Waliofanikiwa Kibiashara Mara Nyingi Hawayasemi Haya

Mambo yakikorogeka katika biashara, Mjasiriamali hukosa raha na amani

Rafiki,

Kuna watu wanaingia katika ujasirimali, wanaanzisha biashara wanayoipenda, inakuwa kubwa, na inawapatia mafanikio kiuchumi, kwa kuwa tokea mwanzo hawaoni sababu ya kumtumikia mtu mwingine ili awapangie jinsi ya kuendesha maisha yao.

Watu hawa husukumwa kuanzisha biashara zao binafsi wakiongozwa na hamasa ya kutafuta uhuru binafsi kiuchumi.

Wapo watu wengine ambao huvutiwa na mafanikio waliyoyapata Wajasiriamali hawa, na hupata hamu ya kuingia katika biashara wakiwa na fikra kuwa, kumbe ukishaanza biashara, baada ya muda mfupi utafanana na waliofanikiwa.

Mara nyingi watu hawa hupata simulizi kutoka kwa waliofanikiwa, ya kwamba ulipata wazo, anza….na ukishaanza tia juhudi na maarifa…na ukiweza kufanya haya utafanikiwa.

Hadithi hizi mara nyingi hugusia maeneo chanya zaidi, yanayomwacha msimuliwaji akiwa na hisia kuwa kumbe ukishaanza na kutia juhudi basi utafanikiwa kama waliotangulia.

Hata hivyo, wakati ni muhimu kusikia upande chanya wa ujasiriamali, ili upate hamasa ya kuanza, unapaswa pia kujua kuwa kuna upande hasi. Kwa bahati mbaya upande huu huwa hauongelewi sana na Wajasiriamali waliokwisha fanikiwa.

Huu ni upande uliogubikwa na changamoto za milima, mabonde, miiba, visiki na mahangaiko mengine, ikiwa ni pamoja na kufeli.

Ukifuatilia simulizi nyingi kuhusu mafanikio katika biashara utakutana na maelezo mengi mazuri, ya kutia moyo na hamasa. Hili ni jambo zuri kwa kuwa haifai kumpa mtu anayetaka kuingia katika biashara simulizi ambazo zitamkatisha tamaaa na kumfanya aogope, na hivyo asianze.

Naomba sasa leo nikupatie simulizi kidogo kutoka upande wa pili wa sarafu. Huu ni ule upande usiopenda kuongelewa sana lakini ni wa muhimu. Makala hii itakupatia mambo saba yanayowapata Wajasiriamali, kama ifuatavyo:

Moja, msongo wa mawazo. Unapoingia katika biashara kwa umakini hasa, unawekeza rasilimali zote muhimu katika kitu unachofanya; muda, fedha, nguvu na kadhalika. Wapo wanaokopa fedha nyingi na kupiga kazi kisawasawa, bila uzembe, lakini wanafeli vibaya!

Likitokea hili, utamwona mtu kama amechanganyikiwa, kapata uchizi hivi! Msongo mkubwa wa mawazo unamwandama asijue nini afanye ili mambo yarudi katika mkondo wa mafanikio. Mtu akifikia hatua hii ni muhimu akapata washauri wa biashara, ambao humsaidia kutafuta sababu za kufeli, na njia za kurudisha mambo sawa.

Mbili, mafanikio huja taratibu na kwa taabu. Waliofanikiwa, wengi hawakupitia mteremko. Kuna watu wakiwaona waliofanikiwa wanadhani mafanikio hayo yamepatikana mara moja tu, kufumba na kufumbua. Haiko hivyo.

Kukuza biashara hadi kuifanya iweze kutoa manufaa yanayoonekana ni jambo linalohitaji muda wa kutosha wa uwekezaji wa nguvu, juhudi, maarifa na uvumilivu. Utaanza biashara, utakua kiasi fulani, utaanguka, utainuka kwa taabu na utaanza kukua tena hadi kufikia mafanikio.

Tatu, hupata misukosuko ya madeni. Ili kuingiza mtaji katika biashara na kuifanya isimame vizuri Wajasiriamali hulazimika kukopa. Mikopo hupatikana katika mabenki na taasisi za fedha. Mikopo hii huja na masharti kadhaa ikiwa ni pamoja na riba.

Mzunguko wa biashara huathiri sana uwezo wa mfanyabiashara kulipa mkopo. Hali hii ikitokea na gharama za uendeshaji biashara zikawa kubwa, uwezo wa kulipa madeni hupungua na jambo hili hugeuka kuwa mzigo na kero kubwa  ambayo watu wasiohusika hawawezi kuibaini.

Nne, hukumbana na changamoto za kodi na tozo. Kodi na tozo za serikali ni wajibu zilipwe bila kukosa. Malipo haya hutoka katika mapato ya biashara husika. Sasa inapotokea mzunguko wa biashara ukawa mdogo na gharama za uendeshaji zikawa kubwa; au biashara ikikumbwa na majanga kama bidhaa kuharibika, suala la kodi na tozo huwa lipo palepale. Jambo hili husababisha maumivu makubwa kwa Mjasiriamali.

Tano, muda wa kufurahia maisha hupungua. Kimaumbile, watu hupenda kufurahia maisha. Hupenda ‘kujirusha’! Hupenda wakutane na marafiki zao waongee, wale na kunywa pamoja huku wakicheza muziki n.k. Yote haya ni mema.

Hata hivyo, ili upate kufanikiwa kibiashara unapaswa uwekeze muda wa kutosha. Ukijikita kikamilifu katika kazi mara nyingi unakosa muda wa kufurahia maisha, au kujirusha. Utalazimika kuamka mapema na kuchelewa kulala, lakini hata muda wa kupumzika mchana au siku za mwisho wa juma huwa mdogo.

Hili huwasononesha wengi ambao hulazimika kuvumila wakiwa na imani kuwa baada ya mambo kukaa vizuri muda wa kujirusha utafika.

Sita, afya zao huzorota. Ukiwa umebanwa sana na kazi utajikuta muda mwingi unakimbizana na majukumu yaliyopangwa au yanayotokea ghafla ili kutimiza mipango iliyopo. Kwa kufanya haya, wengi hukosa muda wa kupumzika, kwani hulala masaa machache na kusafiri sana.

Mara nyingi pia hula chakula kisichopangiliwa au kupikwa vizuri na hawali kwa muda unaotakiwa. Mazingira haya huzorotesha sana afya zao na kusababisha madhara ya mwili endapo tahadhali haikuchukuliwa.

Saba, mahusiano na jamii huzorota. Ili wafanikishe malengo yao Wafanyabiashara kutwa nzima hukimbizana na fursa au jinsi ya kutatua changamoto.

Fursa au changamoto ikitokea Mjasiriamali husahau kuwa kuna watu wanamhitaji yeye pia; watoto, mke, ndugu, rafiki n.k, wapo na wangependa kupata ushauri, msaada n.k. Inapotokea mtu huyu muda wote unatumika kusaka pesa ni wazi atakosa muda wa kufuatilia mambo ya kijamii na kifamilia, na hili ni jambo linalomuumiza yeye na jamii pia.

Kwa hiyo basi msomaji wangu, usione mtu kafanikiwa ukawa na mtazamo mmoja. Ni vizuri kufuatilia nyuma ya pazia kujua yale mengine ambayo mara nyingi huwa hayazungumzwi. Ni muhimu kuyajua haya ili kujiandaa kisaikolojia au kuweka mikakati maalum ya kupunguza athari zake.

Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasirimali kivitendo.

Anapatikana kwa simu: 0718219530; e-mail: nzyy2001@gmail.com

Mameneja Wengi Hawana Stadi Hizi Muhimu

Meneja mwelevu hupenda kusikiliza kwa umakini ili apate undani wa jambo

Habari rafiki

Makala hii naiandika ili kuhusisha stadi za maisha na suala zima la usimamizi katika shughuli zinazohusu ujasiriamali. Nimeandika katika makala zangu za nyuma kwamba pamoja na elimu na ujuzi walionao watu, wapo ambao wanapungukiwa stadi muhimu za maisha, na hii ni hatari.

Tunapoongelea ujasiriamali tunamuongelea pia mtu anayefanya ujasiriamali. Wajasiriamali wengi huanza ujasiriamali wakiwa peke yao au katika timu ndogo. Lakini jinsi biashara inavyokuwa wanalazimika kuwa na wasaidizi chini yao. Hawa huitwa wafanyakazi, na viongozi wao huitwa Mameneja au Mabosi.

