na kuishia kuharibika. Hii ni habari nyingine… inayopaswa kushughulikiwa ki-upekee. Lakini wapo pia wazazi, ambao kwa uzembe tu, huwafanya watoto wao wakose maarifa muhimu kwa maisha yao. Sasa, watoto wakijitambua, na wakagundua hili, mzazi hawezi kukwepa kuzodolewa!

Hapo zamani kidogo, katika jamii za kiafrika kulikuwa na mila zilizohakikisha mtoto kabla ya kuingia katika umri wa kiutu uzima anapata maarifa au stadi ambazo zinalenga kumfanya awe mwanajamii anayejielewa, kujitambua na kuwajibika. Kulikuwa na ‘shule maalum’ za malezi ya vijana, kupitia matamasha ya jando na unyago. Cha kusikitisha, mila hizi zinazidi kumomonyoka kutokana na kasi ya ‘maendeleo’ ya utandawazi.

Hivi sasa, kutokana na sababu kadhaa, baadhi ya wazazi hawapati nafasi, au hawajali, au labda hawamudu, kuwapatia watoto wao stadi hizi, na sasa baadhi ya vijana wameanza kulalamikia kuikosa haki yao hii. Wanawalaumu wazazi wao kwa uzembe au kushindwa kuwajibika.

Katika hili, kijana mmoja Alexis, anasema, “wazazi wangu walishindwa kunifundisha stadi muhimu za maisha, na sasa nimegundua kwa kuzikosa stadi hizo utotoni, naona nimepungukiwa vitu muhimu sana katika maisha yangu. Nilipowauliza kwa nini hawakujali kunipa maarifa hayo, walijibu kwamba hata wao hawakuwahi kufundishwa na wazazi wao. Nilisikitika!”

Kijana mwingine Gavin anasema, “najua wapo wazazi wanaowafundisha watoto/vijana wao stadi za maisha…lakini najua pia kuwa wapo ambao hawana muda huo kwa kuwa hata wao hawakuwahi kufundishwa, au hata kama walifundishwa…wao hawana uwezo wa kuwafundisha watoto wao, na hili ni tatizo! Hata hivyo, najua pia kuna watoto ambao ni wakaidi, hawataki kujifunza,…pamoja na jitihada za wazazi wao”

Akitoa maoni katika mdahalo mmoja, kijana Bitter anasema, “nimekuzwa na wazazi ambao msisitizo wao mkubwa ulikuwa kusoma kwa bidii ili nifaulu masomo yangu vizuri, na waliniambia kila mara, ‘elimu ndio kila kitu’! Kwa kuzingatia maelekezo yao, nimekuja kugundua kuna maarifa muhimu sana, nje ya darasa, sikuweza kuyapata, mfano ujenzi wa fikra tunduizi, uthubutu, ujasiri, uchambuzi, kutoa maamuzi, na uwezo wa kujitegemea.

Akionesha madhara mengine ya kunyimwa stadi hizi, Kijana Bitter anasema, “kuna kitu muhimu ambacho nimekuja kugundua hivi karibuni, ambacho kimenisononesha sana. Nimegundua sikupewa hata stadi zinazonigusa moja kwa moja; kama kufanya usafi, kuoga, kupika, kufua, na hata kupiga mswaki. Sikuwahi kufikiria kitu hiki zamani, kwamba vitu hivi kumbe huwa vinafundishwa na wazazi majumbani, inasikitisha!”

Kijana mwingine anasikitika kwa kusema, “jinsi ninavyokuwa mtu mzima na kuanza kutambua mambo ndivyo ninavyobaini kuwa wazazi wangu hawakuwajibika ipasavyo kwangu. Ukweli, hawakunipa zana au ‘silaha’ kwa ajili ya kuyajenga na kuyalinda maisha yangu. Kuna mambo nahangaika kuyafanya mwenyewe hivi sasa, ingawa ukweli napata wakati mgumu, na wazazi wangu hawana namna ya kunisaidia, wameshachelewa!”

Sasa, ukifuatilia maoni haya utakubaliana na mimi kuwa baadhi ya watoto wanaofika katika umri wa kiutu uzima wakiwa hawana stadi muhimu za maisha, hawakutaka kuwa hivyo. Walijikuta hivyo ukubwani na baadaye kugundua kuwa kumbe wazazi wao kuna kitu hawakuwafanyia. Hata hivyo vijana hawa hawapaswi kukata tamaa; na kuacha kufanya jambo. Wanapaswa kujiongeza.

Mchangiaji mmoja katika mjadala kuhusu suala hili anasema, “nawasikitikia na kuwapa pole vijana wote waliokosa stadi muhimu za maisha, kwa kuwa wazazi wao walishindwa kuwajibika. Hata hivyo, pamoja na wazazi kukunyima stadi hizi, angalau wape shukrani, kwani walikulea ukawa na afya njema, na pengine kuhakikisha umepata elimu nzuri ya darasani.”

“Kwa kuwa sasa wewe ni mtu mzima, na sasa unajitambua, na unatambua nafasi yako katika jamii, unapaswa kuchukua hatua haraka! Acha kulalamika na badala yake anza kujifunza mwenyewe vitu vyote ulivyovikosa utotoni. Hili linawezekana, na wapo waliobadili maisha yao kabisa hadi watu wakawashangaa!”

Anasema, “ni kweli kama mtoto, ulipaswa kupendwa, kupewa malezi bora, kufundishwa maadili n.k. Lakini kama hukupata bahati hii utotoni, usianze kulia-lia. Kubali hili limeshatokea, kilichobaki ni kufanya kitu. Cha kuzingatia ni kwamba stadi yoyote unayoihitaji sasa, ambayo hukuipata utotoni, jiwekee mpango na mkakati wa kuipata. Na hata wale waliopatiwa stadi hizi, bado kuna haja ya kujifunza zaidi ili kujenga umahiri.”

Hatua ya kuchukua: wakati kijana unaweza kuungwa mkono, na kusikitikiwa na kila mtu, pale utakapoonesha kusononeshwa na matokeo ya wazazi wako kushindwa kuwajibika na kukupatia maarifa muhimu kwa ajili ya maisha yako, kwa upande mwingine unapaswa kukumbuka msemo huu, ‘yaliyopita si ndwele, tugange yajayo’!

Ukishalijua hili, una wajibu sasa wa kulibeba jukumu hili wewe mwenyewe. Unapaswa kutafuta njia mbalimbali za kukupatia maarifa na stadi zote ulizozikosa. Uzuri, tayari sasa unajua unahitaji nini katika maisha yako, au unataka kuwa nani, na unataka kukuza vipaji gani, hivyo chukua hatua!

Wakati fulani inabidi tuwasamehe wazazi wetu kwa kushindwa kuwajibika. Wazazi wengine walijaribu kufanya walichoweza, kulingana na jinsi wao wenyewe walivyolelewa, habati mbaya hawakufikia viwango stahiki. Pamoja na hayo, ujumbe muhimu kwao ni kwamba wanapaswa kuujua ukweli huu, na kujifunza kwamba walishindwa kutimiza wajibu.

Mzazi anapaswa kujua kuwa suala sio kuzaa na kumleta mtoto duniani – hapana. Kilicho muhimu ni kuhakikisha kuwa mtoto, mapema kabisa, anasimamiwa ipasavyo ili aweze kuwa na maarifa na taarifa zote muhimu kumfanya awe kijana anayejitambua, kufanya mambo kwa usahihi na kuyamudu vyema mazingira yake. Asipofanya jukumu lake hili ajue atalaumiwa, ataaibika na atazodolewa!

Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasirimali kivitendo. Anapatikana kwa e-mail: nzyy2001@gmail.com; Simu 0718219530

Je, Ni Salama Kuanzisha Biashara Nyingi Kwa Wakati Mmoja?

Je unaweza kufuata njia zote kwa wakati mmoja? Labda!

Habari,

Makala ya leo inahusu mbinu za uendeshaji biashara. Kuna wakati nilimsikia mfanyabiashara mmoja akitoa ushauri kwa jamaa yake. Alimwambia: “Mfanyabiashara mzuri ni yule anayefanya biashara nyingi kwa wakati mmoja. Yaani, unatakiwa usitegemee biashara moja peke yake; unatakiwa uwe na vyanzo vingi vya mapato kwa wakati mmoja.”

Aliendelea kwa kusema: “Ukiwa na biashara nyingi, na unazifanya kwa pamoja, zinasaidiana kuingiza pesa, lakini pia zinakufanya usitetereke; kwani moja ikidorora, nyingine inakukomboa. Ukitegemea chanzo kimoja tu, ujuwe ukianguka ndiyo basi tena; umekwisha!”

Mjasiriamali ukiyasikia maneno haya harakaharaka, utaona ni maneno mazito, au siyo? Utaona huu ni ushauri uliojaa busara na nia njema kabisa; ukilenga kukuletea manufaa na kukuepusha na hatari katika biashara. Na wapo watu wengi tu wenye mtazamo huu; wasomi wa biashara, na fani nyingine; na wasio wasomi pia. Utasikia wakisema: “Usiweke mayai yote kwenye kapu moja, likianguka yote yanavunjika.”

Labda kuna ukweli katika mtazamo huu – lakini kuna tafiti zinazoonesha kuwa kuna tatizo mahala fulani.  Mwandishi mmoja anasema kwamba ni rahisi mtu kuanzisha biashara mpya kila baada ya muda fulani mfupi. Lakini swali la kujiuliza ni je, unapata mafanikio yaliyokusudiwa katika kila biashara? Mafanikio katika biashara ni pamoja na kumpatia mteja bidhaa au huduma bora; kuwapatia wadau mapato stahiki; kuwapatia wafanyakazi ujira bora; na kutengeneza faida ya kutosha.

Mtendaji Mkuu wa Kampuni ya Apple, Tim Cook aliwahi kusema: “Moja ya kanuni ambazo Steve Jobs alisisitiza  katika Kampuni hii ni umuhimu wa kuwa focused, yaani kujikita katika kufanya kile unachoweza kufanya vizuri sana.” Kumbuka, Marehemu Steve Jobs ni mwanzilishi mwenza, na baadaye Mtendaji Mkuu wa Apple.

Kwa mujibu wa Tim Cook, Steve Jobs alisisitiza hili kwa kusema, “Ni rahisi kuongeza biashara zaidi, lakini ni vigumu kubakia focused.” Maana ya kuwa focused, kwa mujibu wa Jobs, ni kusema ‘hapana’ kwa mawazo mia kadhaa yanayozunguka kila mara ndani ya akili yako; hata baada ya kuchagua kwa umakini wazo moja zuri uliloamua kulifanya ki-vitendo.

Tunaambiwa kwamba, Steve Jobs hakujishughulisha na wingi wa vitu anavyofanya, kwa mfano, umezalisha au umeuza vipande vingapi vya bidhaa, hapana! Yeye alijishughulisha zaidi na kufanya ‘kitu fulani kilicho bora’, hata kama ni kimoja tu.

