Mapenzi Yanayoleta Mahusiano Ya Kudumu, Siyo ‘Romantic Love’!

Ukimpenda – ‘romantic love’ – tenga muda wa kutosha kumfahamu kiundani!

Katika hali ya kawaida kijana anapoanza kujitegemea, baada ya muda fulani angependa kuwa na mwenza (mke/mume). Sasa, wataalam wa Saikolojia wanasema vijana wengi huingia katika mahusiano, hadi ndoa, kwa kusikiliza zaidi hisia tu! Ni hisia zinazochochewa na mvuto wa nje, kwa msichana/mvulana, unaoitwa ‘romantic love’.

Wanasema ‘romantic love’ huzaa mshikamano mkubwa sana mwanzo, lakini baada ya muda, vile vitu vilivyokuwa sababu ya ‘stimu’ huanza kuonekana vya kawaida; na hapo ndipo mshikamano huanza kulegea. Wawili hawa huanza kugundua kuwa kuna mambo mengi ya msingi hawaivi. Kile ulichokuwa unavutiwa nacho kikiondoka, mapenzi nayo huondoka, na hapo ndipo mivutano na migogoro huanza kumea.

Yakitokea haya, mahusiano ya ndoa huanza kumomonyoka na mapenzi hugeuka kuwa ugomvi na mitafaruku isiyoisha. Katika mazingira haya, siyo rahisi mipango ya maana kufanywa. Nani hapa atakuwa na muda wa kujenga mawazo ili kuziona fursa za biashara? Mazingira haya hayawezi kujenga fikra za kuweka akiba wala kuwekeza, kwani matumizi ya ovyo, au ya kukomoana – hutamalaki!

Ukifuatilia, utagundua kuwa wajasiriamali na wafanyakazi (walio na biashara) hulalamikia kushindwa kuendesha vyema biashara zao; kwa kukosa mtaji au msaidizi bora wa usimamizi; wakati mke au mume wake yupo, na pengine hana kazi. Sababu mojawapo ni hiyo hapo juu! Ukiwa na mwenza asiye na upendo wa dhati, weledi wala bidii; sio rahisi kufanikisha malengo yako! 

Lakini pia, mahusiano mabaya ya wenza yana nafasi kubwa ya kuwagawa hata watoto; hivyo kuwanyima malezi bora. Watoto hugawanyika; wakawepo watoto baba na wa mama. ‘Mtoto wa mama’ atafuata zaidi maelekezo ya mama, kiasi cha kuweza kukubali hata kumwibia, kutumia pesa ovyo, au kuhujumu miradi ya baba; ili tu kumridhisha mama,..na kinyume chake!

Mwanasaikolojia Rossana Snee anasema mapenzi ya kweli, yanayoleta mahusiano ya kudumu, siyo ‘romantic love’. Ni mapenzi yanayotokana na ‘shared values’; yaani vile vitu vya msingi ambavyo kila mmoja anavikubali na kuviamini kwamba ndivyo vinatengeneza gundi kati yao. Hivi ni vitu vyenye mashiko; ambavyo unaviona kwa mwenzi wako…vinavyokufanya ujisike utakuwa salama na mwenye amani endelevu.

Kwa hiyo, iwapo uchaguzi wa mwenza utaufanya vizuri, kwa kuzingatia ‘shared values’, ndoa hii itajaa heshima, maelewano, na majadiliano; kuwezesha  kupanga na kuweka mikakati ya maendeleo ya familia. Na kama ulishakosea kuchagua, ukathamini zaidi ‘fahari ya macho’ – ni vyema umshirikishe Mungu, ili aweke mkono wake; kwani bila maelewano ya kweli, maisha ya ndoa huwa ya mashaka makubwa.

Kwa mujibu wa wanasaikolojia, zifuatazo ni ‘shared values’ ambazo ndizo hasa hutengeneza kiunganishi cha uhakika kati ya mawili wapendanao, waliomua kuishi pamoja:

Kwanza, kuaminiana na kumcha Mungu. Kuaminiana ni jambo muhimu katika maisha ya ndoa. Tunaambiwa kuwa wanandoa wanaoaminiana hawajengi mawazo hasi, au kuchokonoa-chokonoa maneno au matendo ya wenza wao. Mara zote hutazama matendo na maneno ya wenza wao kwa mtazamo chanya wenye lengo la kuboresha mahusiano. Suala la imani ya dini lina maana sana pia. Ni vizuri wapenzi wakawa na imani moja; kwa kuwa tofauti ya imani mara nyingi huishia katika mitafaruku.

Pili, mawasiliano thabiti. Hili ni jambo la msingi sana kwa kuwa ndio hasa huanzisha mahusiano. Kama unatamani furaha endelevu katika mahusiano ya ndoa, basi unapaswa kuhakikisha panakuwepo mawasiano bora kati yenu; tokea mwanzo. Kutokuelewana katika jambo lolote kukitokea, majadiliano ni muhimu; ili kuweka mambo sawa. Mawasiliano thabiti  yakiwepo huzaa fikra, mipango na mikakati ya maendeleo; na huondoa mitafaruku.

Tatu, uaminifu. Hiki ni kiunganishi muhimu sana katika mahusiano; kwa sababu bila uaminifu hata neno ‘nakupenda sana mpenzi wangu’ hukosa maana, au huonekana ni unafiki! Kama wewe na mwenza wako mmejijengea uaminifu wa kutosha, na kila mmoja anamwamini mwenzake; basi kiwango cha mshikamano huwa cha hali ya juu; na hulifanya penzi kuwa lenye uhakika, na furaha endelevu.

Nne, nidhamu binafsi. Huu ni uwezo wa kujipanga vizuri na kudhibiti tabia au matendo binafsi. Kwa mfano, unaweza kujizoeza kuamka saa 11 asubuhi, ukafanya mazoezi, ukasali, ukaoga… na kisha ukaanza shughuli zako za kazi mapema. Sasa hebu fikiria utajisikiaje ukiwa na mwenza; amka yake ni saa 2 asubuhi, asiyeweza kufanya usafi, hawezi kupika; akiwa na nja anataka akale mgahawani, asiyependa kujituma…utajisikiaje? Kwa vyovyote baada ya muda, hata akiwa mzuri kama malaika, utamchoka!

Tano, matumizi ya fedha. Katika hili jaribu kujiuliza je, wewe ukipata fedha unapenda kuzitumiaje? Kitu gani ni muhimu sana kwako katika matumizi ya fedha zako? Je, ni uwekezaji katika vitu au shughuli za maendeleo? Je, ni kujiendeleza ki-elimu? Je, ni kujijengea makazi bora? Sasa, hebu mtazame mwenza wako – akiwa na fedha anafanyia nini? Je, unamwona ana mtazamo kama wako, au mwelekeo wake uko zaidi katika matanuzi na ununuzi wa vitu vya anasa? Ukigundua hilo, tambua uwezekano wa mahusiano haya kukwama, huko mbele, ni mkubwa. 

Sita, mtindo wa maisha. Moja kati ya gundi muhimu sana katika mahusiano ni staili ya maisha. Kila binaadamu ana hulka yake, na vitu anavyopendela kuwa navyo; au kuvifanya katika maisha yake. Wapo wanaopenda anasa na kujionesha, na wapo wasiotaka makuu. Wapo wanaopenda sifa, na wengine hufanya mambo yao kwa usiri. Wakati wewe unapenda kubana matumizi, kuweka akiba, na kuwekeza – unakuta mwenzio anawaza ‘shopping’ ghali, na kujirusha; karibu kila siku! Hali hii ikitokea, mshikamano huanza kulegea, na ndoa huwa katika hatihati.

Saba, hamu ya kujiendeleza kimaisha. Wapo watu wanawaza muda wote kufanya vitu ili kubadili maisha yao; yawe bora zaidi. Hawa hupenda kujifunza mfululizo, kupanga mipango na mikakati ya maendeleo…na kuweka ratiba za utekelezaji wa mipango hiyo. Sasa, mtu huyu akigundua mwenza wake hana kitu hiki kichwani mwake; yaani yeye mradi anakula, anavaa na kupata mahitaji ya kawaida – basi kwake inatosha; hapa uwezekano wa mahusiano haya kuwa ya furaha huko mbele, ni ndoto.

Nane, utayari wa kuwajibika ki-familia. Ikumbukwe; maisha ya ki-afrika yanabebwa na familia pana (extended family). Moja ya tabia za ki-afrika ni kusaidiana na kubebena, pale inapoonekana ndugu au watoto wa ndugu wanahitaji msaada. Sasa, kama mmoja anatamani kubeba jukumu hili, (la kusaidia, kutembelea au kujali ndugu) – lakini mwenzake haoni haja ya kufanya hivi; uhusiano huu, huko mbele, una nafasi ndogo ya kuwa na afya. 

Kwa hiyo basi, ili kutengeneza mahusiano ya kudumu, endelevu na yenye furaha, yatakayoleta ndoa yenye amani, maelewano na maendeleo; ni jambo la maana sana kuchagua mwenza kwa kuangalia ‘shared values’, badala ya kunasa katika mtego wa ‘fahari ya macho’; ambayo huzaa penzi feki, la muda mfupi, na lenye mitafaruku isiyoisha!

Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasirimali kivitendo. Anapatikana kwa e-mail: nzyy2001@gmail.com; Simu 0718219530

Jinsi Jando Na Unyago Vilivyojenga Maadili Ya Vijana

Je, ni zawadi gani ukimpa kijana wako wa kiume au kike utakuwa umempa ‘silaha’ ya kumlinda katika maisha yake yote?

Habari rafiki,

Siku hizi, kutokana na sababu zilizo halali na zisizo halali, baadhi ya wazazi hawajali, au hawapati nafasi, au labda hawamudu, kuwapatia watoto wao maarifa au stadi muhimu kwa ajili ya maisha yao, na sasa baadhi ya vijana wameanza kulalamika kwa kuikosa haki hii; wanawalaumu wazazi wao kwa kushindwa kuwajibika.

Kwa mfano, yupo kijana mmoja anayekiri waziwazi kuwa wazazi wake hawakumpatia maarifa ya msingi kuyamudu maisha yake. Anasema, “hivi sasa, ukubwani, ndio nimegundua kuwa wazazi wangu hawakunipa ‘silaha’ kwa ajili ya kuyajenga na kuyalinda maisha yangu. Walizembea, na sasa nahangaika, kwa taabu, kufanya vitu walivyopasa kunifundisha utotoni; hii inanisononesha!”

Ukiitafakari kauli ya kijana huyu, utabaini kuwa, baada ya kupata akili za ki-utu uzima, amebaini kuwa ni wajibu wa mzazi kumfundisha mtoto maarifa, tabia na maadili mema, toka akiwa mdogo. Hata hivyo, tujiulize, ni wazazi wangapi wanafanya hili? Ukweli ni wachache. Je wasiofanya hivi wana sababu za msingi?

Akifafanua hili, Mwl. Vicensia Shule, kupitia mahojiano yake na Redio moja nchini, anasema kwamba kutokana na uzembe wa wazazi, vijana wengi, hata wanaohitimu elimu za juu, wanakosa stadi muhimu za maisha ikiwa ni pamoja na kujitambua, kazi za nyumbani, usafi, maarifa ya kujiajiri, na hata uwezo wa kutafuta kazi. Anasisitiza kuwa hili ni janga kwa Taifa.

Zamani kidogo, katika jamii za kiafrika, kulikuwa na mila na desturi zilizohakikisha mtoto au kijana, kabla ya kuingia katika umri wa ki-utu uzima, anapata maarifa au stadi ambazo zililenga kumfanya awe kijana shupavu, anayejitambua na anayewajibika kikamilifu.