Ukifanya mahojiano na wafanyakazi kuhusu tabia za viongozi wao sehemu za kazi utapata mengi. Wapo watakaokusimulia kuhusu uwezo mdogo wa ujuzi wa kazi walionao mabosi wao, na kadhalika.

Kama hiyo haitoshi, wapo watakaokusimulia kuhusu udhaifu walionao baadhi ya Mameneja kuhusu stadi au maarifa ya kiuongozi, kwa kiwango cha kuathiri kabisa utendaji na motisha ya wafanyakazi.

Utasikia wafanyakazi wakisema, viongozi hawa, kama kweli walipewa mafunzo ya uongozi basi walifundishwa tu kupanga na kugawa majukumu ya kazi kwa walio chini yao, na kuwabana pale ambapo kazi haikufanyika walivyotaka wao, basi!

Wanasema, mabosi wa aina hii hawana maarifa ya kuzielewa hisia za wengine wala uwezo wa kuziunganisha timu za kiutendaji. Kiujumla mabosi hawa hawana ujuzi wa usimamizi wa rasilimali watu makazini.

Katika Karne hii, mbinu ya usimamizi wa wafanyakazi ambayo mfanyakazi hupangiwa majukumu ili afanye, na akifanya vizuri anapewa zawadi fulani aliyoahidiwa…na akishindwa kufanya anapewa adhabu, haina nafasi tena. Mbinu hii huitwa karoti na bakora!

Dunia ya leo watu hupewa hamasa ya kufanya kazi kwa kuzigusa hisia zao moja kwa moja. Imethibitishwa kuwa motisha ya watu kazini hufikia kiwango cha juu pale ambapo watagundua kuwa kiongozi wao anawathamini, kuwasikiliza na kuwashirikisha katika maamuzi kadhaa muhimu.

Sasa, kuna stadi tano ambazo mameneja wengi wanapungukiwa linapokuja suala la usimamizi wa wafanyakazi, kwa kiwango cha kujenga mazingira ya kazi yasiyo rafiki, na hii husababisha kushuka kwa utendaji. Mameneja wengi hupungukiwa stadi zifuatazo:

Moja, hawazifahamu hisia za wafanyakazi. Ili uwe meneja mzuri unapaswa kuwa na uwezo mkubwa wa kugundua mambo yanayowasibu wengine na kuyatazama kwa mtazamo wao. Stadi hii ni muhimu kwa kuwa inahusisha uwezo wa kuzisikiliza hisia za wengine na kujitahidi kuzielewa.

Ukweli uliopo ni kwamba viongozi wengi wana ubinafsi na wanapenda kuzisikiliza nafsi zao zaidi, na hawajali jinsi watu wao wa chini wanavyojisikia, kabla ya kutoa maamuzi, na jambo hili hupunguza sana furaha yao.

Mbili, hawana subira ya maamuzi. Uwezo wa kuvuta subira ni jambo linalowashinda wengi. Kiongozi akiwa na maarifa haya hujenga tabia ya utulivu; kusubiri ‘maji yatulie’ kabla ya kuchukua hatua au kutoa maamuzi fulani, hasa pale jambo baya au taarifa mbaya imepatikana kuhusu mtu au timu ya watu kazini.

Wapo mabosi ambao hupatwa na jazba au hasira. Hawa hupaniki haraka na kutoa maamuzi mara tu wasikiapo au kuona jambo wasilolipenda. Hii sio tabia nzuri.

Meneja mzuri huupa muda ubongo wake kujadili yaliyotokea ili kupata busara ya hatua inayopaswa kuchukuliwa. Huyu ni kiongozi ambaye huwapa pia wasaidizi wake fursa ya kutoa maoni au hata kujadili yaliyotokea kwa lengo la kusaidiana kutatua.

Tatu, hawana uwezo wa kusikiliza. Katika sehemu za kazi utakutana na bosi ambaye hata hujamaliza kuongea tayari keshadakia na katoa maelekezo ya nini cha kufanya, akimaanisha kuwa tayari ameshakuelewa, na hilo ndilo jibu lake. Mara nyingi inakuwa kinyume chake. Anakuwa hajaelewa!

Ukiwa na uwezo mdogo wa kusikiliza ni wazi kuwa utakosa maarifa au taarifa muhimu za kukuwezesha kufanya maamuzi au kutenda jambo kwa usahihi. Hali hii huharibu kazi na kuleta migogoro pia.

Nne, uwezo mdogo wa kufikiri kiudadisi. Mtu mwenye fikra dadisi ni yule anayefikiri kwa kiwango cha juu zaidi na hategemei tu maarifa ya kufundishwa darasani. Mtu huyu ana uwezo wa kuyaangalia mambo kupitia pande nyingi.

Kumbuka kuwa mashuleni watu hufundishwa zaidi kwa kukaririshwa maarifa maalumu yaliyochaguliwa, ambayo ukimudu kuyakumbuka wakati wa mtihani basi wewe una akili!

Utakuta mengi ya maarifa haya wala hayatumiki katika maisha ya kila siku. Mameneja wanapaswa kuwa na maarifa ya kufikiri kiudadisi ili wapate picha halisi itakayowafanya watoe maamuzi yenye ubora zaidi.

Tano, hawajiamini na hawana unyenyekevu. Haipendezi, pale kitu fulani kisipoenda vizuri tu, tayari Meneja ameshashika nyundo na kuanza kubomoa watu vichwa! Yaani mambo yasipoenda anavyotaka yeye tu, basi umelikoroga!

Meneja anayejiamini huzizuia hisia au hasira zake na hatumii nguvu au mamlaka yake kulazimisha mambo yaende atakavyo yeye. Meneja huyu anajua kuwa ana mamlaka, lakini hupenda kujishusha kidogo na kuonesha unyenyekevu, akiamini kuwa hawezi kuwa na majibu ya matatizo yote.

Hatua ya kuchukua. Kama wewe ni kiongozi katika sehemu yoyote ya kazi jitahidi kuzijua stadi hizi kwa kuwa zinakujenga kuwa mtu unayejitambua na kujiamini kwa kila unachofanya na zinakupa uwezo wa kufanya mambo sahihi na kwa usahihi.

Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasirimali kivitendo.

Anapatikana kwa e-mail: nzyy2001@gmail.com; Simu 0718219530

Jinsi Ya Kupambana Na Pepo La Kukata Tamaa

Matumaini yakipotea mtu kuishiwa nguvu na kukata tamaa

Habari rafiki,

Mtaalam mmoja wa Saikolojia amenukuliwa akisema, “kukata tamaa ni ile hali ya mtu kupoteza matumaini baada ya kushindwa kupata njia ambayo ingeweza kumfanya atatue au ajitoe katika matatizo au changamoto inayomkabili.”

Katika uhalisia, kukata tamaa ni jambo la kawaida, na hali hii humtokea kila binaadamu kwa namna moja au nyingine. Wapo ambao huathiriwa sana na hali hii hadi wanapoteza mwelekeo… lakini wapo wastahimilivu, ambao hupambana hadi kushinda.

Katika maisha ya kuajiriwa au kujiajiri kuna wakati watu hukumbana na changamoto au misukosuko ambayo huwafanya baadhi yao kukata tamaa na kusalimu amri!

Mwandishi mmoja anatuambia kuwa kuna namna mbili za kukata tamaa.

Namna ya kwanza ni kupoteza kujiamini wakati wa kulitia wazo au jambo katika vitendo. Hapa, mtu amekwisha anza utekelezaji wa wazo lake ambalo amejiridhisha kuwa litampatia mafanikio.

Sasa katika utekelezaji, kunatokea vikwazo au changamoto. Yaani ni sawa na mtu aliyeanza safari ya msituni, halafu njiani akakutana na mnyama mkali, akapatwa na woga na kuamua kukatisha safari na kurudi alikotoka.

Namna ya pili ni kukata tamaa kunakotokana na woga wa kuthubutu, ambapo mtu hukata tamaa ya kufanya jambo hata kabla hajalianza. Yaani akifikiria kuanza tu, anapatwa na kigugumizi au hofu. Hata kama mwanzoni aliona jambo hilo linawezekana, ghafla analiona gumu lisilowezekana.