Wafanyabiashara wengi wakubwa wamejikita katika jambo moja, wakijitahidi kulifanya jambo hilo kwa ubora zaidi kila siku. Angalia wafanyabiashara hawa wakubwa: Henry Ford alijikita kutengeneza magari; Pablo Picasso alijikita katika sanaa ya uchoraji na rangi; Bill Gates alijikita kwenye uzalishaji wa software; na Mark Zucherberg amejizatiti katika Facebook.

Kitu cha kuzingatia hapa ni kwamba, hawa wamefanikiwa kwa viwango hivyo kwa sababu walikuwa focused. Walikuwa na hamu, motisha  na mshawasha wa kupata kwanza hicho kimoja walichokuwa wanakipenda na kukimudu zaidi.

Tunaambiwa kuwa, wafanyabiashara wachache wakubwa unaowaona wanafanya biashara au wana Kampuni zaidi ya moja, mfano Mzee Reginald Mengi, Tanzania, hawakuanzisha biashara zote kwa pamoja. Walianza na moja, wakaipa uhai hadi ikaweza kusimama vizuri peke yake, ndipo ikaanzishwa nyingine.

Mfano mwingine ni Bw.Richard Branson. Tajiri huyu Mwingereza, kwa miaka kumi na tatu, aliifanya Kampuni ya Virgin ijishughulishe na muziki tu, Virgin Records, kabla ya kujitanua baadaye hadi kuanzisha Kampuni za usafirishali na nyinginezo.  

Ushauri unaotolewa hapa ni kwamba kufanya biashara nyingi kwa wakati mmoja inaweza kuonekana ni mbinu au ujanja wa kupunguza vihatarishi au risk ya kile kinachosemwa hapo juu kwamba, ‘Usiweke mayai yote kwenye kapu moja,…….’ Lakini upo ushahidi unaoonesha kuwa wafanyabiashara waliojaribu kufanya biashara nyingi kwa wakati mmoja, ama biashara zote zilidhoofika au zilikufa.

Tatizo kubwa katika hili ni kwamba mfanyabiashara anapoanza kufanya jambo moja na kabla hajaliwezesha kumpatia tija sahihi tayari amerukia jambo jingine – huyu anakosa maono na mwelekeo. Anakosa focus na hivyo anaanza kutangatanga asijuwe lipi alifanye, alifanye saa ngapi, na kwa kiwango gani.

Kukibwa zaidi ni kwamba rasilimali zinazohitajika kufanya haya zinaanza kugawanyika vipande vipande. Rasilimali hizo ni fedha, muda, akili, wafanyakazi, vifaa, majengo n.k. 

Utakuta kila biashara mpya inayoanzishwa, kabla ya ile ya kwanza kukomaa, ina tabia ya kutaka kujitwalia rasilimali hizi na kujimilikiasha yenyewe, na hivyo kuzinyima pumzi biashara zilizotangulia. Hapa, baada ya muda rasilimali zinakuwa kidogo kutosheleza mahitaji ya kila biashara, na hapo ndipo biashara zote zinakonda na kufa!

Mwandishi mmoja anasisitiza hili kwa kusema: “Angalia vitu kadhaa ambavyo vinamgusa mtu, au watu wanavipa umuhimu mkubwa, mfano mapenzi, kujali, umakini n.k. Jinsi unavyovitawanya vitu hivi kwa watu wengi zaidi ndivyo jinsi unavyofanya thamani yake ipungue.”

Kwa kumalizia, tunashauriwa kuwa focused. Yaani, tusihangaike huku na kule wala kuondoa macho katika fursa iliyo wazi mbele yetu. Hivyo, jitahidi kuweka mkazo, macho, akili,  nguvu na rasilimali zote katika fursa moja yenye uhakika wa kukupatia faida kubwa, mpaka uikamate vizuri na kuyaona bayana matokeo yaliyokusudiwa.

Baada ya kufanikisha biashara moja vizuri, basi hapo unaweza kuanzisha nyingine; ukiwa tayari umeshakusanya rasilimali mpya za kutosha kuanzisha na kuendesha biashara mpya kwa tija, bila kuiathiri biashara yako ya mwanzo.

Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasirimali kivitendo. Anapatikana kwa simu: 0718219530; e-mail: nzyy2001@gmail.com

Hii Ndio Njia Bora Zaidi Ya Kumwadhibu Mtoto Ili Kumjenga Kimaadili

Wapo wanaoamini kuwa fimbo au viboko ndio mwarobaini wa ujenzi wa maadili ya mtoto

Habari,

Malezi bora ya watoto ni jambo muhimu sana; na lazima kila mzazi alizingatie. Malezi humkuza mtoto kuwa na maadili bora, na kumfanya aishi vyema katika jamii yake. Mtoto akilelewa bila maadili huwa kituko na machukizo kwa wazazi na jamii nzima. Watu hutumia njia nyingi kuwalea watoto wao. Kwa mfano, mtoto akikosea wapo wazazi ambao hutumia njia ya kipigo ‘kumrudi’, na wengine hutumia zaidi maelekezo. Je, ni njia ipi yenye tija zaidi?

Kuna mjadala ulifanyika katika mtandao mmoja wa kijamii uliohusu jinsi bora ya kumwadhibu mtoto nyumbani. Nilivyoutafakari, ulikuwa ni mjadala wenye lengo la kuwasaidia wazazi ili wapate taarifa na maarifa sahihi ambayo wakiyatumia watalifanya jambo hili kitaalamu zaidi na bila jazba; ili kuwasaidia kufanya malezi yenye manufaa kwao wenyewe, kwa mtoto, na jamii nzima.

Katika mjadala ule, wapo waliochangia uzoefu wao binafsi, na wengine walichangia kwa kutumia utaalamu na elimu walizosomea, nakadhalika. Kwa muktadha wa makala haya, sitatumia majina yao halisi.

Kwa mtazamo wa Atanasio, viboko vina nafasi katika kumjengea mtoto maadili, lakini anasisitiza kwamba vitolewe kwa makosa makubwa tu. Anasema, “mimi naona ili mtoto anyooke ni lazima awe na hofu ya wazazi ‘kuwa mbogo’ akikosea. Hili linamsaidia kujiepusha na uzembe au ukorofi. Adhabu ya viboko inafaa kwa makosa makubwa, yanayoweza kuleta hasara kubwa; na itolewe kwa uchache sana ili mtoto asijenge usugu

Dolifia anasisitiza kwamba viboko ndio adhabu sahihi kwa mtoto mkosefu. Anasema, “mimi mtoto akikosea simlei-lei. Nampiga mkwala mzito hadi aone ‘stimu-stimu’; na kama kosa ni kubwa sana ajiandae kula viboko hadi 10 matakoni mpaka ashike adabu! Mimi ‘sipendagi’ ujinga…na watoto wangu wanalijua hili!”

Anasema, “unajua, watoto wengine ni wabishi, wakaidi na hawasikii. Mimi ninae wa hivi; hivyo huwa namkanya siku ya kwanza tu. Ikizidi hapo anapokea ‘mboko’ hadi anasikia kizunguzungu! Mimi mwenyewe nimekula ‘mboko’ za kutosha, hivyo mtoto ‘akizingua’ anapata habari yake!”

Zuberi pia anaamini katika adhabu ya kuchapa. Hata hivyo yeye anasisitiza aina ya uchapaji. Anasema, “nakubali mtoto anaweza kuchapwa, kama ametenda kosa kubwa au amerudia kosa alilotenda na akaonywa. Hata hivyo sikubaliani na wazazi wanaowachapa watoto wao bakora kama mvua, au wale ambao hudiriki kutumia ngumi, mateke au makofi.”

Anasema mtoto akichapwa fimbo tatu matakoni huku akifafanuliwa kosa lake ataelewa tu! Baada ya kukiri kosa, na kuahidi kutorudia, mzazi anapaswa kuingiza urafiki haraka; ili mtoto ajue kwamba nia ya mzazi ni kumjenga na sio kumkomoa.

Hamadi, yeye anaamini katika mazungumzo na viboko. Anasema, “mwanangu akifanya kosa huwa namkanya, kumuelimisha na kumtaka asirudie. Huwa nasamehe kosa la kwanza na la pili. Nikiona mtoto harudi kwenye mstari – hapa ‘mboko’ lazima zihusike!”

Hata hivyo anasema huwa hamchapi mtoto kwa kumkomoa. Huwa analenga kuboresha tu. Na mara nyingi humchapa mtoto baada ya kumfafanulia kosa na akaelewa; na ukweli huwa harudii. Hamadi huufanya mkakati huu kuwa kitu endelevu, kwani kukosea kwa mtoto (hata mtu mzima) ni kitu kinachotokea mara kwa mara.

Kwa upande mwingine; Yunus anasema kwamba yeye haamini kwamba kumchapa mtoto ndio njia ya kumjengea maadili. “Mimi huwa situmii viboko, wala kufoka-foka ovyo! Mwanangu akifanya kosa huwa napenda ajue madhara yatokanayo na uzembe au kitendo kibaya alichofanya; na hili huwa nalifanya kwa kwa upole, lakini kwa msisitizo mkubwa, ili liendelee kuzunguka katika akili yake.”

Tusiime anasema yeye hutumia zaidi mbinu za ki-mahakama. “Mimi, mtoto akikosea huwa namhoji ili nihakikishe kama amelijua kosa lake. Nikithibitisha amekosea, humpa nafasi anieleze kwa nini amefanya kosa hilo; na anadhani anastahili adhabu gani. Muda wote huu huwa namsikiliza kwa umakini. Mara nyingi watoto wangu huonesha kujutia makosa yao na kuomba msamaha. Mchakato huu umenisaidia sana kuwafahamu vizuri, na kuwajengea umakini na nidhamu.”

Steve, yeye pia, haamini katika viboko. Anasema, “mimi nina watoto wawili, mmoja ana miaka 7 na mwingine miaka 10. Nimewalea tokea utoto wao tuwe marafiki. Hata hivyo nimewaweka wazi kuwa urafiki huu utapotea wakati wowote wakinikosea kijinga. Najua hakuna mtoto asiyefanya makosa, hivyo mtoto wangu akikosea kwa mara ya kwanza, huwa namwita na kumfafanulia kosa alilofanya na madhara yake, kirafiki kabisa, halafu humuuliza kama ameelewa.”

“Akisema ameelewa, tunawekeana ahadi ya kutokurudia; na kwamba akirudia ‘urafiki’ wetu utapotea. Na kweli; akirudia kosa hilo au kufanya uzembe mwingine, huwa nabadilika na kuvaa sura tofauti! Hili limenisaidia sana kuwajenga ki-maadili, kwani watoto wangu hawakuzoea kuniona nikiwa na hasira. Kwa hiyo aliyefanya kosa, haraka sana, hugalagala chini akiomba msamaha; na kuahidi kutorudia tena.”