Kwa hiyo kulikuwa na ‘shule maalum’ za malezi ya vijana, kupitia Makambi ya Jando na Unyago. Siyo rahisi kujua kwa uhakika hivi sasa, ni familia au koo ngapi ambazo bado zinawapa vijana wao fursa hii. Kilicho wazi na kinachosikitisha ni kwamba mila hizi zimetelekezwa kitambo. Je zimeonekana hazina tija? Labda! Lakini ukweli ni kwamba zilisaidia sana kuwajenga vijana; na ushahidi uko wazi kabisa.

Kiuhalisia, kwa sasa, maadili ya watoto na vijana yameshuka sana, na madhara yake yanaonekana wazi katika utu uzima wa kijana, ambapo mtu mzima, pamoja na elimu yake kubwa, pengine ya Chuo Kikuu, anaonesha upungufu mkubwa kifikra, kitabia na kivitendo.

Katika zama hizi za utandawazi, malezi ya vijana yanakumbwa na changamoto nyingi. Kwa mfano, vijana wanakosa ‘mwalimu’ sahihi wa kuwafanya wajitambue na kujua kiundani juu ya ukuaji wao, maarifa wanayotakiwa kuwa nayo, na namna wanavyoweza kuzitambua hatari au fursa zinazoambatana na maendeleo ya sayansi na teknolojia, ili waweze kuchukua hatua stahiki. Vitu hivi vilifanyika katika makambi ya Jando na Unyago, pamoja na uduni wa mazingira ambamo vilifanyika.

Zamani walimu wa Jando na Unyago walikuwa  Mangariba au Makungwi, kwa niaba ya wazazi. Ilizoeleka kwamba sio mambo yote mzazi anaweza kuongea na mwanae. Kwa mfano, haikuzoeleka baba kuongea na binti wake kuhusu masuala ya hedhi; au hata mama, kumfafanulia binti yake mambo ya falagha atakayomfanyia mumewe mtarajiwa. Ombwe hili lilijazwa na Makungwi au Mangariba. Hawa hawakuficha kitu, kila kitu kiliwekwa wazi, vijana wajifunze.

Akisisitiza mafunzo haya, katika moja ya ziara zake, aliyekuwa Makamu wa Pili wa Rais Zanzibar, Balozi Seif Iddi, alisema: “Wizara ya Utamaduni, na wadau, jitahidini kurudisha utamaduni huu (Jando na Unyago), na kuyaboresha mafunzo yaliyotolewa, badala ya kuacha Taifa lizolewe na wimbi la utandawazi linalobeba na kuzienzi tamaduni za ki-magharibi, za kutojali na kupuuza maadili.”

Kwa hiyo, Jando na Unyago ilikuwa ‘chuo cha malezi’ bora. Yalikuwa ni mafunzo ya kumwingiza kijana katika utu uzima, ili awe mtu aliyekamilika ki-maadili na ki-utendaji. Kuhusu Unyago, mabinti ‘walichezwa’ mara tu walipovunja ungo. Hii ilikuwa ni ngoma ya kuwaingiza mabinti katika utu uzima, ikiwa ni pamoja na maisha ya ndoa.

Kama sehemu ya mafunzo haya, kila binti alishiriki michezo mbalimbali ikiwa ni sehemu ya mazoezi ya kumfanya awe na maadili yaliyotakiwa, na uwezo wa kupambana na changamoto zilizopo katika mazingira yake, kama mwanajamii na mke mtarajiwa.

Mafunzo ya Jando hali kadhalika. Vijana walipewa mafunzo maalum. Ni mafunzo ya kuwafanya kuwa watu wazima ili wawe na uwezo wa kutunza familia na jamii nzima. Ngariba alihusika kuwafanyia tohara na kuwapatia stadi za kazi na stadi za maisha pia. Wavulana baada ya kutahiriwa, wakisubiri kidonda kupona, walipatiwa mafunzo ya kuwajengea maadili bora.

Ili kumjengea kijana uelewa na umahiri wa stadi au maarifa yaliyokusudiwa, mafunzo haya yalijaa matumizi ya hadithi, nyimbo, misemo ya lugha za asili na vitendo vingi, vilivyolenga kujenga tabia za vijana na kutengeneza umoja, upendo na mshikamano wa kiukoo na kijamii.

Mzee mmoja aliyepitia mafunzo haya anasema, “hadithi, nyimbo na vitendo tulivyofanyiwa Jandoni vilijaa mafunzo matupu. Tulifundishwa mambo yote muhimu ya maisha hadi tukaiva. Tulifundishwa mila, desturi na miiko ya ukoo, nidhamu na kuheshimu watu, uwajibikaji, ujasiri, uvumilivu na majukumu ya kuilinda familia.”

Kungwi mmoja alipoulizwa kuhusu mafunzo aliyowapa mabinti alisema, “tuliwafundisha mila na desturi, usafi binafsi na mazingira ya nyumbani, kutunza nyumba, kupika, kutunza familia, malezi ya watoto, heshima, kufanya kazi kwa bidii, na jinsi ya kufanya mapenzi ili kudumisha ndoa.”

Kwa ujumla, mafunzo ya Jando na Unyago yalisaidia sana kujenga maadili ya vijana wa kike na kiume katika jamii hizo. Yalisaidia kuwaondoa vijana kutoka katika umri wa utoto kwenda umri mkubwa, na kujenga tabia zinazoendana na umri huo mpya. Mafunzo haya yaliwapa vijana uwezo wa kujitambua, kupambana na changamoto, kudumisha amani na upendo, kuzijua mila zao na kuwajibika.

Sasa, kama alivyoshauri Balozi Seif Iddi, wadau mbalimbali wanapaswa kujitahidi kurudisha utamaduni huu mzuri, na kuyaboresha mafunzo yaliyotolewa. Hata hivyo, kutokana na miundo mipya ya koo na famila zetu siku hizi, huenda imekuwa vigumu kuandaa na kutoa mafunzo haya au yanayofanana na haya, kama zamani.

Lakini tujiulize, je tuache tu mambo yajiendeshe yenyewe? Je, tuuache utandawazi ukitafune kizazi chetu? Hapana, tuna wajibu wa kujenga mifumo mipya inayoendana na maendeleo ya sasa. Na kwa kuanzia, sisi wazazi tuna wajibu mkubwa juu ya watoto wetu. Tuanze sisi, kuwape maadili mazuri kuanzia utotoni, na tuendelee kuwa nao karibu hadi wakiwa shuleni au vyuoni. Tukifanya hivi tutaiokoa jamii yetu inayoangamia!

Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasirimali kivitendo. Anapatikana kwa e-mail: nzyy2001@gmail.com; Simu 0718219530

Fuata Hatua Hizi Uyaanze Maisha Ya Kustaafu Kiulaini

Maisha ya furaha baada ya kustaafu hayaji hivi-hivi, yanajengwa!

Habari rafiki,

Ukiweza kuongea na Wafanyakazi kuhusu  suala la kustaafu utagundua kuwa wengi huliona suala hili kama ‘tukio’ la siku moja, la mstaafu kufanyiwa sherehe na kisha kuagwa na wenzake wanaobaki kazini. Nasema hapana!

Kustaafu sio tukio, ni mchakato, unaohusisha mfanyakazi kujiandaa kuachana na maisha ya utumishi, na kuanzisha maisha binafsi, yanayotarajiwa kuwa ya raha, amani na mafanikio.

Katika kipindi cha ajira, mara nyingi ni vigumu kumtenganisha mtumishi na kazi aifanyayo – kwa jinsi wanavyoambatana; muda wote, kila siku, siku zote, kama uji na mgonjwa! Ndio maana wapo wafanyakazi wanapofikia siku ya kustaafu (tukio), hawajui pa kuanzia – hivyo hubabaika na kukosa amani, kwa kuwa hawakuwahi kujihusisha  na mchakato, kabla.

Wafanyakazi wenye maono hujihusisha na mchakato wa kustaafu kwa kuona mbali mapema na kuweka mipango…jinsi ya kujitengenezea maisha yenye staha baada ya kustaafu.

Kipindi cha mpito kuelekea kustaafu kina hatua au vipindi ambavyo ni vizuri kuvifahamu ili ujipange na kujiwekea mikakati stahiki.

Kwanza, kipindi kabla ya kustaafu. Kuna watu wanapendekeza kipindi hiki kiwe miaka 5 hivi, kabla ya tukio la kustaafu. Wengine wanasisitiza kuwa maandalizi yanapasa kuanza mara tu mtu anapoajiriwa. Hiki ni kipindi ambacho mtumishi anayejitambua huanza kughubikwa na fikra au ndoto za kustaafu, na pengine anakuwa keshaanza maandalizi.

Katika kipindi hiki, wapo wafanyakazi ambao huanza kubadili mwelekeo wa fikra zao; kutoka fikra za kujijenga kikazi (kujiongezea ujuzi, maarifa n.k.), kwenda katika fikra za kujiweka vizuri kiuchumi (mipango ya fedha), ikiwepo kuweka akiba au kuwekeza, wakijua siku ya kuachana na ajira iko karibu.

Kipindi hiki, huwa kimechanganya hamasa ya kutaka kustaafu, kwa baadhi (waliojipanga); na hofu, woga na wasiwasi kwa wengine, hasa mwaka mmoja au miwili kabla ya tukio.                                                                                                                                                

Woga hutokana na hisia kwamba huenda hawatakuwa na akiba ya kutosha, wakistaafu, kumudu majukumu kama: madeni, ada za watoto, ujenzi au tiba. Vilevile hawajui kama mafao watakayolipwa – yatalipwa kwa wakati, na kama yatawawezesha kuyamudu maisha baada ya kustaafu.

Pili, kipindi cha tukio la kustaafu. Hiki ni kipindi kifupi zaidi kuliko vipindi vingine vyote. Hii ni ile siku maalum…siku ya kusitisha ajira rasmi. Ki-ukweli hatua hii inatarajiwa ijae furaha, ndio maana huambatana na sherehe na burudani ambapo ndugu, marafiki na wafanyakazi wanaobaki hujumuika kumshika mkono wa heri mstaafu.

Hii ni hatua inayompatia mstaafu ‘uhuru’. Ni uhuru kutoka kwa mwajiri pamoja na sheria, taratibu, miongozo na majukumu yake – kuingia katika maisha binafsi nje ya ajira.

Wastaafu katika hatua hii hujiona kama wamefunguliwa minyororo, ambapo sasa huanza kufikiria kufanya mambo waliyoshindwa kuyafanya kutokana na kubanwa kazini – kama kusafiri, kuwa karibu na familia, kufanya vitu wavipendavyo (hobbies), na wengine huwaza kuendeleza miradi yao.

Wengine huamua kupumzika tu ili kuondoa msongo wa mawazo baada ya miaka mingi ya ‘kusota’ kazini, kimwili na kiakili. Ni kama harusi na fungate kwa wanandoa.

Tatu, kipindi cha kutojiamini-amini. Wakati tukio la kustaafu hujaa hisia zilizochanganyika na furaha ya uhuru, baada tu ya tukio hilo, mstaafu ghafla hujikuta hana furaha! Yaani mstaafu anapata unyonge ghafla, na kuhisi kuna kitu kinapungua, kinyume na matarajio.

Anaanza kujiona mpweke, mkiwa na asiye na kitu cha kufanya. Wakati mwingine hujiona kama hana maana yoyote mtaani, na hapa ndipo msongo wa mawazo huanza. Ni sawa na wanandoa – baada ya fungate kuna kipindi cha vitu kupishana-pishana kati yao, lakini baada ya muda huyazoea mazingira na mambo huwa sawa.

Ili kuepusha hali hii, inahimizwa mfanyakazi kujipanga vizuri katika kipindi cha kwanza. Mipango ya kiuchumi na kisaikolojia iliyolelewa kipindi cha kwanza matunda yake huanza kuonekana hapa.