Kwa mujibu wa mwanafalsafa mmoja…mwanadamu ni mwili, nafsi na roho; na kwamba nafsi na roho zinapokosa nguvu, binaadamu anakuwa na uwezo mdogo wa kuzikabili changamoto, na hii humfanya awe rahisi kukata tamaa. Nafsi na roho zinapokuwa imara, mtu huyu anajenga ujasiri na uwezo mkubwa wa kupambana.

Mwanafalsafa huyu anasema kwamba roho chakula chake ni imani, na kwamba kila binaadamu ana imani fulani. Anasema pia kwamba, nafsi chakula chake ni maarifa.

Anadai kwamba mtu mwenye imani hujenga uhakika wa uwepo wa kitu ambacho kwa wakati huo hakionekani au ni cha kufikirika tu, ambacho humpa uwezo wa kufanya jambo fulani.

Na mtu mwenye maarifa ni yule mwenye ujanja wa kuzitumia kanuni au taarifa mbalimbali kupata kitu unachokitaka. Hivyo mtu mwenye vyote, imani na maarifa, huwa na uwezo mkubwa wa kuepuka kukata tamaa.

Kwa mujibu wa mtaalamu huyu wa Saikolojia, kukata tamaa husababishwa na vitu vifuatavyo:

Kwanza, kukosa maono. Mtu akikosa maono au mtazamo chanya, anakosa mwelekeo. Akikosa mwelekeo anapatwa na hali ya kujiona hana uwezo. Hii inasababisha apoteze uwezo wa kujiamini, na akipoteza kujiamini anatengeneza mchafuko wa akili, unaomfanya aogope kufanya jambo.

Pili, kuzungukwa na watu wasio sahihi. Hawa ni watu waoga tayari, na hivyo wanakufanya kuwa na hofu; na jinsi unavyozidi kukaa karibu na watu hawa unazidi kupatwa na hali hii na kushindwa kuchukua hatua.

Tatu, kukosa matumaini. Matumaini yakikosekana huwa yanaondoa motisha, na motisha ikiondoka, ujasiri na uwezo wa kujiamini vinaondoka.

Nne, vikwazo au changamoto. Hivi ni vitu mtu anakutana navyo kabla au wakati wa kutekeleza ndoto yake. Kwa mfano sheria au kanuni za kufanya biashara fulani ambazo zina urasimu mwingi, na rushwa; vitu ambavyo vinavunja sana moyo.

Tano, kuathirika kisaikolojia. Hii ni hali inayomfanya mtu kujiona hana uwezo au ana uwezo mdogo wa kupambana. Hapa, mtu anajiona dhaifu na kwamba hata akijitahidi hawezi kufanya lolote, anaishia kukata tamaa tu.

Sita, udhaifu au uzembe kuwashirikisha watu. Hii ni hali ya mtu kushindwa kuwashirikisha wenzake yale yanayomsibu na kumkatisha tamaa, ili atiwe moyo au apewe ushauri.

Mtu aliyekata tamaa hukosa ule msukumo wa ndani, au motisha ya kufanya mambo inakuwa ndogo. Anajiona hawezi na anajenga woga wa kuthubutu kuanza au kutekeleza shughuli fulani. Anaghubikwa na kulalamika kusikoisha. Kulalamika ni dalili ya mtazamo hasi, na hili huongeza hali ya kukata tamaa.

Kuna Mambo ambayo yakifanyika yatakuepusha kukata tamaa, kama ifuatavyo:

Unapaswa kuweka dhamira yako, akili yako, nguvu zako na muda wako katika hilo ulilokusudia kulitimiza.

Unapaswa kujenga ujasiri. Siri  ya kufaulu ni uwezo wa kivishinda vikwazo, na kuzidhoofisha nguvu za changamoto.

Usitarajie mafanikio yatakuja bila ujasiri na juhudi za kupambana. Yaani usibweteke ukadhani mambo yatajileta yenyewe. Ili kufikia faraja unayoiona katika ndoto zako ni lazima upambane na pepo la kukatisha tamaa.

Mtafutaji kukumbana na vikwazo, changamoto na mikwamo ni kawaida, hivyo unapaswa kujenga uvumilivu, ujasiri na hamasa itakayokuletea mafanikio.

Ukiona shida, mikwamo au changamoto zinazidi ujue hapo mafanikio yapo jirani. Kwa hiyo akili yako inapaswa ijitanue zaidi kupambana zaidi ili kutekeleza yaliyokusudiwa.

Kwa hiyo, kama wewe ni mjasiriamali au unakusudia kuanza, unatakiwa uwe na ujasiri. Unatakiwa utie nguvu, maarifa na imani katika kila unachokusudia kufanya. Kukata tamaa ni tabia mbaya isiyofaa kabisa kwani hudhoofisha mafanikio, hivyo inapaswa kuepukwa.

Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasirimali kivitendo.

Anapatikana kwa simu: 0718219530; e-mail: nzyy2001@gmail.com

Je, Unakosa Ujasiri? Jifunze Kwa Chura Huyu!

Kama chura anaweza wewe utashindwaje?

Habari rafiki,

Sina shaka kuwa unamfahamu chura. Namuongelea yule mnyama anayependa kuishi kwenye vijito, visima au mabwawa. Yule anayependa kupiga kelele za croo…cruu…crooo…, hasa alfajiri na jua linapozama. Ni yule mtaalamu wa kuruka-ruka huku na kule.

Ndio, namzungumzia chura ambaye wakati wa masika hupenda kurukaruka huku akiimba na kufurahia manyunyu ya mvua na maji yanayomzunguka. Naam, huyohuyo, sasa nataka tujifunze somo kutoka kwake…, “Ujasiriamali unahitaji Ujasiri!”

Siku moja vyura kadhaa walikuwa, kama kawaida yao, wakicheza na kuruka-ruka. Eneo hilo lilikuwa na bwawa kubwa na visima ambavyo vilichimbwa na binaadamu kwa ajili ya kujipatia maji ya kunywa. Visima hivi vilikuwa virefu sana na maji yake yalionekana kwa mbali.

Wakati vyura hawa wakiendelea kucheza wakifurahia maisha, ghafla vyura wawili wakateleza na kudumbukia ndani ya kisima kimoja kirefu. Vyura wengine wakapatwa na mshtuko na simanzi. Wakajikusanya ili waone namna watakavyowaokoa wenzao kutoka katika kisima kile.

Walipochungulia ndani ya kisima ndipo walipogundua urefu halisi wa kisima kile. Wakajiinamia kwa huzuni huku wakisema kwa urefu ule isingewezekana wao kufanya lolote, na hivyo wakawasihi wale vyura wawili waanze kusali tu, kwani kifo chao kilikuwa kimewadia.

Wakionesha hali ya kutokukubaliana na ushauri wa wenzao, vyura wale walijitutumua kwa kuruka juu, kwa nguvu zao zote, lakini waliishia kuanguka tu, na kurudi chini kabisa ndani ya kisima.

Baadhi ya vyura walianza kuwatolea maneno makali, wakiwalaumu vyura wale kwa ukaidi, uzembe na kutojali kanuni na taratibu zao wakati wakifanya michezo yao ya kurukaruka. Walisema, “nyie mlipuuza kanuni zetu…laiti mngezifuata msingetumbukia kisimani…mmeponzwa na ubishi!”

Wakati vyura hao wakitoa lawama, vyura wale wawili waliendelea kujirusha juu, wakijaribu kujiokoa kwa nguvu zaidi. Hata hivyo ushawishi wa vyura wengine uliendelea ukiwataka kuacha kujitutumua bila sababu, kwani kulikuwa na uwezekano mdogo sana wa kujiokoa. Hivyo waliwashauri wakubaliane tu na hali halisi kuwa kifo chao tayari kimefika.

Aliposikia msisitizo wa vyura wale, na akiwa hoi kwa kuruka, chura mmoja mle kisimani akashawishika na kusalimu amri. Akaacha kuruka na kujilaza chini kabisa ya kisima na baada ya muda si mrefu akapoteza uhai.

Kuna kitu kiliwashangaza vyura pale juu. Pamoja na kauli zao za kukatisha tamaa, yule chura mmoja alionekana anazidi kuwa na nguvu zaidi! Pamoja na uchovu na majeraha aliyokuwa amapata aliongeza bidii ya kuruka.

