Vitu Hivi Huchochea Uwezo-Ubunifu Wa Mjasiriamali

Ubunifu ni matokeo ya udadisi wa kina na kuufikirisha ubongo

Habari rafiki,

Nimeeleza katika makala zangu zilizopita kuwa dunia ya kibiashara hivi sasa imetawaliwa na mazingira ya ushindani wa kiwango cha juu.

Kwa hiyo, ubunifu ndiyo njia pekee inayotumiwa na wajasiriamali wengi wanaojitambua ili kupambana na ushindani katika soko la bidhaa na huduma.

Ubunifu unaelezewa kama uundwaji wa bidhaa au modeli mpya; au uundwaji wa bidhaa au huduma fulani iliyoboreshwa.

Ubunifu unaelezewa pia kama bidhaa, huduma au modeli ya biashara iliyokuwepo lakini inaingizwa kwenye soko jipya kwa mara ya kwanza.

Makala hii inalenga kukupatia njia sita zinazoweza kuchochea akili yako na kukufanya uweze kujenga uwezo mkubwa wa kufanya ubunifu.

Moja, usongo au hamu ya kufanikiwa. Ukijenga nia au hamu ya kupata kitu, usongo huo huendelea kuisumbua akili yako. Jinsi unavyotia nia akili yako inafanya kazi ya ziada kuzalisha wazo bunifu au njia ya kutatua jambo.

Mbili, mfadhaiko. Unaposhindwa kupata kitu ulicholenga kukipata – unajisikia vibaya,, au unafadhaika.

Mfadhaiko unaotokea baada ya jitihada za kufanikisha kitu kukwama huuchochea ubongo ambao huanza kugonganisha mawazo kwa lengo la kupata njia mbadala ya kufanikiwa. Mgongano huu ndio huzaa ubunifu.

Tatu, udadisi. Kudadisi ni ile hali ya kusaka ukweli au kuufahamu undani wa jambo. Udadisi unapofanyika kichwani husababisha mishipa ya fahamu ya ubongo kujituma zaidi ili kuleta majawabu.

Kwa mfano unapojiuliza, “naona kuna tatizo hapa hivi chanzo ni nini? Hivi nani anahusika? Hivi utatuzi wake ni nini? Hivi nani anaweza kusaidia utatuzi?

Udadisi ukifanyika kwa umakini matokeo yake ni upatikanaji wa wazo bunifu.

Nne, kujenga husuda. Unapohusudu kitu maana yake una mapenzi nacho. Sasa, unapopenda kitu au mtu, unajenga hamu ya kuboresha uhusiano kati yenu.

Angalia mambo unayomfanyia mtu umpendaye ndipo utagundua jinsi ubunifu unavyofanya kazi katika akili za watu.

Kwa mfano unapopanga kumpatia zawadi mpenzi wako – unaanza kuwaza, “hivi zawadi gani ataifurahia zaidi? Kama ni nguo, hivi rangi gani anaweza kuipenda zaidi…, aina ya kitambaa…, mshono je,…sijui niifungashe namna gani n.k?”

Jinsi unavyowaza haya ili utoke na kitu cha kumfurahisha mpenzi wako ndivyo akili yako inavyotanuka na kukupatia wazo bora zaidi, na hivyo kukufanya uzidi kujenga uwezo mkubwa wa ubunifu.

Tano, kujenga chuki. Kwa kawaida siyo jambo zuri mtu kuwa na tabia ya kuchukia watu. Tunahimizwa kupendana na kujaliana.

Mara nyingi unapomchukia mtu au kitu hupenda kitu au mtu huyo aangamie au apate wakati mgumu, na hii si sawa; hii ni ‘chuki hasi’! Tunapaswa kuwa na ‘chuki chanya’.

Ukiwa na chuki chanya unalenga kumchukia mtu au kitu kwa nia ya kukiboresha. Yaani unachukia, au unajisikia vibaya jinsi kitu au mtu alivyokaa kihasara-hasara.

Kwa mfano, unachukia jinsi nyumba ya wazazi wako ilivyochakaa au jinsi ndugu yako alivyo mlevi kupindukia. Unaona aibu! Unaanza kuufikirisha ubongo wako ili kutatua hali hiyo, hadi unafanikiwa. Hapa unajenga ubunifu.

Sita, kuweka malengo. Tunahimizwa kuishi kwa malengo. Unapokuwa na lengo au malengo yanayoisumbua akili yako, kila siku, unaujengea ubongo wako shauku ya kufanikiwa.

Ukiwa na malengo hauwezi kubweteka. Utajituma sana kufikiri na kuchanganua mambo ili ufanikiwe. Kwa jinsi unavyoufikirisha ubongo ndivyo unavyouchochea kufanya kazi zaidi – na hapa uwezo wa ubunifu unakomaa.

Hatua ya kuchukua: Makala hii imekupatia vitu sita vinavyoweza kuchochea akili yako na kukufanya uweze kujenga uwezo mkubwa wa kufanya ubunifu.

Unapaswa kuzitumia njia hizi na zingine za namna hii ili kuchochea uwezo wako katika kufikiri na kufanya ubunifu.

Hili likifanyika, kasi ya ubunifu itakuwa kubwa miongoni mwa wajasiriamali na maisha au biashara zetu zitapiga hatua zenye mafanikio makubwa.

Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasirimali kivitendo.

Anapatikana kwa e-mail: nzyy2001@gmail.com; Simu 0718219530

Nini Hufanyika Ndani Ya Ubongo Ili Kuumba Wazo Bunifu?…(2)

Matokeo ‘chanya’ katika maisha ni matunda ya kuwaza ‘chanya’

Habari rafiki,

Katika sehemu ya kwanza ya makala hii nilijadili mahusiano yaliyopo kati ya ubongo na uumbaji wa mawazo mbalimbali akilini, yakiwepo mawazo bunifu.

Nikasema kuwa, kwa kawaida mawazo hutungwa ndani ya ubongo wa mwanadamu, na kwamba ubongo umebeba kitu kiitwacho akili, ambacho hakionekani wala kushikika.

Kisha nilijadili sehemu mbili za akili ya mwanadamu, yaani akili ya nje na akili ya ndani ambazo zina kazi tofauti.

Nilisema kuwa akili ya nje hufanya kazi ya kutambua vitu vinavyotokea kupitia milango ya fahamu kama kuona, kusikia na kunusa, na kuvipatia majibu.

Nilipozungumzia akili ya ndani nilisema hii ni sehemu ambayo huhifadhi kumbukumbu zote zinazotoka katika akili ya nje pamoja na zile zinazotoka katika ulimwengu wa roho.

Nilieleza kuwa wakati mwingine unaona wazo tayari limeingia katika ubongo wako ukiwa huna hili wala lile, wakati fulani ukiwa usingizini.

Tunaambiwa kuwa mawazo ya aina hii yanatoka katika ulimwengu wa roho; yaani ukiwa usingizini unaona wazo fulani zuri ambalo hukuwahi kulifikiria, kulisoma au kulisikia popote, linakuja tu, na unaona lina manufaa.

Sasa, sifa kuu ya sehemu hii ya pili ya akili ni uwezo wa kuzitoa nje ya mwili kumbukumbu za mambo au mawazo yaliyohifadhiwa humo, ili yawe kitu halisi au yajidhihirishe katika uhalisia ki-vitendo, muda unapowadia.