Nne, kipindi cha kutulia na kusonga mbele. Hiki ni kipingi kigumu zaidi katika safari ya kustaafu na huhitaji uvumilivu, bidii na nidhamu. Kipindi hiki kinahusisha kupata majibu ya maswali: hivi mimi ni nani sasa, kusudi langu ni nini, nitafanya shughuli gani sasa, na nitautumiaje muda wangu?

Ukimudu kuunda utambulisho wako mpya unakuwa tayari, rasmi, umejitoa katika mikono ya mwajiri na kuanzisha maisha ya kujitegemea. Sasa, ili kuyaanza maisha haya kwa mguu mzuri, inashauriwa uanze na shughuli unayoipenda, au uliyokuwa ukiifanya taratibu katika kipindi cha kwanza. Ukianza kujitegemea kwa furaha, unapata tulizo la moyo, ambalo ni chanzo cha hamasa na afya njema uzeeni.

Tano, kipindi cha maisha yenye matumaini. Hiki ni kipindi kilichobaki hadi siku ya mwisho wa maisha ya mstaafu. Hiki ni kipindi ambacho mstaafu anapaswa kuwa ametulia, akifanya shughuli anayoipenda, inayompatia kipato na utulivu. Hapa anakuwa amejijengea mazingira na matumaini ya kumaliza maisha yake kwa amani.

Ikumbukwe, hiki ni kipindi ambacho wastaafu hukabiliwa na matatizo mengi ya ki-afya, yanayotokana na umri. Magonjwa ya moyo, presha na kisukari ni ya kawaida, hivyo inatarajiwa pawepo maandalizi mapema. Bima ya afya, chakula bora na mazoezi, ni moja ya maandalizi haya.

Kwa kumalizia, kupanga mapema kabla ya kustaafu ndio ‘siri ya urembo’. Wafanyakazi walio makini huwa na maono na muda wa kupanga. Hupanga jinsi maisha yao yatakavyokuwa baada ya kustaafu. Hupanga watafanya nini wakistaafu, na hupanga pia jinsi ya kuishi maisha ya furaha.

Kwa kufanya hivi, Wafanyakazi hawa huingia katika kustaafu ki-ulaini, bila woga wala kubabaika, wakijua wanaenda kuishi maisha ya kustaafu yenye heshima.

Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasirimali kivitendo. Anapatikana kwa e-mail: nzyy2001@gmail.com; Mobile: 0718219530

Kwa makala zangu zaidi, kuhusu Maisha ya Kustaafu, soma gazeti la MWANZO, la kila jumapili.

Jinsi Hadithi Zilivyochochea Kujenga Maadili Ya Vijana

Zamani, maadili ya vijana yalijengwa na kudumishwa kupitia hadithi simulizi

Habari rafiki,

Dhana ya mmomonyoko wa maadili inaelezewa kama hali ya kuanguka au kuzorota kwa maadili ya jamii fulani. Tafiti zinaonesha kwamba hili ni tatizo na usambaaji kwake ni wa kasi sana, hasa kwa vijana, kuliko wazee.

Kuna sababu kadhaa zinazosababisha hali hii ikiwa ni pamoja na utandawazi ambapo vijana wamekuwa na tabia ya kujifananisha na watu wa nchi nyingine  kwa kuiga hata mambo yasiyofaa. Sababu nyingine ni ukuaji wa teknolojia na mawasiliano ambapo kupitia mitandao ya kijamii vijana huona na kusoma kila kitu, kizuri au kibaya, na kufuata bila kuhoji.

Wazazi kutotimiza wajibu wao ni sababu nyingine ambapo wazazi wengi hushindwa kuwaelekeza au kufuatilia mienendo ya watoto wao. Yaani mzazi anakuwa hajishughulishi kabisa na kijana wake hadi anaanguka kabisa kimaadili na kuwa mtu asiye na hadhi yoyote.

Sababu nyingine ni ushawishi wa makundi rika. Hawa ni watu wenye umri unaokaribiana. Wanaweza kuwa marafiki, majirani au wanafunzi wanaosoma pamoja. Hawa wakikosa uangalizi hushawishiana kuanza kufanya maovu. Kuna kijana mmoja aliiga tabia fulani mbaya ya wenzake. Alipoulizwa baadaye ilikuwaje…alijibu, “niliambiwa niache ushamba wangu la sivyo watanitenga!

Kuna sababu moja ambayo huwa haisemwi sana! Ushawishi wa Makampuni ya biashara (promotions) kuwavuta watu kununua, una athari kubwa katika kubomoa maadili. Kuna tangazo moja nilikuta limebandikwa ukutani kwenye duka moja. Lililenga ‘ku-promote’ sigara fulani, hivyo lilionesha vijana watano wakiwa na vinywaji (pombe) mkononi na wamezungukwa na packet kadhaa za sigara.

Caption iliyotumika ilisema, “haya ndiyo maisha!” Sasa tujiulize, je kijana asiye na mtu wa kumuongoza atapona hapa? Wakati anaambiwa wazi kuwa kumbe maisha ni hizo pombe na hizo sigara? Je kijana huyu akija kuwa na pesa, halafu akawa mlevi, au akajenga uraibu wa uvutaji, tutamlaumu?

Maadili yanaelezewa kama kanuni zinaoonekana nzuri, zinazofaa na muhimu kwa jamii inayotaka hadhi na heshima. Sasa tujiulize, je ni njia gani zinafaa sasa kutumika ili kutibu mmomonyoko huu kwa vijana? Je, njia zilizotumiwa na wazee wetu zimepitwa na wakati? Hebu tujikumbushe historia kidogo, jinsi wazee wetu walivyotumia ‘hadithi simulizi’ kujenga maadili ya vijana wao, labda itatusaidia kufanya kitu.

Kupitia hadithi, wazee wetu wa zamani, pamoja na kutokuwa na elimu rasmi ya darasani, walifanya makubwa. Walitoa mafunzo kwa vijana wao, na msisitizo uliwekwa katika kuzijua na kuziishi mila na desturi. Walikuza uwezo wa kazi za mikono na kujenga uwezo wa kuzielewa stadi za maisha.

Tafiti zinaonesha kuwa hadithi simulizi zilipendwa sana na watoto, vijana na hata watu wazima. Hadithi mara nyingi zilisimuliwa wakati wa usiku kwa malengo matatu hivi. Kwanza kutoa burudani, pili kuwakusanya pamoja wanafamilia wakisubiri au baada ya chakula cha jioni, na tatu kuwapatia vijana mafunzo ya mila, desturi na maadili ya familia au ukoo wao.

Hadithi zilikuwa zinasimuliwa na wazee, hasa bibi au babu, kwa kuwa mara nyingi watu wa familia au koo hizo waliishi pamoja. Hadithi hizi zilisimuliwa kutegemea utamaduni wa jamii husika, hivyo kila jamii ilikuwa na hadithi zake kulingana na mazingira, mila na matukio. Lengo kubwa lilikuwa kujenga maadili ya vijana yaliyokusudiwa, ndani ya jamii hiyo.

Zamani zile kulikuwa na hadithi ndefu zilizoweza kusimuliwa hata siku nzima, kutoka kichwani mwa mtu. Hata hivyo kulikuwa pia na hadithi fupi, au ngano, ambazo nazo zilihifadhiwa kichwani na kutolewa ki-masimulizi kutoka kizazi hadi kizazi.

Ngano nyingi zilihusu mazingira yaliyomzunguka binaadamu kwa ujumla, yaani vitu vinavyogusa maisha yake. Zilikuwa zimebeba maudhui (ujumbe) kutoka katika matukio yaliyowahi kutokea au ya kutungwa. Lengo lilikuwa kutoa mafunzo maalum na kujenga maadili stahiki yanayoendana na mazingira yao.

Ngano hizi ziliweka uzito mkubwa katika simulizi zenye maadili ambayo mtambaji (msimulizi) alipenda yafike kwa hadhira (wasikilizaji) iliyokusudiwa.  Kwa mfano kama dhamira ni kusisitiza madhara ya uvivu au udokozi, basi ngano nzima itaelekezwa kusimulia jambo hilo. Mwisho wa hadithi mtambaji aliwaasa watoto/vijana wasifanye kama alivyofanya mhusika mkuu wa simulizi hiyo.

Kwa mfano kuna ngano iliyoitwa: “Mchelea mwana kulia mwisho hulia yeye”. Ngano hii ilisimulia kuhusu mzazi mzembe aliyemdekeza mwanae, akamwacha afanye anavyotaka, bila kumkanya, na mwisho wake mtoto huyo alianza kufanya ujambazi na ubakaji katika kijiji chake. Mambo yalivyozidi alikamatwa, akapigwa na kuishia jela!

Umuhimu wa hadithi hizi ulikuwa kutoa burudani, kuelimisha, na kukuza ushirikino, umoja na mshikamano katika jamii husika. Ngano pia zilitia mkazo katika kuonya, kuelekeza, kuhimiza na kutoa nasaha, ili kukuza maadili mema.

Mwandishi Kiango anasema, “hadithi ni chombo kilichotumika kuyabeba na kuyafikisha maadili kwa jamii. Kwa hiyo, kwa mtoto/kijana kusikiliza hadithi alijifunza maadili na namna bora ya kuishi na familia yake, na jamii kwa ujumla. Kwa kutumia hadithi, elimu ya maadili ilifika kwa walengwa haraka, kwa ufasaha na kwa msisitizo uliotakiwa.”

Kulikuwa na aina tatu za hadithi zilizosimuliwa siku hizo. Zilikuwepo hadithi zilizosisitiza makuzi mema ya mtoto, faida na hasara zake. Kulikuwa na hadithi zilizofundisha bidii ya kazi, umoja, ushujaa, ushirikiano na uvumilivu. Lakini pia zilikuwepo zilizosisitiza maadili ya ndoa, malezi ya watoto na upendo kwa famila.

Tofauti na hadithi zilizoandikwa, ngano zilisisimua zaidi. Ili kuwatia hamasa wasikilizaji, ya kusikiliza na kujifunza, msimulizi alitakiwa kuwa mwenye kumbukumbu nzuri, mchangamfu, mcheshi, msanii, na mjuzi wa mila na desturi za jamii husika. Hamasa pia ilichochewa na matumizi ya nyimbo, methali, misemo, lugha ya picha, na hata utani katika masimulizi.

Kuna athari kubwa ya utandawazi katika mmomonyoko wa maadili, lakini pia katika kudhoofisha vyombo au njia zilizotumika kubeba na kujenga maadili ya vijana, kama hadithi.

Vyombo vya habari navyo, siku hizi, vimejikita katika kuonesha fasihi za kigeni zaidi kuliko za kienyeji. Ukijumlisha na kushuka kwa utamaduni wa vijana/wazee kujisomea, hata maudhui yaliyomo katika ngano zilizoandikwa bado haziwafikii walengwa, na hii ni hatari katika ujenzi wa maadili ya jamii.

Sasa tujiulize, je tutumie njia gani ili tuukomeshe mmomonyoko huu wa maadili kwa vijana wetu?  Je, wazazi tunajua cha kufanya? Hili lilikuwa jukumu letu siku za nyuma. Je, baada ya kupuuza mbinu za wazee wetu, tumeweka nini badala yake? 

Jinsi wazee wetu walivyotumia hadithi simulizi kujenga maadili ya vijana wao, sisi wazazi wa leo tuna wajibu kama huu kwa vijana wetu. Ni wakati sasa wa kujipanga, kubuni mbinu, na kufanya kitu, la sivyo kizazi chetu kitanuka uozo!

Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasirimali kivitendo.