Alexanda pia anaona adhabu ya viboko haina mashiko! Anasema, “kwa uzoefu wangu, siamini kama adhabu ya viboko inaweza kumjengea mtoto maadili mema. Mimi nikiwa mdogo, kila kosa nililofanya nilichapwa, tena sana! Kuna wakati nilichapwa bila hata kujua nimekosa nini, au ubaya wa kosa lenyewe. Ukweli viboko havikunisaidia bali vilinijengea usugu tu; nikawa mbaya zaidi.”

“Nilipopata watoto, nilianza kutafakari aina ya malezi niliyopewa na wazazi wangu, nikagundua walikosea sana! Kwa hiyo mimi nimewalea watoto wangu bila viboko; natumia zaidi mazungumzo. Naanza na mtoto akiwa mdogo, kumuelekeza, kirafiki, lipi jema na lipi baya, kila siku; na hapa ndipo wazazi wengi hukosea katika malezi…hawaanzi mapema!”, anasema.

Anasema, “mtoto akikosea, haraka sana, namfahamisha alichokosea na ubaya wake; na kumtaka aombe radhi kwa kutamka kosa, ubaya wake, na madhara. Akifanya hivyo namwambia, kwa msisitizo, ‘nimekusamehe na usije kurudia’! Hili limenisaidia sana kuwafanya wanangu wawe watoto wema sana!”

Kwa mujibu wa Mwanasaikolojia Amy Morin, kuwaadhibu watoto kwa viboko ni jambo linalozua mijadala dunia nzima. Anasema, wakati wataalamu wengi wa Malezi ya Watoto hawaamini katika adhabu hii…ni wazazi wachache sana ambao wanakiri kuwa hawajawahi kuwachapa watoto wao. Hii inaonesha kuwa wazazi wengi wanaona mtoto hawezi kuwa na maadili mema bila fimbo!

Hata hivyo, wataalamu wa Malezi wanasema kuchapa ovyo watoto sio njia sahihi ya kuwajengea maadili mema. Inatakiwa mtoto anapokosea aelimishwe na kutengenezewa kanuni za kufuata. Ikitokea akakosea akumbushwe; na huu ni wajibu wa kila siku wa mzazi hadi amjenge mtoto kuwa raia mwema.

Wataalamu hawa wanasema ni jambo jema kwa mzazi kujenga tabia ya kukaa karibu na watoto wao; kuongea nao kirafiki, tena kwa msisitizo, kwa lengo la kuwaelekeza mema ya kufanya na yasiyo mema ya kuepukana nayo. Watoto waliolelewa hivi, huwa wanashika miongozo ya wazazi, na mara nyingi nafasi ya kufanya makosa huwa ndogo. Watoto hawa hujengewa uwezo wa kujitambua na kuyaelewa matakwa ya wazazi na jamii zao. Mazingira haya huwafanya wajenge tabia ya kuuliza-uliza ili kupata ufafanuzi, au kuwa waangalifu; kwa kila wanachotaka kufanya.

Pamoja na hayo, wapo watoto ambao kwa maumbile yao ni waadilifu, wapole na wanajielewa tokea utoto wao. Fikiria mtoto anakosea halafu, haraka sana, anagundua kakosea na tayari keshakuja kwa mzazi kwa unyenyekevu na majuto kuomba msamaha; na kuahidi kutorudia!

Mtoto huyu anajitambua! Mtoto wa hivi ukiamua kumchapa fimbo unamtoa katika reli, asiweze kujitambua mwenyewe; bali ajitambue kwa mabavu ya mzazi. Mazingira haya humnyong’onyeza mtoto na kumfanya ajenge nidhamu ya woga; ambayo haimjengei hulka ya kujiamini.

Kwa mujibu wa Mwanasaikolojia Octavio, njia bora kabisa ya kumjenga mtoto ki-maadili ni kumtengenezea mfumo utakaomfanya ajenge tabia ya kupenda kufanya mambo mema. Anasema mtoto apewe vichocheo vitakavyobadilisha fikra na matendo yake kuelekea kupenda kutenda mambo mema.

Vichocheo hivi ni pamoja na zawadi (rewards) au pongezi; kila mtoto akifanya jambo jema. Hili linamsaidia mtoto kujikita zaidi (ku-focus) kwenye vitu ambavyo wakivifanya watapata manufaa kutoka kwa wazazi au jamii; kuliko kupoteza muda mwingi katika kusisitiza tabia mbaya ambazo watoto wanatakiwa kuziacha.

Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasirimali kivitendo. Anapatikana kwa e-mail: nzyy2001@gmail.com; Simu 0718219530

Zijue Sababu Zinazowafanya Wastaafu Kusota Uzeeni -3

Je, ukistaafu utakuwa na furaha kama huyu jamaa?

Habari,

Katika makala ya wiki iliyopita tulimalizia kwa kujadili sababu ya tatu, ambayo inahusu wastaafu kuendekeza ‘matanuzi’ na anasa, na hivyo kujiandalia maisha ya taabu wakistaafu. Tuendelee sasa kujadili sababu nyingine.

Nne, mahusiano mabaya ya Wanandoa. Kuna uhusiano mkubwa kati ya maisha baada ya kustaafu na mahusiano ya wanandoa kabla, na baada ya kustaafu. Kwamba mstaafu ataishi maisha mazuri au atasota, akistaafu, inategemea sana mahusiano kati ya wanandoa.

Katika hali ya kawaida kijana anapoajiriwa, baada ya muda angependa kuwa na mwenza (mke/mume). Sasa, wataalam wa Saikolojia wanasema vijana wengi huingia katika mahusiano, hadi ndoa, kwa kusikiliza zaidi hisia tu! Ni hisia zinazochochewa na mvuto wa nje, kwa msichana/mvulana, unaoitwa ‘romantic love’.

Wanasema ‘romantic love’ huzaa mshikamano mkubwa sana mwanzo, lakini baada ya muda, vile vitu vilivyokuwa sababu ya ‘stimu’ huanza kuonekana vya kawaida; na hapo ndipo mshikamano huanza kulegea. Wawili hawa huanza kugundua kuwa kuna mambo mengi ya msingi hawaivi. Kile ulichokuwa unavutiwa nacho kikiondoka, mapenzi nayo huondoka, na hapo ndipo mivutano na migogoro huanza kumea.

Yakitokea haya, mahusiano ya ndoa huanza kumomonyoka na mapenzi hugeuka kuwa ugomvi na mitafaruku isiyoisha. Katika mazingira haya, siyo rahisi mipango ya maana kufanywa. Nani hapa atakuwa na muda wa kujenga mawazo ili kuziona fursa za biashara? Mazingira haya hayawezi kujenga fikra za kuweka akiba wala kuwekeza, kwani matumizi ya ovyo hutamalaki. Haya hutokea kabla au hata baada ya kustaafu, na huwa chanzo kikubwa cha umaskini.

Wafanyakazi wengi hulalamika kushindwa kuendesha biashara kwa kukosa mtaji au msimamizi bora, wakati mke au mume wake yupo, na pengine hana kazi. Sababu mojawapo kubwa ni hiyo hapo juu! Ukiwa na mwenza asiye na upendo wa dhati, weledi wala bidii, sio rahisi kufanikisha malengo yako. 

Lakini pia, mahusiano mabaya ya wenza yana nafasi kubwa ya kuwagawa hata watoto; hivyo kuwanyima malezi bora. Watoto hugawanyika; wakawepo wa baba na wa mama. ‘Mtoto wa mama’ atafuata zaidi maelekezo ya mama, kiasi cha kuweza kukubali hata kumwibia, kutumia pesa ovyo, au kuhujumu miradi ya baba, kwa lengo la kumkomoa; ili tu kumridhisha mama,..na kinyume chake.

Wanasaikolojia wanasema mapenzi ya kweli, yanayoleta mahusiano ya kudumu, siyo ‘romantic love’. Ni mapenzi yanayotokana na ‘shared values’; yaani vile vitu vya msingi ambavyo kila mmoja anavikubali na kuviamini kwamba ndivyo vinatengeneza gundi kati yao. Kwa mfano; imani na kumcha Mungu, mawasiliano thabiti, uaminifu, staili ya maisha, matumizi ya fedha, mipango ya maendeleo, utayari wa kubeba majukumu, nakadhalika.

Kwa hiyo, iwapo uchaguzi wa mwenza utaufanya vizuri, kwa kuzingatia ‘shared values’, ndoa hii itajaa heshima, maelewano, na majadiliano; kuwezesha  kupanga na kuweka mikakati ya maendeleo ya familia. Na kama ulishakosea kuchagua, ‘ukathamini harusi badala ya ndoa’, ni vyema umshirikishe Mungu, ili aweke mkono wake; kwani bila maelewano ya kweli maisha kabla na baada ya kustaafu huwa ya mashaka makubwa.

Tano, mzigo wa majukumu ya ki-familia. Wapo wafanyakazi ambao huamua kuzaa sana. Sawa,..kuzaa siyo dhambi! Lakini ieleweke kwamba ni jukumu la mzazi kuhakikisha anawasaidia watoto wake hadi waweze kuendesha maisha yao. Hapa kuna gharama za elimu, afya na mahitaji mengine.

Wapo wengine ambao, mbali na watoto wake, hupewa kulea ndugu au watoto wa ndugu, ili ‘kuwavusha’ pia, kwa kipato hicho hicho. Hili nalo ni jema tu! Lakini, jukumu hili siyo dogo, na mara nyingi huendelea hadi baada ya kustaafu, na huwayumbisha wafanyakazi hawa, kazini na hata baada ya kustaafu, na kuwadidimiza sana kiuchumi.

Katika mazingira haya mfanyakazi unatakiwa kujenga umakini mkubwa. Kwanza unatakiwa kubuni mbinu za kujiongezea kipato, ili uongeze uwezo wa kumudu gharama hizo. Halafu; wape maarifa na uwezo mke, ndugu na watoto unaowalea ili wakusaidie katika kukuza kipato chako; kila mmoja kwa kadri ya uwezo wake. Yaani asiwepo mtu wa kukaa bila kitu cha kufanya, kama yupo nje ya shule/chuo.

Jifunze kubana matumizi, na kuepuka anasa, ili uweze kukuza mtaji utakaokuwezesha kuendesha miradi utakayoanzisha. Anzisha vyanzo vingi vya mapato ili visaidiane kuongeza kipato cha familia. Lakini pia punguza gharama za kusomesha kwa kuchagua shule/vyuo vyenye unafuu. Ukishindwa kufanya haya, safari yako ya kuelekea kustaafu itakuwa yenye mashaka.  

Sita, wastaafu kujichanganya na waliobaki. Kujichanganya na kubakiza mawasiliano/mahusiano na wafanyakazi, mahala ulipotoka, ni jambo zuri sana. Uliowaacha kazini wana taarifa na maarifa ambayo ukiyafanyia kazi yanaweza kuboresha shughuli/biashara zako, na huenda wao ndio wakawa wateja wako wa kwanza.