Hata hivyo bado vyura wale waliamini hawezi kufanya lolote. Walizidisha kelele wakimtaka aache kujitutumua na kujiumiza bila sababu, na kwamba akubali tu kuwa huo ndio mwisho wake. Yaani walimtaka ajitulize tu ili naye afe kama mwenzake.

Waswahili husema Mungu hamtupi mja wake! Kelele za vyura wale zilipozidi yule chura alipata hamasa ya ajabu na ghafla alifyatuka kiajabu na kujikuta yuko nje ya kisima!

Yalikuwa ni maajabu kabisa! Kuona maajabu hayo vyura wale walikusanyika wasiamini walichokiona. Kelele zao za kukatisha tamaa zilibadilika ghafla na kuwa vifijo na nderemo kwa ushujaa wa chura yule.

Wakiwa wanamshangilia, walimuuliza ilikuwaje akaendelea kujirusha, pamoja na kelele za kumkatisha tamaa na kumtaka asalimu amri? Wakati wanamuuliza swali hili alikuwa makini kuisoma midomo yao ili ajue wanasema nini.

Alipoelewa wanachomuuliza aliwajibu kuwa yeye ni kiziwi! Na kwamba zile kelele walizokuwa wakipiga na kurusharusha mikono alipata picha kuwa walikuwa wanamtia moyo na kumhimiza ajitume zaidi. Kwa hiyo alijikuta anapata nguvu nyingi zilizomfanya ajirushe hadi nje. Wote walishangaa!!

Somo muhimu hapa ni kwamba katika jitihada zako za kupambana na maisha, hasa katika ujasiriamali, kuna wakati utaandamwa na majanga makubwa, mengine yakitaka kukuangamiza kabisa. Kuna changamoto nyingi katika safari ya ujasiriamali.

Ukiwa katika hali hiyo utashangaa kuona wapo watu, wengine wa karibu kabisa na wewe, badala ya kukutia moyo, wanakuwa na  mtazamo hasi. Wanakushawishi uachane kupambana, wakidai huwezi kufanikiwa katika mazingira yaliyopo. Yaani bora uache na ufanye kitu kingine.

Ukiwaangalia harakaharaka, utaona kama wanakutakia mema hivi au wanakuepusha na balaa kubwa zaidi mbele yako. Jihadhari na watu hawa! Hawa sio watu wema, wana lao jambo. Cha kufanya ni kuziba masikio na kujirusha kwa nguvu zaidi ili uzishinde changamoto zilizo mbele yako.

Tatizo ni kwamba ukiwasikiliza utashawishika kukubaliana nao na utakata tamaa. Ukikata tamaa utapoteza uwezo na ujasiri uliokuwa nao, na hivyo utaacha kujirusha, utanyong’onyea, utarudi chini ya kisima, na hatimaye utakufa.

Kumbuka dunia imejaa watu wa jinsi hii, wenye roho mbaya na wasiowatakia mema wenzao. Unachopaswa kufanya ni kuwa na msimamo, kuziba masikio na kupambana hadi upate ushindi.

Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasirimali kivitendo. Anapatikana kwa simu: 0718219530; e-mail: nzyy2001@gmail.com

Wajasiriamali Waliofanikiwa Wana Sifa Hizi (2)

Mjasiriamali hufikiri kwa kina na huongozwa na maono kujua nini cha kufanya

Katika makala iliyopita nimeongelea sifa tano muhimu walizonazo wajasiriamlai waliofanikiwa. Nimesema, “…ili mtu aitwe mjasiriamali anapaswa kuwa na sifa fulani muhimu ambazo humtofautisha na mtu ambaye si mjasiriamali.”

Ninaamini kuwa ukiweza kuzijua sifa hizi na kuziiga itakusaidia sana katika jitihada za kulitia wazo lako la kijasiriamali katika vitendo na kuweza pia kujipima kama upo katika mstari sahihi au la. Maarifa haya yatakusaidia sana katika kufanya maboresho ambayo yatakuongezea tija.

Nikitumia matendo na misimamo ya wajasiriamali wawili maarufu; Mwingereza Richard Branson na Mtanzania Mzee Reginald Mengi, naomba leo nikutajie sifa nyingine kumi kama ifuatavyo:

Moja, hamu ya kujua mambo kupitia kujifunza. Richard Branson amekuwa muumini mkubwa wa kujifunza kupitia waliofanikiwa, hasiti wala kuona aibu kuuliza au kuhoji ili apate kufahamu mambo kwa kina. Lakini anasoma sana vitabu, majarida n.k., kupata maarifa mapya kila siku.

Mbili, uwezo wa kufikiri kwa kina. Richard Branson anaamini kuwa huwezi kufanya maamuzi sahihi haraka haraka. Anaamini maamuzi madogo madogo ndiyo yanaweza kufanyika bila kufikiri sana, lakini maamuzi ya msingi yanahitaji muda wa kufikiri. Hivyo kufikiri humuwezesha mtu kuangalia pande nyingi za fursa, changamoto au tatizo kabla ya kulikabili.

Tatu, imani katika ubunifu. Kama ndio unaanza, au bila kujali mafanikio uliyokwisha pata, lazima uelewe kuwa kila siku mambo hubadilika na usipokuwa mbunifu utapitwa na wakati. Richard Branson anaamini sana katika ubunifu na ugunduzi na hii imemsaidia sana kujiongeza.

Mbunifu ni mtu mwenye uwezo wa kuangalia vitu, changamoto au matatizo kwa jicho la kidadisi, lenye nia ya kuleta mabadiliko au utofauti fulani utakaoleta matokeo bora zaidi na yenye tija.

Nne, mjasiriamali hapendi kuridhika au kubweteka. Kuna watu wakizoea kufanya kitu kwa utaratibu fulani, ni vigumu sana kuwabadilisha. Hawa watu ni waoga kuanzisha kitu kipya kwa vile tu hawajawahi kukifanya au hakipo katika mazingira waliyoyazoea, na wakiweza kufanya kitu kidogo basi wanaona inatosha. Richard Branson amejizoeza kujaribu kila anachowaza, wala habweteki, na tabia hii imemsaidia kufanikisha mengi.

Tano, mahusiano mazuri na wadau. Wadau ni watu au taasisi ambazo zina mahusiano ya karibu na mjasiriamali, mfano wateja, wafanyakazi, wabia n.k. Mjasiriamali anapaswa kuwafahamu wadau wake wote ili atengeneze mkakati mzuri wa mahusiano nao. Ongea vizuri, msikilize na mwelewe kila mdau upate mchango wake. Tumia uwezo wako wa kushawishi kusukuma mambo yaende.

Sita, uwezo wa uongozi na uratibu wa kazi. Mjasiriamali anapoanzisha au kuendesha shughuli yake anakuwa na watu wanaomsaidia kufanya mambo yaende. Hawa ni wafanyakazi au wasaidizi wake. Kwa hiyo anatakiwa awe na upeo mkubwa wa usimamizi, uongozi na uratibu mzuri wa kazi ili kazi ifanyike kama ilivyopangwa, kwa wakati na kwa ubora. Mzee Mengi alikuwa na kipaji cha uongozi uliotukuka.

Saba, uwezo wa kutumia rasilimali iliyopo kusonga mbele. Mjasiriamali hasubiri hadi awe na kila rasilimali mkononi. Anaanza na kile kidogo alichonacho kisha anatia nguvu, bidii na ubunifu. Anayasoma mazingira, anaongea na wadau na kutoa ushawishi…. na mwisho anajenga kikubwa juu ya kile kidogo alichoanza nacho.

Nane, mjasiriamali anatakiwa kuwa muadilifu. Yaani anatakiwa aaminike na awe na sifa au tabia zinazomfanya aheshimiwe. Anatakiwa awe mkweli katika kila anachofanya au kuwafanyia wadau wake.

Hii ina maana kuwa mafanikio ya mjasiriamali yanatokana na imani (trust)… yaani idadi ya watu wanaomuamini na wako tayari kufanya kazi na yeye, kumkopesha bidhaa au pesa, kununua bidhaa zake au kumpatia msaada wakati wa matatizo.

Tisa, mjasiriamali anatakiwa kujichanganya na watu wengine (networking). Mzee Reginald Mengi anasema yeye amekuwa na tabia ya unyenyekevu na ukaribu kwa watu wote. Anasikiliza maoni yao, hata yale yanayompinga, na tabia hii imemfanya aweze kuwa na mahusiano mazuri na watu wa aina na rika zote, na hii imemsaidia sana kukuza biashara zake.