Anapatikana kwa e-mail: nzyy2001@gmail.com; Simu 0718219530

Mzazi Ukiwa Mzembe Ki-Malezi Utazodolewa na Wanao


Makabila mengi ya kiafrika yaliendesha mafunzo maalum kwa vijana kuwapatia stadi muhimu za maisha

Kimsingi, ni wajibu wa mzazi kumsaidia mtoto au kijana wake kuwa na taarifa au kukuza maarifa muhimu katika maisha yake. Na hili laweza kufanyika kupitia Stadi za Maisha. Haya ni maarifa ambayo yakitumika na kusimamiwa vizuri humjenga mtoto/kijana kuwa na mtazamo chanya kuhusu maisha yake binafsi na maisha yake ndani ya jamii.  

Stadi za Maisha ni moja ya masomo muhimu sana kwa mtoto/kijana kwani humpatia maarifa kuhusu anavyoweza kukabiliana na changamoto za maisha, na kupata uwezo wa kuziona fursa, na kuzikamata. Stadi hizi hujumuisha mbinu zinazoweza kumsaidia kuyafanya maisha yake yawe na uelekeo ulio sahihi, kujitambua, kuwa na nidhamu, na kufanya vitu sahihi, mahala sahihi na wakati sahihi.

Nimesema huu ni wajibu wako mzazi, kimsingi. Sasa, usipokuwa makini utajikuta unazodolewa na mwanao mwenyewe, na naomba usije kumlaumu mtu, pale mwanao atakapoanza kujitambua, kupata akili za ki-utu uzima, na kuanza kuhoji mambo. Watoto hawa hugundua kuwa udhaifu au upungufu wao katika maadili, kumbe umesababishwa na uzembe wa wazazi wao walioshindwa kutimiza wajibu.

Kiukweli wapo wazazi wanaojitahidi kuwalea watoto au vijana wao kimaadili lakini watoto hushindwa kuzingatia maelekezo, wakawa wakaidi, na kuishia kuharibika. Hii ni habari nyingine… inayopaswa kushughulikiwa ki-upekee. Lakini wapo pia wazazi, ambao kwa uzembe tu, huwafanya watoto wao wakose maarifa muhimu kwa maisha yao. Sasa, watoto wakijitambua, na wakagundua hili, mzazi kuwezi kukwepa kuzodolewa!

Hapo zamani kidogo, katika jamii za kiafrika kulikuwa na mila zilizohakikisha mtoto kabla ya kuingia katika umri wa kiutu uzima anapata maarifa au stadi ambazo zinalenga kumfanya awe mwanajamii anayejielewa, kujitambua na kuwajibika. Kulikuwa na ‘shule maalum’ za malezi ya vijana, kupitia matamasha ya jando na unyago. Cha kusikitisha, mila hizi zinazidi kumomonyoka kutokana na kasi ya ‘maendeleo’ ya utandawazi.

Hivi sasa, kutokana na sababu kadhaa, baadhi ya wazazi hawapati nafasi au hawajali au labda hawamudu kuwapatia watoto wao stadi hizi, na sasa baadhi ya vijana wameanza kulalamikia kuikosa haki yao hii. Wanawalaumu wazazi wao kwa uzembe au kushindwa kuwajibika.

Katika hili, kijana mmoja Alexis, anasema, “wazazi wangu walishindwa kunifundisha stadi muhimu za maisha, na sasa nimegundua kwa kuzikosa stadi hizo utotoni, naona nimepungukiwa vitu muhimu sana katika maisha yangu. Nilipowauliza kwa nini hawakujali kunipa maarifa hayo, walijibu kwamba hata wao hawakuwahi kufundishwa na wazazi wao. Nilisikitika!”

Kijana mwingine Gavin anasema, “najua wapo wazazi wanaowafundisha watoto/vijana wao stadi za maisha…lakini najua pia kuwa wapo ambao hawana muda huo kwa kuwa hata wao hawakuwahi kufundishwa, au hata kama walifundishwa…wao hawana uwezo wa kuwafundisha watoto wao, na hili ni tatizo! Hata hivyo, najua pia kuna watoto ambao ni wakaidi, hawataki kujifunza,…pamoja na jitihada za wazazi wao”

Akitoa maoni katika mdahalo mmoja, kijana Bitter anasema, “nimekuzwa na wazazi ambao msisitizo wao mkubwa ulikuwa kusoma kwa bidii ili nifaulu masomo yangu vizuri, na waliniambia kila mara, ‘elimu ndio kila kitu’! Kwa kuzingatia maelekezo yao, nimekuja kugundua kuna maarifa muhimu sana, nje ya darasa, sikuweza kuyapata, mfano ujenzi wa fikra tunduizi, uthubutu, ujasiri, uchambuzi, kutoa maamuzi na uwezo wa kujitegemea.

Akionesha madhara mengine ya kunyimwa stadi hizi, Kijana Bitter anasema, “kuna kitu muhimu ambacho nimekuja kugundua hivi karibuni, ambacho kimenisononesha sana. Nimegundua sikupewa hata stadi zinazonigusa moja kwa moja; kama kufanya usafi, kuoga, kupika, kufua, na hata kupiga mswaki. Sikuwahi kufikiria kitu hiki zamani, kwamba vitu hivi kumbe huwa vinafundishwa na wazazi majumbani, inasikitisha!”

Kijana mwingine anasikitika kwa kusema, “jinsi ninavyokuwa mtu mzima na kuanza kutambua mambo ndivyo ninavyobaini kuwa wazazi wangu hawakuwajibika ipasavyo kwangu. Ukweli, hawakunipa zana au ‘silaha’ kwa ajili ya kuyajenga na kuyalinda maisha yangu. Kuna mambo nahangaika kuyafanya mwenyewe hivi sasa, ingawa ukweli napata wakati mgumu, na wazazi wangu hawana namna ya kunisaidia, wameshachelewa!”

Sasa, ukifuatilia maoni haya utakubaliana na mimi kuwa baadhi ya watoto wanaofika katika umri wa kiutu uzima wakiwa hawana stadi muhimu za maisha, hawakutaka kuwa hivyo. Walijikuta hivyo ukubwani na baadaye kugundua kuwa kumbe wazazi wao kuna kitu hawakuwafanyia. Hata hivyo vijana hawa hawapaswi kukata tamaa na kuacha kufanya jambo. Wanapaswa kujiongeza.

Mchangiaji mmoja katika mjadala kuhusu suala hili anasema, “nawasikitikia na kuwapa pole vijana wote waliokosa stadi muhimu za maisha, kwa kuwa wazazi wao walishindwa kuwajibika. Hata hivyo, pamoja na wazazi kukunyima stadi hizi, angalau wape shukrani, kwani walikulea ukawa na afya njema, na pengine kuhakikisha umepata elimu nzuri ya darasani.”

“Kwa kuwa sasa wewe ni mtu mzima, na sasa unajitambua, na unatambua nafasi yako katika jamii, unapaswa kuchukua hatua haraka! Acha kulalamika na badala yake anza kujifunza mwenyewe vitu vyote ulivyovikosa utotoni. Hili linawezekana, na wapo waliobadili maisha yao kabisa hadi watu wakawashangaa!”

Anasema, “ni kweli kama mtoto, ulipaswa kupendwa, kupewa malezi bora, kufundishwa maadili n.k. Lakini kama hukupata bahati hii utotoni, usianze kulia-lia. Kubali hili limeshatokea, kilichobaki ni kufanya kitu. Cha kuzingatia ni kwamba stadi yoyote unayoihitaji sasa, ambayo hukuipata utotoni, jiwekee mpango na mkakati wa kuipata. Na hata wale waliopatiwa stadi hizi, bado kuna haja ya kujifunza zaidi ili kujenga umahiri.”

Hatua ya kuchukua: wakati kijana unaweza kuungwa mkono, na kusikitikiwa na kila mtu, pale utakapoonesha kusononeshwa na matokeo ya wazazi wako kushindwa kuwajibika na kukupatia maarifa muhimu kwa ajili ya maisha yako, kwa upande mwingine unapaswa kukumbuka msemo huu, ‘yaliyopita si ndwele, tugange yajayo’!

Ukishalijua hili, una wajibu sasa wa kulibeba jukumu hili wewe mwenyewe. Unapaswa kutafuta njia mbalimbali za kukupatia maarifa na stadi zote ulizozikosa. Uzuri, tayari sasa unajua unahitaji nini katika maisha yako, au unataka kuwa nani, na unataka kukuza vipaji gani, hivyo chukua hatua!

Wakati fulani inabidi tuwasamehe wazazi wetu kwa kushindwa kuwajibika. Wazazi wengine walijaribu kufanya walichoweza, kulingana na jinsi wao wenyewe walivyolelewa, habati mbaya hawakufikia viwango stahiki. Pamoja na hayo, ujumbe muhimu kwao ni kwamba wanapaswa kuujua ukweli huu, na kujifunza kwamba walishindwa kutimiza wajibu.

Mzazi unapaswa kujua kuwa suala sio kuzaa na kumleta mtoto duniani – hapana. Kilicho muhimu ni kuhakikisha kuwa mtoto, mapema kabisa, anasimamiwa ipasavyo ili aweze kuwa na maarifa na taarifa zote muhimu kumfanya awe kijana anayejitambua, kufanya mambo kwa usahihi na kuyamudu vyema mazingira yake. Usipofanya jukumu lako hili ujue utalaumiwa, utaaibika na utazodolewa hata na mwanao mwenyewe!

Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasirimali kivitendo.

Anapatikana kwa e-mail: nzyy2001@gmail.com; Simu 0718219530

Kwa Mfumo Huu Wa Elimu Tutawapoteza Vijana Wengi!

Mtoto akijengewa tabia ya udadisi uwezo wake wa kufikiri, kuchambua na kuhoji mambo hupanuka

Habari rafiki,

Katika makala hii nimejadili tabia ya udadisi waliyonayo watoto. Nimesema, “wanapokuwa wadogo, watoto ni wadadisi sana na wana hamu ya kukifahamu kila kitu kwa kina. Watoto hudadisi mambo mapya na hupenda sana kuuliza maswali.” Kutokana na tabia hii, watoto hujenga uwezo mkubwa wa ubunifu.

Mtafiti wa Saikolojia ya Watoto, Prof. Susan Engel anasema uwezo wa mtoto kudadisi mambo kwa kuuliza maswali, huendelea kupungua jinsi mtoto anavyokuwa, na anapofikia umri wa utu uzima, uwezo huu hufifia kabisa.

Sasa, ili tuweze kujua kwa nini uwezo huu hupungua ni vyema tukafuatilia makuzi ya watoto. Je watoto wanalelewa katika utaratibu gani? Je wakiwa shule wanafundishwa nini na kwa njia gani? Je hayo wanayofundishwa, na njia inayotumika, yanawasaidia kujenga au kukuza uwezo wao wa kufikiri na kudadisi?

Maswali haya yanatupeleka katika kuudodosa mfumo wetu wa elimu kwa mtazamo wa jumla, hasa nchini Tanzania. Katika mfumo wetu, mwalimu ndiye mjuzi wa mambo. Mwanafunzi kazi yake ni kusikiliza na kufuata maelekezo ya mwalimu!

Katika shule zetu, watoto wanazoeshwa kufanya vitu kama walivyoelekezwa na mwalimu, na wanaaminishwa kuwa huo ndio uwezo, yaani hiyo ndiyo akili. Mtoto mwenye uwezo wa kukariri kila kitu kama mwalimu alivyoandika ubaoni, huyo ni kipanga…huyo ana akili!

Mtoto mwenye uwezo wa kukumbuka vitu vichache alivyofundishwa lakini akajaribu kujadili,…kuongeza vitu vingine, kwa mtazamo wake, huyu ni mjinga, yaani hana akili. Na ukweli, huyu anapata alama ndogo na kuishia kufeli.