Hata hivyo, uangalifu mkubwa unahitajika, kujua staili itakayotumika katika kujichanganya. Kwa mfano, wapo wastaafu wenye tabia ya ulevi, wanaochukulia kujichanganya kama ile hali ya kukaa na ‘wadau’ katika vikao vya starehe; huku wakipiga ‘kilaji’. Sijasema ukistaafu hauruhusiwa kustarehe, hapana! Nasema tumia akili, kwani kuna starehe za maana na zingine za ovyo!

Ninachosisitiza hapa ni kwamba hao ‘wadau’, unaokaa nao hapo kijiweni, kustarehe, bado wanalipwa mshahara na marupurupu kadhaa. Wanakuweka karibu wakijua kwamba hapo ulipo una ‘mpunga’ wa mafao. Hivyo, wanachofanya wao, ni ‘kuanzisha safari’ kwa kukupa ofa, wakijua ‘majibu’ yako yatakuwa ya uhakika!

Wakati wao wanatumia pesa za safari, wewe unajitutumua kwa mafao ya kustaafu! Hali hii ikiendelea, muda si mrefu mafao yatakauka; na hutaamini macho yako utakapoona ‘wadau’ waliokuchangamkia siku zote, wanaanza kukukwepa, na pengine kukusengenya.

Na hapo ndipo mtu mzima hukutwa akiongea peke yake. Yakitokea haya kinachofuata sio umaskini tu, baada ya kustaafu,..lakini pia magonjwa yanayohusishwa na ‘stress’ huanza kuibuka, kama presha na sonona; na mwisho wake huwa mbaya!    

Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasirimali kivitendo. Anapatikana kwa e-mail: nzyy2001@gmail.com; Simu 0718219530

Zijue Sababu Zinazowafanya Wastaafu Kusota Uzeeni -2

Wastaafu hupatwa na masaibu mengi…maandalizi ya mapema na umakini ni muhimu sana

Ndugu mstaafu mtarajiwa, huu ni mwendelezo wa makala ya wiki iliyopita ambapo tunajadili sababu zinazowafanya wastaafu wengi wafilisike, waishi maisha duni uzeeni, na pengine waishi muda mfupi baada ya kustaafu. Tulijadili sababu ya pili; kwamba “wastaafu ni ‘target’ ya matapeli”, naomba tuendelee…

Matapeli hawa, wengine ni marafiki au hata ndugu, wana mbinu nyingi za kuwanasa wastaafu. Mojawapo ni kuanzisha au kuboresha urafiki na mstaafu mtarajiwa. Huitumia mbinu hii kama mtaji wake, na akishajua tayari umestaafu, huja rasmi kukuletea ‘mchongo’, na kukushawishi jinsi utakavyonufaika na ‘uwekezaji’ huo. Na hapo ndipo wastaafu wengi huishia ‘kupigwa’!

Matapeli hufanikiwa kuwanasa wastaafu kwa sababu wamegundua wazee wengi, kwa kukosa maarifa stahiki, hushawishika kiurahisi kuwaamini vijana wanaoonekana werevu, wachacharikaji, na wenye mikakati; wakiamini kupitia kwao wataziona fursa, na hivyo wakiingiza pesa zao zitaleta manufaa.

Kitu kingine ni kwamba wastaafu, kwa uzee wao, na pengine uzoefu mdogo wa kushika fedha, huziona fedha za mafao kuwa nyingi sana. Na wakishawishiwa kwa mfano, kutoa nusu ya mafao yao, kwa ajili ya ‘mchongo’ fulani, bado fedha zinazobakia huonekana nyingi tu, ambazo ‘haziwezi kwisha hivi karibuni’. Cha ajabu; kufumba na kufumbua, akaunti inasoma sifuri!  

Kuepukana na matapeli, kwanza kabisa elewa kuwa kuna matapeli! Halafu jifunze kutilia shaka urafiki au mazoea ya kulazimisha ya watu, hata wa karibu, katika kipindi cha kustaafu; wakikushawishi utumie kiasi kikubwa cha fedha mara moja, katika ‘mchongo’, ili ujizolee faida kubwa haraka.

Jiepushe na watu usiowajua, au hata unaowajua; wanaokushawishi, hasa kwa simu, au njia nyingine, utoe taarifa za akaunti zako za benki au simu. Hawa watu mara nyingi wana nia mbaya. Ili kupata ukweli wowote kuhusu akaunti zako, nenda mwenyewe benki au ofisi za mtandao husika wa simu, uongee nao. Mbinu kubwa zaidi ya kuepukana na haya ni kujenga maarifa stahiki, ndani ya ajira.

Tatu, sababu nyingine inayowafanya wastaafu kusota uzeeni ni kuendekeza ‘matanuzi’ au anasa. Umaskini unaotokana na hili, tunaweza kuuita umaskini wa kujitakia. Watu wa aina hii ni wale wasiopenda kujinyima au kujipa shida, na mara nyingi, pengine kuanzia mwanzo wa ajira zao, huwa wana matumizi yasiyo ya lazima, yasiyolingana na vipato vyao.

Mtafiti mmoja anasema: “Asilimia 46 ya familia za wastaafu hutumia, kwa mwezi, kiasi kikubwa zaidi cha fedha, kuliko kilichotumika wakati mstaafu akiwa kazini.” Ukiyachunguza matumizi haya utakuta yanachochewa na kitu kiitwacho ‘show-off’ (kujionesha), au ulimbukeni!

Wastaafu wengine wakipata mafao hujiona kama ndio wamezaliwa leo. Wapo ambao huwekeza fedha zao katika anasa au uzumbukuku mwingine wa maisha, kwa kukosa maarifa na nidhamu. Nawafahamu wastaafu waliowekeza katika ulevi, ufuska na ununuzi wa vitu ghali, visivyo na umuhimu, kwa lengo la kuwakoga watu. Tunaaswa, matumizi juu ya vipato vyetu ni hatari, na mwisho wake ni kufilisika au madeni.

Angalia, wapo wafanyakazi ‘hulikoroga’ wenyewe. Wengine, wakiwa kazini, hujitengenezea bomu linalowalipukia wanapostaafu. Na wengine hujitengenezea bomu wakiwa tayari wamestaafu. Kwa kutaka kujitutumua tu, wapo wafanyakazi ambao hujiingiza katika mikopo ya hatari, yenye riba kubwa, ili-mradi wamiliki vitu wanavyovitamani. Sio kosa kutamani kitu, kosa ni kukurupuka!

Mfanyakazi; unamuona rafiki, jirani au mfanyakazi mwenzio anamiliki ‘gari kubwa’ au ‘nyumba kubwa’. Sawa, wala sio kosa kumiliki gari au nyumba, hivi ni vitu muhimu. Tatizo ni kwamba, bila kujua siri nyuma ya mali zile, na sababu hasa ya umiliki wa mali hizo, tayari na wewe unataka sasa hivi! Kwa sababu hutaki kupitwa!

Sasa, wengi bila tahadhari hujikuta wamejiingiza katika mikopo yenye riba kubwa, wanayoilipa kwa muda mrefu, kiasi cha kuwafanya waishi kwa kubangaiza na kukosa akiba; na hivyo kushindwa kufanya uwekezaji wowote ndani ya ajira, ikiwa ni maandalizi ya maisha ya kustaafu.

Kwa upande wa ‘gari kubwa’ kuna gharama ambazo watu huwa hawazifikirii kabisa mwanzoni; kama mafuta, vipuli, matengenezo, bima, leseni nakadhalika. Ni baada ya kuingia barabarani ndipo ‘mwiba’ huu huanza kuchoma mguu! Gharama hizi zote hutakiwa zitoke katika mshahara wa mfanyakazi, na hili huanzisha safari ya msoto uzeeni.

Hata wanapostaafu; wapo wafanyakazi ambao hukimbilia kununua ‘magari makubwa’ bila sababu ya msingi. Sisemi gari halina maana, hapana. Cha muhimu ni kujua unalinunua hasa likusaidie nini, ni gari la aina gani na unalinunua kwa gharama gani. Magari mengine ni rahisi kununua lakini ni ghali sana kuyaendesha. Je una taarifa hizi?

Hata nyumba, nilikuwa karibu (urafiki) na mstaafu mmoja aliyeniambia, “nimepata mafao yangu, sasa nakwenda kujenga ‘nyumba ya ndoto yangu’…’’. Ni kweli alijenga nyumba hiyo, tena ya kuishi tu. Hakutaka kuishi pembeni ya mji, hivyo alinunua kiwanja mjini, kwa bei kubwa.

Alitaka nyumba kubwa…vyumba vinne vikubwa vyenye huduma zote, sebule mbili zinazoweza kubeba seti mbili mbili za masofa, jiko kubwa, chumba cha chakula, valanda mbili, na ukuta mkubwa kuzunguka kiwanja chake. Ukweli alimaliza kujenga nyumba hiyo, akanunua na gari; lakini yaliyofuatia yanasikitisha.

Alimaliza mafao yake yote, asibakiwe na fedha yoyote ya maana kwa ajili ya kujiingizia kipato endelevu, akaishia kuishi kimaskini ndani ya jumba la kifahari. Unajua kilichofuata?

Aliweka gari mnadani, na lilinunuliwa kwa nusu ya bei yake halisi, na bado hakuweza kuanzisha mradi wowote, kwani hakuwa na maarifa hayo, na kibaya zaidi tayari alishaanza kupakini! Hii ni sababu ya tatu, kwa nini wastaafu wengi huishia kusota uzeeni. Tutajadili sababu nyingine katika toleo lijalo. 

Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasirimali kivitendo. Anapatikana kwa e-mail: nzyy2001@gmail.com; Simu 0718219530

Hizi Ndizo Sababu Zinazowafanya Wastaafu Kuhangaika Uzeeni -1

Uchapakazi na uzalendo kazini ni jambo muhimu sana kwa mtumishi, lakini…….!

Habari

Leo nimepanga kuongea na wewe mstaafu mtarajiwa. Naomba nianze kwa kukuuliza je, umewahi kujiuliza kuwa utafanya nini baada ya kustaafu? Je, umejipanga vipi kuishi maisha tofauti na uliyoyazoea kwa miaka mingi ukiwa kazini? Kama huna unachopanga au kufanya, kuhusu maisha yako ya uzeeni, ni wazi unajiandalia matatizo/masaibu huko uendako.

Baada ya utangulizi huo, naomba sasa nijadili masaibu yanayomkabili mstaafu, sababu zake, na njia za kujiepusha nayo. Eneo hili linahusu mambo yanayofanya maisha ya mfanyakazi, baada ya kustaafu, yawe duni, yasiyo na amani, furaha wala heshima. Lengo hapa ni kutoa mafunzo ambayo yanaweza kumuepusha mfanyakazi na makosa ya watangulizi wake, ili achukue tahadhari mapema. Naomba nianze na sababu zinazowafanya wastaafu wengi kusota uzeeni.

