
Habari rafiki,
Ukifanya uchunguzi leo, utagundua kuna watu wazima wengi walioelimika vizuri ingawa wapo pia wasio na elimu ya kutosha. Wapo wengi wenye elimu ya Chuo Kikuu ingawa wapo wasio na elimu hii lakini wana ujuzi mkubwa katika fani zao, kwa mfano mafundi, wasanii na hata wanamichezo.
Pamoja na elimu na ujuzi walionao watu hawa ukweli ni kwamba wengi wao bado wana upungufu. Wengi wanapungukiwa stadi muhimu za maisha, na upungufu huu una madhara makubwa katika maisha yao na ya jamii.
Kwa mfano siyo jambo la ajabu leo kumwona mtu mzima anahangaika kupata jawabu la hesabu ndogo tu ambayo ungetarajia aifanye kwa kichwa. Hesabu kama 42 gawanya kwa 7 kimsingi ni hesabu ya kichwa, lakini utamsikia mtu akiomba simu au kikokotoo ili apate jawabu.
Maarifa ya kumudu kufanya hesabu hii ni yale yanayopatikana katika ngazi ya shule ya msingi. Sasa tujiulize je, tatizo ni mfumo wetu wa elimu hauwapi wahitimu maarifa ya kutosha….au tuilaumu teknolojia… au tujilaumu sisi wenyewe kwa kupuuzia vitu muhimu kama hivi?
Kiukweli kuna mambo ambayo mwalimu au mfumo wa elimu unaweza kulaumiwa. Hata hivyo kimsingi jukumu kubwa la mwalimu ni kumpatia mwanafunzi maarifa ya msingi, na mbinu za kujifunza…baada ya hapo linabaki jukumu la mtu binafsi nje ya darasa kusaka maarifa ili kupambana na mazingira yake.
Mtu anapokosa stadi muhimu za maisha hujikuta amejiweka katika wakati mgumu ikiwa ni pamoja na kuzikosa fursa za mafanikio, kuingia matatani au kujidhalilisha mbele ya jamii.
Kwa muktadha huu inasisitizwa kuwa watu wajifunze stadi za maisha ili waboreshe maisha, wapambane vizuri na changamoto na wayamudu vizuri mazingira yao.
Zifuatazo ni stadi za maisha ambazo watu wengi hawana na wanapungukiwa mambo mengi kwa kutokuwa nazo, hivyo wanahimizwa kujifunza.
Leo nitaanza na stadi moja ambayo ni uwezo wa kutumia akili ya kuzaliwa – halafu katika makala zijazo nitajadili stadi nyingine. Akili ya kuzaliwa hujionesha kupitia maneno au matendo ya mtu. Haya ni maarifa ambao mara nyingi watu hawafundishwi.
Ili mtu aonekane anatumia vyema akili yake ya kuzaliwa inampasa mtu huyu kujijengea umakini wa kutosha kwa kila anachofanya ili kilete matokeo chanya au kisilete madhara kwake na kwa wengine.
Kwa mfano upo jikoni unakaanga vipande vya nyama kwenye kikaangio, juu ya jiko. Akili ya kawaida inapaswa kukuongoza kuwa unapotaka kutoka jikoni ama uipue mboga au upunguze au uzime moto, la sivyo unaweza kuunguza kila kitu ikawa balaa.
Vilevile hatutarajii mtu makini akatize barabara kubwa, yenye wingi wa magari, huku anaandika au kusoma meseji kwa simu yake. Ukosefu wa umakini unanikumbusha maafa ya kutisha yaliyotokea Arusha siku za nyuma.
Mama mmoja alipaki gari lake juani, pembeni kidogo mwa duka kubwa la bidhaa za matumizi ya nyumbani, Supermarket. Alikuwa na watoto wadogo watatu ndani ya gari. Kabla ya kushuka alipandisha vioo vyote vya gari na kufunga milango kwa loki akiwaacha watoto wale ndani ya gari.
Aliingia dukani na kuanza manunuzi ambayo yalimchukua muda mrefu. Alipotoka nje alikuta umati wa watu wamezingira gari lake wakitaka kulivunja ili wawaokoe watoto waliokuwa wakihangaika kwa joto na kukosa hewa. Alipofungua milango alikuta tayari watoto wako hoi na baadaye walifariki.
Hatua ya kuchukua: Akili ya kuzaliwa ni uwezo wa kujiongeza na kufikiri kwa haraka, kwa kina na umakini mkubwa kila unachotaka kufanya au kusema ili kilete matokeo mazuri au kisikutie katika matatizo.
Kwa mtazamo huo, mtu mzima hahitaji kukumbushwa kuacha kuongea na simu wakati anaendesha gari kwani balaa lolote linaweza kumtokea bila kutarajia. Yupo mtaalam mmoja wa falsafa aliwahi kusema, “akili ya kuzaliwa ni bora kuliko akili ya darasani.”
Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasirimali kivitendo.
Anapatikana kwa e-mail: nzyy2001@gmail.com; Simu 0718219530