Darasani, watoto wanafundishwa kukaa kimya na kutulia. Wanahimizwa kusikiliza zaidi kuliko kuongea, hivyo fursa ya kuuliza maswali huja kwa nadra. Katika andiko moja, Mwandishi Jenerali Ulimwengu anahoji kama watoto wetu, siku hizi, wanafundishwa udadisi, kisha anatoa maoni…, “mtoto aliyelelewa katika msingi wa kuuliza maswali…huyu ndiye mwanajamii bora zaidi kwa Taifa.”

Mfumo wa elimu tulionao, huchagua aina ya masomo ambayo kila mtoto anapaswa kuyasoma. Watoto wanatakiwa kusoma masomo yanayofanana na kusisitizwa kuyaweka kichwani na kuyarudiarudia kwa ajili ya mtihani.

Wakishafundishwa, baadaye mwalimu huwapa watoto mtihani ulio na maswali sawa kwa wote ambapo kwa kila swali linaloulizwa kuna jibu moja tu lililochaguliwa na mwalimu kuwa ndilo ‘jibu sahihi’. Ukijibu nje ya hapo wewe huna uwezo, ni ‘kilaza’.

Mwalimu Richard Mabala, katika makala moja anasema, “siku hizi mfumo wetu wa elimu kuna kitu kinaitwa ‘majibu sahihi’. Mtoto akijibu tofauti na majibu hayo, huyo hajui, na atafeli! Majibu yanayoonesha kuchambua, kutafakari na kuhoji mambo yaliyozoeleka, hayatakiwi!”

Katika jukwaa moja la mijadala, mchangiaji mmoja aliandika, “mwalimu wangu wa historia, kidato cha tatu, alikuwa na tabia…ukiandika jibu tofauti na points zilizomo kwenye notes alizofundisha, ujue hupati maksi…ukweli sikupenda staili hii ya ufundishaji wa kukaririshwa!”

Sasa, kwa mfumo huu, watoto wanajenga utegemezi mkubwa kwa mwalimu, na hivyo hawawezi kufikiri na kuandika kwa mtazamo na staili yao. Mwandishi mmoja anasema hapendezwi na mfumo huu wa elimu; yaani mfumo ambao unamnyima mtoto uwezo wa kudadisi na kuchambua mambo.

Huu ni mfumo ambao mtoto anafundishwa kuwa kukosea ni udhaifu, hivyo anajitahidi kumsikiliza vyema mwalimu na kukariri alichofundishwa, na mtihani ukija anajibu bila kukosea. Ukweli, kumkataza mtoto kukosea ni kumnyima fursa ya kujifunza kutokana na makosa ili ajue kujirekebisha.

Mfumo wetu wa elimu unamsikitisha mwananchi mmoja ambaye anasema, “nimesikitika kusikia, siku hizi, vile vitabu vya fasihi ya Kiswahili na Kingereza, wanafunzi hawasomi tena. Vitabu hivyo, sasa vimetengenezewa muhtasari kwa ajili ya watoto kukariri na kujibu mtihani. Kama hii ni kweli, hamu na uwezo wa mtoto kusoma vitabu, na kudadisi, itazidi kushuka.”

Kwa hali hiyo, vipaji vya watoto huanza kufa taratibu, na watoto huanza kutengenezwa kuwa watu wanaofanana kitabia, kiujuzi na kifikra, na hata uwezo wao wa ubunifu huzidi kudidimia kila siku.

Ukweli, elimu inatakiwa iwezeshe ukuaji wa fikra na vipaji vya watoto. Elimu inapaswa kuwaongezea watoto hamasa ya kuhoji na kujaribu vitu vipya. Wapo watoto ambao wangependa kuchambua mambo na kujibu maswali kwa mawazo yao, lakini wamejikuta wakilazimishwa kutoa majibu ‘yanayotakiwa’. Baada ya muda watoto hawa hugeuka makasuku!

Mwandishi mmoja anaandika, “elimu yetu inazalisha watu wenye uwezo mdogo sana wa kufikiri, kwa kuwa tunajali sana yale tunayofundishwa darasani, kwa mujibu wa mtaala uliopo. Hakuna msisitizo katika usomaji wa vitabu, hasa vya ziada, wala kujifunza stadi za maisha, nje ya darasa. Hii inashusha sana uwezo wetu wa kuitazama dunia kwa mapana yake.”

“Elimu nje ya darasa ni muhimu sana. Nimekutana na mtu, ana digrii lakini hawezi kuandika wasifu (CV) yake. Mwingine ana digrii ya Teknolojia ya Habari (ICT), lakini hawezi kabisa kutuma barua pepe (e-mail).”

“Suala hili limeniumiza sana kichwa, na mwisho nimebaini kuwa haya ndio matunda ya mfumo wa elimu, wa kukaririsha watoto. Mtoto aliyepewa elimu kwa kukariri hawezi ‘kujiongeza’, kupata maarifa mtambuka, kwa kuwa akili yake imefanywa kuwa tegemezi kwa mwalimu au mada za darasani tu. Upungufu huu hujionesha wazi katika interview au katika utendaji, kazini” Anasema.

Kikubwa hapa ni kwamba mfumo wetu wa elimu, na mbinu za ufundishaji vinatakiwa  kumjengea mtoto mazingira ya kujifunza ambayo hayataua uwezo wake wa kufikiri na kuhoji. Kama ilivyo kwa wazazi, walimu pia wanapaswa kuwa makini, kugundua vipaji vya watoto, kuvikuza, na kuwaongezea uwezo na hamu ya kujua mambo kwa kuhoji na kudadisi, badala ya kukariri!

Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasirimali kivitendo.

Anapatikana kwa e-mail: nzyy2001@gmail.com; Simu 0718219530

Kipi Bora – Kuweka Akiba Au Kuwekeza?

Kuziacha pesa zako nyingi, zikae benki muda mrefu, ni hasara. Jifunze Uwekezaji!

Habari rafiki,  

Kuna swali nimewahi kuulizwa, “je kipi bora zaidi kati ya kuweka akiba na kuwekeza?” Yaani kati ya kuweka akiba na kuwekeza, uamuzi gani unaleta manufaa zaidi. Nilitoa jibu langu…lakini nilibakiwa na dukuduku…kupata undani wa swali hili, hivyo nilianza uchunguzi. Nilitaka kujua kipi kina tija zaidi, lakini pia kipi kinatangulia.

Katika utafiti wangu, nimebaini kuna mitazamo tofauti katika kujibu swali hili.  Wapo wanaosema kuweka akiba kuna manufaa zaidi. Wengine wanasema uwekezaji ndio uamuzi wenye tija zaidi. Kwa majibu haya nimegundua hakuna muafaka katika hili.

Wanaosema kuweka akiba kuna manufaa zaidi wana hoja, na wanaosema kuwekeza kuna tija zaidi wana hoja pia, ingawa ukichunguza ataona vitu hivi vina uhusiano mkubwa. Mwandishi mmoja  anasema, “mtu anapoamua kuweka akiba anakuwa na malengo yake anayotaka kuyafanikisha.”

Anasema kuna manufaa au faida tatu katika kuweka akiba, zinazobebwa na malengo ya mtu. Kwanza, kudunduliza fedha kwa ajili ya dharura, ili tatizo likitokea fedha ziwepo tayari kulitatua. Pili, kudunduliza fedha ili kufanya au kukamilisha jambo, hasa linalohitaji kiasi kikubwa cha fedha, kwa mfano ujenzi wa nyumba. Tatu, kudunduliza fedha kwa ajili ya uwekezaji.

Ukizichunguza, faida zote hizi zina tija. Suala la dharura linafahamika wazi, kwa kuwa hakuna anayejua atapata tatizo gani wakati gani; kuna ajali, magonjwa, majanga n.k. Hivyo unapokuwa na akiba, unapata urahisi na uharaka wa kukabiliana na dharura hiyo.

Kuweka akiba kwa ajili ya kukamilisha jambo kubwa, linalohitaji pesa nyingi,  ni uamuzi wenye tija pia. Kama una lengo la kujenga nyumba au kununua gari , miaka mitatu au minne ijayo, maana yake ni kwamba utahitaji pesa nyingi zitumike. Hapa uamuzi unaweza kuwa kuweka akiba hadi ufikishe kiasi kinachotosha. Wapo pia wanaoweka akiba kwa ajili ya kulipia ada za watoto.

Lakini kuna hili la kuweka akiba kwa lengo la uwekezaji. Sasa angalia, unapoifikia pointi hii, kuna jibu unapata, kwamba kuweka akiba, na kuwekeza, ni vitu vyenye uhusiano mkubwa. Kumbe huwezi kuwekeza kama huna akiba.

Hata hivyo, tofauti na akiba kwa ajili ya kufanyia jambo kubwa, kama kununua nyumba, akiba kwa ajili ya uwekezaji sio lazima ifikie kiasi kikubwa sana, ndipo uwekezaji au biashara ianze.

Katika suala la uwekezaji, kinachotangulia huwa ni wazo, yaani unataka kufanya shughuli au biashara gani. Ukishalijua hili unaweza sasa kulikatakata lengo lako kuu kuwa malengo madogo-madogo ili usilazimike kuanza na kitu kikubwa sana mwanzo.

Fahamu, biashara inahitaji kuendewa kwa umakini, kidogo-kidogo, huku ukijifunza kwa jinsi unavyoendelea. Kwa kuanza kidogo-kidogo inasaidia pia kupunguza kiasi cha mtaji wa kuanzia.

Kwa hiyo, unapoweka akiba kwa ajili ya kuwekeza, hakuna sababu ya kusubiri hadi fedha ziwe nyingi sana ndipo uanze. Weka akiba ukilenga kwanza kiasi cha kuanzishia biashara. Ukishaianza tu kinachobaki ni kuikuza kidogo-kidogo kila unapopata fedha za ziada.

Unaweza kuwa na akaunti ya akiba kwa ajili ya dharura, kwani hii ni muhimu kuwepo. Unaweza kuweka kiwango fulani cha fedha kinacholenga dharura tu. Kwa hiyo pesa yoyote inayozidi kiwango hicho unaiingiza katika uwekezaji.

Uwekezaji sio kitu rahisi, ingawa sio kitu cha kuogopwa pia. Ili umudu uwekezaji unatakiwa kujifunza maarifa ya kuendesha biashara. Unatakiwa ujue unataka kufanya nini na ujue siri za hicho unacholenga kukifanya. Siri hizo utazipata kupitia utafiti, unaotakiwa kuufanya.

Wapo wafanyakazi wanaoweka akiba kwa maandalizi ya kustaafu. Wakati, huu ni uamuzi mzuri kufanya, kuna kitu cha ziada hapa. Kustaafu ni kitendo cha kuachana na mwajiri, kwenda kuanzisha maisha binafsi, yanayotarajiwa kuwa mazuri na yenye mafanikio.

Mfanyakazi ukistaafu unatakiwa uendelee kuwa na kipato kinachofanana au kuzidi kile cha mwajiri. Hivyo, unatakiwa ajijengee uwezo ili ukistaafu upate urahisi wa kutengeneza kipato hicho. Kwa hiyo, wakati tabia ya kuweka akiba ni jambo zuri, kujifunza tabia ya uwekezaji, ndani ya ajira, ni jambo zuri zaidi.

Tatizo la kujaribu kukusanya kiasi kikubwa cha akiba ni kwamba kuna hatari ya kukuta, siku moja, kiasi hicho kimetumika na kwisha. Inaweza kuwa kwa sababu ya dharura, au matumizi tu yasiyo na maana, ya kuridhisha nafsi.  