Wastaafu, wengi tu, hupatwa na masaibu mengi. Wapo ambao huyaweka wazi yaliyowakuta, na wapo ambao masaibu yao hujionesha wazi kwa kila mtu kuona. Wengine hubakiza masaibu yanayowapata kuwa siri yao, na wengine hufa na siri hizo. Itoshe tu kusema kuwa kuna upande mmoja wa maisha ya kustaafu una shida!

Mstaafu mmoja anasema, “ mimi nilistaafu mwaka 2013, nikapewa mapema tu, shilingi milioni 68. Pamoja na kwamba nilishajenga tayari, nyumba ya kuishi, na nilishamaliza kusomesha watoto…huwezi kuamini; mafao haya yaliisha ndani ya mwaka mmoja tu, ndipo nikagundua kuna tatizo mahali fulani. Nikaanza kufikiri…huenda hata mfumo wetu wa elimu una walakini, yaani pengine kuna vitu fulani muhimu hatufundishwi!”

Kuna utafiti mmoja uliofanyika Marekani unasema asilimia 38 ya wafanyakazi wanaokaribia kustaafu huko, hawana imani au matumaini kama wataishi maisha ya furaha na amani watakapostaafu. Sijui utafiti huu ukifanyika Tanzania asilimia itakuwa ngapi; kwa sababu wenzetu kwanza wana mifumo imara ya hifadhi ya jamii, lakini pia wengi wana bidii ya kutafuta maarifa, na nidhamu katika kuweka akiba na uwekezaji; wakijiandaa kustaafu.

Waandishi kadhaa wametoa sababu…zinazowafanya wastaafu wengi wafilisike, waishi maisha duni uzeeni, na pengine waishi muda mfupi sana baada ya kustaafu, na nitajadili hapa:

Kwanza, ‘uadilifu na uzalendo’ wa mfanyakazi kwa Mwajiri. Hili linatia ukakasi kidogo, au siyo? Uadilifu na uzalendo ni sifa ambazo mfanyakazi ukiwa nazo unakuwa mfano wa kuigwa, na kila mwajiri hupenda kuwa na watu hawa kiwandani kwake. Waajiri huthamini sana watu waadilifu, wanaojituma na wanaojali muda. Sasa mbona leo sifa hii inageuka kuwa kitu kisichofaa? Nitaeleza!

Mara nyingi watu waadilifu huutumia muda wao kazini ‘vizuri sana’. Wapo ambao huingia kazini mapema sana, wengine saa moja au zaidi, kabla ya muda uliopangwa, na huondoka kazini saa kadhaa baada ya muda rasmi wa kuondoka; wakiwa wanatekeleza wajibu wao kazini, ikiwa ni pamoja na kumalizia viporo vyao vya kazi.

Nitoe angalizo hapa: mazingira ya kazi na taratibu zake zinatofautiana sana, kutoka mwajiri mmoja hadi mwingine, hivyo kila mfanyakazi anawajibu wa kuyasoma vizuri, kuomba ufafanuzi, na kuyajua mazingira na taratibu za mwajiri wake, ili ajipange ipasavyo.

Sasa, kama wapo wafanyakazi waadilifu; wapo pia ‘waajiri waadilifu’. Waajiri hawa huwajali sana wafanyakazi wao. Huwalipa ujira mzuri na marupurupu mengine mengi, ikiwa ni pamoja na malipo ya saa za ziada (over-time). Kimsingi wanafanya uungwana mkubwa kwa wafanyakazi, na kuonesha kujali. Lakini utashangaa nikisema hawa ndio ‘wachawi’ wa wastaafu wengi. Utauliza, ki-vipi tena? Nitakujibu!

Rais Mstaafu, Jakaya Kikwete aliwahi kusema: “Huwezi kupata kitu mpaka kwanza wewe utoe kitu”. Yeye alitumia maneno yenye ukakasi kidogo! Waajiri hawa, wakishaingia gharama hizi, huwabana wafanyakazi kisawa-sawa, ili wawajibike ipasavyo! Sasa, ili kulipa fadhila na kuonesha ‘uzalendo’, wapo wafanyakazi ambao husahau kabisa maisha yao binafsi, na wengine husahau hata kama kuna kitu kinaitwa kustaafu.

Wao, muda wao wote, huutumia katika kazi za mwajiri, kwa kiwango cha kupoteza uhuru wao binafsi, hata wa kuwaza tu – kwamba maisha ya ajira yana mwisho, na baadaye watatakiwa waanze maisha yao binafsi. Hali hii ya kuzoea kupewa, ‘kunyimwa’ muda, kupangiwa na kuelekezwa cha kufanya, hudumaza kabisa akili za wafanyakazi wengi, wakakosa uwezo wa kufikiri, kubuni na kupanga mikakati ya maisha yao.

Watu hawa, wakistaafu, kichwani wanabaki na mawazo/tabia ya kusubiri kuambiwa. Ni kama kuku aliyekuwa amefungwa kamba siku nzima, akifunguliwa huendelea kulala tu, asijue kama tayari yuko huru! Ni vigumu sana Mfanyakazi huyu kumudu kuanzisha kitu chake. Huyu amelemaa tayari, hata ukimpa mamilioni, hawezi kuyafanyia kitu. Je, unajua cha kufanya katika mazingira haya? Huu ni mjadala wa siku nyingine.

Pili, wastaafu wengi ni ‘target’ ya matapeli. Kuna utapeli mwingi unaofanyika kila siku. Wapo matapeli wanaoweza kuja na kukupa wazo na kukushawishi uingize fedha zako, ili uje kuvuna mamilioni. Tumesikia juzi hapa suala la Kampuni ya Q-net likijadiliwa, na ushuhuda wa wahanga wake. Tumesikia sana kuhusu Freemason, na unavyoweza kutajirika ukijiunga nao. Pia kuna biashara za kubahatisha (betting) nakadhalika.

Unachopaswa kujua ni kwamba, wastaafu ndio walengwa wakuu (target) wa matapeli hawa; na wana mbinu za kujua ni nani, lini na wapi kuna mtu anastaafu. Wanajua pia, kuwa wastaafu wengi hawana maarifa ya fedha na uwekezaji, ni wazee tayari, na ni rahisi kushawishika. Itaendelea …

Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasirimali kivitendo. Anapatikana kwa e-mail: nzyy2001@gmail.com; Mobile: 0718219530

Jinsi Manunuzi Ya Ovyo Yanavyobomoa Maisha Ya Kustaafu

Uraibu wa ‘kununua’ unaelezewa kama “ugonjwa” au “utumwa”, usipojihadhari utakutia umaskini uzeeni

Neno ‘uraibu’ linatokana na lugha ya kiarabu; likiwa na maana ya mtumwa au mfungwa. Hii ni ile hali ya kutawaliwa na tendo au tabia fulani, na hivyo kuwa mgonjwa au tegemezi wa tendo hilo. Kuna uraibu wa aina nyingi: pombe, sigara, madawa ya kulevya, kamari, ngono na simu janja – hii ni mifano tu!. Mbali na mifano hiyo; kuna uraibu usio bayana sana, lakini una athari kubwa, nao ni uraibu katika ‘manunuzi binafsi’.

Kuna mambo kadhaa ambayo mfanyakazi anayejiandaa kustaafu anatakiwa kuyazingatia ili mambo yasimwendee kombo uzeeni. Moja ya mambo hayo ni ujenzi wa tabia ya kujiwekea akiba. Hili ni jambo umuhimu, ambapo mtu anaweza kudunduliza kidogo-kidogo hadi kutimiza kiwango cha fedha kinachoweza kutumika kujiandalia makazi au kufanya uwekezaji katika miradi au biashara anayoweza kuchagua kuifanya.

Kuna suala la kujijengea maarifa/elimu ya uwekezaji katika miradi hiyo ya ki-biashara na ubunifu; yaani namna ya kuwekeza, na vitu muhimu vinavyotakiwa katika uwekezaji; lengo likiwa ni kumfanya mfanyakazi kujitengenezea kipato cha ziada na endelevu kinachoweza kuchukua nafasi ya mshahara anaoupata katika ajira yake.

Sasa, ili awe na uwezo wa kuweka akiba, na hatimaye kufanya uwekezaji, ni lazima mfanyakazi huyu, pamoja na mengine, awe na uwezo wa kubana matumizi au kuepukana na manunuzi yasiyofaa. Haya, ni manunuzi yasiyo na tija; au kama yana tija, yanafanywa wakati ambao si sahihi. Unakuta kitu sio adimu, wala hakihitajiki wakati huo; lakini kwa kuwa mtu ana hela, ananunua tu; na akifika nyumbani pengine hakitumii…na huenda asikumbuke kama aliwahi kukinunua!

Kwa kuzingatia hili, leo napenda tujadili vitu kadhaa vinavyosababisha mtu awe na tabia hii. Tabia ya kutaka kumiliki kila anachokiona; na yuko tayari kutoa fedha nyingi ili aweze kuondoka na chochote, alichokitamani. Ukizijua sababu hizi, utajitathmini wewe mwenyewe; na ukihamasika utachukua hatua ya kujinasua katika uraibu huu usio na maana!

Moja, bongo zetu zimeumbwa kuvutiwa na vitu vipya. Kwa tabia hii, mtu hupenda kumiliki vitu, au kuwa katika mazingira mapya, kila wakati. Kwa mfano, unaingia dukani, na ghafla macho yako yanagongana na mtindo wa mavazi, au nguo inayokuvutia sana! Hukupanga, lakini kwa ushawishi wa mvuto tu, unashindwa kujizuia…unainunua! Cha kusikitisha; ukifika nyumbani unagundua hiyo ni nguo ya kawaida sana; halafu jirani yako anayo kama hiyo; hivyo huivai! ‘Wadada’ hukabiliwa sana na hali hii!

Mbili, akili ya binaadamu imeumbwa kukinai. Moja ya sababu zinazomfanya mtu kuanza kutazama huku na kule, ili apate kitu kitakachompatia ridhiko la moyo…ni kukinai. Nimewahi kumsikia mtu anasema, “mimi siwezi kukaa na simu janja zaidi ya miezi sita…lazima ntaiuza, ninunue mpya”! Huyu ametawaliwa na hulka ya kukinai, na hununua kwa ajili hii; hata kama hakuna ulazima!

Tatu, binaadamu hupenda kujiliwaza. Tafiti zinaonesha, wapo watu hupata furaha ya ndani, wanapofanya ‘shopping’; na hasa kina dada! Ni kama mtu mwenye kiu wakati wa joto; akipata maji baridi anahisi mwili kutulia. Kwa bahati mbaya watu wa aina hii, kiu hii huwa inaisha kwa muda tu, kisha hurudi tena. Katika manunuzi, hali hii huwafanya watu kutumia fedha, hadi wakaishiwa; ili tu watulize kiu yao!