Kwa hiyo, unapowaza au kutamka kwa muda mrefu kuhusu kitu fulani, akili huamini kuwa hicho ukiwazacho au kukitamkatamka ndicho unachokihitaji na kwa hiyo akili, kupitia nguvu ya uumbaji tuliyopewa na Mungu, itakihifadhi ili kitumike baadaye.

Utendaji huu wa akili unashirikiana kwa kiwango kikubwa na mawazo na maneno yetu tunayosema kwa kurudiarudia na kwa msisitizo. Haya huingia katika ubongo na kuhifadhiwa na akili ya ndani, na huwa yanajidhihirisha ki-uhalisia baadaye.

Kuna watu wanawaza na kujisemeasemea kuwa wanataka mafanikio makubwa ya kifedha, na wakifanikiwa watafanya mabadiliko makubwa kwao na kwa jamii zao. Haya ni maono. Watu hawa wana nafasi kubwa ya kutimiza ndoto zao.

Ndio maana Mwandishi John F. Paul anatuhimiza tusitawaliwe na mawazo hasi; kwa mfano unaposema, “aah mimi sifai kwa lolote bwana, wala sidhani kama nitafanikiwa maishani”, huku ni kuwaza hasi.

Anasema kuwa akili zetu hazikuumbwa ili kukaa na hasi, kwani unapokuwa mtu wa kuwaza au kusema hasi, kumbukumbu hizo zinahamishiwa sehemu ya pili ya akili na kuhifadhiwa, na baadaye kutokea ki-uhalisia.

Mwandishi anatuhimiza tuwaze au tuseme ‘chanya’. Mawazo au maneno chanya ni yale yaliyojaa matumaini, imani, ujasiri na uhakika. Haya ni mawazo ya kutokubali kushindwa.

Kwa mfano, ukiwaza au kutamka mara kwa mara kuwa, “Niko imara katika nafsi, mwili na roho yangu, na nina uhakika wa kufanikisha jambo nililopanga kulifanya”, kumbukumbu hii huhifadhiwa na mara nyingi hutokea dhahiri.

Kuwaza chanya huzalisha matokeo chanya, na kuwaza hasi huzalisha matokeo hasi.

Kama wewe ni mpenzi wa mpira wa miguu utakuwa unamfahamu sana mchezaji maarufu, mshambuliaji,  Mohamed Salah, ambaye kwa sasa anachezea timu ya Liverpool, ya Uingereza.

Mo Salah alishinda tuzo ya Mchezaji Bora wa mwaka wa ligi ya Uingereza (2018).  Akizungumza na waandishi wa habari, wakati akikabidhiwa tuzo hiyo, aliulizwa kama aliwahi kuwa na fikra au wazo la kufanya vizuri kiasi hicho wakati akijiunga na timu hiyo.

Akijibu swali hilo Mo Salah alisema, “Ndiyo, jambo hilo kwa muda mrefu limekuwa linazunguka akilini mwangu. Nikiwa club ya Chelsea na baadaye Roma, sikuweza kutimiza ndoto zangu, kwani niliwekwa benchi muda mwingi.”

“Hata hivyo wazo la kufanya vizuri pindi nikipata fursa lilizunguka ndani ya ubongo wangu siku zote, na sikulipuuza.”

“Kwa hiyo nilipopata fursa ya kujiunga na Liverpool, na wakaniamini, niliona huo ndio hasa wakati wa kutimiza ndoto zangu, na kweli zilitimia kiuhalisia, na haya ndiyo matunda yenyewe.”  

Kwa kumalizia napenda kuweka msisitizo kuwa ili upate wazo bora la ki-bunifu unapaswa kuanza kuwaza chanya.

Unapaswa pia  kujizoeza kuitumia vizuri milango yako ya fahamu ili uweze kutambua na kupambanua  vitu vinavyotokea kupitia milango hii.

Lakini pia unatakiwa ujenge imani ya uwepo wa ulimwengu wa roho, na kwa imani hii utashushiwa maono au ufunuo utakaokuonesha kitu cha kufanya na nguvu ya kukidhihirisha kitu hicho kiuhalisia.

Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasirimali kivitendo.

Anapatikana kwa e-mail: nzyy2001@gmail.com; Mobile: 0718219530.

Kijana Ukifanya Makosa Haya Utajutia Baadaye (2)

Habari rafiki,

Huu ni mwendelezo wa sehemu ya kwanza ya makala hii, ambayo nimejadili makosa ambayo vijana wengi hufanya kwa kukosa maarifa tu – na huyajutia makosa haya maisha yao yote.

Ukichukua hatua stahiki sasa utajitengenezea baadaye iliyo bora

Yaani baada ya kufanya makosa haya ujanani, vijana wakifikia umri wa kiutu uzima au uzeeni, huishia kusema, “laiti ningejua!” Ingawa wanakuwa tayari wamechelewa.

Makala iliyopita nilijadili makosa mawili. Leo nitaongelea makosa mengine manne ambayo hufanywa na vijana, kama ifuatavyo;

Moja, vijana hukubali haraka ushauri wa ‘wazee’. Akili za vijana wengi zinachemka na wana hisia na maoni yao.

Hata hivyo, baadhi ya vijana wana uwezo mdogo wa kuyapima na kuyachuja mawazo au ushauri wa watu wazima, au wazee.

Wazee wengi wana akili nzuri na busara za kutosha, na vijana wanapaswa kuwasikiliza. Hata hivyo, wanachotakiwa kufahamu vijana ni kwamba sio kila mtu mzima au mzee amebarikiwa busara.

Wapo wazee ambao uwezo wao wa kufikiri na kuchambua mambo ni mdogo na hawawezi kutoa ushauri wenye tija. Ni wajibu wa kijana kupima kila ushauri unaopewa, kabla ya kuuamini na kuukubali.

Kipindi cha ujana kinapaswa kuwa kipindi cha kudadisi mambo na kujifunza kwa bidii. Uwezo wa kuuliza maswali na kudodosa mambo ni sifa kubwa ya kijana anayejitambua.

Dadisi kila unachoambiwa, usiogope. Dodosa ili upate undani wa kila jambo. Ukiwa mchunguzi utaweza kugundua kuwa kitu ulichoambiwa ni cheupe kumbe rangi yake halisi ni krimu. Ukigundua hivyo chukua hatua.

Mbili, vijana wanawekeza pesa bila kufanya utafiti. Wakisikia au kusoma hadithi au simulizi kuwahusu watu waliofanikiwa ki-maisha, kupitia uwekezaji fulani, huwafanya vijana kuingia kichwa kichwa kufanya uwekezaji huo.

Kufanya uwekezaji au kufungua mradi fulani ni jambo la maana kabisa. Hata hivyo umakini unahitajika. Kufungua mradi mpya sio kitu rahisi ki-hivyo.

Kama kijana, unapaswa kufanya utafiti wa kutosha ili upate taarifa zinazohusiana na mradi huo, na namna bora zaidi ya kuuanzisha na kuuendeleza.

Ukiwekeza vibaya una hatari ya kupoteza hata kile kidogo ulichonacho.

Tatu, vijana hukata tamaa kiurahisi. Ni ukweli kwamba maisha yana changamoto nyingi, na wakati mwingine mambo huwa magumu. Je, hali ikiwa hivyo tunapaswa kukata tamaa?

Mwandishi mmoja aliwahi kusema kuwa vijana wengi mambo yakiwa magumu ni rahisi sana kukata tamaa.