Hili hutokea, kwani kuna wakati watu hutumia akiba zao kununua vitu visivyo na maana, vinavyotumika mara moja tu halafu basi; wakati vimetumia fedha nyingi. Watu hununua vitu hivyo kuwakoga au kuwafurahisha wengine n.k.

Pamoja na hayo, kuziacha pesa zako nyingi, zikae benki muda mrefu, ni hasara! Riba za benki kwa pesa ya akiba ni ndogo, na faida yake ni ndogo, isiyo na tija. Kwa hiyo, wakati nahimiza tabia ya kuweka akiba, nataka pia kuhamasisha tabia ya kuwekeza.

Kwa kuwa uwekezaji huanza na uwepo wa akiba, kuna namna mbili za kuweka kiwango cha akiba. Unaweza kutumia asilimia ya kipato chako, mfano asilimia 15; au unaweza kuweka kiwango fulani, mfano shilingi 20,000 kila mwezi, na jitahidi usiziguse! Na hii ndio nidhamu ya kuweka akiba.

Napenda kusisitiza maarifa ya uwekezaji, watu wajifunze, na hili ni kwa wote; wafanyakazi na wajasiriamali. Na hapa siongelei uwekezaji kwenye stocks au bonds, naongelea biashara. Wanaoyakosa maarifa haya hujikita zaidi katika kuweka akiba tu. Ukifanya hili peke yake, ukakosa mipango, huwezi kupata maendeleo. Usije kushangaa siku moja tu kujikuta huna akiba hiyo!

Unapaswa kuwa na mipango na mikakati ya kutumia akiba yako kama mtaji, ili mtaji huu utumike kukuzalishia kipato zaidi kupitia shughuli au biashara unayoendesha. Kwa hiyo, ukishaanza kusanya akiba (mtaji) anza mara moja kufikiria utafanya biashara gani, utahitaji kiasi gani kuanzia, na lini utaanza. Ukiyaweza haya, una nafasi kubwa ya kufanikiwa!

Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasirimali kivitendo.

Anapatikana kwa e-mail: nzyy2001@gmail.com; 0718219530

Wahitimu Wa Chuo Kikuu Naombeni Masikio Kidogo!

Kuifikia ngazi hii ya elimu ni mafanikio makubwa, ndio maana utaona furaha waliyonayo wahitimu hawa!

Habari rafiki,

Hii ni makala maalum kwako wewe mhitimu mpya. Nakuandikia makala hii katika kipindi ambacho vyuo vingi nchini Tanzania vipo katika msimu wa mahafali au graduation. Ni kipindi cha furaha kubwa kwako, na kwa ndugu, marafiki na walimu wako pia. Kifupi, hiki ni kipindi muhimu sana kwako, ambapo unavuka rasmi mstari unaotenganisha maisha ya chuo na maisha halisia nje ya darasa.

Katikati ya furaha hii, ukiwa unasheherekea kumaliza chuo na kutunukiwa cheti, stashahada, shahada ya kwanza au shahada ya uzamili, usije ukajisahau. Unapaswa kukumbuka kuwa sasa ndio unaingia rasmi kwenye ‘maisha halisia’. Ndio, una shahada, lakini hicho unachopewa mkononi ni kipande cha karatasi tu ‘kinachovutia’. Usipoweza kukibadilisha kuwa pesa kitabaki kikaratasi tu, na hakitakuwa na maana.

Juzi juzi katika gazeti moja la nchi jirani limekutana na maoni ya msomaji mmoja wa gazeti hilo yakisema, “mimi kama mmoja wa wahitimu wa chuo kikuu, Kenya, wakati fulani nawaona watoto wamevalia sare zao nzuri wanaenda shule…najiuliza hivi hawa wanasoma ili waende wapi…wakati mimi nazunguka na vyeti vyangu kutoka ofisi moja kwenda nyingine, wala sijaiona hiyo ajira”.

Hapa Tanzania pia katika mtandao mmoja nimekutana na bango lililobebwa na kijana mmoja likiwa limeandikwa, “ndugu zangu Watanzania naombeni ajira…ni mimi Electrical Technician (mtaalamu wa umeme) ambaye sina mtu wa kunishika mkono.” Huyu ni mmoja wa vijana wengi wanaomaliza vyuo, wanaingia mtaani kutafuta kazi. Je unajua mtaani kukoje?

Lengo la makala hii ni kukutaarifu wewe mwanachuo unayeingia mtaani, kuwa ajira (kuajiriwa) kwa sasa zinazidi kuadimika. Hii inatokana na idadi ndogo ya ajira zinazozalishwa katika uchumi kupitia sekta binafsi na sekta za umma…ikilinganishwa na idadi ya wanafunzi wanaoingia katika soko la ajira kila mwaka. Vilevile nakusudia kutoa maoni ya nini cha kufanya.

Kimsingi kuna changamoto kubwa inayowakabili vijana wengi kwa sasa. Ni changamoto ya ukosefu wa ‘ajira rasmi’ serikalini, katika mashirika ya umma/binafsi, au katika taasisi zingine. Na kwa kuzingatia hili ndio maana tunasema ni wakati sasa vijana wetu wajitambue, na wayajue mazingira yalivyo sasa ki-uhalisia ili wachukue hatua stahiki.

Hapa kuna vitu kadhaa vya kujadili. Wakati fulani unaweza kuinyooshea kidole serikali, kwa kushindwa kuwa na mikakati ya kuzalisha ajira katika uchumi. Tena unaweza kuwanyooshea kidole wazazi, kwa kuwasisitizia watoto njia moja tu, ya elimu ya darasani, kama mwarobaini wa maisha yao. Au unaweza kuinyooshea kidole mitaala ya vyuo, au walimu, kwa kushindwa kuwapa watoto stadi za maisha nje ya darasa.

Kutokana na hayo, ni muhimu sasa kuzingatia kuwa, pamoja na maarifa ya darasani, watoto wajifunze pia maarifa nje ya darasa, yaani wayajue maisha halisi, ya mtaani. Haya ni maisha ya kutumia akili na ubunifu binafsi…na  yakichanganywa na yale ya darasani, mseto unaopatikana una tija kubwa. 

Mwandishi Scott Berkun anaandika kwamba kuna aina mbili ya watu ‘smart’ (wenye akili). Kuna Book Smart na Street Smart. Anasema book smart ni mtu mwenye akili au maarifa mengi ya darasani. Kwa bahati mbaya haya ni maarifa yaliyochaguliwa na watu fulani, kwa lengo lao fulani. Wanampatia mtu maarifa haya kwa kiasi na utaratibu fulani, ili akifaulu awafanyie kazi yao fulani kwa utaratibu fulani, halafu wanamlipa mshahara fulani.

Mhitimu huyu akiajiriwa anafanya kazi kwa miongozo maalum (rules, theories au principles) aliyofundishwa. Huyu akipata tatizo, haraka anakimbilia kusoma miongozo inasemaje, na anaifuata hiyo ili kutatua tatizo. Anapofikiria kupanda cheo anaomba kwenda kusoma shahada ya juu zaidi ambako anafundishwa theories na principles mpya ili azitumie akiwa katika nafasi ya juu kazini.

Watu ambao ni book smart, hupenda sana kijiendeleza kielimu kwenye fani zao, na wengi ni wazuri sana darasani, na ndio maana baadhi ya waajiri huwatafuta hawa inapotokea nafasi ya kazi. Tatizo la hawa, wasipoajiriwa, hawana plan B, na hii huwachanganya sana. Hawa huwa hawana macho ya kuona zaidi ya ‘upeo wa ajira’. Hawazioni fursa na wakitokea kuoneshwa hawana ujasiri wa kupambana.

Kwa upande mwingine kuna street smart. Hawa ni wale vijana ambao wanaweza kuwa na elimu ndogo tu, lakini wana maarifa ya ziada kichwani. Haya ni maarifa ya nje ya darasa. Watu hawa wana uwezo mkubwa wa kujenga fikra bunifu (imaginations), na kuziona fursa. Hawa wana ujasiri/uthubutu wa kuanza na kupambana ili kuyatafsiri mazingira yao kuwa kipato.

Maisha ya vijana hawa huwa hayana kanuni maalum wala hayaongozwi na principles – bali ujasiri na uthubutu. Vijana hawa, kwa kutumia fikra bunifu, wana uwezo wa kuanzisha biashara yoyote…wakaongeza kitu juu ya biashara hiyo…au wakapunguza, kulingana na mazingira yalivyo, na kwa kufanya hivi wakajitengenezea kipato kizuri kwa ajili ya maisha yao.Sasa jichunguze mwenyewe, hivi wewe ni book smart au street smart?

Ukiichunguza mitaala ya elimu yetu utaona kuwa bado ina misingi ile ile ya kikoloni – yaani kuwaandaa vijana wachache, kwa kuwapa elimu ya darasani inayolenga kuwapatia wahitimu maarifa yanayotakiwa katika kufanikisha shughuli zao za kiutawala, na siyo kuwapa maarifa ya kuwawezesha kujitegemea.

Kwa hiyo hata sasa vijana wanaendelea kuamini katika hili – kwamba wanasoma ili waje kuajiriwa. Kwa aina hii ya mtaala kijana akimaliza chuo anabaki na elimu ya darasani tu. Hana maono…hana fikra bunifu…hazioni fursa na hivyo hawezi kujiajiri. Huyu asipoajiriwa anaona huu ndio mwisho wa dunia!

Sisemi kwamba kujiajiri ni kitu rahisi, hapana, sio rahisi na kuna changamoto nyingi, hasa kwa wanaoanza, na hasa wanaotoka katika chungu cha taaluma, vyuoni. Kuna suala la mtaji, ushindani katika soko, uzoefu mdogo wa biashara, na uwezekano wa kupata hasara kwa kile unachokifanya.

Wala sijasema maarifa ya darasani sio muhimu, la hasha. Ninachosema ni kwamba kila mtu ajitahidi kupata elimu ya darasani, lakini wakati unaingiza maarifa haya usisahau kuwa kuna maarifa mengine muhimu pia nje ya darasa. Ukiwa na maarifa haya unakuwa na balance nzuri katika maisha, na utaepuka kuwa tegemezi wa ajira pekee.

Vijana wenye maarifa nje ya darasa utawaona jinsi ‘wanavyochacharika’ na kujaribu kila kinachowezekana. Hawa huwa hawaoni haya, hawaogopi jua, vumbi wala mvua. Vijana hawa hawachagui kazi – wao kilicho muhimu kwao ni kipato halali na matamanio ya ‘kutoboa’. Hawa si watu waoga, ni watu wenye ujasiri na uvumilivu.

Vijana hawa utawaona wakikaanga chips, samaki au mihogo na kuitembeza mitaani. Wengine utawaona wakiuza juisi za miwa na wengine wakitengeneza sabuni na viungo vya mboga. Utawaona wengine wakilima bustani za mboga na wengine wakipamba maharusi na kupika vyakula vya sherehe, ili mradi kila mmoja anaingiza kipato na kuendesha maisha yake.

Wengi wa vijana hawa hawana vyeti vya kitaaluma kutoka vyuoni, wanatumia uzoefu wao wa maisha ya ‘kitaa’. Sasa wewe ‘msomi’ ukiingia mtaani na majivuno yako ya vyeti vya stashahada au shahada, utabaki unashangaa! Wakati unamaliza soli za viatu ukizunguka na bahasha yako ya kaki, au ukijibizana na wadogo zako mkigombea remote ya TV, ukisubiri msosi, vijana hawa wako mtaani wakiingiza rupia.

Ni aibu kwa msomi wa chuo kikuu kuwa tegemezi kwa wazazi au ndugu zako. Tena wapo wasomi ambao hawana hata aibu, huwasumbua vijana waliowaacha mtaani, ambao wengine ni darasa la saba tu, wakiwaomba hadi hela ya nauli, kwenda mjini kutembea.