Nne, ushawishi wa makundi rika. Wanasaikolojia wanasema binaadamu hupima huzuni au furaha yake akijilinganisha na watu wanaomzunguka.  Utakuta, mtu anafanya manunuzi  yasiyo na maana ili kutaka kujilinganisha au kuwapita wenzake ki-uwezo au kimwonekano tu. Jirani kanunua seti ya sofa – na wewe unataka; tena sasa hivi! Je, ulipanga kununua leo? Je, kuna ulazima huo? Sababu hii huchangia sana baadhi ya wafanyakazi hushindwa kujiandaa kustaafu.

Tano, matumizi ya kukomoana. Hali hii hujitokeza sana mahusiano ‘yanapokorogeka’; hasa ya ndoa! Kwa wanandoa waliokorofishana, haya ni matumizi yanayoitwa ‘mkomoeni’; yaani mtu ananunua vitu kama kapagawa, kutaka kumkomoa au ‘kumwadhibu’ mwenzi wake, ili aumie tu! Ni matumizi ya kupunguza hasira. Tatizo, hali hii ikiendelea kusababisha ‘kuchalala’, au kufilisika; na hili huathiri maisha ya kazini, na yale ya kustaafu!

Sita, kuondoa mazingira yaliyoleta mateso zamani. Haya ni matumizi yanayolenga kuiridhisha nafsi. Wapo watu ambao hupatwa na hamu ya kununua, ili kuziba pengo lililokuwepo zamani. Mfano ni mtu aliyeishi maisha ya ki-masikini; akiwa hawezi kununua chochote. Au mtu aliyenyanyaswa zamani kwa kukosa uwezo wa fedha. Huyu akipata fedha hutaka ‘kulipizia’, na hivyo hununua kila kinachomvutia; hata kisichohitajika!

Saba, hamu ya kutaka kuwakoga wengine. Aina hii ya manunuzi ni ile ambayo lengo lake hasa sio kukidhi haja za mahitaji; bali hufanywa na mtu ili kujionesha kuwa na yeye ana uwezo. Ni manunuzi yanayolenga kuchokonoa hisia za watu fulani; wajue kuna mtu, yupo mahala fulani; sio maskini, na ni mtu katika jamii…mwenye hadhi yake. Walengwa hapa ni mahasimu, au wabaya wa mtu huyo!

Nane, tabia ya uchoyo au husda. Siyo rahisi kukubali; lakini kuna utafiti unaoonesha kuwa roho ya binaadamu imeghubikwa na ubinafsi na uchoyo! Hivi karibuni, Padri Richard Mjigwa, wa Vatican, alimnukuu Baba Mtakatifu Francisco, akiwaalika waamini kusali pamoja, ili kuombea masuala kadhaa, aliyoyaita ‘magonjwa mazito’, ili Mungu atuepushe nayo. Moja ya magonjwa hayo ni ‘ubinafsi na uchoyo’! Watu wanapenda kuonesha uwezo wao kwa kujilimbikizia mali.

Ukifuatilia historia… utaona kuna vitu kama vita, rushwa na mapambano ya kushika madaraka. Watu hutoana macho kwa lengo la kujikusanyia tu; hata pale wenzao hawana chochote! Utakuta mtu ananunua kitu, sio kwamba anahitaji akakitumie; la hasha! Anataka awe nacho tu kitu hicho! Na ikitokea mwingine akanunua kitu kama hicho, yeye hukwazika; na huamua kuongeza kingine…ili muda wote awe juu ya wote. Na tabia hii sio kitu kingine…huu ni uchoyo!

Kwa hiyo, matumizi/manunuzi ya aina hii, huwa yana athari kubwa sana kwa maisha ndani ya ajira…na hasa baada ya kustaafu. Fedha inayotumika kufanya manunuzi haya, yasiyo na maana wala tija, zingeweza kudundulizwa, zikawa nyingi (akiba), na zikatumika katika uwekezaji ambao ungekupatia kipato endelevu na kuyafanya maisha yako baada ya kustaafu yakawa bora na yenye furaha. Chukua hatua sasa!

Mwandishi wa makala hii ni Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasiriamali. Anapatikana kwa simu 0718219530; E-mail: nzyy2001@gmail.com

Ukitaka Biashara Ikunyookee Jifunze Stadi Hizi – 2

Majadiliano ni muhimu kwa wafanyabiashara, ikiwa ni njia ya kujenga na kuboresha mahusiano na kuongeza tija ya biashara

Habari!

Katika makala iliyopita nimejadili ‘ukweli’ kwamba…kuwa na sifa za kielimu (elimu ya darasani) pekee yake haitoshi; kwa mtu aliye na hamu ya kupiga hatua katika maisha yake. Hii ni kwa sababu upo ushahidi wa watu wenye elimu ya shahada au zaidi, lakini hawana mafanikio yoyote ya maana (utajiri); na maisha yao ni duni.

Lakini upo ushahidi pia unaoonesha kuwa wapo watu waliopata mafanikio makubwa ya kiuchumi wakiwa hawana sifa yoyote ya maana ya elimu ya darasani. Matajiri hawa, mfano Ariko Dangote, wana sifa ya kutumia maarifa ambayo mara nyingi hayafundishwi darasani. Ni maarifa yanayopatikana zaidi nje ya darasa.

Maarifa haya, ukiweza kuyajua na kuyafanyia kazi, utamudu kuanzisha, kusimamia na kuendeleza ipasavyo biashara/miradi yako; na hivyo kujijenga vyema kiuchumi. Hizi ni  stadi zinazokufanya kuwa na uwezo mkubwa wa kuzikamata fursa, lakini pia kupambana na changamoto ambazo  huathiri ustawi wa biashara/miradi mingi.

Katika sehemu ya kwanza ya makala hii nilijadili stadi tatu. Naomba sasa tuendelee kujadili stadi nyingine kama ifuatavyo:

Nne, hisia-mwenzi au ‘empathy’.  Huu ni uwezo wa kutamani kufahamu hisia au masaibu ya watu wengine kwa lengo la kuyafanyia kazi. Ni ile hali ya kujiweka katika mazingira ya wengine, kihisia, ili kupata undani wake kwa lengo la kutaka kusaidia au kutoa ushirikiano.

Kwa mfano, kama wewe ni mfanyakazi, tunatarajia ujitahidi kuyajua matatizo au matamanio ya wateja wako vizuri, ili ujue ni kwa kiasi gani huduma zako zinafikia kiwango cha kuwafanya waondoke katika biashara yako wakiwa na furaha. Wakati unaanza biashara, ni muhimu kuzijua changamoto za wateja wako tarajiwa, ili ujipime kama ‘majibu’ (huduma/bidhaa) unayopanga kuwapatia yatakidhi matarajio yao.

Kwa mujibu wa tafiti kadhaa; kukosekana kwa hisia-mwenzi zinazohusu masoko huwa sababu kubwa ya biashara nyingi mpya kufeli. Yaani, kama mwanzoni kabisa utajitahidi kuzifahamu hisia za wateja wako, utajua ni bidhaa/huduma gani wanazihitaji, na wangependa kuzipata katika ubora, wakati na mazingira gani.

Wateja wakijenga hisia, mwanzoni kabisa, kuwa kuna mtu anajali hisia zao, na yuko tayari kuwasikiliza, na kuchukua hatua, kuhusu matatazo/matamanio yao, basi utakuwa umewasha moto, na kuwajengea imani thabiti ndani yao, inayotengeneza gundi imara katika mahusiano yenu. Haya ni mazingira yanayowajengea imani wateja…kwamba wewe, mfanyabiashara, unajitahidi kutengeneza uhusiano mzuri kati yako na wao, kwa lengo la kutatua matatizo yao; na sio kwa lengo la kujitengenezea faida yako!

Tano, maarifa ya kupanga mipango. Kama unafikiri kwamba ukiwa na wazo zuri au umeiona fursa, na tayari una mtaji, basi utaingia tu, na kuanza biashara – utakuwa unakosea sana! Elewa kuna vitu vingi vinaingilia maisha yetu, kila siku; vikwazo, vizuizi na mabadiliko katika mazingira tunayoishi.

Kwa hiyo, usipoweka mipango, ya muda mfupi na mrefu; na mikakati – ujue uhai wa biashara yako uko mashakani. Kuna mipango ya aina nyingi katika biashara. Ipo mipango ya fedha, uwekezaji, uzalishaji, masoko, wafanyakazi na kadhalika. Ukiyavunja-vunja malengo yako ya muda mrefu, ukapata malengo madogomadogo, utakuwa unajenga uhakika wa kufanikiwa, mbele ya safari.

Sita, umahiri katika kufanya mauzo. Kama una hisia nzuri, au macho mazuri ya kuona, utagundua kuwa ujuzi/maarifa yanayoweza kuifanya biashara yako ionekane anang’aa, na kurusha mwanga kwa watu – ni mauzo!

Ujuzi wa mauzo ndio chachu ya biashara yako. Biashara inayoshindwa au kukosa mbinu za kufanya mauzo ya huduma/bidhaa – ujue hiyo inakwenda kufa. Ndio itakufa! Pamoja na wabunifu, mafundi, wanunuzi, wahasibu nakadhalika, ulionao katika biashara yako – ukikosa watu wanaoweza kufanya mauzo…umefeli!

Na sio kuuza tu bidhaa au huduma – lakini hata ukitaka kukopa, kupata mwekezaji au kutoa ushawishi ili upate mshirika wa biashara (partner), unahitaji kuwa na maarifa ya kuuza; yaani kuuza wazo, mipango na mikakati yako…na kuonesha kitu unachotaka kupata kutoka kwa taasisi au mshirika unayemtaka.

Lakini pia, hata katika familia na kazi zetu, tunatumia sana mbinu za mauzo au ushawishi kupata vitu/huduma mbalimbali. Kwa mfano, ushawishi wa watoto kwa wazazi, au wafanyakazi kwa mwajiri. Kwa hiyo, kwa mtazamo huu, ukitaka kupata fedha katika biashara yako, ni lazima ujijengee uwezo wa kuuza.

Saba, uwezo wa kujenga ushirikiano. Kiuhalisia, na hata kitafiti – ni ukweli kwamba ili kufanikiwa katika biashara ni umuhimu sana kujenga umoja au ushirikiano baina ya wadau. Methali isemayo “umoja ni nguvu, utengano ni udhaifu” ina maana sana katika hili. Inatupa tahadhari kwamba si vizuri mtu au taasisi kutaka kufanya mambo peke yake; kwani kuna madhara.

Umoja ni kama msingi wa nyumba…ambao ukiwa imara, hata ukuta ukiwa mzito utabebwa juu yake bila taabu. Biashara au mradi ukifanywa kwa ushirikiano uliojengwa vizuri, kila mshiriki atapata fursa nzuri ya kuchangia mawazo/rasilimali alizonazo; kwa mfano mawazo, mtaji, ujuzi, uzoefu, vifaa, taarifa nakadhalika. Ushirikiano unaweza kuwa wa ndani ya kampuni (idara) au unaohusisha wadau wa nje ya kampuni.