Tabia ya kuacha kufanya jambo uliloanzisha na kurukia jingine inaweza kuonekana haina tatizo wakati fulani, yaani siyo kitu kibaya; lakini kiukweli kitu kibaya ni kukata tamaa.

Uwezo wa kushikilia na kuendelea kufanya jambo hasa baada ya ‘magumu’ ndio hasa sifa bora ya kijana.

Mambo yakiwa magumu kijana ongeza juhudi na uvumilivu zaidi. Unapaswa kuendelea kupambana na kujituma hadi kieleweke.

Nne, vijana hufikiri kuwa tamaa ya mwili ndio mapenzi yenyewe. Tafiti nyingi zinaonesha kuwa vijana wengi huingia katika mahusiano ambayo hufikia hadi hatua ya kuoana, kwa kusikiliza hisia zao tu.

Wataalamu wa saikolojia wanasema kuwa mapenzi yanayotokana na kusikiliza hisia zinazotokana na mvuto alionao msichana au mvulana si mapenzi halisi. Wao huyaita ‘romantic love’.

Wanasema mapenzi haya huwatengenezea wapenzi hawa mvuto na mshikamano mkubwa sana mwanzoni tu, tena kwa muda mfupi.

Baada ya muda huo wapenzi wote au mmoja wao anaanza kuona yale yote yaliyokuwa yakimvutia na kumpa ‘stimu’ yamechuja na kuwa ya kawaida, na hapa ndipo mshikamano huanza kumomonyoka.

Mwanzoni, kwa mapenzi ya aina hii, ni rahisi sana kudhani wawili nyie mnapendana sana, kumbe siyo; muda si mrefu mnagundua hamuivi wala hamuendani katika mambo mengi tu.

Mapenzi ya kweli, yanayoleta mahusiano ya kudumu, siyo romantic love. Mapenzi ya kweli ni yale yanayobebwa na ‘shared values’; yaani vitu vya msingi ambavyo wote wawili mnaviamini na kuvikubali kuwa ndivyo hasa vinavyowaunganisha.

Ni imani ya kila mmoja katika vitu hivi na kwamba vitu hivyo ndio hasa msingi wa nyie wawili kuishi pamoja. Huu ni upendo wa ndani kabisa ambao mara nyingi hutengeneza gundi imara kati ya wawili.

Hatua ya kuchukua leo. Ni wajibu wako kijana kuujua ukweli huu, kujitambua mapema na kuchukua hatua. Usipofanya hivyo sasa utaishia tu kusema, “aah laiti ningejua!” Utakuwa umechelewa!

Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasirimali kivitendo.

Anapatikana kwa e-mail: nzyy2001@gmail.com; Simu 0718219530

Nini Hufanyika Ndani Ya Ubongo Ili Kuunda Wazo Bunifu? …(1)

Habari rafiki.

Maarifa au elimu ya ubunifu ni muhimu sana katika dunia hii ya utandawazi na maendeleo kupitia taarifa.

Akili ya mtu hukaa ndani ya ubongo

Maarifa katika ubunifu, au uwezo wa mtu kujenga tabia ya kufikiri ki-ubunifu humfanya mhusika kujitengenezea ubongo maalum ambao una nguvu ya ziada ya kuchakata mambo kwa lengo la kupata ufumbuzi wa matatizo, au kuunda kitu kipya.

Katika makala hii nitazungumzia mahusiano ya ubongo na uumbaji wa mawazo mbalimbali bunifu. Kwa mfano, kama wewe ni mjasiriamali, au unapanga kuanzisha biashara, jambo la kwanza kabisa ni kupata wazo la biashara. Yaani nini unataka kufanya.

Kikawaida, mawazo mbalimbali hutungwa ndani ya ubongo wa mwanadamu yakiwemo mawazo ya kibunifu kama kufungua biashara au kuanzisha stadi fulani, mfano uchongaji wa vinyago.

Sasa, kuna vitu ambavyo hufanyika ndani ya ubongo, na  hupangwa na kuratibiwa vizuri ili baadaye vije kujionesha nje vikiwa ni vitendo halisi.

Ndani ya ubongo kuna kitu kinaitwa akili.  Akili au uwezo wa kufikiri na kuchambua mambo, hutokana na michakato mbalimbali ndani ya ubongo.

Kwa sehemu kubwa mwili wa binaadamu hujiendesha kwa kutumia akili au ufahamu. Huwezi kuishika akili, kama unavyofanya kwa ubongo. Bali, akili hujionesha kupitia mawazo, maneno na matendo ya binaadamu.

Mwandishi John F. Paul, katika kitabu chake kiitwacho ‘Weka Ufahamu Wako Huru’, anasema kuna sehemu tatu za akili ya mwanadamu na zina kazi tafauti. Kwa muktadha wa makala hii nitazungumzia na kuchambua sehemu mbili za mwanzo.

Sehemu ya kwanza ya akili ameiita ‘akili ya nje’, ambayo  hufanya kazi wakati mtu yuko macho na ana ufahamu, yaani hajalala.

Hii ni sehemu ambayo hufanya kazi ya kufikiri na kupambanua mijadala ya ndani ya ubongo ambayo huwatokea binaadamu kila siku.

Sehemu hii pia hufanya kazi ya kutambua vitu vinavyotokea kupitia milango ya fahamu kama kuona, kusikia na kunusa, na kuvipatia majibu. Kwa mfano uwezo wa kutambua sura au sauti ya mtu akiongea.

Sehemu hii huhifadhi vitu kwa muda mfupi sana kabla ya kuvihamishia sehemu ya pili ya akili.

Sehemu ya pili ya akili ameiita ‘akili au ufahamu wa ndani’. Sehemu hiii ina kazi kubwa kwa binaadamu. Ina kazi ya huhifadhi kumbukumbu zote. Mawazo ya mtu, ya muda mrefu, na maneno anayosema mara nyingi huhifadhiwa hapa.

Sehemu hii pia hupokea na kuhifadhi kumbukumbu kutoka sehemu ya kwanza ya akili. Kwa mfano, wakati fulani unaweza kuona au kusikia kitu, halafu ukaona ni kitu cha kawaida tu wakati huo. Taarifa au kumbukumbu hii huhifadhiwa katika akili ya pili.

Sasa, hutokea siku moja unapata tatizo au unawaza kufanya kitu, unawazaaa…. lakini hupati jawabu. Mara, umetulia kidogo, unaona kitu kama filamu hivi kikipita katika akili yako, kinayaleta kama picha, yale yote uliyoyaona au kuyasikia zamani.

Yanakuja kama kitu halisi ambacho kimeambatana na maarifa ya kutatua tatizo au kuchakata jambo. Unapata jawabu la tatizo au unapata maarifa ya kibunifu.

Lakini kingine muhimu ni kwamba sehemu hii hupokea pia na kuhifadhi kumbukumbu zote zinazotoka katika ‘ulimwengu wa roho’ na hufanya zieleweke bayana. Kumbukumbu zinazotokana na ulimwengu wa roho ndizo ambazo huitwa maono au ufunuo.

Kumbukumbu hizi hujitokeza tu; yaani mtu umekaa mahala, na hasa ukiwa peke yako, au unatembea au umejilaza tu ukitafakari, wazo linaingia!