Msomi usieweza kuziona fursa na kuzichangamkia, wewe ni msomi butu. Unazidiwa na kijana wa darasa la saba, halafu unajitutumua hapa…! Hivi maana ya elimu ni nini? Elewa usomi sio vyeti, ni uwezo wa kutengeneza vitu au thamani katika jitihada za kujitengenezea kipato.

Hatua ya kuchukua: kijana unaliyemaliza chuo na sasa unafanya mahafali una kitu muhimu cha kujifunza. Kitu hicho ni kujitambua. Tambua kwamba wewe ni msomi, na una maarifa, lakini kwa mfumo wetu wa elimu, bado unatakiwa kujiongeza. Jiepushe na kushupaza shingo kwa kufikiria ajira peke yake…kwani ajira hazipo za kutosha sokoni. Unapaswa kuelewa kuwa watu wanakwenda shule ili kupata maarifa, siyo kazi. Kazi ikitokea… sawa!

Ile kasumba inayokumbatiwa na wazazi wengi, kwamba mwanangu nakupeleka shule/chuo kizuri, soma kwa bidii ‘masomo ya maana’ ili ufaulu vizuri mitihani, upate alama za juu, baadaye kidogo utaajiriwa na kampuni nzuri, na utalipwa mshahara mkubwa, imepita! Hali imebadilika sasa. Ndio maana tunahimiza vijana wajifunze stadi za maisha ili wawe na mbinu mbadala za kupambana na kujitengenezea kipato bila kusubiri ajira.  

Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasirimali kivitendo.

Anapatikana kwa e-mail: nzyy2001@gmail.com; Simu 0718219530

Ukiamua Unaweza Kuwa Chochote Unachotaka!

Ni mazoezi tu na kujituma, hakuna kisichowezekana katika maisha

Habari rafiki,

Unaweza kuwa na elimu ndogo, au unatoka katika familia duni, lakini kumbe ukiamua, ukaweka nia na kutia bidii, maarifa na ubunifu, kisha ukaweka ujasiri, unaweza kufanya makubwa na kuwa chochote unachotaka. Utaniuliza kivipi? Nitakusimulia!

Hivi karibuni, nikiwa napitapita katika mitandao ya kijamii nilikutana na habari moja iliyonivutia. Ilikuwa na kichwa cha habari, “Shigongo atangazwa mwanafunzi bora, wahitimu wa shahada, Chuo Kikuu cha Tumaini.

Namfahamu Eric Shigongo, kupitia makala, vitabu, na magazeti yake, na mafundisho yake kupitia semina mbalimbali. Najua ana uwezo mkubwa ki-akili na ki-ubunifu, na ni mjasiriamali anayesifika.

Lakini najua pia kuwa hakuwahi kupata elimu ya sekondari, hivyo kwa taratibu ninazozijua, hana sifa ya kujiunga na Chuo Kikuu. Kwa sababu hii nilitamani kufuatilia kwa kina kujua undani wa jambo hili…hili la Shigongo kutunukiwa shahada ya Chuo Kikuu.

Ni baada ya kuisoma habari ile nilipobaini kuwa ni kweli Shigongo bado ana elimu ya darasa la saba tu, na kufahamu kuwa kumbe baadaye alipata sifa mbadala ya kusoma Chuo Kikuu. Aliingia Chuo kupitia mfumo uitwao Recognition of Prior Learning (RPL) ulioidhinishwa na Tume ya Vyuo Vikuu Tanzania (TCU). Kwa sasa kozi na mitihani ya RPL hutolewa na Chuo Kikuu Huria cha Tanzania (OUT).

Ilinibidi nifuatilie ili niufahamu vizuri mfumo huu wa elimu kwani najua wapo watu wengi wanaofanana na Shigongo kwa sifa za ki-elimu (darasa la saba au kidato cha nne waliopungukiwa sifa) lakini wana uwezo, vipaji na maono, na wana hamu ya kupata mafanikio ya ki-elimu (Shahada) kama yeye; tatizo… hawajui njia ya kupita ili kufanikisha hilo.

Katika kufuatilia nilibaini kuwa mfumo wa RPL umewekwa ili, pamoja na mambo mengine, uweze kuwasaidia kufika Chuo Kikuu watu wenye vipaji maalum – ambao kwa vipaji vyao wametoa mchango mkubwa katika jamii kupitia sekta au tasnia fulani walizojizatiti nazo. Kupitia mfumo huu mwombaji hupatiwa mafunzo maalum, na mtihani, ambao akiufaulu anapata sifa za kujiunga na Chuo Kikuu, kusomea Shahada. Shigongo alipitia njia hii.

Sasa, chini ya hiyo habari, niliyoisoma mtandaoni, kulikuwa na maoni yaliyotolewa na wasomaji kuhusu mada hii. Yaani mada inayohusu mhitimu wa darasa la saba (Eric Shigongo) kupata nafasi ya kuingia Chuo Kikuu bila kwanza kupata elimu ya sekondari. Nilipata hamu ya kujua watu wanasema nini juu ya jambo hili, na juu ya Bw. Shigongo mwenyewe.

Watoa maoni waligawanyika ki-mtazamo. Wapo waliouunga mkono mfumo wa RPL, kwamba ni mfumo mzuri na sahihi, na wapo waliouponda wakisema hautendi haki na umewekwa ili kuwabeba watu fulani maalum ili wapate sifa za ki-elimu bila kusotea.

Wapo waliompongeza Shigongo kwa jitihada, uthubutu na kujituma katika mambo anayoyafanya ki-jamii na ki-uchumi, na katika kujielimisha binafsi. Wapo pia waliomkejeli kwa kuchagua njia waliyoiita “ya mkato na ujanjaujanja”- kupata shahada ya Chuo Kikuu.

Walioandika maoni ya kuponda walisema mengi tu. Yupo aliyeandika, “yeye mwenyewe Shigongo amekiri hajapitia elimu ya sekondari, sasa kwa nini anatunukiwa shahada wakati hana sifa, hii ni aibu! Mimi ninachojua ni kwamba ili usome degree unapitia certificate halafu diploma na kisha degree. Sasa huyu Shigongo kapitia wapi? Haya ni maigizo, na kama kuna huu mfumo basi haufai!”

Mwingine aliandika, “shahada za kupewa hizo, watu tunasota kupata cheti cha kidato cha nne halafu muimba ngonjera mmoja anapewa bure shahada – aibu! Mimi naona mfumo huu umewekwa kuwabeba watu maarufu wasio na sifa. Na kama ni hivyo hakuna haja ya kwenda shule.”

Kuna aliyeandika, “yaani degree zetu siku hizi zinakosa hadhi kabisa. Hii itakuwa degree ya rushwa, maana degree za ngono na rushwa zimejaa siku hizi. Fikiria mtu anapata division three kidato cha sita lakini hapati fursa ya kujiunga na chuo kikuu, halafu mtu wa darasa la saba anaruhusiwa…huu ni upendeleo wa wazi! Yaani darasa la saba hadi chuo kikuu, …duu, hii kali!”

Walioandika maoni ya kupongeza walisema mengi pia. Yupo aliyeandika, “nawashangaa wanaolalamika Shigongo kupewa degree, wanachekesha! Kama umesoma, umepata vyeti, halafu hujawahi hata kuandika makala gazetini…hujawahi kutunga hata hadithi fupi… huo usomi wako uko wapi. Hivyo vyeti vinakusaidia nini? Sisi tunataka kuiona elimu yako katika vitu ulivyofanya. Shigongo amefanya hayo, na hiyo ndio maana ya elimu.”

Mwingine aliandika, “hongera Shigongo, na hapa ndipo utagundua maana ya elimu – elimu ni vitendoni matokeoni vitu vinavyoshikika na kuonekana. Elimu sio makaratasi na vyeti.” Anasema yeye siku zote alidhani Shigongo ni msomi wa Chuo Kikuu, kumbe alikuwa darasa la saba tu! “Kwa uzuri, mvuto na ubora wa hadith zake, na mafunzo mbalimbali anayotoa katika semina zake, huyu hawezi kuwa darasa la saba…na kama ni hivyo, basi Mungu kamjalia elimu asilia na kipaji cha aina yake!” Anasema.

Yupo aliyeandika kwamba yeye anaona tatizo ni sisi Watanzania. Tunathamini sana makaratasi. Anasema huyu Shigongo kafanya mengi makubwa. Yaani hata kama asingepitia njia hiyo, kwa maoni yake anasema alistahili kupewa hata degree ya heshima, kutambua mchango wake katika jamii.

Anasema huyu siyo darasa la saba tu, bali darasa la saba mwenye akili, uwezo, ubunifu na uzoefu, na kwamba wapo wenye elimu ya sekondari hadi Chuo Kikuu lakini hawana maendeleo yoyote, wala kitu chochote cha kuonesha, walichowahi kufanya kwa ajili yao au kwa jamii.

Mwingine aliandika, “wafuatiliaji wa hadithi, makala na semina za Shigongo nadhani wanaelewa jinsi mtu huyu alivyo na akili kubwa. Huyu anawazidi wasomi wengi hata wenye PhD. Yaani huyu ni daraja lingine huyu!”

Anasema, Mwanasayansi Albert Einstein na magwiji wengine wa zamani waliopewa sifa ya u-genius, sio wote walikuwa na elimu kubwa. Wapo ambao hawakuwahi kukaa darasani ila walikuwa na vipaji. Walibuni, waliunda, walitunga, walichonga na mambo mengi ya ajabu; yaani walifanya mambo ya kuibadilisha dunia.

Anasema, huyu Shigongo kaamua tu kutafuta njia ya kupata degree kama alama rasmi iliyowekwa inayoonesha ‘usomi’. Lakini hata asingepitia njia hiyo yeye tayari ana uwezo na kipaji cha kufanya mambo makubwa. Kwa mfano anasema vitabu kama ‘The secret that tortured my life’, ‘Why did you kill me Patricia’, na ‘The President loves my wife’, ni baadhi tu ya kazi zilizotukuka za huyu jamaa, halafu anakuja mtu anasema huyu ni darasa la saba…ajabu!

Albert Einsten aliwahi kueleza maana halisi ya elimu. Alisema, “elimu ni kile kitu kinachobaki kichwani baada ya kutoa yote uliyojifunza shuleni.” Kwa muktadha huu ndio kusema Shigongo ameonesha kuwa na elimu kubwa hata kabla ya kukaa darasani (sekondari). Hivi angekaa huko darasani ingekuwaje? Ndio maana alipofanikiwa kuingia Chuo Kikuu ameweza kuwa mmoja wa wahitimu waliofaulu kwa kiwango cha juu kabisa.

Mtoa maoni mmoja aliandika kwamba hata hivyo siyo Shigongo peke yake aliyepitia njia hii ya RPL, wako wengi, ni vile Watanzania wengi sio wadadisi wala wafuatiliaji wa vitu vya maana….wanaendekeza uswahili na bla-bla…na hii inasababisha wengi kupishana na fursa, wakaishia kulalamika tu. Anahimiza watu waachane na ujinga huu.

Kuhusu Tume ya Vyuo Vikuu Tanzania (TCU), mchangiaji mmoja aliandika, “binafsi naona TCU wameweka mfumo mzuri sana wala hawakukosea. Kwa vyovyote walifanya utafiti, wakaandaa mitaala kisha wakatengeneza taratibu na miongozo ili wenye kukidhi vigezo waitumie njia hii wajipatie shahada ya Chuo Kikuu.

Huko mtaani kuna watu wengi wanafanya mambo makubwa yasiyoweza kufanywa na wanaojiita wasomi. Wapo wenye upeo mkubwa wa kuelewa mambo, wamefanya mambo makubwa na wanaheshimika mtaani…hawa sasa wamepewa njia ya kupitia.

