
Habari rafiki,
Kwa mujibu wa Mwandishi nguli, Freddy Macha, yupo Profesa mmoja Mzambia, aliongea katika kongamano moja, akisema: “Waafrika hatufundishwi kufikiri. Tunafundishwa kukariri tu!” Kwa mfano, anasema utakuta usiku kucha mtoto anakariri idadi ya meno ya mbwa au sayari zilizopo angani, akijiandaa kujibu mtihani wa sayansi kesho yake.
Elimu hii, anasema, ina lengo la kutengeneza ‘wasomi’ kwa kazi za kutumwa, na sio kujenga uwezo wa kijana kuwa mchunguzi, mdadisi, mgunduzi au mbunifu. Yaani haimpi kijana uwezo wa kufikiri na kuchambua mambo.
Kwa kuzingatia hili, mtaalamu wa masuala ya elimu, Brian Oshiro, anasema tukitaka vijana wetu waweze kuhimili vishindo vya dunia hii ya ushindani tunapaswa kuwafundisha kufikiri. Anasema ili tuwafanye wawe wajanja, ambao watakuwa tayari kupokea taarifa, kujenga maarifa, kukamata fursa na kutatua haraka changamoto, ni lazima tuwafundishe kufikiri.
Kufikiri ni shughuli inayofanyika ndani ya ubongo, na kinachozalishwa huitwa fikra. Fikra ni mtazamo anaokuwanao mtu juu ya jambo fulani – ndio maana utasikia mtu anasemwa ana fikra chanya au hasi kuhusu jambo fulani. Kijana akijengewa uwezo wa kufikiri anapewa uwezo wa kuyatazama mambo kwa jicho maalum, lenye udadisi.
Fikra ni kitu kinachotengenezwa ndani ya ubongo au akili ya mtu katika hali isiyoonekana. Kuna vitu (vyanzo vya fikra) ambavyo vikiingizwa ndani ya akili ya binaadamu vinatengeneza fikra zake. Vyanzo vya fikra ni vitu vinavyopatikana katika mazingira au maeneo ambayo kijana anaishi au anapendelea kuwepo.
Kisayansi, kompyuta au simu huonesha video au kucheza muziki uliowekwa humo kabla. Kompyuta inafanya kazi kulingana na program iliyoingizwa. Kioo cha compyuta kina kazi ya kutoa taswira ya kitu kilichoingizwa humo. Ukiweka picha ya utupu, kioo kitaonesha picha hiyo. Ndivyo alivyo binaadamu. Akiwekwa katika mazingira hasi, ataingiza vitu hasi katika akili yake, na baadae ataonesha vitu hivyo kwa jamii.
Aina ya vitu, na namna kijana anavyoingiza vitu hivyo ndani yake, ndivyo uwezo wake wa kufikiri unavyojengwa. Kuna msemo usemao, “limjaalo mtu ndilo limtokalo”. Wapo vijana walioathirika na mazingira au aina ya malezi waliyopewa, wakawa na fikra zisizojenga. Kumbuka binaadamu tunaishi katika jamii yenye watu wa aina tofauti. Hivyo, kupitia maongezi au vitu anavyoviona, mtoto au kijana hujenga msingi mzuri au mbaya wa kufikiri.
Hii ndio sababu wazalishaji wa filamu wana utaratibu wa kuzipanga filamu zao kulingana na maudhui yaliyomo, na umri unaoendana na maudhui hayo. Kwa mfano filamu ya X hairuhusiwi kutazamwa na mtoto chini ya miaka 18. Lengo ni kuzuia vitu ambavyo vikiingia akilini mwake vitamwathiri na kumjengea namna fulani ya kuyatazama mambo, na mwisho vitajenga msingi wa matendo yake.
Kwa maana hiyo ni muhimu vijana wajengewe uwezo wa namna ya kupokea, kufikiri na kuchambua mambo. Wajue mambo yepi yachukuliwe (kupitia kuangaliwa au kusikilizwa) na yepi yaachwe. Wajue yepi ni sahihi na yepi si sahihi, na kwa nini.
Fikra au mtazamo hutengenezwa ndani ya mtoto au kijana toka akiwa katika umri mdogo, nyumbani na shuleni. Tukijikumbusha mtazamo wa Profesa Mzambia hapo juu, kuhusu elimu yetu Waafrika, kuna mazuri yaliyomo katika elimu yetu, ingawa yapo ya kurekebisha. Kwa mfano kuna aina ya maswali wanayopewa watoto katika mitihani ambayo siyo fikirishi.
Na kwa bahati mbaya maswali haya ndio hupendwa zaidi na watoto. Kwa mfano, swali kama, “taja sababu zinazoleta mabadiliko ya hali ya hewa” sio fikirishi. Mtoto yeyote mwenye uwezo wa kukariri anaweza kulijibu, hivyo halimjengei uwezo wa kufikiri. Ukitaka kumjenga kifikra mtoto usiishie hapo, muulize, “kwa kila sababu uliyotaja eleza kwa vipi sababu hiyo inaathiri mabadiliko hayo”. Swali hili linamtaka mtoto atumie akili zaidi kwa kufanya tafakuri.
Kama nilivyosema, uwezo wa kufikiri kwa mtoto au kijana unapaswa kujengwa kuanzia nyumbani na baadaye shuleni.
Tukianza na nyumbani, mzazi unapaswa uwe makini katika malezi na makuzi ya mtoto wako. Jifunze kumjengea mtoto mazingira ambayo yatamjenga na hayataua uwezo wake wa kufikiri, kuchambua na kuhoji vitu. Ukiweza kumfanya mtoto awe na ujasiri wa kufikiri nje ya mazoea, badala ya kukariri, utamfanya mtoto ajiamini na kuyaamini mawazo yake; na kuna njia kadhaa ambazo mzazi akizitumia zinaweza kumjengea mtoto au kijana uwezo mkubwa wa kufikiri.
Kwa upande wa shule, kuna njia (approach) ambazo zikitumika ipasavyo kila mtoto au kijana atajengeka na kupata uwezo wa kufikiri na kuchambua mambo. Akijenga tabia ya kuhoji mambo anajenga uwezo wa uthubutu na ubunifu unaomfanya amudu kuzielekeza fikra zake katika kufanyika kwa vitu halisi.
Msomaji wangu, hii ni sehemu ya kwanza ya makala hii. Katika makala ijayo nitakuletea sehemu ya pili, ambapo nitaingia ndani zaidi kufafanua wajibu wa mzazi, na njia ambazo mzazi anapaswa kuzitumia ili kumjenga mtoto au kijana wake ili awe na uwezo mkubwa wa kufikiri.
Katika sehemu hiyo ya pili nitajadili pia wajibu wa shule, hasa mwalimu, na njia wanazopaswa kutumia ili kumsaidia mtoto au kijana kujenga na kukuza uwezo wake wa kufikiri.
Mtoto akijengeka kifikra, akaweza kufikiri kwa mtazamo chanya, anafanywa kuwa na uwezo wa uchunguzi, udadisi, ugunduzi na ubunifu; na uwezo huu unamsaidia kuziona fursa mbalimbali za kimaendeleo zinazoweza kumkomboa kiuchumi na kijamii, lakini pia anapata uwezo wa kukabiliana na changamoto mbalimbali za maisha.
Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasirimali kivitendo.
Anapatikana kwa e-mail: nzyy2001@gmail.com; mobile: 0718219530…