Wakati mwingine unakuwa umelala usingizi, na ghafla wazo kubwa linakujia kama ndoto fulani hivi; wazo la maana ambalo hujawahi kulifikiria, kulisoma au hata kulisikia mahala popote, linakuja tu na unaona lina maana na unaweza kulitumia kupata manufaa.

Rafiki yangu, hii ni sehemu ya kwanza ya makala hii. Tafadhali ungana na mimi katika sehemu ya pili.

Katika sehemu ya pili nitaendeleza nilipoishia na kukupatia mfano halisi wa jinsi wazo linavyoingia katika ubongo na jinsi linavyochakatwa kuwa kitu halisi, na kipi cha kufanya ukipata wazo la maana kichwani mwako. Nitaeleza pia jinsi na umuhimu wa kuwaza chanya.

Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasirimali kivitendo.Anapatikana kwa e-mail: nzyy2001@gmail.com; Mobile: 0718219530

Kijana Ukifanya Makosa Haya Utajutia Baadaye (1)

Habari rafiki,

Katika makala zangu za nyuma nimeeleza kijana ni nani kwa mujibu wa vyanzo na muktadha mbalimbali.

Kijana ninayemuongelea katika makala hii ni yule mwenye umri wa angalau miaka 18 hadi 35. Namuongelea mtu aliyekomaa kimwili na kiakili, na ana uwezo wa kujitegemea na kufanya maamuzi.

Vijana wakiwa nazo hupenda kujirusha

Kwa hiyo makala hii inakuhusu wewe kijana mwenye umri huu, na inalenga kukuonesha makosa ambayo vijana wengi hufanya kwa kukosa maarifa tu – na huyajutia makosa haya maisha yao yote.

Baada ya kufanya makosa haya ujanani, vijana wakifikia umri wa kiutu uzima au uzeeni, huishia kusema, “laiti ningejua!” Hata hivyo wanakuwa tayari wamechelewa kwa kuwa ‘saa ya umri’ huwa hairudi kinyumenyume.

Leo nitaongelea makosa mawili ambayo hufanywa na vijana, kama ifuatavyo;

Moja, vijana wakishapata elimu au ujuzi fulani hudhani tayari imetosha. Huenda hili sio kosa lao. Labda tunapaswa kuilaumu jamii nzima kwa udhaifu huu wa kufikiri.

Utakuta kijana akishamaliza kiwango fulani cha elimu au ujuzi fulani basi hana hamu tena ya kujielimisha zaidi.

Fikiria, kijana anamaliza chuo halafu humuoni akigusa hata gazeti, na zama hizi za mitandao ya kijamii, anachoweza kufanya ni kujipiga picha na kupost face book au whatsap, zikisindikizwa na ‘captions’ zisizo na tija yoyote.

Ukweli ni kwamba unapohitimu elimu ya chuo, ukapata cheti, diploma au digrii; hapo ndipo elimu imeanza. Yaani usiseme ‘nimemaliza chuo’ – badala yake sema ‘ninaanza chuo’.

Unapoondoka chuoni unapewa ‘tool-kit’, au boksi la vifaa ambalo ukifika mtaani utalifungua na kuanza kulitumia kuunda vitu. Unapojaribu kuunda vitu kwa msaada wa elimu yako ya chuo – hapa ndipo unajifunza sasa.

Yaani hiki sasa ndio chuo halisi. Chuo halisi ni vitendo katika uhalisia wake. Chuo hiki kinataka umakini zaidi kwani ukifanya masihara kidogo unagalagazwa na unaweza usiinuke.

Unaweza kupata shida kukubaliana na hili, lakini maisha halisi ya msomi huonekana nje ya vyumba vya madarasa. Wapo wasomi ambao ndani ya madarasa wastani wao ni ‘A’, lakini wakiingia mtaani huporomoka hadi ‘D’.

Vijana waliofanikiwa ni wale waliomaliza vyuo na wakaendelea kujielimisha na kuyasoma mazingira ya nje ya darasa, na kuyakabili, ili yawaletee manufaa katika maisha yao.

Hata hivyo, vijana wengi siku hizi, wakimaliza chuo, husitisha zoezi la kijisomea ili kujiongezea maarifa, hivyo hukosa stadi muhimu za maisha, na hili huwaingiza wengi katika umaskini.

Kinachotakiwa, baada ya chuo, kijana soma vitabu, fuatilia vipindi mbalimbali vya redio na TV, hudhuria semina au maonesho mbalimbali, n.k.

Kuna stadi nyingi za maisha ambazo hazifundishwi vyuoni. Hizi zinapatikana mtaani, nje ya darasa, na ukizitumia ipasavyo maisha yatakunyookea.

Mbili, vijana wanatumia pesa kwa vitu visivyo na maana. Hii ina maana kwamba wapo vijana ambao baada ya kujipatia ajira au kujiajiri wanaanza kuingiza pesa.

Vijana hawa wanapata furaha kwa kuwa sasa ‘wanazo’ na maisha yao ni mazuri.

Tatizo la vijana wengi ni kwamba wakishapata pesa kwa njia yoyote ile, hupenda sana kujirusha. Vijana wanapenda starehe!

Vijana wanahusudu maisha mazuri ya watu waliofanikiwa sana. Wakiwaona vijana wenzao kupitia katika mitandao; mavazi, magari, starehe sehemu ghali n.k, hupenda na wao waishi maisha kama yale, sasa hivi.

Vijana wanatamani kwenda na wakati, wavae nguo fasheni kali za kileo, wabebe simu kubwa na za kisasa zaidi, wavae cheni za bei mbaya, na pia waendeshe ‘magari makubwa’ ya bei mbaya.

Kupenda starehe au kwenda na wakati siyo dhambi lakini yapo ya kuzingatia kwanza. Kama unalenga kuyafurahia maisha hadi uzeeni, jukumu la kwanza ni kujitambua na kujenga msingi imara wa kipato kabla ya kuanza kujirusha.

Ili kufanikisha hili unapaswa kujenga tabia ya kutumia kidogo na kuweka akiba ya kutosha kwa kila kipato unachoingiza.

Akiba unayoweka baadaye unaitumia kufanya uwekezaji mkubwa zaidi utakaokupatia mfereji mkubwa zaidi wa mapato.

Sasa, ukiweza kuwa na uhakika wa kujiingizia pesa ya kutosha, mfululizo, na uhakika kuwa vitega uchumi vyako vinajiendesha kwa faida, basi siyo mbaya ukijirusha.

Usipofanya hivyo tambua hutafika mbali kabla ya kipato chako kuanza kusinyaa na hadi unafikia umri wa uzeeni tayari huna pa kushika na maisha yanakugeukia.

Hatua ya kuchukua leo. Ni wajibu wa kijana mwenyewe kujitambua na kuchukua hatua ya kujifunza stadi hizi muhimu za maisha.

Ukitimiza wajibu wako mapema na ukafanya mambo haya katika umri wa ujana utatengeneza msingi mzuri wa maisha yako na hata uzee ukiingia hutakuwa na kitu cha kujutia.

Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasirimali kivitendo.

Anapatikana kwa e-mail: nzyy2001@gmail.com; Simu 0718219530

Stadi Muhimu Za Maisha; Ndani Ya Maisha Ya Kuajiriwa – (2)

Habari rafiki,

Katika sehemu ya kwanza ya makala hii, nimetoa maelezo na ufafanuzi kuhusu stadi tatu muhimu kwa maisha ya kuajiriwa.