Kumi, mjasiriamali anatambua kufeli kupo. Katika Kitabu chake cha I can, I must, I will, Mzee Mengi anasema, kitakwimu, biashara nyingi zinazoanzishwa hufeli. Hata hivyo mjasiriamali wa kweli analitambua hili na wala haliogopi! Anachokitanguliza yeye ni shauku yake ya kutimiza maono na malengo yake, akizingatia kujenga nidhamu, umakini na kuchukua kila tahadhari kwa kila anachofanya.

Kwa mfano, Richard Branson anasema amewahi kuanzisha biashara kadhaa ambazo zilifeli; zikiwemo Virgin Cars, Virgin Publishing na Virgin Clothing. Lakini anasema aliendelea kuwa na mtazamo chanya, hakuogopa wala kukata tamaa, bali alijengea hamasa zaidi na motisha binafsi kuendelea kufanya kila alichoona kinawezekana.   

Kwa hiyo, kuzijuwa sifa hizi ni muhimu kwa kila mtu anayefikiria kuingia katika ujasiriamali. Na kwa walio ndani ya fani tayari basi wafanye maboresho ili waweze kupiga hatua kubwa zaidi.

Mwandishi wa makala hii ni Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasiriamali kivitendo.

Anapatikana kwa e-mail: nzyy2001@gmail.com; Mobile: 0718219530

Wajasiriamali Waliofanikiwa Wana Sifa Hizi (1)

Kufanya Tafakuri ni sifa mojawapo muhimu ya Mjasiriamali

Ili mtu aitwe mjasiriamali anapaswa kuwa na sifa fulani muhimu ambazo humtofautisha na mtu ambaye si mjasiriamali. Ukiweza kuzijua sifa hizi itakusaidia wewe ambaye una wazo tu au tayari umeanza kulitia wazo lako katika vitendo, kuweza kujipima kama upo katika mstari sahihi au la, na hii itakusaidia kufanya maboresho ambayo yatakuongezea tija.

Profesa Bruce Bachenheimer, wa Chuo Kikuu cha Pace, Marekani, anafundisha ujasiriamali. Kwa mujibu  wa Profesa huyu, kitovu cha ujasiriamali kiko katika fikra, yaani namna ya kufikiri na pia kutenda. Ukiweza kuzijua sifa hizi itakusaidia kuzijenga tabia na fikra zako ili ziendane na sifa hizi.

Msomaji, bila shaka unawafahamu wajasiriamali na wafanyabishara wakubwa kutoka nchi zilizoendelea, kama Richard Branson. Huyu ni Mwingereza, na mmiliki wa makampuni ya Virgin, yanayofanya biashara mbalimbali ikiwemo ya usafirishaji wa anga, Virgin Atlantic Airlines, ambayo imepata umaarufu mkubwa nchini Uingereza, ikishindana kwa ukaribu na British Airways.

Sio Ulaya tu, lakini hapa Tanzania kuna wajasiriamali wengi waliofanikiwa na kupata umaarufu kama Mzee Reginald Mengi, ambaye alikuwa Mwenyekiti wa Makampuni ya IPP. Yupo pia Mzee Said Bakhresa ambaye ni mwasisi na Mwenyekiti wa Makampuni ya Bakhresa yanayomiliki biashara nyingi zikiwepo za vyombo vya habari, vyakula na usafirishaji.

Kuna vitu vya kujifunza kupitia kwa watu waliofanikiwa kibiashara kama wazee hawa, na wengine, ambao wengi wao walianzia chini kabisa hadi wakayafikia mafanikio waliyonayo. Wakianzia mahala fulani chini, walijenga fikra na maono, wakafanya vitu fulani kwa utaratibu fulani na mwisho wakapata mafanikio hayo.

Kwa mfano, katika kitabu chake cha I can, I must, I will, Mzee Mengi anatueleza kuwa maisha yake yalianzia katika umaskini kiasi kwamba alikwenda shule akiwa pekupeku, bila viatu. Lakini baadaye alijigeuza kuwa mtu tofauti. Ukiwachunguza matajiri hawa, utagundua wana tabia au sifa fulani ambazo zimebeba mafanikio yao.

Kwa hiyo, sisi ambao tuna hamu ya kupata mafanikio kama wao au zaidi hatuna budi kuzijua sifa hizo ili tuziige, zitusaidie kupiga hatua mapema. Kuiga kimkakati ni moja ya siri ya mafanikio. Ukipata fursa ya kujifunza kutoka kwa waliotangulia ni rahisi zaidi kupiga hatua  kwani tayari ramani ipo. Zifuatazo ni baadhi ya sifa hizo.

Kwanza, mjasiriamali anapaswa kuwa na nia ya dhati toka moyoni kutaka kuanzisha na kukuza kitu anachoota kukifanya (maono). Mjasiriamali anasukumwa na mawazo pevu. Kwa vile tayari ana maono, hawezi kurudishwa nyuma na wengine asifanye yale yaliyo moyoni mwake. Atapambana kutimiza ndoto zake hadi afanye kitu.

Kauli mbiu ya Mzee Mengi, ya I Can, I Must, I Will, inaashiria ushupavu,kujiamini na utayari wa kuishi katika kile alichoamua kukifanya.

Pili, mjasiriamali ana uwezo wa kudadisi na kuyasoma mazingira yake na kugundua mahitaji, matatizo au changamoto zilizomo kisha kuchukua hatua haraka. Kwa mfano, Mjasiriamali Reginald Mengi anasimulia kupitia kitabu chake cha I can, I must, I will, kuwa alipata msukumo wa kuanzisha biashara yake ya kwanza mwaka 1983 akiwa jijini Dar-Es-salaam.

Alikuwa ameishiwa kalamu ya wino (peni) na akapita katika maduka kadhaa akitaka kununua, bila mafanikio. Alipofanya ufuatiliaji ndipo akagundua kulikuwa na uhaba wa peni nchini Tanzania, kutokana na hali ya uchumi wa nchi wakati huo, na akagundua kuwa kumbe peni kidogo zilizoonekana madukani zilikuwa zikitoka nchi jirani.

Hapo ndipo wazo likamjia la kuingia katika biashara ya utengenezaji wa peni. Uamuzi huu ulilenga kutatua shida za wananchi waliokuwa na uhitaji wa bidhaa hii, lakini pia ulikuja kuwa chanzo cha yeye kujitengenezea kipato kikubwa. Huu ni mfano mmoja mkubwa wa sifa za mjasiriamli.

Tatu, uwezo wa kuthubutu. Hii ni tabia ya mtu ambaye anaamua kuanzisha jambo akijua kabisa kuwa mbele yake kuna vihatarishi (risks) na vikwazo. Anaanza tu akiwa amejiandaa kukabiliana na chochote kitakachotokea.

Kwa mfano, Mwingereza Richard Branson alipoamua kuanzisha biashara ya usafiri wa ndege, Virgin Atlantic Airways, alijua kulikuwepo na kampuni yenye jina kubwa, British Airways, ikiwa tayari na mafanikio makubwa Ulaya lakini alijitosa, akathubutu na mwisho akaweza, na anasonga mbele.

Nne, mjasiriamali anapaswa kuwa na uwezo wa kupanga (planning). Mtaji utoke wapi, nini kifanyike kwa utaratibu gani, mipango ya kuitangaza biashara, mipango ya mauzo, mipango ya manunuzi, kodi, ubunifu, na usimamizi wa  rasilimali zote (watu, fedha, muda, vitu nk). Wataalamu wanasema ukishindwa kupanga umepanga kufeli.

Tano, mtazamo chanya. Mjasiriamali akiwa na sifa hii anakuwa na fikra za kusonga mbele. Huyu hakati, wala kukatishwa tamaa. Hata pale mambo yanapokwenda vibaya au anapokabiliwa na changamoto au matatizo katika biashara au kazi yake, yeye hushikilia tu msimamo wake hadi mwisho wa safari.

Mwisho, kuzijuwa sifa hizi ni muhimu kwa kila mtu anayefikiria kuingia katika fani hii; na kwa walio ndani ya fani tayari basi wajiboreshe zaidi ili waweze kupiga hatua kubwa. Usikose makala ijayo ambapo nitamalizia sifa zilizobakia.