Mfano mzuri katika ushirikiano ni ule wa makampuni ya Mastercard, BancABC na Vodacom. Ushirikino baina ya Makampuni haya, yenye utaalamu na rasilimali tofauti, uliweza kufanikisha utengenezaji wa kadi iitwayo M-Pesa Virtual Card, inayowezesha manunuzi ya mtandaoni, hasa kupitia tovuti za kimataifa; kitu ambacho hakikuwepo zamani.

Nane, maarifa ya majadiliano. Kwa mtazamo wa mtaalamu mmoja, maarifa ya majadiliano yanapaswa kufundishwa kama hisabati, kuanzia darasa la kwanza. Stadi za majadiliano hazitakiwi kuachwa watu wajifunze ukubwani kwa shida na maumivu.

Kila siku binaadamu tunafanya majadiliano; na wazazi, marafiki, majirani, ndugu au mwenza. Kitu cha kipekee hapa ni kwamba utaalamu unaotumika kujadiliana majumbani, sokoni, madukani, safarini nakadhalika, ni ule wa ‘asilia’. Kwa kuzingatia hili, ni muhimu wafanyabiashara wakaenda mbali zaidi ya ‘ujuzi asilia’ pekee. Wao inafaa wajifunze kwa kina na bidii zaidi.

Tunahitaji maarifa haya, tena yaliyopangiliwa vizuri, ili tuweze kujadiliana vyema katika mauzo, manunuzi, kujenga ushirikiano na washirika, wawekezaji, wateja, wamiliki wa majumba, na hata wafanyakazi wanaokuja wakitaka ajira au nyongeza ya mshahara.

Tisa, maarifa ya kufanya maamuzi. Katika uhalisia wa maisha, haijalishi unajua nini, na kwa kiwango gani…au unaonekana unafanya nini. Watu wanaofanikiwa ni wale wanaochukua hatua; kutenda na kuonesha matokeo. Haidhuru unawaza kiasi gani, unapanga nini, unafanya utafiti kiasi gani, hutafanikisha chochote kama hutaingiza utendaji.

Uzoefu unaonesha kwamba ‘wasomi’ wengi hupoteza muda na rasilimali nyingi kutafiti jambo kupita kiasi – kitu ‘kinachotia ganzi’ akili, isiweze kuamua kutia mipango katika matendo. Hali hii huitwa ‘laana ya maarifa’, yaani mtu tayari ana maarifa/taarifa zote, lakini anabaki kusita-sita tu, asiweze kuanza utekelezaji.

Na hii inaweza kuwa sababu inayowafanya baadhi ya wasomi wa elimu ya uchumi au biashara, au hata madaktari wa falsafa, kushindwa kuanzisha biashara/miradi yao binafsi; wakaishia kuwafanyia kazi watu wengine, na pengine wenye elimu ndogo kabisa.

Yaani, unakuta mtu ana elimu ya fedha, biashara, uzalishaji, masoko nakadhalika, lakini hawezi kujipanga ili kufanya jambo lake. Anachoweza ni kujijengea uwezo wa kujibu maswali katika usaili – kueleza jinsi anavyoweza kuitumia elimu yake kufanya kazi za wengine!

Hivyo, watu wanapaswa kujijengea uwezo wa kufanya maamuzi; hata pale wanapokuwa wana taarifa kidogo tu. Wafanyabiashara waliofanikiwa ni wale walio tayari ‘kujitosa majini’ na kufanya kitu…badala ya kusubiri hadi wapate taarifa kwa asilimia mia moja. Uwezo wa kufanya maamuzi ni stadi ambayo wajasiriamali wote wanatakiwa kujifunza na kuimudu ipasavyo.

Kwa hiyo, kwa kila mtu anayefikiria kuanzisha na kuendesha biashara kwa ubora na ufanisi, ni jambo la maana kujijengea stadi/maarifa haya. Kwa walio ndani ya biashara tayari; lakini hawana stadi hizi, basi wajitahidi kujifunza. Kwa kufanya hivyo watapiga hatua kubwa zaidi kibiashara.

Mwandishi wa makala hii ni Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasiriamali. Anapatikana kwa simu 0718219530; E-mail: nzyy2001@gmail.com

Ukitaka Biashara Ikunyookee Jifunze Na Kuzielewa Stadi Hizi – 1

Moja kati ya mbinu nzuri za kujijengea ‘nembo binafsi’ni kujiuza kupitia mitandao ya kujamii

Habari!

Kama sifa za kielimu (elimu ya darasani) ndio maarifa anayotakiwa kuwa nayo mtu ili apige hatua katika maisha yake, basi watu wote wanaoitwa ‘wasomi’ wangekuwa matajiri, wenye mafanikio, na wenye furaha tele!

Hata hivyo, upo ushahidi unaoonesha kwamba kuwa na shahada ya uzamili katika biashara (MBA), au hata kuwa na shahada ya udaktari wa falsafa (PhD), sio garantii ya mafanikio katika maisha (utajiri). Kinyume chake ni kwamba watu wanaofahamika duniani kwa utajiri au mafanikio makubwa katika biashara au ujasiriamali ni wale wasio na sifa yoyote ya maana ya elimu ya darasani; kwa mfano Steve Jobs, Bill Gates na Ariko Dangote.

Hii inaonesha kwamba kuna maarifa au stadi (nje ya darasa) ambazo mtu akiwa nazo zinamuwezesha kuwa na uwezo mkubwa wa kujenga mawazo, kubuni, kuanzisha na kuendeleza biashara hadi ikamletea mafanikio makubwa (utajiri). Cha ajabu ni kwamba pamoja na umuhimu wake; stadi hizi mara nyingi hazifundishwi mashuleni/vyuoni. Kwa kiasi kikubwa mitaala ya shule/vyuo huwaandaa wanafunzi kuajiriwa na sio kujiajiri (ujasiriamali).

Sasa, ikiwa unataka kuwa mjasiriamali makini, kuna stadi ambazo unazihitaji katika dunia ya leo ya kibiashara; ambazo ukizijua zitakubeba, ili usiachwe nyuma na fursa mbalimbali zinazojitokeza. Hizi ni  stadi zitakazokufanya kuwa na uwezo mkubwa wa kuzikamata fursa, lakini pia kupambana na changamoto ambazo  huathiri ustawi wa biashara nyingi.

Kwa hiyo, ili biashara yako ikunyookee na uifanye kwa ufanisi mkubwa unahitaji kuwekeza katika kujifunza stadi hizo. Ukiweza kuzijua na kuzifanyia kazi, utakuwa katika nafasi nzuri zaidi katika  kuianzisha, kuisimamia na kuindeleza ipasavyo biashara yako. Naomba sasa tuzijadili stadi hizi kwa pamoja.  

Moja, mawasiliano madhubuti. Stadi hii humfanya mtu kuwa na uwezo wa kumtumia taarifa mtu mwingine kwa ufanisi na tija stahiki. Ifahamike kuwa lengo kuu la mfanyabiashara ni kuhakikisha biashara yake inakua kutoka hali duni hadi hali bora. Hivyo, inapotokea kukawa na mawasiliano mabovu, yasiyoonesha uelekeo sahihi, yasiyo timilivu, na yasiyoleta matokeo; biashara huathirika. Mawasiliano bora yana nafasi kubwa ya kutia uhai katika biashara, bidhaa au nembo (brand) husika.

Mjasiriamali nguli, Steve Jobs anasifika sana kwa uwezo wake mkubwa wa kuwasiliana, na kwa uwezo huo alifanikiwa sana kuifanya Apple kuwa moja ya makampuni yenye thamani kubwa duniani. Kwa hiyo, mjasiriamali makini anapaswa kuwekeza vya kutosha katika kujifunza mbinu bora za mawasiliano. Pamoja na ujuzi huu; anapaswa pia kuhakikisha wasaidizi au watumishi wake wote wanapata maarifa haya na kuyatia katika vitendo.

Pili, ujenzi wa nembo (brand) binafsi. Kujenga nembo ya biashara ni kufanya mchakato wa kuwasilisha kwa wateja pendekezo la kipekee la mauzo;  ambalo linaifanya biashara, bidhaa au huduma ionekane tofauti, na ya kipekee; ikilinganishwa na ile ya washindani – kwa kutumia logo (mchoro), kaulimbiu au viashiria fulani. Kwa hiyo, kuna tofauti kati ya kujenga ‘nembo ya biashara’ na ‘nembo binafsi’.

Kama ambavyo nembo ya biashara, bidhaa au huduma –  ya biashara moja; hujitofautisha na biashara, bidhaa au huduma – ya biashara nyingine; nembo binafsi nayo iko hivyo hivyo. Nembo binafsi inaongelea zaidi jinsi ambavyo mmiliki wa biashara anajipanga ili kukuza jina na sifa zake binafsi; akijitofautisha na wamiliki wengine wanaomiliki biashara shindani.

Nembo binafsi inakuelezea wewe, mfanyabiashara. Inasimulia hadithi yako na kutoa picha kwa wengine; ya tabia, mwenendo, mtazamo na mvuto ulionao kwa wengine. Nembo binafsi ni taswira ambayo watu wengine wanaiona kwako wakiangalia haiba, maarifa, ujuzi, uzoefu na tabia unazoonesha. Nembo yako binafsi; ikiwa ina nuru inayong’aa, ni rahisi kwa miale yake ming’aavu kusambaa na kung’aa juu ya nembo ya biashara, bidhaa au huduma unayotoa; na kuifanya biashara yako kujipambanua kirahisi kwa wateja.

Mfano mzuri ni wakati wa uchaguzi ndani ya vyama. Pamoja na jina, au sifa, ya chama husika, wapo watu huamua makusudi kabisa kumpigia kura mtu binafsi; kwa kuvutiwa na nembo (brand) yake binafsi. Wagombea wenye nembo binafsi zenye nguvu, na zinazong’aa hupata mafanikio makubwa katika siasa za vyama.

Kabla ya kuingia internet watu walijenga nembo zao kwa kutumia ‘business cards’, au kujichanganya kwenye vikao au matukio mbalimbali ya kijamii. Siku hizi watu wanatumia zaidi mitandao ya kijamii kujenga nembo zao binafsi kwa kuonesha vitu, sifa au tabia ambazo wangependa watu wawafahamu kwazo kupitia mitandao; ingawa business cards bado zipo pia.

Tatu, elimu ya msingi ya fedha. Tunapotaja stadi hii tunakuwa tunaongelea ujuzi au maarifa ya msingi ya kuzifahamu mbinu zinazohusu fedha; yaani jinsi fedha zinavyozalishwa, zinavyotumiwa, na zinavyofanya kazi…hasa katika kuendesha uchumi binafsi. Hapa hatuongelei elimu ya cheti au shahada ya uhasibu au usimamizi wa fedha/biashara, ambayo unaweza kuwa nayo. Hapana! Hapa tunaongelea ‘mambo ya msingi yanayohusu fedha’.