Nilieleza kwamba pamoja na elimu, ujuzi na uzoefu wa miaka mingi ambao mwajiriwa anaweza kuwa nao kazini, kitu kinachowakwamisha wafanyakazi wengi, wasipate mafanikio kazini, ni elimu ndogo ya stadi hizi.

Nilitoa angalizo kwa vijana kwamba mafanikio katika ajira yana kanuni zake na wala hayaji kiurahisi kama wengi wanavyofikiria.

Uwezo wa kujenga mahusiano na mawasiliano bora kazini ni sifa muhimu

Sasa, ni stadi zipi hizi za maisha unazohitaji kuwa nazo katika sehemu za kazi ili kukuinua hadi ufikie matawi ya juu? Fuatana na mimi katika sehemu hii  ya pili, ambapo nitaongelea stadi nyingine tano, kama ifuatavyo;

Nne, jenga tabia ya kuwaamini na kuwawezesha wafanyakazi wenzio. Katika sehemu ya kazi, watu wengi hufanya kazi wakiwa katika timu, kwa kushirikiana, na kila mtu hutoa mchango wake ili kufanikisha malengo.

Siri ya mafanikio hapa ni kuaminiana na kuwezeshana. Unapaswa kujenga tabia ya kuamini kuwa kila mmoja wenu ana uwezo na maarifa, na ana nia ya dhati ya kufanikisha malengo ya timu nzima.

Uwezo wa kuwaamini, kuwawezesha na kuwasaidia wenzio ili wafikie viwango vya juu vya uwezo wa utendaji kazi ni jambo kubwa.

Jambo hili linaweza kuwashawishi ‘wakubwa’ kuwa wewe una uwezo wa kuwaelewa na kuwaunganisha wenzio; na hapa utakuwa umejitengenezea ngazi nzuri ya kupandia kuelekea matawi ya juu.

Tano, Uwezo wa kubadilika ili kuendana na mazingira. Mabadiliko ni jambo la kawaida kazini, na wakati fulani huwezi kuzuia yasitokee. Kwa kulifahamu hili maana yake ni kwamba wewe ndio unatakiwa kujiweka tayari kubadilika.

Yaani, yakitokea mazingira yanayolazimisha watu wabadili namna yao ya kufanya mambo, au taratibu za utendaji, au tabia, basi unapaswa uwe mwepesi kubadilika.

Ukiwa na sifa hii muhimu, utawavutia wenzio, lakini ujue pia kuwa viongozi wana macho na wasikio, hivyo taarifa hizi zitawafikia na baada ya muda utaona matunda yake.

Sita, uwezo wa kutatua matatizo kazini. Katika utendaji kazi wa kila siku, makazini, migogoro ni kitu cha kawaida. Wafanyakazi ndani ya idara moja huweza kutofautiana hadi wakalumbana.

Ipo migogoro inayotokana na mambo ya kawaida, yaani mahusiano binafsi. Ipo pia migogoro inayotokana na tofauti ya mitazamo ya namna ya kufanikisha jukumu fulani kazini.

Mtu mwenye uwezo wa kuingilia kati, kusuluhisha, na kuonesha njia iliyo bora ya kutatua tatizo au mgogoro uliojitokeza, huyu anaboresha mahusiano kazini.

Huyu mtu, muda si mrefu, sifa yake nzuri husambaa hadi kuwafikia viongozi wa juu. Watu wenye sifa hii hupendwa, kukubalika na kuhitajika sana. Ukijijengea sifa hii hakika una nafasi kubwa ya kupewa nafasi ya juu kazini.

Saba, uwezo wa kujadiliana na kutetea hoja. Mahala pa kazi huwa wakati fulani zinaibuka hoja zinazopingana. Watu wanakuwa na uelewa tofauti wa suala lililojitokeza, na namna ya kulitafutia majawabu.

Ukiwa na uwezo wa kuchambua mambo, kupangilia hoja na kuziwasilisha vyema kwa wenzio hadi mwafaka ukapatikana basi wewe una uwezo wa kutengeneza makubaliano na usuluhishi.

Ukiwa na uwezo huu ujue ‘wakubwa’ wanaona, na usije kushangaa siku moja, inapotokea nafasi ya juu, jina lako likawa la kwanza kutajwa ili kuchukua nafasi hiyo.

Nane, uwezo wa kujiamini na kujisimamia. Waajiri wengi humpenda mtu mwenye uwezo wa uongozi.

Wapo vijana makazini, wadogo tu kwa umri, na wengine wapo katika nafasi za chini tu kazini, lakini wana uwezo wa kujisimamia na kuibua mambo ya maana.

Uwezo wa kijisimamia humwezesha mtu kupanga, kuratibu na kujua kipi kianze kufanyika, kipi kifuate, kifanywe kwa utaratibu gani, rasilimali gani zitumike na nani wahusike katika utekelezaji.

Mtu mwenye sifa hii hutafuta tu kuyajua majukumu na mipaka yake ya utekelezaji wa majukumu yake. Akishayajua hahitaji tena kusukumwa ili afanye kitu.

Huyu mtu ana maono na mbinu za kujua nini cha kufanya na huingia katika utekelezaji bila jitihada kutoka kwa wasimamizi wake. Huyu anajitambua na ana msukumo binafsi kutoka ndani wa kutaka kufanikisha mambo.

Mtu mwenye sifa hii hahitaji kupiga kelele ili watu wajue kuna mtu anafaa kupewa uongozi. Hapana. Kila kitu huwa wazi kwa kila mtu kuona, na mara nyingi viongozi huchukua muda mfupi sana kabla ya kumpendekeza kwa nafasi za juu.

Hatua ya kuchukua leo: kijana unapoingia katika maisha ya kuajiriwa – jitahidi uzielewe stadi hizi, na zingine.

Ukiweza kuzifanyia kazi vyema hakika utaaminiwa na kupata heshima kazini. Viongozi watakutazama kwa jicho maalum ambalo litakupaisha hadi nafasi za juu. Na hayo ndio mafanikio yanayotarajiwa na vijana wengi makazini.

Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasirimali kivitendo.

Anapatikana kwa e-mail: nzyy2001@gmail.com; Simu 0718219530

Stadi Muhimu Za Maisha; Ndani Ya Maisha Ya Kuajiriwa – (1)

Habari rafiki,

Baada ya maisha ya muda mrefu ya kutafuta elimu shule na baadaye chuo, kuna njia kuu mbili zinazofuatwa na vijana katika kujipatia kipato.

Njia ya kwanza ni kujiajiri, ambapo kijana mwenye kipaji fulani au wazo la biashara, huamua kukigeuza kipaji au wazo lake kuwa kitu cha kumwingizia fedha.

Njia ya pili na inayofuatwa na vijana wengi ni kutafuta kazi ya kuajiriwa. Hapa kijana hutuma maombi ya kazi maeneo mbalimbali na akibahatika huitwa kuanza kazi.

Bila kujali ni njia gani kijana kaamua kupitia ili kujipatia riziki yake, kilicho muhimu ni mafanikio katika maisha. Na kila mtu ana maoni yake kuhusu nini maana ya mafanikio.

Katika kazi  ya kuajiriwa mafanikio ni pamoja na kulipwa ujira mzuri na hivyo kumudu gharama za maisha, kupata heshima ndani na nje ya Kampuni, na kushika nafasi za juu za uongozi katika kampuni.