Mwandishi wa makala hii ni Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasiriamali. Anapatikana kwa simu 0718219530; E-mail: nzyy2001@gmail.com

Wengi Hufanya Makosa Haya Wanapoanza Biashara

Changamoto za biashara ni nyingi na zikizidi huumiza kichwa

Habari rafiki.

Kwa maelezo ya kawaida ujasiriamali ni uwezo wa kuwaza, kupanga na kutenda kimkakati unaomfanya mtu kubuni, kuanzisha, kuboresha na kuongeza thamani ya kitu, kazi au biashara.

Kwa ufupi, ujasiriamali ni uwezo wa kugeuza changamoto mbalimbali zilizopo katika jamii yetu kuwa fursa.

Kiuhalisia, msingi wa ujasiriamali ni kutambua au kuziona fursa, ikifuatiwa na uthubutu wa kuchukua hatua katika kuifanya fursa fulani ilete manufaa kwa mjasiriamali mwenyewe au jamii yake.

Sasa, katika jitihada za kuanzisha na kuendesha shughuli ya ujasiriamali, Wajasiriamali wengi hufanya makosa kadhaa ambayo huchangia sana  kukwamisha jitihada za kuyatimiza malengo yao. Haya ni baadhi ya makosa ambayo hufanyika:

Moja, kutamani au kushawishika kuacha. Ukweli ni kwamba kuanzisha na kuendesha biashara kiufanisi siyo kitu rahisi. Kuna changamoto nyingi ambazo zinaambatana na jukumu hili hivyo kwamba bila uvumilivu na ujasiri ni rahisi kukata tamaaa na kuacha.

Kutokana na hali hii wapo watu ambao wakikutana na changamoto hizi hunyong’onyea haraka. Hisia huwajia kichwani kuwa kumbe kweli ujasiriamali si mchezo, na labda haupo kwa ajili yao.

Watu hawa hupata pia hisia za kuwaamini wote wanaowaambia kuwa biashara sio lelemama, na kwamba fani hii ina wenyewe, sio wao.

Napenda nikuambie kwamba hisia hizi huwapata watu wengi, hasa kipindi cha mwanzo cha kuanza kulitia wazo katika vitendo. Unachotakiwa kufanya ni kuzipuuza hisia hizi na kujisemea kimoyomoyo, “mimi ni shujaa na siwezi kushindwa, hivyo siachi, nasonga mbele na nitafanikiwa.”

Mbili, kutafuta ushauri kutoka kwa watu wengi. Msomaji, hasa kama wewe ni mama na una mtoto tayari, utakubaliana na mimi kuwa muda mfupi baada ya kujifungua, na hasa mtoto wa kwanza; idadi na aina ya ushauri unaopokea kila siku kuhusu malezi ya mtoto wako ni kubwa.

Usipokuwa mwangalifu utashindwa kujua upokee na kufanyia kazi ushauri upi. Kila mtu anasema lake. Atakuja mtu atakwambia mtoto hatakiwi kunyonya maziwa ya kwanza, yana madhara. Mwingine atasema ili mtoto atambae haraka mkalishe nje, mavumbini. Ukimtandikia mkeka hatambai mapema, ili muradi kila mtu anasema lake.

Ukikaa peke yako ukatulia utagundua kuwa sio kila ushauri unafaa. Upo ushauri wenye madhara makubwa. Kwa hiyo kikubwa cha kufahamu ni kwamba hayo ni maoni yao. Huwezi kuziba masikio ili usiyasikie. Lakini na wewe una akili na uzoefu fulani katika maisha.

Hata katika biashara yanatokea mambo kama haya. Unatakiwa kuchukua ushauri kutoka kwa watu wanaotoa ushauri ‘unaokuingia akilini’, unaoenda sambamba na mawazo au hisia zako. Angalia watu waliofanikiwa kufanya vitu na wakavifanya kwa usahihi na ubora, wasikilize hao.

Ukiwa mjasiriamali unapaswa kujifunza kuomba ushauri kutoka kwa watu sahihi, tena wachache. Waulize watu ambao unalingana nao kibiashara kiasi fulani, au waliowahi kufanya vitu vinavyofanana na vya kwako kwa sasa.

Kwa mfano unaweza kuuliza, “je ulipokutana na tatizo hili kipindi hicho, hivi ulilitatuaje?” Hata hivyo jitahidi sana kutenda kile unachoambiwa kulingana na mazingira yako ya sasa.

Tatu, kujifanya mjuaji sana. Mjuaji ni mtu ambaye anajifanya kujua kila kitu. Kabla hujamaliza kumwambia kitu mjuaji tayari kesha dakia akidai anafahamu unachosema. Mjuaji pia ana tabia ya kupenda kuongea zaidi kuliko kusikiliza, na anachosema hupenda kiaminiwe kuwa ni sahihi.

Mwanafalsafa Socrates aliwahi kusema, “ninavyofahamu mimi ni kwamba mimi sijui chochote.” Sasa kama binaadamu anayeheshimika kwa uwezo wa kufikiri na kuelewa mambo anasema hivi, je wewe ni nani useme kuwa unajua kila kitu?

Wakati fulani kuna vitu unafanya vinafanikiwa – lakini sio kwamba tayari unajua kila kitu, hapana. Yapo usiyoyajua pia! Unapaswa kujifunza kuwa mbunifu zaidi. Kufanya maboresho na kujiongeza. Kitu unachotilia shaka unapaswa kuuliza… na utashangaa kuona unapata maarifa usiyoyatarajia kabisa.

Nne, kutaka kufanya biashara nyingi kwa wakati mmoja. Kuna watu wanaamini kuwa mfanyabiashara mzuri ni yule anayefanya biashara nyingi kwa wakati mmoja.

Wanasema usitegemee biashara moja peke yake; unatakiwa uwe na vyanzo vingi vya mapato kwa wakati mmoja. Ukifanya hivi unazifanya biashara zisaidiane kuingiza pesa, na kwamba moja ikidorora, nyingine inakukomboa.

Hata hivyo, kwa mujibu wa Steve Jobs ni rahisi kuongeza biashara zaidi, lakini ni vigumu kubakia focused.” Maana ya kuwa focused kwa mujibu wa Steve, ni kusema ‘hapana’ kwa mawazo mia kadhaa yanayokuzunguka.

Kwa mtazamo huu, unatakiwa kujielekeza katika bidhaa au tasnia moja tu kwanza hadi uielewe kiundani. Ukifanikisha moja ndipo unaweza kujitanua zaidi.

Kwa kumalizia napenda nisisitize kwamba ili ufanikiwe katika ujasiriamali huna budi kujitahidi kuepukana na makosa haya au yanayofanana na haya kwani kwa kufanya hivyo ni rahisi kujikuta unaharibikiwa.

Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasirimali kivitendo. Anapatikana kwa simu: 0718219530; e-mail: nzyy2001@gmail.com

Jinsi Uthubutu Unavyoweza Kuchochea Mafanikio Yako

Uthubutu ni kujitoa hasa bila kujali hatari zilizo mbele yako

Habari rafiki, 

Katika makala hii nimeandika kuwa wapo watu wengi katika nchi yetu wanaishi na umaskini mkubwa. Watu hawa, sio kwamba wameumbwa hawana bahati, hapana; bali tatizo ni kwamba wamekosa uwezo wa kujaribu au kuthubutu kufanya mambo.

Kuna watu wamefanikiwa katika nyanja mbalimbali; kiuchumi, kijamii au hata kisiasa, na ukiuliza sababu kuu ya mafanikio yao utaambiwa ni nguvu waliyonayo na msukumo wa kusema, “nitaanza, nitafanya na nitafanikiwa.”

Ile nguvu ya kusema nitaanza, nitafanya na nitafanikiwa ndiyo kwa lugha nyingine tunaita uthubutu.

Uthubutu ni neno linalobeba msingi wa mwanzo wa mtu kufanya mambo makubwa na kupata mafanikio. Kuthubutu ni uwezo wa kuchukua hatua za makusudi katika kutenda jambo fulani. Inahusisha kuamua kufanya jambo kwa ujasiri, bila woga, bila kusitasita, wala kujali watu watasema nini.

Kuthubutu ni ile hali ya kuhamasika kufanya kitu ambacho kinatokana na  msukumo wa ndani unaokuamrisha kufanya jambo. Uthubutu unaanzia ndani ya mtu, kutaka kufanya kitu anachokipenda kwa dhati ili ayafikie malengo fulani. Uthubutu unahusisha pia ujasiri na kujituma.