Kama unaweza kufanya uchunguzi, utaona tabia za vijana siku hizi, wakipata fedha. Angalia vitu wanavyonunua. Mavazi ghali, ‘magari makubwa’, na matumizi ya anasa yanayoitwa ‘matanuzi’; ambayo kwa wengi, ni matumizi ya kujikweza na kujionesha, kwa kufanya vitu visivyo na maana yoyote. Sio vijana tu; hata watu wazima nao wamo, na wanafanya hayo!

Wapo watu, jinsi wanavyoingiza fedha zaidi ndivyo ambavyo matumizi yao ya anasa yanavyoongezeka zaidi. Wapo ambao wakipata fedha hawana muda wa kufikiri kuhusu matumizi ya fedha zao. Hawa wako tayari kununua ndege kabla hata ya kujua wataipaki katika uwanja gani wa ndege, na ikiharibika watapata wapi fundi au vipuli vyake.

Ukiwa makini – utagundua wanaofanya ‘matanuzi’ haya, wengi wao wamebahatisha tu kupata fedha hizo; kwa mfano mtu anauza bidhaa adimu katika kipindi cha majanga, kama mafuriko au ukame…anapata fedha nyingi na kuanza matanuzi! Utashangaa sasa, baada ya muda fulani, vitu vya anasa alivyonunua kipindi ana fedha, vinageuka kuwa mzigo kwake – hasa vyanzo vyake vya mapato vinapokauka. Mara nyingi huishia kuviuza vitu hivyo kwa bei ya hasara na kurudi upya katika umaskini.

Cha kujifunza hapa ni kwamba matajiri wengi wanaovuma duniani sio ‘extravagant’. Yaani hawana matumizi yasiyo na mpangilio wala kutapanya fedha ovyo-ovyo; kama wengi wanavyofikiria. Wanapoamua kutumia, hutumia kwa lengo la kuzalisha fedha zaidi. Matajiri hawa hutafuta mitaji, wanayoitumia kuwekeza; na kila mara hujiwekea akiba.

Ujuzi wa kuizungusha fedha ki-biashara ili izalishe fedha zaidi; na matumizi ya fedha kwa mpangilio; kwa kununua vitu vya msingi, ili kuepusha upotevu wa fedha kizembe, ndio elimu ya msingi ya fedha tunayohitaji watu waipate.

 Kwa hiyo, kujijengea maarifa haya ni jambo muhimu kwa kila mtu anayefikiria kuanzisha na kuendesha biashara kwa ubora na ufanisi. Na kwa walio tayari ndani ya biashara lakini wakawa hawana stadi hizi, basi wajiongeze kwa kujifunza ili waweze kupiga hatua kubwa zaidi kibiashara. Usikose sehemu ya pili ya makala hii ambapo nitajadili stadi nyingine zaidi.

Mwandishi wa makala hii ni Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasiriamali. Anapatikana kwa simu 0718219530; E-mail: nzyy2001@gmail.com

Je, Unataka Kustaafu Kwa Furaha? Jijengee Tabia Hizi Sasa!

Siku ya sherehe yao, wastaafu huonesha sura ya furaha. Je furaha hii ni endelevu?

Maisha ya kustaafu hayapaswi kuwa ya kujutia hadi kufikia hatua ya kusononeka na kusema kimoyomoyo: “Sioni raha ya maisha; laiti kungekuwa na uwezekano ningerudi zangu kazini niendelee na furaha niliyokuwa napata huko!”. Ukweli ni kwamba kustaafu ni jambo la heri; linalopasa kumpa mstaafu furaha, huku akikumbuka mchango alioutoa kazini kwake kwa kipindi kirefu.

Kuna tabia ambazo mfanyakazi unatakiwa kujijengea, toka ukiwa kazini; ili ujiweke katika nafasi nzuri ya kustaafu kwa furaha. Tabia hizi ni kama mbegu ambayo mtu anaipanda mapema na anaitunza ili iendelee kustawi. Anapostaafu anaanza kuyaona matunda yake, na hivyo anaingia uzeeni akiwa na furaha na amani ya moyo, kitu ambacho humwongezea pia umri wa kuishi. Nitajadili tabia hizo:

Moja, jenga uthabiti wa moyo. Uthabiti ni ile hali ya kujiweka sawa au kurudi haraka katika hali ya awali baada ya kupatwa na masaibu fulani. Kustaafu huambatana na mabadiliko ya maisha, kutoka mazoea ya kazini. Ikumbuke pia kuwa katika maisha kuna kufanikiwa au kufeli; hivyo ukifeli au kushindwa kupata kitu ulichotarajia, hutakiwi kugalagala.

Ukikutana na mazingira magumu, ukapepesuka, ukayumba au kuanguka –  unapaswa kutuliza akili, kuinuka, kujiweka sawa na kusonga mbele. Kwa kuwa uthabiti ni stadi inayofundishika, kujifunza uthabiti mapema kuna msaada mkubwa katika kujijengea ustawi na furaha katika maisha ya kustaafu. 

Mbili, jiweke karibu na jamii. Hili linatokana na ukweli kwamba wafanyakazi wengi huutumia muda wao mwingi kazini; hivyo mahusiano yao makubwa ya kijamii ni yale ya wao na wafanyakazi wenzao. Mahusiano na watu wengine huwa ya nadra; na mara chache hufanyika siku za mwisho wa wiki, au likizo, tena kwa ‘kushinikizwa’ na viongozi wa mtaa/dini. Wafanyakazi hawa, wakistaafu ndio, kwa kuchelewa, hugundua kuna pengo hili; na ndipo huanza kuchacharika!

Kuliziba pengo hili baada ya kustaafu sio kazi rahisi, kama hukujiandaa mapema kulifanya hili kama sehemu ya tabia yako. Hivyo, kuepukana na upungufu huu, jenga tabia, ukiwa kazini, ya kujichanganya na jamii. Jiunge na vyama au makundi ya kijamii mtaani. Shiriki kazi za kijamii; kama kujitolea na mikusanyiko inayojadili masuala ya kijamii. Kwa kufanya haya utajikuta unajenga uhusiano, urafiki na mtandao mkubwa ambao utakupa manufaa makubwa baada ya kustaafu.

Tatu, jifunze kupangilia matumizi. Katika maisha ya kustaafu ukikosa nidhamu utaharibu au utaharibikiwa. Kwa mfano, kuna tabia za watu, wanapokwenda ziara za mapumziko (outing), mara nyingi hawawi na ratiba au hata bajeti. Wananunua kinachopita mbele ya macho yao, bila mpangilio. Wanakula na kunywa, bila mpangilio. Wapo wanaorudi nyumbani mifuko mitupu, na wengine wanaacha madeni huko! Hii sio tabia nzuri. Maisha ya kustaafu yanapaswa kuwa yenye furaha endelevu, hivyo yanahitaji mipangilio.

Nne, jenga tabia ya uwekezaji. Wafanyakazi wengi hujawa na fikra, na pengine uhakika; kwamba mafao ya kustaafu watakayolipwa ni fedha nyingi, hivyo hakuna haja ya kuwa na presha. Husema watakapolipwa, mengine yatajulikana wakati huo. Huku ni kukosa maarifa!

Wafanyakazi wenye busara hujijengea tabia ya kubana matumizi, kuweka akiba na kuwekeza. Kama unatamani kuishi kwa furaha uzeeni jiwekee mipango na mikakati ya kiuchumi ili ukistaafu uwe na uhakika wa kuendelea kujiingizia kipato endelevu.

Tano, jifunze kujiwekea ratiba ya utendaji. Katika safari ya kustaafu unahitajika kufanya mambo yako kwa utaratibu mzuri. Kazini; karibu kila kazi huwa katika ratiba maalum, inayoendana na malengo na muda wa utekelezaji. Hata ukistaafu, unapaswa kuweka mambo yako namna hii hii; na tabia hii hukujengea mazoea ya kupanga na kutimiza mambo, ambayo huwa chanzo cha hamasa na furaha uzeeni. 

Sita, jizoeze kupangila ulaji. Mtindo wa ulaji una athari kubwa katika maisha baada ya kustaafu. Wakiwa kazini, wako watu hupendelea kula aina fulani ya chakula, ili kutafuta kiitwacho ‘ujiko’; yaani sifa! Hawa hupendelea kula vyakula vyenye wanga na mafuta mengi kama ‘chips mayai’, huku wakishushia na soda (huu ni mfano tu). Aina ya chakula, maandalizi, wingi na mpangilio mara nyingi hukosa ubora kitaalam; na hivyo huwa chanzo cha matatizo ki-afya. Hivyo, jiepushe na ‘junk food’, ni hatari!

Saba, jizoeze kufanya mazoezi. Kama mazoezi sio jambo ulilozoea kulifanya ukiwa kazini, basi unahitaji kufikiria upya, na kuchukua hatua. Mazoezi yana nafasi kubwa katika kujenga afya uzeeni. Kukaa bila mazoezi ni hatari, kwani kuna magonjwa huibuka kwa sababu hii, na huwatesa wastaafu. Kwa hiyo jenga tabia ya kufanya mazoezi, angalau mara tatu kwa juma. Jizoeze pia kutembea mara kwa mara; mfano unapokwenda ibadani, dukani, sokoni nakadhalika; kama sio mbali na kwako usitumie usafiri, tembea!

Nane, kinga ni bora kuliko tiba. Sio siri…jinsi tunavyousogelea uzee ndivyo afya zetu zinavyozidi kuzorota. Na sio siri…gharama za matibabu ni kubwa hadi zinatisha! Hata wale wenye bima ya afya, sio magonjwa yote hutibiwa kwa bima; na kuna wakati, na bima yako, unaambiwa dawa ulizoandikiwa hazipo, hivyo unapaswa kununua. Kwa sababu hii ni vizuri kujitahidi kujikinga na maradhi kabla hayajaingia au kuwa makubwa.

Maradhi yanayoambatana na umri yanajulikana. Ili kuepukana na ugonjwa wa moyo, kiharusi, presha, figo, kisukari nakadhalika, jiwekee utaratibu wa kupima afya yako mara kwa mara. Madaktari watakupa ushauri stahiki, au kukupa tiba mapema, kabla hali haijawa mbaya; kwa kufanya hivi mwili utaimarika na furaha itatawala uzeeni.

Tisa, jitahidi kupumzika. Umri wa kustaafu ukifika mara nyingi uwezo wa mtumishi, ki-nguvu na ki-akili unakuwa umepungua; hivyo anatakiwa kupumzika. Sasa, kwa kuwa kupumzika ni sehemu ya maisha ya kustaafu, ni muhimu mtumishi ukajiandaa mapema, ili ukistaafu uwe na shughuli maalum, na mifumo itakayokuwezesha kuingiza kipato endelevu; lakini bado ukabaki na muda wa kutosha wa kupumzika. Hivyo jipange sasa!

Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasirimali kivitendo. Anapatikana kwa simu: 0718219530; e-mail: nzyy2001@gmail.com