Leo naomba niongelee zaidi kuhusu mafanikio katika kazi ya kuajiriwa. Napenda kuwapa angalizo vijana kwamba mafanikio katika ajira yana kanuni zake na wala hayaji kiurahisi kama wengi wanavyofikiria.

Mara nyingi watu wanapoajiriwa huanzia ngazi za chini kabisa ambazo pia huwa na maslahi kiduchu. Jinsi mfanyakazi anavyopanda ngazi kuelekea nafasi za juu za uongozi ndivyo anavyozidi kupata maslahi bora zaidi.

Sasa, pamoja na hamu ya kupata maslahi bora zaidi kazini, wafanyakazi wengi hawana maarifa kuhusu mbinu za kuwawezesha kufikia matawi ya juu.

Ukweli ni kwamba pamoja na elimu, ujuzi na uzoefu wa miaka mingi kazini, kitu kinachowakwamisha wafanyakazi wengi ni elimu ndogo ya stadi za maisha ya kuajiriwa.

Wafanyakazi walioipata elimu hii wana nafasi kubwa ya kuziteka hisia za wafanyakazi wenzao pamoja na viongozi wa ngazi za juu, kitu ambacho huwainua hadi kuzishika nafasi muhimu katika Kampuni husika.

Kwa kujifunza na kuziendeleza stadi hizi muhimu mfanyakazi huyu huboresha uhusiano wake na wenzake pamoja na mabosi wake na mwishowe mambo humnyookea.

Mawasiliano bora huongeza tija sehemu za kazi

Ni stadi zipi hizi za maisha unazohitaji kuwa nazo katika sehemu za kazi ili kukuinua hadi ufikie matawi ya juu? Fuatana na mimi katika sehemu ya kwanza ya makala hii ambapo nitaongelea stadi tatu kama ifuatavyo;

Moja, stadi za mawasiliano. Uwezo na umahiri katika mawasiliano ni stadi muhimu sana sehemu ya kazi. Stadi hii sio tu inaboresha uhusiano lakini pia inajenga imani miongoni mwa wafanyakazi.

Katika dunia hii ya kidigitali kuwa na uwezo wa kuwasiliana vizuri na watu ni sifa muhimu.

Na suala hapa sio uwezo wa kuongea sana, bali uwezo wa kupokea kwa usahihi na kupeleka kwa ubora na usahihi data na taarifa muhimu kwa matumizi ya ndani na nje ya Kampuni, kwa kutumia njia mbalimbali.

Mawasiliano bora sio tu yanaongeza tija kazini lakini pia yanaleta uwazi na kuwaunganisha wafanyakazi kuelekea katika kufanikisha lengo kuu la Kampuni.

Mbili, kuwaelewa na kuwaheshimu wenzako. Sehemu ya kazi hupata mafanikio pale ambapo wafanyakazi wanaongea lugha moja. Uwezo wa kuwaelewa wenzako ni sifa ya maana sana.

Kuna wakati kazini utagundua watu wana mitazamo yao kuhusu jambo fulani, pengine tofauti na mitazamo yako.

Katika mazingira haya, uwezo wa kuheshimu mawazo na mitazamo ya wengine ni muhimu sana. Yaani mnatofautiana katika mtazamo lakini hamgombani, na jambo hili hujenga mahusiano bora kabisa.

Tatu, uvumilivu. Hii ni moja ya sifa muhimu sana kwa mfanyakazi kuwa nayo hasa wakati mazingira ya kazini yamekorogeka kidogo. Ukiwa na uwezo wa kuvumilia, kujishusha kidogo na kuepuka kutunisha misuli bila sababu, utaheshimika.

Uvumilivu katika machafuko huifanya akili yako ifanye kazi kwa utulivu na iwe na uwezo mkubwa wa kufikiri na kukabiliana na matatizo ili kuyatafutia ufumbuzi.

Mfanyakazi mwenye sifa hii sio tu anaonwa na wenzake bali pia anaonwa na viongozi wa juu wa Kampuni. Viongozi humpenda sana mfanyakazi asiyepaniki hasa wakati wa mtikisiko.

Ukiaminiwa na viongozi ni rahisi kufikiriwa kushika nafasi za juu kazini ambazo zitakunufaisha pia kimaslahi.

Hatua ya kuchukua leo: kijana unapoingia katika maisha ya kuajiriwa – jitahidi uzielewe stadi hizi, na zingine (soma sehemu ya 2 ya makala hii).

Ukiweza kuzifanyia kazi vyema hakika utaaminiwa na kupata heshima kazini. Na imani hii itawaingia hadi viongozi wakuu kazini ambao watakutazama kwa jicho maalum.

Ni jicho hili maalum ndilo litakalokuondoa katika nafasi yako ya chini uliyonayo leo na kukupaisha hadi ukayakamata matawi ya juu ambayo ndio mafanikio yanayotarajiwa na wengi.

Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasirimali kivitendo.

Anapatikana kwa e-mail: nzyy2001@gmail.com; Simu 0718219530

Mambo Yanayolalamikiwa Mara Nyingi Na Wateja

Habari rafiki,

Huduma kwa mteja ni jambo muhimu sana ambalo kila mfanyabiashara anapaswa kulijua na kulifanyia kazi ipasavyo. Bila mteja biashara au shughuli yoyote ya ujasiriamali haitafanya vizuri.

Mteja asipopata huduma bora mara nyingi ataanza kwa kukasirika na baadaye kulalamika, na akiona pamoja na kulalamika hakuna jambo la maana linafanyika ataamua kuondoka kwa hasira, na huenda asirudi tena.

Mteja akihudumiwa vyema hujawa na furaha na hushikamana na Kampuni husika

Sasa, kuhusu huduma kuna mambo manane ambayo mara nyingi mteja huyalalamikia. Makala hii inalenga kuyaongelea mambo hayo, kwa mtazamo wa mteja, na kutoa ushauri wa jinsi ya kushughulika nayo.

Moja, “nimesubiri kwa dakika ishirini na hakuna mtu wa kunipa huduma.” Hii hutokea ana kwa ana lakini hata katika simu, kwa watoa huduma kwa simu. Yaani unapiga simu kwa mtoa huduma, inaita tu na hakuna mtu wa kuipokea.

Na kibaya zaidi, unaweza kuwatafuta watoa huduma hawa, kwa simu, kwa zaidi ya dakika thelathini nzima, bila majibu, mpaka ukaamua kukata simu.

Baada ya kukata simu, matarajio ni kwamba wao wataona miss – call yako itakayowaonesha kuwa kuna mteja alipiga, ili wao wapige –  sahau jambo hili, wengi hawapigi!

Mbili, “bidhaa haifanyi kazi kama inavyopigiwa debe na mtoa huduma.” Hili huwachukiza sana wateja. Ni uongo au utapeli kumpa mtu matarajio yasiyo na uhalisia au usiyoweza kuyatimiza.

Ni afadhali ukasema ukweli kwa kumwambia mteja upungufu katika bidhaa yako, ili mteja aamue mwenyewe kununua au la. Akiamua mwenyewe hawezi kuja kulalamika.

Tatu, “napata majibu yaliyochelewa kwa barua za mtandaoni; barua pepe au meseji (sms).” Yaani unatuma meseji ya kutaka maelezo, ufafanuzi au malalamiko kuhusu bidhaa– majibu yanakuja baada ya siku tatu au zaidi, au hayaji kabisa, kitu kinachowafanya wateja kulalamika.