Kuna mambo mengi ya kujifunza kupitia Eric Shigongo. Huyu ni mtu ambaye pamoja na kushindwa kuingia sekondari wakati huo, ni mpambanaji. Alikiona kipaji chake na kuamua kukifanyia kazi bila ajizi. Hakutazama elimu yake ndogo au umaskini wa familia yake, kama kizuizi. Alijichanganya na watu wenye elimu kubwa, uwezo na vipaji, na kuanza kujifunza hadi akaweza kufanya yale aliyoyafanya, yaliyompatia sifa ya hatimaye kuingia Chuo Kikuu.

Alipopewa nafasi ya kushukuru baada ya kutunukiwa shahada yake Eric Shigingo alisema, “…unaweza kuwa chochote unachotaka kuwa. Ukifuatilia maisha yangu ndio utaamini haya. Mimi ni darasa la saba, lakini leo natunukiwa Shahada ya Chuo Kikuu…unaijua sababu? Katika maisha tia nia, jitume, fanya kazi kwa bidii…utafanikiwa.”

“Mimi naamini hakuna bahati inayokuja peke yake, kinachotangulia ni bidii. Jinsi unavyojituma ndivyo unavyopata bahati zaidi. Mimi nilijiunga na Chuo hiki kupitia kipaji changu cha kuandika na uzoefu mkubwa nilioujenga kwa muda mrefu. Nilipoomba kujiunga hapa, pamoja na kufanya mitihani yao, nilionesha pia kazi zangu mbalimbali zilizoonesha uwezo nilionao.”

Kwa hiyo, kwa kumalizia, napenda kusisitiza kuwa Bw. Eric Shigongo, na wengine, wameisafisha njia. Kuna watu wengi ambao hawakuwahi kuijua njia hii aliyopita Shigongo hadi kujipatia Shahada. Hata hivyo, cha kuzingatia ni nia, bidii na kujituma, kama anavyohimiza Shigongo. Hakuna kitu kinachopatikana kirahisi.

Shigongo hakupata fursa ya kusoma Shahada kirahisi. Alikiona kipaji chake na kuanza kukifanyia kazi. Alianza kufanya vitu…alianza kuandika…na baadaye alitoa semina na mihadhara, na kazi zake zikafahamika na kuheshimika. Hata alipoamua kuomba Chuo Kikuu hakuwa na kizuizi, alibebwa na kazi zake nzuri.

Hivyo, kila mtu, na hasa vijana wanapaswa kuiga mambo na njia aliyopitia huyu jamaa. Najua wapo watu wengi wanaofanana na Shigongo kwa sifa za ki-elimu (darasa la saba au kidato cha nne waliopungukiwa sifa) lakini wana uwezo, vipaji na maono, na wana hamu ya kupata mafanikio ki-elimu (Shahada) kama yeye; tatizo… hawajui njia ya kupita.

Sasa njia imepatikana, lililobaki na kuifuata. Hakuna lisilowezekana. Unaweza kuwa chochote unachotaka katika maisha, ukiamua. Amua sasa!

Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasirimali kivitendo. Anapatikana kwa e-mail: nzyy2001@gmail.com; 0718219530

Fanya Hivi Kumjengea Mtoto Uwezo Wa Kufikiri (2)

Ukijenga ukaribu/urafiki na mtoto…anapata uhuru na utulivu wa akili na fikra…na anajenga udadisi

Habari rafiki,

Katika sehemu ya kwanza ya makala hii nimemnukuu mtaalamu wa masuala ya elimu, Brian Oshiro, akisema tukitaka vijana wetu waweze kuhimili vishindo vya dunia hii ya ushindani tunapaswa kuwafundisha kufikiri. Anasema ili tuwafanye wawe wajanja, ambao watakuwa tayari kupokea taarifa, kujenga maarifa, kukamata fursa na kutatua haraka changamoto, ni lazima tuwafundishe kufikiri, badala ya kuendekeza kukariri.

Katika makala hiyo nimejadili kwa ujumla juu ya umuhimu wa mtoto au kijana kujengewa uwezo wa kufikiri, nikasema hili ni jukumu ambalo linatakiwa kubebwa na mzazi, nyumbani, na mwalimu shuleni.

Hii ni sehemu ya pili, ambapo nitaingia ndani zaidi kufafanua wajibu wa mzazi, na njia ambazo mzazi anapaswa kuzitumia ili kumjenga mtoto au kijana wake ili awe na uwezo mkubwa wa kufikiri. Lakini nitajadili pia wajibu wa shule, hasa mwalimu, na njia wanazopaswa kutumia ili kumsaidia mtoto au kijana kujenga na kukuza uwezo wake wa kufikiri.

Kuna njia kadhaa ambazo mzazi ukizitumia zinaweza kumjengea mtoto au kijana wako uwezo mkubwa wa kufikiri, kama ifuatavyo;

Moja, mzazi jizoeze kumuuliza mtoto maswali yenye ‘kwa nini’.

Jitahidi, katika kila kazi au mchezo anaoshiriki mtoto, aulizwe ‘kwa nini’. Kwa mfano, “unadhani kwa nini tunapanda miti kuzunguka nyumba yetu” – na siyo, “nyumba yetu imezungukwa na miti mingapi” Sikiliza hoja zake, ukionesha kujali, kisha kwa lugha rahisi msaidie kuziweka vizuri hoja zake, au msahihishe alipokosea.

Mbili, mtoto akiuliza swali usimjibu moja kwa moja.

Jenga tabia ya kulisoma swali lake kisha muulize taratibu, “kabla sijakujibu, wewe unadhani jibu la swali lako ni nini”. Lengo hapa ni kuanza kuitanua ‘misuli’ ya ubongo wake, kufikiri. Msikilize kwa umakini akijibu, kisha toa maoni yako na ufafanuzi.

Tatu, fuatilia vitu mtoto wako anafanya na onesha kujali.

Ukiona anataka kufanya kitu cha hatari, ingilia kati, muulize kwa nini anataka kufanya hivyo, msikilize. Hapa ataitumia akili yake kutoa ufafanuzi, baadaye mweleze hatari iliyopo na madhara yake, na njia bora ya kufanya jambo hilo.

Nne, jadiliana na mtoto kuhusu changamoto zake

Mtoto anapokutana na tatizo au changamoto akaomba msaada, jenga tabia ya kutatua changamoto hizo kwa kujadiliana naye chanzo cha tatizo na njia kadhaa za utatuzi, kisha mpe yeye nafasi ya kutoa utatuzi wa mwisho, na aseme kwa nini kachagua njia hiyo. Mzoeze mtoto kujua vitu kwa ushahidi, siyo kwa kudhania tu. Hapa anapata uwezo wa kujenga fikra na kutoa maamuzi.

Tano, usipende kumdhibiti mtoto bila sababu.

Naomba niseme kuwa uwezo wa mtoto kufikiri huanza kuuawa nyumbani, chini ya usimamizi wa wazazi wake. Baadhi ya wazazi huwapokonya kabisa uhuru watoto wao, wakidhani wanawasaidia.

Yaani kila anachotaka kufanya mtoto, mzazi anaingilia kati. Utasikia, “acha kuchezea simu yangu…utaniharibia”, au “nisikuone unachezea makopo au kisu, ukijikata nakuchapa!” Kauli hizi hutolewa na wazazi wakimuona mtoto ana tabia ya utundu. Bila kujua, wazazi hawa huchangia kuua vipaji na uwezo wa kufikiri wa watoto wao. Kumsaidia mtoto huyu mwezeshe kufanya hayo bila yeye kuathirika au kuharibu kitu chako.

Kwa upande wa shule, kuna njia (approach) kadhaa ambazo mwalimu akizitumia zinaweza kumjengea mtoto uwezo mkubwa wa kifikra, kama ifuatavyo;

Moja, kijana ajengewe uwezo wa kuchambua mambo

Walimu wana nafasi nzuri ya kushawishi mitaala ya elimu ifanyiwe marekebisho, ili iweze kumjengea kijana uwezo wa kuumba mawazo na kuja na ubunifu. Mfumo wa ufundishaji na utungaji mitihani uboreshwe ili umjengee kijana uwezo wa kufikiri na kuchambua mambo.

Kwa mfano, darasani, swali likiuliza, “taja au orodhesha vitu” lisiishie hapo. Kuwepo na nyongeza ya “kwa vipi” au “kwa nini”. Ukiuliza ‘taja’ peke yake, siku hizi ni rahisi mtoto ku-google akaja na majibu kibao. Lakini ukiongeza “kwa nini”, hapa mtoto atalazimika kusugua kichwa, kufikiri, na hapa ndipo akili yake inajengeka.

Mbili, walimu waondoe utamaduni wa kupenda kuogopwa na wanafunzi.

Tabia hii inaonekana sana katika nchi za Kiafrika ambapo kuna ukuta mkubwa kati ya mwalimu na mwanafunzi, unaoondoa kabisa uhuru wa kijana kuuliza, kuhoji au kumkosoa mwalimu. Walimu huwa wakali muda mwingi, wengine wakitembea na bakora ili mtoto akikosea aadhibiwe haraka. Hali hii huwatia hofu wanafunzi, kuwaondolea hamu ya shule, na kudidimiza uwezo wao wa kufikiri na kuhoji.

Tatu, walimu wajenge urafiki na ukaribu na mtoto

Huu ni ukaribu unaomjengea mtoto hali ya kujiamini na kuamini kuwa mwalimu yupo kwa ajili ya kumsikiliza na kuongoza jitihada zake za kujifunza. Walimu wawape nafasi watoto kufafanua mambo, kuuliza au kupinga (bila kuogopa kuchapwa). Mtoto akifanywa kuwa mwoga, hawezi kuuliza au kutoa maoni yake, na hii kumfubaza kifikra.

Nne, mtoto azoeshwe kujadili mambo au changamoto kwa mitazamo tofauti.

Hili ni muhimu kwa kuwa, kwa kufanya hivi, mtoto anapata uwezo wa kuyaona mambo kupitia pande nyingi, akilenga kujua upande wa uzuri na ule wa ubaya. Mjadala huu ukihusisha vijana wengi, mtoto anapata fursa ya kusikiliza maoni ya wenzake na hivyo kujifunza vitu kwa njia shirikishi.

Tano, mtoto azoeshwe kushiriki kufanya mambo kwa vitendo.

Katika hili, mtoto aelekezwe kuunda wazo kichwani ili aje na kitu kipya kutokana na uwezo wake wa kuyaona au kuyasikia mambo katika mazingira yake. Kuchora, kuchonga, kufinyanga, kushona na kutunga hadithi au nyimbo ni baadhi ya vitu anaweza kufanya –   ikiwa ni mazoezi mazuri ya kukuza uwezo wa kufikiri.

Hatua ya kuchukua: Tukianzia nyumbani, mzazi unapaswa kumjengea mtoto mazingira ambayo yatamjenga na hayataua uwezo wake wa kufikiri, kuchambua na kuhoji vitu. Kwa upande wa shule, walimu watumie njia sahihi kumjengea kijana tabia na uwezo wa kuhoji mambo, uthubutu na ubunifu unaomfanya amudu kuzielekeza fikra zake katika kufanyika kwa vitu halisia.

Mtoto/kijana akiwezeshwa, akajengwa kifikra, anaweza kufikiri na kuchambua mambo nje ya mazoea. Hali hii inamfanya kuwa na uwezo wa uchunguzi, udadisi, ugunduzi na ubunifu; na uwezo huu unamsaidia kuziona fursa mbalimbali za kimaendeleo na kukabiliana kikamilifu na changamoto za maisha.

Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasirimali kivitendo.

Anapatikana kwa e-mail: nzyy2001@gmail.com; Simu 0718219530