Kuna mtu aliwahi kuuliza, “hivi kwa nini tutumie neno ‘kuthubutu’ iwapo tunafanya kitu tunachokipenda?” Akimaanisha kuwa aonavyo yeye kama tayari una mapenzi na kitu basi unakifanya tu; labda kama hukipendi ndipo dhana ya uthubutu inahusika.

Hoja hii inaweza kujibiwa kwamba kama hujakipenda kitu siyo rahisi kujenga msukumo kutoka ndani. Kama kutakuwepo msukumo basi msukumo huo utakuwa kutoka nje, na huu sio uthubutu halisi bali utii unaosukumwa na shuruti. Utii wa aina hii huondoka mara tu shuruti inapoondoka.

Tunapozungumzia uthubutu tunaongelea msukumo wa kufanya kitu unachokipenda lakini kina vihatarishi ndani yake. Vihatarishi ni matukio ambayo yanaweza au yasiweze kutokea; lakini yakitokea yanaweza kusababisha hasara.

Mfano wa vihatarishi ni pamoja na kukosa wateja, kukata mtaji, usumbufu, gharama isiyo na tija na upotevu wa muda. Katika biashara vihatarishi  vinapaswa kuangaliwa kwa ukaribu na umakini mkubwa.

Ni vizuri kabla hujaanza biashara ufanye tathmini ili uvijuwe vihatarishi vilivyopo kuona kama unaweza kuvimudu, au kama unaweza kuyabeba matokeo ya vihatarishi hivyo, mfano kupata hasara.

Na hapo ndipo suala la uthubutu linapoingia; yaani una wazo lako, unafanya utafiti kubaini vihatarishi na ukivijua unajiandaa kisaikolojia kukabiliana navyo na kuwa tayari kuyapokea matokeo yoyote ukiwa salama, bila changanyikiwa.

Kuna wakati watu wanashindwa kuthubutu kutokana na kuzidiwa na nguvu ya msukumo kutoka kwa watu wa karibu wenye mawazo hasi. Kiubinadamu tu, watu huathiriwa sana na mawazo au mitazamo ya watu wengine.

Ndani ya mtu huwa kuna nguvu (forces) ambazo ni chanya na hasi zinazomsukuma mtu kufanya au kuacha kufanya jambo. Kikawaida, kuna mawazo huzunguka ndani ya ubongo wa mtu kila anapotaka kufanya jambo. Kwa mfano, “hivi nikifeli itakuwaje, au nikipata hasara si ndio mwisho wangu?”

Wakati fulani unapanga kufanya jambo unakutana na watu wanaokuvuta kwa nyuma usifanye. Kwa mfano, kila unachopanga kufanya unakutana na mawazo pingamizi kutoka kwa marafiki na hata wazazi, wakikwambia huwezi kufanikiwa.

Kwa kauli hizi, kama wazo hilo halitoki ndani ya nafsi yako, lazima utakata tamaa. Hapa ndipo inahitajika nguvu ya ziada kutoka ndani; lakini pia hamasa kutoka kwa watu wenye nia njema.

Hatua ya kuchukua: Kama wewe ni mjasiriamli elewa huwezi kufanya kitu chochote kama una udhaifu katika uthubutu. Ni watu wenye ujasiri tu ndio wanaoweza kuthubutu kuanzisha kitu na kukisimamia hadi kikaleta manufaa.

Kuthubutu inahusisha kuamua kufanya jambo kwa ujasiri, bila woga, bila kusitasita, wala kujali watu wanasema nini. Ni uwezo wa kuchukua hatua za makusudi katika kutenda kutokana na msukumo kutoka ndani.

Jambo kubwa ambalo mjasiriamali unapaswa kuwa nalo ni uwezo wa kujenga wazo la kitu anachotaka kufanya. Kinachofuata ni kufanya tathmini na kisha ni kukusanya nguvu ya kulitia wazo hilo katika vitendo haraka ili lilete matokeo tarajiwa. Na huu ndio uthubutu wenyewe!

Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasirimali kivitendo.

Anapatikana kwa simu: 0718219530; e-mail: nzyy2001@gmail.com

Hizi Ni Stadi Za Maisha Ambazo Wengi Hawana (2)

Habari rafiki,

Katika makala hii nimeandika kuhusu umuhimu wa watu kuwa na maarifa au stadi za maisha. Nimesema kwamba pamoja na elimu na ujuzi walionao watu, wengi wao wanapungukiwa stadi muhimu za maisha, na upungufu huu una madhara.

Nimeandika kwamba mtu anapokosa stadi muhimu za maisha hujikuta amejiweka katika wakati mgumu ikiwa ni pamoja na kuzikosa fursa za mafanikio, kuingia matatani au kujidhalilisha, na nikahimiza watu wajifunze stadi hizi.

Nilianza na stadi moja muhimu ambayo ni uwezo wa kutumia akili ya kuzaliwa katika kufanya mambo au kutoa maamuzi– naomba sasa niendelee na stadi nyingine kama ifuatavyo:

Moja, uwezo wa kuzielewa hisia za wengine. Stadi hii ni muhimu kwa kuwa inahusisha uwezo wa kuzisikiliza hisia za wengine na kujitahidi kuzielewa kwa mtazamo wao. Ni stadi ambayo mtu hujitahidi kuzitambua na kuzidhibiti hisia zake binafsi kulingana na hisia za wengine.

Ukweli uliopo ni kwamba watu wengi wana ubinafsi na wanapenda kuzisikiliza nafsi zao zaidi, na hawajali jinsi wengine wanavyojisikia ndani ya nafsi zao.

Ukiweza kijitambua na kuzitambua hisia zako utajiweka katika nafasi ya kujua jinsi wengine wanavyoitazama na kuichukulia dunia, na hii itakufanya ujenge uhusiano bora na kila mtu.

Uhusiano huu ndio utakaokupa uwezo wa kutoa hamasa au ushawishi kwa wengine ili waweze kubadili hisia walizonazo kwa wenzao. Na ukiweza kumudu hili utakuwa umejijengea heshima na kuwa kimbilio la wengi.

Mbili, ustahimilivu na uvumilivu. Uwezo wa kuvumilia ni jambo linalowashinda wengi. Kwa mfano watu wengi wana uwezo mdogo wa kusubiri kitu ambacho huchukua muda mrefu kufanyika.

Wengi wanapenda kila jambo litokee haraka, wapate mafanikio sasa hivi, na wako tayari kuyasukuma mambo yaende upesi-upesi bila hata kufanya utafiti wa kutosha wa matokeo yake.

Mfano hai ni ajali ya gari lililobeba familia, wakitoka kwenye mahafali ya binti yao. Njiani mvua kubwa ilinyesha na maji kufunika daraja moja. Walipofika pale walikuta wengine wakisubiri maji yapungue. Wao, kwa kukosa subira walijitosa… na gari lao kusombwa na maji. Familia yote ikaangamia!

Tatu, nidhamu na uadilifu. Tukiongelea suala la nidhamu tunaongelea uwezo wa mtu kujiheshimu na kuheshimu wengine. Tunaongelea tabia njema ya mtu. Inahusisha jinsi tunavyoongea, tunavyofanya mambo na jinsi tunavyoonesha matendo yetu kwa wengine.

Ukifuatilia sehemu za kazi, ndani ya mabasi, mitandaoni, hata ndani ya nyumba za ibada, utagundua baadhi ya watu wasivyo na nidhamu wala chembe ya adabu au maadili. Jinsi walivyovaa, wanavyoongea, wanavyotenda na kadhalika, ni aibu!

Je, kuna mtu wa kulaumiwa kwa tabia ya watu kukosa nidhamu? Tuwalaumu wazazi? Walimu? Jamii nzima au…? Wapo wanaowatupia lawama wazazi, wakidai kuwa wao ndio wajenzi wa msingi wa nidhamu ya mtoto. Wanadai mzazi akishindwa kumpa mtoto malezi bora nyumbani si rahisi mtu baki kummudu ukubwani.

Mtu asiye na nidhamu au maadili hana uwezo wa kutoa salamu, kushukuru, kuomba msamaha, kutoa msamaha au kuthamini hisani anayofanyiwa. Kwa mfano kwa maadili ya ki-afrika, kijana anapaswa kumheshimu mtu mzima bila kujali uhusiano wao. Kinyume chake pia ni sahihi.