Nne, “makampuni au watoa huduma wengine huduma zao ni sawa na sifuri kabisa.” Yaani hawa, katika nyaraka zao za kawaida na za mtandaoni, hawana namba za simu wala majina ya wahusika.

Unatafuta mamba ya kampuni mtandaoni huipati, au kama utaipata basi ukijaribu kupiga namba hiyo utaambiwa haipo au haipatikani kwa sasa, muda wote! Hii ni hatari kwa uendeshaji wa biashara.

Hatua ya kuchukua; kama wewe ni mjasiriamali jifunze kila mara kufuatilia malalamiko ya wateja wako ili uone kama yana ukweli na uhalisia, kisha uone jinsi ya kuyatafutia ufumbuzi.

Lakini kikubwa ni kwamba usingojee hadi mteja alalamike ndipo uchukue hatua, hapa unakuwa umechelewa. Jifunze kutabiri malalamiko ya wateja kabla hatajatokea na kufanya kitu fulani kabla mteja hajaingia katika malango ya biashara yako.

Unapaswa kuwapa mafunzo wasaidizi wako ili kila mmoja awe na ujuzi na maarifa ya kutoa huduma itakayowafurahisha wateja. Usipowajali wateja wako ujue bishara yako tayari imekushinda.

Kumbuka ni rahisi kumpata mteja mpya lakini ukiamua kumuudhi ujue hatarudi na atapeleka sifa hiyo mbaya kwa rafiki na ndugu zake wengi, na hao utawakosa pia.

Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasirimali kivitendo.

Anapatikana kwa e-mail: nzyy2001@gmail.com, 0718219530

Jifunze Kujiamini Na Kuyaamini Mawazo Yako

Habari rafiki,

Nimewahi kumsikia mtu akimwambia mdogo yake aliyetaka kuacha kufanya kazi fulani baada ya kuambiwa na rafiki yake kuwa kazi hiyo haina hadhi. Alisema , “dogo, hivi unamjua binaadamu wewe?”

“Kama humjui tambua leo kuwa binaadamu ameumbwa kuongea, na hakosi la kusema!”

“Kazi zenyewe za kugombania, halafu anataka uchague kazi – atakupa kazi yeye? Achana naye!”

Jambo hili likanikumbusha hadithi fupi niliyoisikia mahala fulani inayomhusu mzee mmoja, mkewe na punda wao, waliokuwa wakisafiri kutoka kijiji kimoja kwenda kingine.

Ukiamini utalifikisha jiwe hili juu, shikilia imani yako, asitokee mtu wa kukukatisha tamaa.

Wakiwa wamempanda punda, wote wawili, njiani walikutana na vijana wawili. Vijana wale walionekana wakiwashangaa wazee hawa na kusikika wakisema, “hawa wazee hawana huruma kabisa; yaani na uzito wao, wamekaa mgongoni mwa punda, si watamuua?

Wazee wale walisikia maneno yale, wakajisikia vibaya. Hivyo mke akamwambia mumewe basi mimi nashuka, nitatembea, wewe endelea kumpanda punda.

Muda si mrefu wakakutana na vijana wengine, wakawasikia wakilalamika wakisema, “huyu mzee mkoloni kama nini, yaani anathubutu kumtembeza mkewe, huku yeye akibebwa na punda.”

Wale wazee wakasikia maneno yale, na mzee anajisikia vibaya. Akaamua kushuka na kumpandisha mkewe juu ya punda, naye akawa anatembea kwa miguu.

Walipofika mbele kidogo wakawakuta vijana wengine, wakawasikia wakilalamika wakisema, “huyu mzee ni mjinga, huenda katawaliwa na mkewe, tazama anatembea kwa miguu wakati mkewe anajivinjari juu ya punda.”

Wale wazee walisikia maneno yale, wakajisikia vibaya, wakaamua wote washuke na watembee kwa miguu pamoja na yule punda.

Hata hivyo mbele kidogo waliwakuta vijana wengine na wakawasikia wakisema, “jamani, hawa wazee mataahira kweli; yaani hawajui hata matumizi ya punda.” Wazee wale walichanganyikiwa!

Kutokana na hadithi hii kuna vitu vingi vilipita ndani ya kichwa changu.

Nilianza kuifikiria sentensi hii, “hivi unamjua binaadamu wewe? Kama humjui tambua leo kuwa binaadamu ameumbwa kuongea, na hakosi la kusema!” Nikashusha pumzi.

Katika maisha karibu kila mtu ana mambo na malengo yake anayoyaamini na kuona kuwa yana nafasi ya kumfikisha katika maisha fulani anayoyatamani.

Watu hawa pengine huwa tayari wana mawazo yao, mazuri tu, na pengine wanajua wanavyoweza kuyabadili kuwa vitu halisia vyenye thamani.

Hata hivyo, kama ilivyo kwa simulizi hapo juu, dunia imejaa watu wa aina na mitazamo mingi. Jamii inayotuzunguka mara nyingi ina athari kubwa katika matendo na maamuzi tunayofanya.

Wakati fulani watu hujikuta wakiishia kufanya vitu wasivyoviami, na visivyo katika mipango au malengo yao kutokana na sauti za watu wengine. Hujikuta wanaburuzwa na misimamo au ushawishi wa watu wengine.

Kutokana na ushawishi huu watu hujikuta wameacha yale yote mazuri waliyokuwa nayo na mwisho wanaharibikiwa, na pengine wanafedheheka.

Kwa kutekwa na mawazo ya wengine watu hawa wanajikuta wakijiweka katika hatari ya kushindwa kutimiza ndoto zao, na hii inatokana na kuogopa kuonekana hawawezi kufikiri sawasawa. 

Watu hawa hujifedhehesha. Na fedheha hii inasababishwa na jitihada za  watu hawa kujaribu kujikinga na hisia za watu wengine kuhusu wao na mambo au maamuzi wanayofanya. Watu hawa wanajaribu kuficha vitu wanavyohisi watu wengine hawawaungi mkono.

Badala yake wanajitahidi kujiweka katika hali au mazingira ambayo wanahisi watu wengine wangependa wawe. Wanaficha vitu ambavyo wengine wanasema, kwa mitazamo yao, kuwa siyo vitu vizuri.

Sasa, ukweli ni kwamba kusikiliza mno wanayosema wengine juu yetu, kinyume na yale tunayoamini sisi – ni utumwa! Tunakuwa mateka wa matakwa ya watu wengine, jinsi ambavyo wao wangependa sisi tuwe.

Tunapaswa kuwa na mtazamo chanya. Tunapaswa kujiamini na kuamini kila tunachofikiri na kutenda badala ya kutegemea mitazamo ya watu wengine. Tunapaswa kufuata maadili yanayoongoza maisha yenye unyoofu.

Kwa hiyo badala ya kushughulika na imani za watu wengine kuhusu masuala yetu ya maisha, yafaa tujikite katika kufanya mambo au maamuzi yanayoendana na maadili yetu.

Kwa mfano, kuna dada mmoja msomi wa Shahada ya kwanza huko Mwanza anafanya biashara ndogo ya kutengeneza, kufungasha na kutembeza dagaa, kwa kichwa, katika maofisi kadhaa akiwalenga wateja wa maofisi hayo.

Kuna watu, wanawake wenzake na wanaume pia, ambao walijaribu kumkatisha tamaa wakimwambia kuwa biashara hiyo haiendani na hadhi na usomi wake.

Lakini kwa vile huyu dada anajiamini na kuamini anachofanya hajawahi kutetereka – anaendea kusonga!

Binaadamu ‘wanachonga’ sana, na ukitaka kusikiliza kila kitu wanachosema juu yako utachanganyikiwa na utaanguka kimaisha.

Kumbuka kuna watu takriban billion saba duniani – kwa hiyo kuna uwezekano wa kupata maoni karibu billion saba kwa siku.

Jifunze kuishi ndani ya imani na maadili yako bila kujali mitazamo ya watu wengine, kwani huwezi kuwaridhisha watu wote.

Maana yake ni kwamba, kama unaishi kwa yale unayoyaamini huwezi kupata fedheha au kujisikia vibaya, hata kama utakabiliwa na mambo fulani magumu.

Kuwa na msimamo haina maana kuwa utapuuza kila kitu unachoshauriwa, hapana.

Kuna wakati kwa mfano utasikia watu wakisema, “aah ndugu yetu huyu naona amezidisha ulaji wa chakula na wala hafanyi mazoezi, si unaona anavyozidi kunenepa, asije akapasuka!” Maoni ya aina hii ukiyapuuza utaishia pabaya.

Hatua ya kuchukua: usije ukapuuza maoni fulanifulani ya watu, yana maana. Kikubwa ni kwamba lenga katika kufanya kitu sahihi badala ya kufanya kitu kwa kumfurahisha mtu.

Katika kufanya hivyo unaweza kukosea lakini kwa kuwa umefanya kitu ulichokiamini huna kikubwa cha kupoteza, rekebisha kisha songa mbele.

Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasirimali kivitendo.

Anapatikana kwa simu: 0718219530; e-mail: nzyy2001@gmail.com

Stadi Za Maisha – Muhimu Kwa Maisha Ya Ndoa

Habari rafiki,

Kuingia katika maisha ya ndoa ni hatua muhimu sana kwa kijana yeyote. Pamoja na kwamba suala la kujielimisha ni endelevu, kuna maarifa ambayo ukiyapata mapema utapata manufaa makubwa ndani ya ndoa.

Kufanikisha maisha ya ndoa yenye furaha kunahitaji maarifa

Ndoa ni jambo muhimu, na ndio maana utaona sherehe za harusi, watu wakifunga ndoa, zinapewa uzito mkubwa kuliko hata vitu kama mahafali ya kumaliza elimu ya chuo kikuu.

Ndoa ni muungano kati ya mwanamke na mwanaume kwa lengo la kuishi pamoja kama mume na mke muda wote wa maisha yao.

Ndoa yenye furaha ni ile ambayo kila mmoja anafahamu wajibu wake na anautimiza ipasavyo.

Kwa hiyo, inahitaji ujuzi wa stadi kadhaa za maisha kwa wanandoa kuweza kuishi pamoja kwa furaha na upendo. Ndoa zilizokosa maarifa haya zimeishia kuyumba na nyingine kuvunjika, tena mapema sana.

Kuna stadi nyingi za maisha ambazo vijana wakiwa nazo kabla na baada ya kufunga ndoa zina msaada mkubwa kwa maisha yao.

Kujenga tabia na maadili mema ni moja ya stadi muhimu. Hili linahusisha utunzaji wa miili ili iwe safi, yenye afya bora na inayoheshimika. Inahusisha pia kuwa na imani katika dini na kutii amri za Mungu.

Maarifa ya kujenga mahusiano bora, yenye upendo, kati ya wanandoa kabla na ndani ya ndoa ni stadi nyingine muhimu. Hili linahusisha pia mahusiano na watu mbalimbali, wakiwamo wa jinsia na rika tofauti.

Stadi nyingine muhimu ni maarifa ya kuwasiliana kwa ukamilifu. Ukiingia ndani ya ndoa unahitaji kuelewana na mwenzio. Kwa hiyo unapaswa kujua kuongea na kusikiliza.

Jifunze kipi cha kuongea na kipi cha kuacha. Fikiria ni kitu gani kiongelewe sasa na kipi kiongelewe baadaye. Jifunze pia kipi kiongelewe nje, kipi sebuleni na kipi chumbani.

Unapaswa kujifunza kitu gani kiongelewe kwa mdomo, ana kwa ana, na kipi kiongelewe kwa simu. Kama kwa simu, kipi kwa simu ya maongezi na kipi kwa ujumbe wa maandishi – yote haya yanalenga kuboresha mahusiano na upendo.

Mwanandoa unapaswa kujifunza jinsi ya kujifunza. Jifunze kujali elimu na ujuwe kuwa elimu haina mwisho wala umri. Jifunze teknolojia mpya zinazoingia na jinsi zitakavyokusaidia kukuza upendo katika ndoa yako.

Jifunze kufanya maamuzi sahihi. Ukiwa katika ndoa jiulize kila wakati maamuzi gani ni bora kuliko mengine. Jifunze kupima umuhimu wa vitu ili kujua kipi kianze na kipi kifanyike au kije baadaye.

Jifunze jinsi ya kupambana na changamoto za maisha. Ndoa zina changamoto nyingi; maisha nayo yana vikwazo kibao!

Zielewe nguvu na maadili yako, na ujue yanavyoweza kukusaidia katika maisha ndani ya ndoa yako. Jifunze kutawala msongo wa mawazo na ujue mbinu za kuupunguza.

Jifunze kufanya tafakuri tunduizi. Kufikiri kwa umakini kunakuza uwezo wa kutoa maamuzi ya maana. Kufikiri kwa umakini huzaa ubunifu.

Katika ndoa lazima kuwe na mipango. Mbinu za kupanga malengo ya maisha ni muhimu. Ukiwa ndani ya ndoa unakuwa na vitu vingi unavyotaka kuvitimiza.

Kwa hiyo, ili ufanikiwe, vipange vitu hivyo kwa umuhimu wake, kisha weka malengo na program ya utekelezaji kwa kila lengo, kulingana na rasilimali ulizo nazo.

Jifunze matumizi ya pesa. Jifunze jinsi ya kutumia fedha kwa busara na tija. Fahamu ubora wa bidhaa ikilinganishwa na bei yake. Jifunze kupanga na kufuatilia bajeti. Jifunze wakati gani utumie pesa, na wakati gani uweke akiba.

Jifunze unyenyekevu. Ndoa inahitaji nidhamu ya hali ya juu. Jifunze kuwa na heshima, unyenyekevu na upendo. Mheshimu mwenzi wako kutokana na hadhi yake na jiepushe na ubinafsi.

Hatua ya kuchukua leo: kabla kijana hujaingia katika maisha ya ndoa – jiandae. Zielewe stadi hizi, na zingine muhimu na uzishike.

Ukiweza kuzishika vyema kwa kuzielewa na kujua umuhimu wake utaingia katika ndoa kwa mguu mzuri na ndoa yako itakuwa na furaha na baraka.

Ukiingia tu alimradi na wewe umo katika jahazi hili basi ujue muda wako wa kuishi humo ni mfupi au utaishi humo kama uko ndani ya tanuru la moto.

Makala hii imeandikwa na Bw. Laurent Fungavyema, mtaalamu wa fani ya biashara na mjasirimali kivitendo.

Anapatikana kwa e-mail: nzyy2001@gmail.com; Simu 0718219530