Nne, uwezo wa kusikiliza (usikivu). Uwezo mdogo wa kusikiliza ni tatizo kubwa sio tu kwa watu wa kawaida majumbani au mtaani bali pia kwa viongozi wa sehemu za kazi.

Wapo watu ambao hawana subira. Yaani hata hujamaliza kuongea tayari keshatoa jibu na katoa maelekezo ya nini cha kufanya, akimaanisha kuwa tayari ameshakuelewa na hilo ndilo jibu lake.

Mara nyingi watu wa aina hii hujifanya wana maarifa au akili kubwa kuliko yule anayeongea nae, au ni watu wa kujikweza. Kuna watu wanasema Mungu hakukosea alipotuumba wanadamu tukiwa na mdomo mmoja na masikio mawili, wakimaanisha kuwa tusikilize zaidi kuliko kuongea.

Ukiwa na uwezo mdogo wa kusikiliza ni wazi kuwa utakosa maarifa au taarifa muhimu kukuwezesha kufanya maamuzi au kutenda jambo kwa usahihi. Hivyo kusikiliza kwa umakini ni sehemu kubwa ya kujenga mawasiliano bora.

Hatua ya kuchukua. Popote ulipo jitahidi kujifunza stadi hizi za maisha kwa kuwa zinakujenga kuwa mtu unayejitambua na kujiamini kwa kila unachofanya na zinakupa uwezo wa kufanya mambo sahihi kwa usahihi pia.

Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasirimali kivitendo.

Anapatikana kwa e-mail: nzyy2001@gmail.com; Simu 0718219530

Je, Kufanikiwa Kimaisha Kuna Ukomo Wa Umri?

Mmiliki wa KFC Bilionea Colonel Sanders alifikia utajiri huu akiwa mzee

Habari rafiki

Ni watu wachache sana, na wanaendelea kupungua kila siku, wasiojua kuwa dunia sasa imehamia na inazidi kujichimbia ndani ya mitandao ya kijamii. Yaani mambo yanaenda kidigitali zaidi wakati huu.

Ukitaka kujua kwa wakati, na wakati mwingine kwa uhalisia, nini kinatokea duniani, basi ingia kwenye mitandao ya kijamii. Kutokana na hali hii, redio na magazeti mengi yamelazimika kuhamia humo.

Nikiwa navinjari katika mtandao mmoja wa kijamii nilikutana na bandiko (mada) moja lililobeba kichwa cha habari: “Ni umri gani ukifika ‘kutoboa’ ndio mwisho?”

Nilivutiwa na mada hii na katika kuifuatilia niliona inafikirisha na kuibua mjadala, na mwisho niliona ni vizuri nikushirikishe na wewe kwa kuwa ni mada yenye kuelimisha na kuhamasisha.

Mtoa mada, Bw. Juma Ally (siyo jina lake), aliyedai ana umri wa miaka 35 aliiweka wazi hamu yake ya kupata mafanikio katika maisha (kutoboa); lakini pia alionesha hali ya kukata tamaa kwa kuhisi kwamba huenda umri tayari umeshamtupa mkono, na kwa hiyo hana nafasi tena ya kufanikiwa.

Katika bandiko lake Bw. Juma anatudokeza kuhusu vitu ambavyo kwa mtazamo wake angevipata, basi angekuwa ‘ametoboa’. Anasema: “Maana hadi sasa sina nyumba wala gari, ingawa nina viwanja 3 na shamba la ekari 20.”

Kinachomtia shaka zaidi bwana huyu, kulingana na maelezo yake, ni pale ambapo katika maongezi na wenzake fulani – wanamwambia kwamba wanavyojua wao maendeleo yana ukomo wa umri; yaani ukivuka umri fulani basi sahau kupata maendeleo. Umeshachelewa!

Kwa mrejesho huu kutoka kwa wenzake kijana huyu anaonesha kujutia uamuzi aliochukua miaka kadhaa nyuma wa kuwasomesha wadogo zake. Anadai: “Mimi ‘kilichonilostisha’ (kilichonipotezea uelekeo) ni uamuzi wa kuwasomesha wadogo zangu kwa mshahara wangu mdogo.”

Sasa, kuna hoja tatu za kujadili hapa. Kwanza je, kwa umri alionao sasa tayari amechelewa kutoboa? Pili je, malengo yake ni gari na nyumba tu, kwamba akipata vitu hivi atajiona tayari ametoboa? Tatu je, mali alizonazo, na mafanikio ya wadogo zake kielimu, haya kwake sio mafanikio? Tujadili.

Hoja ya umri ilipata wachangiaji wengi. Mmoja aliandika: “Kwa umri wako kaka bado una nafasi kubwa ya kutoboa, kikubwa jitahidi kuishi kwa malengo, jenga nidhamu ya fedha na usitake kupata vyote kwa pupa. Kingine, usipende kujilinganisha na wengine kwani hujui njia zao.”

Mchangiaji mwingine aliandika: “Nijuaavyo mimi kila mtu ana muda wake katika maisha, kwa hiyo usitake kuishi muda wa mtu mwingine. Maana yake ni kwamba kutoboa hakuna muda, maana kila mtu anapata mafanikio kwa muda aliopangiwa.”

Mwingine aliandika kwamba katika umri huo wapo watu ndio kwanza wako  vyuoni; yaani wanatarajia wakimaliza aidha waajiriwe au wajiajiri, ndio waanze sasa kufikiria kupata mafanikio. Pia, katika umri huo wapo vijana wanaofunga ndoa, wengine wanaanza kujenga nyumba na wengine ndio wanapata mtoto wa kwanza n.k.

Kuhusu umri wa kutoboa mchangiaji mmoja alitoa mfano wa mmiliki wa Migahawa ya KFC (Kentucky Fried Chicken) Bw. Colonel Sanders, Mmarekani aliyesota sana, lakini akafanikiwa kuwa bilionea katika umri wa uzee wa miaka 62. Huyu ndoto yake ilikuwa kuwa bilionea siku moja.

Kifupi, mafanikio ni hali anayokuwa nayo  mtu  anapoweza kusogea kutoka hatua moja kwenda nyingine katika jitihada za kutimiza malengo yake ya maisha. Mafanikio ni kutimiza malengo uliyojiwekea, bila kujali umefanikiwa ukiwa na umri gani.

Yuko mchangiaji mmoja aliandika: “Mimi mwenzenu ‘kutusua’ (kufanikiwa) ni uwezo wa kulipa kodi ya nyumba, kula vizuri, kupata huduma ya afya, kuvaa nadhifu na kuwa na furaha, bila kujali umri. Hayo mengine ni mbwembwe tu!”

Kwenye bandiko lake Bw. Juma ameandika kwamba ana viwanja vitatu na shamba la eka 20, na ‘lengo lake’ ni kujenga nyumba na kununua gari. Kutokana na hilo yupo mchangiaji anayemshangaa kwa kulalamika wakati tayari ana mali.

Anamshauri kwamba kama nia yake ni kununua gari na kujenga nyumba, kwa nini basi asiuze viwanja vyake viwili na eka kadhaa za shamba? Kwani akifanya hivyo tu atakuwa tayari ametoboa.

Na hapa ndipo hoja ya tatu inapopata mashiko kwa maana kwamba mali alizonazo na malengo yake vinatosha kwa yeye kupata mafanikio anayoyataka. Anachotakiwa kufanya ni kujua ni jinsi gani atazitumia mali hizi kupata mafanikio yake katika umri alionao sasa.

Kwa kumalizia, mafanikio yoyote yanaanza na maono uliyonayo na jinsi ya kuyafanya yawe katika uhalisia kivitendo. Unatakiwa ujiwekee malengo kwa kila unachotaka kukipata katika maisha yako na kisha uweke mikakati ya utekelezaji. Mchakato huu ni endelevu.

Na kama mchakato ni endelevu basi suala la umri halina nafasi. Bila kujali una umri gani, mradi akili yako imekutuma kufanya kitu ili ufanikiwe kimaisha basi anza kufanya. Cha msingi tia nia, jenga imani, weka malengo na mikakati kisha tia jitihada – hakika utatoboa!

Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasirimali kivitendo.

Anapatikana kwa simu: 0718219530; e-mail: nzyy2001@gmail.com